Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,483
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba,Jaji Joseph Warioba.
Na Waandishi wetu
21st March 2014
Baadhi ya Wajumbe wa Bunge la katiba kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameipongeza hotuba ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.
Seleman Jafo, alisema Jaji Warioba ameibua vitu vingine ambavyo hajawai kuvisikia tangu awe mwanasiasa na kwamba msimamo wake mpaka sasa ni kusimamia ukweli bila kuangalia maslahi ya Chama chake anachotoka.
Alisema kuwa Jaji Warioba ameweka wazi na kufanya mustakabali wa taifa hili unaweza kwenda sehemu ambayo sio nzuri endapo hatua za haraka hazitachukuliwa kuhusiana na suala hilo la Muungano.
Jaji Warioba hakuwa na kosa lolote amewasilisha maoni ya wananchi, sasa iliyobaki ni juu yetu sisi kufanya maamuzi na mimi nitakuwa mkweli daima kusimamia ukweli katika hili sitoogopa Chama hayo ndio maoni yangu, alisema Jafo ambaye ni Mbunge wa Kisarawe.
Paulo Kimiti alisema kuwa licha ya kuunga mkono hotuba ya Jaji Warioba, lakini vitu alivyoeleza vyote ni vya msingi katika mustakabali wa Taifa.
Alisema kwa mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 2010, kutambua Zanzibar ni nchi huru ndani ya Muungano kunaufanya Muungano kuwa wa nchi mbili na serikali mbili badala ya nchi moja.
Kimiti alisema kinachopaswa kufanywa sasa na wajumbe wa bunge hilo ni kujadili rasimu bila ushabiki wa vyama na makundi.
Innocent Kalogeris, Mbunge Morogoro kusini, CCM alisema taarifa aliyotoa Jaji Warioba inadhihirisha udhaifu wa uongozi kwani tayari katiba imevunjwa, lakini kinachotakiwa ni kufanya marekebisho ya kusaidia kuimarisha Muungano na sio kuanzisha Serikali tatu.
Ezekiel Maige, alisema Rasimu iliyowasilishwa inahitaji kufanyiwa marekebisho makubwa na Bunge hilo kwa kuwa haijaziba mianya ya upotevu wa rasilimali za nchi.
Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, zimeunga mkono hotuba ya Jaji Warioba.
Akizungumza waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Msemaji Mkuu wa Jumuiya hiyo, Rajabu Katimba, alisema:
Tulipendekeza katiba mpya ya Serikali tatu na huu ndio msimamo wetu kwamba muungano wetu wa Serikali tatu uwe na Serikali ya Tanganyika, Serikali ya Zanzibari na Serikali ya Muungano, alisema.
Imeandikwa na Enles Mbegalo, Dar, Ashton Balaigwa na Emmanuel Lengwa, Dodoma.
CHANZO: NIPASHE