Udasa: Tume ya katiba ni mali ya rais

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
Udasa: Tume ya katiba ni mali ya rais
Wednesday, 12 January 2011 21:22

Salim Said
JUMUIYA ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udasa), imesema haitoacha kutoa elimu kwa Watanzania jinsi ya kutoa majibu kwa Tume ya katiba itakayoundwa na Rais Jakaya Kikwete kutekeleza mchakato wa katiba mpya, kwa sababu wanaamini tume hiyo sio shirikishi.
Akitoa salamu za kuuaga mwaka jana na kukaribisha mwaka huu, Rais Kikwete alitangaza kuanza mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya.

Kikwete alisema ameamua kuunda Tume maalum ya Katiba, itakayoongozwa na mwanasheria aliyebobea na itakuwa na wajumbe wanaowakilisha makundi mbalimbali kwenye jamii yetu kutoka pande zetu mbili za Muungano. Lakini kabla, Rais Kikwete hajatangaza tume hiyo, Udasa ilisema tume hiyo ni mali ya rais mwenyewe na haitakuwa shirikishi.

Kutokana na hali hiyo, ili kuepukana katiba mpya ambayo itakuwa mbaya kuliko hata iliyopo, Udasa imeamua kufanya mfululizo wa makongamano ya wazi ya kutoa elimu kwa Watanzania kuandaa majibu ya kutoa pindi Tume hiyo itakapoundwa na kuanza kutafuta maoni.

Kongamano la kwanza litafanyika Januari 15, mwaka huu ukumbi wa Nkurumah Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kwamba, tayari Udasa imealikwa watu mbalimbali kutoka serikalini, vyama vya siasa na vyama vya kiraia na jamii. Makamu Mwenyekiti wa Udasa, Dk Kitila Mkumbo, alisema tume ya kupitia katiba ya Rais Kikwete haitokuwa shirikishi.

“Sio shirikishi kwa sababu inateuliwa na mtu mmoja, hivyo hatuwezi kusema ni shirikishi, kungekuwa na utaratibu wa kitaifa wa kuunda tume hiyo, basi tungekubali kuwa ni shirikishi,” alisema Dk Mkumbo. Dk Mkumbo alisema hawajui idadi ya makongamano watakayoendesha kwa mwaka, lakini yatakuwa mfululizo kwa ajili ya kuelimisha Watanzania.

“Sisi hatuna bajeti kubwa, tunatumia fedha yetu, hatujaomba msaada kutoka kwa mfadhili yeyote na shughuli nyingi zinafanywa na vijana wetu hapa, hivyo hatuna haja ya kutengeneza bajeti kubwa,” alisema Dk Mkumbo na kuongeza: “Tumeshamwalika Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, makatibu wakuu wa vyama siasa na jamii au kiraia, lakini pia tunawaalika wananchi wa kawaida waje kwa wingi.”

Alisema makongamano hayo yanalenga kuonyesha udhaifu na ubora wa katiba iliyopo, kuonyesha haja, maudhui na mchakato bora wa katiba mpya ya Watanzania sio kundi moja la jamii au kisiasa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Udasa, Profesa Mushumbusi Kibogoyo, alisema kuandaa makongamano hayo kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma, hawajaingilia kazi za rais wala waziri yeyote, bali wanatimiza lengo lao kwa mujibu wa katiba yao.

“Kama Rais alikuwa na nia ya kuunda tume kwa lengo la kuwanyamazisha wengine wasiseme katika mchakato wa katiba, basi amechanganyikiwa. Tume ni mali yake, ana mamlaka ya ripoti yake na yeye ndiye ataamua kuitoa ikimridhisha au kuificha iwapo hataridhika nayo,” alisema Profesa Kibogoyo.
 
JUMUIYA ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udasa), imesema haitoacha kutoa elimu kwa Watanzania jinsi ya kutoa majibu kwa Tume ya katiba itakayoundwa na Rais Jakaya Kikwete kutekeleza mchakato wa katiba mpya, kwa sababu wanaamini tume hiyo sio shirikishi.

Hawa wasomi waache ubabaishaji wadai Mkutano wa kikatiba tu ndiyo upewe nguvu ya kisheria na Bunge kuwa wenye mamlaka ya kutuandikia Katiba mpya...........................mengineyo ni kupoteza lengo................................
 
BAADA ya malumbano, mijadala mbalimbali kuhusu Katiba Mpya ya nchi na Rais Jakaya Kikwete kuridhia kuwa nayo, wasomi nchini wamejipanga kutoa mchango wao.

Hatua hiyo imetokana na Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udasa), kuandaa makongamano endelevu ya kujadili mchakato wa Katiba hiyo.

Kwa mujibu wa Udasa, makongamano hayo yatafanyika kwa mwaka mzima ambapo pamoja na mambo mengine, haja na maudhui ya Katiba iliyopo na mpya vitajadiliwa kwa kina.

Katika Kongamano la kwanza litakalofanyika Januari 15 kuanzia saa nne asubuhi pamoja na mambo hayo, pia ubaya na uzuri wa kuundwa Tume ya kushughulikia uratibu wa Katiba vitajadiliwa.

Suala la uundwaji wa Tume alilisema Rais Kikwete alipotoa hotuba yake ya salamu za Mwaka Mpya mwishoni mwa mwaka jana, ambapo aliridhia mchakato wa uundwaji wa Katiba mpya na kueleza kuwa ataunda Tume kufanikisha hilo.

Wakizungumza na waandishi wa habari jana chuoni hapo, viongozi wa Udasa akiwamo Mwenyekiti wake, Dk Mashumbusi Kabogoya, Makamu Mwenyekiti, Dk Kitila Mkumbo na mwakilishi wa wanajumuiya hiyo, Dk Azaveli Lwaitama, walisema kongamano hilo linatarajiwa kutoa mwongozo wa namna nzuri ya upatikanaji wa Katiba mpya.

Akijibu maswali ya waandishi waliotaka kujua kama kongamano hilo halina mwelekeo wa kumwingilia Rais katika utekelezaji wake wa kuunda Tume Huru ya kushughulikia mchakato wa Katiba, Dk Kabogoya alisema," tutazungumzia ubaya na uzuri wa Tume, hatumwingilii Rais kwa namna yoyote, maana sisi tutazungumza kitaaluma, na sidhani kama Rais atawaza hilo kwa namna ninavyomfahamu."

Akifafanua zaidi, Mratibu wa Kongamano hilo, Dk Mkumbo alisema, "hata hivyo Tume
ikiteuliwa na mtu mmoja, si Tume shirikishi hiyo, kwa kuwa itapaswa kuwajibika kwa aliyeiteua, Tume shirikishi inateuliwa kwa kushirikisha."

Dk Mkumbo bila kubainisha tume hizo, alisema nchi hii ina historia ya tume nyingi zilizoundwa kwa kazi maalumu kama hiyo, lakini mwisho wa kazi walipaswa kuwajibika kwa aliyewatuma na si kwa wananchi kama inavyopaswa kufanya Tume shirikishi.

Katika hilo, alisema ndiyo sababu ya kuwapo kongamano hilo ambalo ni ufunguzi wa makongamano endelevu kama hayo, ya kuchambua kwa pamoja, haja ya Katiba mpya, maudhui, ubaya na uzuri wa Tume na kuhadharisha kuwa jukwaa hilo halitakuwa na mwekeleo wa kutetea chama chochote cha siasa.

Kwa mujibu wa Dk Kabogoya, mwaliko umetolewa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Waziri wa Katiba na Sheria, vyama vya siasa na vya kiraia na wananchi wa kawaida wenye nia ya kujifunza na si ushabiki wa siasa.

Dk Kabogoya aliongeza kuwa watakaowasilisha mada katika kongamano hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Nkrumah ni Profesa Issa Shivji na Jenerali Ulimwengu.

Alisema wana mpango wa kurejesha hadhi ya chuo hicho ambacho zamani kilikuwa na makongamano ya kuibua mijadala yaliyokuwa yakihudhuriwa hata na Rais Julius Nyerere, lakini baadaye yalitoweka.

Awali akielezea mantiki ya kongamano hilo, Dk Kabogoya alisema lengo ni kutoa fursa kwa wananchi kufahamu misingi ya jumla ya Katiba ya sasa, kupendekeza njia bora itakayotumika katika mchakato wa uundwaji Katiba mpya ili kuepuka malalamiko na Katiba isiyo na viwango.

"Hatuji Jumamosi kutengeneza Katiba mpya, watu wajue hilo mapema, hatuna uwezo huo, ila Katiba yetu ya Udasa imetupa nafasi ya kuibua na kuhamasisha masuala ya kitaaluma, tusipokuwa makini katika hili, tutakuwa na Katiba mbovu kuliko inavyodhaniwa," alisema Dk
Kabogoya.

Mwenyekiti huyo wa Udasa alitumia pia fursa hiyo, kubainisha msimamo wa jumuiya hiyo kuhusu Katiba mpya kwa kusema msimamo wao ni Katiba mpya na kuongeza: "Kila mwananchi anahitaji hilo sasa, sisi tutakuwa wa ajabu tukilikataa."

Lwaitama, alisisitiza kuwa, mustakabali wa Taifa hili uko mikononi mwa wananchi hivyo kuwataka wenye nia ya kufahamu Katiba iliyopo na umuhimu wa mpya kama upo, kujitokeza kwa wingi kuhudhuria kongamano hilo.
 
Kuna mambo fikirishi ambayo tunapaswa kujiuliza kuhusu hoja za JK juu ya suala la katiba mpya

1. Huyo mwanasheria makini ambaye anataka kumteua kuongoza tume yake ya katiba, kwa nini hakumteua kuwa waziri wa katiba au meanasheria mkuu wa serikali au amegundua kwamba yupo mara baada ya sisi kuanza kudai katiba mpya?

2. Hivi nani atakayeandaa hadidu rejea (terms of reference) za hiyo tume? nani ataipitia ripoti ya tume na kumshauri JK ipasavyo? natumaini hatakuwa Kombani wala Werema ambao walishaweka msimamo wao hadharani. ni kichekesho cha mwaka kwa JK kuongelea juu ya suala la katiba mpya huku akiwa amewakumbatia washauri wake wakuu wa masuala ya katiba na sheria ambao hawaoni umuhimu wa katiba mpya.

3. Hivi JK alishawahi kuunda tume ipi makini katika uongozi wake ili watanzania tumuamini aunde tuma ya katiba kwa niaba yetu?

4. Hivi JK ni lini alishawahi kufanyia kazi mapendekezo ya tume yake yoyote "makini"? ili watanzania tumuamini tena kwamba atayafanyia kazi mapendekezo YOTE yatakayotolewa na hiyo tume "makini" Hebu tukumbushane yaliyotokea kwa tume ya EPA iliyopewa miezi 6 kufanyia kazi mambo yaliyokuwa wazi kwa kila mtu isipokuwa JK. baada ya miezi 6 kupita, "hasira" za JK zikawa zimeisha na akaishia kuwasamehe mafisadi wa EPA tena mbele ya Bunge na hatimae hotuba ya msamaha wa mafisadi kutokomea kutoka kwenye kumbukumbu za Bunge! na hadi leo mafisadi wanatesa ila watanzania tumeombwa kumsaidia JK kupambana na tatizo hewa la udini huku ufisadi ukishamiri bila kuwa na mpambanaji yoyote. Au pengine JK atayafanyia kazi mapendekezo ya tume kama alivyoyafanyia kazi kwa "umakini" mkubwa mapendekezo ya tume ya madini ya jaji Paul Bomani ambaye bado analalamikia ripoti yake kupuuzwa kama zilivyo ripoti zote kuanzia tupate uhuru

WATANZANIA HATUTAKI KUUNDIWA TUME NA JK ITAKAYOISHIA KWENYE MAKABATI YA IKULU KAMA ZILIVYO NYINGINE (KUUNGUA KWA BENKI KUU MIAKA YA 80, KIFO CHA SOKOINNE, TUME ZA NYALALI NA ROBERT KISANGA, TUME YA BOMANI, YA NTUKAMAZINA, YA SAID MWEMA (Mwovu?); HOSEA NA MWANYIKA, NK, NK.
TUNATAKA MKUTANO WA KATIBA NA JK ATATOA MAONI YAKE KAMA ATAKUWA NAYO KWA SABABU SUALA LA KATIBA MPYA HALIJAWAHI KUWA AGENDA YAKE, KOMBANI, WEREMA, MAKAMBA NA CHAMA CHAO. WATANZANIA TUWE MAKINI TUSIJE TUKAPORWA HOJA YETU.
 
Back
Top Bottom