Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,125
Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkulo
Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkulo amemaliza kusoma bajeti ya serikali ya TSh 9.5 trilioni. Muhtasari wa bajeti hiyo na Picha kibao kwa yaliyojiri kwenye kikao hicho cha bajeti shuka mwisho wa habari hii. Kwa kiwango kikubwa bajeti iliyosomwa leo ilichambuliwa jana na Rais Jakaya Kikwete, hasa katika eneo la kupambana na msukosuko wa uchumi. Kipya alichoeleza ni jinsi ya kupata ongezeko la bajeti kutoka 7.2 trilioni za mwaka 2008/09.
Sehemu ya bajeti
Mheshimiwa Spika, kutokana na maelezo niliyoyatoa hapo juu, Bajeti ya mwaka 2009/10 imezingatia mikakati ya kitaifa inayolenga kuchangia katika kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania. Mchanganuo wa Bajeti kwa baadhi ya sekta ukijumuisha mishahara ya watumishi wa umma kwa mwaka 2009/10 ni kama ifuatavyo:
(i) Elimu imetengewa shilingi bilioni 1,743.9 ikilinganishwa na shilingi bilioni 1,430.4 kwa mwaka 2008/09, sawa na ongezeko la asilimia 22. Sekta hii bado inaendelea kuchukua sehemu kubwa ya Bajeti kutokana na umuhimu wake.
(ii) Kilimo kimetengewa kiasi cha shilingi bilioni 666.9 ikilinganishwa na shilingi bilioni 513.0 za mwaka 2008/09 pamoja na fedha za marejesho za EPA, sawa na ongezeko la asilimia 30. Aidha, serikali inadhamini mikopo ya Benki kwa sekta ya kilimo kupitia vyama vya ushirika na makampuni ya watu binafsi kwa mazao mbalimbali.
(iii) Miundombinu imetengewa jumla ya shilingi bilioni 1,096.6 ikilinganishwa na shilingi bilioni 973.3 mwaka 2008/09, sawa na ongezeko la asilimia 12.7;
(iv) Afya imetengewa shilingi bilioni 963.0 ikilinganishwa na shilingi bilioni 910.8 mwaka 2008/09, sawa na ongezeko la asilimia 5.7;
(v) Maji imetengewa shilingi bilioni 347.3 ikilinganishwa na shilingi bilioni 231.6 zilizotengwa mwaka 2008/09 sawa na ongezeko la asilimia 50; na
(vi) Nishati na madini imetengewa shilingi bilioni 285.5 ikilinganishwa na shilingi bilioni 378.8 zilizotengwa mwaka 2008/09, sawa na upungufu wa asilimia 24.6 Hali hii imesababishwa na kumalizika mikataba ya kuzalisha umeme kwa makampuni ya kukodi ya Dowans, APR na Aggreko. Hatua nyingine zinachukuliwa katika mwaka 2009/10 kutafuta mikopo kutoka mashirika ya kimataifa na nchi marafiki ili kuweza kupata rasilimali zaidi za kufanikisha miradi ya nishati nchini. Nchi na mashirika ya fedha ya kimataifa yameonesha nia ya kutusaidia zikiwemo Korea ya Kusini, Saudi Fund, BADEA, na OPEC Fund.