EasyFit
JF-Expert Member
- Jul 4, 2011
- 1,269
- 1,082
JINAMIZI la kisiasa linazidi kumwandama Rais Mstaafu Benjamin Mkapa baada ya wanasiasa na wasomi nchini kuzidi kumshambulia , wakikosoa kauli yake ya hivi karibuni, kudai kwamba hamtambui Mbunge wa Musoma mjini, Vincent Nyerere kuwa ni miongoni mwa familia ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Wamesema kuwa wanachotaka wananchi, ni kusikia jinsi wagombea wanavyonadi sera zinazolenga kutatua matatizo yanayowakabili, si kufanya kampeni za kuhusisha watu na kwamba, kauli ya Rais huyo mstaafu dhidi ya Vincent Nyerere, sio suluhisho la kumaliza umasikini wa Watanzania. Machi 12 mwaka huu wakati akifungua kampeni za CCM katika jimbo la Arumeru Mashariki, Mkapa alidai hamtambui mbunge huyo kuwa ni miongoni mwa wanafamilia ya Mwalimu Nyerere kwani katika kipindi chote alichofanya kazi na Mwalimu, hakusikia jina hilo.
Siku moja baadaye, kauli hiyo ilipingwa vikali na Vincent akisema si jambo la ajabu Mkapa kutomfahamu yeye kwasababu Mkapa si sehemu ya ukoo wao. Alimrushia lawama kuwa akiwa madarakani, Mkapa alishinikiza Mwalimu Nyerere kupelekwa Hospitali ya St Thomas, Uingereza, kinyume na matakwa ya familia yao.
Kama hiyo haitoshi, Madaraka Nyerere ambaye ni mtoto wa Mwalimu Nyerere, aliibuka siku moja baadaye na kuthibitisha kuwa Mbunge huyo ni mdogo wao na mwanafamilia hiyo, kwani ni mtoto wa baba yao mdogo, marehemu Josephat Kiboko Nyerere.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam(UDSM), Profesa Gaudence Mpangala, alisema siasa za vyama vingi hasa katika miaka ya hivi karibuni, zimekuwa hazina tija kwa wananchi kwani wagombea hujikita zaidi kuzungumza mambo yasiyokuwa na mantiki kwa wananchi. "Hili ni tatizo na ushauri wangu kwa wananchi ni kuhakikisha kwamba inatungwa sheria ya kuonyesha aina ya ushindani wa mfumo wa vyama vingi, huku kuzungumzia watu badala ya nini kifanyike, ni kuwahadaa wananchi" alisema Profesa Mpangala.
Alisema kuwa kilichomkuta Mkapa ni kitendo cha aibu mbele ya jamii, huku akishangazwa na hatua cha chama hicho tawala kumpeleka rais huyo mstaafu katika ufunguzi wa kampeni zake. "Hata Vincent kwa kulinda heshima ya Mkapa, angeweza kukaa kimya tu, angejikita zaidi kueleza mgombea wa Chadema atawafanyia nini watu wa Arumeru Mashariki kama wakimchagua kuwa mbunge wao," alisema Mpangala. Alisema kuwa asilimia kubwa ya Watanzania ni masikini, hivyo wanaosimama majukwaani kuomba kura wanatakiwa kulifahamu hilo. Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Bashiru Ally alisema kuwa siasa za namna hiyo ni za kawaida katika kampeni nyingi nchini.
"Tunatakiwa kujiuliza nini chanzo cha siasa za aina hii, kwanini vyama vya siasa nchini vikiwa katika kampeni vinajikita zaidi kuzungumzia watu kuliko maisha halisi ya wananchi na jinsi ya kuyamaliza?" Alihoji Ally. Alisema kuwa hata katika uchaguzi mdogo wa Igunga, yalitokea kama yanayotokea Arumeru Mashariki na kuongeza kuwa wananchi kabla ya kuamua nani wamchague, wanatakiwa kujiuliza maswali mengi juu ya siasa za kupakana matope. Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustino Mrema, alisema siasa za namna hiyo zinaweza kujenga chuki katika jamii na kwamba binafsi hawezi kuziunga mkono.
"Siasa nyingine zinajenga chuki, siasa za kinafiki siwezi kuziunga mkono, tufikie wakati tutofautishe mambo binafsi na mambo ya umma," alisema Mrema. Mrema ambaye pia ni mbunge wa Vunjo, alisema kampeni za kupigana ‘vijembe' kuwa mgombea fulani hana mke, nyumba sio wanachokitaka wananchi. "Sio Mkapa tu, wapo wengine ambao wanazungumza mambo yasiyofaa katika jamii, binafsi nadhani sio njia nzuri ya kuomba kura kwa wananchi" alisema Mrema.
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Samwel Ruhuza aliwataka Watanzania kuwapopoa mawe viongozi wa vyama vya siasa nchini wanaojikita kuzungumzia watu badala ya kujikita katika mikakati ya kuendeleza sehemu husika. "Nilimshangaa sana Rais Mstaafu Mkapa, badala ya kuzungumza sera, anazungumzia watu, sasa kauli yake hiyo itaweza kuwasaidiaje wananchi? Umefikia wakati wa kuacha ‘mipasho' katika kampeni, sasa kama sio mtoto wa Nyerere, alitaka wananchi wafanyaje?" Alihoji. Alisema kuwa hata kitendo cha CCM kusema kuwa mgombea wake akichaguliwa atamaliza tatizo la migogoro ya ardhi katika jimbo hilo, inaonyesha jinsi chama hicho kisivyokuwa na nia ya kuwasaidia wananchi.
"Sasa CCM ndio Serikali yenyewe, huku wakiwa mbele ya Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa na viongozi wengine wa mkoa, wanaeleza wazi kuwa mgombea wa CCM akichaguliwa atamaliza tatizo la ardhi pale Arumeru, huu si uhuni jamani!" alisema Ruhuza. Mwenyekiti wa chama cha UPDP, Fahm Dovutwa licha ya kusema kuwa vyama vingi vya siasa nchini havina sera zinazoeleweka, alisisitiza kuwa huenda rais mstaafu Mkapa alitoa kauli hiyo bila kukusudia.
"Unajua ukoo wa Nyerere wapo wengi sana na Mkapa asingeweza kuwafahamu wote nadhani aliteleza tu..., naishangaa sana CCM inazungumza kuwa itatekeleza baadhi ya mambo kama mgombea wake akichaguliwa kuwa mbunge, ina maana asipochaguliwa kila kitu kinabaki kama kilivyokuwa awali?" Alihoji Dovutwa.
Naye mwenyekiti wa chama cha Sauti ya Umma (SAU), Paul Kyara, alisema umefikia wakati kwa vyama vya siasa kujikita zaidi kuzungumzia matatizo ya wananchi na kwamba majibizano, kejeli na kunyosheana vidole, havina manufaa kwa taifa.
Gazeti la Mwananchi
Wamesema kuwa wanachotaka wananchi, ni kusikia jinsi wagombea wanavyonadi sera zinazolenga kutatua matatizo yanayowakabili, si kufanya kampeni za kuhusisha watu na kwamba, kauli ya Rais huyo mstaafu dhidi ya Vincent Nyerere, sio suluhisho la kumaliza umasikini wa Watanzania. Machi 12 mwaka huu wakati akifungua kampeni za CCM katika jimbo la Arumeru Mashariki, Mkapa alidai hamtambui mbunge huyo kuwa ni miongoni mwa wanafamilia ya Mwalimu Nyerere kwani katika kipindi chote alichofanya kazi na Mwalimu, hakusikia jina hilo.
Siku moja baadaye, kauli hiyo ilipingwa vikali na Vincent akisema si jambo la ajabu Mkapa kutomfahamu yeye kwasababu Mkapa si sehemu ya ukoo wao. Alimrushia lawama kuwa akiwa madarakani, Mkapa alishinikiza Mwalimu Nyerere kupelekwa Hospitali ya St Thomas, Uingereza, kinyume na matakwa ya familia yao.
Kama hiyo haitoshi, Madaraka Nyerere ambaye ni mtoto wa Mwalimu Nyerere, aliibuka siku moja baadaye na kuthibitisha kuwa Mbunge huyo ni mdogo wao na mwanafamilia hiyo, kwani ni mtoto wa baba yao mdogo, marehemu Josephat Kiboko Nyerere.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam(UDSM), Profesa Gaudence Mpangala, alisema siasa za vyama vingi hasa katika miaka ya hivi karibuni, zimekuwa hazina tija kwa wananchi kwani wagombea hujikita zaidi kuzungumza mambo yasiyokuwa na mantiki kwa wananchi. "Hili ni tatizo na ushauri wangu kwa wananchi ni kuhakikisha kwamba inatungwa sheria ya kuonyesha aina ya ushindani wa mfumo wa vyama vingi, huku kuzungumzia watu badala ya nini kifanyike, ni kuwahadaa wananchi" alisema Profesa Mpangala.
Alisema kuwa kilichomkuta Mkapa ni kitendo cha aibu mbele ya jamii, huku akishangazwa na hatua cha chama hicho tawala kumpeleka rais huyo mstaafu katika ufunguzi wa kampeni zake. "Hata Vincent kwa kulinda heshima ya Mkapa, angeweza kukaa kimya tu, angejikita zaidi kueleza mgombea wa Chadema atawafanyia nini watu wa Arumeru Mashariki kama wakimchagua kuwa mbunge wao," alisema Mpangala. Alisema kuwa asilimia kubwa ya Watanzania ni masikini, hivyo wanaosimama majukwaani kuomba kura wanatakiwa kulifahamu hilo. Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Bashiru Ally alisema kuwa siasa za namna hiyo ni za kawaida katika kampeni nyingi nchini.
"Tunatakiwa kujiuliza nini chanzo cha siasa za aina hii, kwanini vyama vya siasa nchini vikiwa katika kampeni vinajikita zaidi kuzungumzia watu kuliko maisha halisi ya wananchi na jinsi ya kuyamaliza?" Alihoji Ally. Alisema kuwa hata katika uchaguzi mdogo wa Igunga, yalitokea kama yanayotokea Arumeru Mashariki na kuongeza kuwa wananchi kabla ya kuamua nani wamchague, wanatakiwa kujiuliza maswali mengi juu ya siasa za kupakana matope. Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustino Mrema, alisema siasa za namna hiyo zinaweza kujenga chuki katika jamii na kwamba binafsi hawezi kuziunga mkono.
"Siasa nyingine zinajenga chuki, siasa za kinafiki siwezi kuziunga mkono, tufikie wakati tutofautishe mambo binafsi na mambo ya umma," alisema Mrema. Mrema ambaye pia ni mbunge wa Vunjo, alisema kampeni za kupigana ‘vijembe' kuwa mgombea fulani hana mke, nyumba sio wanachokitaka wananchi. "Sio Mkapa tu, wapo wengine ambao wanazungumza mambo yasiyofaa katika jamii, binafsi nadhani sio njia nzuri ya kuomba kura kwa wananchi" alisema Mrema.
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Samwel Ruhuza aliwataka Watanzania kuwapopoa mawe viongozi wa vyama vya siasa nchini wanaojikita kuzungumzia watu badala ya kujikita katika mikakati ya kuendeleza sehemu husika. "Nilimshangaa sana Rais Mstaafu Mkapa, badala ya kuzungumza sera, anazungumzia watu, sasa kauli yake hiyo itaweza kuwasaidiaje wananchi? Umefikia wakati wa kuacha ‘mipasho' katika kampeni, sasa kama sio mtoto wa Nyerere, alitaka wananchi wafanyaje?" Alihoji. Alisema kuwa hata kitendo cha CCM kusema kuwa mgombea wake akichaguliwa atamaliza tatizo la migogoro ya ardhi katika jimbo hilo, inaonyesha jinsi chama hicho kisivyokuwa na nia ya kuwasaidia wananchi.
"Sasa CCM ndio Serikali yenyewe, huku wakiwa mbele ya Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa na viongozi wengine wa mkoa, wanaeleza wazi kuwa mgombea wa CCM akichaguliwa atamaliza tatizo la ardhi pale Arumeru, huu si uhuni jamani!" alisema Ruhuza. Mwenyekiti wa chama cha UPDP, Fahm Dovutwa licha ya kusema kuwa vyama vingi vya siasa nchini havina sera zinazoeleweka, alisisitiza kuwa huenda rais mstaafu Mkapa alitoa kauli hiyo bila kukusudia.
"Unajua ukoo wa Nyerere wapo wengi sana na Mkapa asingeweza kuwafahamu wote nadhani aliteleza tu..., naishangaa sana CCM inazungumza kuwa itatekeleza baadhi ya mambo kama mgombea wake akichaguliwa kuwa mbunge, ina maana asipochaguliwa kila kitu kinabaki kama kilivyokuwa awali?" Alihoji Dovutwa.
Naye mwenyekiti wa chama cha Sauti ya Umma (SAU), Paul Kyara, alisema umefikia wakati kwa vyama vya siasa kujikita zaidi kuzungumzia matatizo ya wananchi na kwamba majibizano, kejeli na kunyosheana vidole, havina manufaa kwa taifa.
Gazeti la Mwananchi