WAKATI ikiwa katika mgogoro na madiwani wake wa Arusha, Chadema imepata pigo baada ya mmoja wa madiwani wake Singida kujiengua na kurudi katika Chama Cha Mapinduzi (CCM), akidai hataki kuwa sehemu ya machafuko nchini.
Diwani huyo, Simon Tyosela wa kata ya Urughu, Iramba Magharibi, alisema hayo jana katika Ofisi ya Makao Makuu ya CCM mjini Dodoma, mbele ya Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM anayeshughulikia masuala ya Uchumi na Fedha, Mwigulu Mchemba.
Tyosela aliyehamia upinzani wakati wa mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 baada
ya kuanguka katika kura za maoni ndani ya CCM, alisema hakushawishiwa kuihama Chadema na kurejea CCM, bali amenusa hatari kwa taifa katika siku za usoni.
Alisema, maandamano yenye sura ya uchochezi kila kukicha, yamemkosesha amani na
kujiona msaliti mbele ya Watanzania.
Haya ya kushinikiza wananchi kuiga maandamano katika nchi za wenzetu, tena yasiyo ya amani, binafsi yamenishinda. Chadema hakuna demokrasia ya kweli na nilitarajia ingekuwa mstari wa mbele kuhangaikia maendeleo ya wananchi. Nimejiondoa kwa sababu mimi ni mpenda amani kwa nchi yangu.
Kwa mtindo huu niliona kabisa hatuwezi kufikia malengo ya millennia, kwa sababu
kila kukicha ni maandamano, hakuna la maana linalofanyika kwa ustawi wa nchi
yetu, alisema diwani huyo.
Alisema, hana cha kujutia kwa sababu wananchi ndio waliokuwa wamemshawishi kuingia Chadema wakitaka atumie chama kingine chochote kuingia madarakani, baada ya kushindwa kura za maoni.
Mchemba alimpongeza na kuitaka jamii kutokubali kuburuzwa na vyama vingine vya siasa kwa maslahi ya watu wachache wenye mwelekeo wa kulazimisha kushika madarakani kwa nguvu.