MAMBO MATANO MUHIMU KWA CHADEMA.
Kwa sasa Chadema ndicho chama kikuu cha upinzani Tanzania,ambacho kinawanyima usingizi vigogo wa CCM ambao wako kwenye fungate la kufurahia uhuru wa Tanzania.Mara nyingi tumezoea,vyama vya upinzani kuilalamikia CCM kwenye mambo kadhaa,lakini sasa kibao kimegeuka.Wenye dola ndio walalamishi,na kutwa kuishambulia Chadema as if CDM ndio Chama Tawala.Kifupi CCM imechoka,imevubaa na imesinyaa.Kuendelea kuwapa kinachoitwa kura kama sio kula CCM ni kuendelea kuchimba kaburi la mauti.
Kuna msemo wa Waliopo hatuwataki,na wanaotaka hatuwaamini.Je,unaamini Chadema wanaweza kuziba pengo la marehemu mtarajiwa CCM?Kwa jibu lolote utakalotoa,Chadema kama kweli inataka kushika dola kwa masilahi ya Watanzania wanahitaji kujirekebisha,na kuonyesha utofauti wao na marehemu mtarajiwa,mheshimiwa CCM.
Mezani kwangu hapa nina mambo matano ya kuwashauri CHADEMA.Mambo hayo ni kama ifuatavyo;
1. Chadema achaneni na Dr.Slaa,jengeni chama.
Dr.Slaa ni moja kati ya watu muhimu sana katika Chadema na Taifa kwa ujumla.Tangu Dr.Slaa awe mbunge (1995) ameonyesha utendaji makini na kuweka masilahi ya Taifa mbele.Hata alipoteuliwa na Chadema kuwa mgombea Urais 2010 sikushangazwa.Pamoja kwamba alishindwa kwa goli la mkono la CCM lakini ni wazi kwamba alionyesha ushindani mkubwa JK.
Inasemekana Dr.Slaa hakutaka kugombea urais na badala yake alitaka kuendelea na ubunge.Ushawishi wa Kamati Kuu ya Chadema ulifanya Dr.Slaa kukubaliana na ombi hilo ila kwa masharti.Kwamba ikitokea kushindwa kwenye urais,basi alipwe mshahara kama wa mbunge.Chama kilikubaliana na masharti hayo,na mambo yanaendelea.
HOJA YANGU: Chadema inawekeza zaidi kwa Dr.Slaa kuliko wanachama (wapiga kura)
Umaarufu na nguvu alizonazo Dr.Slaa ndani ya Chadema unaweza kukiangamiza chama kuliko kukisaidia.Kwa jinsi nionavyo ni kwamba Dr.Slaa yuko juu ya Chadema,kitu ambacho ni hatari sana.Chama kinajaribu kwa kina namna kumbembeleza na kusahau wapiga kura.Lazima Chadema watafute balance ya chama.Wakati Dr.Slaa analipwa pesa nyingi chini ya makubaliano maalum,ofisi za mikoani,wilayani na vijijini ziko hoi.
Dr.Slaa ni mtu muhimu sana ndani ya Chadema na Taifa,lakini hawezi kuwa juu ya Chama.Chama kiwekeze kwa wanachama kwa kutumia rasilimali fedha kidogo walizonazo.
2. Fedha za Ruzuku.
Hoja hii inafanana kiasi na hiyo hapo juu.Hili ni suala muhimu sana likazingatiwa na Chadema.Kumekuwepo na madai mengi,kwamba ruzuku inatumiwa vibaya.Sijui ukweli ukoje,ila mimi ningewashauri kuelekeza ruzuku wanazozipata huko matawini.Inawezekana wanafanya hivyo,lakini impact yake haiendani na hali halisi.Ofisi za mkoa na wilayani ziko hoi.
Muda wa kujenga chama ni huu,wasisubiri wakati wa uchaguzi.Kuna watu wengi sana wako tayari kusaidia harakati bila malipo,lakini ni vema chama kikatambua na angalau kuwawezesha vitendea kazi.Support wanayopata chadema (hata ukiangalia chaguzi ndogo zilizopita) ni ndogo sana ukilinganisha na mwamko wa wananchi.
3.DECENTRALIZATION.
Chadema wana sera ya majimbo,sasa ingekuwa vema wangeanza kuifanyia kazi ndani ya chama ili iwe mfano.Hapa juzi walichagua viongozi wa kuongoza kanda,Sawa,lakini suala hili linatakiwa la kiutendaji zaidi.Wananchi/wanachama wapewe mamlaka/madaraka ya kujiamulia mambo yao (kwa kufuata katiba).Hili suala la hata jambo dogo kuamuliwa makao makuu sio jema,lina harufu ya udikteta na linazua malalamiko mengi.Chadema ijenge chama kwa kuwawezesha wanachama wao kuelewa katiba na miongozo mingine ya chama,ili waendeleze harakati mahala walipo,tofauti na hivi sasa ambapo kila kitu kinahitaji kufanyiwa kazi makao makuu.
4. WABUNGE WA CHADEMA.
Kwa bahati nzuri sana,CDM ina wabunge ambao bongo zao zinafanya kazi.Licha ya kwamba ni wachache bungeni,sauti zao zinasikika zaidi.Sasa ni vema wakatumia nafasi hiyo kuwatetea wananchi.Suala la kususia vikao,sasa waachane nalo.Wapaze sauti na kujenga hoja kistaarabu kila wapatapo nafasi.Hata kama mawazo yao yatapuzwa,lakini wananchi wanajua nani nani anawatetea.Wapunguze jazba licha ya kwamba uongozi wa bunge unaonyesha wazi kupendelea Chama Tawala/Serikali.
Pia ni vema wakayatendea haki majimbo yao.Wahakikishe wanafanya kila linalowezekana kutatua kero za wananchi.Wafanye majimbo yao yawe mfano wa kuigwa ili 2015 iwe rahisi zaidi na kuongeza idadi ya viti vya ubunge.Watambue kwamba wananchi wao ndio maboss wao,wajue kujishusha na kuwa na karibu na wananchi wa kawaida.Ukichaguliwa kuwa mbunge,haina maana kwamba una akili zaidi kuzidi wapiga kura.
5.MIKUTANO YA HADHARA.
Mikutano ya hadhara ni muhimu sana kwa uhai wa chama chochote cha siasa.Chadema wamekuwa wakifanya mikutano ya hadhara kila inapowezekana.Kwa mfano Operation Sangara ilifanikiwa sana kwa kuwaamsha watanzania wengi waliolala.
Chadema inafanya mikutano ya hadhara katika mazingira magumu sana na ya hatari,kwa sababu CCM wanatumia kila mbinu kukwamisha.Na hivi karibuni tumeshuhudia machafuko (mauaji) katika mikutano ya Chadema.Machafuko haya yanasababishwa na polisi ambao wamepewa jukumu jipya (tofauti na tunalolifahamu) la kuiharibia Chadema.
Sijajua Plan B ya Chadema.Lakini hali hii kiendelea hivi,na kama hakutakuwa na makubaliano (Pinda anasema wapigwe tu),ili kuepusha maafa zaidi kwa wanachama wao,watanzania wenzetu,hebu wajaribu kubadilisha mbinu.Mikutano ya hadhara ambayo haina ulazima wa kuwepo Viongozi wakuu wa chama waachane nayo.
Sasa waanze kampeni ya nyumba kwa nyumba,mtaa kwa mtaa,mtu kwa mtu.Na kazi hii inatakiwa kufanyika na viongozi wa vijiji,kata,wilaya n.k.Kitu cha msingi wawawezeshe.Mikutano mikubwa ifanyike pale panapokuwa na ulazima.