Zuberi Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Naibu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema na Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi amekataa kupokea poso ya vikao (Sitting Allowance). Anasema si halari kulipwa fedha hiyo kwa kuwa kukaa kwenye vikao vya bunge na vingine anavyoshiriki kama mbunge ni sehemu ya kazi zake kama mbunge.Mbunge wa Arusha Mjini (chadema) Godbless Lema na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema anamwona Zitto mnafiki kwa kile anachodai kukataa kwake posho ni hadaa kwa wananchi yenye lengo la kujipatia manufaa ya kisiasa, na kamwe (Zitto) hana chembe ya uzalendo kwa kuwa umasikini sio kipimo cha uzalendo. Hii ndio ajenda iliyokuwa ikitawala katika mitandao ya kijamii na magazeti hivi karibuni.Ukifuatilia msingi wa hoja hii tangu uibuke miaka miwili iliyopita, na ukisoma kwa makini maandiko ya Zitto na Lema katika mitandao ya kijamii waweza kugundua kuwa hawa wanasiasa wawili wana ajenda inayofanana, tofauti yao ni uwasilishaji, bila shaka na nia zilizojificha nyuma yao.Kwa mujibu wa Lema mbunge hupokea kiasi cha Tsh 70,000 kwa kila siku anayoshiri vikao vya bunge na kamati zake. Kwa mantiki hii mbunge anapokea zaidi Tsh 12,000,000 kwa vikao vyote vya Bunge kwa Mwaka. Pia Lema anadai kuwa Zitto kama Mwenyekiti wa PAC anapokea posho ya kikao kati Tsh 700,000 hadi 1,000,000 kwa kikao kimoja katika vikao vinvyofanywa na mashirika mbali mbali hususani Mashirika ya hifadhi za Jamii. Mashirika haya kwa ujumla kama yatafanya vikao vikao ishirini kwa mwaka Zitto atakuwa amepokea kiasi cha Tsh 14,000,000. Kiasi hiki kinaweza kuongezeka kama mpaka 20,000,000 kwa kuwa Zitto kama mwenyekiti wa PAC hupata mialiko wa kuhudhuria vikao mbali mbali.Tarehe 7 Juni, 2011 Zitto alimwandikia Katibu wa Bunge barua ya kumuelekeza kuwa posho zake za vikao zielekezwe katika taasisi ya Kigoma Development Initiative (KDI) kupitia akaunti Na. 0IJ1087940900 ya benki ya CRDB tawi la Kigoma. Tarehe 10 Juni, 2011 Katibu wa Bunge alimwandikia Zitto barua ya kumtaarifu kuwa, ameelekezwa na Spika amueleze kuwa utaratibu wa Bunge ni kumlipa mbunge stahiki zake moja kwa moja, na kuwa mbunge mwenyewe anaweza kutoa pesa na kuzipeleka anakotaka. Siku hiyo hiyo ya tarehe 10 Juni, 20111 Zitto alimwandikia Katibu wa Bunge akimwelekeza asimlipe posho za vikao.Kwetu Ukerewe tunazo changamoto nyingi za maendeleo. Jitihada zozote zile, ziwe kubwa au ndogo za kupunguza changamoto hizi zinakaribishwa. Umasikini wa kipato umekuwa ukiongezeka. Elimu ya watoto wetu na ndugu zetu imekuwa ikishuka kadri miaka inavyokwenda. Shule hazina walimu, kuna upungufu mkubwa wa vitabu vya kiada na ziada, nyumba za walimu na vyumba vya madarasa. Huduma za afya bado hazirizishi. Vituo vya afya havitoshi, na katika vijiji ambavyo kuna vituo vya afya watoa hudumu hawatoshi. Katika zahanati ambako dawa zinapatikana, wananchi hawa uwezo wa kuzigharimia huduma za afya. Upatikanaji wa maji bado ni kitendawili, na wakati wa kiangazi hali huwa mbaya zaidi.Kama ningekuwa mbunge nisingekataa posho kama anavyofanya Mbunge wa Kigona Kaskazini Zuberi Zitto Kabwe. Wapiga kuwa wangu wangeniuliza yego usarile? Wengine wangeniita mbula bhwenge. Ingekuwa vigumu kwao kunielewa. Ningekosa ujasiri wa kusimama mbele yao. Nitaupata wapi ujasili wakati nimekataa Tsh 60,000,000 za posho za vikao vya bunge kwa kipindi cha miaka mitano niliyo wawakilisa ? Wangeniambia ulipaswa kuchukua posho utuletee tuitumie. Nusu ya kiasi hicho kingesaidia kujenga shule ya msingi Chibasi kule Malelema ili kupunguza mateso kwa watoto wanaotembea kilometa nyingi kwenda kusaka elimu katika shule ya msingi Mubule. Kiasi kilichobaki kingesaidia kumalizia ujenzi wa shule ya Sekondari Nyakuna, ambayo wananchi wa kata ya Nyamanga wamekuwa wakijitahidi kumaliza kwa kipindi cha miaka minne.Ningekuwa mbunge wa ajabu kama Zitto kwa kukataa 70,000,000 ambazo ni posho za vikao vya mashirika ya umma kwa mwaka. Wananchi wa Chibasi wangeniuliza kwa nini nisingepokea pesa hizo niwapelekee wamalizie ujenzi wa zahanati yao ili kupunguza mateso kwa akina mama wanaosafiri mpaka Nyamanaga kutafuta tiba?Ningekwepa kupita Bukonyo ili nisisikie kilio chao cha uchakavu wa zahanati na kukosekana kwa nyumba ya mganga, hali inayiomlazimu (mganga) kusafiri umbali mrefu kufika kazini.Watoto wa kike wamekuwa waathirika wakubwa wa ukosefu wa mabweni katika shule nyingi za Ukerewe. Wanakaa geto. Wengi wao wamepata ujauzito na kukatisha masomo yao. Hitaji la mabweni ni kubwa sana. Dhamira yangu ingenisuta kama ninge kataa posho ya vikao vya baraza za madiwani na RCC. Kwangu mimi ni uendawzimu kukataa posho ya wananchi. Wao ndio walipa kodi wakuu. Kuchukua posho yao na kuwarudishia ndio uwajibikaji. Tatizo ninaloliona kwa wanasiasa wetu ni ubinafsi. Tunakataa posho kwa manufaa binafsi, na wanaozipokea, na hata kudai ziongewe ni kwa masilahi binafsi.Awali Zitto alipendekeza posho yake ipelekwe kwenye taasisi ya maendeleo ya Kigoma (KDI). Hii ilikuwa hoja ya msingi kwa kuwa lengo la taasisi hii ni kupeleka maendeleo kwa wananchi. Ningemuona Zitto mzalendo zaidi kama angepokea posho na kuzipeleka kwa wananchi kupitia taasisi hii kuliko kuzikataa wakati watu wa jimboni kwake hawana uhakika na elimu bora, afya na maji safi.Naunga mkono hoja ya kupitia mfumo wa kutoa posho, hasa kwa wabunge. Kama mantiki ni kuwa hizi pesa ni za wananchii na kuwa si jambo jema kwa wabunge kujinufaisha kwa pesa za wananchi, wakati wenye nazo wanataabika, basi serikali iweke utaratibu wa posho kuelekezwa katika mfuko ya jimbo ambako zitatumika kwa maelekezo ya wananchi wenyewe.