Taarifa Kwa Vyombo vya Habari
UZOEFU WA ACT WAZALENDO KATIKA KUSHIRIKI CHAGUZI ZA MARUDIO ZA 16 MEI 2021
Chama cha ACT Wazalendo kilishiriki katika chaguzi ndogo za marudio katika Majimbo ya Muhambwe na Buhigwe na Kata 5 kati ya Kata 17 zilizokuwa zinachagua Madiwani. Tuliamua kushiriki katika chaguzi hizi kama kipimo cha kuona kama kutakuwa na Mabadiliko yeyote katika uendeshaji wa chaguzi katika Awamu ya Sita ya Uongozi wa Nchi yetu kutoka hali iliyokuwapo Wakati wa Awamu ya Tano.
Kutokana na ushiriki wetu katika chaguzi hizi tumeweza kuona sura mbili tofauti za uendeshaji na usimamizi wa uchaguzi chini ya Tume Moja ya Uchaguzi;
1. Sura ya kwanza ni Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kusimamia mchakato mzima wa uchaguzi kwa uhuru na haki kwa vyama vyote. Hali hii imejitokeza kwenye jimbo la Muhambwe na Kata kadhaa. Katika maeneo haya Chama chetu kiliweza kushiriki kwenye kampeni bila bughudha kipindi chote cha kampeni, siku ya uchaguzi mawakala wetu waliruhusiwa kutekeleza majukumu yao wakati wote hadi zoezi lilipo kamilika na utangazaji wa matokeo uliakisi matokeo halisi yaliyotoka katika vituo vya kupigia kura. Licha ya kuwa na hitilafu ndogo ndogo kama vile vitisho kwa baadhi ya viongozi wetu, kutekwa kwa Kiongozi wetu mmoja siku ya uchaguzi, bado tunaweza kusema Msimamizi na wasimamizi wasaidizi kwenye maeneo haya waliendesha uchaguzi kwa uhuru na haki. Katika hatua hii tulikubali matokeo na kuwapongeza walioshinda, utamaduni mzuri kabisa katika kukomaza demokrasia yetu. Mgombea wa ACT Wazalendo alimpongeza Mgombea wa CCM kwa ushindi. Kiongozi wa Chama chetu pia alikipongeza Chama cha Mapinduzi kwa ushindi huo. Vile vile tulimpongeza Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Muhambwe kwa kuendesha uchaguzi kwa mujibu wa sheria, kanuni na utamaduni wa Demokrasia ya Vyama Vingi. Utamaduni huu ni muhimu kuendelezwa Nchini kwetu.
2. Sura ya pili ni Tume ya Taifa ya Uchaguzi - NEC kusimamia uchaguzi kwa kukandamiza uhuru wa vyama vingine na kupendelea wagombea wa chama tawala, CCM. Hali hii imejitokeza kwenye jimbo la Buhigwe na kata za Miuta Wilaya ya Tandahimba, Ligoma Wilaya ya Tunduru na Buziku Wilaya ya Chato. Licha ya kuwa zoezi la Kampeni liliendeshwa vizuri lakini siku ya uchaguzi iligubikwa na hila na uvunjifu wa sheria dhidi ya wagombea wa Chama chetu. Hitilafu na hila zilizojitokeza ni kama zifuatazo;
- Mawakala wetu walitolewa kwenye vyumba vya kupigia kura
- Kukamatwa kura bandia kwa mfano Kijiji cha Kasumo kata ya Kajana jimbo la Buhigwe na Kata ya Ligoma Wilayani Tunduru.
- Wasimamizi wa vituo kutumika kuingiza kura kwenye masanduku ya kupigia kura, sambamba na wasimamizi ambao sio wapiga kura ndani ya jimbo la Buhigwe kuruhusiwa kupiga kura
- Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo la Buhigwe kubainika kupiga kura mara tatu (kwenye vituo vitatu tofauti)
- Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi kuongeza kura Kwa mgombea wa CCM Wakati wa kutangaza matokeo katika Kata ya Ikizu Wilaya ya Chato
- Kutekwa kwa baadhi ya wanachama wetu
- Kukamatwa kwa Kiongozi wetu, Katibu wa Mkoa wa Selou (unaojumuisha majimbo ya Tunduru Kusini, Tunduru Kaskazini na Namtumbo) Ndg. Mtutura Abdallah Mtutura na viongozi wengine watatu kukaa Polisi kwa zaidi ya Siku sita kinyume cha Sheria kwa makosa ya kubambikiwa.
- Vyombo vya dola kutumia nguvu kubwa ikiwemo kupiga mabomu vijiji vyenye uchaguzi usiku wa manane bila kuwepo vurugu yoyote ili kutisha wapiga kura. Hili lilitokea Kata ya Ligoma Wilaya ya Tunduru.
Kwa hiyo, kutokana na hali tuliyoiona katika chaguzi hizi, kwa sasa bado uendeshaji wa uchaguzi unategemea utashi na hisani ya mtu anayesimamia uchaguzi (Msimamizi wa Uchaguzi). Hizi ni dalili za hatari kwa uhai wa demokrasia ya vyama vingi.
Chaguzi zinapaswa kuendeshwa kwa mujibu wa Katiba, Sheria, Kanuni na utamaduni wa misingi ya demokrasia ikisimamiwa na chombo kinachoaminika na pande zote zinazoshiriki katika Uchaguzi.
Hivyo Basi,
A. Tumeamua kuchukua hatua za kukata rufaa mahakamani kupinga matokeo katika Jimbo la Buhigwe na Kata za Miuta, Ikizu na Ligoma.
B. Kiongozi wa Chama Ndg. Zitto Zuberi Ruyagwa Kabwe amemuandikia Barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumweleza changamoto zilizotokea ili Hatua ziweze kuchukuliwa.
Kiongozi wa Chama amemweleza Rais kuwa mifano ya yaliyojiri katika chaguzi hizi haitoweza kutimiza nia Yake Njema aliyonayo juu ya kuendeleza demokrasia, na kuweka mwelekeo wa shughuli za kisiasa zenye tija na maslahi kwa Nchi yetu kama alivyoahidi katika hotuba Yake Bungeni alipolihutubia Taifa.
Katika barua hiyo, Chama cha ACT Wazalendo imewasilisha Kwa Rais Samia Suluh Hassan mapendekezo yafuatayo ili kuzifanya chaguzi kuwa za ushindani, huru na zenye uwanja sawa wa vyama vyote vina vyoshiriki;
1. Kuanzishwa Kwa mchakato wa kuifanya Tume ya Taifa ya uchaguzi kufanya shughuli zake kwa uhuru. Kwamba Tume ya Taifa ya Uchaguzi iwe na Watumishi wake wanao wajibika kwa Tume tu na wasiwe ni makada wa chama kingine cha siasa.
2. Kuanzishwa Kwa mchakato shirikishi wa kupitia upya Sheria ya Vyama vya Siasa ili kuondoa vifungu vyote vinavyobana uhuru wa vyama vya siasa kutekeleza majukumu yake. Tumetaka Vyama vya Siasa viwe na Uhuru wa kufanya mikutano yake bila bugudha.
3. Kwa kupitia Taasisi zinazomilikiwa na Vyama vya Siasa Nchini hususan Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), Rais aanzishe majadiliano miongoni mwa Vyama ili kujenga kuaminiana na kutatua migogoro kwa njia za amani pale inapotokea.
4. Kutekelezwa Kwa makubaliano ya Mabadiliko ya Msingi katika Katiba na Sheria ya Uchaguzi (minimum reforms) ya Septemba 2014 kati ya Serikali na Vyama vya Siasa kupitia TCD ili kuwezesha Siasa zenye Tija na chaguzi kuwa Huru.
5. Kuvinasihi vyombo vya Ulinzi na Usalama kutenda haki kwa wote na kuachia mara moja Wanachama wetu na wa vyama vingine vya Siasa waliokamatwa na kuwekwa magerezani nyakati za chaguzi.
Imetolewa na
Salim Bimani
Katibu wa Uenezi na Mawasiliano Kwa Umma
ACT WAZALENDO
19/5/2021
View attachment 1790860