ChoiceVariable
JF-Expert Member
- May 23, 2017
- 43,100
- 49,795
CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimemtaka Jaji wa Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma na aliyekuwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), ambaye kwa sasa ni Jaji, Biswalo Mganga, wajiuzulu kupisha uchunguzi wa sakata la fedha zilizopatikana kupitia mchakato wa kisheria wa makubaliano ya kukiri kosa (Plea Bargaining). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.
Ni baada ya Rais Samia Suluhu Hassan, hivi karibuni kuagiza tume aliyoiunda kuangalia namna ya kuboresha mfumo wa haki jinai nchini, kupitia upya mchakato huo ili kubaini fedha zilizokusanywa ambazo hazijulikani zilipo.
Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 2 Februari 2023 na Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, kupitia taarifa yake aliyoitoa kwa umma.
Kupitia taarifa hiyo Zitto amedai kuwa, Prof. Ibrahim na Jaji Biswalo, wanapaswa kujiuzulu ili kupisha uchunguzi wa suala hilo kwa ajili ya kulinda hadhi ya mahakama.“Kwa maelezo hayo ya Rais, aliyekuwa msimamizi mkuu wa mhimili wa haki nchini ni mahakama, ambaye bado ni Jaji Mkuu wa Tanzania, na aliyekuwa DPP wakati wa uvunjifu wa haki na sasa harufu ya ufisadi ikinukia, Jaji Biswalo, hawana tena sifa ya kuendelea kutumikia nyadhifa za kisheria walizo nazo sasa,” imesema taarifa ya Zitto.
“Sisi ACT-Wazalendo tulilisemea kwa kina jambo hili wakati wa uchambuzi wetu wa ripoti ya CAG ambaye alionyesha kuwa fedha zilizokusanywa hazijulikani zilitumikaje. Taarifa ya juzi ya Rais Samia imethibitisha yaliyosemwa na CAG na imetonesha vidonda vya uchungu na maumivu makali ambayo watanzania walipitishwa na mfumo uliopo sasa wa haki jinai,” imesema taarifa ya Zitto na kuongeza:
“ACT-Wazalendo tunawataka Jaji Mkuu, pamoja na Jaji Biswalo kujiuzulu ili kupisha uchunguzi wa kina wa jambo hili na pia kuusitiri mhimili wa mahakama ambao tukitumia lugha ya kiungwana ulinajisiwa mbele ya macho yao. Ni muhimu waondoke ili kulinda hadhi ya mahakama.”