Vema serikali imewakumbuka wafugaji baa la ukame, lakini...

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
Hatimaye wafugaji waliogeuka masikini wa kutupwa baada ya ukame wa kati ya mwaka 2008-2010 kuua mifugo yao yote, sasa neema imeanza kuwashukia kutokana na Serikali kutambua janga lililowapata na hivyo kutenga kiasi cha Sh. bilioni 11.2 kwa ajili ya mradi wa uwezeshaji kwa waliopoteza mifugo ili warejee katika maisha yao ya awali.

Mradi huo unaolenga kaya 6,128 za wilaya za Longido, Monduli na Ngorongoro mkoani Arusha, tayari umezinduliwa na Rais Jakaya Kikwete wilayani Longido kwa kugawa mitamba na mbuzi kwa kaya 16, mifugo hiyo ni mbegu ili kuwawezesha wafugaji hao kuanza upya. Misaada hiyo inakwenda kwa kaya zote 6,128.

Ili kukamilisha kazi hiyo, halmashauri zote zilizoathirika zimetakakiwa kuharakisha utayarishaji wa zabuni na kuwasilisha serikalini ili fedha zitolewe kwa ajili ya ununuzi wa mifugo ya kuwapa wafugaji walioathirika.
Wakati akikabidhi mitamba hiyo kama ishara ya uzunduzi wa mradi huo, Rais Kikwete alitoa angalizo kwa madiwani, kwanza akiwataka kuwa wakali

katika usimamiaji wake ili watendaji wasiuchakachue, lakini pia alisisitiza kuwa ng’ombe wanaotakiwa kununuliwa na kupewa wafugaji ni mitamba na si ambao wameacha kuzaa.

Katika mradi huu kasi ya halmashauri katika kuitisha zabuni na kuiwasilisha serikalini ndiyo itasaidia upatikanaji wa fedha kwa haraka ili wafugaji wapewa mitamba na hivyo kuanza kujijenga upya.

Misaada hiyo pamoja na agizo la kutaka kutolewa kwa mafunzo kwa wafugaji, ili kuongeza uwezo wao wa kufuka kisasa na kupata faida kubwa zaidi huku wakilinda mazingira, ni juhudi ambazo zinategemea sana uadilifu wa wale watakaosimamia mradi huo unaolenga kuwakomboa wafugaji nchini, hususan waliopatwa na baa la ukame na kupoteza mifugo yao yote kati ya mwaka 2008-2010.

Kwanza tunaipongeza serikali kwa kufikia uamuzi huu wa kuwasaidia wafugaji hawa, ni maamuzi ambayo hayana tofauti sana na yale ya stimulus package, yaliyolenga kusaidia kampuni za kununua mazao ya wakulima, hususan pamba, ambao yalifilisika kutokana na mdororo wa ukiuchumi ulioikumba dunia mwaka 2008. Hizi hapana shaka ni hatua ambazo zilikuwa zinasubiriwa kwa shauku kubwa na wafugaji hao.

Rais alitoa angalizo kwa madiwani ili wawe wakali na kuwasimamia watendaji wa serikali katika halmashauri wakati wa utekelezaji wa mradi huo kwa sababu katika miaka ya hivi karibuni imekuwa ni kama fasheni kwa miradi ya serikali kuhujumiwa na watumishi wake wenyewe.

Hujuma hizi ziko za aina nyingi, yawezekana ni wakati wa uitishaji na utoaji wa zabuni, yawezekana ni wakati wa utekelezaji wa mradi au hata wakati wa usimamizi tu; katika hatua yoyote kati ya hizi watu wanaweza tu kuzembea si kwa bahati mbaya, ila kwa makusudi ili kutoa mwanya kwa faida binafsi miongoni mwa wasimamizi.

Ni kwa kutambua ukweli huo Rais Kikwete aliwataka madiwani kusimamia mradi huo ili walengwa ambao ni wafugaji wanufaike na si kuzidi kutunisha matumbo ya watumishi wasio waaminifu. Tunatambua kuwa angalizo hili lina mashiko kwa kuwa taarifa za ubadhirifu, hujuma na vitendo vingi vya

ukiukaji wa taratibu, kanuni na sheria za manunuzi na matumzi katika halmashauri nchini si jambo la uficho tena.
Mwaka baada ya mwaka taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zimethibitisha udhaifu huu katika halmashauri nyingi,

kamati za udhibiti za Bunge nazo mara kadhaa zimethibitisha haya pia, kwamba ndani ya watumishi wa serikali wapo mchwa wanaokula fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi na matokeo yake ni kuzidi kuongezeka kwa umasikini nchini.

Kwa bahati mbaya sana, mradi wa kuwasaidia wafugaji unalenga kundi la watu walioathirika mno na janga la ukame, ni watu waliogeuzwa kuwa masikini wa kutupwa, lakini baya zaidi ni watu ambao kwa hakika hawana elimu kubwa na kugundua kwa urahisi vitendo vya kilaghai vya watu waliozoea kugeuza kalamu kwa manufaa yao binafsi.

Ndiyo maana Rais amewataka madiwani kuwa macho ya wafugaji hao ili Sh. nilioni 11.2 zisije kuishia mikononi mwa wajanja wacheche ndani ya ofisi za umma badala ya kuwakomboa wafugaji waliopigika sababu ya ukame. Tunapongeza hatua zote za kuwakumbuka wafugaji hao, lakini pia tungependa vyombo vingi vya serikali vielekeze macho katika mradi huu ili usije kugeuzwa epa ndogo ya watumishi wa halmashauri husika.

CHANZO: NIPASHE

 
Back
Top Bottom