Tumehuisha kampeni ya kumdai Ben. Tumefanya mkutano na waandishi wa habari leo

Francis12

JF-Expert Member
Sep 30, 2016
7,533
22,276
Umoja wa kizazi cha kuhoji Tanzania (UTG) umewasilisha malalamiko kwenye Tume ya Haki za binadamu na Utawala Bora kwa ajili ya kushughulikia matukio ya watu kupotea, kuteswa na wengine miili yao kuokotwa wakiwa wamekufa.

Akizungumza leo (Jumamosi) Mwenyekiti wa umoja huo Godlisten Malisa amesema wameikimbilia tume hiyo kwa kuwa ina mamlaka kikatiba kusikiliza malalamiko ya ukiukwaji wa haki za binadamu na ina mamlaka ya kuwahoji viongozi mbali mbali katika nchi.
===================
Leo tarehe 15/04/2017 Umoja wa Kizazi cha kuhoji nchini (UTG) umefanya mkutano na waandishi wa habari kuzungumzia masuala mbalimbali ikiwemo sakata la kupotea kwa ndugu Ben Saanane.

Vyombo vya habari vilivyoshiriki:

#TV
1. ITV
2. EATV
3. StarTV
4. AzamTV

[HASHTAG]#MAGAZETI[/HASHTAG]
1. TanzaniaDaima
2. Mwananchi
3. The Guardian
4. Nipashe

[HASHTAG]#RADIO[/HASHTAG]
1. E-fm Radio
2. East Africa Radio
3. TimesFm

[HASHTAG]#BLOGS[/HASHTAG]:
1. Today News
2. Full Habari
3. Habari 101
____________________________

UMOJA WA KIZAZI CHA KUHOJI TANZANIA (UTG)
______________________________________________

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
(Sakata la Ben Saanane na matukio ya kupotea/kutekwa kwa baadhi ya watanzania).
______________________________________________

Utangulizi,
Ndugu waandishi wa habari,
Mnamo tarehe 11 mwezi Disemba mwaka jana (2016), Umoja wa Kizazi cha kuhoji Tanzania (UTG) tulifanya mkutano na waandishi wa habari nchini kueleza kuhusu suala la kupotea kwa aliyekua Katibu Mkuu wa UTG Tanzania Ndg.Bernad Focus Saanane, maarufu kama Ben Saanane.

Ndugu Saanane ambaye aliondoka nyumbani kwake siku ya tar.18/11/2016 majira ya asubuhi, hadi sasa hajulikani alipo licha ya juhudi mbalimbali zilizofanyika kumtafuta.

Hadi tunafanya mkutano wetu wa kwanza na wandishi wa habari mnamo tarehe 11/12/2016, UTG ilijiridhisha kupitia Idara ya Uhamiaji kwamba Ben hakuwa amesafiri nje ya nchi kama ilivyokua ikidaiwa na baadhi ya watu. Pia hakuwemo katika hospitali yoyote nchini kama mgonjwa au kama marehemu. Pia Jeshi la Polisi lilituhakikishia kwamba Ben hajashikiliwa katika kituo chochote cha polisi wala hajawekwa mahabusu katika magereza yoyote ile.

Tarehe 9 mwezi Disemba mwaka jana (2016) tulikwenda Bagamoyo kukagua maiti 7 zilizookotwa mto Ruvu, ili kujiridhisha kama Ben alikua mmoja wapo. Lakini kwa bahati mbaya tulikuta maiti 6 kati ya hizo zimeshazikwa, na maiti moja iliyobakia haikua ya Ben.

MAPUNGUFU TULIYOYAONA KATIKA ZOEZI LA KUMTAFUTA BEN:

1. UTG inatilia shaka ukweli wa taarifa ya mawasiliano ya mwisho ya Ben. Mawasiliano yaliyowasilishwa jeshi la polisi kitengo cha uhalifu wa kimtandao (Cyber crime) ambayo na sisi tumeweza kuyaona, yanaonesha kuwa Ben aliwasiliana mara ya mwisho kupitia simu yake mnamo tarehe 16/11/2017.

Lakini Ben aliondoka nyumbani kwake tarehe 18/11/2017. Kwa mujibu wa mawasiliano yaliyowasilishwa polisi, yanaonesha kuwa Ben hakuwasiliana kabisa kwa muda wa siku mbili yani tarehe 17 na tarehe 18 jambo ambalo UTG tunaamini si kweli.

Kama Ben aliondoka nyumbani kwake tarehe 18/11/2017 iweje mawasiliano yake ya mwisho yawe tarehe 16/11/2017? Kwa siku mbili kabla ya Ben kupotea je hakupiga simu kabisa? Hakupigiwa? Hakutuma ujumbe wowote wa sms wala kutumiwa?

UTG tunaamini kwamba mawasiliano ya Ben ya siku mbili za mwisho (tar 17 na 18) yamefichwa kwa sababu maalumu.

2. Katika mawasiliano yanayoishia tarehe 16 yaliyowasilishwa polisi, zipo namba za simu ambazo tunazitilia mashaka. Namba hizo si za ndugu wa Ben, si za marafiki wake wala jamaa zake. Namba hizo zinaonesha kuwasiliana na Ben siku za mwishomwisho kabla ya kupotea na hazijawahi kuwasiliana nae kabisa katika kipindi cha awali.

UTG kwa kushirikiana na familia ya Ben, tumelitaka Jeshi la Polisi kufuatilia namba hizo ili kuwabaini wahusika na waweze kuhojiwa juu ya mawasiliano yao na Ben lakini hadi sasa hatujapata taarifa rasmi kutoka Jeshi la Polisi kuhusu kukamatwa kwa watu hao.

Ikiwa Polisi wana nia ya kweli ya kusaidia jambo hili, kwanini wasifuatilie namba hizo zinazotiliwa mashaka, wakamate wahusika na kuwafanyia mahojiano? Kuna ugumu gani katika hili? Bado hatuelewi kwanini polisi wanapata kivugumizi kwenye suala ambalo lipo wazi kama hili.

3. Majibu yasiyoridhisha kutoka jeshi la polisi. Tangu Ben amepotea hadi sasa tumefanya mawasiliano na jeshi la polisi (ana kwa ana au kwa njia ya simu) zaidi ya mara 21. Katika mara zote hizo Polisi wamekua wakituambia kuwa wanaendelea na uchunguzi. Lakini hawajapata kusema wamefikia wapi katika uchunguzi wao huo.

Tunaheshimu utaratibu wa jeshi la polisi kufanya uchunguzi lakini tunaomba watujulishe ama waijulishe familia hatua waliyofikia katika uchunguzi wao. Majibu yao ya mkato kwamba wanaendelea na uchunguzi hayaleti taswira nzuri sana hasa kutokana na suala hili kugubikwa na sintofahamu kubwa.

4. Kauli ya IGP. Mkuu wa Jeshi la polisi nchini Ernest Mangu akihojiwa na gazeti la RaiaMwema la jumatano wiki hii alisema Ben anatafutwa kama "missing person" yani kama ambavyo watu wengine walioripotiwa kupotea wanavyotafutwa.

Kwanza tunamshukuru sana IGP kwa kukiri kwamba anafahamu suala la Ben na kwamba wanamtafuta. Lakini tunaamini kutokana na sakata la Ben lilivyo si sahihi kumtafuta kama missing person. Ben hakuwa mtoto, hakuwa na ugonjwa wowote wa akili, hakuwa ktk msongo wa mawazo, anatafutwaje kama missing person?

Ben amewahi kutoa taarifa Polisi juu ya kupigiwa simu na kutumiwa sms za vitisho. Mtu wa aina hii hawezi kutafutwa kama missing person. Kwanini polisi wasione tukio hili kuwa ni la tofauti na matukio mengine ya watu kupotea kutokana na mazingira yanavyoonesha?

HATUA ZILIZOCHUKULIWA:

Suala la kupotea kwa Ben ni moja ya matukio ya kupotea kwa watanzania mbalimbali yaliyoripotiwa sana kwa siku za karibuni. Baadhi ya mtukio hayo yanaogofya kwani yanaambatana na vitendo vya utekaji/utesaji na hata kifo. Msanii wa muziki wa kizazi kipya Roma Mkatoliki, alipotea kwa siku 3 na alipoibuka alidai kutekwa (yeye pamoja na wenzie) na kufanyiwa vitendo vya kinyama huko walipokua.

Kijana Erick Msyaliha alichukuliwa nyumbani kwake maeneo ya Sinza mnamo tarehe 13/03/2017 na watu wanaodhaniwa kuwa ni polisi na hadi sasa hajulikani alipo.

Ndugu Honorati mkazi wa Bunju jijini Dar, alipotea jioni ya tarehe 10/04/2027 akiwa ametoka kwenye shughuli zake za kuuza maziwa, na hakujulikana alipo hadi tarehe 13/04/2017 mwili wake ulipookotwa huko misitu ya Mabwepande akiwa kauawa.

Kijana Patrick Godson Kimario mkazi wa mji mdogo wa Sanya Juu, wilayani Siha mkoani Kilimanjaro alipotea jioni ya tarehe 11/04/2017 kabla ya mwili wake kuokotwa kesho yake tar.12/04/2017 akiwa ameuawa na macho yake kutobolewa.

Dada Anitha Kimario alitoweka tar.27 February mwaka huu huko wilayani Rombo alipokua akiishi, na mwili wake kuokotwa tar.02 March 2017 katika mashamba ya miwa ya TPC, ukiwa na majeraha yanayoonekana aliuawa.

Hii ni mifano michache tu ya watanzania kadhaa walioripotiwa kupotea/kutekwa, na vitendo vilivyoambatana na kupotea kwao kama mateso na wengine vifo.

Kufuatia vitendo hivyo, Taasisi ya UTG Tanzania imechukua hatua zifuatazo;

1. Kuwasilisha malalamiko rasmi (ya maandishi) Tume ya haki za binadamu na utawala bora, ambayo kikatiba ina mamlaka ya kusikiliza mashauri/malalamiko yanayohusu ukiukwaji wa haki za binadamu na utawala bora.

Kwa mujibu aa ibara ya 130 na 131 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Tume hii ina mamlaka ya kumuita na kumhoji mtu yeyote katika Jamhuri ya Muungano isipokuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Makamu wa Rais na Rais wa Zanzibar.

Tunaamini kwa mamlaka ambayo tume hii imepewa kikatiba inaweza kuwaita wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama nchini na kuwahoji juu ya matukio ya kuogofya yanayoendelea nchini ya watu kupotea na wengine kuripotiwa kuteswa au miili yao kuokotwa wakiwa wamekufa.

2. UTG imewasilisha maombi rasmi kwa Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora imuagize Mkemia mkuu wa serikali (kwa kushirikisna na mamlaka zingine) wafukue miili ya watu 7 waliyoizika kando ya mto Ruvu wilayani Bagamoyo ili ifanyiwe vipimo vya vinasaba (DNA test). Hii itasaidia watanzania waliopoteza ndugu zao kupata fursa ya kwenda kuoanishwa vinasaba hivyo kubaini kama ndugu zao waliopotea ni miongoni mwa watu hao 7 waliozikwa kienyeji wilayani Bagamoyo.

Tunaamini hata kama miili ya watu hao imeharibika ardhini, bado vipimo vya DNA vinaweza kufanyika kwa kupitia mifupa yao, kwa sababu hata Faru John alipimwa DNA kupitia mifupa yake. Kitendo cha serikali kutumia mamilioni ya fedha kupima DNA yafaru John huku ikipuuza kupima DNA kwa miili ya binadamu wenzetu iliyookotwa, hakileti tafsiri nzuri kwa wananchi. Wengi wanaona kuwa serikali inathamini zaidi uhai wa wanyama kuliko watu.

3. Taasisi ya UTG imekiomba kituo cha sheria na haki za binadamu nchini (LHRC) kupeleka malalamiko rasmi Umoja wa mataifa (UN) juu ya matikio ya watanzania kupotea. Mapema mwezi uliopita Mkurugenzi wa kituo hicho Dr.Hellen Kijo Bisimba alishiriki mkutano wa umoja wa mataifa wa taasisi za kiraia zinazoshughulika na masuala haki za binadamu ambapo aliweza kupenyeza hoja kuhusu watanzania kupotea katika mazingira ya kutatanisha akihusisha suala la Ben Saanane.

Baada ya kuwasilisha hoja hiyo Umoja wa mataifa ulimtaka Dr.Kijo kuwasilisha kwa maandishi malalamimo hayo ili Umoja wa mataifa uweze kutuma wataalamu wake kuja kuchunguza. Ieleweke kwamba Umoja wa mataifa una chombo huru cha uchunguzi kiitwacho "The Observer" na kina uwezo wa kuchunguza matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu katika nchi yoyote mwanachama (Tanzania ikiwemo).

Hivyo basi UTG tulishirikiana na LHRC kuhakikisha kuwa barus hiyo inaandikwa na kufika Umoja wa mataifa katika utaratibu rasmi ili waweze kutuma wataalamu wake kuja kuchunguza. Tayari barua hiyo imeshaandikwa na tunasubiri majibu.

MAPENDEKEZO:

1. Serikali itangaze operesheni maalumu ya kukomesha vitendo vya utekaji/upoteaji na mauaji kwa raia nchini, kama ambavyo jeshi la polisi limetangaza operesheni ya kupambana na majambazi.

Nguvu ileile na dhamira ileile ambayo Polisi wameionesha kupambana na majambazi waoneshe ktk kupambana na watu wanaohusika na vitendo vya utekaji wa raia. Tunaamini kuwa uchungu uleule ambao polisi wameupata baada ya askari wao kuuawa, ni uchungu huohuo wanaousikia watanzania ambao ndugu zao wamepotea, wametekwa ama kuuawa.

2. Jeshi la Polisi litoe taarifa ya mwenendo wa uchunguzi katika suala la Ben Saanane. Lieleze limefikia wapi, na limechukua hatua gani hadi sasa.

3. TCRA ifanye uchunguzi kubaini mawasiliano ya Ben ya siku mbili (tar.17 na 18) kama yalifichwa. Ikibainika hivyo waagize kampuni ya simu ambayo Ben alikua akitumia mtandao wake itoe mawasiliano yake, na waichukulie hatua za kisheria kampuni hiyo.

4. Tume ya Haki za binadamu na utawala Bora ichukue hatua juu ya hali ya usalama nchini kwa kufanyia kazi barus tuliyowasilisha kwao.

5. Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lijadili hoja kuhusu kuforora hali ya usalama nchini kufuatia matukio ya kupotea, kuteswa, na hata kuuawa kwa baadhi ya watanzania. Ikiwezekana iundwe kamati teule ya bunge ya kushughulikia suala hili, au kamati ya kudumu ya ulinzi na mambo ya nje inaweza kutumika kufanya uchunguzi wa hali ya usalama nchini na kuwasilisha ripoti bungeni.

6. Vyombo vya habari vizipe uzito mkubwa habari za kupotea kwa binadamu, kuliko habari za kupotea kwa wanyama. Ni Tanzania pekee ambapo mnyama anaweza kupewa thamani kubwa kuliko binadamu, ikiwemo kuandaliwa bajeti ya mamilioni ya fedha kupima vinasaba, huku watanzania wakiripotiwa kupotea na wengine miili yao kuokotwa lakini hakuna anayehangaika kupima vinasaba.

Ni Tanzania pekee ambapo habari ya mnyama kupotea inawekwa ukurasa wa mbele wa gazeti lakini habari ya kupotea binabamu ikipewa nafasi ndogo au isipewe nafasi kbs. Tunaamini hii si sahihi.

Imetolewa na:

1. Noel Shao
N/Katibu Mkuu
UTG - Tanzania

2. Godlisten Malisa
Mwenyekiti
UTG - Tanzania
tmp_29312-FB_IMG_1492259256181-1817596311.jpg
tmp_29312-FB_IMG_1492258328354-1138348626.jpg
 
Weka yapi ambayo hatuyajui ? We tunajua kuliko wewe sema tupo kimya
 
Hongereni ila angalieni msije mkatekwa na nyie mkirudi muanze kutangaza neno la mungu kama ndugu yetu anayeimba nyimbo za dini sasa hivi au lema anayehubiri neno LA mungu sikuhizi bungeni.
 
Kwa alichokua anakidai /anakisimamia Ben, sijui kama atarudishwa....
Huko uliko nakuombea shem lake
 
Mkuu uliyeshika mike kumbe zile harakati zako kipindi kile pale kwa Prof Kikula pande za Idodomya ulikuwa
ni mwana UFIPA hai, hongera sana mangi. Sasa umeeleweka vema sana mwalimu ticha. Ila usiwapandikize wakusoma
itikadi za kiuna harakati.

tmp_29312-fb_img_1492259256181-1817596311-jpg.496383
 
Kwa alichokua anakidai /anakisimamia Ben, sijui kama atarudishwa....
Huko uliko nakuombea shem lake

Badala ya kudai kutatuliwa kero za kimaendele, wanadai Rais kazungumza nini leo!

Vidomodomo vya humu pia vitafungwa tu, mapapa wa uvuvuzela watakapokuwa wamesalimu amri.
 
Back
Top Bottom