Upendo Peneza ''siku 30 Mgodi wa (GGM) kuwalipa fidia wananchi wanaoishi ndani ya Mgodi

R.B

JF-Expert Member
May 10, 2012
6,296
2,573
ggm4.jpg


Mbunge wa Viti Maalum Geita (CHADEMA), Upendo Peneza, akizungumza wakati wa kikao baina ya Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani na wawakilishi wa wananchi wa Geita wakiwamo wabunge na madiwani husika kuhusu malalamiko mbalimbali kutoka kwa baadhi ya wananchi wanaoishi jirani na Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kwamba shughuli zinazofanywa na Mgodi huo zinawaathiri kwa namna mbalimbali.

Serikali imetoa siku 30 kwa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kuwalipa fidia wananchi wanaoishi ndani ya eneo la leseni ya Mgodi huo au kuwaruhusu rasmi waendelee kuishi humo na kufanya shughuli za kiuchumi.


Sambamba na agizo hilo, pia Serikali imeupa Mgodi huo siku 14 kuziba Tuta lililopasuka ambalo huzuia maji machafu kutoka Mgodini yasiende katika makazi ya wananchi.

Aidha, kufuatia taarifa iliyowasilishwa na timu ya wataalam wa mitetemo kutoka Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST), baada ya kukamilisha kazi waliyopewa kutafiti chanzo cha mipasuko ya baadhi ya nyumba za wananchi na majengo mbalimbali yaliyo jirani na Mgodi wa GGM, Serikali imeagiza timu hiyo kufanya tathmini maalum ya idadi ya waathirika.

Iliagizwa kazi hiyo ifanyike kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, Kitengo cha Maafa na Kitengo cha Mazingira pamoja na uongozi kuanzia ngazi za vijiji mpaka madiwani na wabunge husika kwa muda wa siku Saba tu kuanzia tarehe 29 mwezi huu na kuiwasilisha serikalini ili hatua stahiki zichukuliwe.

Maagizo hayo yalitolewa hivi karibuni mjini Geita na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani katika kikao chake kilichomshirikisha Mkuu wa Mkoa wa Geita na wawakilishi wa wananchi wa Geita wakiwamo wabunge na madiwani.

Dkt Kalemani alisema kuwa maagizo hayo ni kufuatia maelekezo aliyoyatoa mapema mwezi Februari mwaka huu alipotembelea mkoani humo na kusikiliza kero za wananchi wa vitongoji vya Katoma na Nyamalembo. Alisema maagizo hayo yasipotekelezwa ipasavyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa, chini ya sheria ya madini na sheria nyingine za nchi.

Akifafanua zaidi kuhusu masuala hayo yaliyosababisha Serikali kufikia hatua husika, Naibu Waziri alisema kuwa mwezi Februari alipotembelea Geita, wananchi walieleza kero kubwa walizokuwa nazo kuwa ni baadhi ya nyumba zao kupasuka kiasi cha kutoweza kukalika na nyingine kukalika lakini zimeharibika kutokana na ulipuaji wa baruti (blasting) wa Mgodi wa GGM.

Malalamiko mengine yalihusu wananchi ambao wanaendelea kuwa na makazi ndani ya eneo la leseni ya GGM, ambayo ina ukubwa wa kilomita za mraba 196. 7 ambao walikuwa wanadai fidia ili waondoke katika eneo husika au waendelee kubaki na kufanya shughuli zao za maendeleo.

Pia, baadhi ya wananchi wanaoishi karibu na Mgodi na hasa maeneo ya chini ya Mgodi, walilalamikia maji machafu ambayo yalikuwa yanakingwa na tuta ambalo lilikuwa limebomoka na kuruhusu maji kutiririka kuelekea kwenye makazi yao na hivyo kuwepo uwezekano wa kuathiri afya zao. Walitaka hatua madhubuti zichukuliwe kuzuia mtiririko huo wa maji.

Alisema kuwa, baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote mbili, kwa suala la mipasuko, aliunda timu ya wataalam wa Serikali kutoka GST na kuiagiza kufanya utafiti wa kisayansi ili kubaini chanzo cha mipasuko husika kwa kushirikiana na wawakilishi wa wananchi wa maeneo hayo.

Timu hiyo ilikamilisha kazi hiyo na kukabidhi taarifa yake kwa Serikali mwezi Julai mwaka huu ambapo ilibainisha vyanzo vikuu viwili vya mipasuko hiyo kuwa ni udhaifu wa majengo yaliyoathirika lakini pia milipuko inayofanywa na GGM hasa ya miaka ya nyuma hususan kuanzia mwaka 2007 hadi 2010 ambayo ilikuwa na kipimo cha juu cha mitetemo kinachofikia 57.

Kuhusu wananchi wanaoishi kwenye eneo la leseni, Dkt Kalemani alisema kuwa alimwagiza Afisa Madini wa Geita kuwaandikia GGM ili wathibitishe kwa maandishi kati ya kuwaondoa wananchi wale kwa kuwafidia kama eneo hilo lilivyo kwenye leseni yao au kuwaruhusu waendelee kuishi na kufanya shughuli za maendeleo, jambo ambalo Mgodi haukutekeleza badala yake walisema wananchi hao ni wavamizi.

Aidha, kuhusu suala la Tuta, Naibu Waziri alieleza kuwa, aliagiza lizibwe mara moja ili kuepusha madhara ambayo yangeweza kujitokeza kama maji yangeendelea kutiririka kuelekea kwenye makazi ya wananchi, ambalo pia halijatekelezwa hadi sasa.

“Ni kutokana na hali hiyo, sasa Serikali tumeona tutoe maagizo ya mwisho ili yatekelezwe na yasipotekelezwa, hatua kali za kisheria zitachukuliwa.”

Naibu Waziri alisema kuwa Serikali haina nia mbaya kwa Mgodi husika isipokuwa ni wajibu wa Serikali kuhakikisha pia sheria zinafuatwa ili pande zote zipate haki stahiki.

“Tunapenda sana wawekezaji muwekeze kwa sababu ndiyo mnatupa ajira, mnalipa mirabaha na kodi lakini lazima tuzingatie sheria.”

Dkt Kalemani alizitaka Mamlaka zinazohusika kusimamia zoezi hilo kikamilifu.
 
Back
Top Bottom