Akata kichwa cha mtoto na kutokomea nacho

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,322
33,126
MATUKIO ya ukatili kwa watoto yamezidi kuutikisa Mkoa wa Kagera baada ya mkazi wa kijiji cha Kyerere kata ya Kamuli wilaya mpya ya Kyerwa (jina linahifadhiwa) kudaiwa kukata kichwa cha mtoto aitwaye Fotidatus Focas(7) na kutokomea kusikojulikana.

Tukio hilo lilitokea wiki moja baada ya Diana Dionis(17)aliyekuwa mfanyakazi wa ndani eneo la Kashabo mjini Bukoba kukutwa amenyongwa na mwili wake kuning'inizwa kwa waya kwenye mpapai.

Watuhumiwa katika kesi hiyo ni Hidaya Felix aliyekuwa amemwajiri binti huyo na Prosper James (16) aliyekuwa rafiki wa kiume wa binti huyo.

Akizungumza kwa njia ya simu na Mwananchi ,ofisa mtendaji wa kijiji cha Kyerere Ponsian Behesha alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo juzi majira ya saa 12 jioni.

Akisimulia mkasa huo, ofisa huyo alisema mtuhumiwa alikuwa na malalamiko dhidi ya mtoto huyo kuwa alichoma moto uliosababisha kuungua kwa maharage yake yaliyokuwa nje ya nyumba na kudai uliunguza pia pesa alizokuwa amezihifadhi kwenye maharage.

Mtoto aliyeuawa alikuwa mwanafunzi wa darasa la awali katika kituo cha Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Usharika wa Nyakatuntu, Dayosisi ya Karagwe.

"Alileta malalamiko yake ofisini na leo(jana) tulikubaliana tungekuwa na kikao cha usuluhishi kati ya mtuhumiwa na baba yake na mtoto aitwaye Focas Fulgence juu ya marehemu huyo kuunguza maharage,"alibainisha mtendaji huyo kwa njia ya simu.

Pia alidai mtuhumiwa ambaye ni baba yake na marehemu baada ya makubaliano ya kukutana kesho yake kwa ajili ya usuluhishi alifuata panga nyumbani kwake na kwenda kufanya unyama huo.

Alisema mtuhumiwa ambaye husafiri mara kwa mara baadaye alionekana akitokomea kwenye msitu unaopakana na nchi jirani ya Uganda na juhudi za kumsaka zilikuwa bado zikiendelea.

Akizungumza kwa njia ya simu, mwenyekiti wa kijiji hicho. Fidelis Anathory alithibitisha kuwepo kwa mauaji hayo na kudai leo(jana)ndiyo ilipangwa kuwa siku ya usuluhishi kwa ndugu hao wawili baada ya mtuhumiwa kudai kuharibiwa mali na fedha zake.

Mwenyekiti huyo alilaani mauaji ya mtoto huyo ambapo alisema suala hilo halikuwa kubwa sana kiasi cha kulipiza kisasi kwa mauaji ya mtoto aliyedaiwa kuchoma moto uliounguza maharage ya mtuhumiwa.

Naye kamanda wa polisi mkoa wa Kagera, Henry Salewi alipoulizwa juu ya mauaji hayo kwa njia ya simu alisema alikuwa hajapata taarifa hiyo na kuahidi kutoa ufafanuzi baada ya kufuatilia.

chanzo: Akata kichwa cha mtoto na kutokomea nacho
 
Back
Top Bottom