nameless girl
JF-Expert Member
- Apr 22, 2012
- 4,195
- 2,664
- Thread starter
- #21
***
Kiti cha Kombora kilikuwa kama chenye moto. Hakikukalika, mara aliinuka mara aliketi kana kwamba alikalia kaa ambalo lilikuwa likimchoma. Mkononi alikumbatia redio call yake kwa utulivu kama roho yake. Aliitazama na kuitingisha kama yai ambalo hakuwa na hakika kama ni zima au bovu.. Hata hivyo, alikuwa na kila hakika kuwa haikuwa mbovu. Ni ile ya upande wa pili ambayo alihitaji kuitilia shaka.
Muda mfupi tu uliopita alikuwa akiwasiliana na Koplo Shoka toka Lang’ata. Mara mawasiliano hayo yakakatika. Hakujua kama ilitokana na ubovu wa chombo hicho au Shoka alikata ghafla maongezi kuepuka mtu ambaye angeweza kuyasikia. Alichokuwa ameambulia ni “…Afande … tumempata…” na kisha “ amefika…” kisha chombo kikazimwa. Juhudi zote za Kombora kumpigia tena hazikuzaa matunda.
Wazo la kufanya uchunguzi kwa makini hapo Lang’ata lilimjia Kombora kutokana na uzoefu wake juu ya tabia za muuaji. Mara kwa mara katika kesi nyingi za mauaji hutokea muuaji akapenda kutembelea eneo na hata nyumba yalimotokea mauaji hayo.
Mara nyingine hutokea muuaji akadiriki hata kuhudhuria mazishi ya mtu aliyemuua. Kitu ambacho Kombora alikuwa haelewi ni sababu ipi ambayo hufanya wauaji hao wafanye hivyo. Hakujua kuwa walikuwa katika upelelezi wa kuelewa polisi wamefikia wapi katika uchunguzi wao, ama ni yaleyale waliyosema wahenga kuwa “damu nzito…” kwani mara kadhaa wauaji wengi wamepatikana kutokana na makosa hayo. Ni hilo tu ambalo lilimfanya amwamuru Shoka kuendelea na uchunguzi wake hapa Lang’ata ingawa siku mbili zilizopita hazikuwa na mafanikio.
Hivyo basi, redio yake ilipopata uhai na sauti ya Shoka ilipojitokeza na kusema “Tumempata” alijisikia kulia kwa furaha. Mara ukimya huu ukazuka. Dakika saba sasa zilikuwa zimepita. Aliendelea kuisubiri redio ya Shoka ipate uhai, aendelee kumwarifu alichogundua.
Dakika nane.
Dakika tisa.
Mara Kombora akaruka kama aliyeguswa na waya wa umeme. Akapiga ngumi kwa nguvu juu ya meza. Ameanza kuwa mzee? alijiuliza kwa hasira akiutia mkono katika fungati la meza yake na kuutoa ukiwa umeshikilia bastola yake kubwa ambayo aliitia mfukoni mwake.
Akatoka nje ya ofisi yake na kuchungulia ofisi ya msaidizi wake. Hakuwepo. Chumba cha pili alimpata askari mmoja ambaye alimtumia kuwakusanya askari wote waliokuwa ofisini wakati huo. Ukiwa usiku wa saa tano kasoro kituo kilikuwa na askari wanne tu. Wengine walikuwa katika shughuli nyinginezo au mapumzikoni. Kombora aliwachukua askari wawili na kumwamuru mmojawao aendeshe gari kasi iwezekanavyo kuelekea Lang’ata.
Gari lilikuwa likiruka, nusura lipae, lakini Kombora alizidi kumhimiza kijana huyo akanyage mafuta. Mara mbili askari mmoja alijaribu kumdadisi Kombora Lang’ata kulikoni lakini hakupata jibu lolote. Si kwamba Inspekta hakupenda kuzungumza, la! Isipokuwa hakuiamini sauti yake.
Hisia za hatari zilikuwa zikichemka akilini mwake na kumjaza hofu kila alipoyakumbuka maneno ya Shoka “…tumempata…” na kisha maongezi kukatika. Ni hili la mwisho lililomtisha zaidi. Amefika! Bila shaka ni Kakakuona. Amefika wapi? Alikuwa amefika katika ukumbi au alimfumania Shoka akiipiga redio hiyo? Kama ni hivyo kipi kinachofuata? Kombora alimwamini Shoka. Lakini pia aliamini kuwa Kakakuona yu kiumbe hatari zaidi ya simba aliyejeruhiwa. Ni hilo lililomtoa kasi ofisini.
Wakati wanafika mbele ya lango la ukumbi huo walisikia muziki ukikatika ghafla na kimya kikubwa kuzuka ndani ya ukumbi.Kombora aliruka nje ya gari na kumwambia askari mmoja alinde lango, asiingie wala kutoka mtu yeyote. Askari wa pili aliamriwa kufuatana naye.
“Kakakuona,” Kombora aliwanong’oneza. “Inawezekana yumo humu ndani. Picha zake mnazo. Mkimwona, kama hana silaha, msisite kumuua kwanza, maswali tutamuuliza baadaye. Okey?”
Ndani aliwakuta watu wakizungumza kwa sauti ya hofu na minong’ono. Umati mkubwa ulikuwa ukipambana kuingia choo cha wanaume ambako kila aliyetoka huko alikuwa kimya, aliyeduwaa kama aliyeona mzimu.
“Kuna nini?” Kombora alimuuliza mtu mmoja.
“Mtu amepigwa risasi.”
“A-me-kufa?” Kombora aliuliza akijaribu kuficha mshituko uliomkumba ghafla.
“Ataponaje? Unajua risasi mzee?” Kijana huyo alimjibu.
Ilimchukua Kombora na msaidizi wake dakika tatu nzima kuweza kupenya umati huo kuyafikia maiti. Hakuwa na haja ya kuyatazama kwa makini kabla ya kumtambua Shoka ambaye alilala kifudifudi kama anayechungulia kitu katika shimo la choo huku damu ikiendelea kutiririka na kufanya bwawa dogo jekundu liendelee kupanuka.
Kombora aliyasaga meno yake kwa hasira. Kisha alimwamuru mgambo ambaye alikuwa mbele ya mlango huo wa choo, akijaribu kuwazuia watu, kuufunga mlango wa choo hicho na kuulinda. Akarudi mlangoni ambako alitoa amri mpya. Watu wote watoke ukumbini humo, lakini si kabla ya kukaguliwa kila mmoja, tangu mifuko hadi vitambulisho.
Polisi wa Kituo cha Magomeni ambako tayari walikuwa wamepigiwa simu walipewa amri hiyo pia na kusaidiwa kuitekeleza. Wasichana, watoto na watu ambao hawakuwa na haja ya kushukiwa walitoka kwa urahisi. Watu wenye vitambulisho halali na shughuli zinazofahamika pia waliachiwa bila tabu. Lakini kuna wale ambao hata wao wenyewe hawazifahamu kazi zao, wale wenye zaidi ya kitambulisho kimoja, wao walitokwa jasho kwa maswali.
Baadhi yao walijikuta wakitupwa katika magari ya polisi na kupelekwa kituoni ambako waliendelea kuchunguzwa.
Muda wote huo Inspekta Kombora alikuwa nje ya ukumbi, kaegemea gari lake, mkono mfukoni ukiipapasapapasa bastola yake. Macho yake yalikuwa makini yakiuangalia kila uso na kila sura. Hakuiona dalili yoyote ya Kakakuona. Wala hakuwa na matumaini makubwa ya kuiona. Alivyomfahamu, kama mauaji hayo alikuwa kayatenda yeye, kwa vyovyote muda huo alikuwa maili kadhaa nje ya eneo hilo.
Hata hivyo, yawezekana akawa hakuyafanya yeye. Mtu aliyeyafanya anaweza akazubaa humo ukumbini, au akawa ameshirikiana na mtu ambaye atazubaa. Hilo ndilo lililomfanya asisitize uchunguzi wa makini kwa kila mtu.
Baada ya muda alimwita mgambo mwingine aliyekuwa akilinda magari na kumuuliza taratibu, “Ulikuwepo muda wote au ulitoka?”
“Nilikuwepo mzee.”
Unaweza kukumbuka ni magari mangapi yameondoka dakika kumi kabla ya tukio hili.”
“Kama sikosei, ni magari matano tu mzee.”
“Jaribu kukumbuka taratibu, unieleze magari hayo ni ya aina gani, yaliwachukua kina nani na yaliwapeleka wapi?”
Mgambo huyo alikuwa na kumbukumbu kali ambayo ilimfurahisha sana Kombora. Aliweza hata kukumbuka namba za magari matatu kati ya hayo, mawili ya kwanza yakiwa ya wenye disko hilohilo lililokuwa likipigwa hayakumvutia Kombora. Gari la tatu ambalo lililokuwa na wavulana wawili na wasichana wao pia halikumsisimua. Magari mawili ya mwisho ndiyo yalimfanya amtazame mgambo huyo kwa makini zaidi huku akitoa daftari lake dogo.
“Datsun nyekundu! Unasema ilikuwa na shombe wawili tu! Ambao walifika wakakaa dakika tano na kuondoka?”
“Ndiyo, mzee.”
“Namba yake…”
“TZA 42112”
Kombora aliinakili na kuuliza “Ilielekea wapi?”
“Sikumbuki vizuri nadhani ilielekea mjini.”
“Na hii nyingine unasema ni TZB 414, sio?”
“Ndiyo.”
“Toyota Corolla?”
“Ndiyo.”
“Ilikuwa na mtu mmoja tu! Ulimwangalia vizuri?”
“Sikupata nafasi ya kumwona vizuri. Lakini kwa harakaharaka nilimwona kama afisa hivi. Hata mavazi yake yalikuwa ya bei. Alitembea taratibu sana mkono mmoja mfukoni na kuingia katika gari lake. Nilitegemea atanipa walao asante kwa kumlindia gari lake, lakini hata kuniaga hakuniaga. Nadhani hiyo ndiyo sababu iliyonifanya niitazame gari yake na kuiweka namba akilini.”
Kombora alimsikiliza kwa makini na kunukuu hili na lile. Wakati akitaka kumtupia swali lingine, aliitwa mlangoni haraka. Mtu mmoja alikuwa amekamatwa na bastola. Alijaribu kuificha katika mapaja yake lakini mikono ya askari hao, ambayo imeelimika, ikaifikia.
Akapelekwa katika chumba cha ofisi ambamo aliendelea kuhojiwa huku Kombora akiifungua bastola hiyo na kuangalia risasi. Ilikuwa na risasi sita. Haikuwahi kufyatuliwa. Kibali cha kuwa na silaha? Hakuwa nacho. Kazi anayoifanya? Hakuijua. Kwa nini alikuja kwenye starehe na silaha? Hakujua. Kwa mtazamo wa harakaharaka, Kombora hakumwona kama mtu wake. Hivyo, aliamuru apelekwe kituoni pamoja na watuhumiwa wengine.
Hadi anahojiwa mtu wa mwisho ilikuwa yakaribia saa tisa alfajiri. Ndipo Kombora aliporudi ofisini baada ya kuhakikisha maiti yanapelekwa Muhimbili na familia yake kuarifiwa.
Ofisini Kombora aliinua simu na kumpigia Mkuu wa Usalama Barabarani, Mkoa wa Dar es Salaam. Bosi huyo, akiwa na usingizi mzito, alikoroma kwa hasira katika chombo cha simu “Nani?”
Lakini aliposikia jina na sauti ya Inspekta Kombora usingizi ulimtoka mara moja, akakiacha kitanda na kuuliza kwa upole, “Nikusaidie nini, mzee?”
“Samahani kwa kukusumbua,” Kombora alimwambia. “Ni suala ambalo haliwezi kulala. Naomba uwaambie vijana wako ambao wako zamu wanitafutie habari za magari haya mawili. TZB 414 na Datsun TZA 42112. Ikiwezekana waambie wayafuatilie kuona sasa hivi yako wapi. Waonye wasiwaulize wenyewe swali lolote ambalo linaweza kuwafanya washukiwe. Sawa?”
“Sawa.”
“Naweza kuyapata maelezo haya ofisini hapa kesho kabla ya saa moja asubuhi?”
“Tutajitahidi… nadhani tutapata.”
Kombora akaizima simu na kumtazama kijana wake mmoja ambaye alikuwa ameingia chumbani humo na kusimama kama aliyeitwa.
“Enhe?” Kombora akamtupia.
“Nimepokea simu kwa niaba yako mzee, baada ya kuona una simu nyingine. Imetokea Central ambako wanasema wamearifiwa na wavuvi juu ya maiti ya msichana mcheza disko ambayo wameiokota ufukweni. Wanasema amenajisiwa na kulawitiwa…”
“Kwa nini waniarifu mimi?” Kombora alimkatiza kwa ukali kidogo.
“Sura”
“Sura?”
“Wameniambia kwamba nikikwambia sura yake…”
“Inatosha!” Kombora alimwambia akiinua mkono wake kuuegemeza kwenye kichwa chake. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake alihisi uzee ukianza kumshinda nguvu.
Kiti cha Kombora kilikuwa kama chenye moto. Hakikukalika, mara aliinuka mara aliketi kana kwamba alikalia kaa ambalo lilikuwa likimchoma. Mkononi alikumbatia redio call yake kwa utulivu kama roho yake. Aliitazama na kuitingisha kama yai ambalo hakuwa na hakika kama ni zima au bovu.. Hata hivyo, alikuwa na kila hakika kuwa haikuwa mbovu. Ni ile ya upande wa pili ambayo alihitaji kuitilia shaka.
Muda mfupi tu uliopita alikuwa akiwasiliana na Koplo Shoka toka Lang’ata. Mara mawasiliano hayo yakakatika. Hakujua kama ilitokana na ubovu wa chombo hicho au Shoka alikata ghafla maongezi kuepuka mtu ambaye angeweza kuyasikia. Alichokuwa ameambulia ni “…Afande … tumempata…” na kisha “ amefika…” kisha chombo kikazimwa. Juhudi zote za Kombora kumpigia tena hazikuzaa matunda.
Wazo la kufanya uchunguzi kwa makini hapo Lang’ata lilimjia Kombora kutokana na uzoefu wake juu ya tabia za muuaji. Mara kwa mara katika kesi nyingi za mauaji hutokea muuaji akapenda kutembelea eneo na hata nyumba yalimotokea mauaji hayo.
Mara nyingine hutokea muuaji akadiriki hata kuhudhuria mazishi ya mtu aliyemuua. Kitu ambacho Kombora alikuwa haelewi ni sababu ipi ambayo hufanya wauaji hao wafanye hivyo. Hakujua kuwa walikuwa katika upelelezi wa kuelewa polisi wamefikia wapi katika uchunguzi wao, ama ni yaleyale waliyosema wahenga kuwa “damu nzito…” kwani mara kadhaa wauaji wengi wamepatikana kutokana na makosa hayo. Ni hilo tu ambalo lilimfanya amwamuru Shoka kuendelea na uchunguzi wake hapa Lang’ata ingawa siku mbili zilizopita hazikuwa na mafanikio.
Hivyo basi, redio yake ilipopata uhai na sauti ya Shoka ilipojitokeza na kusema “Tumempata” alijisikia kulia kwa furaha. Mara ukimya huu ukazuka. Dakika saba sasa zilikuwa zimepita. Aliendelea kuisubiri redio ya Shoka ipate uhai, aendelee kumwarifu alichogundua.
Dakika nane.
Dakika tisa.
Mara Kombora akaruka kama aliyeguswa na waya wa umeme. Akapiga ngumi kwa nguvu juu ya meza. Ameanza kuwa mzee? alijiuliza kwa hasira akiutia mkono katika fungati la meza yake na kuutoa ukiwa umeshikilia bastola yake kubwa ambayo aliitia mfukoni mwake.
Akatoka nje ya ofisi yake na kuchungulia ofisi ya msaidizi wake. Hakuwepo. Chumba cha pili alimpata askari mmoja ambaye alimtumia kuwakusanya askari wote waliokuwa ofisini wakati huo. Ukiwa usiku wa saa tano kasoro kituo kilikuwa na askari wanne tu. Wengine walikuwa katika shughuli nyinginezo au mapumzikoni. Kombora aliwachukua askari wawili na kumwamuru mmojawao aendeshe gari kasi iwezekanavyo kuelekea Lang’ata.
Gari lilikuwa likiruka, nusura lipae, lakini Kombora alizidi kumhimiza kijana huyo akanyage mafuta. Mara mbili askari mmoja alijaribu kumdadisi Kombora Lang’ata kulikoni lakini hakupata jibu lolote. Si kwamba Inspekta hakupenda kuzungumza, la! Isipokuwa hakuiamini sauti yake.
Hisia za hatari zilikuwa zikichemka akilini mwake na kumjaza hofu kila alipoyakumbuka maneno ya Shoka “…tumempata…” na kisha maongezi kukatika. Ni hili la mwisho lililomtisha zaidi. Amefika! Bila shaka ni Kakakuona. Amefika wapi? Alikuwa amefika katika ukumbi au alimfumania Shoka akiipiga redio hiyo? Kama ni hivyo kipi kinachofuata? Kombora alimwamini Shoka. Lakini pia aliamini kuwa Kakakuona yu kiumbe hatari zaidi ya simba aliyejeruhiwa. Ni hilo lililomtoa kasi ofisini.
Wakati wanafika mbele ya lango la ukumbi huo walisikia muziki ukikatika ghafla na kimya kikubwa kuzuka ndani ya ukumbi.Kombora aliruka nje ya gari na kumwambia askari mmoja alinde lango, asiingie wala kutoka mtu yeyote. Askari wa pili aliamriwa kufuatana naye.
“Kakakuona,” Kombora aliwanong’oneza. “Inawezekana yumo humu ndani. Picha zake mnazo. Mkimwona, kama hana silaha, msisite kumuua kwanza, maswali tutamuuliza baadaye. Okey?”
Ndani aliwakuta watu wakizungumza kwa sauti ya hofu na minong’ono. Umati mkubwa ulikuwa ukipambana kuingia choo cha wanaume ambako kila aliyetoka huko alikuwa kimya, aliyeduwaa kama aliyeona mzimu.
“Kuna nini?” Kombora alimuuliza mtu mmoja.
“Mtu amepigwa risasi.”
“A-me-kufa?” Kombora aliuliza akijaribu kuficha mshituko uliomkumba ghafla.
“Ataponaje? Unajua risasi mzee?” Kijana huyo alimjibu.
Ilimchukua Kombora na msaidizi wake dakika tatu nzima kuweza kupenya umati huo kuyafikia maiti. Hakuwa na haja ya kuyatazama kwa makini kabla ya kumtambua Shoka ambaye alilala kifudifudi kama anayechungulia kitu katika shimo la choo huku damu ikiendelea kutiririka na kufanya bwawa dogo jekundu liendelee kupanuka.
Kombora aliyasaga meno yake kwa hasira. Kisha alimwamuru mgambo ambaye alikuwa mbele ya mlango huo wa choo, akijaribu kuwazuia watu, kuufunga mlango wa choo hicho na kuulinda. Akarudi mlangoni ambako alitoa amri mpya. Watu wote watoke ukumbini humo, lakini si kabla ya kukaguliwa kila mmoja, tangu mifuko hadi vitambulisho.
Polisi wa Kituo cha Magomeni ambako tayari walikuwa wamepigiwa simu walipewa amri hiyo pia na kusaidiwa kuitekeleza. Wasichana, watoto na watu ambao hawakuwa na haja ya kushukiwa walitoka kwa urahisi. Watu wenye vitambulisho halali na shughuli zinazofahamika pia waliachiwa bila tabu. Lakini kuna wale ambao hata wao wenyewe hawazifahamu kazi zao, wale wenye zaidi ya kitambulisho kimoja, wao walitokwa jasho kwa maswali.
Baadhi yao walijikuta wakitupwa katika magari ya polisi na kupelekwa kituoni ambako waliendelea kuchunguzwa.
Muda wote huo Inspekta Kombora alikuwa nje ya ukumbi, kaegemea gari lake, mkono mfukoni ukiipapasapapasa bastola yake. Macho yake yalikuwa makini yakiuangalia kila uso na kila sura. Hakuiona dalili yoyote ya Kakakuona. Wala hakuwa na matumaini makubwa ya kuiona. Alivyomfahamu, kama mauaji hayo alikuwa kayatenda yeye, kwa vyovyote muda huo alikuwa maili kadhaa nje ya eneo hilo.
Hata hivyo, yawezekana akawa hakuyafanya yeye. Mtu aliyeyafanya anaweza akazubaa humo ukumbini, au akawa ameshirikiana na mtu ambaye atazubaa. Hilo ndilo lililomfanya asisitize uchunguzi wa makini kwa kila mtu.
Baada ya muda alimwita mgambo mwingine aliyekuwa akilinda magari na kumuuliza taratibu, “Ulikuwepo muda wote au ulitoka?”
“Nilikuwepo mzee.”
Unaweza kukumbuka ni magari mangapi yameondoka dakika kumi kabla ya tukio hili.”
“Kama sikosei, ni magari matano tu mzee.”
“Jaribu kukumbuka taratibu, unieleze magari hayo ni ya aina gani, yaliwachukua kina nani na yaliwapeleka wapi?”
Mgambo huyo alikuwa na kumbukumbu kali ambayo ilimfurahisha sana Kombora. Aliweza hata kukumbuka namba za magari matatu kati ya hayo, mawili ya kwanza yakiwa ya wenye disko hilohilo lililokuwa likipigwa hayakumvutia Kombora. Gari la tatu ambalo lililokuwa na wavulana wawili na wasichana wao pia halikumsisimua. Magari mawili ya mwisho ndiyo yalimfanya amtazame mgambo huyo kwa makini zaidi huku akitoa daftari lake dogo.
“Datsun nyekundu! Unasema ilikuwa na shombe wawili tu! Ambao walifika wakakaa dakika tano na kuondoka?”
“Ndiyo, mzee.”
“Namba yake…”
“TZA 42112”
Kombora aliinakili na kuuliza “Ilielekea wapi?”
“Sikumbuki vizuri nadhani ilielekea mjini.”
“Na hii nyingine unasema ni TZB 414, sio?”
“Ndiyo.”
“Toyota Corolla?”
“Ndiyo.”
“Ilikuwa na mtu mmoja tu! Ulimwangalia vizuri?”
“Sikupata nafasi ya kumwona vizuri. Lakini kwa harakaharaka nilimwona kama afisa hivi. Hata mavazi yake yalikuwa ya bei. Alitembea taratibu sana mkono mmoja mfukoni na kuingia katika gari lake. Nilitegemea atanipa walao asante kwa kumlindia gari lake, lakini hata kuniaga hakuniaga. Nadhani hiyo ndiyo sababu iliyonifanya niitazame gari yake na kuiweka namba akilini.”
Kombora alimsikiliza kwa makini na kunukuu hili na lile. Wakati akitaka kumtupia swali lingine, aliitwa mlangoni haraka. Mtu mmoja alikuwa amekamatwa na bastola. Alijaribu kuificha katika mapaja yake lakini mikono ya askari hao, ambayo imeelimika, ikaifikia.
Akapelekwa katika chumba cha ofisi ambamo aliendelea kuhojiwa huku Kombora akiifungua bastola hiyo na kuangalia risasi. Ilikuwa na risasi sita. Haikuwahi kufyatuliwa. Kibali cha kuwa na silaha? Hakuwa nacho. Kazi anayoifanya? Hakuijua. Kwa nini alikuja kwenye starehe na silaha? Hakujua. Kwa mtazamo wa harakaharaka, Kombora hakumwona kama mtu wake. Hivyo, aliamuru apelekwe kituoni pamoja na watuhumiwa wengine.
Hadi anahojiwa mtu wa mwisho ilikuwa yakaribia saa tisa alfajiri. Ndipo Kombora aliporudi ofisini baada ya kuhakikisha maiti yanapelekwa Muhimbili na familia yake kuarifiwa.
Ofisini Kombora aliinua simu na kumpigia Mkuu wa Usalama Barabarani, Mkoa wa Dar es Salaam. Bosi huyo, akiwa na usingizi mzito, alikoroma kwa hasira katika chombo cha simu “Nani?”
Lakini aliposikia jina na sauti ya Inspekta Kombora usingizi ulimtoka mara moja, akakiacha kitanda na kuuliza kwa upole, “Nikusaidie nini, mzee?”
“Samahani kwa kukusumbua,” Kombora alimwambia. “Ni suala ambalo haliwezi kulala. Naomba uwaambie vijana wako ambao wako zamu wanitafutie habari za magari haya mawili. TZB 414 na Datsun TZA 42112. Ikiwezekana waambie wayafuatilie kuona sasa hivi yako wapi. Waonye wasiwaulize wenyewe swali lolote ambalo linaweza kuwafanya washukiwe. Sawa?”
“Sawa.”
“Naweza kuyapata maelezo haya ofisini hapa kesho kabla ya saa moja asubuhi?”
“Tutajitahidi… nadhani tutapata.”
Kombora akaizima simu na kumtazama kijana wake mmoja ambaye alikuwa ameingia chumbani humo na kusimama kama aliyeitwa.
“Enhe?” Kombora akamtupia.
“Nimepokea simu kwa niaba yako mzee, baada ya kuona una simu nyingine. Imetokea Central ambako wanasema wamearifiwa na wavuvi juu ya maiti ya msichana mcheza disko ambayo wameiokota ufukweni. Wanasema amenajisiwa na kulawitiwa…”
“Kwa nini waniarifu mimi?” Kombora alimkatiza kwa ukali kidogo.
“Sura”
“Sura?”
“Wameniambia kwamba nikikwambia sura yake…”
“Inatosha!” Kombora alimwambia akiinua mkono wake kuuegemeza kwenye kichwa chake. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake alihisi uzee ukianza kumshinda nguvu.