!!chadema chama tawala nje ya ikulu!!

Technician

JF-Expert Member
Mar 30, 2010
841
222
CHADEMA sasa ndicho chama ‘tawala’
ban.blank.jpg


Martin Kaswahili​

TANGU kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge, na madiwani mwezi Oktoba mwaka jana, nchi yetu imeshuhudia matukio kadhaa ya kipekee ambayo huenda yakawa kiashirio cha matukio mengine makubwa na ya kihistoria katika siasa za Tanzania katika siku za usoni.

Si nia yangu katika makala hii kudodosa kila jambo lililojitokeza wakati na baada ya uchaguzi huo ambao matokeo yake, hasa yale ya urais, yaliacha minong’ono na miguno miongoni mwa wananchi kiasi cha kuamsha chuki na uasi wa kimoyomoyo (passive resistance), uliopelekea kujengeka kwa ujasiri wa kupinga waziwazi yale yanayofanywa na watawala. Ujasiri huo ndiyo umekuwa chanzo cha maandamano makubwa na ya kihistoria ambayo yameitisha si serikali iliyoko madarakani tu bali hata chama kilichotakiwa kuwa chama tawala. Nitafafanua.

Kwa kawaida, baada ya uchaguzi kumalizika na serikali kuundwa, kazi kubwa ya serikali mpya ni kuanza kutekeleza kwa vitendo ahadi zilizoahidiwa na viongozi wa chama tawala wakati wa kampeni za uchaguzi kwa mujibu wa ilani yao ya uchaguzi. Kwa upande mwingine, vyama vya upinzani navyo huanza mara moja kutimiza wajibu wao wa kidemokrasia wa kuikosoa, kuisimamia, na kuiwajibisha serikali iliyoko madarakani, kwa njia ama ya bunge (kama chama kimepata wabunge) au kwa njia nyingine za kisiasa.

Kwa mantiki hii, mara baada ya uchaguzi wananchi hutarajia kuona serikali yao ikianza kwa nguvu kutimiza wajibu wake wa kutatua kero zao bila kujali mashambulizi ya vyama vya upinzani kupitia bunge au majukwaa ya kisiasa. Hii ndiyo kawaida katika ulingo wa siasa za vyama vingi katika nchi zote zinazofuata mfumo wa kidemokrasia.

Hutasikia mahali popote serikali iliyowekwa madarakani kwa kura halali za wananchi walio wengi ikitolewa kirahisi kwenye ajenda yake muhimu ya kuwatumikia wananchi walioichagua na kuanza kutumia muda wake mwingi kushughulikia chama au viongozi wa upinzani, kama inavyotoea sasa hapa nchini.

Kwa upande mwingine, kazi ya chama kinachokuwa kimeshinda uchaguzi ni kuisaidia serikali na viongozi wake katika kutekeleza majukumu yao ya kufanyia kazi yale yaliyoahidiwa katika ilani ya chama hicho. Chama tawala hutakiwa kuwa mlinzi wa serikali iliyopo madarani kwa kuikumbusha wajibu wake na kuitetea kwa wananchi kwa njia za kisiasa.

Kwa maneno mengine, CCM kwa kutumia jukwaa la kisiasa, kilitakiwa kuwa cha kwanza kuitetea serikali yake dhidi ya mashambulizi toka vyama vya upinzani badala ya kuiachia serikali kujitetea yenyewe kwa kutumia nguvu ya dola ya vitisho, mabavu, na propaganda za enzi za mfumo wa chama kimoja.

Tangu siku ya kikao cha kwanza cha bunge la sita, ambapo wabunge wa CHADEMA waliamua kutoka nje ya ukumbi wa bunge wakati ya hotuba ya Rais ya ufunguzi wa bunge kuthibitisha msimamo wao wa kutokubaliana na ujanja uliotumika katika kuhalalisha ushindi wa rais Kikwete, serikali na chama tawala viliingia katika majaribu makubwa ambayo bado hawajaonekana kuyashinda.

CHADEMA, kama chama cha upinzani chenye nia ya dhati ya kutwaa madaraka ya nchi kwa njia ya kidemokrasia, kilikuwa kimejipanga kuihenyesha serikali iliyoko madarakani tangu siku hiyo ya kwanza kazini.

Na kwa vile wengi wetu tulikuwa hatujawahi kuona siasa za upinzani wa kweli zinavyofanya kazi, tuliduwazwa na kitendo cha wabunge wa CHADEMA kuondoka bungeni kiasi cha kuingiwa na hofu kuwa serikali na chama tawala wasingekubali kurambwa chenga za maudhi katika dakika hizo za mwanzo kabisa za mchezo bila wao kujibu mapigo kwa pupa. Tulihisi kuundwa haraka kwa mkakati maalumu wa kuichezea CHADEMA rafu za kila aina ili wasizidi kuiadhiri serikali na chama chake kwa kutumia mbinu zao za siasa za kidot.com!

Na kama ilivyotarajiwa baada ya tukio hilo la kushtukiza bungeni, CCM walijipanga kuhakikisha CHADEMA inanyamazishwa kwa njia yoyote ile. Mbinu ya kwanza ilikuwa ya kutumia ‘vitisho’ kupitia katibu wa itikadi na uenezi wa wakati huo, yaani John Chiligati.

Kwa mtindo wa amri za kijeshi unaotokana na kazi yake ya zamani, Chiligati alitoa aliwaamuru wabunge wa CCM kuangalia uwezekano wa kupeleka azimio la ‘kuwafukuza’ bungeni wabunge wote wa CHADEMA kwa kitendo chao cha kumdalilisha Rais wa nchi.

Baadhi ya watu waliamini jambo hilo lingewezekana na kwa hiyo wabunge wa CHADEMA wangesimamishwa wasihudhurie vikao vya bunge. Lakini kwa wale wanaelewa demokrasia ya vyama vingi, na hasa inapotokea kuna chama makini cha upinzani kama CHADEMA inavyoinukia wakati huu, mbinu za CCM na serikali yake zilionekana za kizamani na hazikufua dafu mbele ya chama kinachoungwa mkono na nguvu kubwa ya umma uliochoshwa na ubabaishaji wa muda mrefu wa serikali ya CCM.

Mwisho wa siku wabunge wa CHADEMA hawakufukuzwa au kuzuiwa kuhudhuria vikao vya bunge, na kazi ya kuihenyesha serikali ndio kwanza ikashika kasi. Umaarufu wa CHADEMA kama chama chenye msimamo na kisichobabishwa ukazidi kuongezeka. Kwani kila aliyekuwa na hofu kwamba CHADEMA ingetishwa, ingeminywa, na hatimaye kufyata mkia, alishangaa kuona ujasiri mpya wa kidemokrasia ukiota mizizi nchini.

Vidonda vya maumivu ya ‘kuporwa’ matokeo ya urais waliokuwa nayo wananchi nchi nzima yalianza kupata ahueni ya ghafla. Matarajio ya CCM na serikali yake ya kujiendeshea mambo kama vile nchi hii ni mali ya kundi dogo la watu wanaojiona wenye bahati ya kipekee yalianza kutoweka ghafla. Hofu kuu ikaanza kuwaingia viongozi wa serikali na Chama tawala, na mkakati wa kuibinya CHADEMA ‘kwa nguvu zaidi’ ukapangwa.

Yaliyotokea kwenye maandamano ya Arusha ulikuwa ni ushahidi wa wazi wa kuwepo kwa mkakati maalum wa kuhakikisha CHADEMA haiendelei kuipigisha kwata serikali na kukifunika chama tawala, kama ilivyotokea katika awamu ya kwanza ya utawala wa Kikwete. Mabavu yaliyotumika kushambulia waandamanaji na hata kuzuia mkutano halali wa kisiasa, vikifuatiwa na propaganda za kufunika ukweli wa kilichotokea huko Arusha vilinikumbusha utawala wa kikomunisti wa Urusi ezi zile.

Ni mtindo huo huo uliotumiwa zamani na wakoloni kwa lengo la kuwadhibiti waafrika wasidai haki yao ya kuwa huru kwa njia ya maandamano na mikutano. Kwa wanaoelewa historia ya serikali zinazotumia udikteta wa kidemokrasia, ukatili wa askari wetu kule Arusha ulikuwa wa kisiasa zaidi badala ya mbinu za kawaida za kuthibiti fujo.

Linganisha matukio ya Arusha na maandamano yaliyofuatia kanda ya ziwa ambapo katika mikoa minne hakuna mtu hata mtu mmoja aliyeripotiwa kupoteza hata ‘kandambili’ kwa kukimbia kipigo cha askari! Kule Arusha askari ndio waliowashambulia wananchi wasiona na silaha wala nia ya kupambana na mtu yeyote. Watanzania hawana utamaduni wa kushambulia askari bila kuchokozwa.

Lengo la matumizi ya mabavu katika maandamano ya Arusha ilikuwa ni kutengeneza jukwaa la propaganda maalum ya kuuaminisha umma kwamba CHADEMA ni chama cha fujo, kinachochea vurugu na ni hatari kwa nchi. Hata hivyo pamoja na jitihada za serikali na CCM kuelekeza lawama kwa CHADEMA kama chanzo cha vurugu na mauaji huko Arusha, wananchi waliamua kuzipuuza propaganda hizo na kuzidi kuiunga mkono CHADEMA.

Kinyume na mipango na matarajioa ya CCM na serikali yake, tukio la Arusha liliamsha hasira ya wananchi nchini nzima dhidi ya uonevu, ukandamizaji na unyanyasaji wa serikali ya chama tawala ambao huko nyuma ulivumiliwa kwa maumivu ya kimya kimya. Hali ya uasi wa kimomoyo ikazidi kushamiri. Huruma kwa wahanga wa mauji ya Arusha ikaongeza hamu ya wananchi kutaka kuwaonesha hadharani nguvu walio nayo kupitia chama kinachotetea maslahi ya wanyonge walio wengi.

Kwa wepesi wao wa kuelewa mambo, CHADEMA wakaamua kukidhi kiu ya walio wengi. Wakaanzisha maandamano ya kupinga unyonyaji, unyanyasaji na dhuluma za wazi zinazofanywa na viongozi wa serikali na chama tawala.

Hata hivyo kabla CHADEMA hawajanza maandamano yao nchi nzima, CCM wakapanga mkakati mwingine wa kucheza rafu bungeni. Kwa kumtumia spika wa bunge, ambaye tangu kuchaguliwa kwake ilijulikana wazi jinsi ambavyo asingeweza kuvaa viatu vya mtangulizi wake, wabunge wa CCM waliamua kupindisha kwa makusudi kanuni za bunge ili kuizuia CHADEMA isiunde kambi rasmi ya upinzani, kama ilivyokuwa kwa CUF katika awamu mbili huko nyuma.

Mpango huu ulilenga kuzuia uwezo wa CHADEMA kuibua uoza ndani ya serikali kupitia kamati tatu za fedha wabungeni. Mkakati huu pia ulilenga kukigombanisha CHADEMA na vyama vingine vya upinzani ili kuwaaminisha wananchi kwamba CHADEMA wanapenda kujitega na ni chama chenye ubinafsi.

Kwa bahati mbaya mkakati huu ulifanikiwa kwa sehemu kubwa, na wananchi wakajionea wenyewe mchezo unaochezwa na CCM dhidi ya upinzani nchini. Vyama vya NCCR-Mageuzi, TLP, CUF, na UDP vilijikuta vikiungana na Chama tawala katika kuunda ‘kambi isiyo ramsi ya upinzani’ dhidi ya CHADEMA.

Na kwa mara ya kwanza katika historia ya mfumo wa vyama vingi nchini, chama tawala ‘kilivipiga busu’ vyama vidogo vya upinzani kwa lengo la kukishambulia chama kikuu cha upinzani! Siku hiyo CHADEMA kilionekana kama ndio chama tawala kwa jinsi kilivyovizidi umaarufu na mbinu vyama vingine vyote hata wakajikuta wanafunga ‘ndoa ya dharura’ (marriage of convenience) ili kukikabili.

Na tangu siku hiyo CCM na vyama vingine vimekuwa vikifanya kazi kama ndivyo vyama vya upinzani dhidi ya ‘chama tawala CHADEMA’. Lakini hata baada ya kuvipa ‘kumbato’ vyama vingine vya upinzani bungeni, serikali na CCM hawakujua kuwa bao jingine la kisigino lilikuwa linakuja muda si mrefu.

Maandamano ya kihistoria ya Mwanza yalipeleka msiba mwingine kwenye kambi ya CCM na serikali yake. Tofauti na matarajio ya wengi kwamba vurugu na kipigo cha Arusha vilikuwa fundisho tosha kuwatisha waandamanaji wengine kujitokeza kuwaunga mkono CHADEMA, maandamano ya Mwanza yalidhihirisha kile ambacho watawala wetu wamekuwa wakidhani hakipo yaani ujasiri wa watanzania kujitokeza hadharani na kuwaambia watawala ‘hatutaki kusukumwa’!

Watu wa Mwanza, ambao huko nyuma walionekana kama ‘wateja watiifu’ wa CCM, waliushangaza ulimwengu kwa kuonesha ujasiri ambao haujazoeleka hapa nchini. Damu ya mauaji ya Arusha ilikuwa imeanza kujenga taifa la wanaoweza kudai haki zao bila kutishwa na binadamu wenzao.

Kuanzia Mwanza, Mara, Shinyanga hadi Kagera, CHADEMA walibeba kilio cha wanyonge juu ya ugumu wa maisha, kupanda kwa bei za bidhaa kulikochochewa na kupanda kwa bei za umeme, na wakati huo huo kuwepo kwa mgao wa umeme nchi nzima.

CHADEMA iliwakumbusha wananchi juu ya ahadi walizopewa na viongozi wa CCM na jinsi ambavyo ahadi hizo zilikuwa hazitekelezwi kwa visingizio vile vile vya siku zote vya ‘kupanda kwa bei ya mafuta katika soko la dunia’ na ‘kuharibika kwa uchumi wa dunia’.

Kwa umahiri wao mkubwa katika kuwasilisha ujumbe, viongozi wa CHADEMA waliendelea kuushawishi umma kwamba serikali iliyopo madarakani haina uwezo wala nia ya dhati ya kutatua matatizo yao sugu bali ipo kwa ajili ya kuneemesha vigogo wachache na familia zao kwa njia za kifisadi kama vile ya Dowans, ambayo serikali ilikuwa tayari kuilipa mabilioni ya fadha za walipa kodi bila hata chembe ya woga wala aibu.

Kama chama cha siasa chenye kuzijua kanuni za mchezo wa siasa za kidemokrasia, CHADEMA waliishambulia serikali kiasi cha kuifanya ilazimike kutekeleza baadhi ya madai halali ya wananchi. Moja ya mambo ambayo serikali ilikubali kuyatekeleza baada ya shinizo la CHADEMA ni pamoja na kuwepo kwa mchakato wa kuandika upya katiba ya nchi, kitu ambacho CCM haikuwa tayari kukifanya na wala haikukiingiza katika ilani yake ya uchaguzi uliopita.

Jambo jingine lililotimizwa na serikali kwa shinikizo la maandamano ya CHADEMA ni amri ya Waziri Mkuu ya kuwataka wafanya biashara wa sukari nchini kushusha bei ya bidha hiyo toka shilingi 2000 hadi 1700. Suala hili lilitekelezwa muda wa saa chache tu baada ya CHADEMA kuanza kulitumia kama mfano wa bidhaa zinazozidisha ugumu wa maisha ya wananchi wa kawaida.

Baadaye tukasikia Rais, akiwa katika ziara ya kutembelea wizara ya nishati na madini, akiomba bei ya umeme ipunguzwe ili kupunguza makali ya maisha kwa wananchi. Yote haya yalikuja kutokana na shinikizo la chama kimoja cha upinzani kinachojua wajibu wake. Kweli CHADEMA waliipelekesha serikali utadhani wao ndio chama tawala!

Hata hivyo, wakati CHADEMA wakifanikiwa kuiadabisha serikali kiasi cha kuanza kutimiza matakwa ya wananchi, CCM waliamua kuja na rafu kali zaidi kuizuia CHADEMA isiendelee kuchukua nafasi yake. Safari hii Rais na mwenyekiti wa CCM aliingia ulingoni kuongeza nguvu za mapambano dhidi ya CHADEMA. Kupitia hotuba yake ya mwisho wa mwezi wa pili, Rais aliudhirishia umma wa Tanzania jinsi CHADEMA ilivyokuwa inaihenyesha serikali yake.

Mbali na kujikuta akijibu baadhi ya madai ya CHADEMA yaliyotakiwa kujibiwa ndani ya siku tisa, Rais alianzisha propoaganda mpya za kuishambulia CHADEMA kwa kulalamika kuwa ilikuwa ikiwachochea wananchi waanzishe vurugu za kuipindua serikali yake kwa njia ya maandamano. Wengi waliduwazwa na maneno hayo ya woga kutolewa na amiri jeshi mkuu wa nchi.

Hata hivyo baadhi yetu tuligundua mapema kuwa huu ulikuwa ni mkakati mwingine wa kuhakikisha CHADEMA inadhibitiwa. Mpango huu ulilenga mambo kadhaa. Kwanza kuwatisha tamaa wananchi ili wasizidi kuiunga mkono CHADEMA, kwa kuwaaminisha kuwa CHADEMA kilikuwa kinaandaa maasi nchini, kitu ambacho serikali ingekuja kukizima kwa nguvu ya dola na kusababisha wananchi wengi kuumia vibaya.

Pili, kuharibu taswila CHADEMA kwa kukionesha kuwa ni chama cha vurugu na viongozi wake washari wanaopenda madaraka kwa gharama yoyote.

Tatu, kuwapa makada wa CCM na baadhi ya viongozi wa serikali, hasa mawaziri, kitu cha kufanyia propaganda nchi nzima kwa lengo la kuuaminisha umma kwamba mandamano ya CHADEMA hayana lengo zuri la kisiasa hivyo wananchi wasiyaunge mkono na ikishindikana nguvu zitumike kuyadhibiti, ikiwa pamoja na viongozi wake kupigwa, kuumizwa, au hata kuundiwa mashitaka ya uongo kwa kisingizio kwamba ‘serikali ililazimika kuchukua hatua za ziada kuepusha umwagaji damu nchini’.

Sote tunakumbuka kilichotokea baada ya hotuba ya Rais. Waliokuwa wametayarishwa katika mkakati huu walianza kujitokeza.

Kwanza tulimskia waziri wa nchi mahusiano, Stephen Wassira, kama kawaida yake, akitumia lugha za kibabe kuwatisha CHADEMA eti ‘wasije kuilaumu serikali’ kwa kutumia nguvu kuwashughulikia kama hawataacha uchochezi kwenye mikutano yao.

Kisha tukamsikia msajiri wa vyama vya siasa bwana John Tendwa akiwaandikia CHADEMA barua ya kuwaonya wasitumie ‘lugha za matusi’ katika mikutano yao vinginevyo angekifutia chama usajiri wa kudumu. Baadaye wakafuata kina Anna Kilango Malecela na viongozi wengine wa aina hiyo, kabla Sophia Simba na Bernard Membe hawajaja na mpya kwa kudai kuwa maandamano ya CHADEMA yalikuwa yanafadhiliwa na mataifa ya nje kupitia balozi zake hapa nchini. Kana kwamba haitoshi, tukasikia vijana wa Dar es Salaam wameandaa maandamano kupinga maandamano ya CHADEMA.

Nasikia maandamano haya ya vijana yalizuiwa na polisi kwa kisingizio cha kuleta usumbufu kwa wakazi wa jiji. Taarifa zilizoko ni kwamba mpango huu wa maandamano ya vijana ulipangwa ili polisi wawanyime kibali cha maandamano kwa lengo la kuandaa mazingira ya kuja kuwanyima CHADEMA kibali cha maandamano watakapotaka kuandamana popote Dar es Salaam. Tunasubiri kujionea.

Baada ya kiini macho cha maandamano ya vijana wa Dar es Salaam, yalifuatia maandamano ya kina mama kupinga maandamano ya CHADEMA, ambayo pia hayakuleta mvuto wowote. Baadaye tukasikia mpango wa maandamano ya vyama vyote vidogo vya siasa nchini kupinga maandamano ya CHADEMA, kabla hajatokea Profesa Lipumba huko Tanga na kuwashangaza wengi kwa kuishambulia CHADEMA kwa namna ambayo iliwadhihirishia wengi kwamba kweli sasa CUF ilikuwa imeungana rasmi na CCM kikishambulia CHADEMA.

Hapa ndipo nilipoamini bila shaka yoyote kwamba kwa sasa, CHADEMA ndio chama tawala, ambacho hakikupewa tu nafasi ya kuunda serikali kutokana na kuibiwa matokeao ya uchaguzi mkuu. Itakuwaje serikali na vyama karibia vyote vya siasa vijikute vikiungana katika kuishutumu, kuibeza au kuishambulia CHADEMA kana kwamba ndio chama tawala?

Ndio maana wananchi wameamua kuweka pamba masikioni na kuwapuuza wale wote wanaojaribu kuihujumu CHADEMA. Tangu Rais alipotumia muda wake mwingi wa hotuba kuishambulia CHADEMA ikifuatiwa na maandamano-maigizo na vitisho vyote vya kuishughulikia CHADEMA, wananchi wamezidi kuelekeza mioyo yao kwa CHADEMA huku wakiiona CCM na serikali yake kama wasaliti.

Iweje chama ambacho hakina serikali, hakina idadi kubwa ya wabunge, na hakina pesa kama CCM, kitese akili za viongozi wa nchi kwa kiasi hiki? Kwa nini chama kinachounda serikali kiungane na vyama vingine vyote nchini kukishambulia chama kimoja tu cha upinzani utadhani ndio chenye serikali iliyoko madarani?

Kwa nini serikali ihangaike kuandaa watu, vikundi, na hata dola kushughulikia namana ya kuzima harakati halali za kisiasa za chama kimoja tu cha upinzani nchini? Nadhani haya yote yanatokea kwa sababu moja tu, kwamba katika mioyo ya watu wengi, CHADEMA kwa sasa ndio chama tawala japo hakiongozi toka ikulu. Ukweli ndio huo.


My Take:This is true History
Thanks Martin Kaswahili.
GOOD ANALYSIS.
 
Huo ndo ukweli anayepinga ni mwenye mtindio wa ubongo na hakuhitaji kuwa na elimu kubwa kubainisha ukweli na uongo wote ni mashuhuda wa hayo.
 
yani sangara hujaelewa chochote hapo. basi wewe una tofauti na wavua gamba labda na wewe hujalivua hebu vua gamba unaweza ukaelewa japo kidogo
 
asee ungeacha nafasi kati ya paragraph moja na nyingine atleast maelezo yako yavutie kusoma.
 
ndio nini hii...pumba za leo

Ni hivi ndugu Sangara, wakati wa Campaign CDM walisema wataanzisha MCHAKATO wa katiba mpya ndani ya siku 100(apporx 3 months) na pia wangewashuglikia mafisadi. CCM on the other hand hawakuwa na andiko linalogusia katiba mpya kwenye manifesto yao! plus hata neno UFISADI wengi wao walisema hawajui maana yake (Makinda, 2010). Fast foward, Jan 2011, less than miezi mitatu baada ya uchaguzi CCM kupitia mwenyekiti wao walitangaza kuwa mchakato wa Ku-ihuisha katiba utaanza ili kupata katiba inayoendana na Taifa lenye umri wa miaka 50 (Mh. Kikwete, salamu za mwaka mpya 2011). Na sasa CCM is heavily involved kwenye theotrical ya uvuaji magamba lengo likiwa ni kuondoa ufisadi. Kumbuka agenda zote mbili zilikuwa kwenye manifesto ya CDM na sio CCM. Hata baada ya CCM kudandia agenda ya CDM na kuupeleka mswada wa katiba bungeni lakini CDM wamegundua mapungufu mengi sana na kuukata. Guess what? Serikali ya CCM had no option but to withdrawal it. Now, ni nani hasa anaogoza hii nchi???

Hata hivyo wakati CCM wanapitia-pitia manifesto ya CDM ili kujua nini chan kufanya, wanatakiwa wakumbuke ahadi ya 'Maisha bora kwa kila mtanzania' pamoja na manjonjo haya hapa chini;

1.Kujenga reli mpya kutoka Dar es Salaam mpaka mikoa ya Kanda ya ziwa - Nzega, Tabora
2.Mkoa wa Tanga kuwa Jiji la Viwanda - Tanga mjini
3.Tabora kutumia maji ya Ziwa Victoria - Igunga
4.Kulipa madeni ya chama cha Ushirika mkoa wa Shinyanga (SHIRECU) - Shinyanga
5.Kumaliza migogoro ya Ardhi nchini - Dodoma
6.Wakulima kuacha kutumia jembe la mkono - Dodoma mjini
7.Kuwapatia trekta wakulima - Kata ya Mrijo, Dodoma
8.Wananchi kutoondolewa kwenye Ranchi ya Misenyi - Kagera
9.Kujenga Uwanja wa Ndege Misenyi - Kagera
10.Kupanua Uwanja wa Ndege Bukoba - Bukoba Mjini
11.Kujenga uwanja wa ndege mkubwa Kigoma - Kigoma Mjini
12.Mtukula kupatiwa umeme kutoka Uganda - Kagera
13.Mikoa ya Kagera, Kigoma, Lindi, Rukwa na Ruvuma kuunganishwa katika gridi ya taifa ya umeme - Kagera
14.Kuimarisha Takukuru kwa miaka mitatu - Kagera
15.Hukumu kwa waliopatikana na hati ya kuua albino - Mbeya
16.Kununua meli kubwa kuliko MV Bukoba - Kagera
17.Kuanzisha benki ndogondogo kwa ajili ya wajasiriamali
18.Serikali kuvisaidia vyama vya ushirika - Mwanza
19.Kuimarisha usalama Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika kwa kupeleka kikosi maalum chenye vifaa kupambana na wahalifu - Mwanza
20.Wilaya ya Geita kuwa hadhi ya mkoa Januari mwakani - Geita
21.Kulinda muungano kwa nguvu zote - Pemba
22.Kuwajengea nyumba waathirika wa mafuriko Kilosa - Morogoro
23.Kununua meli mpya kubwa Ziwa Nyasa - Mbeya mjini
24.Kujenga bandari Kasanga – Rukwa
25.Kumaliza tatizo la walimu miaka mitano ijayo - Songea
26.Kufufua mgodi wa makaa ya mawe Kiwira - Mbeya
27.Kuzuia hatari ya kisiwa cha Pangani kuzama - Tanga
28.Kununua bajaji 400 kwa ajili ya kubeba wajawazito hasa vijijini - Iringa
29.Kujenga barabara yenye kiwango cha lami kutoka Same mpaka Kisiwani – Kihurio na kuiunganisha na barabara kuu ya Moshi - Dar es salaam - Same mkoani Kilimanjaro
30.Kumaliza tatizo la maji katika wilaya ya Same - Same Mjini
31.Kuboresha barabara za Igunga - Tabora
32.Kusambaza walimu 16,000 katika shule za sekondari zenye upungufu makubwa wa walimu - Kisesa Magu
33.Kununua vyandarua viwili kwa kila kaya - Mbeya Mjini
34.Kuzipandisha hadhi hospitali maalumu saba nchini kuwa za rufaa ili kuipunguzia mzigo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MHN) - Hydom Manyara
35.Kulinda amani nchini kwa kuzuia chokochoko za kidini, kikabila na kisiasa - Musoma
36.Kulinda haki za walemavu - Makete
37.Kujenga baabara ya Njombe - Makete kwa kiwango cha lami,urefu wa kilomita 109 - Iringa mjini
38.Kujenga barabara Musoma – Mto wa Mbu Arusha - Arusha
39.Kuanzisha jimbo la Ulyankulu- Shinyanga Mjini
40.Kujenga barabara ya lami Manyoni-Kigoma – Kaliua,Tabora
41.Kukarabati barabara ya Arusha Moshi - Arusha Mjini
42.Kuboresha barabara ya Handeni, Kondoa, mpaka Singida - Dodoma
43.Kuwafidia wanakijiji ng'ombe waliopotea wakati wa ukame mwaka 2009 - Longido
44.Vijiji vyote vilivyoko kilomita 15 kutoka kwenye bomba kuu la mradi mkuu wa maji wa Ziwa Victoria - Shinyanga-Kahama kuunganishiwa maji - Shinyanga
45.Tatizo la umeme kufikia kikomo Novemba mwaka huu mkoani Arusha – Arusha mjini
46.Kukopesha wavuvi zana za kilimo - Busekera, Wilaya ya Musoma
47.Kuwapatia maji wakazi wa Wilaya ya Longido - Longido
48.Kujenga barabara ya lami kupitia pembezoni mwa Hifadhi ya Taifa ya Seregenti – Ngorongoro
49.Utekelezaji wa mpango wa maendeleo ya kilimo kuwasaidia wafugaji kuweza kupata na kutunza mifugo yao vizuri - Mbulu mkoani Manyara
50.Kusambaza maji nchi nzima - Babati vijijini
51.Kusambaza umeme, utoaji wa huduma za afya, na uboreshaji wa kilimo cha umwagiliaji na utoaji ruzuku kwa wakulima. mwaka 2010-2015 - Babati vijijini
52.Kuongeza mara tatu idadi ya wananchi wanaonufaika na ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa mfumo wa vocha - Iringa
53.Kuhakikisha Isimani inapata maji ya uhakika - Iringa
54.Kuiwekea lami barabara inayokwenda katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, ambayo ndiyo hifadhi kubwa kuliko zote Tanzania - Iringa
55.Kulinda usalama wa wananchi kwa ujumla ili kudumisha amani na sifa ya nchi -Ifunda
56.Kutokomeza malaria 2015 - Bunda, mkoa wa Mara
57.Kuwapa wanawake nafasi zaidi - Kilolo, Iringa
58.Ahadi kuisadia Zanzibar kuendeleza miradi mbalimbali ya kijamii - Kibandamaiti Mjini Zanzibar
59.Kuipandisha hadhi hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar kuwa ya rufaa - Kibandamaiti mjini Zanzibar
60.Kuisaidia Zanzibar kila panapohitajika msaada - Kibandamaiti
61.Serikali kujenga upya bandari ya Mbambabay - Ruvuma
62.Ununuzi wa Meli mpya yenye uwezo wa kubeba tani 400 - Mbambabay Ruvuma
63.kufufua chama kikuu cha ushirika cha wakulima wa Mbinga (MBICU) – Ruvuma
64.Ahadi Rais wa Marekani Barack Obama kuimwagia misaada Tanzania – Ruvuma
65.Ahadi hakutakuwa na umwagaji wa damu baada ya uchaguzi-Dar es Salaam
66.Mtwara kuwa mji wa Viwanda – Mtwara
67.Ahadi ujenzi wa kwanda cha dawa ya kuua viluilui vya mbu - Kibaha
68.Hospitali ya Tumbi kuwa ya mkoa - Kibaha
69.Halmashauri ya manispaa ya Kibaha kutenga eneo maalumu la viwanda - Kibaha
 
ndio nini hii...pumba za leo
Basi bana kama utakuwa huelewi kuwa CDM ndio wanaongoza nje ya Ikulu basi utakuwa kwenye profile ya chini sana.
Kwa taarifa yako Mh Raisi wa Shirikisho Tanzania Jakaya Kikwete anamtambua Rais wa Tanganyika iliyo huru Mh Dr Willbroad Peter Slaa.
Hii inatokana na matamko yake kufanyiwa kazi kwa ARI,NGUVU NA KASI MPYA.kwa ssm kujivua gamba bila kutoa sumu iliyoko mwilini ambayo itaendelea kuitafuna,kuwapaka watakaoingia mifano ni kama wakina Nape Mnauye wameshaanza kuonja sumu ya nyoka aliyejivua gamba.wamebaki wakiropoka tuu majukwaani maskini hawajui wanalofanya mpaka sasa.
 
Back
Top Bottom