Vijana na maendeleo ya taifa

heroone

Member
Dec 15, 2011
24
3
Natambua fika kuwa sisi vijana tunakumbana na matatizo mengi, tunazo changamoto nyingi zinazokwamisha kabisa jitihada zetu za kufika kilele cha mafanikio. Changamoto hizo hupelekea baadhi yetu kukata tamaa huku wakiamini kuwa mafanikio siyo sehemu ya maisha yao. Lakini leo hii naomba sote kwa pamoja tuungane, tushikamane, tuongozane ili tu kwa pamoja tufikie mafanikio tunayoyaota kila kukicha.


Naomba tuamini kuwa kesho hujengwa na leo na vijana ndiyo samadi ya mafanikio katika taifa lolote lile.
Kwa nadharia kabisa vijana tunaonekana tumesahaulika lakini kivitendo naomba niweke wazi vijana tumejisahau wenyewe na ndiyo sababu inayotufanya tuendelee kuwa tegemezi. Hivyo leo nawaomba vijana wenzangu tuamke na kwa nguvu zetu, kwa wepesi wetu na wingi wetu tushiriki katika shughuli zote za maendeleo hasa zilizo nyanja za kufanya maamuzi yanayotuhusu.


Kushiriki kwetu ndiko kutaondoa changamoto, kero, matatizo na vikwazo vya mafanikio yetu katika nyanja zote za maendeleo. Tufahamu kuwa maendeleo hayaletwi na mtu mmoja, “maendeleo ni matokeo ya kuunganisha nguvu za watu, akili na ujuzi.” Ni wazi kuwa ushiriki wetu katika nyanja za maendeleo ni wa kubabaisha sana. Inawezekana kabisa ushiriki wetu huu ndiyo ikawa chanzo cha sisi kuendelea kuwa tegemezi kwa kila jambo. Pia inawezekana kabisa ushiriki huu mdogo na wa kubabaisha unasababishwa na uoga kwa baadhi yetu huku wengine wakiamini muda wao bado haujafika.


Naomba niwatoe uoga vijana wenzangu na niwaase kuwa kundi la vijana ndilo kundi pekee ambalo linaweza kuleta mabadiliko chanya ya kifikira na si kundi jingine. Hivyo tunalojukumu na wajibu wa kujitolea kuipigania nchi yetu dhidi ya wale wote wasio na dhamira ya kweli. Na moja kati ya njia ya kizalendo na kishujaa ya kuipigania nchi yetu ni kuomba dhamana ya uongozi kuanzia ngazi ya udiwani mpaka ubunge badala ya kuendelea kulalamika kuwa watawala wa sasa hawatimizi matakwa yetu ya kila siku.


Nia nyingine ya kizalendo na ya kishujaa ya kuihami nchi ni ile ya kushiriki kikamilifu, kinadharia na kivitendo katika mchakato mzima wa uchaguzi kwa kupigia kura vijana wenzetu ambao wamejitolea dhamana ya kutaka kutuongoza kutoka hapa tulipo na kutupeleka kwenye nchi ya mafanikio. Ndugu zangu, vijana wenzangu tuwaunge mkono vijana wenzetu, tuwape nauli hiyo, tuwatume wakatutumikie ili kesho tusijilaumu wenyewe. Naomba tukumbuke kuwa mafanikio yetu ya kesho ni matokeo ya nguvu zetu tulizoziunganisha leo. Tushiriki katika siasa ili tuongeze nguvu ya kutuamulia mawazo yetu wenyewe.


Na njia ya tatu na muhimu kabisa ni kushiriki kikamilifu na kwa ukaribu wa hali ya juu katika mchakato mzima wa kuundwa kwa katika mpya. Ni haki yetu ya msingi kabisa kushiriki na ni wajibu wetu kushiriki, kwani katiba ndiyo chombo ambacho kitalinda haki zetu na uhuru wetu.


Ndugu zangu vijana, tutambue kuwa kudorora kwa uchumi barani afrika kunatokana na kukosekana kwa nguvu kazi. Ushiriki wetu katika shughuli za kiuchumi bado si wa kuridhisha sana kwani kiwango cha ajira katika taasisi za serikali na zile za binafsi hakiridhishi sababu ni vijana wachache sana waliobahatika kuajiriwa huko. Wengi ambao hawajapata bahati hiyo wao wamekimbilia katika shughuli za umachinga, ukuli huku wakina dada wakiangukia kwenye shughuli za ubaa medi, kazi za ndani na kazi zingine zisizo lipa kipato kizuri. Pia vijana wengine huangukia katika udokozi, vibaka na ulevi wa madawa ya kulevya kwa sababu ya kukosa kazi za kufanya.


Hali hii kiujumla inadumaza uchumi wa vijana wengi sana kwani pamoja na juhudi zinazofanywa na wachache wetu lakini bado vitu kama elimu duni, ukosefu wa mtaji wa kutosha na ukosefu wa vifaa vya uzalishaji bado ni vikwazo kwa vijana na ni tatizo sugu linalokwamisha maendeleo ya vijana hasa katika nyanja hii ya uchumi pia ukosefu wa lishe bora kwa vijana na njaa pamoja na ukeketaji kwa wasichana bado ni tatizo linalokwamisha maendeleo ya uchumi wetu na wa taifa kwa ujumla. Na ili hili liweze kutatuliwa basi hatuna budi kama vijana kuongeza nguvu hasa sehemu za maamuzi muhimu yanayogusa maisha yetu ya kila siku.


Ndugu zangu, vijana wenzangu, tukumbuke kuwa pamoja na changamoto hizo zote zilizotajwa lakini kubwa zaidi ni hili la vijana kuwa waathirika wakubwa wa magonjwa hatari na yasiyo na tiba. Magonjwa kama malaria, kifua kikuu na ukimwi yamekuwa tishio hasa kwa vijana. Vijana wengi tumejisahau na kuwa watumwa wa magonjwa hatarishi. Magonjwa haya ndiyo yanayomaliza nguvu kazi yetu na kudumaza uchumi wetu. Inatakiwa ifike kipindi sote kwa pamoja tutamke “UKIMWI SASA BASI, TUNATAKA MAENDELEO ENDELEVU.”


Mwisho ndugu vijana wenzangu, hatuna budi kwa wingi wetu, kwa wepesi wetu, kwa fikra zetu, kwa utashi wetu, kwa umri wetu na kwa nafasi yetu tunaweza kabisa kuiandika historia mpya ya nchi yetu. Historia itakayobadili kabisa misamiati ya lugha yetu, historia itayorudisha furaha yetu iliyopotea miaka mingi iliyopita lakini historia hii haiwezi kuandikwa kwa uoga na usaliti. Ni wazi tunatakiwa kuwa na mioyo ya kizalendo ambayo itatusukuma kushiriki moja kwa moja katika kufanya maamuzi muhimu na magumu yahusuyo taifa letu.


Niwazi kuwa miongoni mwetu tunahitaji tuwapate wakina Nyerere wengine, Salim Ahmed Salim, Amina Chifupa wengine. Tunahitaji kuwaona watu kama James Mbatia wengi miongoni mwetu. Tunahitaji kuwaona vijana kama Martin Luther King, Malcolm X enzi za uhai wao, Abdulwaheed Sykes enzi za TAA na TANU. Tunahitaji kuwapata wakina Halima Mdee, John Mnyika na Zito Kabwe wengi katika taifa hili.
Tunahitaji kupata vijana wenye muono wa mbali, walio na moyo wa kuthubutu na waliotayari kulitetea na kulilinda taifa lao kwa nguvu zao, kwa umri wao, kwa wingi wao, kwa utayari wao na hata kwa mawazo na hoja zao.


Hatuwezi kuwapata vijana hawa kama hatutashiriki kivitendo katika nyanja zote za maendeleo. Hatuwezi kuwapata vijana hawa kama tutaendelea kuogopa naomba tutambue kuwa “uoga katika mafanikio ni sawa na umasikini” hatuwezi kuwapata vijana hawa kama tutaogopa mabadiliko. Vijana tuamke, tushikamame tena mshikamano thabiti, tushiriki na kuingia katika vyombo muhimu vya maamuzi kama hatua ya kuuenzi ujana wetu na kuilinda nchi yetu.


Nawatakia kazi njema za kuendeleza na kukuza uchumi wetu.


Imeandaliwa na Siraji Muksin (heroone)
 
Mkuu natamani ujumbe wako ungeweza kuwafikia vijana wote mmoja baada ya mwingine ausome kwa makini na kuuelewa kwani nadhani utawagusa sana na kila mmoja wetu atachukua hatua ambayo wote kwa pamoja tutafika pale ulipoleka ktk ujumbe ulopo kwenye thread yako
 
Ujumbe muhimu sana kwetu vijana kama wajenzi wa taifa.
Tunachohitaji hapa ni mapinduzi ya kifikra kama ambavyo umeeleza... vijana inabidi tuhubiriane ufahamu wa mahusiano kati ya bidii au uvivu wetu na kustawi au kudorora kwa taifa...
Tulio wengi ni ama hatulioni hilo, au tunaamua kupuuzia. Ni kweli kukua kwa uchumi na mabadiliko mengine chanya ktk jamii hutegemea juhudi za jamii yenyewe ktk kufikiri na kutenda... kwa hiyo uvivu na woga wa mtu m1 m1 una madhara makubwa sana...
Tunautumia muda vibaya. Kwa mfano mimi sasa hivi naandika reply hii nikiwa nimekaa kwenye comp kwa zaidi ya masaa 5 mfululizo, na sina mpango wa kuondoka sasa hivi, ninachokifanya - rubish, ilhali nafahamu fika kuwa ningeweza kuigawa siku ya leo na kufanya kazi fulani huko nje... ila kwa kuwa nimemwachia Mungu maisha yangu... nasema aaah itaeleweka mbele kwa mbele...
Taifa linadidimia...
Vijana Tubadilike... Naomba kuwasilisha:poa
 
Nashukuru mkuu kwa hilo cha misingi ni kujitambua sisi wenyewe kama vijana na nafasi yetu ya kuweza kubadili historia ya jamii yetu na taifa letu kwa ujumla... sisi tunatakiwa tuanze wengine (serikali na jumuiya zake) wafate... inatakiwa tufanye kila tunachokitaka huu sasa si muda wa kukaa vilingeni na kulalamika kuwa mambo hayatuendei vizuri....... huu ni muda wa vitendo kwa vijana tuamke, tushikamane tuamamue mambo yetu wenyewe katika njia iliyo ya haki na yenye manufaa kwetu na kwa taifa kwa ujumla "MAENDELEO NI MATOKEO YA KUUNGANISHA NGUVU ZA WATU, AKILI NA UJUZI" TUTAMBUE HILO KAMA VIJANA....
 
Back
Top Bottom