Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,125
Serikali ilipotangaza rasmi kwamba Nyerere hatunaye tena, uchungu na simanzi uliikumba nchi nzima na dunia kwa ujumla hususani kwa wale waliokuwa wanamjua Nyerere na kujua alichokuwa akikisimamia na alichokiamini. Bara la Afrika likawa limempoteza kipenzi chake, mtoto wa Afrika ambaye thamani ya mchango wake katika ukombozi wa bara la Afrika haina kipimo. Mpaka anafariki dunia alikuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha amani barani Afrika.Mfano mzuri ni mgogoro wa Burundi aliokuwa akijaribu kuusuluhisha. Mwenyewe aliwahi kutamka kwamba yeye ni mwafrika kwanza na kisha mjamaa.
Mpaka leo hii jina la Nyerere linabakia kuwa kitambulisho chetu kikubwa .Wakati mwingine zaidi hata ya jina la nchi yetu yaani Tanzania.Wapo watu wanaolijua jina la Nyerere na wala wasijue jina la Tanzania au hata Tanganyika. Haishangazi, alikuwa ni mwana wa Afrika kamili. Kadiri siku zinavyopita, taratibu baadhi yetu, hususani vijana wanaoitwa wa kizazi kipya, wanazidi kulisahau jina la Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Viongozi wetu wengi wa sasa( ingawa wakati wa msiba wake waliahidi kumuenzi kwa hali na mali) wanaelekea kusahau kabisa ahadi zao! Wengi wanabakia kumuenzi kwa maneno na sio vitendo.
Lakini je,sote tunafahamu japo kidogo tu historia ya Mwalimu Nyerere? Uwezekano ni kwamba sio wote,hususani vijana wa sasa. Kwa kifupi na kwa msaada wa vyanzo mbalimbali hii hapa historia fupi ya Hayati Baba wa Taifa;
Kipaji chake cha kitaaluma na kiuongozi kilionekana tangu mapema. Kwa msaada wa waliokuwa waalimu wake pale Tabora (ma-father wa kanisa katoliki) baadaye alijiunga na Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda kusomea ualimu. Fikra za kimapinduzi na kusaidia waafrika wenzake zilianza kuonekana wazi akiwa Makerere.