Bonde la kukata maneno

nebuchadnezzer

JF-Expert Member
May 10, 2013
245
341

Bonde la kukata maneno ni nini?​


Yoeli 3:14 “Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno! Kwa maana siku ya Bwana i karibu, katika bonde la kukata maneno.
15 Jua na mwezi vimetiwa giza, na nyota zimeacha kuangaza.
16 Naye Bwana atanguruma toka Sayuni, atatoa sauti yake toka Yerusalemu; na mbingu na nchi zitatetemeka; lakini Bwana atakuwa kimbilio la watu wake, na ngome ya wana wa Israeli”.
Biblia inatuambia kuna wakati unafika hapa mbele yetu ambao Mungu atayaleta mataifa yote katika bonde lijulikanalo kama bonde la kukata maneno, biblia imeliita pia kama Bonde la Yehoshafau ukisoma kuanzia mstari wa 12. Yehoshafua maana yake ni YEHOVA-ANAHUKUMU..Hivyo bonde hilo litakuwa ni bonde la Yehova kuya hukumu mataifa yote..

Unaweza ukajiuliza ni kwanini pia limeitwa bonde la kukata maneno.. Kwa lugha rahisi kukata maneno ni sawa na kusema kumaliza hoja, au malumbano,.. kwamfano mahali ambapo, pana malalamiko mengi labda tuseme katika Taifa fulani wananchi wake wanalamika kila siku miundo mbinu ni mibovu,..

wanashindwa kufanya shughuli zao za kimaendeleo, wanashindwa kusafiri, wanashindwa kwenda mashambani n.k.

sasa kama serikali italiona hilo na kuacha kuchukua hatua watu wake wataendelea kulalamika hivyo hivyo hata kwa karne na karne,.. sasa ili kukata maneno hayo, viongozi huwa wanachukua uamuzi wa lazima na wa haraka, aidha watalazimika kwenda kukopa pesa ili watimizie wananchi matakwa yao au watatoa katika bajeti yao wahakikishe tu kuwa jambo hilo linafanyika haraka sana ili kukata maneno ya wananchi yasiendelee kuwasumbua..hivyo Kukata maneno ni kutoa suluhisho. (kwa kiingereza linaitwa Valley of decision).

Vivyo hivyo na kwa Mungu pia, leo hii yapo makundi makuu mawili ya watu yanayomlilia na kumpelekea tuhuma zao kila kila siku kundi la Kwanza ni lile linalomlilia Mungu na kumwambia ni lini Bwana utakomesha uovu juu ya nchi ili maasi yasiendelee?.

Ni lini utatulipizia kisasi juu ya maadui zetu na maadui zako? Ni lini ufalme wako utakuja duniani?…Ni lini Bwana…?

Ufunuo 6:9 “Na alipoifungua muhuri ya tano, nikaona chini ya madhabahu roho zao waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu, na kwa ajili ya ushuhuda waliokuwa nao.
10 Wakalia kwa sauti kuu, wakisema, Ee Mola, Mtakatifu, Mwenye kweli, hata lini kutokuhukumu, wala kuipatia haki damu yetu kwa hao wakaao juu ya nchi?
11 Nao wakapewa kila mmoja nguo ndefu, nyeupe, wakaambiwa wastarehe bado muda mchache, hata itakapotimia hesabu ya wajoli wao na ndugu zao, watakaouawa vile vile kama wao”.
Na kundi la pili ni lile linalodhihaki, na kusema, huyo Yesu mnayemngojea mbona harudi amekufa?., kundi linalolikufuru jina la Mungu bila hofu yoyote, kundi linalojiamulia kufanya maovu tu bila kujali kuwa yupo Mungu juu, kundi linalosema hakuna Mungu,.. kama yupo basi ajitokeze tumwone, akisimama hapo na kushusha moto mbinguni, ndipo tutamsujudia..mbona anajificha, anajifichia nini ikiwa yeye ni Mungu n.k..

Umeona? Makundi yote haya yanapeleka malalamiko yao..Sasa Bwana ameiandaa siku ambayo ATAKATA MANENO HAYA YOTE..Siku hiyo ndugu usitamani uwepo..Kwasababu kabla hajatenda tendo lolote atahakikisha kwanza mataifa yote yamekusanyika pamoja, kisha atayafanya yaelekeze uso wao pale Israeli.. na uwanja wa mapambano utakuwa katika lile bonde la Yehoshefau au bonde la kukata maneno..

Sasa wakati wameshajiweka tayari kwa vita biblia inatuambia ghafla, jua na mwezi vitatiwa giza, yaani kwa wale ambao watakuwa upande wa mchana kipindi hicho watalishuhudia jua likizama saa 7 mchana, na kuwa giza tororo duniani kote,. wala hata mwezi nao hautaonekana, wala hizi nyota, wala tochi, wala taa za barabarani haziwaka..duniani kote hakutakuwa na chanzo chochote cha mwanga kwa ufupi.

Amosi 8:9 “Tena itakuwa siku hiyo, asema Bwana MUNGU, nitalifanya jua litue wakati wa adhuhuri, nami nitaitia nchi giza wakati wa nuru ya mchana”.
Kipindi hicho dunia itakuwa imeshaingiwa na hofu, wakiomboleza ni nini hiki kimetokea hapo ndipo wakatakapomwona Kristo akishuka na wingu kutoka juu pamoja na majeshi ya mbinguni..(watakatifu waliokuwa wamenyakuliwa), hapo ndipo Bwana atawaua kwa upanga utokao katika kinywa chake,.

Ufunuo 19:11 “Kisha nikaziona mbingu zimefunuka, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita.
12 Na macho yake yalikuwa kama mwali wa moto, na juu ya kichwa chake vilemba vingi; naye ana jina lililoandikwa, asilolijua mtu ila yeye mwenyewe.
13 Naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa, Neno la Mungu.
14 Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi.
15 Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.
16 Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA Bwana WA MABwana.
17 Kisha nikaona malaika mmoja amesimama katika jua; akalia kwa sauti kuu, akiwaambia ndege wote warukao katikati ya mbingu, Njoni mkutane kwa karamu ya Mungu iliyo kuu;
18 mpate kula nyama ya wafalme, na nyama ya majemadari, na nyama ya watu hodari, na nyama ya farasi na ya watu wawapandao, na nyama ya watu wote, waungwana kwa watumwa, wadogo kwa wakubwa.
19 Kisha nikamwona huyo mnyama, na wafalme wa nchi, na majeshi yao, wamekutana kufanya vita na yeye aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake”.
Katika kipindi hichi baada ya Kristo kuwaangamiza wale wote waliokuja kufanya vita kinyume chake ambao watakuwa ni mamilioni kwa mamilioni, hatua inayofuata ataketi na kuwahukumu wale waliosalia,.. huo ndio ule wakati wa kutenganishwa kondoo na mbuzi, mbuzi watatupwa katika lile ziwa la moto..Na hao wengine watapata neema ya kuingia katika ule utawala wa miaka 1000. Na kipindi hicho sio kwamba watu watakuwa ni wengi duniani hapana, biblia inasema watu wataadimika kuliko Dhahabu, (Soma Isaya 13:12), hivyo pengine ni watu 100 kati ya bilioni 7 waliopo duniani leo watakaosalimika, kama vile ilivyokuwa katika siku za Nuhu ilikuwa ni watu 7 kati ya mabilioni..Mungu hana wengi wape,..haangalii wingi wa watu wasiomwamini kama kigezo cha kuturehemu.

Na wakati huo sasa ndio Kristo atakapoitengeza tena hii dunia ndipo atakapotawala kama mfalme wa wafalme duniani, pamoja na wale watakatifu waliokwenda naye kwenye unyakuo na kurudi naye na wayahudi waliokuwa wamefichwa..Hao pekee ndio watakaofanana na malaika, watakaokuwa na miili ya umilele, lakini wengine watazaliana na kuongezeka mpaka mwisho wa ule utawala wa miaka 1000 utakapofika..

Hivyo unaweza ukaona ni jinsi gani hii dunia inavyoelekea pabaya, mambo hayo usidhani yatakuja kutokea miaka 800 mbeleni, tunaweza kuyashuhudia katika kizazi chetu hichi,.. kwani mataifa mengi tayari yameshaelekeza silaha zao Israeli kwa lengo la kuliondoa katika uso wa dunia unadhani ni kitu gani kimesalia..

Bonde la kukata maneno!! Lisiwe sehemu ya maisha yako.Mkaribishe Kristo maishani mwako leo ili akufanye kuwa kiumbe kipya, na kukuepusha na hukumu inayokuja..

Bwana akubariki.

www.wingulamashahidi.org
Whatsapp: +255693036618
 
Back
Top Bottom