Donatila
JF-Expert Member
- Oct 23, 2014
- 8,273
- 25,297
Kama ilivyo kwenye vita ya kupambana na rushwa na ufisadi, hili kwake halina mjadala, na kimsingi ni suala jema.
Ni suala jema kwa sababu kodi inayokusanywa na serikali ndiyo inayotumika kugharimia shughuli zake mbalimbali za kuwapatia huduma za msingi wananchi.
Kwenye baadhi ya nchi, pamoja na kuwa kulipa kodi ni suala la kisheria kwa mwananchi yeyote mwenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea, lakini pia kulipa kodi ni wajibu wa kiraia.
Raia wema huona fahari kulipa kodi, kwa kuwa wanajua inaenda kugharimia shughuli kwa ajili ya ustawi wao.
Rais Magufuli ameendelea kuhimiza wananchi walipe kodi, kupitia majukwaa mbalimbali.
Amenukuliwa kupitia vyombo vya habari, akihimiza wananchi wenye sifa ya kulipa kodi wafanye hivyo.
Kwamba hata pale wanapoenda kufanya manunuzi ya bidhaa dukani ama kulipia huduma yoyote ile ya kibiashara, amehimiza wananchi wadai risiti.
Kwamba katika kila bidhaa ama huduma inayolipiwa, kuna asilimia ya serikali inayobakia ambayo inapaswa kwenda serikalini kwa ajili ya kugharimia shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
Mjadala unaona pengine kuna baadhi ya watu hushangaa wanaposikia serikali ikishupalia watu walipe kodi.
Ieleweke kwamba, serikali ikiwa ni pamoja na mihimili mingine ya dola kama vile Bunge lenye jukumu la kutunga sheria na Mahakama yenye jukumu la kutafsiri sheria, pamoja na idara zake mbalimbali, zinahitaji fedha ili ziweze kutimiza majukumu yake barabara.
Mbali na fedha kwa ajili ya uendeshaji wa mihimili hiyo, kunahitajika fedha za kuwalipa watumishi wa serikali, wabunge, majaji na mahakimu, na yote hiyo inatokana na kodi inayokusanywa na serikali kutoka kwa walipa kodi.
Kuna kodi za aina mbalimbali, kuanzia ile ya mapato, ambayo kimsingi mfanyakazi yoyote hulipa kutegemeana na mshahara wake.
Kwamba kuna asilimia ambayo hukatwa na kupelekwa hazina, kwa ajili ya shughuli za kiserikali.
Kuna kodi ya majengo au mali isiyohamishika ambayo hulipwa kutokana na thamani ya mali ama jengo lenyewe.
Aidha, kuna kodi ya mauzo ambayo Dk.Magufuli amekuwa akiisisitiza mara kwa mara, inayopatikana pale mtu anapoenda kununua bidhaa dukani ama huduma sehemu panapouzwa huduma.
Kwa kila bidhaa inayonunuliwa, kuna asilimia inayokatwa na muuza duka ama mtoa huduma kama kodi ya serikali.
Hata hivyo, Mjadala unaona kwamba, pamoja na juhudi zote zinazoonyeshwa na Dk. Magufuli za kuhimiza wananchi kudai risiti pale wanaponunua bidhaa dukani, bado mwitikio uko katika kiwango cha chini.
Nasema hivyo kwa sababu, Mjadala umekuwa akishuhudia wananchi wengi wanaoenda kununua bidhaa kwenye baadhi ya maduka, tena mengine ya jumla jumla, wakiwa wanatoka bila ya risiti.
Kimsingi, kitendo hicho hakina maelezo mengine zaidi ya kuwa ni cha kukwepa kodi.
Ni cha kukwepa kodi toka kwa mwananchi mwenyewe aliyenunua bidhaa na akaacha kudai risiti, lakini vilevile kwa muuzaji.
Hali hii haiko kwenye biashara za maduka yanayouza bidhaa tu, bali hata kwenye maduka ya dawa.
Kimsingi kitendo hiki ni cha kumuangusha rais wetu mwenye dhamira ya kuona wananchi wakifaidika na keki ya taifa kupitia huduma za elimu, afya, maji, miundombinu, ulinzi na usalama, masoko na zinginezo.
Nimesema kwamba suala la kulipa kodi katika nchi zingine ni la kisheria na wajibu kama ilivyo hapa kwetu.
Pengine tofauti iliyopo kwa sasa ni kuwa Dk. Magufuli, anajaribu kupandikiza kwa wananchi moyo wa kulipa kodi ili waone kuwa ni wajibu wao kama raia.
Ni kwa misingi hiyo ndipo Mjadala unapowaasa wananchi kudai risiti kwa kila bidhaa ama huduma wanayonunua ili kodi yote ya serikali iweze kupatikana kwa ustawi wa taifa.
Chanzo: Nipashe