Vijana wa kileo na uuzaji wa dawa za kuongeza nguvu za kiume

DustBin

JF-Expert Member
Jun 3, 2021
544
558
Maisha yamebadilika sana hata hapa kwetu Tanzania. Pesa imekua ngumu mtaani, vyuma vimekaza kama wanavyosema vijana. Ajira zimebana vijana wengi hawana kazi. Katika kujikwamua na changamoto hizo limezuka kundi kubwa la vijana wengi wao wakiwa wahitimu wa vyuo vikuu kujiingiza kwenye shuguli ya kutengeneza na kuuza dawa za kuongeza nguvu za kiume bila kujali hawana ujuzi juu ya fani hiyo ya kitabibu.

Tiba mbadala (tiba ya dawa asili) ni fani ya kitaalamu inayoitaji mhusika (muuzaji) awe na ujuzi wa kutosha kwani ni fani inayohusu afya za watu na maisha yao kwa ujumla. Sina hakika kama hospitali wamekosa kabisa dawa za kutibu ugonjwa huu sugu kwa wanaume wa kileo, ugonjwa wa upungufu wa nguvu za kiume. Maana madaktari wa tiba mbadala wamelishikia bango sana hili la kutibu ugonjwa huu sugu.

Baada ya kutambua kuwa watu wengi leo hii wanasumbuliwa na tatizo sugu la upungufu wa nguvu za kiume, vijana wameona hiyo ndio fursa ya wao kujiongezea kipato. Na kweli dawa zinauzika kwa kasi kubwa sana, na hata wengine na ndio wengi huuza zisizokua dawa. Shuguli hiyo imeingiliwa na matapeli wa mjini wanachanganya viungo vyao vya tangawizi, vitunguu thoumu, iliki na karafuu wakichanganya na asali basi wanaanza kuinadi na kuuza kuwa ni dawa ya kuongeza nguvu huku wakizipa majina tofauti tofauti ya kuvutia kama vile jembe, mashine, tatu bomba, kibamia, dume la shoka, kombora, mkwaju, nzahea, fataki, nk. Ni jambo jema kuona vijana wamejiajiri katika sekta binafsi kwani imepunguza kundi la wengi wanaoishi bila ya kuwa na kazi ya kufanya.

Wengine wakaendana na ukuaji wa teknolojia, biashara hii inafanywa kwenye mitandao (online) na wenyewe wanasifia kwamba hii biashara inalipa sana. Sio kama ninapinga uuzwaji wa dawa hizo, au ninawavunja moyo vijana walioamua kujikwamua kimaisha kwa shuguli hiyo, au kuua soko la dawa za nguvu za kiume, Hapana! Angalizo langu ni juu ya uwezo wa dawa zinazouzwa na hawa vijana ambao wengi wao hawana weledi wa mambo ya tiba za asili. Maadamu wamejua soko lipo basi wanaenda mbio kufanya kila liwezekanalo wakuvutie mteja uweze kununua bidhaa zao na kwa hakika wanavuna pesa sio mchezo. Lakini matokeo yake ni hasi, kwa sababu dawa zinazouzwa na kusambazwa na vijana wengi hazina ubora na uwezo wa kutibu tatizo hilo. Kinachoangaliwa ni namna ya mtu kuvuna pesa tu na sio kutatua tatizo la mteja.

Hivyo ninatoa wito kwa watu wote, hasa wanaume wenye mazoea ya kutumia hizi dawa kuweni makini. Mnaibiwa, hakikisha anaekuuzia dawa ni kweli ni mtaalamu wa elimu ya mambo ya tiba asili na sio kishoka. Wahudumu na madaktari wa kweli wapo, chukueni dawa kwao na sio kila unaeona ametuma tangazo kwenye mtandao unachukua namba na kuomba akutumie mzigo. Vinginevyo hayo madawa mnayojishindilia mtasababisha matatizo mengine mwilini na baada ya muda baadae habari ikalala moja kwa moja badala ya kuiimarisha.

Lakini pia wito kwa Serikali kuwatambua watoa huduma hii na kuwapa vibali ili watambulike. Vinginevyo afya zetu zinakuwa mashakani kwa kupata tiba isiyo ya uhakika kwa hawa wakunga wasioaminika ambao leo hii wamekithiri. Au kwenye vituo vya afya vya serikali kuwepo kitengo maalumu cha tiba mbadala hususani kuhusu magonjwa ya aina hii ya kukosa au kupungua nguvu za viungo vya kibaiolojia.

Leo sijichoshi kwa kuandika sana. Hayo yanatosha.

DustBin
 
Back
Top Bottom