Kikwete kuzindua mradi gesi kesho
Na Mwandishi wetu
7th November 2012
Rais Jakaya Kikwete kesho anatarajiwa kuzindua mradi wa ujenzi wa mitambo ya kusafisha gesi asilia kutoka Mtwara na Songosongo na bomba la mafuta la kusafirisha gesi hiyo hadi jijini Dar es Salaam.
Uzinduzi huo utafanyika katika eneo la Kinyerezi Ulongoni, Manispaa ya Kinondoni, mahali ambapo mitambo na bomba hilo vinatarajiwa kujengwa.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasili katika eneo hilo ikiwa ni ziara yake kwa ajili ya kuweka sawa mazingira ya uzinduzi huo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki, akiambatana na menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), na wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, alisema ameridhika na maandalizi hayo na kwamba hakuna sababu ya kufanya uzinduzi huo usifanyike.
Sadiki pia aliwataka wananchi na wakazi wanaoishi kuzunguka eneo hilo kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya uzinduzi huo baada ya Rais kuwasili eneo hilo saa 3: 00 asubuhi.
Kamishna wa Nishati na Petroli, Mhandisi Hosea Mbise, alisema kuwa jumla ya mitambo minne yenye uwezo wa kuzalisha Megawati 840 inatarajiwa kujengwa katika eneo hilo kwa mgawanyiko wa maeneo manne ikitokea Mnazi Bay, Somanga Funga na kukutana Songosongo hadi Kinyerezi na kusafirishwa hadi Tegeta kupitia Ubungo jijini Dar es Salaam.
Mbese aliitaja migawanyiko ya maeneo hayo kuwa ni Kinyerezi ambako mitambo yenye uwezo wa kuzalisha Megawati 150 inatarajiwa kujengwa, Kinyerezi II mitambo ya Megawati 240, Kinyerezi III mitambo ya Megawati 300 wakati mitambo ya Megawati 150 itajengwa katika eneo la Kinyerezi 1V.
Kwa mujibu wa Joyce Kisemo, Mkurugenzi Masoko na Vitega Uchumi TPDC, Joyce Kisemo, mradi huo ulianza mwaka mmoja na nusu uliopita na kutarajiwa kukamilika Januari mwakani kwa gharama za Dola za Kimarekani bilioni 1.225 ambazo ni mkopo nafuu kutoka Serikali ya Watu wa China.
Halafu ni. watu wangapi wanauwezo wa kuvuta gesi majumbani mwao?Kama maji Dar ni shida sembuse gesi?
Huu ni mpango tu wa wakubwa.