Wabunge EAC wampongeza Magufuli kutumbua majipu

singidadodoma

JF-Expert Member
Nov 11, 2013
4,394
1,531
WABUNGE wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kutoka Tanzania wamesema hatua zinazochukuliwa na Rais John Magufuli kutumbua majipu hasa katika Bandari ya Dar es Salaam zimezipa matumaini nchi wanachama kuwa bandari hiyo itafanya kazi zake kwa ufanisi.

Bandari ya Dar es Salaam imekuwa ikitumiwa na nchi za Rwanda, Burundi na Uganda kwa kupitisha mizigo yake kutoka hapa nchini na Kenya.

Akizungumza jana na waandishi wa habari mara baada ya kukutana na Spika wa Bunge, Job Ndugai, Mbunge wa Afrika Mashariki, Shyrose Bhanji alisema Bunge la EAC lilishatoa pongezi kwa hatua hiyo ya Rais Magufuli kutumbua majipu.

“Tumekuja hapa kwanza kumpongeza Spika kwa kuchaguliwa, lakini pia kufikisha salamu zetu kutoka kwa Bunge la EAC kuwa tumeridhishwa kwa kiasi kikubwa na kasi ya utendaji kazi wa Rais John Magufuli,” alisema Shyrose.

Alisema, kutokana na kutumbuliwa majipu hayo chini ya mfumo wa kufanya ziara za kushitukiza anazofanya, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, umma wa Watanzania umetambua namna ambavyo baadhi ya watendaji katika taasisi hiyo nyeti walikuwa wanafuja mali za umma.

Kuhusu Ndugai, Shyrose alisema, wabunge hao ambao jimbo lao la uchaguzi ni Bunge la Tanzania, wameona vema kwenda kumpongeza kwa kuchaguliwa kuwa Spika mpya wa Bunge la 11.

Alisema, mwanasiasa huyo alistahili nafasi hiyo kwa kuwa alifanya vizuri wakati akiwa Naibu Spika.

Aliongeza kuwa, pamoja na pongezi hizo, wameona ipo haja ya mambo yanayojadiliwa ndani ya Bunge la EAC yawe yanafikishwa pia kwenye Bunge la nchini kuwapa fursa wabunge kujua kinachoendelea ndani ya jumuiya hiyo.

Kwa upande wake, Ofisa Habari Mkuu wa Bunge, Owen Mwandumbe akizungumza kwa niaba ya Spika alisema, Ndugai amewahakikishia kuwapa ushirikiano wa kutosha watekeleze majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
 
Back
Top Bottom