CAG akataa hesabu za vyama vya siasa
Zaina Malongo
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali (CAG) amekataa kupokea ripoti ya vyama vitano vya siasa vilivyowasilisha hesabu kwa miaka tofauti.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam CAG, Lodivick Utough alisema amepitia hesabu hizo na kubaini kuwa zimekaguliwa na wakaguzi wa kampuni binafsi na siyo ofisi yake kama sheria inavyotaka.
CAG Utough alisema kampuni hizo zinatambuliwa na Bodi ya Wahasibu (NBAA).Utou ambaye alikuwa akizungumzia ukaguzi wa vyama vya siasa na wagombea walioshiriki katika uchaguzi mkuu, uliofanyika Oktoba 31, mwaka jana alisema, vyama vilivyowasilisha hesabu hizo ni Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kwamba mwaka 2008 ilikaguliwa na kampuni ya TAC, Chama Cha Wananchi (CUF), mwaka 2009 ilikaguliwa na kampuni ya Imara Consultants wakati Tanzania Labour (TLP) kwa mwaka 2009 kilikaguliwa na kampuni ya Shebril Campany.
Kwa upande wa Chama cha NCCR Mageuzi, mwaka 2010 ilikaguliwa na kampuni ya Eliable Consultants, UDP na kwamba mwaka 2007 ilikaguliwa na Kampuni ya Philip.
"Ni wazi kuwa wakaguzi waliokagua hesabu hizo walikuwa na sifa za kufanya ukaguzi huo, hata hivyo hesabu hizo hazikuwasilishwa kwa wakati unaotakiwa kisheria.
"Ninapenda kuwakumbusha kifungu cha sheria namba 14 (1) cha sheria ya vyama vya siasa namba 5 ya mwaka 1992 kama ilivyofanyiwa mabadiliko na sheria namba 7 ya mwaka 2009, vinatakiwa vyama vyote vyenye usajili wa kudumu kuwasilisha kila mwaka kwa msajili wa vyama vya siasa hesabu zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali,"alisisitiza.
Utouh alisema kwa mantiki hiyo, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali ndio mwenye wajibu wa kukagua hesabu za vyama vya siasa.
"Baada ya kuchambua kwa kina ripoti hizo imeonekana dhahiri kwamba haitakuwa vema nikae kimya bila kutoa maelezo kwa umma kwani utaratibu uliotumika wa kuwasilisha hesabu zilizokaguliwa na kampuni binafsi za ukaguzi si sahihi na zinakiuka taratibu,"alifafanua.
Alisema ili kudumisha uwazi na uwajibikaji katika rasilimali za umma wa Tanzania ofisi iko makini na itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria ya vyama vya siasa ya mwaka 1992 kama ilivyo fanyikanyiwa mabadiliko na sheria namba 7 ya mwaka 2009.
Alisema Ofisi ya taifa ya ukaguzi itaendelea kwa lengo la kuhakikisha mapato na matuminzi yanayofanyika kwa manufaa ya umma.
Alisema mwaka jana, mahtasari wa ukaguzi wa vyama vya siasa na wagombea walioshiriki katika ukaguzi mkuu imemtaka CAG kukagua hesabau za vyama vya siasa na wagombea walioshiriki.
Utouh alisema hesabu za vyama vya siasa zilizo wasilisha kwake ni za vyama vitano tu kwa ajili ya maandalizi ya awali ya ukaguzi.
Alivuitaja vyama hivyo kuwa ni CCM, Chadema, CUF, Jahazi Asilia na TLP.
Alisema kifungu cha 20 (1) cha sheria kimesema chama cha siasa na kila mgombea ambaye anatakiwa kwa masharti ya sheria kutoa taarifa ya kiasi na chanzo cha fedha kinachotarajiwa kutumika kama gharama za ukaguzi, akishindwa kutoa taarifa ya fedha hizo, bila ya kuwa na maelezo yanayoridhisha, chama au mgombea hataweza kushiriki katika uchaguzi.
Utouh alisema ni kosa kutowasilisha au kuchelewa kuwasilisha hesabu kulingana na kifungu cha 19 (4) na 20 (10) kinavyoangiza.
Alisema ofisi ya taifa ya ukaguzi wa hesabu za serikali inawahimiza wagombea wote na vyama vya siasa kuzingatia sheria kwa ajili ya maslahi ya umma na kudhibiti matuminzi mabaya na kuepuka vitendo vinavyokatazwa.
Alisema tayari taarifa 10,000 kutoka kwa wagombea wa mwaka jana tayari zimepokelewa na kuchambuliwa, na ofisi imejipanga kwa ajili ya uhakiki.