Simulizi ya Fahari, halili na madhalili

nasrimgambo

JF-Expert Member
Jan 10, 2017
1,858
2,348
Karibu wana forum humu ndani nitakuwa nawapostia simulizi yangu iitwayo Fahari,

Simulizi inayomuhusu kijana Leo, anayeonekana kuwa mwenye akili sana na mzee tajiri aitwaye Habib Nasri, tena mzee huyo anamuona kijana huyo kuwa atakuja kuwa mwenye mafanikio makubwa katika maisha yake

Lakini pale huyo kijana Leo anapotaka kumchumbia binti wa mzee Habib, aitwaye Sunaina ndipo mgogoro unaanzia
Je! Itatokea huyo mzee kukubali bintiye wa fahari kubwa kuolewa na kijana Leo mwenye akili nyingi ila tokea familia maskini.
 
IMG_20170108_101516.jpg
 
Sehemu ya kwanza



Leo alikuwa ni baraka na kheri kwa mama yake, ambaye japo ya umaskini wake alijitahidi sana kumlea kwa maadili na kumpa kila kitu alichohitaji katika makuzi yake
Leo alikuwa ni kheri, kwa mdogo wake wa kike, Sanura. Dada yake huyo alimuona Leo kuwa ni shujaa, alimuona ni kaka aliyeongoza njia, ya mfano wa kufuata, kwa kila sifa, utiifu, nidhamu na kujituma kwa bidii na kufanya vizuri katika masomo.

Kiujumla, Leo alikuwa na haiba ya pekee. Haiba iliyomfanya apendwe na watu wengi katika mitaa yao ya huko uswahilini alikokuwa akiishi, mitaa ya Kwarara, katikati ya mji wa Morogoro.
Kila mtu aliyeishi mitaa ya Kwarara alifahamu moja kati ya sifa nyingi nyingi za Leo.
Washkaji zake kitaani walimfahamu kuwa, Leo alikuwa ni mjuzi wa mpira wa miguu, sifa ambayo ilimfanya wampende sana. Wamama kwa wababa na wazee wa mitaa hiyo walimfahamu Leo kama kigezo chema, hata ikatokea wakiwa wanawasema vijana wenye tabia mbovumbovu mfano wao walioutolea, ili kuwa vijana waovu waufuate mara nyingi ulikuwa ni mfano wa kijana Leo.
Ilikuwa kawaida mitaa ya Kwarara kusikia mwanamama mwenye mwanae mtukutu akimsema mwanae na kumalizia kwa kauli ya “hivi huwezi kuwa kijana mwenye tabia njema kama Leo”, basi ndio hivyo Leo alikuwa, habari zake zilikuwa kubwa.

Leo alikuwa na mvuto wa kipekee. Kimuonekano alikuwa mrefu, mweusi hivi na mwili mkubwa wa kuvutia, mabinti wa Kwarara nao hawakuwa nyuma kutumbukia katika shimo la kuvutiwa nae kwa sifa zake, sifa za kimuonekano wake wa kuvutia na nyinginezo kedekede zilizogeuzwa wimbo mitaa hiyo ya Kwarara.
Moja kati ya manzi waliovutiwa sana na Leo, alikuwako aliyeitwa Nema.
Na alikuwa yuko karibu sana na Leo, kwasababu kadha, mamake Leo na mamake huyo Nema walikuwa marafiki wakubwa na walikuwa wakifanya pamoja kazi ya kuuza samaki maji chumvi katika soko kuu hapo katika huo mji wa Morogoro. Pia Nema alikuwa akielewana sana na Sanura, mdogo wa kike wa Leo, yani dadake.
Pia, Nema, alisoma pamoja na leo katika shule ya Eastsides Secondary, tena darasa moja la kidato cha sita.

Hivyo Nema alikuwa yuko karibu na Leo. Alikuwa siku zote yupo viwanja vya mpira kumshangilia Leo kila alipocheza mpira. Na kwakuwa walisoma darasa moja, Nema alikuwapo darasani kumpigia makofi Leo kila Leo aliporudishiwa mitihani na testi walizofanya, ambayo mara nyingi ilikuwa eidha Leo ndio kaongoza ama yuko miongoni mwa top’ tano ya wanafunzi walioufaulu kila mtihani uliorudishwa. Hii ilipelekea Nema kuwa mpiga makofi maarufu darasani mwao maana ilikuwa lazima apige makofi mana ilikuwa Leo lazima afaulu, halafu nayeye hangeweza kuacha kupiga makofi na aliyapiga makofi hayo kwa moyo mmoja.
Kwa Nema, Leo alivutia sana. Hata hakukumbuka alianza lini kumuona Leo anavutia jinsi hiyo, alihisi kuwa alivutiwa nawe toka yuko mdogo kabisa.

……

Hata, ikatukia siku moja Nema alikaa katika baraza ya nyumba yao hapo mtaani kwao Kwarara, huku akisikiliza kipindi cha jioni cha masihara mengi kilichoitwa Jahazi, na watangazaji wakawa wanazungumzia kitu kilichoitwa “first love”. Watangazaji walizungumzia jinsi kuwa kwa kila mwanadamu kuna yule mtu wa kwanza ambaye inatokea amempenda, kwa dhati, amevutiwa nae kwa dhati na kuhisi kuwa na hamu ya kuwa nae tu kupiga nae stori, akiwa mbali nae anammisi. Watangazaji hao waliendelea kuzungumza kuwa hali hiyo imtokeapo mtu kwa mara ya kwanza kabisa, kuwa mtu anahisi moyoni mwake hakuwahi kabla ya hapo kumtamani mtu mwengine jinsi hiyo ila hiyo ndo mara ya kwanza, basi hiyo inaitwa “first love”.

Nema aliyekuwa akisikiliza maongezi ya watangazaji hao wa kipindi hicho cha alasiri alijikuta akiguswa sana na mada waliyoiongelea. Ilikuwa kama walikuwa wakiongelea kitu kilichokuwa kikimtokea yeye.
Alihisi moyoni mwake na aliona kwa hakika kuwa yeye alikuwa katika hiko kitu kinaitwa “first love”. “First love”, kwa Leo. Kwa hakika moyoni mwake alihisi anampenda, anakuwa na hamu nae kuzungumza nae tu kila apatapo wasaa na hata wakati mwengine alijikuta akiwaza vitu vya kushangaza kichwani mwake.

Leo na Nema walikua wote hapo mitaa ya Kwarara. Walisoma wote toka wako wadogo. Mama zao waliokuwa marafiki wakubwa walifanya Nema kuwa karibu na Leo na dadake, Nema alikumbuka jinsi tangu wako wadogo walikua wakicheza pamoja,
Leo na Nema walifundishana kuendesha baiskeli, utukutu wa kupanda juu ya miti, kushona mipira ya sodo. Nema alikumbuka jinsi walikuwa wachelewaji namba na usafi waliokubuhu kipindi wako shule ya msingi, kabla ya kuanza kubadilika na Leo kuanza kubeba sifa nzurinzuri shuleni na mtaani.
Sasa ilikuwa ni dhahiri kwa Nema kuwa hakumchukulia Leo kama tu rafiki, ama kaka, kama ambavyo ingetegemewa kwakuwa wamekua wote, yeye Nema alivutiwa na Leo, kimapenzi.

--------------------

Basi bwana, iaktukia jioni moja, Nema alikuwapo kwa kina Leo.
Ni hisabati zilizohusisha kukotoa hisabu za kuzidisha na vipeo na vipeuo na ‘logarithms’, ndizo zilimfanya awepo hapo kwa kina Leo jioni hiyo, kufundishwa na jiniasi ili kuelewa hisabu hizo zilizokuwa ngumu.
Darsa lao lilienda vizuri, ila kila mmoja kati yao alikuwa na yake akiwaza moyoni.
Nema aliwaza jinsi alivyokaa kwa karibu kabisa na Leo hapo katika kimeza kidogo cha kusomea. Alikuwa kakaa hapo akielekezwa hisabati, ila mwili wake ulikuwa umehemka, na kichwani mwake aliwaza vitu vya kushangaza kabisa. Habari kubwaa.
Kwa upande wa Leo, yeye naye aliwaza mengi kichwani mwake pia.
Kwanza kabisa, hadi wakati huo ilikuwa dhahiri kwake kuwa Nema alikuwa akivutiwa nae. Mana, kwa muda sasa hata yeye Leo aliona vijitabia vya Nema kuwa vilikuwa na dalili vya kumtakataka.
Yani ilikuwa ni habari kubwa, mara binti huyo ampigie makofi meeengi hadi kushangaza watu darasani kila wakirudishiwa mitihani, ama binti huyo kutumia nguvu nyiiingi kumshangilia Leo, kila Leo alipokuwa uwanjani akicheza mpira. Na hii haikuwa kawaida kwasababu Nema hakuwa hivyo kabla.
Pia rafiki zake wa shule walikuwa wakimtania Nema jinsi kila mara, manzi huyo anavyojichangamsha kila amuonapo Leo.
Sasa, hali ilikuwa dhahiri kwa Leo kuwa vijitabia vya Nema alivyovihisi, vilikuwa wazi hata kwa watu wengine wa karibu ikiwamo marafiki wa shule. Na alihisi kabisa kuwa Nema alikuwa akivutiwa nae.
Wakiwa bado wapo hapohapo mezani, sebuleni kwa kina Leo wakisoma, Leo akajikuta akimtumbulia macho Nema, ambaye kwa wakati huo alikuwa bizi na kalamu na daftari lake akisovu mfano wa swali moja gumu la kuzidisha.
Leo alimtumpia macho Nema, na kumuangalia vizuri motto huyo.
Huku kichwani mwake akiwazia muonekano wa kuvutia wa manzi huyo.

Hakika, Nema alikuwa ni binti mzuri, kwa sura ya uchangamfu, na macho makubwa hivi ya kike ya kuvutia,na rangi yake nyeusi ya kuvutia, alikuwa mrefu, mwenye mwili mwembamba wenye nyamanyama mkakamavu hivi na umbo la kuvutia, huku nywele zake za kiuanafunzi zilikuwa zikimpendeza, hata harufu yake tu ilimvutia sana.
Bila ya kufikiria mbali zaidi, Leo akajikuta akisogeza uso wake karibu na uso wa Nema, na wakakutana macho kwa macho na binti huyo hapo mezani.
Kwa sekunde chache wakawa wakiangaliana moja kwa moja machoni.
Kila mmoja damu na mihemko ikichachamaa miilini mwao.
Mara, Leo akagutuka hivi, na kutaka kutoa uso wake toka karibu na uso wa Nema.
Ndipo mara bila ya kutarajia, Nema akachukua mkono wake wa kushoto na kurudisha kichwa cha Leo karibu yake na kisha akjikuta akiweka midomo yake minene ya kike ya kuvutia katika midomo ya Leo na kumbusu, busu kwa hisia na kujikuta wote wakifumba macho huku wamebakisha midomo yao wakibusiana.
Miili yao ilichemka, walihisi damu zao kuchemka kama maji moto.
Mara ghafla Leo akajitoa toka kwenye uso wa Nema na kurejea kukaa vizuri katika kiti chake na mikono kuiweka juu ya meza, kisha akamtupia macho binti huyo. Nema nae ambae, ilikuwa ndio mara ya kwanza kupigana busu la kimahaba namna hiyo, akawa kama ni mwenye kuona haya, Na kuanza kukusanya madaftari yake hapo mezani eti asepe zake.

Mara Leo akamujhoji,“Unafanya nini na daftari, Nema?”, “unakimbiilia wapi Nema?”, alimuhoji na kumshika mkono manzi huyo, ambaye sasa alishakusanya daftari zake na alishanyanyanyuka kitini ili kuondoka humo kwa akina Leo.
“Niache nisepe zangu, Leo, hapa kwa hali hii, tena peke etu wawili tu, hatuwezi kusoma tena”, alijibu Nema.
Ila Leo aliyekuwa na nguvu nyingi, alimvuta binti huyo na kumkalisha kitini tena.
“Kwa hiyo unanikimbia?”, alihoji Leo, huku Nema akimtazama, “samahani sana kama hukutaka nikubusu ila sikuweza kujizuia, hivi unajua una mvuto yani singeweza kabisa”, Leo alimuambia Nema, naye Nema akajikuta akimkatisha.
“Ni mimi ndie niliyeanza kukubusu wewe, ni mimi”, Nema alisema, na kumfanya Leo atabasamu.
“Kutoka moyoni nilikuwa nashindwa nikwambie jinsi gani moyoni mwangu nahisi juu yako nakupenda sana”, alisema Nema, huku akimtazama Leo machoni wakawa wakitazamana, wote walikuwa wakivutiana na kutamaniana, ilikuwa ni hali ya mtego kweli ndani humo jioni hiyo walikuwa wawili peke yao wangeweza kwenda mbali zaidi ya hapo hubusiana walikofikia.
Ila mara mlango wa sebule hiyo waliyokuwamo ukafunguliwa.
Nao wakashtuka na kutupia macho mlangoni na kuona aliyeingia kuwa ni Sanura, dadake Leo.

“Jamani wasomi mnasoma hata leo, mitihani mbona badobado”, alianza kuongea Sanura huku akiweka pembeni viatu alivyovua miguuni.
Kisha akawaelekea hapo mezani walipokuwapo, nao Leo na Nema hawakuwa na la kuongea wakabaki wakimuangalia.
Na mara Nema akashika daftari zake vizuri na kusimama tena ili aondoke.
“hivi unaondoka mara hii, Nema, usinisikilize mie kilaza jinsi ninavyoshangaa mnavyosoma, someni mwaya mfaulu”, aliendelea kuongea Sanura alipoona Nema anataka kuondoka.
Ila Nema akadai kuwa, kweli alitaka kuondoka muda huo kabla hata Sanura hajaingia.
“Sasa basi tumoro, Leo, basi kesho skuli utanielekeza na masomo mengine English na jogi. Jamani kwaherini”, aliaga Nema na kuondoka zake. Na kuwaacha Leo na dadake Sanura.
Sanura aliona kama ilikuwa ajabu kidogo Nema kujikimbiza kuondoka hapo sebuleni mwao baada tu ya yeye kuingia sebuleni hapo.
Basi hapo sebuleni Sanura akaanza kumtwanga maswali kakake, “Hivi Nema kanikimbia mimi au ana haraka gani, nahisi kama kanikimbia mimi”, na Leo akajibu haraka kuwa kwa vyovyote Nema hangeweza kumkimbia Sanura kwa mana hana sababu ya kumkimbia.

“Yani nimehisi tu mana nimeingia, naye huyo kainuka”, aliendelea Sanura,
“Hamna kitu kama hicho wewe, yeye kaondoka kwakuwa alikuwa na plani za kuondoka”, alijibu Leo na Sanura aliona jinsi kakake alivyokuwa kama akimtetea Nema.
“Mbona unatumia nguvu nyingi kumtetea Nema?”, hili swali lilikuwa la kizushi, na Leo hakujibu akamshauri dadake aendelee na shughuli ingine zenye maslahi na amuache na maswali juu ya Nema.
Ila hiyo haikutosha, na Sanura akauliza swali lengine, “Hivi kaka ni kweli huyu Nema ni ‘girlfriend’ wako, mana nakwambia kila mtu anahisi hivyo”
Leo akamrushia macho dadake, na kumjibu, kuwa hakuna kitu kama hicho.
“Siwezi kabisakabisa kuwa na kagirfriend ka Nema kabisa kabisa”, alijitetea Leo, na Sanura akacheka, jinsi kakake alivyotumia nguvu nyingi kukanusha.

…………….


Kitendo cha Nema kufunguka ukweli na kumuambia Leo jinsi gani anampenda ilikuwa ni udhaifu mkubwa.
Mana Leo, hangeweza kuwa na mahusiano na Nema.
Wakati, Nema alimpenda sana Leo, yeye Leo aliona Nema ni mrembo na anavutia ila hakika aliona warembo wengine zaidi kila kona huko shuleni, nyumbani, manjiani, kila pande tena mapini kumzidi Leo na aliamini wengi wao walimkubali kwa mionekano yake ya kuvutia, wala hakujali sana juu ya Nema, ambaye alikua nae pamoja toka utotoni.
Hii ilimfanya Nema kujiona kuwa alifanya kitendo cha udhaifu sana kudhihirisha kwa Leo jinsi alivyohisi katika moyo wake.
Hakuna kilichojengeka kati yao wawili, ila baina yao ilikuwa wazi hisia za Nema kwa Leo.



……………

Shule ya sekondari Eastsides, ambayo ilikuwako mashariki ya maeneo ya kati ya mji huo wa Morogoro, ilikuwa ni shule kongwe na yenye sifa nyingi, hasa ya kuwa shule iliyotoa watu waliopata mafanikio makubwa.
Haikuwa ajabu kusikia info juu ya watu wa habari kubwa kubwa kama wakurugenzi, viongozi wa serikali, wafanyabiashara hata wasanii maarufu ambao walipata kusoma katika shule hiyo.
Miongoni mwa watu hao maarufu waliopitia kusoma shule hiyo alikuwa ni mfanyabiashara maarufu mzee, Habib Nasri.
Habib Nasri mwenyewe, alikuwa ni mmiliki wa mashamba makubwa ya miwa, na ya kilimo cha matunda, pia alimiliki maduka maarufu ya manunuzi ya ‘Habib Malls’ pia alimiliki kituo cha televisheni cha ‘ON tv’. Makampuni hayo yote na mengine kadha yalikuwa chini ya kundi moja lililoitwa ‘Habib Nasri & Family Group of Companies’, ambalo aliliongoza yeye na watu wa familia yake.

Basi watu wotewote walifahmu kuwa shule ya Eastsides ndio shule ambayo alisoma mfanyabiashar huyo Habib Nasri, nayeye mwenyewe aliithamini sana hiyo shule hata ikatokea akatoa ahadi ya kuwa mtu anayegharamia zawadi maalum apewayo mwanafunzi bora kwenye kila mahafali ya kidato cha sita ya shule hiyo ya Eastsides.
Na zawadi hiyo ya mwanafunzi bora, iliangalia sana mwanafunzi aliyekuwa akifanya vizuri katika masomo yake kiujumla, kipindi chote mwanafunzi huyo akiwa anasoma shule hiyo.

Nayo ilikuwa ni zawadi yenye ushindani mkubwa sana wanafunzi walichuana sana madarasani kwa ndoto kuwa waweze kupewa zawadi maalum ya mwanafunzi bora, zawadi ya nishani ya Habib Nasri.

Basi, Leo, ambaye alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi waliokuwa wakifanya vizuri shuleni hapo, Eastsides, alitazamiwa na wengi, ikiwamo wanafunzi weziwe na hata walimu kuwa ni mwanafunzi aliyekuwa na uwezo hasa wa kupokea zawadi ya mwanafunzi bora ya nishani ya Habib Nasri.

Ila, haikuwa tu kitu kidogo cha mchezo mchezo yeye kupewa tu hiyo zawadi ya mwanafunzi bora mana kulikuwapo pia na wanafunzi vichwa wengine wawili shuleni hapo mwaka huo, na walikuwa na sifa hasa za juhudi za kimasomo na waliwania vilivyo zawadi ya mwanafunzi bora, chini ya udhamini wa Habib Nasri.
Kulikuwa na vichwa viwili kimoja kiliitwa Gibson Maganga. Huyo alikuwa ndiye mwanafunzi ambaye alionesha uwezo wa hali ya juu kabisa wa kushindana na Leo.
Mana ngoma ilikuwa, Leo akiongoza katika economics, basi Gibson kapata tisini na tano katika hisabati, na ikatokea Gibson kapata A kwenye somo la histori basi ijulikane, ilikuwa ni Leo aliyeongoza darasa na A yake ya somo la jeografia.
Sasa bwana, nguli wa pili wa masomo, alikuwapo manzi shuleni hapo aliyeitwa Amina, huyu nae hakuwa wa mchezo mchezo huyu yeye alisoma masomo ya sayansi hivyo hakushindanishwa na kina Leo ambao hawakusoma sayansi, ila huyu alikuwa na kila sifa ya kuwa mwanafunzi bora mana alikuwa ni mtu wa kupata A, na ma B+ bhas!, hakuwahi kupata C huyo, toka aingie kidato cha sita somo alilokuwa akifeli sana katika darasa lake la PGM, lilikuwa ni hiyo M, ya mathematics/hisabati, hata ikatukia siku moja kapata B plain ya somo hilo alilia saaaana na hakuhudhuria shule siku mbili kwa uchungu.
Basi ilikuwa ni mshikemshike, kila mtu shuleni Eastsides alitaka afahamu hiyo siku ya mahafali ni nani atabeba zawadi ya mwanafunzi bora, ya kudhaminiwa na mfanyabiashara maarufu, mzee Habib Nasri, iwe ni Leo, Gibson Maganga ama jiniasi Amina.
Moja kati ya watu waliokuwa wanaisuburi hiyo siku kwa hamu na gamu, alikuwa ni mwalimu wao wa somo la jeografia, mwalimu Hemedi Mkumba. Yeye alifundisha wote Amina, Gibson na Leo somo la jeografia na alijua kipaji cha hali ya juu cha kufanya vizuri masomoni kwa kila mmoja wa wanafunzi wake hao, alikuwa na hamu kubwa kutaka kujua idara ya taaluma shuleni hapo itampa zawadi mwanafunzi bora nani kati ya wanafunzi hao watatu ambao yeye mwenyewe alikiri moyoni mwake hakuwahi ona wanafunzi wenye juhudi na akili katika masomo kama wao.

………

Basi kama tu vile waswahili hawakudanganya na kusema siku hazigandi, nazo siku bila hiyana hazikuganda, na siku ya siku ikafika, wanafunzi wa kidato cha sita kuhitimu baada ya kufanya mitihani yao ya mwisho na siku yao ya mahafali ikawadia, siku ilokuwa ikisubiriwa na hamu kubwa, kwa wadau wote, kuanzia walimu, wanafunzi na wazazi wao.
Miongoni mwa watu waliokuwapo shuleni hapo katika mahafali ni mamake Leo, pamoja na mamake Nema, huku Sanura mdogo ake Leo nae alihudhuria pamoja nao.
Ilikuwa ni siku ya kujua nani zaidi kati ya Amina, Leo ama Gibson, nani angethibitishwa kuwa jiniasi wa kidato hicho cha sita cha mwaka huo wa 2007, na ambaye angestahili kuchukua zawadi ya mwanafunzi bora ambayo ilitolewa na mfanyabiashara Habib Nasri.

Siku hiyo ya mahafali, wanafunzi wa kidato cha sita walipendeza sana katika sare zao, walionekana wasafi sana. Wanafunzi wengine wote nao walipendeza na walikuwa na shangwe kama walivyojawa shangwe waalimu wao.
Mgeni rasmi siku hiyo alikuwa ni naibu waziri wizara ya elimu, sayansi na teknolojia na moja kati ya watu waliohudhuria siku hiyo alikuwako huyo Habib Nasri, mdhamnini hasa wa zawadi ya mwanafunzi bora.

Basi shughuli zote za shamrashamra zilifana sana kwa ngonjera, nyimbo na risala na hotuba ya mgeni rasmi, kisha ikafika ule muda wa kutoa zawadi mbalimbali kwa wanafunzi wanaohitimu.
Kila aliyekuwako mahafalini hapo alitega sikio lake vizuri. Na zawadi zikatolewa za nidhamu, usafi, na ya mwanafunzi mwenye kipaji cha uongozi. Zawadi ambayo ilibebwa na Nema rafiki ake Leo, ilikuwa ni mwanafunzi mwenye kipaji cha uongozi. kisha zikaanza zawadi za somo moja moja ambapo Leo alibeba zawadi ya kuongoza jeografia, Gibson akaopoa zawadi ya kuongoza Economics na asiye na mchezo mchezo Amina aliongoza katika somo la fizikia.
Wakawa wanapishana tu jukwaa kuu kuchukua zawadi zao huku umati wa wanafunzi wezao na wazazi ulikuwa ukipiga shangwe.
Sasa ikawadia muda wa kuchukua zawadi ya mwanfunzi bora, wote watatu, Leo, Amina na Gibson wakarushiana macho ya kiiushindani kama tu kila mmoja akimuambia mwezake kuwa yeye ndiye hasa mshindi wa ngoma hiyo, huku umati wa wanafunzi wezao waliokaa wakiwatazama ulilipuka kwa shangwe kuuubwa.

Basi kabla zawadi hiyo kutolewa mwalimu wa taaluma ambaye ndiye alikuwa akitoa hiyo zawadi akamkaribisha mzee Habib Nasri mwenyewe asimame aongee chochote kabla ya zawadi ya mwanafunzi bora aliyoidhamini kutolewa.
Naye akasimama huku akipigiwa makofi, akashika maiki kuzungumza.
“Ndugu mgeni rasmi, mheshimiwa naibu waziri wa elimu, ndugu mkuu wa shule ya Eatsides, waalim, wanafunzi, wageni waalikwa na wazazi wa wahitimu wa kidato cha sita, Asalaam Aleikum”, basi umati ukamuitika kwa kelele “Waaleikum salaam”, kisha akatoa salmu ingine, “tumsifu yesu kristo”, basi nao umati ukaitikia tena na kumalizia kwa shangwe.
Kisha akatulia na kutupia macho wahitimu na akaendelea na hotuba yake,
“Miaka takriban ishirini na sita iliyopita, mnamo mwaka 1986, nilikuwa nahitimu kidato cha sita kama ninyi hapa shuleni Eastsides, sikujua kama baada ya miaka hii mingi baadae ningerudi tena hapa Eastsides kama mtu anayeidhamini zawadi za wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo yao, lakini moyoni mwangu na akilini mwangu nilikuwa na ndoto ya kuwa na mafanikio. Nilikuwa nandoto ambazo leo hii naweza sema zimetimia tena zimepita hata vile nilivyokuwa nikiwazia ndoto hizo”, wakati huo umati wote ulikuwa kimyaa ukimsikiliza kwa makini, naye akawa akiendelea kuhutubia.
“Nilikuwa na ndoto za kupata elimu ya chuo kikuu na kuwa mtaalam hasa wa masuala ya uhasibu ili nije kusaidia vyema biashara iliyokuwa ikiyumba sana ya mzee wangu, marhum Mzee. Jasiri Nasri. Na kweli elimu yangu niliyotafuta iliweza kuletea mabadiliko makubwa biashara yake, nami nawaambia hayo yangu yote ya kufika chuo na kuwa mtu mwenye ilm kubwa yalitokana na msingi mzuri wa elimu niliojengewa ndani ya shule hii ya Eastsides sekondari”,
“Hiyo ilinifanya nionee hata zaidi umuhimu wa elimu niliyokuwa nimeipata ambayo hivi kwamba ndani ya miaka hii ishirini na kitu hivi katika kampuni ya Habib and Family Group nilitoa mchango mkubwa wa kuifanya kampuni hiyo kuwa na jina lenye heshima.
“Hivyo nikaamua lazima nichangie katika juhudi za serikali na taifa letu katika kuchagiza utoaji wa elimu, na mimi nikaona lazima nirejee shuleni kwangu nilikosoma hapa Eastsides, na kutoa michango mbalimbali ikiwamo kufadhili medali ya mwanafunzi bora, kwa gharma zangu ili kuleta uhindani chanya wa kujisomea miongoni mwa wanafunzi kwa lengo la yule aliye bora basi na ashinde hiyo zawadi.”
Baada ya kusema hayo mwalimu wa taaluma aliyekuwa kasimama pembeni ya bwana, Habib Nasri akapewa karatasi ya jina la mwanafunzi aliyeshinda zawadi ya mwanafunzi bora.
Mwalimu wa taaluma huku akiwa na shangwe akashika kipaza sauti na kuanza kuongea,
“Ni ukweli uliowazi toka zawadi ya mwanafunzi bora kuanza tolewa katika historia ya shule hii, haijawahi kutokea mwaka ambao, kulikuwa na ushindani mkubwa kama mwaka huu, lakini lazima apatikane mshindi mmoja wa zawadi ya mwanafunzi bora naye aliyeshinda zawadi hiyo nii…………..”,
mara umati wote ukapiga kimyaaa wakimtolea macho mwalimu wa taaluma na kumsikiliza nani alikuwa anabeba zawadi ya mwanafunzi bora, je ni nguli la uchumi, Gibson, mwanajeografia Leo ama jiniasi la fizikia Amina.
“Mshindi niii Amina Magdangaaaa”, umati wote ukamwagika kwa shangwe za furaha, mana walikuwako wengi waliokuwa wakihisi Amina angebeba, japo pia wengi walifikiri ni Gibson pia kundi kuuubwa hasa la wanafunzi hasahasa wa kike walifikiri ni Leo, ndie hasa angebeba zawadi hiyo. Ila laaa!, haikuwa nyota ya Gibson wala Leo kubeba zawadi hiyo bali ilikuwa ni shangwe za kujigamba Amina, ambaye aliburuza kombi zote za sayansi, hasa kombi yake ya PGM, hasa katika somo matata la Physics.

Basi huku machozi ya furaha yakimdondoka, Amina alitimua mbio hadi jukwaa kuu kupokea zawadi yake iliyotiwa kwenye bahasha na kisha kuvishwa medali ya zawadi hiyo iliyokuwa na maneno “Best Student, Eastsides Secondary, Class of 2007”, ikimaanisha kuwa yeye ndo alikuwa kinara wa kidato cha sita katika shule hiyo kongwe ya Eastsides, ya hapo mjini Mororgoro kwa mwaka huo wa 2007.

Basi Gibson na Leo wakakubali kushindwa na wakaachia tabasamu la sapoti kwa Amina na wakampigia makofi, ikawa shangwe mahafalini hapo, jiniasi lilishabeba zawadi yake.

Basi, sherehe yenyewe ikawa ikifikia ukingoni na watu wote waliokuwako hapo wakawa wakipiga picha na mgeni rasmi, ila mara Leo akasikia sauti ya mwalimu wake wa taaluma ikimuita. Na mara alipomfuata mwalimu huyo akamuambia kuwa Mzee Habib Nasri aliomba apige picha nayeye Leo, pamoja na Gibson na Amina kwa maana alihitaji sana kumbukumbu hiyo ya wanafunzi waliowahi fanya vizuri katika masomo yao hivi kwamba haikuwahi tokea katika histori kongwe ya zaidi ya miaka hamsini ya shule ya Eastsides Secondary School.

Basi picha ikapigwa Amina Magdanga, Gibson Maganga na Leo pamoja na bwana Habib Nasri. Baada ya picha hiyo Habib akawapa mkono kila mmoja wao, na alipompa mkono Leo akautikisa kwa nguvu na furaha hata Leo mwenyewe akafurahi, na mzee Habib akaanza kusema,
“Toka uko vidato vya awali walimu wako wamekuwa wakiimba sifa zako kila nikihudhuria masuala yao mbalimbali na nilihisi kuwa wewe ndo ungeshinda zawadi hii ya leo, ila huyu Amina kakupiku”, wote wakacheka, kisha mzee Habib akaendelea, “Kijana japo umekosa zawadi hii ya mwanzafunzi bora nakwambia kwa juhudi zako ulizoonesha utafika mbali sana”, kisha akaingiza mkono wake mfukoni na kutoa kadi kadhaa na kutoka humo zenyewe akachagua moja na kumpa Leo, ambapo Leo alipoisoma ikawa imeandikwa National Youth For Change Alliance (NYCA), huku ikiwa na tarakimu za namba za simu na adresi ya e-mail. Kisha mzee Habib Nasri akamuambia kuwa NYCA ni umoja wa vijana wenye maono ambapo hukutana kuchagiza na kuzungumzia masuala kama ya kuepuka vishawishi, mbinu za kufanikiwa darasani na kushiriki mambo muhimu muhimu ya kitaifa,
“kijana nina imani kubwa wewe utatumia nafasi nzuri ukijiunga humo na utaweza kutumia nafasi hiyo kukutana na vijana wezio na watu wakubwa na kukufungulia dunia katika ndoto zako za unayotaka kufanikiwa”, alisema mzee Habib na Leo akafurahi sana na kushukuru.
Mara, mamake Leo, pamoja na mdogo ake wa kike Sanura wakiwa na Nema na mamake Nema wakawa wamefika hapo karibu wamesimama, wakiwa na kiwewe cha furaha kumuona mzee Habib mtu mfanyabiashara mkuu akiongea kitu na Leo tena wakiwa na tabasamu kana kwamba hivi ni wanaofahamiana, mara mamake Leo akaomba wote wapige picha na Mzee Habib ambaye naye alifurahi kupiga ingine tena na Leo kijana mwenye juhudi, akiwa pamoja na familia yake. Na wakapiga picha hiyo, kubakia katika kumbukumbu.

Naam, hiyo ilikuwa ndio mara ya kwanza kwa Leo kuonana na Mzee Habib Nasri, lakini kama waswahili hawakudanganya katika kauli zao ya kuwa hakika hakuna ajuaye yanayojipika ili kutoka huko siku za kesho, na kweli wote, si mzee Habib Nasri, wala Leo na mamake ama dadake wala kina family friend Nema na mamake, wote hawakujua kuwa huo ni mwanzo tu wa familia ya kina Leo na ile ya mzee Habib, mfanyabiashara maaruf kuja kuwa zenye ukaribu mkubwa.


Itaendelea………………..
 
Sehemu ya pili;


Maisha baada ya kumaliza kidato cha sita yalimfungua sana akili Leo.
Kipindi chote baada ya kuhitimu alikitumia kumsaidia mamake katika shughuli za uuzaji samaki maji chumvi, Biashara ambayo familia yao iliachiwa na marehemu baba yake alipofariki.
Kumsaidia mamake katika biashara hiyo kulimfanya Leo afahamu jinsi gani mamake alikuwa ni hodari katika shughuli zake hizo. Kumsaidia mamake katika shughuli hizo za uuzaji samaki wa maji chumvi katika soko kuu la mjini kwao kulimfanya aone ni jinsi gani mamake alikuwa ni mwanamke aliyejituma .
Biashara hiyo iliyokuwako katika soko kuu la mji huo wa Morogoro, ilikuwa katika duka kubwa lililokuwa na maneneo,”Kwa wapogoro Fisheries”. mlangoni mwake, duka hilo la samaki lilikuwa maarufu mji wotewote.
Akiwa dukani hapo akimsaida mamake shughuli za hapo dukani Leo alikumbuka jinsi miaka kumi iliyopita, baba yake alivyofariki katika ajali ya gari, na kutia simanzi sana familia yao, na kuwaacha Leo na dada yake wakiwa na mama yao.
Leo alikumbuka jinsi enzi hizo mama yake alijawa na hofu kama angeweza kuendesha biashara hiyo na kuwalea Leo na mdogo ake peke ake. Leo aliona ni jinsi gani mamake aliweza kusimama na kuiendesha biashara hiyo vyema kabisa, hata kufikia wakati huo akawa kaitanua na kuifanya kuwa ni biashara kubwa na yenye umaarufu kwa wakazi wengi wa mji wao, ambao walifunga safari toka kona zote zote za mji kufika hapo sokoni na kununua samaki kwenye duka hilo lao tu.
Leo alipenda sana uzoefu wa mamake wa kupatana bei na wauzaji wakubwa wa samaki wa Dar es Salaam, na jinsi alivyokuwa makini kuhifadhi mzigo wa samaki usiharibike, na mbinu zake za kibiashara kwa ujumla.
Wachuuzi wengi wadogowadogo wa samaki walinunua samaki hapo dukani kwa amake na migahawa kadha ya kuuza chakula ilipata samaki kwa kusambaziwa na duka hilo.
Hivyo moja kati ya mambo aliyokuwa akiyafanya Leo ilikuwa ni kupeleka samaki wabichi katika migahawa, iliyokuwa ikitoa oda ya mzigo dukani mwao.
Basi, moja kati ya migahawa aliyopelekea samaki ulikuwa ni mgahawa ulioitwa “Mahanjumati Restaurent”, uliokuwako katika mtaa maarufu ulioitwa Konga. Mgahawa wenyewe ulimilikiwa na mwanamama mmoja hivi. Basi, siku ya kwanza kufika mgahawani hapo, Leo alipenda sana mazingira ya mgahawa huo, alipenda usafi wa eneo hilo harufu za vyakula za mgahawani hapo hata akawa kasimama ndani ya mgahawa huo, akishangaashangaa uzuri wake wakati akisubiri malipo ya samaki alopeleka hapo, toka kwa mama mmiliki wa mgahawa huo.
Huku akiwa anaangaliaangalia uzuri wa mgahawa huo, mara akagutuliwa na sauti ya kike, sauti ya kuvutia ya kike, ikimwambia, “kaka pesa yako hii hapa”, Leo akamgeukia huyo dada aliyekuwa akimpa malipo ya kupeleka samaki dukani hapo siku hiyo.
Msichana huyo alivutia sana, hivi kwamba, macho yalimtoka Leo na kumrushia msichana huyo. Ndani ya muda mfupi tu akampitishia macho mwili mzima na kumfanyia uchambuzi yakinifu wa harakaharaka kichwani mwake.
Kabla hata hajapokea pesa alokuwa akipewa na mlibwende huyo, Leo akawa kesha toa tathmini kichwani mwake kuwa binti huyo alikuwa ni kifaa cha aina yake, Kwa haraka tu aliona uzuri wa macho ya binti huyo, macho makubwa madogo hivi ya kusinzia mithili ya macho ya mnyama mbuzi. Huku binti huyo aling’ara kwa ngozi yake ya weusi wa kupendeza, mfano wa rangi ya tunda chungwa. Mrembo huyo ambaye alikuwa kavalia tu mavazi ya kupikia katika mgahawa huo alipendeza sana, hivi kwamba. hata Leo akajiuliza harakaharaka, kuwa binti huo alionekanaje avaliapo nguo za kupendeza ikiwa ni mwenye kuvutia hata avaapo manguo ya kufanyia kazi ya kupika.
Muda huo wote Leo akiwa anafanya tathmini zake kichwani, binti wa watu alikuwa akimsubiri apokee pesa ya malipo ya samaki alowaleta, hata mtoto wa watu akawa akimshangaa Leo, na kujiuliza kijana huyo kapigwa na bumbuwazi gani hata hapokei hela yake ya samaki bali kabaki kumkodelea yeye macho.
“Samahani kaka pokea hela yako, unanisimamisha”, alilalama msichana huyo kwa sauti yake ya kuvutia na kumgutua Leo,
“hebu rudia tena, nikusikie vizuri tena”, kwa tabasamu Leo aliomba msichana huyo aongee tena ili mradi tu asikiie tena sauti ya kuvutia ya msichana huyo, ambaye sasa alianza kutia na nyodo za hasira, kumbe hivyo alivyofanya ndio kama alikuwa akizidisha uzri wa sauti yake.
“Nakwambia beba hela yako ya samaki ulo leta nashangaa unanitumbulia macho”, aliongea huyo binti huku akibinua binua midomo yake na sasa akawa mkono mmoja kashika kiuno badili ya ule mwengine aloushika hela alizokuwa akimpa Leo kama malipo ya kuleta samaki mgahawani hapo.
Lakini Leo akazidisha tabasamu lake na akafikicha macho yake kana kwamba amuone vizuri binti hiyo utadhani hakumuona vizuri hadi wakati huo.
Basi, akaipokea hela yake na kumtazama binti huyo na kumtolea maneno, “dada hongera sana, mimi nakwambia sijawahi sikia sauti nzuri kama hii ilotoka kinywani mwako”, hata binti wa watu akaogopa
“Hee we vipi, hiyo sauti yangu vipi iwe hivyo, wakaka wengine sijui mkoje”, safari hii mtoto wa watu alijikaza na kuongea kwa hasira kidogo ila Leo akawa akiyasikilizia kwa maneno yakemakali kwa kufumba macho kabisa, tena kwa hisia, hakika hakuwahi sikia sauti nzuri kama hiyo, kwa mara ya kwanza aliisikia sauti iliyoweza kumtoa nyoka pangoni. Basi huku kafumba macho yake na huku katabasamu na kumshangaza mtotot wa watu alokuwa kamsimamisha tu hapo, Leo akajiongelesha kwa kujiapiza kwa mungu eti, “hakika mungu wangu nashuhudia zile sauti za kutoa nyoka pangoni ni kweli umeziumba na wala si simulizi za kufikirika”
Kufumbua macho yake, akajikuta katupia macho yake kwenye midomo ya binti huyo, midomo minene minene ya kikike iliyovutia saaana.
“Hivi wewe ni malaika?”, Leo aliuliza, na binti wa watu akatoa macho kwa kushangaa, kichwani mwake alihisi, labda huyo mleta samaki mahala hapo siku hiyo alikuwa hayuko sawa kiakili.
Ila mara, wote wawili wakagutuliwa kwa sauti ya ukali ya mama mwenye mgahawa huo, ikitokea toka jiko la mgahawa huo,“we Zuena hebu harakisha kusafisha samaki waloletwa, unafanya nini huko”. Na binti huyo akaitikia na kugeuka haraka kumuacha Leo na matabasamu yake kasimama hapo mgahawani. Leo akabaki kamkodolea macho binti huyo ambaye alielekea mlango wa jiko la mgahawa huo,
ila mara kabla Leo hajageuka kuondoka mahala hapo alimuona binti huyo akigeuka na kumchungulia toka mlango wa huko jikoni, na wakagongana macho na kutazamana, huku Leo akimtazama kwa tabasamu na binti huyo akimtazama Leo kwa mshangao. Kisha binti huyo akatokomea humo jikoni.
Leo, akawa kama asiyejielewa akatoka mgahawani humo huku kafurahi na kutabasamu na kuelekea pikipiki yake alokuja nayo hapo na kuipanda kurejea dukani kwa mamake.
Moyoni mwake alifurahi sana kufahamu jina la binti huyo, Zuena, jina ambalo lilimkumbusha wimbo moja hivi aliousikia utotoni mwake wenye mashairi yaliyomsifu binti mrembo wa kuvutia na tabia za kupendeza aliyeitwa Zuena.

Basi ikawa siku zilizofuata Leo alipeleka tena samaki katika mgahawa huo ambao Zuena alikuwako, na kila siku alifurahia tu kumuona huyo Zuena. Na kila siku aliyopeleka samaki hapo alizidi kumuona Zuena kuwa ni binti aliyevutia na kupendeza.
Huo ukawa ndo mwanzo wa mazoea ya wao wawili. Urafiki wao ukakua zaidi, baada ya Leo kuchukua namba ya simu ya Zuena na kuanzisha mawasiliano ya simu baina yao. Wakawa ni watu wenye maongezi mareefu kwenye simu kila siku, ama kuchati na kutumiana jumbe fupifupi. Na kwa vile wote walikuwa waongeaji, hakuna aliyemchoka mwezie.

…………………

Leo hakuweka wazi uhusiano wake na Zuena, kwa watu wake wa karibu ikiwamo, Nema, binti ambae walikua wote toka wako watoto.
Lakini kila mtu aliyekuwa karibu nae alihisi kuwa Leo kabadilika, kwa maana hakuwa akionekana onekana sana mtaani na hakuwa na muda wa kupiga porojo mtaani na washkaji zake kama zamani, kumbe mwezao muda wake ulikuwa ni yeye na Zuena, Zuena na yeye.
Huyo Nema mwenyewe ambaye alikuwa akimtaka sana Leo, ila Leo hakumtaka, alikuwa na hamu sana ya kufahamu ni kipi hasa kilichokuwa kikimfanya Leo awe biiize zaidi ya kumsaidia mamake kuuza samaki, hivi kwamba alikuwa hana muda wa kuwepo mtaani kupiga stori.
Ila wala haikuchukua muda picha ikaanza kujichora yenyewe, mana mdogo wa kike wa Leo, alikuwa ni mropokaji. Siku moja Nema alikuwa akipiga stori, barazani kwao na rafiki zake, huko nyumbani kwao katika barabara moja ya mitaa ya Kwarara, mmoja wa hao rafiki zake alikuwa ni huyo mdogo wa Leo, Sanura.
Kwenye maongezi yao wakawa wakizungumzia watu wasioonekana mtaani kutokana na kuwa bize, sasa mmoja wa watu hao akatajwa Leo, na wakamzungumzia sana kuwa yuko biize haonekani. Ndipo mdogo wake akaanza kuropoka kuwa kakake lazima atakuwa yuko bize na demu fulani mjini hapo ila tu yeye hamfahamu.
Sanura akropoka zaidi kuwa Leo siku hizo alikuwa ni mtu wa kuongea kwenye simu kwa suti ya chini kwa muda mrefu, kuchati huku akicheka mwenyewe, mida mingine kuchelewa kurudi hom, mdogo wake huyo akaapia kuwa wallahi tena Leo alikuwa na kila dalili alikuwa na demu mahala ambaye alikuwa akimfanya awe biize.
Wakati huo, Nema ambaye aliwahi kufunguka kwa Leo kuwa anampenda sana akabaki akisikiliza jinsi Sanura alivyofunguka juu ya ukweli wa mambo.
Basi ikawa wazi kwake kuwa Leo alimpenda msichana mwengine mbali kabisa na yeye, kwenye moyo ilimuuma na alitaka amfahamu huyo msichana, ili tu kujua huyo msichana alikuwa na vigezo gani vya ajabu hasa hata Leo ampotezee yeye na awe na huyo msichana mwengine.

…………………

“namba unayopiga haipatikani kwa sasa tafadhali jaribu tena baadae”, hiyo ndiyo ilikuwa sauti ya ujumbe aliyopewa Leo kila alipojaribu kumpigia simu mpenzi wake mpya, Zuena, toka asubuhi ya siku hiyo, alishamtumia meseji kibao ila wala hazikujibiwa na Zuena.
Sasa hata alianza kupata wasiwasi, hiyo ilikuwa ni saa sita mchana siku hiyo ya jumapili, na haikuwa kawaida Zuena kutopatikana kwenye simu kwa muda mrefu.
Na kwa kawaida Leo alizoea siku kama hiyo ya jumapili, Zuena alikuwa free hakwenda kufanya kazi mgahawani.
Hivyo kwa vyovyote kulikuwa na jambo lilimfanya Zuena asipatikane kwenye simu, muda wote alokuwa akimtafuta toka asubuhi.
Huku akiwa anaendelea kuchezea simu yake aina ya motorola bapa ya kubofyabofya mara akashangaa mlango wa hapo sebuleni kwao ukifunguliwa na mara akamuona Nema akiingia sebuleni humo. Nema alikuwa usoni machozi yakimtiririka na akionekana mwenye uchungu mwingi sana.
Leo alipomuona Nema tu akajikuta anakunja uso. Kwa maana alifahamu nini kimemleta Nema sebuleni kwao hapo, mana toka jana ya siku hiyo Nema alikuwa haeshi kumsumbua kwenye simu, akimlalamikia Leo kwanini alikuwa na mahusiano na msichana mwengine zaidi yake yeye, wakati yeye Nema alimpenda sana,
Tena Nema alimlalamikia kwa kilio kwanini hakumwambia hapo kabla kuwa ana mahusiano na msichana mwengine hadi akaja kujua kupitia kwa watu mtaani, wakati yeye Nema alimfungukia Leo ukweli wake wote wa jinsi gani alimpenda sana.
Basi huku michozi ikimtiririka sana machoni huku akionekana kuwa na mauchungu mengi Nema akaingia sebuleni humo na kusimama katikati ya sebule hiyo huku akimtazama Leo ambaye sasa alijawa na hasira kwa kumuona Nema hapo, nae Leo akasimama basi, wakawa wakitazamana na Nema, Nema na michozi yake ya uchungu na Leo na hasira zake nyingi.
Huko kujilliza kwa Nema ndiko kulimfanya Leo akasirike hata zaidi, sasa akawa kama anataka kulia kwa hasira, na akaanza kufoka kwa hasira.
“Nema nilishakwambia sikuwahi kuwa na mahusiano na wewe, sijawahi kukutaka, wala sistahili kuona machozi yako ya uchungu kwangu, mimi sikupendi japo unanipenda, lakini dada unaanza kuwa kero, tangu jana unanitumia meseji zako za kunilaumu kwanino niko na msichana mwengine kana kwamba hivi tuna mahusiano wakati hatuna kitu kati yetu”, alifoka Leo.
Kufokewa huko kulimtoa machozi Nema hata zaidi nayo hayo machozi yakamkarahisha Leo hata zaidi,
“Leo, mimi ninakupenda sana, hata nilishakuambia ya moyoni mwangu kwako,”
Wakati huo Leo alimkata Nema bonge la jicho, yani jicho lingekuwa linauwa Nema angeanguka kufa mahala hapo, naye Nema akawa akiendelea kufunguka,
“kweli nimependa nisipopendwa”, aliongea Nema huku akijiliza zaidi, kitu kilichozidi kumtia hasira Leo hata akawa kama anataka kulia kwa hasira, basi wakawa wote kama wanalia sebuleni hapo.
“Umenionesha kwa kila hali kuwa hunipendi hata kidogo, wakati moyoni mwangu nakupenda kwa hakika”alijiliza Nema hata zaidi.
“Nimekuja hapa kukuonesha chozi langu kwa kwa mara ya mwisho, nisingeweza kuongea nawe tu kwenye simu, nimekuja hapa kukuonesha chozi langu la mara ya mwisho, ulione chozi langu labda utanifikiria Leo”,
Leo alishtuka kidogo, “Nikufirie vipi, wewe hebu toa kilio chako sebuleni kwetu nisimfikirie mpenzi wangu nimpendae kwa dhati Zuena nikufikirie wewe, unayetaka mapenzi kimabavu, mtu hakutaki we unamtaka”, alijibu Leo kwa hasira, na Nema akaangua kilio hata zaidi na Leo sasa akawa kamchoka binti huyo, ambaye walikua wote toka wako wadogo na kusoma wote na kuhitimu wote kidato cha sita hata mama zao walikuwa marafiki wakubwa., ila sasa ilionekana mapenzi yalimliza huyo mmoja wa kike tena peke ake.
“Leo, mimi nakutakia kheri katika mahusiano yako na huyo unayemuita Zuena, mimi ukweli wangu unaufahamu jinsi ninavokupenda ila kweli siwezi lazimisha penzi”, aliongea Nema na kuanza kujikaza kutotoa machozi, “Namuomba mungu nami aninyooshee nipate mtu mwengine nitakaye mpenda naye akanipenda kama nionavyo wewe umpendavyo huyo Zuena, hakika huyo Zuena ni binti mwenye bahati sana”, alimaliza kuongea Nema.
Basi, sasa Nema akawa kanyamaza na akaondoka sebuleni humo na kumuacha Leo kabaki mwenyewe sebuleni mwao katibuka akili.
Nema alipotoka tu Leo kwa hasira akauendea mlango wa sebuleni kwao na kuufunga kwa kufuli kana kwamba binti huyo asiingie tena ndani mwao.
Basi akaelekea chumbani kwake na kujitupa kitandani na kufikiria kilio alichokileta Nema sebuleni mwao na kukasirika zaidi, ndipo mara akasikia simu yake ikiita na kukata huko sebuleni, akajiinua na kurejea huko sebuleni na kuona kuwa simu yake ilikuwa na “missed call”toka kwa Zuena.
Haraka sana akampigia, na mara baa ya simu hiyo kupokelewa akasikia sauti ya kilio upande wa pili,
“Zuena vipi mbona kama una kilio mpenzi wangu, halafu mbona hupokei simu yangu mchana wote toka asubuhi?”, aliuliza Leo, na mara Zuena akajibu kuwa alikuwa kafiwa na mama yake na habari ndio alikuwa kapata asubuhi ya siku hiyo, hata simu yake akasahau kuichaji hivyo hata hakupatikana katika simu toka asubuhi.
Leo alishtuka sana na kumwambia Zuena kuwa muda huo huo atafanya haraka afike huko kwao, kisha wakakata simu. Mbiombio Leo akafunga safari kwenda huko kwa kina Zuena alikokuwa akikaa.
Zuena mwenyewe alikuwa akiishi kwa dadake mitaa fulani iliyokuwa ikiitwa mtoni Street, na hapakuwa mbali toka mitaa ya Kwarara kwa akina Leo, hivi kwamba nusu saa tu baade Leo akawa kafika huko mitaa ya mtoni na kuonana na huyo Zuena wake.
Zuena alimuambia Leo kuwa mamake aliyekuwa akiishi huko Babati, alikuwa amefariki kwa mshtuko wa moyo usiku wa kuamkia siku hiyo, na kwamba wao taarifa waliambiwa kwenye simu asubuhi ya siku hiyo. Ilikuwa ni huzuni sana, Zuena alikuwa kajawa na machozi na kulia kwa uchungu.


Basi, huo msiba ulimfanya Zuena aondoke kwenda huko Babati kwa mazishi.
Safari ya huko Babati ambayo Leo alitegemea Zuena angerejea Morogoro ilikuwa ndio kimoja, mana baada ya mazishi Zuena aliombwa na ndugu zake abakie hapo Babati kusaidia kulea wadogo zake ambao mamake aliwaacha.
Hiyo ikawa ndo changamoto ya mwanzo na mwisho ya mahusiano yao hayo ya mwezi mmoja na nusu, Zuena akawa yuko huko Babati, Leo yuko Morogoro, mapenzi yao yakabaki kuwa ya kwenye simu.

…………………

Na muda nao haukuganda kama mwezi mmoja hivi tangu Zuena kuondoka kwenda kwao Babati, matokeo ya kidato cha sita ya mwaka huo wa 2007 yakatoka.
Shule ya sekondari Eastsides ambayo Leo ndiyo alikuwa akisoma ilifanya vizuri sana mwaka huo mana wanafunzi wake wote walifaulu, wengi wakiopoa divisheni wani za pointi za juu kabisa wengine wakipata divisheni ya pili na kadhaa tu wakipata divisheni ya tatu, huku ikitia fora mji mzima wa Morogoro kwa kukosa divisheni nne hata moja, na kupiku shule kadhaa za binafsi na serikali katika ufaulu mwaka huo wa 2007.
Na kama kawaida vichwa vitatu vya hapo Eastsides sekondari, Amina, Gibson na Leo walikuwa ni vinara kila mmoja akipata daraja la kwanza kabisa na kuongoza katika manispaa na mkoa kwa ujumla.
Siku yenyewe ya kupokea hayo matokeo, wakazi wa mitaa hiyo ya Kwarara wote walijua kuwa Leo alikuwa ni miongoni mwa wanfunzi walioongoza katika mitihani hiyo ya kidato cha sita katika ngazi ya mkoa, siku hiyo mtaa mzima uliripuka kwa shangwe na kila aliyemfahamu Leo alimshangalia humo mitaani kila alipoonekana.

Ambaye hakika alifurahi kuliko wote kuwa Leo kafaulu kwa kiwango cha juu kabisa alikuwa ni mamake, bi. Sofia.


“Kila kona ya mitaa ya Kwarara nikipita najua watu wananiangalia, na kunizungumzia kwa kitu cha kujivunia, ‘ona yule anakatiza mamake Leo, yule kijana aliyeongoza mkoa katika matokeo ya mtihani wa kidato cha sita”, mamake alimuambia Leo kwa furaha na kujivuna huku akimkumbatia mwanae na huku wote wakicheka kwa furaha.
“Haya mama ni madogo sana sasa nakwambia, ninaenda chuo kikuu, kubeba na shahada na huko naapia nitaongoza nawe utapata hata sababu nyingi zaidi za kujivunia”, Leo alimuambia mama yake kuendelea kumfurahisha,
“Utazunguka mtaani, huku ukisikia tena watu wakikuzungumzia ‘ona yule Bi. Sofia Mpogoro akipita yule ndo mama wa mwanazuoni maarufu nchini yule kijana Leo Chande’na wakimuona mdogo wangu pia watamzungumzia kuwa yeye ndiye Sanura Chande, dadake ake Leo, aliyebobea”aliendelea kumuambia mamake na wote wakawa wenye furaha humo ndani mwao.

…………………………

Mwaka huo wa 2007, Leo alibahatika kuchaguliwa kujiunga na chuo kikuu kikongwe nchini, chuo kikuu cha Dar es Salaam.
Alifurahia sana kupata nafasi ya kwenda kusoma chuo hicho ambacho alisikia sana juu ya ukongwe na heshima yake alisikia mengi kuhusu chuo hicho.
Chuo chenyewe kilikuwapo huko jijini Dar es Salaam, nacho kilikuwa chuo kikubwa hasa,kilichokuwa kimejengwa katika mandhari eneo la kilima, la juu kidogo penye muinuko hata matokeo yake jina lengine maarufu la chuo hiko likawa ni Mlimani.
Chuo kilikuwa na mandhari ya kuvutia, chenye hewa na maeneo mengi ya kusomea pia miti mingi, na kutoka katika moja ya kona za mlimani hapo chuoni, mtu angeweza kuona mandhari ya majengo ya kuvutia ya Dar es Salaam kutokea kwa mbali.
Leo alifika chuoni hapo kusomea masula ya benki na usimamizi wa fedha. Kitu ambacho alikuwa na ndoto nacho kusomea toka alipokuwa kidato cha sita.
Chuo hicho kikubwa kilikuwa chenye wanafunzi wengi, toka maeneo yoteyote nchini, mabinti waliosoma chuoni hapo walivutia sana na walionekana wa kisasa.
Kila binti aliyesoma hapo alikuwa na mambo ya kizungu,kastaarabika, ana nywele ndefu na rangi ya kuvutia.
Basi huko kwenye hosteli Leo alikofikia, wanafunzi wa mwaka wa pili walikuwa haweshi kuwatisha wao wanafunzi wa mwaka wa kwanza, “ Madogo kuweni makini, UDSM kuna mengi hapa, mademu wetu wa hapa wako wa aina nyingi”, alianza kutoa vitisho, roommate mmoja wa Leo.
“Wapo, walibwende wenye hadhi kubwa na majina katu hamuwezi kuwapata wanatoka na watu wa maana, madogo mkiwatokea hao mtaumia, kuna wala bata, madogo hamna hela za kuwalisha bata hao muwaache, kuna wake za watu hao watasababisha mfe, halafu UDSM hakuna mapenzi hapa ukiwa na demu wako jua ni demu wa chama lote, washkaji zako tu wanaweza kubeba sa usiulize wadau wengine, wanapakua tu, ukipakuliwa demu wako hapa usilielie ”, roommate huyo alisababisha wezie wote wacheke.
Ndipo, mwengine akadakia, “Kuna mademu wengine wana moto, wanavutia, wana akili, wana tokea kwenye pesa na kila kidume hakika angetamani kuwa na mademu kama hao,”chumba kizima kilimgeukia huyo jamaa aliyeongea maneno hayo hapo kitandani mwake alipolala nae akawageukia, na kuendelea kuongea,
“Demu kama Sunaina, ndio kwanza kaingia chuo mwaka huu lakini ni kama vile chuo chote tunamjua, demu huyo ni pini,mtoto kaumbika, kila pande anasifiwa, halafu toto nasikia kichwa noma na pesa hashangai kwao zimejaa”
Basi kila mmoja aliyelala chumba hicho, Leo akiwa mmojawapo alipata hamu hasa ya kumuona huyo asiwaye Sunaina.

……………………

Sunaina mwenyewe alikuwa ni habari nyengine, alikuwa ni binti toka familia ya kitajiri. Aliyevutia sana, japo hapo chuoni alikuwa ndo kwanza kajiunga first year alikuwa tayari kashakuwa maarufu kutokana na ukweli kuwa yeye alikuwa na marafiki wenye majina makubwa makubwa kama vile waigizaji maarufu na wanamziki, pia aliwahi kuonekana katika video ya mwanamziki machachari wa enzi hizo aliyeitwa Jeey Master, na moja kati ya rafiki zke alikuwa ni Wema Wolper ambaye aliwahi kushiriki shindano la ulibwende la taifa, na kuibuka kuwa Miss Tanzania namba mbili mwaka wa 2006.
Sunaina pia alikuwa ni binti mwenye akili sana na aliyesomea katika shule internationale, kama vile Feza girls, pia alisoma sana nje ya nchi, ambapo alisomea nchini uingereza ambako baadhi ya ndugu zake walikuwa wakiishi.
Na ilisemekana chanzo cha kuamua kusomea chuo cha UDSM, ilikuwa ni kukataa kwake kusoma nje ya nchi kwa kuwa alichoka kuzunguka ughaibuni, kitu kilichokuwa tofauti kabisa na watoto wengi wa kitanzania ambao hupendelea kusoma ughaibuni pale uwezo wa familia zao unaporuhusu, yeye ulaya alipachoka hakutaka kusomea huko.
Na tena kutokana na uzuri wake Sunaina aliitwa a.k.a nyingi sana ikiwamo,‘toto Suna’, pia kutokana na rangi yake ya chungwa watu walipenda kumuita ‘orange Suna’, huku mashoga zake walimuita ‘shostito Suu’, huku jina mbadala alilovuma nalo saana lilikuwa ni ‘Miss California’hii ilitokana na ukweli kuwa aliishi mtaa wa matajiri ulioitwa California ambao ulikuwako huko mitaa ya fahari kubwa jijini Dar es Salaam, mitaa ya Oysterbay.
Ila mwenyewe hasa alipenda kuitwa jina lake halisi la Sunaina, na alipenda zaidi kujidhihirisha uwezo wake wa akili kuliko urembo wake, ila tu kwa majaaliwa yake mungu, uzuri wake uling’ara hivi kwamba hangeweza kujizuia watu kumuita majina mengine ya kumuadmire.
Kwanza hapo chuoni alikuwa na jopo lake lake la marafiki wawili ambao muda woote walikuwa wamemzunguka na kumfuata kwa nyuma, alikuwa ndio role model wao, kiongozi kundi lao na ndo staa wao.
Basi bwana, kwa misifa yoote ya Sunaina hakika hakuna mtu ambaye angeweza kuacha kuwa ‘amaized’na binti huyo, hata Leo nae hakujizuia akafuatilia sana habari za binti huyo.
Na siku aliyomuona hakika akakiri moyoni mwake kuwa sifa zimuendee mwenyezi mungu mwingi wa rehema kwa kuijaza dunia kwa kheri nyingi nyingi ikiwamo kheri ya dunia kuwa na kifaa kama huyo Sunaina. Mana haikuwahi tokea, yeye Leo kuona binti mrembo kama Sunaina.

……………………….

Basi bwana, Siku moja Leo alikuwa kenda kufuata kitambulisho chake cha chuo. Basi alisimama kwa muda mrefu katika foleni ili apate kitambulisho hadi akawa akifikia fikia dirisha la mgawa vitambulisho hivyo vya chuo, huku akishukuru kuwa hatimaye kafikia karibu na kupata hicho kitambulisho.
Ila mara mrembo Sunaina nae akafika eneo hilo kufuata kitambulisho chake, na akakuta foleni kuubwa, basi akaitazamaa hiyo foleni na kuona jinsi ilivyo ndefu.
Woote waliokuwa kwenye foleni hiyo walikuwa ni boys na wasichana wachache, na wote walipogundua Sunaina kafika hapo wakamgeukia kumtazama na kumfurahia kama vile waliopigwa bumbuwazi.
Basi Sunaina kuona watu wote wanamchekeachekea akawasogelea karibu na kujilizaliza kikike, “jamani guys, nachelewa kipindi naombeni mnisaidie, guys, nichukue kitambulisho changu please guys, just once”, alilalama mtoto wa kike hapoo nayo majitu katika foleni kama yamechanganyikiwa wakamruhusu awaruke woote akaenda mbele kabisa pale dirishani kuchukua kitambulisho chake.
Leo hakuamini, haikumuingia akilini, yani muda wooote alopoteza kusubiria foleni apate kitambulisho halafu anatokea mtoto wa mtu kisa eti ana shavu zuri kama dodo bivu akubaliwe tu kuiruka foleni,
Basi na yeye Leo akaona haiwezekani akaenda moja kwa moja dirishani pembeni kabisa ya Sunaina na kudai pia apewe kitambulisho, mara kundi la watu wote waliokuwa katika foleni wakamjia juu, akwende zake pale mbele arudi kwenye foleni yake, Leo hakuelewa akapayuka, “mbona huyu Sunaina mna mruhusu kuruka foleni, kwani ana nini kimstahilicho sana kuruka foleni?”, aliuliza Leo, mara wezie wakaanza kumrushia karatasi, “acha ufala toka hapo”, “kaa foleni mbuzi we”, walio kwenye foleni walimtusi na kumzomea hadi akarudi kwenye foleni yake.
Naye Sunaina alipomaliza kuchukua kitambulisho chake dirishani akapita karibu na Leo na kumtizama huku akimtabasamia kisha akarusha nywele zake ndefu za wigi na kuziweka mgongoni, kisha akaaga watu walioko kwenye foleni na kuwashukuru na kusepa. Leo hakuamini kabisa kilichotokea, aliona ni ubaguzi wa hali ya juu.
Ila kilichotokea kilimfanya aone Sunaina alikuwa ni demu matawi kiasi gani, hii ikamtia shauku kumjua Sunaina kiundani zaidi
, basi wala haikumchukua muda akamuelewa vizuri.

Mana, Leo alipoingia chuoni hapo alikuwa na lengo la kujiunga na kundi la vijana lililojiita , National Youth For Change Alliance (NYCA), kundi ambalo Leo alishauriwa ajiunge na mfanyabiashara maarufu aliyehudhuria mahafali yao, kwa kile mfanyabiashara huyo aliona kuwa Leo alistahili kuwa katika umoja kama huo ili kuendeleza uelewa wake wa mambo mbalimbali.

Basi siku ya kwanza tu kwa Leo kuhudhuria kikao cha kundi hilo la wana NYCA, Sunaina naye alikuwapo huko, tena akawa kapewa kiti cha mbele, Leo alistaajabu sana juu ya hadhi zote kubwakubwa anazopewa binti huyo, aliona watu wanamnyenyekea sana binti huyo, eti kisa mzuri na ana jina lenye kaumaarufu.
Basi katika kikao hicho Sunaina alisimama kuongea kama mwanamemba wa kundi hilo la NYCA na kwamba yeye alikuwa ni mwanachama wa NYCA toka zamani, na akajitambulisha kwamajina yake kuwa aliitwa Sunaina Habib Nasri, kisha watu wakampigia makofi naye akakaa chini.
Leo mara moja akagundua kitu, kumbe Sunaina ni binti ake na Mzee Habib Nasri, mzee mfanyabiashara maarufu wa maduka makubwa ya Habib malls. Na mmliki wa mashamba ya miwa na matunda. Mzee ambaye ndiye alidhamini zawadi ya mwanafunzi bora shuleni mwao, zawadi ambayo yeye Leo aliishindania ila hakuipata.
Leo akabaki akimtazama Sunaina aliyekaa meza kuu alimtazama kwa makini binti huyo. Ila akajikuta alitabasamu kwa maana ilikuwa ndio kwa mara ya kwanza kwake kukutana na msichana wa aina ya Sunaina, alifurahia sasa kuonana na mtu wa aina hiyo chuoni, na hakika, aliona atafurahia chuo chake hicho cha UDSM, kama kutakuwepo na watu wa aina hiyo.


Itaendelea……………………….
 
Sehemu ya pili;


Maisha baada ya kumaliza kidato cha sita yalimfungua sana akili Leo.
Kipindi chote baada ya kuhitimu alikitumia kumsaidia mamake katika shughuli za uuzaji samaki maji chumvi, Biashara ambayo familia yao iliachiwa na marehemu baba yake alipofariki.
Kumsaidia mamake katika biashara hiyo kulimfanya Leo afahamu jinsi gani mamake alikuwa ni hodari katika shughuli zake hizo. Kumsaidia mamake katika shughuli hizo za uuzaji samaki wa maji chumvi katika soko kuu la mjini kwao kulimfanya aone ni jinsi gani mamake alikuwa ni mwanamke aliyejituma .
Biashara hiyo iliyokuwako katika soko kuu la mji huo wa Morogoro, ilikuwa katika duka kubwa lililokuwa na maneneo,”Kwa wapogoro Fisheries”. mlangoni mwake, duka hilo la samaki lilikuwa maarufu mji wotewote.
Akiwa dukani hapo akimsaida mamake shughuli za hapo dukani Leo alikumbuka jinsi miaka kumi iliyopita, baba yake alivyofariki katika ajali ya gari, na kutia simanzi sana familia yao, na kuwaacha Leo na dada yake wakiwa na mama yao.
Leo alikumbuka jinsi enzi hizo mama yake alijawa na hofu kama angeweza kuendesha biashara hiyo na kuwalea Leo na mdogo ake peke ake. Leo aliona ni jinsi gani mamake aliweza kusimama na kuiendesha biashara hiyo vyema kabisa, hata kufikia wakati huo akawa kaitanua na kuifanya kuwa ni biashara kubwa na yenye umaarufu kwa wakazi wengi wa mji wao, ambao walifunga safari toka kona zote zote za mji kufika hapo sokoni na kununua samaki kwenye duka hilo lao tu.
Leo alipenda sana uzoefu wa mamake wa kupatana bei na wauzaji wakubwa wa samaki wa Dar es Salaam, na jinsi alivyokuwa makini kuhifadhi mzigo wa samaki usiharibike, na mbinu zake za kibiashara kwa ujumla.
Wachuuzi wengi wadogowadogo wa samaki walinunua samaki hapo dukani kwa amake na migahawa kadha ya kuuza chakula ilipata samaki kwa kusambaziwa na duka hilo.
Hivyo moja kati ya mambo aliyokuwa akiyafanya Leo ilikuwa ni kupeleka samaki wabichi katika migahawa, iliyokuwa ikitoa oda ya mzigo dukani mwao.
Basi, moja kati ya migahawa aliyopelekea samaki ulikuwa ni mgahawa ulioitwa “Mahanjumati Restaurent”, uliokuwako katika mtaa maarufu ulioitwa Konga. Mgahawa wenyewe ulimilikiwa na mwanamama mmoja hivi. Basi, siku ya kwanza kufika mgahawani hapo, Leo alipenda sana mazingira ya mgahawa huo, alipenda usafi wa eneo hilo harufu za vyakula za mgahawani hapo hata akawa kasimama ndani ya mgahawa huo, akishangaashangaa uzuri wake wakati akisubiri malipo ya samaki alopeleka hapo, toka kwa mama mmiliki wa mgahawa huo.
Huku akiwa anaangaliaangalia uzuri wa mgahawa huo, mara akagutuliwa na sauti ya kike, sauti ya kuvutia ya kike, ikimwambia, “kaka pesa yako hii hapa”, Leo akamgeukia huyo dada aliyekuwa akimpa malipo ya kupeleka samaki dukani hapo siku hiyo.
Msichana huyo alivutia sana, hivi kwamba, macho yalimtoka Leo na kumrushia msichana huyo. Ndani ya muda mfupi tu akampitishia macho mwili mzima na kumfanyia uchambuzi yakinifu wa harakaharaka kichwani mwake.
Kabla hata hajapokea pesa alokuwa akipewa na mlibwende huyo, Leo akawa kesha toa tathmini kichwani mwake kuwa binti huyo alikuwa ni kifaa cha aina yake, Kwa haraka tu aliona uzuri wa macho ya binti huyo, macho makubwa madogo hivi ya kusinzia mithili ya macho ya mnyama mbuzi. Huku binti huyo aling’ara kwa ngozi yake ya weusi wa kupendeza, mfano wa rangi ya tunda chungwa. Mrembo huyo ambaye alikuwa kavalia tu mavazi ya kupikia katika mgahawa huo alipendeza sana, hivi kwamba. hata Leo akajiuliza harakaharaka, kuwa binti huo alionekanaje avaliapo nguo za kupendeza ikiwa ni mwenye kuvutia hata avaapo manguo ya kufanyia kazi ya kupika.
Muda huo wote Leo akiwa anafanya tathmini zake kichwani, binti wa watu alikuwa akimsubiri apokee pesa ya malipo ya samaki alowaleta, hata mtoto wa watu akawa akimshangaa Leo, na kujiuliza kijana huyo kapigwa na bumbuwazi gani hata hapokei hela yake ya samaki bali kabaki kumkodelea yeye macho.
“Samahani kaka pokea hela yako, unanisimamisha”, alilalama msichana huyo kwa sauti yake ya kuvutia na kumgutua Leo,
“hebu rudia tena, nikusikie vizuri tena”, kwa tabasamu Leo aliomba msichana huyo aongee tena ili mradi tu asikiie tena sauti ya kuvutia ya msichana huyo, ambaye sasa alianza kutia na nyodo za hasira, kumbe hivyo alivyofanya ndio kama alikuwa akizidisha uzri wa sauti yake.
“Nakwambia beba hela yako ya samaki ulo leta nashangaa unanitumbulia macho”, aliongea huyo binti huku akibinua binua midomo yake na sasa akawa mkono mmoja kashika kiuno badili ya ule mwengine aloushika hela alizokuwa akimpa Leo kama malipo ya kuleta samaki mgahawani hapo.
Lakini Leo akazidisha tabasamu lake na akafikicha macho yake kana kwamba amuone vizuri binti hiyo utadhani hakumuona vizuri hadi wakati huo.
Basi, akaipokea hela yake na kumtazama binti huyo na kumtolea maneno, “dada hongera sana, mimi nakwambia sijawahi sikia sauti nzuri kama hii ilotoka kinywani mwako”, hata binti wa watu akaogopa
“Hee we vipi, hiyo sauti yangu vipi iwe hivyo, wakaka wengine sijui mkoje”, safari hii mtoto wa watu alijikaza na kuongea kwa hasira kidogo ila Leo akawa akiyasikilizia kwa maneno yakemakali kwa kufumba macho kabisa, tena kwa hisia, hakika hakuwahi sikia sauti nzuri kama hiyo, kwa mara ya kwanza aliisikia sauti iliyoweza kumtoa nyoka pangoni. Basi huku kafumba macho yake na huku katabasamu na kumshangaza mtotot wa watu alokuwa kamsimamisha tu hapo, Leo akajiongelesha kwa kujiapiza kwa mungu eti, “hakika mungu wangu nashuhudia zile sauti za kutoa nyoka pangoni ni kweli umeziumba na wala si simulizi za kufikirika”
Kufumbua macho yake, akajikuta katupia macho yake kwenye midomo ya binti huyo, midomo minene minene ya kikike iliyovutia saaana.
“Hivi wewe ni malaika?”, Leo aliuliza, na binti wa watu akatoa macho kwa kushangaa, kichwani mwake alihisi, labda huyo mleta samaki mahala hapo siku hiyo alikuwa hayuko sawa kiakili.
Ila mara, wote wawili wakagutuliwa kwa sauti ya ukali ya mama mwenye mgahawa huo, ikitokea toka jiko la mgahawa huo,“we Zuena hebu harakisha kusafisha samaki waloletwa, unafanya nini huko”. Na binti huyo akaitikia na kugeuka haraka kumuacha Leo na matabasamu yake kasimama hapo mgahawani. Leo akabaki kamkodolea macho binti huyo ambaye alielekea mlango wa jiko la mgahawa huo,
ila mara kabla Leo hajageuka kuondoka mahala hapo alimuona binti huyo akigeuka na kumchungulia toka mlango wa huko jikoni, na wakagongana macho na kutazamana, huku Leo akimtazama kwa tabasamu na binti huyo akimtazama Leo kwa mshangao. Kisha binti huyo akatokomea humo jikoni.
Leo, akawa kama asiyejielewa akatoka mgahawani humo huku kafurahi na kutabasamu na kuelekea pikipiki yake alokuja nayo hapo na kuipanda kurejea dukani kwa mamake.
Moyoni mwake alifurahi sana kufahamu jina la binti huyo, Zuena, jina ambalo lilimkumbusha wimbo moja hivi aliousikia utotoni mwake wenye mashairi yaliyomsifu binti mrembo wa kuvutia na tabia za kupendeza aliyeitwa Zuena.

Basi ikawa siku zilizofuata Leo alipeleka tena samaki katika mgahawa huo ambao Zuena alikuwako, na kila siku alifurahia tu kumuona huyo Zuena. Na kila siku aliyopeleka samaki hapo alizidi kumuona Zuena kuwa ni binti aliyevutia na kupendeza.
Huo ukawa ndo mwanzo wa mazoea ya wao wawili. Urafiki wao ukakua zaidi, baada ya Leo kuchukua namba ya simu ya Zuena na kuanzisha mawasiliano ya simu baina yao. Wakawa ni watu wenye maongezi mareefu kwenye simu kila siku, ama kuchati na kutumiana jumbe fupifupi. Na kwa vile wote walikuwa waongeaji, hakuna aliyemchoka mwezie.

…………………

Leo hakuweka wazi uhusiano wake na Zuena, kwa watu wake wa karibu ikiwamo, Nema, binti ambae walikua wote toka wako watoto.
Lakini kila mtu aliyekuwa karibu nae alihisi kuwa Leo kabadilika, kwa maana hakuwa akionekana onekana sana mtaani na hakuwa na muda wa kupiga porojo mtaani na washkaji zake kama zamani, kumbe mwezao muda wake ulikuwa ni yeye na Zuena, Zuena na yeye.
Huyo Nema mwenyewe ambaye alikuwa akimtaka sana Leo, ila Leo hakumtaka, alikuwa na hamu sana ya kufahamu ni kipi hasa kilichokuwa kikimfanya Leo awe biiize zaidi ya kumsaidia mamake kuuza samaki, hivi kwamba alikuwa hana muda wa kuwepo mtaani kupiga stori.
Ila wala haikuchukua muda picha ikaanza kujichora yenyewe, mana mdogo wa kike wa Leo, alikuwa ni mropokaji. Siku moja Nema alikuwa akipiga stori, barazani kwao na rafiki zake, huko nyumbani kwao katika barabara moja ya mitaa ya Kwarara, mmoja wa hao rafiki zake alikuwa ni huyo mdogo wa Leo, Sanura.
Kwenye maongezi yao wakawa wakizungumzia watu wasioonekana mtaani kutokana na kuwa bize, sasa mmoja wa watu hao akatajwa Leo, na wakamzungumzia sana kuwa yuko biize haonekani. Ndipo mdogo wake akaanza kuropoka kuwa kakake lazima atakuwa yuko bize na demu fulani mjini hapo ila tu yeye hamfahamu.
Sanura akropoka zaidi kuwa Leo siku hizo alikuwa ni mtu wa kuongea kwenye simu kwa suti ya chini kwa muda mrefu, kuchati huku akicheka mwenyewe, mida mingine kuchelewa kurudi hom, mdogo wake huyo akaapia kuwa wallahi tena Leo alikuwa na kila dalili alikuwa na demu mahala ambaye alikuwa akimfanya awe biize.
Wakati huo, Nema ambaye aliwahi kufunguka kwa Leo kuwa anampenda sana akabaki akisikiliza jinsi Sanura alivyofunguka juu ya ukweli wa mambo.
Basi ikawa wazi kwake kuwa Leo alimpenda msichana mwengine mbali kabisa na yeye, kwenye moyo ilimuuma na alitaka amfahamu huyo msichana, ili tu kujua huyo msichana alikuwa na vigezo gani vya ajabu hasa hata Leo ampotezee yeye na awe na huyo msichana mwengine.

…………………

“namba unayopiga haipatikani kwa sasa tafadhali jaribu tena baadae”, hiyo ndiyo ilikuwa sauti ya ujumbe aliyopewa Leo kila alipojaribu kumpigia simu mpenzi wake mpya, Zuena, toka asubuhi ya siku hiyo, alishamtumia meseji kibao ila wala hazikujibiwa na Zuena.
Sasa hata alianza kupata wasiwasi, hiyo ilikuwa ni saa sita mchana siku hiyo ya jumapili, na haikuwa kawaida Zuena kutopatikana kwenye simu kwa muda mrefu.
Na kwa kawaida Leo alizoea siku kama hiyo ya jumapili, Zuena alikuwa free hakwenda kufanya kazi mgahawani.
Hivyo kwa vyovyote kulikuwa na jambo lilimfanya Zuena asipatikane kwenye simu, muda wote alokuwa akimtafuta toka asubuhi.
Huku akiwa anaendelea kuchezea simu yake aina ya motorola bapa ya kubofyabofya mara akashangaa mlango wa hapo sebuleni kwao ukifunguliwa na mara akamuona Nema akiingia sebuleni humo. Nema alikuwa usoni machozi yakimtiririka na akionekana mwenye uchungu mwingi sana.
Leo alipomuona Nema tu akajikuta anakunja uso. Kwa maana alifahamu nini kimemleta Nema sebuleni kwao hapo, mana toka jana ya siku hiyo Nema alikuwa haeshi kumsumbua kwenye simu, akimlalamikia Leo kwanini alikuwa na mahusiano na msichana mwengine zaidi yake yeye, wakati yeye Nema alimpenda sana,
Tena Nema alimlalamikia kwa kilio kwanini hakumwambia hapo kabla kuwa ana mahusiano na msichana mwengine hadi akaja kujua kupitia kwa watu mtaani, wakati yeye Nema alimfungukia Leo ukweli wake wote wa jinsi gani alimpenda sana.
Basi huku michozi ikimtiririka sana machoni huku akionekana kuwa na mauchungu mengi Nema akaingia sebuleni humo na kusimama katikati ya sebule hiyo huku akimtazama Leo ambaye sasa alijawa na hasira kwa kumuona Nema hapo, nae Leo akasimama basi, wakawa wakitazamana na Nema, Nema na michozi yake ya uchungu na Leo na hasira zake nyingi.
Huko kujilliza kwa Nema ndiko kulimfanya Leo akasirike hata zaidi, sasa akawa kama anataka kulia kwa hasira, na akaanza kufoka kwa hasira.
“Nema nilishakwambia sikuwahi kuwa na mahusiano na wewe, sijawahi kukutaka, wala sistahili kuona machozi yako ya uchungu kwangu, mimi sikupendi japo unanipenda, lakini dada unaanza kuwa kero, tangu jana unanitumia meseji zako za kunilaumu kwanino niko na msichana mwengine kana kwamba hivi tuna mahusiano wakati hatuna kitu kati yetu”, alifoka Leo.
Kufokewa huko kulimtoa machozi Nema hata zaidi nayo hayo machozi yakamkarahisha Leo hata zaidi,
“Leo, mimi ninakupenda sana, hata nilishakuambia ya moyoni mwangu kwako,”
Wakati huo Leo alimkata Nema bonge la jicho, yani jicho lingekuwa linauwa Nema angeanguka kufa mahala hapo, naye Nema akawa akiendelea kufunguka,
“kweli nimependa nisipopendwa”, aliongea Nema huku akijiliza zaidi, kitu kilichozidi kumtia hasira Leo hata akawa kama anataka kulia kwa hasira, basi wakawa wote kama wanalia sebuleni hapo.
“Umenionesha kwa kila hali kuwa hunipendi hata kidogo, wakati moyoni mwangu nakupenda kwa hakika”alijiliza Nema hata zaidi.
“Nimekuja hapa kukuonesha chozi langu kwa kwa mara ya mwisho, nisingeweza kuongea nawe tu kwenye simu, nimekuja hapa kukuonesha chozi langu la mara ya mwisho, ulione chozi langu labda utanifikiria Leo”,
Leo alishtuka kidogo, “Nikufirie vipi, wewe hebu toa kilio chako sebuleni kwetu nisimfikirie mpenzi wangu nimpendae kwa dhati Zuena nikufikirie wewe, unayetaka mapenzi kimabavu, mtu hakutaki we unamtaka”, alijibu Leo kwa hasira, na Nema akaangua kilio hata zaidi na Leo sasa akawa kamchoka binti huyo, ambaye walikua wote toka wako wadogo na kusoma wote na kuhitimu wote kidato cha sita hata mama zao walikuwa marafiki wakubwa., ila sasa ilionekana mapenzi yalimliza huyo mmoja wa kike tena peke ake.
“Leo, mimi nakutakia kheri katika mahusiano yako na huyo unayemuita Zuena, mimi ukweli wangu unaufahamu jinsi ninavokupenda ila kweli siwezi lazimisha penzi”, aliongea Nema na kuanza kujikaza kutotoa machozi, “Namuomba mungu nami aninyooshee nipate mtu mwengine nitakaye mpenda naye akanipenda kama nionavyo wewe umpendavyo huyo Zuena, hakika huyo Zuena ni binti mwenye bahati sana”, alimaliza kuongea Nema.
Basi, sasa Nema akawa kanyamaza na akaondoka sebuleni humo na kumuacha Leo kabaki mwenyewe sebuleni mwao katibuka akili.
Nema alipotoka tu Leo kwa hasira akauendea mlango wa sebuleni kwao na kuufunga kwa kufuli kana kwamba binti huyo asiingie tena ndani mwao.
Basi akaelekea chumbani kwake na kujitupa kitandani na kufikiria kilio alichokileta Nema sebuleni mwao na kukasirika zaidi, ndipo mara akasikia simu yake ikiita na kukata huko sebuleni, akajiinua na kurejea huko sebuleni na kuona kuwa simu yake ilikuwa na “missed call”toka kwa Zuena.
Haraka sana akampigia, na mara baa ya simu hiyo kupokelewa akasikia sauti ya kilio upande wa pili,
“Zuena vipi mbona kama una kilio mpenzi wangu, halafu mbona hupokei simu yangu mchana wote toka asubuhi?”, aliuliza Leo, na mara Zuena akajibu kuwa alikuwa kafiwa na mama yake na habari ndio alikuwa kapata asubuhi ya siku hiyo, hata simu yake akasahau kuichaji hivyo hata hakupatikana katika simu toka asubuhi.
Leo alishtuka sana na kumwambia Zuena kuwa muda huo huo atafanya haraka afike huko kwao, kisha wakakata simu. Mbiombio Leo akafunga safari kwenda huko kwa kina Zuena alikokuwa akikaa.
Zuena mwenyewe alikuwa akiishi kwa dadake mitaa fulani iliyokuwa ikiitwa mtoni Street, na hapakuwa mbali toka mitaa ya Kwarara kwa akina Leo, hivi kwamba nusu saa tu baade Leo akawa kafika huko mitaa ya mtoni na kuonana na huyo Zuena wake.
Zuena alimuambia Leo kuwa mamake aliyekuwa akiishi huko Babati, alikuwa amefariki kwa mshtuko wa moyo usiku wa kuamkia siku hiyo, na kwamba wao taarifa waliambiwa kwenye simu asubuhi ya siku hiyo. Ilikuwa ni huzuni sana, Zuena alikuwa kajawa na machozi na kulia kwa uchungu.


Basi, huo msiba ulimfanya Zuena aondoke kwenda huko Babati kwa mazishi.
Safari ya huko Babati ambayo Leo alitegemea Zuena angerejea Morogoro ilikuwa ndio kimoja, mana baada ya mazishi Zuena aliombwa na ndugu zake abakie hapo Babati kusaidia kulea wadogo zake ambao mamake aliwaacha.
Hiyo ikawa ndo changamoto ya mwanzo na mwisho ya mahusiano yao hayo ya mwezi mmoja na nusu, Zuena akawa yuko huko Babati, Leo yuko Morogoro, mapenzi yao yakabaki kuwa ya kwenye simu.

…………………

Na muda nao haukuganda kama mwezi mmoja hivi tangu Zuena kuondoka kwenda kwao Babati, matokeo ya kidato cha sita ya mwaka huo wa 2007 yakatoka.
Shule ya sekondari Eastsides ambayo Leo ndiyo alikuwa akisoma ilifanya vizuri sana mwaka huo mana wanafunzi wake wote walifaulu, wengi wakiopoa divisheni wani za pointi za juu kabisa wengine wakipata divisheni ya pili na kadhaa tu wakipata divisheni ya tatu, huku ikitia fora mji mzima wa Morogoro kwa kukosa divisheni nne hata moja, na kupiku shule kadhaa za binafsi na serikali katika ufaulu mwaka huo wa 2007.
Na kama kawaida vichwa vitatu vya hapo Eastsides sekondari, Amina, Gibson na Leo walikuwa ni vinara kila mmoja akipata daraja la kwanza kabisa na kuongoza katika manispaa na mkoa kwa ujumla.
Siku yenyewe ya kupokea hayo matokeo, wakazi wa mitaa hiyo ya Kwarara wote walijua kuwa Leo alikuwa ni miongoni mwa wanfunzi walioongoza katika mitihani hiyo ya kidato cha sita katika ngazi ya mkoa, siku hiyo mtaa mzima uliripuka kwa shangwe na kila aliyemfahamu Leo alimshangalia humo mitaani kila alipoonekana.

Ambaye hakika alifurahi kuliko wote kuwa Leo kafaulu kwa kiwango cha juu kabisa alikuwa ni mamake, bi. Sofia.


“Kila kona ya mitaa ya Kwarara nikipita najua watu wananiangalia, na kunizungumzia kwa kitu cha kujivunia, ‘ona yule anakatiza mamake Leo, yule kijana aliyeongoza mkoa katika matokeo ya mtihani wa kidato cha sita”, mamake alimuambia Leo kwa furaha na kujivuna huku akimkumbatia mwanae na huku wote wakicheka kwa furaha.
“Haya mama ni madogo sana sasa nakwambia, ninaenda chuo kikuu, kubeba na shahada na huko naapia nitaongoza nawe utapata hata sababu nyingi zaidi za kujivunia”, Leo alimuambia mama yake kuendelea kumfurahisha,
“Utazunguka mtaani, huku ukisikia tena watu wakikuzungumzia ‘ona yule Bi. Sofia Mpogoro akipita yule ndo mama wa mwanazuoni maarufu nchini yule kijana Leo Chande’na wakimuona mdogo wangu pia watamzungumzia kuwa yeye ndiye Sanura Chande, dadake ake Leo, aliyebobea”aliendelea kumuambia mamake na wote wakawa wenye furaha humo ndani mwao.

…………………………

Mwaka huo wa 2007, Leo alibahatika kuchaguliwa kujiunga na chuo kikuu kikongwe nchini, chuo kikuu cha Dar es Salaam.
Alifurahia sana kupata nafasi ya kwenda kusoma chuo hicho ambacho alisikia sana juu ya ukongwe na heshima yake alisikia mengi kuhusu chuo hicho.
Chuo chenyewe kilikuwapo huko jijini Dar es Salaam, nacho kilikuwa chuo kikubwa hasa,kilichokuwa kimejengwa katika mandhari eneo la kilima, la juu kidogo penye muinuko hata matokeo yake jina lengine maarufu la chuo hiko likawa ni Mlimani.
Chuo kilikuwa na mandhari ya kuvutia, chenye hewa na maeneo mengi ya kusomea pia miti mingi, na kutoka katika moja ya kona za mlimani hapo chuoni, mtu angeweza kuona mandhari ya majengo ya kuvutia ya Dar es Salaam kutokea kwa mbali.
Leo alifika chuoni hapo kusomea masula ya benki na usimamizi wa fedha. Kitu ambacho alikuwa na ndoto nacho kusomea toka alipokuwa kidato cha sita.
Chuo hicho kikubwa kilikuwa chenye wanafunzi wengi, toka maeneo yoteyote nchini, mabinti waliosoma chuoni hapo walivutia sana na walionekana wa kisasa.
Kila binti aliyesoma hapo alikuwa na mambo ya kizungu,kastaarabika, ana nywele ndefu na rangi ya kuvutia.
Basi huko kwenye hosteli Leo alikofikia, wanafunzi wa mwaka wa pili walikuwa haweshi kuwatisha wao wanafunzi wa mwaka wa kwanza, “ Madogo kuweni makini, UDSM kuna mengi hapa, mademu wetu wa hapa wako wa aina nyingi”, alianza kutoa vitisho, roommate mmoja wa Leo.
“Wapo, walibwende wenye hadhi kubwa na majina katu hamuwezi kuwapata wanatoka na watu wa maana, madogo mkiwatokea hao mtaumia, kuna wala bata, madogo hamna hela za kuwalisha bata hao muwaache, kuna wake za watu hao watasababisha mfe, halafu UDSM hakuna mapenzi hapa ukiwa na demu wako jua ni demu wa chama lote, washkaji zako tu wanaweza kubeba sa usiulize wadau wengine, wanapakua tu, ukipakuliwa demu wako hapa usilielie ”, roommate huyo alisababisha wezie wote wacheke.
Ndipo, mwengine akadakia, “Kuna mademu wengine wana moto, wanavutia, wana akili, wana tokea kwenye pesa na kila kidume hakika angetamani kuwa na mademu kama hao,”chumba kizima kilimgeukia huyo jamaa aliyeongea maneno hayo hapo kitandani mwake alipolala nae akawageukia, na kuendelea kuongea,
“Demu kama Sunaina, ndio kwanza kaingia chuo mwaka huu lakini ni kama vile chuo chote tunamjua, demu huyo ni pini,mtoto kaumbika, kila pande anasifiwa, halafu toto nasikia kichwa noma na pesa hashangai kwao zimejaa”
Basi kila mmoja aliyelala chumba hicho, Leo akiwa mmojawapo alipata hamu hasa ya kumuona huyo asiwaye Sunaina.

……………………

Sunaina mwenyewe alikuwa ni habari nyengine, alikuwa ni binti toka familia ya kitajiri. Aliyevutia sana, japo hapo chuoni alikuwa ndo kwanza kajiunga first year alikuwa tayari kashakuwa maarufu kutokana na ukweli kuwa yeye alikuwa na marafiki wenye majina makubwa makubwa kama vile waigizaji maarufu na wanamziki, pia aliwahi kuonekana katika video ya mwanamziki machachari wa enzi hizo aliyeitwa Jeey Master, na moja kati ya rafiki zke alikuwa ni Wema Wolper ambaye aliwahi kushiriki shindano la ulibwende la taifa, na kuibuka kuwa Miss Tanzania namba mbili mwaka wa 2006.
Sunaina pia alikuwa ni binti mwenye akili sana na aliyesomea katika shule internationale, kama vile Feza girls, pia alisoma sana nje ya nchi, ambapo alisomea nchini uingereza ambako baadhi ya ndugu zake walikuwa wakiishi.
Na ilisemekana chanzo cha kuamua kusomea chuo cha UDSM, ilikuwa ni kukataa kwake kusoma nje ya nchi kwa kuwa alichoka kuzunguka ughaibuni, kitu kilichokuwa tofauti kabisa na watoto wengi wa kitanzania ambao hupendelea kusoma ughaibuni pale uwezo wa familia zao unaporuhusu, yeye ulaya alipachoka hakutaka kusomea huko.
Na tena kutokana na uzuri wake Sunaina aliitwa a.k.a nyingi sana ikiwamo,‘toto Suna’, pia kutokana na rangi yake ya chungwa watu walipenda kumuita ‘orange Suna’, huku mashoga zake walimuita ‘shostito Suu’, huku jina mbadala alilovuma nalo saana lilikuwa ni ‘Miss California’hii ilitokana na ukweli kuwa aliishi mtaa wa matajiri ulioitwa California ambao ulikuwako huko mitaa ya fahari kubwa jijini Dar es Salaam, mitaa ya Oysterbay.
Ila mwenyewe hasa alipenda kuitwa jina lake halisi la Sunaina, na alipenda zaidi kujidhihirisha uwezo wake wa akili kuliko urembo wake, ila tu kwa majaaliwa yake mungu, uzuri wake uling’ara hivi kwamba hangeweza kujizuia watu kumuita majina mengine ya kumuadmire.
Kwanza hapo chuoni alikuwa na jopo lake lake la marafiki wawili ambao muda woote walikuwa wamemzunguka na kumfuata kwa nyuma, alikuwa ndio role model wao, kiongozi kundi lao na ndo staa wao.
Basi bwana, kwa misifa yoote ya Sunaina hakika hakuna mtu ambaye angeweza kuacha kuwa ‘amaized’na binti huyo, hata Leo nae hakujizuia akafuatilia sana habari za binti huyo.
Na siku aliyomuona hakika akakiri moyoni mwake kuwa sifa zimuendee mwenyezi mungu mwingi wa rehema kwa kuijaza dunia kwa kheri nyingi nyingi ikiwamo kheri ya dunia kuwa na kifaa kama huyo Sunaina. Mana haikuwahi tokea, yeye Leo kuona binti mrembo kama Sunaina.

……………………….

Basi bwana, Siku moja Leo alikuwa kenda kufuata kitambulisho chake cha chuo. Basi alisimama kwa muda mrefu katika foleni ili apate kitambulisho hadi akawa akifikia fikia dirisha la mgawa vitambulisho hivyo vya chuo, huku akishukuru kuwa hatimaye kafikia karibu na kupata hicho kitambulisho.
Ila mara mrembo Sunaina nae akafika eneo hilo kufuata kitambulisho chake, na akakuta foleni kuubwa, basi akaitazamaa hiyo foleni na kuona jinsi ilivyo ndefu.
Woote waliokuwa kwenye foleni hiyo walikuwa ni boys na wasichana wachache, na wote walipogundua Sunaina kafika hapo wakamgeukia kumtazama na kumfurahia kama vile waliopigwa bumbuwazi.
Basi Sunaina kuona watu wote wanamchekeachekea akawasogelea karibu na kujilizaliza kikike, “jamani guys, nachelewa kipindi naombeni mnisaidie, guys, nichukue kitambulisho changu please guys, just once”, alilalama mtoto wa kike hapoo nayo majitu katika foleni kama yamechanganyikiwa wakamruhusu awaruke woote akaenda mbele kabisa pale dirishani kuchukua kitambulisho chake.
Leo hakuamini, haikumuingia akilini, yani muda wooote alopoteza kusubiria foleni apate kitambulisho halafu anatokea mtoto wa mtu kisa eti ana shavu zuri kama dodo bivu akubaliwe tu kuiruka foleni,
Basi na yeye Leo akaona haiwezekani akaenda moja kwa moja dirishani pembeni kabisa ya Sunaina na kudai pia apewe kitambulisho, mara kundi la watu wote waliokuwa katika foleni wakamjia juu, akwende zake pale mbele arudi kwenye foleni yake, Leo hakuelewa akapayuka, “mbona huyu Sunaina mna mruhusu kuruka foleni, kwani ana nini kimstahilicho sana kuruka foleni?”, aliuliza Leo, mara wezie wakaanza kumrushia karatasi, “acha ufala toka hapo”, “kaa foleni mbuzi we”, walio kwenye foleni walimtusi na kumzomea hadi akarudi kwenye foleni yake.
Naye Sunaina alipomaliza kuchukua kitambulisho chake dirishani akapita karibu na Leo na kumtizama huku akimtabasamia kisha akarusha nywele zake ndefu za wigi na kuziweka mgongoni, kisha akaaga watu walioko kwenye foleni na kuwashukuru na kusepa. Leo hakuamini kabisa kilichotokea, aliona ni ubaguzi wa hali ya juu.
Ila kilichotokea kilimfanya aone Sunaina alikuwa ni demu matawi kiasi gani, hii ikamtia shauku kumjua Sunaina kiundani zaidi
, basi wala haikumchukua muda akamuelewa vizuri.

Mana, Leo alipoingia chuoni hapo alikuwa na lengo la kujiunga na kundi la vijana lililojiita , National Youth For Change Alliance (NYCA), kundi ambalo Leo alishauriwa ajiunge na mfanyabiashara maarufu aliyehudhuria mahafali yao, kwa kile mfanyabiashara huyo aliona kuwa Leo alistahili kuwa katika umoja kama huo ili kuendeleza uelewa wake wa mambo mbalimbali.

Basi siku ya kwanza tu kwa Leo kuhudhuria kikao cha kundi hilo la wana NYCA, Sunaina naye alikuwapo huko, tena akawa kapewa kiti cha mbele, Leo alistaajabu sana juu ya hadhi zote kubwakubwa anazopewa binti huyo, aliona watu wanamnyenyekea sana binti huyo, eti kisa mzuri na ana jina lenye kaumaarufu.
Basi katika kikao hicho Sunaina alisimama kuongea kama mwanamemba wa kundi hilo la NYCA na kwamba yeye alikuwa ni mwanachama wa NYCA toka zamani, na akajitambulisha kwamajina yake kuwa aliitwa Sunaina Habib Nasri, kisha watu wakampigia makofi naye akakaa chini.
Leo mara moja akagundua kitu, kumbe Sunaina ni binti ake na Mzee Habib Nasri, mzee mfanyabiashara maarufu wa maduka makubwa ya Habib malls. Na mmliki wa mashamba ya miwa na matunda. Mzee ambaye ndiye alidhamini zawadi ya mwanafunzi bora shuleni mwao, zawadi ambayo yeye Leo aliishindania ila hakuipata.
Leo akabaki akimtazama Sunaina aliyekaa meza kuu alimtazama kwa makini binti huyo. Ila akajikuta alitabasamu kwa maana ilikuwa ndio kwa mara ya kwanza kwake kukutana na msichana wa aina ya Sunaina, alifurahia sasa kuonana na mtu wa aina hiyo chuoni, na hakika, aliona atafurahia chuo chake hicho cha UDSM, kama kutakuwepo na watu wa aina hiyo.


Itaendelea……………………….
Sehemu ya tatu lin
 
Sehemu ya 3;




Habib Nasri, aliyekuwa moja kati ya wamiliki na mkurugenzi mkuu wa makampuni maarufu ya ‘Habib Nasri & Family Group’ alikuwa kasimama mbele ya kioo cha chumba chake cha kuvalia nguo, na akawa akiiweka tai yake ya rangi nyeusi vizuri shingoni mwake, tai hiyo ilirandana vyema na rangi nyeusi ya suti yake ya gharama.

Kichwani mwake alikuwa na furaha sana. Mana usiku huo yeye na familia yake walikuwa wakielekea kwenye maadhimisho ya kampuni aliyoiongoza ya ‘Habib Nasri & Family Group’ ama HNF, iliyokuwa ikiadhimisha miongo kadhaa tangu kuanzishwa kwake.

Huku akiangalia uso wake kupitia kioo cha hapo chumbani alijikuta akitabasamu kwa furaha.

Lilikuwa ni tabasamu la mafanikio. Alikumbuka vyema miaka hiyo mingi ilopita, yeye kama kijana mdogo aliweza kuchukua biashara ya baba yake iliyokuwa ikiyumba na hatimaye sasa kampuni hiyo ikaja kuwa ni moja ya makampuni maarufu na zenye mafanikio makubwa nchini.


Mara mlango wa chumba hicho ukafunguliwa. Na akaingia humo mke wake , Bi Zuri.

Bwana Habib akamrushia macho mkewe huyo na kuona jinsi gani alikuwa kapendeza kwa mavazi aliyovalia, pamoja na vito vya thamani alivyovalia. Zuri alikuwa ni mwanamke mzuri sana na jioni hiyo alikuwa kapendeza.

“Umependeza sana”, Bwana Habib alimuambia mkewe ambaye alimsogelea hadi hapo aliposimama mbele ya kioo cha humo chumbani, kisha mkwe huyo akampa busu la shavuni, huku akiwa na tabasamu usoni. Kisha wote wakageukia kioo kilichokuwapo mbele yao na kuona jinsi gani walipendeza, na kila moja kati yao alijivunia moyoni mwake.

Kisha huku bwana Habib kamshikilia mkewe mkono wakatoka chumbani humo, wakiwa na tabasamu usoni na kuelekea huko nje ambako dereva alikuwa akiwasubiri kuwapeleka huko kwenye sherehe ya kuadhimisha hayo makampuni yao waliyomiliki wao familia ya kifahari.

Katika ukumbi mkubwa uliokuwamo ghorofa ya tano katika jengo la Habib Towers, ambalo lilikuwa ndio makao makuu ya hayo makampuni ya ‘Habib Nasri & Family’, watu walikuwa wamo humo weshafika wakisubiri sherehe zianze.

Ukumbini humo mlikuwamo na watu waliovalia maridadi na kupendeza. Ukumbi wenyewe ulikuwa ni wa kifahari uliopendeza kwa mar’mar, taa zake za chandelier pamoja na madirisha yake makuubwa ya vioo ambayo kupitia kwayo mataa ya majengo mbalimbali mji yalionekana yakiwaka kwa kupendeza.

Miongoni mwa watu waliokuwa weshawasili ukumbini humo hadi wakati huo, alikuwa ni Sunaina Habib ambaye alikuwa ndiye binti wa hao Habib Nasri a mkewe, Zuri. Pia alikuwako kijana wao mtoto wa kwanza aliyeitwa Imara Habib.

Basi huyo Sunaina na kakake, walikuwa wako bize kusalimiana na watu mbalimbali waliokuwamo ukumbini humo ambao miongoni mwao mlikuwa na wafanyikazi wa kampuni hiyo, pia mameneja, rafiki wa wazazi wao, wanasiasa maaruf, ikiwamo aliyekuwa mwanasiasa machachari na mashuhuri enzi hizo aliyeitwa, Nape Lema, pia kulikuwa na mastaa kadhaa ikiwamo, Lulu Uwoya, ambaye alitumika mara nyingi kutangazia matangazo ya kampuni hiyo.

Waandishi wa habari nao hawakuwa nyuma ukumbini humo wakiwa tayari kabisa kurekodi na kupiga picha matukio yatakayo tukia usiku huo.

Wakiwa watu ukumbini humo wanapata vinywaji, na kupiga soga hapa na pale huku bendi ikiwa inapiga muziki wa taratibu kwa sauti ya chini mara spika za ukumbini humo zikaanza kutangaza na kila mtu akatulia kuwa makini na kumsikiliza MC, ambaye akatangaza kuwa mkurugenzi wa makampuni hayo ya HNF alikuwa akiwasili huku akiambatana na mke wake.

Basi watu wote ukumbini humo wakageuzia macho kwenye lango la kuingia ukumbini humo na kuwaona jinsi Mzee Habib na mkewe wa,ivyoingia humo ukumbini wakiwa wanapendeza katika mavazi yao yaliyorandana vyema, huku nyuso zao zikiwa zimejaa tabasamu, hakika hakuna aliyweza kuzuia tabasamu ukumbini humo maana kila mtu mwalikwa usiku huo alikuwa kaachia tabasamu.


Habib Nasri na mkewe walikuwa na bahati sana, mbali ya ukwasi wao wa mali nyingi, pia watoto wao wawili waliokuwamo ukumbini hapo waliopendezea sana.

Baadae Mzee Habib akaombwa atoe maneno machache ya hotuba, naye akasimama kuongea jinsi ambavyo, miongo kadhaa iliyopita alipoingia kwenye kampuni hii iliyomilikiwa na baba yake, na hata ikaja kuwa maarufu na miongoni mwa brandi zinazoheshimika zaidi nchini huku kampuni hiyo ikijizatiti katika uzalishaji na uuzaji bidhaa kuanzia sekta za kilimo, uuzaji madini, vituo vya runinga, mahoteli, uwekezaji katika ujenzi wa nyumba na majumba, umiliki wa maduka makubwa ya kifahari na uwekezaji katika biashara za usafirishaji.

Ni hatua kubwa kampuni hiyo ilikuwa imefikia mzee Habib akakiri watu wengi walimsaidia katika juhudi zake, hasa wafanyikazi hodari wa kampuni hiyo na watu wengineo wengi ambao wengine walikuwamo hapo ukumbini usiku huo.

Huku akiwa kasimama mbele kabisa ya watu ukumbini humo Mzee Habib akarusha macho yake na kumtazama kwa mkewe, Zuri ambaye alikaa pamoja na watoto wao, Imara na Sunaina, kisha akaendelea kuongea,

“Katika mafanikio ya mwanamume yeyote hakika kuna malkia pembeni yake, nami nasema kwangu huyo malkia si mwengine bali ni mke wangu mpendwa, Bi Zuri. Kwa zaidi ya miaka thelathini ya ndoa yetu, umekuwa ni mwanamke unayeniunga mkono na kunishauri na pia kuwa mama bora kwa watoto wetu Imara na Sunaina ambao kila siku wananifanya niwe baba mwenye kujivunia, nataka kusema asante sana kwako mke wangu kwa kuwa pamoja name miaka yote hii tunayoendelea kuishi amoja”, basi ukumbi wote ukaanza kumpigia makofi Bi. Zuri aliyekuwa ametulia katika meza pamoja na watoto zake, Imara na Sunaina ambao nao walijiunga na watu wengine humo ukumbini kumpigia makofi mama yao.


………………………………………………….



Leo alikuwa amekaa kwenye moja ya vigweta vilivyoko kwenye moja ya bustani zilizoko hapo chuoni kwao mlimani. Alikaa hapo akijaribu kusomasoma mwalimu aliyowafundisha darasani, lakini pia kichwani mwake alijawa na mawazo ya hali tata ya ukata aliyokuwa nayo mifukoni mwake kipindi hicho.

Fedha ilikuwa imekata kabisa miongoni mwa wanafunzi wa chuo yeye akiwamo, hiyo ilitokana na bodi ya mikopo ya elimu ya juu kuchelewesha kuwekea wanafunzi fedha za kujikimu katika akaunti zao.

Hivyo Leo naye alikuwa ni miongoni mwa hao wanafunzi waliokuwa na ukame wa fedha. Kila alilofanya la kutumia hela aliona ni ubadhirifu kwa wakati huo, sasa hata aliacha kula mlo wa asubuhi na kuamua kula mchana na usiku tu katika kile yeye alikiita kubana matumizi .

Leo alikuwa yuko makini na makaratasi yake akiyasoma hata hakushtuka rafiki zake wawili John na Amiga walipomfikia hapo karibu yake kabisa na akashtukia wamemkalia pembeni wakimcheka, walimcheka jinsi alivyokuwa makini na madaftari ilihali alikuwa kajaa njaa, “unachosoma nini hasa, njaa tu wewe, halaf hakuna hata mitihani”, alitania Amiga huku Leo akijikuta akicheka.

“Tunajua una njaa, una hali ngumu kama mie, bodi wametukazia mwanangu, ila we mwezetu pamoja na njaa zote tulizo nazo za kupiga pasi ndefu na kuskipu milo ya mchana na asubuhi na kufutru jioni, wewe bado una munkari wa kusoma, tena wakati amabo hakuna hata mitihani”, aliongea John, amabaye mkononi mwake alikuwa kashikilia gazeti.

Naye Leo huku akicheka na kusikiliza hilo zogo na soga rafiki zake walilomletea akampokonya John gazeti aliloshikilia na kuanza kulisoma.

Kwenye ukurasa wa juu wa gazeti hilo kulikuwa na picha ya Mzee Habib Nasri na mkewe, ambayo ilichukuliwa jana yake katika sherehe za kuadhimisha kampuni ya HNF, iliyokuwa ikimilikiwa na kuongozwa na mzee huyo na familia yake.

Habari yenyewe ilihusu jinsi hayo makampuni ya HNF yalivyoadhimisha kuanzishwa kwake miaka zaidi ya thelathini iliyopita katika sherehe ya aina yake iliyohudhuriwa na mabalimbali maarufu.

Katika gazeti hilo kulikuwako na picha iliyoonesha Mzee Habib akiwa na bintiye Sunaina katika sherehe hiyo. Sunaina ambaye Leo na weziwe walikuwa wakisoma nae chuo kimoja hapo Mlimanai, alikuwa akionekana kapendeza sana kwenye picha hiyo utadhani malaika, huku usoni mwake akiwa kaachia tabasamu huku kasimama pembeni ya baba yake, tajiri maarufu mji mzima.



Leo aliingalia picha hiyo gazetini na kuona ni jinsi gani Sunaina alikuwa ni binti toka familia ya ukwasi na ufahari mwingi. Wezake alokaa nao hapo wakawa wakiongelea jinsi magazeti na vyombo vyote vya habari siku hiyo vilikuwa vimeandika na kuzungumzia juu yam zee Habib Nasri na familia yake na makampuni yao yenye makubwa.

Leo aliona jinsi ambavyo watu wametofautiana sana katika hali za kimaisha, wakati yeye na rafiki zake walijibanabana na mikopo ya bodi ya elimu, Sunaina na familia yake walikuwa wakidili na ishu kubwakubwa za makampuni ya kifamilia na kutokea kwenye magazeti.




Suanaina mwenyewe hapo chuoni, alikuwa akisomea shahada ya ‘Banking and financial services’, kitu ambacho Leo alisomea pia.



Hivyo mara nyingi Leo na Sunaina, walikutana kwenye vipindi vya darasani ama pia kwenye baadhi ya tutorials na hata walikutana katika vyumba vya kufanyia mitihani pia na huko katika maktaba ya chuo walikokuwa wakienda kujisomea hasa kipindi ambacho walikuwa wakijiandaa na mitihani.

Japo walikutana mara nyingi, haikutokea kuzoeana baina yao, yani pamoja na kukutana mara kwa mara maeneo ya hapo chuoni mlimani katika madarasa, konakona na bustani za chuoni hapo wao mazoea yao yaliishia kwenye kusalimiana juujuu tu.

Sunaina mwenyewe alikuwa ni binti aliyejiweka matawi ya juu sana. Yeye alikuwa ni binti aliyevutia sana halafu alikuwa na kaumaarufu, kila mwanafunzi alimfahamu yeye ni nani. Alitoka katika familia maarufu ya mzee Habib Nasri isitoshe Sunaina alikuwa akifahamiana na watu wengi maarufu wa mjini, na kama haikutosha binti huyo alikuwa ni ‘kichwa’ ile mbaya darasani. Yani kwa ujumla Sunaina alikuwa ndio ‘celebrity’ wao hapo chuoni mlimani.

Leo, alivutiwa sana na Sunaina kwa uzuri wake na sifa zake, kwa wengi ilikuwa ngumu kuona kasoro yeyote kwa binti huyo, ambaye kiukweli alikuwa na kasoro ya kuwa na dharau na kauli chafu kutokana na kujiamini kuliko pitiliza na kukosa tabia ya kujali hisia za wengine


…………………………………………………….



Basi siku moja, ikatokea huko katika kusoma kwao madarasani mhadhiri wao akatoa kazi ya darasa zima ambayo ilitakiwa ifanyike katika makundi ya watu wannewanne, basi kwa mara ya kwanza Sunaina na Leo wakajikuta wako katika kundi moja la kufanya hiyo kazi ya ‘lecturer

Kazi yenyewe ndogo ilikuwa ni ya swali lililosomeka ‘kwa kutumia sababu tano eleza kwanini Tanzania bado ni nchi maskini?’,

Leo ambaye alikuwa ni mwenye mshawasha mkubwa wa kufanya kazi za waalim, kichwani mwake akajikuta ana majibu kama mia, na kuanza kuyatema kwa wezake wayaandike kwenye karatasi, na akaanza kuorodhesha pointi zake kwa sauti weziwe wote wakimsikiliza katika hiyo diskasheni yao ambamo Sunaina alikuwa ni moja ya washiriki, “elimu duni, ufisadi na rushwa, mipango isiyo endelevu, teknolojia changa, ukoloni mamboleo”, Leo alikuwa akielezea pointi hizo, huku wezie wakimsikiliza na kuandika pointi hizo kwenye karatasi.

Mara Sunaina ambaye alikuwapo hapo akiandika pointi za Leo, akaacha kuandika, na kumtupia macho Leo huku akirusha nywele zake za wigi kwa nyuma kana kwamba vile ni mzungu, akawa akimshangaa Leo kwa pointi zake hizo za kujibia swali la mwalimu, yeye Sunaina ambaye alikuwa ‘kichwa kwelikweli aliona hicho ambacho Leo alikuwa anakielezea kuwa ni pumba pointi tupu.

“Tafadhali, hizo pointi zako zitatufanya tupate sifuri swali la mwalimu”, aliongea Sunaina na wanafunzi wezie hapo kwenye diskasheni wakamgeukia na Leo nae akamtupia macho yake kwa Sunaina,

“yani hizo pointi ni ‘too weak’, haziko ‘deep’, ni pointi za vilaza wa kidato cha nne ‘guys’, sie ni chuo kikuu lazima tutoe pointi zilizoshiba sio hizi pumba utusomeazo we kaka”, aliendelea kuongea Sunaina kwa nyodo tele.

Leo akabaki kamtolea macho Sunaina, hadi hapo hakuamini kilichotoka mdomoni mwa huyo msichana, Leo aliona maneno ya Sunaina ni yenye dharau nyingi, kwa muda huo tu alimuona binti huyo kuwa ana mdomo mchafu sana.

Basi wote waliokuwapo hapo kwenye diskasheni wakamuomba Sunaina aelezee pointi anazoona zinafaa kujibia swali la mwalimu.

Huku Leo, akiwa kamkazia macho Sunaina, na moyoni mwake kajawa na hasira ya jinsi binti huyo kamfanyia dharau, Sunaina alianza kuelezea pointi alizoona zilifaa kujibu swali la mwalimu,

Tena alianza kutaja pointi hizo kwa nyodo, huku akiongea lugha mseto, “guys listen, hili swali tushafundishwa katika notes, mwalimu anataka tuelezee sababu ya umaskini wa Tanzania kihistoria na sio kwa vijipointi vyepesi vyepesi”, aliongea Sunaina huku wengine wote wakimsikiliza na Leo nusura apasuke kwa jinsi alivyochukizwa na nyodo na tabia ya dharau ya binti huyo.

Sunaina alitoa pointi kwa wezie kuwa ilikuwa ni histori ya ukoloni, idadi kubwa ya wananchi kuendelea kuishi vijijini, elimu ndogo ya wananchi, mzunguko wa umaskini toka kizazi hadi kizazi na vita vya kagera na athari za kubadili mifumo ya uchumi ya ujamaa na ubepari miaka ya sitini na themanini kuwa ni sababu muhimu zaidi za kihistoria zilizodumaza nchi ya Tanzania kiuchumi.

Baada ya kutoa pointi hizo wote waliokuwa katika diskasheni walifurahia majibu ya Sunaina kuwa kweli kweli yalishiba, kasoro Leo tu ndo hakufurahia majibu hayo, yeye hakupendezwa na dharau za binti huyo. Leo alibaki kakwazika hadi mwisho wa diskasheni hiyo.


Basi, siku hiyo nzima Leo aliwaza sana juu ya dharau aliyofanyiwa na Sunaina na kujiuliza sana, ina maana yeye alionekana na msichana huyo kuwa hana akili, kuwa alikuwa lofa sana ama alionekana namna gani hata binti huyo kumfanyia dharau.

Leo hakuwahi kufanyiwa dharau ya waziwazi namna hiyo na mtu yeyote, yeye toka huko alikotoka alichukuliwa ni mwenye akili. Hakutarajia kuoneshwa dharau na mtu yeyote, hasa mtoto wa kike, yeye Leo alijiona ni mwanaume, iweje mtoto wa kike amdharaudharau kimchezomchezo tu, tena katika diskasheni, mbele ya wanafunzi wezao wengine ambao yeye Leo aliona kama ilikuwa ni kadamnasi ya watu jinsi alivyijihisi vibya kwa kudharauliwa.

Siku nzima chuoni hapo aliwaza juu ya dharau ya Sunaina, hadi akaona ‘maji yamemfika shingoni’, na kushindwa kuvumilia na kuamua kumtafuta Sunaina na kumwambia binti huyo ni jinsi gani hakupendezwa na dharau zake, na kwamba kamwe hangeruhusu kudhalilika na kudharauliwa na mtu kama huyo Sunaina.


Sunaina mwenyewe aliyetia hasira watu siku hiyo hakuwa na habari, siku hiyo kwake ilikwenda shwari hadi akamaliza vipindi na akawa akielekea alikopaki gari yake aina ya ‘harrier’ ya rangi nyekundu, gari hiyo yenyewe ilikuwa ndo zawadi aliyopewa na mama yake kwaajili tu ya sherehe yake ya siku ya kuzaliwa ya mwaka huo wa 2008.

Akiwa anajaribu kufungua mlango wa gari hiyo mara akamuona Leo akimfikia hapo karibu. Usoni Leo alionesha kabisa kuwa alikuwa na hasira na Sunaina.

Leo alimfuata hapo ili amuambie binti huyo kuwa hakupendezwa kabisa na dharau aliyomfanyia muda wa diskasheni na kwamba yeye si kijana wa mchezo mchezo wa kutolewa lugha za kifedhuli na binti huyo.

“Wewe Sunaina ni binti mwenye dharau na mdomo mchafu sana. Labda umekuwa hivyo kutokana na masifa wanayokusifia watu na kaumaarufu kako ulichokuwa nacho hapa chuoni,”, aliongea Leo kwa sauti ya kiume na kumkazia macho Sunaina na kumfanya binti huyo atetemeke kidogo.

“Sasa, huo umaarufu wako hapa chuo isiwe kigezo cha kufanyia watu wengine dharau, kuna watu kama mimi hatujazoea kudharauliwa na kutolewa kauli chafuchafu na watu kama nyie manao jiona matawi ya juu kwa kuwa manaingia chuo na magari hayo ya kupewa na baba zenu”, aliendelea kuongea Leo kwa hasira huku Sunaina akimsikiliza kwa mshangao huku nae hasira zikimpanda binti huyo ambaye kila mara alirusha ama kutupia mkono wake wa kulia kichwani kurejesha nywele zake za wigi mgongoni kana kwamba alikuwa mzungu.

“Nyie mabinti mnaoingia chuo na gari za baba zenu mnadharau sana nyie na kuona sie wengine ni wanafunzi nusu, sasa sikia we mdada, heshima kitu cha bure, ulichonifanyia darasani katika ile diskasheni sijakipenda, naomba uache dharau”, alimaliza kuongea Leo na kubaki kumtazama Sunaina ambaye sasa uso wake aliukunja kwa mshangao na hasira kama anataka kuta[pika.

“unajua we kaka. Inaonekana ni kilaza, nilichofanya kilikuwa ni kujibu maswali ya mwalimu na kukuambia ni jinsi gani vijipointi ulivyokuwa ukitupa vilikuwa ni vya kijinga, sasa kama ulikasirika kwa hilo samahani sana”, aliongea Sunaina kisha akaingia ndani ya gari lake midomo akiibinua kwa dharau, huku akirushia nywele zake za wigi kwa mgongoni utadhani ni binti wa kbrazili kumbe ni mbantu toka kabila la wadigo wa huko Handeni Tanga.

Leo akabaki akimuangalia binti huyo kwa hasira na kutokuamini jinsi binti huyo alivyomjibu tena kwa mara ingine kwa dharau.

Basi Sunaina akawasha gari yake na kuondoka eneo hilo, kuelekea kwao.

Na kumuacha Leo kasimama mahala hapo pa kupakia magari na mihasira yake na kuchukizwa kwelikweli na binti huyo toka familia ya mafakhiri.


Itaendelea……………………………………
 

Attachments

  • Screenshot_2017-01-07-21-23-02~2.png
    Screenshot_2017-01-07-21-23-02~2.png
    236.1 KB · Views: 65

Similar Discussions

Back
Top Bottom