#HABARI:Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga linamshikilia mwanamke mmoja aitwaye Habiba Seleman Fundi kwa tuhuma za kumuiba mtoto mchanga katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto, mkoani Tanga.
Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi, alisema mtuhumiwa alikamatwa Juni 21, 2026, majira ya saa 1:00 usiku katika kitongoji cha Garekaya, Wilaya ya Lushoto, akiwa na mtoto huyo.
Kamanda Mchunguzi alisema kuwa Juni 19, 2026, majira ya saa 11:00 jioni, mama mzazi wa mtoto huyo, Mwanaidi Juma Nyaki, mkazi wa Kijiji cha Kwemakame, alitoa taarifa polisi kuhusu kupotea kwa mwanawe wa siku moja aliyekuwa amelazwa hospitalini hapo.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa awali, mtuhumiwa alitumia mbinu ya kujenga urafiki wa karibu na mama mzazi wa mtoto huyo pamoja na ndugu waliokuwa wakimhudumia hospitalini, jambo lililompa nafasi ya kupata imani yao.
"Baada ya kupata imani hiyo, alitumia fursa hiyo kumchukua mtoto na kumweka ndani ya beseni lenye nguo, kisha akaondoka naye bila kufahamika mara moja," alisema Kamanda Mchunguzi.
Aidha, uchunguzi wa kina umebaini kuwa mtuhumiwa alikuwa akidai kwa muda mrefu kuwa ni mjamzito na alikuwa amewahakikishia ndugu na jamaa wa mume wake kuwa alikuwa akisubiri kujifungua.
Kamanda huyo alisema kuwa baada ya muda aliokuwa ametarajiwa kujifungua kufika bila kujifungua, mtuhumiwa alidaiwa kupanga njama za kumuiba mtoto huyo ili kuthibitisha kwa familia ya mume wake na watu waliokuwa wakimzunguka kwamba alikuwa mjamzito na hatimaye amejifungua.
Jeshi la Polisi limeendelea na uchunguzi wa tukio hilo huku likiwahimiza wananchi kutoa taarifa za haraka wanapobaini matukio yanayohatarisha usalama wa watoto na jamii kwa ujumla.