Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 4,783
- 14,975
Chama cha ACT Wazalendo kimepokea taarifa kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa juu ya uamuzi wake wa kutengua ugombea wa Ndugu Luhaga Joelson Mpina kuwa Mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya ACT Wazalendo.
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Chama inaipitia kwa umakini hatua hii ya Msajili wa Vyama vya Siasa na katika wakati muafaka tutatoa mwelekeo wetu wa kina.
MSIMAMO WA AWALI
Wakati uchambuzi wa awali ukiendelea kufanyika tunapenda kutoa msimamo wetu wa awali juu ya suala hili kama ifuatavyo;
1. Chama cha ACT Wazalendo kinaweka msimamo kuwa hakitofuata maelekezo ya Msajili wa Vyama vya Siasa juu ya suala hili kwa sababu katika mazingira ambayo mchakato wa uchaguzi umeshaanza, Tume ya Uchaguzi imeshatoa fomu na wagombea wakiendelea na taratibu za ujazaji na urejeshaji wa fomu, Msajili wa Vyama vya Siasa hana mamlaka ya kuingilia mchakato huo isipokuwa kwa njia ya pingamizi.
Mgombea wetu wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ndugu Luhaga Joelson Mpina amechukua fomu, amezijaza, amezunguka nchi nzima kusaka wadhamini, amekula kiapo mahakamani na kukamilisha taratibu zote zinazohusu ukamilishaji wa fomu za kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Leo tarehe 26 Agosti 2025 fomu hizo zimehakikiwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi na kesho saa 7.00 mchana zitawasilishwa Ofisi ya Tume Huru ya Uchaguzi kwa ajili ya uteuzi.
2. Chama cha ACT Wazalendo kitafungua kesi Mahakama Kuu kupinga hatua hii ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Katika kesi hiyo, Chama kitaweka zuio (injunction) dhidi ya utekelezwaji wa uamuzi huu hadi kesi ya msingi isikilizwe.
Ado Shaibu,
Katibu Mkuu, ACT Wazalendo
26 Agosti 2025
Pia soma ~ ACT: Tumepokea barua ya Msajili kuhusu Mpina, tutafungau kesi Mahakamani