Wazee wastaafu ambao miaka yote hushiriki sherehe za maadhimisho ya sherehe za Uhuru, mwaka huu hawakuhudhuria, Je, hizi ni chuki na wivu tu kwa JK? ama kuna mengine zaidi? ama ni dharura tu zimeingiliana? TUJADILI
Vigogo wastaafu `wakacha`
Na Muhibu Said
10th December 2009
Yumo Mkapa, Lowassa, Sumaye na Warioba
Wengine ni Dk Salim, Dk Salmin na Malecela
Sherehe za maadhimisho ya miaka 48 ya Uhuru wa Tanganyika, jana zilifana lakini viongozi wengi wastaafu, akiwamo Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa na aliyekuwa Waziri Mkuu katika Serikali ya Awamu ya Nne, Edward Lowassa, kutohudhuria.
Wengine, ambao hawakuhudhuria ni mawaziri wakuu wastaafu, Dk. Salim Ahmed Salim, Cleopa Msuya, Jaji Joseph Warioba, John Malecela na Frederick Sumaye na Rais Mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour na Waziri Kiongozi Mstaafu, Dk. Gharib Bilal.
Hata hivyo, haikuelezwa sababu za viongozi hao kutohudhuria sherehe hizo, zilizoongozwa na Rais Jakaya Kikwete, katika Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam. Katika sherehe hizo, Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad na Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba, walikaribishwa kuketi jukwaa kuu lililotumiwa na viongozi mashuhuri (VIP) wa mihimili ya dola, tofauti na viongozi wengine wa vyama vya siasa, ambao walikaa katika sehemu za kawaida.
Baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani, walioshuhudiwa wakiwa wameketi katika sehemu za kawaida, wakiwamo mabalozi, mawaziri na wabunge, ni pamoja na Mwenyekiti wa United Democtaric Party (UDP), John Cheyo na Rais wa Tadea, John Chipaka.
Jukwaa walilokaribishwa viongozi hao wa CUF kuketi ikiwa ni mara ya kwanza katika historia ya maadhimisho hayo, ni lile aliloketi Rais Kikwete, Spika wa Bunge, Samuel Sitta na Jaji Mkuu, Augustino Ramadhan.
Viongozi wengine mashuhuri waliokaa jukwaa hilo, ni Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha, Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano, Ali Hassan Mwinyi.
Sherehe hizo zilipambwa na burudani mbalimbali, likiwamo gwaride la askari wa vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama, lililoongozwa na Brigedia Jenerali, Wilfred Kabunda.
Pia, zilipambwa na vijana wa halaiki, wasanii wa vikundi vya maonyesho ya sarakasi na ngoma za asili kutoka Uganda, Tanzania Bara na Zanzibar.
Fursa waliyopata viongozi hao wa CUF jana, imetafsiriwa na wengi kuwa ni sehemu ya utekelezaji kwa vitendo wa serikali wa maridhiano ya kuzika siasa za chuki na uhasama kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na CUF Zanzibar.
Maridhiano hayo yalifikiwa kati ya Rais Karume, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Maalim Seif, baada ya kufanya mazungumzo ya faragha, Ikulu ya Zanzibar, Novemba 5, mwaka huu.
Kabla ya Maalim Seif na Profesa Lipumba kukaribishwa katika jukwaa hilo, walifika saa 3:00 asubuhi na kuketi katika sehemu ya kawaida.
Wakati wakisubiri muda wa kuanza kwa maadhimisho hayo, viongozi wa itifaki waliwaelekeza maofisa wao kwenda kuwaondoa Seif na Lipumba sehemu hiyo na kuwakaribisha jukwaa hilo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Mohamed Seif Khatib, alipotakiwa na Nipashe kuzungumzia hatua hiyo alisema: Mimi sijui hilo, kwani mimi si kiongozi wa itifaki. Sherehe hizo zilihudhuriwa na watu mbalimbali, wakiwamo viongozi wa serikali, mashirika ya umma, mawaziri, mabalozi/wawakilishi wao, wabunge, viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama, viongozi wa dini, vyama vya siasa, kiraia, wasomi na wanaharakati wa maendeleo ya jamii na wananchi wa kawaida.
Zilianza rasmi saa 4:15 asubuhi, mara baada ya Rais Kikwete kuwasili uwanjani hapo akiwa kwenye gari la wazi akiwa ameongozana na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Jenerali Davis Mwamunyange.
Kabla ya hapo, wakati viongozi mashuhuri wakiwasili, uwanja mzima ulilipuka kwa kupaza sauti za ruksa!, ruksa!, ruksa! huku wakipeperusha bendera za taifa, alipowasili Rais Mstaafu, Mwinyi.
Rais Kikwete alipowasili gari lake lilimzungusha uwanja mzima, ambapo alitumia fursa hiyo kuwasilimia viongozi na wananchi waliohudhuria sherehe hizo kwa kuwapungia mkono.
Tukio hilo liliwavutia maelfu ya watu waliohudhuria, ambao walimshangilia kila upande wa uwanja alikopita.
Baada ya kuhitimisha zoezi hilo, Rais Kikwete alipanda kwenye jukwaa dogo maalum lililotayarishwa kwa ajili yake na kupokea salamu za heshima kutoka vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama. Akiwa amesimama katika jukwaa hilo, alipigiwa mizinga 21 kuashiria heshima kwake kama Amiri Jeshi wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama na mkuu wa nchi.
Tukio hilo lilifanyika sambamba na kupigwa wimbo wa taifa. Wakati wote huo, watu waliofurika uwanjani hapo, waliungana na Rais kusimama kutoa heshima zao kwa taifa.
Baada ya hapo, Rais Kikwete alikagua gwaride la vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama kabla ya vikosi hivyo kupita mbele yake kutoa heshima zao za utii kwake. Vikosi hivyo vilijumuisha askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wa nchi kavu, majini na anga. Wengine, ni askari wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wanaume na wanawake, Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU)-wanaume na wanawake, polisi wa kawaida (wanaume na wanawake) na Magereza (wanaume na wanawake).
Vikosi vilipita mbele ya jukwaa la VIP kwa awamu mbili tofauti kwa mwendo wa taratibu na kasi na kutoa heshima zao za utii kwa Rais.
Kivutio pekee kilikuwa kwa vikosi vya askari wanawake, ambao walishangiliwa na kutiwa moyo kwa nyimbo za wanawake na maendeleo
kutokana na ukakamavu na ushupavu wa hali ya juu waliouonyesha wakati wa gwaride. Askari wengine walioshangiliwa, ni wa JKT (wanawake na wanaume) na FFU kutokana na mbwembe na ukakamavu walivyovionyesha kila walipokuwa wakipita mbele ya Rais na mbele ya wananchi.
Hata hivyo, vituko vilitokea kwa baadhi ya askari wa Jeshi la Magereza, baada ya kofia walizokuwa wamevaa kudondoka wakati wakishiriki gwaride kwa ukakamavu wa hali ya juu.
Baadhi ya askari wa JWTZ walionekana wakisaidia kuokota kofia hizo kwa vile taratibu za jeshi haziruhusu askari aliyedondosha kitu kukiokota anapokuwa ndani ya gwaride. Tukio lingine lililojiri katika sherehe hizo, lililousu wananchi kadhaa, ambao kila baada ya dakika chache, alionekana mtu akibebwa kwenye machela, baada ya kuishiwa nguvu na kuanguka.
Watu hao walipatiwa huduma ya kwanza katika mahema ya Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross) yaliyoandaliwa uwanjani hapo.
Ukiachilia mbali matukio hayo, sherehe hizo zilipambwa na kikundi cha halaiki kilichoundwa na vijana 1,000, wakiwamo 700 kutoka shule kadhaa za Tanzania Bara na 300 Zanzibar.
Vijana hao wa halaiki, wakiwa wamevalia nadhifu mavazi ya rangi nyeusi, bluu na njano ya bandera ya taifa, waliingia uwanjani kwa mchakamchaka, kisha wakasalimia na kufanya mazoezi.
Kivutio kikubwa kilikuwa kwa vijana hao, baada ya kuunda umbo la Miaka 48 ya Uhuru na kutamka herufi moja moja, herufi zote hizo kwa pamoja na kaulimbiu ya sherehe za mwaka huu isemayo: Tulinde Uhuru na Amani kwa Maendeleo ya Taifa letu.
Vijana hao pia, waliunda halaiki ya umbo la kupiga makasia na kuvua samaki baharini, kuelezea michezo, utamaduni, kilimo kwanza, kukamua maziwa, silaha kwa ajili ya ulinzi, sarakasi, mshazari na kuimba wimbo wa Tanzania Nakupenda.
Baadaye kulikuwa na tafrija Ikulu, kuanzia saa 12:30 jioni mpaka saa 2:30 usiku ikiwa ni sehemu ya maadhimisho hayo.
CHANZO: NIPASHE