Wizara ya Elimu, Mna habari na Ufisadi huu mashulen?

Lekanjobe Kubinika

JF-Expert Member
Dec 6, 2006
3,020
577
Dar es Salaam ni makao makuu ya kila kitu kwa nchi yetu Tanzania, hata kama tutajidai makao makuu yapo Dodoma. Harakati za maendeleo ya nchi karibu kila kona ya maisha kitovu chake kipo DSM, mwenye kukataa hilo ana haki yake kutoafiki.

Sasa mitihani ya kidato cha nne matokeo yake yametoka, lakini hicho kitendo kimenifanya nikumbuke kitu muhimu juu ya elimu, kwani matokeo ya mkitihani ni kilele cha harakati ngumu sana za elimu kwa kila mdau.

Elimu yetu Tanzania itaendelea kuzorota kama msingi wa elimu unapuzwa na au kubezwa na wadau wote pia. Msingi wa elimu unaanzia kwenye familia mojamoja, lakini elimu rasmi yenye mfumo rasmi unaanzia Shule za Msingi. Kama nyumba ina msingi legelege ni rahisi kubomoka ikikutana hata na ghadhabu kiogo tu.

Shule za Msingi DSM zimeonyesha kero ya kudumu ambayo nachelea kusema hata Wizara ya Elimu inachekelea na haina ubavu kuidhibiti. SIelewi kama ni kero iliyogeuzwa kuwa kitu halali kimkandamkanda bila kupitia bunge kimswada. Mtoto asipowapelekea walimu angalau shilingi 100/= kila siku kwa kisingizio cha mitihani ya ila siku, ajue kichapo kiko mbele yake. JUmamosi darasa la saba na la nne lazima kupeleka kwa walimu shilingi 500/= kwa kisingizio kicho hicho.

Kwa mzazi wa kawaida kama anao watoto wawili wa darasa la saba na la nne maana yake ni lazima ajitayarishe kulipa TZS 1000/= kwa uchache kila wiki kwa kila mtoto kwa walimu tu, hapo bado pesa ya kumwezesha mtoto anywe angalau juisi na au maji katika jua kali la DSM anaposhinda shuleni tangu saa 12 asubuhi hadi saa 10 jioni. Kwa watoto wa darasa la saba na la nne kuna tuition walimu wameitengeneza baada ya masomo, ole wake mtoto asiyehudhuria na kulipa kwa kadiri walimu watakavyotamka. Kesho yake ama ni viboko au ni kukutana na mtihani ambao wenzake wamefundishwa jana yake kwenye tuition.

Sasa wazazi hohehahe unaweza kuelewa wanavyopigika, wakitafuta angalau mlo wa siku moja ambao kwa kawaida huwa jioni wakati wote wapo, wakati uo huo piga ua lazima pesa ya "kumlipa mwalimu" iwepo ambayo mtoto anatakiwa kuipeleka asubuhi. Kama mtoto hataenda na pesa hiyo, mkong'oto wa haja uk mbele yake. Kuna kijana mmoja shule moja ya Wilaya ya Kinondoni kule Tegeta alivunjwa mkono siku moja na mwalimu wa zamu, ambaye dhamana yake ilikuwa kukusanya pesa ya mitihani, mtoto yatima hakuwa nayo sababu mfadhili wake alikuwa safarini na pesa ikakosekana. Kijana akashikishwa adabu kwa kipigo cha paka mwizi ati amekula pesa ya mitihani. Wiki nzima alilazimika kuuguliwa.

Mtoto wangu pia shule iyo hiyo, siku moja alikuja amevimba mikono vibaya sana hata alikuwa hawezi kushika kijiko, kisa? Nilisahau kumpa hela sio ya mitihani tu, bali hata ya matumizi yake ya juisi na maji nilisahau kumpa hakuwa nayo na walimu hakikueleweka. Sasa mwanangu kwa kuwa hata mbu akimng'ata huvimba, siku hiyo ilikuwa patashika. Nilipotaka kuchukuwa hatua, nikaonywa kwamba sasa naanzisha vita na system ya walimu ambayo mimi peke yangu sitaiweza, maana japo wazazi wanalalamikia hayo, hata serikali yenyewe imeshindwa. Nikaona bora pesa iwe ndiyo alarm yangu kila ninapoondoka asubuhi kwenda kazini, ambako bahati mbaya ninaowafanyia kazi wanadai kwamba hata kunipa asante ya hiari yao ni rushwa kubwa.

Kwa hiyo kazi yangu ni kila siku kuchomolewa na walimu na mimi ningojee mshahara wa mwisho wa mwezi ambao pia walimu wanapata ulio mkubwa zaidi ya ule wa kwangu, kwa aina ya kazi yangu. Sasa angalau nina kibarua, sielewi yule mlalahoi asiye na nafasi hata ya kuweka tuta la mchicha mbele yake anamudu vipi maisha? Lakini, hivi Wizara ya Elimu ituambie kwamba haijui mambo haya yanayofanyika mbele ya macho yao? Kswa nini wasiseme rasmi kiwamba ada ya mitihani ni 50,000/= ijulikane na kukatiwa risiti, badala ya kinachoendelea miaka nenda miaka rudi? Au viongozi wa wizara ya elimu watoto wao hawasomi shule zetu hizi? Nani anakagua matumizi ya shilingi mia na miatano zinazoliza watoto? Mara nyingi watoto hawaendi shule kwa kuwa hawakuiona pesa ya kuwapelekea walimu. Ndio elimu bure ya Msingi hiyo au danganya toto?

Kufa elimu itaendelea kufa, walimu wataendelea kujidhalilisha kwa kulialia kama vile wako peke yao tu duniani wanaoona maisha ni magumu. Nilitaraji walimu wangekuwa mstari wa mbele kuhakikisha majibu ya kiuondokana na umasikini katika jamii yanapatikana, lakini wanajidhalilisha kwa mia mia kila siku hata hawana nafasi ya kufikiri njia bora ya kupata milioni moja! Pole sana walimu wetu, pole elimu Tanzania. Kipofu akimwongoza kipofu mwenzie, wataweza vipi kuepuka kutumbukia shimoni wakafa wote pia?

Wizara ya elimu, be serious kidogo tu, peleka questionnaire mashuleni uliza watoto kwa upole, mtagundua ufisadi ulivyokomaa na mtajua kina vijisenti wanaonewa, kwa kuwa Richmond inakula pesa pale penye pesa, lakini walimu wanakamua kwa wananchi hohehahe moja kwa moja. Ni vichapo pasipo kuvaa kaptura.

Kuna mahali shule ya Upili hapo DSM, walimu wanapigana makonde ofisini kila mara kwa sababu ya kutoelewana katika kugawana pesa za mitihani kutoka kwa wanafunzi. Ni mfumo waliojiwekea kwamba mtihani uwepo au usiwepo michang lazima ikusanywe ili wanywe chai, wale na wapate nauli na kadhalika. Ni sawa na traffic anayemwambia mkewe ainjike maji ya ugali wakati yeye anavaa sare kwenda barabarani kulkamata magari "yenye makosa" ili kupata mboga ya siku hiyo. Lazima kieleweke siku hiyo, hata gari lililotoka kiwandani jipya kabisa lazima likutwe na osa, maana kama sivyo nyumbani hapatakalika, patakuwa hapatoshi.

Wizara ya elimu, tusifurahie matokeo na au kiulialia kwa kutofaulu vizuri watoto, lakini ondoeni kero za kipumbavu zinazolipeleka Taifa shimoni. Jumuia ya Afrika Mashariki hiyoooooooo....... mpaka kufagia maofisini sasa watatoka nchi za nje, maana sisi tutakuwa tumedumaa kielimu tukitoana macho kwa kupiga debe bodaboda. Tanzania ni wazuri sana kupanga mipango, lakini utekelezaji wa mipango huwa siku zote ni kiini macho> Amkeni watanzania, amkeni walimu, Think big! teaching is a highly valued and nobble profession, achana na miamia!

Leka
 
Back
Top Bottom