Unaikumbuka Milambo!!!!!!!!! Hebu Kumbuka

Ufipa-Kinondoni

JF-Expert Member
Jan 3, 2012
4,582
2,783
Wednesday, September 5, 2012

NJAA YETU ILIIOKOA MILAMBO KUSHUKA DARAJA BAADA YA KUTEMBEA KWA MIGUU KM 16


Timu ya soka marufu kuwahi kutokea hapa mkoani Tabora ilikua ni Milambo,timu hii ilianzishwa mnamo mwaka 1990 na aliyekua mkuu wa mkoa marehemu Dr Lawlence Mtazama Gama, Lengo kuu hasa la kuianzisha timu hii lilikua ni kutafuta namna ya kuwa na timu ya ligi ya daraja la juu mkoani hapa,Dr Gama mara tu baada ya kuteuliwa kuwa mkuu wa mkoa wa huu aliviamulu vilabu vyote kutoa wachezaji wao nyota kwa lengo la kutengeneza kombani ya Tabora ambayo ilipewa jina la Milambo na kuanza kushiriki ligi daraja la tatu. Miongoni mwa wachezaji waanzilishi wa timu hii alikua ni beki Dioniz Paul na hapa ananiadithia moja kati kituko ambacho kamwe hatakisahau katika maisha yake ya kuichezea Milambo ambayo kwasasa haipo tena kwenye ramani ya soka,
Dioniz Paul akiwa uwanjani.

Dioniz Paul hapa anaanza kunipa hadithi hiyo '
Mnamo mwaka 1994 nilikuwa mmoja wa wachezaji muhimu na nahodha wa kikosi cha timu ya mkoa wa Tabora - Milambo. Huu ni msimu ambao ni vigumu sana kuja kuusahau kwenye maisha yangu kwa sababu vitu kadhaa ambavyo nitavielezea kwenye makala haya.
Nakumbuka msimu huo timu ilikuwa chini ya ofisi ya mkuu wa mkoa wa Tabora, na kiukweli hatukuwa tumecheza vizuri sana kwenye ligi na mpaka ligi ikiwa inaelekea mwishoni kulikuwa na kuna uwezekano mkubwa wa timu yetu ya Milambo kushuka daraja - kutoka la kwanza mpaka la pili.
Zikiwa zimesalia mechi tano ligi kuu kuisha uongozi wa mkoa na timu kwa ujumla walishaanza kutukatia tamaa. Nakumbuka tulikuwa tumebakiwa na mechi dhdi ya Ushirika Moshi, Ndovu ya Arusha, Reli Morogoro, Simba SC, na mechi ya mwisho ilikuwa dhidi ya RTC ya Kagera. Mechi zote hizi zilikuwa za ugenini kasoro mechi dhidi ya RTC Kagera tu ambayo ndio tucheze nyumbani kwenye dimba la Ali Hassan Mwinyi.
Tukaenda kanda ya Kaskazini kucheza mechi dhidi ya Ushirika Moshi tukafungwa na tukarudi Arusha napo tukapigwa na hivyo tukazidi kupoteza matumaini ya kuweza kubaki kwenye ligi daraja la kwanza. Mpaka wakati huo tulikuwa tunashika nafasi ya 14 kwenye ligi ya timu 16.
Tuliporudi nyumbani Tabora tukawa tumeweka kambi kwenye chuo cha kilimo na mifugo cha Tumbi. Tukiwa kule kambini huku nyuma uongozi wa mkoa chini ya Dr Lawrence Gama kwa kuwa walishakata tamaa ya timu kubaki kwenye ligi daraja la kwanza kwani walikuwa wanajua kwamba tunakabiriwa na mechi ngumu mbili dhidi ya timu zilizokuwa imara sana wakati huo Simba na Reli. Hivyo kutokana na kulifikiria hilo uongozi wa mkoa ukaja na hoja moja kwamba kuliko kupoteza fedha kwenda Morogoro na Dar es Salaam kucheza na Reli na Simba na huku tukijua tunaenda kufungwa ni bora tubaki tu Tabora na kujiandaa na mechi yetuya mwisho dhidi ya RTC Kagera.
Yakiwa yamebaki masaa kadhaa kabla ya safari ya kwenda Morogoro, uongozi wa mkoa ukiongozwa Dr Gama ukaja kambini na kutueleza kwamba wameona ni bora tusisafiri na kwenda huko kupoteza fedha, nguvu na muda kwa sababu tulikuwa tunaenda kufungwa. Hivyo wakatupatia posho ya shilingi 7,000 kila mchezaji na kutupa ruhusa ya kuendelea kubaki kambini au kwenda majumbani kwa ajili ya kujiandaa na mechi ya mwisho dhidi ya RTC Kagera.
Uongozi wa mkoa ulipoondoka kambini mimi kama nahodha na mchezaji mwenzangu Said Bundala tukapata wazo la kijasiliamali la kupiga hela nyingi zaidi ya zile 7000 tulizopewa na uongozi wa mkoa. Wazo lenyewe lilikuwa na kujichanga wachezaji wote 25 tupate nauli na kwenda kucheza mechi za Reli na Simba na ile fedha ya mgawanyo wa mapato ya mlangoni tungeichukua wenyewe wachezaji. Wazo letu likakubaliwa na wenzetu na mpaka muda huo ikawa ni saa mbili usiku, na huku treni ya kwenda Morogoro mpaka Dar ilikuwa inaondoka saa tano usiku. Kwa maana hiyo tulikuwa tuna masaa matatu ya kutoka Tumbi kwenda stesheni ambapo kuna umbali wa kilomita 16.
Basi wachezaji wote 25 tukabeba vifaa vyetu tukatembea kwa miguu mpaka stesheni kwa bahati nzuri tukakuta treni ndio inajiandaa kuondoka - tukaiwahi na kuingia kwenye treni bila kukata tiketi. Tukiwa tumesimama kwenye korido ya treni akaja mkata tiketi na tukamwelezea kwamba sisi ni wachezaji wa Milambo tulikuwa tunawahi kwenda Morogoro kucheza mechi hivyo akatuelewa. Tukachanga shilingi 1000 wachezaji tukapata 25,000 na tukalipa nauli
Hussein Masha wa Simba akitafuta mbinu ya kumtoka Dioniz Paul.

Tukiwa kwenye treni tukakutana na mganga wa kienyeji ambaye alikuwa nae anaenda kijijini kwake Morogoro, katika mazungumzo yetu akatushawishi atufanyie mambo tushinde mechi zetu zote tunazoenda kucheza kwa malipo japo yalikuwa sio makubwa. Tukakubali na tukaanza kufanya nae mambo.
Safari ikaendelea na tukafika Morogoro saa nane mchana tukiwa tumebakiwa na masaa mawili tu kufika uwanjani kwa ajili ya mechi. Basi tukaamua kufikia gesti moja hivi pale Morogoro lakini tukawa hatuna fedha za kutosha kulipia, hivyo tukaamua kuchukua vyumba viwili kwa mkopo tukiwa tunaamini baada ya mechi tutapata fedha ya kulipia na kuchukua mizigo yetu.
Wakati huo huo sie bila kufahamu uongozi wa mkoa wa Tabora ulishatoa taarifa kwenye vyombo vya habari kwamba timu haitoweza kusafiri kwenda Morogoro na Dar kucheza na Simba na Reli kutokana na ukata. Gazeti la Uhuru likachapisha habari hiyo hivyo watu wakawa wanajua kwamba timu haitoenda uwanjani.
Reli kwa upande wao wakaenda uwanjani kukamilisha taratibu na waweze kuchukua pointi zao mbili za bure. Huku zikiwa zimebaki dakika kadhaa kabla ya refa kuwapa ushindi wa bure Reli - Milambo hao tukaingia uwanjani. Kile kitu kiliwashangaza sana wenyeji wetu Reli, kwa sababu hawakuwa na utayari wa mchezo kwa kuwa walijua Milambo hatutoenda uwanjani basi tukacheza nao na kufanikiwa kutoka nao sare ya bila kufungana.
Mechi ikaisha na kwa bahati mbaya upande wetu uwanja ulikuwa mtupu kwani mashabiki walikuwa na taarifa Milambo haitoenda uwanjani kama ilivyochapishwa na gazeti la Uhuru. Kwa maana hiyo hatukapata kitu katika mapato ya mlangoni ambayo ndio yalikuwa chanzo cha kusafiri kutoka Tabora kwenda Morogoro kucheza na Reli na Dar dhidi ya Simba.
Mechi ilipoisha tukarudi kwenye gesti tuliyofikia kupumzka na kupanga namna ya kwenda Dar es Salaam. Bahati nzuri tukapata gari aina ya Coaster ambayo tuliongea nao vizuri watupeleke Dar kwa mali kauli kwamba tukicheza mechi yetu na Simba tutawalipa.
Basi wale jamaa wakakubali, timu ya wachezaji 25 na mganga wetu tukasafiri mpaka Dar. Tukafikia gesti moja hivi maeneo ya Manzese. Tukalala na kesho yake tukashinda na njaa jioni tukaenda uwanja wa Taifa kucheza na Watoto wa Msimbazi ambao kipindi hicho walikuwa wanatisha sana na sio tu Tanzania mpaka Afrika nzima. Ikumbukwe Simba hiyo ndio iliyokuwa imetoka kucheza fainali ya kombe la CAF na kufungwa na Stella Abdjan msimu mmoja kabla.
Walikua na wakali kama Mohamed Mwameje, George Masatu,Hussein Masha,Nteze John na wengineo.
Mechi ikaanza huku mganga wetu akifanya kazi yake kama kawaida. Mpaka kipindi cha kwanza kinaisha matokeo yalikuwa sare. Kipindi cha pili kilipoanza dakika kadhaa mbele beki wa Simba Kassongo Athumani akamchezea rafu mchezaji wetu Salim Lyandungu kwenye eneo la penati, na mwamuzi akaamulu upigwe mkwaju wa penati. Said John akaweka mpira kimiani na kumfunga Mohamed Mwameja.
Mechi ikaendelea na Milambo tukawa bora zaidi ya Simba, na mambo yalipozidi kuwa magumu viongozi wa Simba wa wakati huo wakaanza kwenda nyuma ya goli na kuanza kumlaghai golikipa wetu Peter Poka.
Poka akalainika bwana, Abdul Mashine akapanda na mpira na kupiga shuti kali sana lakini Poka akalifuata na kudaka kisha kumtemea kwa kusudi Juma Amir Maftah lakini akashindwa kufunga akapaisha mpira ule.
Baada ya kuona Peter Poka kafanya ule upumbavu tukamfuata na kuanza kumpiga mikwara asirudie kufanya vile. Mpira ukaendelea na hatimaye mechi ikaisha Simba 0 - 1 Milambo.
Ukafika muda ambao wote ndio tulikuwa tunausubiri - muda wa mgawanyo wa mapato ya mlangoni tukapata mgawo wa millioni 2 na tukagawana wachezaji wote shilingi 80,000 kila mmoja na baada ya hapo tukatoa kiasi cha 20,000 kila mmoja ili kuweza kulipa madeni tuliyokuwa tunadaiwa kuanzia mganga, gari iliyotuleta Dar, gesti ya Manzese, na ile gesti tuliyoacha vitu vyetu jule Morogoro.
Tunashukuru kupata kiasi kile cha pesa kwasababu baadhi ya wachezaji ndio walikaa magetini ili kusimamia mapato
Basi tukarudi Morogoro, na kufika kule kumbe huku nyuma baada tu ya mchezo wa Reli uongozi wa mkoa ukapata taarifa kwamba wachezaji tulitoroka na kuja wenyewe kucheza mechi zile mbili dhidi ya Reli na Simba. Hivyo tukiwa pale Morogoro Mkuu wa mkoa akatukatiwa wachezaji wote 25 tiketi za treni daraja la pili na tukaanza safari yetu ya kurudi Tabora tukiwa na pointi zetu 3 kibindoni.
Tulipofika Tabora tulipokelewa kwa mbwembwe sana mpaka bendi ya Tabora Jazz iliitwa kutumbuiza. Mkuu wa Mkoa marehemu Dr Lawrence Gama akatupongeza sana kwa kitendo kile cha kishujaa tulichofanya bila yeye kujua kwamba wenzie tulifuata mapato ya mlangoni kama kipaumbele chetu cha kwanza.
Basi timu ikaingia tena kambini kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa mwisho wa ligi daraja la kwanza dhidi ya RTC Kagera. Mungu sio Athumani tukashinda mchezo wetu dhidi ya RTC bao 1-0 na kuweza kubaki kwenye ligi huku tukiwashusha RTC Kagera.
Hivi ndivyo njaa zetu za fedha zilivyoisaidia Milambo kubaki ligi ya daraja la Kwanza mwaka 1994.

Source: Saffih Dauda Blog.
 
Uongozi wa Rage katika chama cha Mpira Tabora ilikuwa changa la macho. Gia ilikuwa kuingia mjengoni. Angalia watu waliokuwa na moyo wa kuendeleza michezo Tz ni pamoja na huyu mkuu wa mkoa.
 
duhu kastori katamu, pamoja na njaa zenu bado mlistahili pongezi kwa ujasiri wenu.!!
 
Back
Top Bottom