Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,125
Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa.
Uhakiki wa wanachama wa Chama Cha Jamii (CCJ) umeanza kwa kudorora mkoani Dar es Salaam.
Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, akifuatana na viongozi wa chama hicho, Richard Kiyabo (Mwenyekiti) na Renatusi Muambhi (Katibu Mkuu), walishiriki uhakiki huo katika viwanja vya Mwembe Yanga jana.
Hata hivyo, kati ya wanachama 247 walioorodheshwa, 40 pekee waliohakikiwa ambapo 13 kati yao wakiwa na sifa za uanachama na wengine 27 wakionekana kuwa `mamluki.
Wanachama hao (mamluki) ambao hawakutambuliwa kwa mujibu wa sheria, ni pamoja na Katibu Mkuu wa CCJ, Muambhi ambaye hakuonekana kwenye fomu ya wanachama iliyopo ofisini kwa Msajili wa Vyama vya Siasa.
Pia Mwenyekiti wake, Kiyabo, hakuwa na kadi ya uanachama kwa madai kwamba aliisahau nyumbani, lakini pia jina lake halikuwepo kwenye fomu ya Msajili.
Majina ya baadhi ya wanachama waliokuwa na kadi hayakuonekana kwenye fomu zilizowasilishwa kwa Msajili, huku kadi ya mwanamke aliyefahamika kwa jina la Joyce, kadi yake ilisomeka John Mwamba.
Pia wengine walipohojiwa, walitaja majina ambayo ni tofauti na yaliyoandikwa kwenye kadi za uanachama.
Kutokana na kujitokeza kwa hali hiyo, viongozi wa CCJ walimuomba Tendwa kusitisha zoezi hilo, kwa madai ya kuwepo dalili za kuhujumiwa.
"Kwa heshima ndugu msajili natamka zoezi hili lisitishwe na chama changu hakipo tayari kushiriki tena, tunahujumiwa, alisema.
Hata hivyo, licha ya tishio la CCJ kutoshiriki katika uhakiki wa wanachama wake, Tendwa alisema hawezi kusitisha kazi hiyo na kwamba leo atakuwa katika viwanja vya Picha ya Ndege mjini Kibaha na Jumamosi atakwenda Mahenge kwa ajili ya uhakiki huo.
CHANZO: NIPASHE