Ukatili!! Akatwakatwa na mumewe kwa upanga na kusababishiwa ulemavu kisa wivu...

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,330
33,139

Mchali akionyesha mkono aliokatwa.Picha na Rehema matowo




  • Baada ya kuwa katika mapenzi na mwanaume huyo kwa zaidi ya miaka 17, wakipendana na kuitana majina yote mazuri unayoyajua yakiwamo kuambiwa ‘mpenzi wangu nakupenda, nikinywa maji nakuona kwenye glasi’…leo mapenzi yamegeuka shubiri.




Kuna mikasa mbalimbali huwatokea watu katika suala zima la mapenzi, kiasi cha kusababisha baadhi yao kutopenda tena kuingia kwenye jambo hilo wakiliona kama ni kitu kisichofaa, ingawa ukweli unaweza kuwa sio huo.
“Sitaki tena wanaume, ni watu wabaya, wameniumiza moyo wangu mno,” anasema Hawa Francis, mkazi wa Ubungo, Dar es Salaam. Sababu kubwa ni kero ambazo amewahi kuzipata katika suala zima la uhusiano. Vivyo hivyo wapo wanaume hawataki kuoa, kwa maelezo kuwa kuna wanawake wamewahi kuwatesa.
Kama wewe ni kati ya watu ambao umekata tamaa na suala la uhusiano, fahamu kuwa si wewe pekee.Kuna kundi kubwa la watu wameshatendewa kiasi cha kufanya wasiwe na raha tena.

Mkasa wa mwanamke kukatwa mkono

Ilikuwa Agosti 7, mwaka huu, saa mbili usiku. Ilikuwa ni siku iliyobadili historia ya maisha yake. Baada ya kuwa katika mapenzi na mwanaume huyo kwa zaidi ya miaka 17, wakipendana na kuitana majina yote mazuri unayoyajua yakiwamo kuambiwa ‘mpenzi wangu nakupenda, nikinywa maji nakuona kwenye glasi’…leo mapenzi yamegeuka shubiri.
Mwanamke huyo, Mchali Kihiyo (35), mama wa watoto sita, aliyepoteza viungo vyake kutokana na ukatili wa kijinsia uliofanywa na mwanaume ambaye wamekuwa na uhusiano nae (jina limehifadhiwa).
“Uhusiano wetu ulikuwa mzuri, hata hivyo kwa sasa naona mambo yamekuwa magumu kwangu, leo hii mimi sina mkono wa kushoto na nimeondolewa sehemu ya viungo vyangu vya upande mmoja,”anasema Mchali,akibubujikwa machozi kutokana na ulemavu alioupata.
Chanzo cha ulemavu
Anasema maisha yao ya uhusiano yalikuwa ya furaha kwa kipindi chote lakini yamegeuka shubiri baada ya mwanamume wake huyo kuonyesha dalili ya kutompenda kama awali, hali ambayo anaitafsiri kama labda alikuwa na mwanamke mwingine.
Mchali, anasema mikasa na mateso ilianza miaka mitatu iliyopita baada ya kuhisi kwamba mwanamume wake huyo amezaa na mwanamke mwingine. Ubaya zaidi ulimtokea baada ya mtoto wa huyo mwanamke mwingine, kutumbukia kwenye kisima cha maji na kisha kupoteza maisha.
“Kifo cha mtoto huyo, ndicho kilichozaa tatizo hili la ukatili dhidi yangu na kunisababishia ulemavu, kwa kuwa huyo mwanaume wangu na huyo mwanamke aliyezaa nae, walidai kwamba mimi ndiyo nilimtupia majini marehemu mtoto wao ili afe,”anasema mama huyo.

Vitisho kabla ya ulemavu

Mchali, anasema mara baada ya msiba wa mtoto kumalizika, mwanamume wake huyo alihamia kwa mke mdogo lakini akawa anarejea nyumbani na kumtukana huku akitishia kufanya lolote analofikiri linafaa.
Anasema baada ya mateso na vitisho kuzidi aliamua kuondoka kwa mumewe huyo toka mwezi Aprili mwaka huu na kuamua kurudi kwa wazazi wake huku akiwaacha watoto wake kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi.
Anasema alilazimika kuwaacha watoto kutokana na agizo la mumewe, aliyekataa asiwachukue, hivyo akaanza maisha mengine ya upweke bila watoto huku akiendesha maisha yake kwa biashara ya kuuza samaki.
Anasema mwanzoni mwa mwezi huu, aliugua malaria na kukaa nyumbani bila kwenda kwenye biashara zake. Agosti saba mwaka huu, alipata nafuu na kuamua kwenda kumsalimia kaka yake, anayeishi mbali kidogo na nyumbani kwao na ndipo yakamkuta yaliyomkuta.
Anaeleza kuwa alikaa kwa kaka yake hadi muda wa futari wakafuturu na kushangaa simu yake ikiita, kuangalia ni namba ya mpenzi wake huyo. Alipoipokea, aliulizwa aliko, yeye alimweleza yuko kwa kaka yake na kumtaka amfuate mnadani akale nyama kitendo ambacho anasema alipingana nacho.
Anasema baadaye aliamua kurudi nyumbani na kusindikizwa na wifi yake hadi karibu na nyumba yao ikiwa ni saa mbili usiku.Walipoagana, ghafla akashangaa kusikia sauti ya mumewe ikimuita, alipogeuka alimwona, kisha akamuuliza alikotoka na kumwambia alikuwa kwa kaka yake.

Kipigo na ulemavu

Anasema mara baada ya kumjibu mwanamume huyo alianza kumpiga na hatimaye alianguka chini na mumewe akatoa panga na kuanza kumkatakata sehemu mbalimbali za mwili wake.
Hakika hujafa hujaumbika. Mchali amecharangwa kwa mapanga kuanzia chini ya goti mguu wa kushoto hadi kwenye makalio, amekatwa sehemu zaidi ya saba mwilini.
Ni kama alitaka kumkata shingo
Anasema kwa namna anavyoona ni kama alidhamiria kumuua akisema kuwa mara nyingi akiwa na huo upanga alikuwa analenga kumtenganisha shingo. Alichofanya mama huyo ni kuweka mikono shingoni kuzuia panga, kitendo kilichosababisha mkono wake wa kushoto kukatwa kabisa.

Hawezi kukaa

Mwandishi wa makala haya baadaye alimwomba mwanamke huyo angalau akae chini, kwani muda mwingi wa mahojiano alikuwa amelala, ndipo alipojibiwa kwamba hawezi kukaa kwa vile kuna nyama kubwa kwenye makalio ambayo imeshindikana kushonwa.
Mama huyo anasema wakati mumewe akimcharanga mapanga, mama yake mzazi aliendelea kupiga ngolo (yowe) kuomba msaada, kaka yake alikwenda lakini akashindwa kutoa msaada kwa kuwa shemeji yake huyo alikuwa akimkimbiza na panga.
Anasema kelele za mama yake zilisaidia kuokoa maisha yake, kwa kuwa majirani walijitokeza, hivyo mwanamume huyo akaanza kuwakimbiza akitaka kuwadhuru kitendo ambacho mama huyo aliona ndiyo nafasi pekee kukimbilia ndani.

Matibabu

Mchali, anasema baadaye ndugu zake, walitafuta usafiri na kufanikiwa kupata matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC ambako alilazwa kwa siku nne na kurejea nyumbani kutokana na ushauri wa daktari anayemhudumia.
Kwa mujibu wa mama huyo, daktari anayemtibu alimtaka Mchali akubali kutibiwa majeraha akiwa nyumbani ili kuepuka maambukizi ya magonjwa nyemelezi pamoja na kuepuka gharama za matibabu.
“Sina uwezo wa kukabiliana na gharama za matibabu kwa kuwa siwezi kutembea, nalazimika kukodi gari na kwa wiki naoshwa mara tatu. Nisaidieni ndugu zangu, ndoa yangu imenifikisha hapa,” anasema.

Mchali na hali ya ukatili mkoani Manyara

Kamanda wa Polisi mkoa wa Manyara, Akili Mpwapwa anasema mtuhumiwa bado hajakamatwa kwa vile hajulikani aliko, huku akiahidi kuendelea kulifanyia kazi suala hilo.
Akielezea zaidi ukatili mkoani Manyara, anasema upo, japo ni mdogo ikilinganishwa na mikoa mingine. Anaamini kuwa bado changamoto ni kubwa kwa wanawake ambao wengi wao wamekuwa wakinyanyasika.

Sababu kubwa za kunyanyasika kwa wanawake ni mfumodume. Akasisitiza kuwa Jeshi la Polisi mkoani humo linaendelea kuelimisha jamii madhara ya ukatili na kusema jitihada hizo zinapaswa kuigwa na wananchi na asasi nyingine kuhakikisha ukatili wa kijinsia unatokomezwa.

Msimamo wa wanaharakati

Mkurugenzi wa asasi ya kiraia ya Kwieco, inayojihusisha na utoaji wa msaada wa kisheria na haki za binadamu mkoani Kilimanjaro,Wakili Elizabeth Minde, anasema hali ni mbaya hasa kwa wanandoa wa kike, kwani wengi ndani ya ndoa hawana nguvu.

Taifa lilipofikia

Hali ya ukatili dhidi ya wanawake nchini bado ni kubwa kutokana na takwimu zinazoonyesha asilimia 39 ya wanawake wenye umri kati ya mika 15 hadi 49 wanafanyiwa vitendo vya ukatili.

Waziri anena

Naibu waziri wa maendeleo ya jamii jinsia na watoto, Ummy Mwalimu alikiri ukatili dhidi ya wanawake kuongezeka na kusema vitendo kama kupigwa na kubakwa ni matukio yanayoongoza zaidi na yanafanywa na wanaume, huku akisisitiza kuendelea kuangalia namna ya kufanya ili wanawake nchini waendelee kufurahia maisha.

Safari ya ndoa

Kwa mujibu wa Mwanasaikolojia, Modesta Kimonga anayefanya shughuli zake za ushauri Mkoani Mbeya, ndoa inaweza kufananishwa na safari ndefu yenye matukio yasiyotazamiwa, mengine yenye kupendeza na mengine yenye kuumiza.
Anasema mafanikio katika ndoa hayapimwi kwa panda shuka za safari bali yanapimwa kwa jinsi wenza wanavyoshughulikia hali hizo Ndio kusema ni suala la msingi kwa walio kwenye ndoa kujifunza namna ya kupambana na changamoto zinapotokea, siyo kutesana au kukimbiana.
Ushauri zaidi
Mshauri maarufu wa ndoa nchini Uingereza, Hussain Zahid anasema katika makala ya kitabu chake cha ‘My marriage’ yaani ndoa yangu kuwa msingi wa kuwa na ndoa nzuri ni kupata muda wa kuzungumza baina ya wanandoa wenyewe ili kuondoa tofauti zao.
“Kila mtu ajione analo deni la kumpenda na kumfanyia mema mwenza wake. Kila mtu ajifunze kauli nzuri na matendo mazuri kwa mwenzi wake…kwamba kabla ya kufanya lolote, tafakari, ungefurahi kufanyiwa hilo unalotaka kulifanya,” anaonya.

Staili mpya ya maisha kwa baadhi ya wanawake

Tafiti zinaonyesha kwamba kutokana na uwepo kwa mikwaruzo mingi katika mapenzi, kuna wanawake hawataki tena kuolewa. Kama lengo ni kupata mtoto au watoto, huwa tayari kuzaa na yeyote hata kama ni mume wa mtu, kisha jukumu la kulea kwa asilimia kubwa hufanya wao au kwa kushirikiana na hao waliozaa nao.

Hata hivyo wataalamu mbalimbali wa masuala ya ndoa, wanashauri watu kuacha tabia hiyo ya kuzaa tu, badala yake wapende kuzaa wakiwa kwenye ndoa kwa sababu mtoto ambaye hana mzazi mmoja, huathiriwa sana na matatizo ya kisaikolojia.

Mfano wa utafiti

Kulingana na utafiti uliotolewa hivi karibuni na Ofisi ya Taifa ya Takwimu Marekani, uko uwezekano mkubwa wa watoto wenye kulelewa na mzazi mmoja kuwa na tabia mbaya zaidi ya watoto wenye wazazi wote.

“Kama ni suala la kuiga tabia na matendo mabaya, watoto ambao wana mzazi mmoja wanaharibika mara tano zaidi ya watoto ambao wana wazazi wote wawili,” inasema sehemu ya utafiti huo.
Utafiti unaongeza kuwa hata wanapofika kwenye umri wa ujana, vijana ambao wana mzazi mmoja, wanaharibika zaidi ya wale ambao wana wazazi wote; Wana uwezekano wa kuharibika mara tatu zaidi ya vijana ambao wanaishi na wazazi wote wawili.

Si wote huharibika

Hata hivyo utafiti unasisitiza kuwa si watoto wote wenye mzazi mmoja huwa na tabia mbaya, bali kinachosemwa ni kwamba kwa asilimia kubwa watoto wa aina hiyo huharibika zaidi ya wale ambao wanalelewa na wazazi wote wawili. Wanaoathirika zaidi ni wale ambao wazazi wao wametalakiana, hasa kwa sababu mara nyingi hata nguvu za kulea watoto hupungua kutokana na wazazi au mzazi husika kuwa na msongo wa mawazo.

Matendo mabaya kama vile ya mzazi mmoja kuteswa na mwingine au mtoto kuona mama au baba yake akimshtaki mwenzi wake, huchangia kwa kiasi kikubwa kuendelea kumuathiri mtoto kitabia.Tabia kama za kupigana au mateso mengine kabla ya wanandoa kuachana, huchangia kuharibu maisha ya mtoto kwa kuona labda kupigana ndio njia nzuri ya kupambana na mtu anayekukwaza au mwingine kutishwa na uhusiano kwamba unaweza kusababisha mateso.

Sababu ya migogoro na tiba yake

Mtafiti maarufu wa masuala ya ndoa kutoka Urusi, Korotayev, A, katika chapisho lake alilolipa jina “Division of Labor by Gender’ yaani mgawanyiko wa majukumu katika jinsia, anasema msingi wa kuwa na uhusiano mbaya katika ndoa nyingi ni kutokuwa na fursa ya kukaa pamoja na kukubali kuondoa kasoro.

“Hakuna mtu ambaye yuko safi kwa asilimia 100. Umekaa tumboni mwa mama yako na kuna wakati mnagombana, iwe mtu ambaye mmekutana tu mitaani?”anahoji Korotayev, huku akiwasisitiza watu walio kwenye ndoa kubuni mbinu za kupendana na kufanya mikakati mingine ya maisha badala ya kuendekeza ugomvi, kufikiria kuachana au kutafuta wapenzi wengine.

 
Huyo mwanaume na yeye angekatwa mguu wa kusho na yeye akackilizia utamu anao upata mwenzie!!, yaani ameniboa!!.
 
huyu ni mmoja kati ya wanawake wengi wanaonyanyasika ndani ya ndoa, ona kama huyu alitoka kwenye hiyo ndoa lakini bado akamfwata, jamani wanaume wakatili ACHENI mana mnakera na hamvumiliki. pole kwa huyu dada maana amekutwa na kubwa zaidi ila wanaopigwa na kudhalilishwa na kupata vilema ni wengi sana sema tu hawajitokezi hadharani hiyo ni ndoa tu. aisee.
 
Back
Top Bottom