Nchi yoyote ile ambayo haina mfumo wa ufuatiliaji uhalali wa vipato vya watu wake, ni dhahiri kwamba watu waovu watatumia mwanya huo kuhujumu nchi kupindukia na hivyo kuwa na ukwasi wa kutisha ambao kwa namna moja au nyingine, kinamna, huutakasa na hivyo kuonekana ni utajiri halali!
Inawezekanaje kwa mfano mtumishi wa umma anakuwa na maghorofa au magari zaidi ya mahitaji yake lakini pia zaidi ya kipato chake na kunakuwa hakuna wa kuhoji? Inakuwaje, kwa mfano mfanya biashara mchanga kwa usiku mmoja anakuwa na ukwasi wa kupindukia bila hata ya kufuatilia mtiririko wa kipato chake kwa uwazi?
Aina hii ya ukosefu wa mfumo wa kutumia takwimu sahihi juu ya aina ya njia kuu za vipato vya wananchi, wigo wa ajira, aina ya raslimali zilizopo na namna zinavyotumiwa katika kuboresha maisha ya wananchi, mfumo wa uzalishaji na masoko, nk , hupelekea watu wengine kutajirika kwa njia haramu na wakati mwingine hata kuua wengine na kuwanyanga'nya mali zao! Nani atawauliza?
Ni wakati mwafaka kuweka utaratibu wa wazi wa vipato vya kila mwananchi na mtiririko wake badala ya kufanya hivyo kwa viongozi tu. Kwani inapokuwa kwa viongozi tu, huo unakuwa mwanya mwingine kwa viongozi hao hao kutumia jamaa au ndugu zao kuficha walichouibia umma / serikali au pesa haramu kutokana na rushwa!
Tijitafakari!