Simulizi: Mtoto wa ajabu

Simulizi: Mtoto wa ajabu

bioto

JF-Expert Member
Joined
Oct 1, 2017
Posts
1,261
Reaction score
2,099
MTOTO WA MAAJABU: 1
Mariam alikuwa na mawazo sana kutokana na ile
mimba aliyobeba kupitiliza muda wa kawaida wa
kujifungua yaani miezi tisa kwani kwasasa mimba
yake ilifikisha miezi ishirini na nne yani miaka miwili
bila ya dalili zozote zile za kujifungua na kumfanya
awe na mawazo zaidi, ukizingatia ameshajaribu njia
nyingi ila imeshindikana na hakuwa kabisa na dalili
ya kujifungua wala nini.
Mumewe alimuona mkewe jinsi ambavyo anakosa
raha kila siku, mara kwa mara huwa anamuuliza ila
leo aliamua kukaa nae na kuongea nae vizuri,
alimuuliza
“Mke wangu tatizo ni nini?”
Ila Mariam hakujibu kitu kanakwamba hakusikia
chochote, hii ni kutokana na mawazo ya mbali sana
aliyokuwa nayo hadi mumewe ikabidi amuite kwa
sauti,
“Wewe Mariam, wewe!!”
Ndipo Mariam alishtuka na kumuangalia mume
wake kisha akamuuliza,
“Kumbe unaongea na mimi?”
“Ndio, unajua nakuona huna raha kabisa”
“Naitoa wapi raha mume wangu? Mimba gani hii
jamani! Kwanini hii mimba inanieleleza hivi?
Nimekosa nini mimi? Miaka miwili hii imepita na
mwezi huo unakatika yani mimba imekaa miezi
ishirini na tano kweli!! Hakuna dalili ya uchungu
wala nini halafu hospitali wanasema nisubiri tu,
kwakweli nimechoka”
“Halafu tumbo limekuwa kubwa sana mke wangu
kupita kawaida!”
“Yani hadi kero mume wangu, nachukia hatari basi
tu ila hii hali inanikera sana”
“Ngoja, kesho tutaenda tena hospitali ili kujua ni
kwanini inakuwa hivi ili kama inawezekana hata
operesheni wakufanyie”
“Kila tukienda wanazingua, mimi nimechoka
kwakweli”
“Sawa, ila tutaenda hospitali nyingine lazima tupate
suluhisho la hiyo mimba mke wangu. Mimi binafsi
sijapenda”
“Bora iwe hivyo, kwakweli nimechoka tena
nimechoka sana. Hata mimi sipendi kabisa hali hii,
mtu unakaa na mimba kama unataka kuzaa tembo!!
Ndio mambo gani haya!”
“Pole mke wangu”
Kwakweli Mariam hakuwa na raha kabisa kutokana
na ile mimba, sababu ilimkosesha raha kabisa na
alishindwa kufanya mambo yake mengi sana.
Kesho yake kama ambavyo walipanga na mumewe,
walienda hospitali kwaajili ya kuangalia maendeleo
ya ile mimba na kwanini ilipitiliza muda wake kiasi
kile, waliamua kubadilisha hospitali kwani waliona
labda hospitali ambayo huwa anaenda hawana ujuzi
mzuri kwani alikuwa ameshachoka kuibeba ile
mimba, moja kwa moja walikutana na daktari
ambaye alikuwa ni mtaalamu wa mambo ya
wanawake na kuongea nae na kuhusu swala zima la
kupitiliza kwa ule ujauzito,
“Umesema imepita miaka miwili?”
“Ndio, tena sio miaka miwili tu maana na mwezi
ushakatika sasa, imepitiliza miezi ishirini na tano.
Kwakweli nimechoka, wakati watu hubeba mimba
kwa miezi tisa tu!! Sasa kwanini mimi inakuwa hivi
jamani!”
“Pole sana, ila ngoja kwanza tukakupige ultrasound
halafu nijue ni kitu gani kinaendelea”
Walikubali na moja kwa moja walienda kwenye
vipimo, majibu yalipotoka walienda kuongea na
daktari,
“Kwanza hongera
sana, inaonyesha umebeba mapacha wa kiume”
“Kheeeee mapacha tena!”
“Mbona unashangaa sasa? Hupendi mapacha au?
Wanawake wengi sana hupenda kuzaa mapacha,
kwani ni raha kuishi nao utapata shida kidogo tu
kwenye malezi kama kipato chako kidogo ila
mapacha ni watoto wazuri sana kwahiyo unatakiwa
kufurahi”
“Haya tuachane na hizo habari dokta, nitajifungua
lini maana nishachoka”
“Sijaona tatizo lolote kwenye mimba yako,
utajifungua tu kawaida”
Basi mume wa Mariam akamwambia daktari,
“Hivi kwani hakuna uwezekano wa mke wangu
kufanyiwa tu operesheni bila kusubiria huo
uchungu?”
“Kwahiyo mnataka kwa operesheni sio!”
“Dokta, nimechoka mimi sijui kama umenielewa
nilivyokwambia kuwa mimba hii imepitiliza miaka
miwili nadhani kitoto kitakachotoka hadi kitakuwa
kinatembea”
Dokta akacheka kidogo huku akitikisa kichwa na
kusema,
“Sawa, ngoja niwapangie siku ya kuja kufanya hiyo
operesheni”
Dokta akaangalia ratiba yake pale na kuwaambia
kuwa waende kesho kutwa kwaajili ya kufanya hiyo
operesheni.
Mariam alifurahi kwani alishachoka kwakweli, basi
walimaliza pale na kuondoka zao kurudi nyumbani
kwao.
Walipofika nyumbani waliongea kidogo ambapo
mume wa Mariam alimuuliza mkewe,
“Nakumbuka mara ya mwisho tulipopiga ultrasound
tuliambiwa ni mtoto mmoja, sasa leo imekuwaje
tena ni mapacha?”
“Yani na wewe unashangaa tu habari za mapacha
badala ya kushangaa swala la kukaa na mimba
miaka miwili jamani!! Yani mimi nimechoka, hata
wawe mapacha sijui vitu gani watoke tu, nimechoka
kwakweli”
Kiukweli Mariam hakuwa na raha kabisa ukizingatia
hii mimba ndio imesababisha hadi yeye na
mumewe kwenda kuhamia sehemu ya mbali kwani
akikumbuka watu wanaomfahamu walikuwa
wakimshangaa sana kuwa bado hajajifungua! Na
yeye ilikuwa inampa hasira sana wakimshangaa
ndiomana na mumewe waliamua kuhamia mbali na
kuishi wenyewe bila ya watu wanaowafahamu vizuri
kuwa karibu.
Mumewe alimuuliza Mariam,
“Leo ungependa kula nini?”
“Kama kuna chakula cha kuleta uchungu basi mimi
ndio nakitaka hiko chakula, sijui kama na wewe
unanielewa kuwa nimechoka!”
Mumewe hakuongea sana kwani alikuwa akijua wazi
muda mkewe njaa ikimshika basi huwahi kwenye
majungu mwenyewe na kutafutiza chakula, ila muda
huu sababu ana hasira ndiomana alijibu hivi.
Siku ilifika ambapo Mariam alitakiwa kwenda
kufanyiwa upasuaji, kwahiyo walijiandaa na vifaa
pamoja na mumewe na kwenda hospitali,
hawakuwaambia ndugu maana sio kwamba hii ni
mara ya kwanza kuamua hivi hapana, ila ilishawahi
kutokea na haikuwa na mafanikio.
Na ndivyo ilivyokuwa hata kwa siku hii, ilionekana
presha ya Mariam ipo juu sana kiasi kwamba
ilikuwa ngumu kwa yeye kufanyiwa upasuaji,
kwakweli Mariam alichukia sana na kurudi na
mumewe nyumbani.
“Jamani Juma, hali hii hadi lini mimi nimechoka”
“Pole mke wangu, ila mimi naamini tu kuwa
mambo yatakuwa sawa”
“Kama hao mapacha si watoke tu, loh nimechoka
sana”
Mariam aliamua kwenda kulala, wakati huo Juma
alimpigia simu mama yake na kumueleza kile
ambacho kimetokea,
“Kheeee mlienda tena hospitali halafu yametoka
kama yale yale?”
“Ndio mama”
“Khaaaa, mimi nataka mjukuu jamani. Kuna mtu
namsubiri kaniambia ataniletea dawa nyingine ya
kieyeji”
“Unadhani hiyo itafanya kazi vizuri mama?”
“Ndio, aliyeniambia safari hii namuamini, hana
mambo ya longolongo kabisa, kwahiyo hata msijali”
“Sawa mama”
Juma alienda kumpa hiyo habari Mariam na
kumfanya Mariam afurahi sana,
“Kheeee afadhari yani, nimechoka sana loh!”
“Usijali, hata mimi nakuonea huruma”
“Ila isiwe kama ile midawa ya kipindi kile jamani,
hakuna kitu kinafanyika wala nini!”
“Mama kasema kwasasa ni uhakika”
Basi Mariam alifurahi sana, na hapo hata kula siku
hii alikula vizuri tu.
Siku hii, alifika mama mkwe wa Mariam na
kumkaribisha pale kwao kwa furaha sana kwani
Mariam alichokuwa anataka ni kupata dawa tu, basi
yule mama alianza kuongea na Mariam pale kuhusu
dawa aliyomletea,
“Kwanza pole mwanangu unajua ni nini,
nimehangaika yani kuipata hii dawa balaa, unajua
mwanzoni nilijua umechezewa yani umerogwa!”
“Ndio nimerogwa mama”
“Hamna Mariam, nasikia kuna kosa umefanya”
“Kheeee kosa gani sasa ambalo mimi silijui?”
“Mimi silijui pia, ila nasikia kuna kosa umefanya,
kuna kitu ulikatazwa kufanya sijui kukila wakati una
mimba halafu wewe ukakifanya na ndio kimekuletea
matatizo hayo”
Mumewe akadakia,
“Inawezekana mama, maana wakati Mimba changa
khaaa Mariam alikuwa anakula hovyo hovyo yani”
“Hata mimi nakumbuka, yani mimba za wenzie
zikiwa changa huwa utakuta tunapatwa na
vichefuchefu na kula kula hovyo hatuwezi mpaka
mimba iongezeke kidogo ila Mariam khaaa ulizidi
mkwe wangu jamani nakumbuka kuna siku
nimekukuta unakula hadi mbegu za mapapai”
“Jamani mama, yani huwezi amini wakati mimba hii
ilivyokuwa changa nilikuwa natamani kila
kilichokuwa kinakuja mbele yangu na nilikuwa
sishibi, nakumbuka kuna vyakula vingine vilikula
hadi aibu kuvisema ila mbegu za mapapai ni dawa
mama”
“Kweli ni dawa ila sio kwa mtindo ule ambao
ulikuwa unakula wewe”
Mumewe akasema,
“Mimi nakumbuka, kuna siku Mariam ulikamata
kindege kidogo ndani ukakinyonga na kukichoma
halafu ukakila khaaa nilikushangaa sana, kwahiyo
inawezekana kweli ulikula vitu vya ajabu”
“Na ndio nilivyoambiwa wanangu, tunaambiwa
hakuna cha mchawi wala nini, inasemekana Mariam
hakurogwa wala nini ila kuna kitu alikosea, ila
nimepewa hii dawa itaenda kumsaidia”
Mariam hakutia neno kwa wakati huu kwani yeye
cha msingi alitaka kusaidiwa tu maswala ya kula
kula hovyo kwanza hakuona kuwa ni tatizo kwani
wenye mimba wengi huwa wanatamani hata vitu
visivyokuwepo, kwahiyo alikuwa akiwasapoti tu
sababu alikuwa akitaka dawa tu kwa muda huo.
Mama mkwe wa Mariam alitoa dawa ambazo
zilikuwa zimefungwa kwenye vifundo vitatu na
kuanza kumuelekeza Mariam namna ya kutumia,
“Ni Hivi, hili fundo la kwanza utaoga siku ya kwanza
yani unachanganya kwenye maji ya kuoga.
Ukishaoga mwenyewe unajimwagia haya maji ya
dawa, hili fundo la kwanza linabeba miezi yote kumi
na mbili yani mwaka mmoja ambao mimba hiyo
imepitilia, halafu siku ya pili utachanganya hili fundo
la pili kwenye maji na lenyewe litabeba mwaka
mzima, halafu hili fundo la tatu utachanganya
kwenye maji siku ya tatu na kuoga, na lenyewe
litabeba huo mwezi mmoja uliopitiliza, baada ya
hapo utapata majibu yake mkwe wangu, lazima
ujifungue, yani nitafurahije jamani! Nataka mjukuu
mimi. Halafu siondoki hivyo, ndio nimekuja moja
kwa moja kwani najua wiki hii hii mambo yatakuwa
tayari”
“Ooooh asante mama, kwahiyo naanza kuoga leo?”
“Ndio, leo leo Mariam, hujalichoka hilo tumbo au?”
“Nimelichoka tena nimelichoka sana”
“Haya, itabidi uanze leo”
“Ngoja nikaianze sasa hivi”
Mariam alichukua ile dawa na kwenda nayo ndani
huku akienda kujiandaa kuoga, basi mama mkwe
wake alibaki na mwanae pale wakiwa wanaongea
ongea kidogo.
“Kwakweli mama nakushukuru sana, nahitaji mke
wangu awe mzima”
“Usijali, mbona huyu anapona kabisa, hakuna tatizo
yule mzee niliyekutana nae unajua hajachukua hata
mia yangu. Kasema kambo yakiwa mazuri basi
nitaenda kumpa zawadi”
“Kheeee kweli huyo ni mganga mama”
“Ni mganga sana, ndiomana kasema ukweli kuwa
Mariam hajarogwa wala nini ila kajiroga mwenyewe”
“Ila sijawahi kusikia mambo haya kabisa mama,
yani nahisi kuna kitu kimejificha hatukijui mama
yangu”
“Tutajua tu hata usijali”
Basi wakaendelea tu na maongezi pale ila Mariam
hakurudi tena pale sebleni wala nini.
Mariam alipomaliza tu kuoga kwa ile dawa akaanza
kujihisi tofauti tumboni, yani kama vile wale watoto
wamefunga kamba tumboni wakiruka ruka.
Alikosa raha na amani kabisa, basi moja kwa moja
akaenda kulala, mumewe akamfata kumuuliza,
“Vipi tena, unajihisi vipi Mariam?”
“Kheeee makubwa yapo hapa jamani, yani hawa
watoto kamavile wanaruka kamba tumboni, yani hii
mitoto itakuwa mikubwa kabisa, mbona kunieleleza
hivi mimi jamani!”
“Pole mke wangu, ila hiyo ya watoto kuruka kamba
tumboni, kweli ni kioja ngoja nikamwite mama”
Mume wa Mariam alimuita mama yake ambapo na
yeye aliambiwa vile vile na Mariam, yule mama
aliupumua kidogo tu na kumwambia Mariam,
“Usijali Mariam, vumilia tu kila kitu kitakuwa sawa.
Naamini kuwa mambo yatakuwa sawa tu, vumilia
Mariam”
“Asante mama”
Basi walimuacha Mariam pale aweze kupumzika
huku wakiendelea na mambo mengine kama
kumtayarishia chakula maana waliona hali yake sio
nzuri kwa wakati huo ila sababu walitaka kuona ile
dawa ikifanya kazi, ilibidi tu wawe wapole na
wavumilie.
Usiku ule ndio Mariam alisema kuwa kidogo tumbo
limetulia na aliweza kukaa na kula chakula kwasasa
huku akiongea na mama mkwe wake,
“Siku hizi utaalamu mwingi, ushajua ni mtoto gani?”
“Mmmmh mama, kwasasa hata jinsia ya mtoto sio
ya muhimu kwangu, cha muhimu ni kushusha huu
mzigo tu”
Mumewe akasema,
“Ni mapacha mama, dokta kasema ni mapacha wa
kiume”
“Ooooh hongera mtoto wangu, ndiomana kuna
mambo ya ajabu yamefanyika hapa kumbe hawataki
hii baraka ije kwetu khaaa!! Hongera sana
mwanangu, umri wako umeenda ila kumbe utapata
mwanamke na atakuzalia uzao wa kwanza midume
miwili”
Mume wa Mariam aliangalia chini tu kiasi kwamba
mama yake alimuuliza,
“Mbona hishangilii sasa?”
“Nishangilie nini mama ikiwa mke wangu anateseka
kwa kiasi hiko? Sikujua kama mapacha ndio
wanasumbua hivi yani, bora angezaa mmoja tu”
“Hamna bhana, huyu uzazi tu umemuendea vibaya,
wala mapacha hawasumbui wala nini ila huyu uzazi
umemsumbua tu huu, sio sababu ya kubeba
mapacha tumboni wala nini!”
Mariam alikuwa kimya kabisa kwani alikuwa
akitamani tu muda ufike aweze kujifungua basi na
sio kuongelea kuhusu watoto aliowabeba tumboni
kwa zaidi ya miaka miwili.
Siku ya pili, Mariam anaenda kuogea tena ile dawa
kama ambavyo alipewa maelekezo na mama mkwe
wake ila baada ya kuoga tu akamsikia mtoto
tumboni kama akibinuka sarakasi na kumfanya
Mariam achukie sana.
Akaenda kwa mama mkwe wake kumlalamikia,
“Mama, yani huyu mtoto kama anabinuka sarakasi
tumboni”
“Khaaaa Mariam, si mapacha hao!! Watakuwa ndio
wanajiandaa kutoka”
“Jamani mama hadi tumbo linaniuma”
“Pole sana”
Mariama akaondoka zake na kwenda kulala ila
kiukweli leo hata kulala hakuweza maana tumbo
lake lilikuwa linacheza cheza muda wote na
kumkosha raha kabisa.
Basi alijigeuza hadi usiku ulifika na hata kula
aligoma kwa siku hii kabisa, yani kwa jinsi
alivyokuwa akijihisi tumboni ilimlazimu kuamua
kwenda kuoga usiku ile dawa ya siku ya tatu kabla
hata siku yenyewe haijafikia vizuri kwani alijihisi
kukereka kwa yale maumivu ya mtoto kujibinua
tumboni.
Sasa alipoanza kuoga na hii dawa akasikia sauti ya
mtoto mdogo,
“Mama, ndio hutaki niendelee kubaki tumboni
mwako?”
Mariam hakutaka kuifatiliza hii sauti wala nini bali
alijimwagia tu ile dawa ila alirudi akiwa na maumivu
makali sana,
“Jamani nakufa, jamani sijawahi kupatwa na
maumivu kama haya, nakufa jamani”
Mama mkwe wake alimfata na alivyomsikiliza vizuri
Mariam akajua tu ni uchungu umemuanza,
“Kheeee mbona mapema kabla hata hujamaliza
dawa?”
Mariam hakumjibu kitu kwani kiukweli alishamaliza
dawa, ule uchungu ulikuwa unamchanganya akili
yake haswaa, yani alikuwa akijihisi vibaya sana.
Basi usiku ule ule mume wa Mariam ilibidi
akatafute usafari ili waweze kuwahi hospitali ili
aweze kujifungua kwa huduma nzuri.
Damu nazo zilianza kummwagika Mariam na
kuonyesha kweli hapo mambo yameiva sasa, mama
mkwe aliendelea tu kumpa moyo,
“Jikaze Mariam, ndio ukubwa huo”
“Mama nakufa mimi, sirudii tena mimi khaaaa ndio
uchungu wenyewe upo hivi! Nakufa jamani, sio kwa
maumivu haya loh!”
Mariam alikuwa akipiga kelel tu, basi usafiri
ulivyofika moja kwa moja waliingia kwenye gari na
kuelekea hospitali.
Walivyofika hospitali, moja kwa moja Mariam
alipelekwa leba maana alionekana kuwa na hali
mbaya tayari.
Daktari alimpiga pale na kusema,
“Khaaaa mtoto katanguliza miguu, hapa hakuna jinsi
ni operesheni tu”
Basi wakaenda kuchukua karatasi za kusaini
waweze kumpeleka Mariam kwenye operesheni ila
muda ule ule wote walishangaa pale Mariam
akijilaza kitandani na mtoto akitoka vile vile akiwa
ametanguliza miguu, yani Mariam alijifungua
kawaida kabisa ingawa mtoto alikuwa katanguliza
miguu.
Kitu ambacho kilimshangaza Mariam, hakujifungua
mapacha bali alijifungua mtoto mmoja, kitu
kilichowashangaza pale leba wote ni kuwa mtoto
wa Mariam baada ya kuzaliwa alikaa mwenyewe
pale kitandani.
 
MTOTO WA MAAJABU 2:
Kitu ambacho kilimshangaza Mariam, hakujifungua
mapacha bali alijifungua mtoto mmoja, kitu
kilichowashangaza pale leba wote ni kuwa mtoto
wa Mariam baada ya kuzaliwa alikaa mwenyewe
pale kitandani.
Walizidi kushangaa zaidi kwa kitendo cha yule
mtoto kushika kitovu na kukikata mwenyewe, yani
pale wodini hakuna aliyebaki kwani wote walikimbia,
alibaki tu Mariam na mtoto wake kwani kila Mariam
alipojitahidi kuinuka alishindwa, alibaki akipiga
kelele tu.
Yule mtoto alimsogelea Mariam na kumuuliza,
“Sasa kelele za nini mama?”
Kisha akajiweka vizuri kwenye mikono ya Mariam na
kuanza kunyonya ziwa la Mariam, kwakweli Mariam
hakuweza kuvumilia hali ile na kujikuta akizimia
pale pale kwa muda ule maana hata nguvu ya
kukimbia hakuwa nayo.
Daktari alienda moja kwa moja kumuita mume wa
Mariam ambapo mume wa Mariam aliambatana na
mama yake kwenda kumsikiliza daktari kuwa ana
hoja gani kwa muda huo kwao,
“Jamani, kuna jambo sio la kawaida limetokea huko
leba”
“Jambo gani tena?”
Dokta aliwaambia tu kifupi halafu akasema,
“Msishangae tumekimbia, katika hali ya kibinadamu
lazima tuogope mambo kama haya, ni kweli
madaktari tunakutana na vitu vya ajabu sana ila
mambo mengine tunaingiwa na uoga”
Basi akaongozana na mume wa Mariam na mama
yake hadi kile chumba ambacho Mariam
alijifungulia maana aliwekwa kwenye chumba cha
peke yake, walimkuta Mariam kazimia ila kale
katoto kapo pembeni kakinyonya na wala hakakuwa
na wasiwasi wowote ule, dokta aliwaambia,
“Mtoto mwenyewe ndio yule pale, hapa hata
nafikiria namna ya kumchukua ili tumfanyie vipimo
kujua kazaliwa na kilo ngapi hata kumpatia chacho
ya kwanza”
Mume wa Mariam akamwambia daktari,
“Sasa dokta, kama wewe unaogopa unataka sisi
tufanyeje? Nenda kamchukue maana hiyo ni kazi
yako”
Basi dokta akataka kwenda kumchukua mtoto ila
huyu mtoto alimpiga jicho hilo dokta na kumfanya
dokta aogope maradufu ila Juma yani mume wa
Mariam alijikuta akijivika ujasiri na kumwambia
mama yake,
“Hivi mama, niogope nini sasa wakati yule aliyelala
pale ni mke wangu na yule ni mtoto wangu!
Niogope nini sasa?”
Juma akasogea karibu na kumchukua mtoto
akamfunga vizuri, kisha akamuomba yule daktari
kumshughulikia mke wake ili waweze kwenda nae
nyumbani.
Na kweli Juma alipombeba yule mtoto ni muda ule
ule yule mtoto alilala kwenye mikono ya Juma ila
hakuna hata mtu mmoja aliyetaka kumshika yule
mtoto kabisa.
Walirudi nyumbani sasa, kiukweli Mariam tangu
ameshtuka hakutaka hata kuulizia habari za mtoto
wala nini ila Juma anamchukua mtoto na kumweka
kitandani karibu na Mariam, hapo Mariam akauliza,
“Hivi mimi ndio nimezaa kiumbe cha ajabu hivi!!”
Mama mkwe wake akamfokea Mariam,
“Weee hebu tema mate chini, kiumbe cha ajabu
kivipi? Ngoja nikuuliza, huyo mtoto hana miguu?”
“Anayo”
“Hana macho, pua, mdomo na masikio?”
“Anayo”
“Hana mikono huyo mtoto? Hana ngozi au hana
nywele”
“Vyote anavyo”
“Sasa unawezaje kumuita mtoto wako mwenyewe
kuwa kiumbe cha ajabu? Tema mate chini Mariam,
hebu angalia jinsi wewe na mumeo mlivyohangaika
kupata hiyo mimba, hebu angalia mlivyohangaika
kumpata huyo mtoto halafu muda huu unasema ni
kiumbe cha ajabu?”
Mtoto aliamka na kuanza kulia, hapa Mariam
alimshangaa zaidi mtoto wake,
“Khaaaa sikumuona jamani, kumbe huyu mtoto ana
meno”
Mariam akaanza kuogopa, basi mama mkwe wake
akaanza kumsema,
“Hebu acha ujinga Mariam, hivi unadhani ni
masikhara kwa mtoto kukaa tumboni miaka miwili?
Lazima mtoto atoke meno hapo, mambo ya dunia
tu yalikuzunguka usiweze kuzaa, sasa umepata
kitoto chako badala ukifurahie unaanza kuhaha na
kasoro za mtoto, sijui ana meno sijui vitu gani, hebu
acha ujinga”
Mariam alikaa kimya na huyu mama mkwe wake
alimtaka Mariam ale chakula ilia toe maziwa mengi
na apate kumnyonyesha mtoto wake, kwahiyo muda
huu mama mkwe ndio alimchukua mtoto
kumbembeleza.
Juma akawapigia simu ndugu zake na ndugu wa
Mariam kuwa Mariam ameshajifungua na hiyo
ilikuwa ni furaha kubwa sana hasa kwa mama yake
Mariam ambaye alikuwa akimuonea huruma sana
binti yake kwa kukawia bila kujifungua,
alimuhurumia kwa kukaa na mimba kwa muda
mrefu.
“Kheee Mungu ni mwema, kwahiyo kaniletea
madume yangu maana aliniambia kuwa ana
mapacha wa kiume”
“Hapana mama, ni mtoto mmoja wa kike”
“Kheeee, si mlisema mmepima hospitali nyie na
kujua jinsia ya mtoto!”
“Ndio mama, ila mara nyingine vipimo navyo
vinakosewa, wale nao ni binadamu wale”
“Mimi nilikuwa nawasikiliza tu na hoja zenu khaaaa,
nitakuja kesho asubuhi huko kumuona mwanangu
na mke mwenzangu, nimefurahi sana. Hongereni
wanangu”
“Asante mama”
Basi kwa muda huu Juma aliamua kwenda mjini ili
kumnunulia vizawadi kidogo mtoto wake ingawa vitu
vingi vya mtoto vilikuwepo ndani ukizingatia
walikuwa wakijiandaa kabisa bila ya mafanikio
yoyote.
Yani usiku wa leo ni Juma tu ndiye aliyeweza kulala
na mtoto pembeni maana Mariam alijikuta
akimuogopa mtoto wake kupita maelezo ya
kawaida, ilikuwa mtoto akiamka na kuanza kulia
ndipo Juma alikuwa akimuamsha mkewe aweze
kumnyonyesha mtoto wao huyu, yani Mariam
hakumtaka kabisa huyu mtoto.
Kesho yake asubuhi na mapema kabisa, alifika pale
mama mzazi wa Mariam na mdogo wake Mariam
aliyejulikana kwa jina la Zayana.
Hata na wao walishangaa kumuona mtoto vile ila
mama mzazi wa Mariam ilibidi tu ajiweke kwenye
nafasi ya umama na kumfundisha mtoto wake
namna ya kumkubali yule mtoto,
“Mariam mwanangu, sijaona tatizo la huyu mtoto”
“Mama, mtoto gani ana meno jamani!”
“Mbona wapo watoto wanaozaliwa na meno
mwanangu?”
“Huwa wanaita meno ya plastiki ila huyu sio meno
ya Plastiki ni meno kabisa ya kikubwa, halafu
ungemuona jana sasa hizo kucha loh! Juma ndio
alimkata”
“Ila mwanangu hiko kitu sio cha kushangaa sana,
mtoto amekaa tumboni kwa miaka miwili! Ulitaka
atoke vile vile akiwa mtoto!”
“Ila mama, laiti na wewe ungekuwepo hospitali na
kuona kituko cha huyu mtoto sijui kama ungemtaka,
unajua kuwa huyu mtoto alijikata kitovu mwenyewe
halafu aliniongelesha!”
“Acha masikhara bhana Mariam, unajua mara
nyingine wazazi tunakumbwa na mambo mengi,
mimi bado sioni tatizo kwa huyu mtoto, leo
mwanao Mariam na umlee kwa furaha tu”
Mama yake aliongea nae kwa muda sana ingawa
kiukweli Mariam hakuwa na raha kabisa maana kuna
matendo mengine ya mtoto yule, hawa wengine
hawayajui ila Mariam pekee anayajua na
kuyatambua matendo hayo.
Basi muda huu Mariam alienda uwani, akamsikia
mdogo wake Zayana akiongea na simu yani kama
alikuwa akimuelezea mtu kuhusu mtoto wa Mariam,
“Kheeee hicho kitoto cha dada sasa huwezi hata
kukishika kwanza unaweza kuhisi kuwa utaota
usiku, mtoto kazaliwa na sura ya utu uzima
nakwambia, akicheka meno yote yamemjaa
mdomoni, halafu halii ng’aaaa ng’aaaa kama watoto
wengine yani analia kama toto kubwa kabisa”
Mariam akamfata mdogo wake na kumfokea pale,
“Hivi wewe Zayana una akili kweli?”
“Nisamehe dada”
“Usimcheke mamba kabla hujavuka mto, hapo ulipo
hujaolewa, hujazaa bado halafu upo kunicheka
mimi. Yani na wewe huwezi kutambua jinsi dada
yako nilivyohangaika na hii mimba? Ni haki yangu
kuzaa mtoto mkubwa, sasa mtoto kaka miaka
miwili tumboni unategemea akitoka atakuwaje?
Tembo ndio huwa wanabeba mimba miaka miwili
ila sio binadamu, kwahiyo kilichotokea kwangu
inamaana mtoto alikuwa akikulia tumboni”
“Ndio miaka miwili jamani dada!”
“Haya, wewe utabeba miezi mitatu, tusisumbuane
akili halafu utaangalia mtoto wangu aliyezaliwa kwa
miaka miwili na wako wa miezi mitatu yupi ni
mtoto”
“Dada!!”
Mariam akaenda zake kwani hakupenda kabisa jinsi
mdogo wake alivyokuwa akimwambia aliyekuwa
anaongea nae kwenye simu, ingawa kiukweli hata
yeye mwenyewe hakuupenda muonekano wa mtoto
wake.
Basi leo mamake Mariam na mama mkwe wake
wanaongea kuhusu jina la kumpa mtoto, basi mama
mkwe wa Mariam akasema,
“Kikawaida jina la mtoto linatoka baada ya siku
saba, kwahiyo baada ya siku saba tutamtajia mtoto
jina lake”
“Sawa hakuna tatizo, ila hivi unavyoona huyu mtoto
yupo sawa kweli?”
“Kwanini umeuliza hivyo wakati nilikusikia ukiongea
na mtoto wako na ulimshauri vizuri tu!”
“Nimefanya vile kwaajili ya kucheza nafasi yangu ya
umama kwa mtoto maana sisi wa nje tukimvunja
moyo Mariam basi tunaweza fanya Mariam
akamchukia huyu mwanae kupita maelezo ila
kiukweli hata mimi nimejivika moyo wa chuma tu,
ndiomana nakuuliza mwenzangu unaonaje?”
“Hata na mimi nimejivika moyo wa chuma hivyo
hivyo, kwanza uzazi wa huyu mtoto ni waajabu
sijapata kuona, hao wakina Mariam
wameshaangaika kama kwa waganga wamemaliza,
mahospitali ndio usiseme hadi mara ya mwisho
kapatana na hoja kuwa ana mapacha wa kiume
tupu, khaaaa madokta nao waongo jamani kumbe
mtoto mmoja tena ni wa kike. Halafu hivi unajua
kuwa mtoto huyu katangulia miguu kuzaliwa baada
ya kichwa?”
“Kheeee, ilikuwaje sasa?”
“Ndio hivyo hivyo, madaktari walivyoangalia
wakasema kuwa ni operesheni tu pale, ila sasa
kabla ya hiyo operesheni alijifungua muda huo huo
na hivyo hivyo mtoto katangulia miguu, halafu
kilichoshangaza zaidi mtoto akakaa na kukata kitovu
mwenyewe”
Mama Mariam kama alishtuka yani na kusema,
“Naogopa, sijui ningezaa mtoto wa hivyo
ningekuwaje tunampa moyo tu Mariam ila kiukweli
jambo hilo linaogopesha sana”
“Yani mimi mtoto nimekuja kumshika tukiwa hapa
nyumbani, yani kutoka hospitali ni Juma ndio
kamshika halafu Juma anamuona mwanae ni wa
kawaida kabisa na hata kukesha usiku anakesha
yeye na sio Mariam yani mwanao ndio nahisi
alitamani hata angeambiwa kuwa mtoto wake
amekufa”
“Mmmmh hapo pagumu, mimi kesho kutwa nitarudi
nyumbani kwangu, yani hata sijui babake Mariam
nitamueleza nini juu ya huyu mtoto jamani khaaaa!”
“Utamueleza tu, yani tuamini tu kuwa ni mtoto wa
kawaida ili tusiishi kwa mashaka maana hali ya
huyu mtoto inaogopesha kwakweli. Inatakiwa
ujasiri”
Walijadiliana sana kuhusu mtoto wa Mariam.
Yani Juma ndio alikuwa pekee wa kumuangalia
mtoto, kumbadilisha nguo, kusema kuwa apewe
maziwa na kila kitu yani Mariam hata hakujisikia
kumnyonyesha huyu mtoto.
Leo Mariam aliamka tu na kuanza kulia, ikabidi
mumewe amuulize kitu kinachomliza,
“Matiti yananiuma”
“Kheeee kwanini sasa?”
“Yametoka viodonda, inaonyesha huyu mtoto usiku
kaning’ata sana hata sijui kaning’ata kwa muda gani
jamani!”
Basi Juma aliamua kumbembeleza mke wake ni
kweli alikuwa na vidonda vikubwa sana, ikabidi
kulivyokucha, Juma aende kutafuta maziwa ya
ng’ombe kwaajili ya kumpa mtoto maana Mariam
ndio alikataa ramsi kumnyonyesha mtoto wake
kutokana na kutokwa na vidonda vingi kwenye
maziwa yake.
Juma alipomletea huyu mtoto maziwa ya ng’ombe
aligoma kuyanywa kabisa na alikuwa akilia sana
hadi ilibidi wale bibi zake wamkorogee uji na
kumpa ambapo alikunywa kidogo tu, basi Juma
akajihimu kwa siku hii kwenda zake mjini ili
kumtafutia mtoto maziwa ya kopo aliona pengine
anaweza akayanywa maziwa hayo.
Juma akiwa mjini, kuna binti alikutana nae mjini
ambapo binti huyu alimsalimia Juma na baada ya
salamu akamwambia Juma,
“Hongera sana kwa kupata mtoto wa kike”
Juma hakuitikia kwanza ila alimuuliza,
“Kwani unanijua?”
“Ndio nakujua vizuri sana, naweza kukueleza historia
ya maisha yako hadi na wewe ukashangaa”
“Mmmmh mbona mimi sikujui”
“Sio hunijui ila tu umenisahau maana ni kitambo
sana, mimi najua kuwa wewe na mkeo hadi
mlihama mtaa sababu ya mkeo kubeba mimba bila
kujifungua, sikia Juma nikwambie, unajua mkeo ana
kiherehere sana, kaambiwa zile dawa ni aoge siku
tatu ila yeye alioga siku mbili kisa tu alitaka
kujifungua ndio avumilie na kulea”
“Sikuelewi ujue”
“Tuachane na hayo, mwanao anaitwa nani?”
“Bado hatujampa jina”
“Nikutajie jina la kumpa?”
“Hapana, sisi wenyewe tuna majina mengi tu
kwahiyo siwezi kukubali jina la mwanangu nitajiwe
na mtu nisiyemjua”
“Sasa mimi unanijua ila umejisahaulisha tu, ila
ngoja nisiongee sana. Ngoja nikwambie cha kufanya
na maziwa hayo, yani hayo maziwa ya unga uwe
unachanganya na yale ya ng’ombe unampa mtoto”
“Kheeee ndio mambo ya wapi hayo? Yani haya
maziwa ya unga yakorogwe kwenye maziwa ya
ng’ombe?”
“Ndio, unatakiwa kufanya hivyo”
Halafu huyu binti akaondoka na kumuacha Juma
akimuangalia tu.
Juma alirudi nyumbani kwake akiwa na makopo
mawili ya maziwa kwaajili ya mtoto na alipofika tu
walimkorogea yle mtoto na kumpa, alikunywa kama
maji mpaka Mariam akashangaa huku akiuliza,
“Jamani hii ni kawaida kweli?”
Mamake Mariam akasema,
“Kwa mtindo huu haya makopo mawili hayawezi
kumaliza hata wiki!”
Mama mkwe wa Mariam akasema,
“Ila jamani tukumbuke huyu mtoto amekaa miaka
miwili tumboni kwahiyo tuache kumuhesabie kitoto
kama tunavyofanya, ndiomana tunapigwa na butwaa
kila muda sababu huyu mtoto tunamuhesabia kitoto
sana”
Basi wakaitikia tu.
Ilifika siku ambayo mamake Mariam alikuwa
anaondoka, ila yule mtoto alikuwa ameshamaliza
yale makopo mawili ya maziwa na alikuwa akilia
njaa, hapo waliangaliana na kukosa jibu kabisa
ikabidi Juma aanze kumbembeleza mwenyewe
mtoto na alipolala alienda kumlaza chumbani na
kurudi sebleni, basi mamake Mariam akashauri,
“Jamani, mimi sioni sababu ya kusubiria siku saba
kwa mtoto mkubwa hivi, kwahiyo nashauri tumpe
jina tu”
Hata mama mkwe wa Mariam naye alikubali hilo na
kumuuliza Juma,
“Eeeeh mwanangu, unataka jina gani kumpa mtoto
wako?”
“Aaaah mama, jina lolote tu mtakaloamua kumpa
kwangu ni sawa, sina tatizo juu ya hilo kabisa.
Ngoja niwahi mjini nikamnunulie maziwa mengine”
Basi Juma akajiandaa haraka na kuondoka zake,
kule nyumbani walibaki wakiongea tu ambapo
mamake Mariam akasema,
“Yani mimi napenda nijue jina la mtoto kabla
sijaondoka”
Basi mamake Juma akasema,
“Sababu huyu mtoto ni wa kike basi aitwe jina
langu”
“Aaaaah, hivi jina lako ni nani vile?”
“Mimi naitwa Ashura, kwahiyo huyu mtoto tumuite
Ashura”
Yani mtoto alikuwa chumbani ila alilia sauti hiyo
hadi wote ikawashtua na kumfanya Mariam aende
kumuangalia kuwa ana tatizo gani.
Mariam alipofika tu akamsikia mtoto wake akisema,
“Mama, sitaki hilo jina”
 
MTOTO WA MAAJABU: 3
Yani mtoto alikuwa chumbani ila alilia sauti hiyo
hadi wote ikawashtua na kumfanya Mariam aende
kumuangalia kuwa ana tatizo gani.
Mariam alipofika tu akamsikia mtoto wake akisema,
“Mama, sitaki hilo jina”
Mariam alijikuta yupo kama kaganda vile, yani
alihisi kupigwa na ganzi mwili mzima kwakweli,
alikodoa macho kumuangalia yule mtoto kwa muda
kidogo halafu ndio akaanza kuogopa na kukimbilia
sebleni,
“Jamani mama, huyu mtoto anaongea”
“Mariam, mtoto mdogo huyo anaongea kivipi?”
“Ila mkumbuke amekaa miaka miwili tumboni,
mbona mengine mnayakubali halafu hili la kuongea
mnalikataa?”
“Haya tumekubali, amesemaje? Amesema anataka
maziwa au?”
“Hapana, ila kasema hataki hilo jina la Ashura”
Mama mkwe wa Mariam akacheka sana na
kumuangalia Mariam kisha akamwambia,
“Hivi Mariam, unajua kama Ashura ni jina langu au
hujui? Kama hujui basi ngoja nikujuze, hili ni jina
langu na mimi nilirithi toka kwa bibi yangu”
Kisha yule mama mkwe wa Mariam alimgeukia
mama yake Mariam na kumuuliza,
“Hivi mwenzangu, huyu mtoto ulimfunda akafundika
kweli?”
Kiukweli mama Mariam alihisi aibu na kumfanya
ainuke na kumvuta mkono Mariam hadi nje na
kuanza kumsema,
“Mariam, unajua sio adabu hiyo yani kabisa
unakataa jina la mama mkwe wako?”
“Hapana mama, mimi sijakataa ila mtoto ndio
kakataa”
“Huyo mtoto akatae kwako wewe kwa ufahamu upi
alionao? Mariam acha kunitia fedheha jamani, sijui
naondokaje na kukuacha mtoto usiyekuwa na adabu
hivi! Si unaweza kumjibu kitu kibaya mama mkwe
wako wewe!”
“Hapana mama, nisamehe”
Mama Mariam alitumia muda kumkanya sana
Mariam kwani hakupenda kabisa, aliona kama
Mariam amemdhalilisha kwakweli.
Kisha walirudi ndani, ambapo Mariam alipiga
magoti kwa mama mkwe wake kumuomba
msamaha maana hata hakuna aliyemuamini pale
kuwa mtoto kakataa jina, ilionekana ni yeye ndio
halitaki lile jina,
“Naomba unisamehe mama, hii kitu haitajirudia tena
mama yangu”
“Mariam, nione mimi kama mama yako na
usithubutu kunivunjia heshima”
“Nimekuelewa mama, nisamehe mama yangu”
Kisha wakapatana pale halafu mama Mariam ndio
akawaaga vizuri sasa halafu mama mkwe wa
Mariam aliinuka kumsindikiza mama Mariam.
Kiukweli Mariam hata hakupenda kubakia peke yake
na mtoto ila afanye nini ilihali yule ni mtoto wake?
Yule ni damu yake? Yani Mariam hakuwa na raha
kabisa.
Muda huu alijikuta tu kainuka na kwenda chumbani
ambapo alimkuta yule mtoto kama yupo tu kucheza
cheza kitoto kitandani, akawaza kuwa muda wote
huyu mtoto angekuwa hivi basi kwake ingekuwa
afadhari ila huyu mtoto alikuwa akimtisha tu.
Mariam alienda kukaa pale kitandani akimtazama
huyu mtoto ila gafla huyu mtoto alianza kuongea
yani Mariam alikuwa kama kapigwa na butwaa tena,
huyu mtoto alisema,
“Mama, mkiniletea yale maziwa ya kopo
mnichanganyie na ya ng’ombe ila msipofanya hivyo
kwa hakika mtaingia umasikini maana mimi
nakunywa sana maziwa”
Mariam alikuwa kama kapigwa gundi maana
hakuweza kuinuka pale kitandani wala nini, ila moyo
wake ulikuwa unaenda mbio sana hadi akaanguka
pale kitandani na kuzimia.
Juma alipokuwa anatoka mjini, akakutana na yule
binti ambaye jana yake alimpongeza kwa kupata
mtoto, huyu binti alimsalimia Juma,
“Habari yako baba Ashura!”
Juma alishtuka na kumuangalia huyu binti kwa
muda bila kusema chochote ambapo huyu binti
akamwambia Juma,
“Hujui kama mwanao kapewa jina la Ashura?”
Juma akamuuliza,
“Unajua sikuelewi? Unaongelea nini?”
“Inamaana hujui jina la Ashura ni la nani?”
“Ni la mama yangu”
“Basi mama yako kampa jina hili mtoto wako, je
umependa?”
Juma alimuangalia huyu binti na kumuuliza pia,
“Kwanini nisipende wakati ni jina la mama yangu?”
Huyu binti akamwambia Juma,
“Ni jina la mama yako ndio ila halimfai mtoto
wako”
“Kwahiyo jina gani ndio linamfaa mwanangu?”
“Hapo sawa ulivyouliza, muite mwanao Mishi”
Juma akashtuka sana na kumuangalia huyu binti
kisha akamwambia,
“Yani mimi nimuite mtoto wangu Mishi!! Hapana
kwakweli”
“Kataa hilo jina ila jina atakalolitaka huyo mtoto
wenu nadhani ndio utalipenda. Kwaheri”
Yule binti akaondoka, yani Juma alimuangalia bila
ya kummaliza kisha yeye akarudi zake nyumbani
kwake.
Juma alimkuta mama yake akiwa na harakati za
kupika kwa muda huu, basi alimsalimia na
kumuuliza mama mzazi wa Mariam,
“Khaaa kashaondoka yule”
“Yani nilikuwa nimechanganyikiwa hata sijamuaga
vizuri masikini jamani, ila nishaleta maziwa. Safari
hii nimeleta makopo manne”
“Yani hayo hesabu wiki tu yatakuwa yameisha”
“Jamani mama!!”
“Mimi nawaambia jamani, watoto kama hawa huwa
tunawapa uji, ukijifanya unapenda kumpa maziwa
sana basi utalia na kufilisika nakwambia mwanangu.
Kwanza huyu mwanamke mwenyewe kakufilisi,
halafu uzao wake nao unataka kukufilisi khaaa
jamani!”
Juma akaenda moja kwa moja ndani ili amwambie
mkewe amuandalie mtoto maziwa, ila alishangaa
sana alipoingia chumbani kumkuta Mariam kalala
hoi halafu yule mtoto yupo pembeni akinyonya ziwa
la Mariam wakati Mariam alishamuachisha mtoto
huyu.
Juma alisogea na kumuondoa yule mtoto huku
akimuamsha Mariam maana aliona kanyonywa
maziwa hadi yamelegea yani, alijikuta akimuonea
huruma tu kwa muda huo.
Juma alijitahidi kumuamsha na hata kummwagia
maji ndipo Mariam aliposhtuka ila alishindwa
kunyanyuka maana alikuwa akihisi kizunguzungu,
alikuwa akinyanyuka anaanguka.
“Khaaa Mariam, itabidi twende hospitali mke
wangu”
Hata kujibu Mariam hakuweza kabisa, ikabidi Juma
amuandae mke wake na kumuacha mtoto kwa
mama yao kisha yeye kumpeleka Mariam hospitali.
Kule hospitali, Mariam alionekana kupungukiwa
damu mwilini mwake, hivyo Juma mwenyewe ndio
alijitolea kumuongezea damu mke wake huku
akimuhurumia sana.
“Pole mke wangu, utapona kabisa”
Kwahiyo Mariam aliachwa kalazwa hapa, halafu
Juma alirudi nyumbani maana kule alimuacha
mama yake peke yake na mtoto.
Alipofika tu nyumbani, Juma akapewa ujumbe na
mama yake,
“Hivi unaweza kuamini?”
“Kuamini nini mama?”
“Huyu mtoto kamaliza kopo lote la maziwa”
“Kheeee!! Huyu huyu mtoto?”
“Ndio, kwani tunamuongelea nani hapa?”
“Nimechoka mama kwa hilo, halafu Mariam
amepungukiwa na damu nimetoka kumuongezea”
“Pole mwanangu, itakuwa sababu ya uzazi,
wanawake huwa tunapoteza damu nyingi sana
wakati wa kujifungua”
“Ndio hivyo mama ila swala la mtoto kumaliza
maziwa kopo lote mbona limenitatiza zaidi!”
Juma aliongea sana na mama yake, ila leo usiku
ilibidi Juma alale na mtoto maana Mariam alikuwa
hospitali.
Leo Mariam alipewa ruhusa ya kurudi nyumbani, ila
alimgomea mumewe kabisa kurudi nyumbani,
“Sasa Mariam unataka kuendelea kukaa hapa
hospitali?”
“Hapana, ila nataka nirudi nyumbani kwetu”
“Khaaaa na mtoto wako je?”
“Huyo mtoto ndio simtaki kabisa, ataniua huyo
mtoto Juma”
“Hapana hakuui ni wasiwasi wako tu”
“Mtoto gani mchanga anaongea?”
“Haongei bhana ila ni hisia zako tu Mariam”
“Basi nikirudi nyumbani naomba ufatane na sharti
langu”
“Sawa nipo tayari ila sitaki uende pengine zaidi ya
kule tunapoishi mimi na wewe”
“Sawa, ila sitaki kulala na huyo mtoto kabisa,
utakuwa ukilala nae wewe”
Juma ilibidi tu akubali kwani yeye kama yeye
hakuona kama kuna tatizo zaidi kwa yule mtoto
ukizingatia huko kuongea hajawahi kumsikia yule
mtoto akiongea.
Basi walikamilisha kila kitu pale hospitali kisha
kupewa ruhusa ya kurudi nyumbani.
Mama mkwe wa Mariam alikuwa akilalamika tu pale
waliporudi kuhusu maziwa maana yule mtoto
alimaliza kopo lingine la maziwa,
“Jamani, kopo la pili la maziwa limeisha, khaaaa
hili ni balaa”
Mariam akadakia na kusema,
“Jamani huyu sio mtoto nawaambia”
Mama mkwe wake akamfokea,
“Acha ujinga Mariam, kwahiyo umezaa kitu gani?
Hebu kumbuka ni kipindi gani umetafuta mtoto,
hebu kumbuka ni kiasi gani umehangaika na uzao
wa mtoto hadi Mwenyezi Mungu kakusaidia
kumpata mtoto huyu, unatakiwa uwe na shukrani
sana”
Mariam alikaa kimya ila hakuwa na raha na huyu
mtoto wake kabisa, kwa muda huu aliamua tu
kwenda kupumzika maana alijihisi bado ana uchovu
wa hospitali.
Mama Juma akaanza kuongea na Juma pale,
“Mwanangu bila maarifa yoyote jua kwamba
itasumbua sana kumlea huyu mtoto!”
“Maarifa gani sasa mama?”
“Nakwambia huyu mtoto tumtengenezee uji tu
hakuna namna, aanze kunywa uji vilivyo, sio kwa
ulaji huu jamani”
Muda huo huo Mariam alitoka ndani na kuwaambia,
“Nimekumbuka kitu, huyu mtoto aliniambia kuwa
tukitaka ashibe basi tumchanganyie maziwa ya unga
na maziwa ya ng’ombe”
Mama mkwe wa Mariam alishangaa sana,
“Weee Mariam, umeanza sasa ndoto zako? Huyu
mtoto kakwambia saa ngapi? Halafu hayo mambo
ya kuchanganya maziwa ya unga na maziwa ya
ng’ombe kumpa mtoto ndio mambo ya wapi?”
“Hata mimi sijui ila huyu mtoto aliniambia kweli”
“Mariam, Mariam unajua mambo mengine uwe
unafikiria kabla ya kuyasema, haya tumekubalia ila
je anapewa kwanza maziwa ya ng’ombe halafu
yanakuja ya unga au anaanza kwa kukorogewa
kwanza ya unga halafu anakuja kunywa ya
ng’ombe?”
“Kwa uelewa wangu ni kuwa yale maziwa ya
ng’ombe tukiyachukua tumkorogee na maziwa ya
unga, yani kwenye maziwa ya unga badala ya
kukoroga maji tumkorogee kwa maziwa ya ng’ombe
kwahiyo kiwango cha maji kiwe ndio kiwango cha
maziwa ya ng’ombe”
“Kheeee makubwa hayo, kwahiyo huyu mtoto
itakuwa maji yake ni maziwa eeeh!! Makubwa haya,
sijapata kuyafikiria”
Juma aliyekuwa kimya kwa muda mrefu alikuwa
akitafakari ujumbe ule na maneno ambayo aliwahi
kuambiw ana yule binti waliyekutana nae kuwa huyu
mtoto akimfanyia hivyo ndio atafurahi, basi mama
mkwe wa Mariam akamshtrua Juma pale kwa
kumuuliza,
“Haya, na wewe unasemaje juu ya kauli ya mkeo
kuwa mtoto akorogewe maziwa ya ng’ombe na ya
unga pamoja!”
“Mama sikia, tusianze kujadili sana kuwa Mariam
kaongea muda gani na huyu mtoto, kwanza
tukumbuke kuwa Mariam ni mama wa huyu mtoto
kwahiyo ni mengi anayaelewa ya mwanae, mengine
tunageleshwa tu sisi hapa. Sikia tufanye hivyo hivyo
alivyosema yeye, huwezi jua uleaji alioupanga juu ya
huyu mtoto”
Mariam alimuangalia mumewe, ila hakupenda ile
kauli ya mumewe kabisa, akainuka na kwenda
chumbani ila muda wote wanaongea hayo mtoto
alikuwa amelala kwenye kochi pale sebleni.
Usiku wakiwa wamelala, ilikuwa kama walivyopanga
kuwa Juma ndio awe analala na mtoto halafu
Mariam asiwe analala na mtoto kabisa ila Juma
alimvizia Mariam akiwa amelala kabisa kisha
akaenda kumuweka mtoto pembeni ya Mariam
ambapo Mariam alilala usingizi mzito sana yani
alikuja kushtuka wakati tayari pameshakucha kabisa
anashangaa tu kumuona mtoto pmbeni,
akamuangalia huyu mtoto akamuona akitabasamu,
kiukweli Mariam kila tendo la huyu mtoto alijikuta tu
kutokulipenda kabisa, kwahiyo kitendo cha huyu
mtoto kutabasamu wala Mariam hakukipenda wala
nini.
Akakaa kama kuogopa hivi ila huyu mtoto kama
alitaka kuongea ila hakuongea kitu chochote zaidi
zaidi Mariam aliona kama muonekano wa mtoto
wake umebadilika yani akawa kama mtoto aliyetoka
kuzaliwa mwenye wiki moja hivi tofauti na ambavyo
huwa anamuona, pale Mariam alishtuka tena na
kuinuka kwenda kumuita mumewe aliyekuwa
akijiandaa kwaajili ya kwenda kwenye shughuli zake
chache,
“Juma, njoo umuone huyu mtoto kabadilika leo”
“Kivipi yani, kabadilikaje?”
“Kawa kama mtoto mchanga”
Juma akamuangalia mkewe kwa makini kisha
akaenda chumbani ambapo walimkuta mtoto akiwa
vile vile kama siku zote, Juma alimuangalia mkewe
na kutikisa kichwa huku akisema,
“Ila Mariam una matatizo sana tena sana”
Halafu Juma akatoka na kuondoka zake, Mariam
alijisemea,
“Hivi mimi nitaweza kweli kumlea huyu mtoto!!”
Mara akamsikia huyu mtoto akisema,
“Utaweza tu mama”
Hapa Mariam aliogopa na kutoka nje ila hakuongea
chochote na mama mkwe wake ukizingatia alikuwa
haaminiki kabisa kwenye swala la kusema kuwa
mtoto anaongea.
Mama mkwe wa Mariam aliona Mariam amekaa
muda mrefu sana nje ikabidi aende kumuuliza
maana hata ile kumaliza vizuri kuhusu uzazi alikuwa
hajamaliza wala nini,
“Unajua Mariam huwa sikuelewi kabisa mwanangu,
kwani huyu mtoto ilikuwaje kwanza?”
“Kivipi mama?”
“Kwanini unamkimbia? Unajua hujamaliza siku
nyingi tangu ujifungue ila ushaanza tabia ya kukaa
muda wote nje na kumuacha mtoto ndani peke
yake, unajua sikuelewi”
“Mama, sidhani kama mnaweza kunielewa hata
nikisema nini bado kunielewa itakuwa ngumu. Hapa
nangoja mwezi ufike tu nianze kufanya shughuli
zangu zingine”
“Mmmmh hivi unafikiri kuwa mimi nitakuwa hapa
siku zote? Hapana, mimi nitaondoka”
“Hamna shida, nitatafuta msichana wa kazi”
“Mmmmh sijapata kuona binti mvivu kama wewe
hata sijui mwanangu alikupendea nini”
“Mama, usitake nikujibu vibaya kabisa. Huyo
mwanao hebu muulize vizuri, alinibembeleza kunioa
balaa na wala nilikuwa simtaki halafu kuhusu swala
la uvivu huyo mwanao anatambua fika kuwa mimi ni
mvivu namba moja, kiasi kwamba hata nguo zake
huwa anajifulia mwenyewe”
“Mmmmmh!! Sijui kama wazazi wako walitambua
wajibu wao kwako jamani loh!! Mimi kesho au
kesho kutwa naondoka, nitakuacha wewe na mumeo
hapa mfurahi”
“Haya hakuna tatizo”
Yani Mariam alimjibu tu mama mkwe wake bila
hata ya kujali, na wala hakuwa anawaza kuwa mama
huyu ndio kamsaidia dawa hadi ya kuweza
kujifungua mimba iliyompeteza kwa miaka miwili ila
muda huu alikuwa akimjibu kwa kujisikia yeye.
Mama mkwe aliondoka zake na kurudi zake ndani
maana hakupenda kubishana kwa muda huo na
Mariam.
Usiku ule, mama mkwe wa Mariam aliamua
kuongea na mwanae Juma maana hapo alishakata
shauri la kuondoka kesho yake maana alihisi
kuendelea kuishi hapo angegombana tu na huyu
mkwe wake Mariam,
“Mwanangu, mimi naondoka kesho”
“Kheee mama, mbona mapema hivyo?”
“Ndio nimeshaamua hivyo, nitaondoka kesho”
“Kwani kuna tatizo lolote mama yangu?”
“Hamna ila kumbuka na mimi nina mji wangu, na
mimi nina majukumu yangu, kama mkeo
nimeshamuhudumia tayari imetosha”
“Mama, hata wiki mbili hazijapita?”
“Sio tatizo, ilimradi kaonekana kuweza kujihudumia
mwenyewe, nibaki nifanye nini mimi? Kesho
naondoka zangu, nielewe tu mwanangu”
“Sawa mama, ila tutakukumbuka sana mama”
“Ila nakuonea huruma maana najua nepi zote utafua
wewe, chakula utapika wewe, na nyumba utasafisha
wewe, huyu mwanamke ni kama umeoa doli tu
ndani ya nyumba”
Juma alicheka kidogo na kutikisa kichwa kisha
akamwambia mama yake,
“Yani mama, huyu Mariam nisingekuwa nampenda
kwa hakika nisingemuoa, sijapata kuona mwanamke
mvivu kiasi hiki”
“Na mimi sijapata kuona wakina Mariam wavivu
kama huyo mke wako!”
“Mama, kuna historia ndefu sana ya huyu mtu ila tu
ni sababu nampenda sana na siwezi kumuacha”
“Ila wewe, kama ni kurogwa basi umerogwa na
kupitiliza. Haya mimi naenda na ninakutakia kazi
njema za humu ndani maana najua zote
zitakuangukia wewe mwenyewe”
Huyu mama alionekana kuongea kwa simanzi sana
kwani toka mwanzoni wakati Juma anaoa alikuwa ni
kinyume kabisa na ndoa hii.
Kesho yake mapema kabisa, mama mkwe wa
Mariam alishajiandaa kwaajili ya safari aliwaita wote
kwaajili ya kuwaaga ambapo Juma alimpa mamake
mtoto wake ili yule mama aweze kumuaga mjukuu
wake.
Basi huyu mama alimkumbatia mtoto halafu
akampakata vizuri na kumwambia,
“Mimi naenda, nitakukumbuka sana mjukuu wangu
Ashura”
Baada ya kusema hayo alishangaa kumsikia mtoto
huyu akimsonya.
 
MTOTO WA MAAJABU: 4
Basi huyu mama alimkumbatia mtoto halafu
akampakata vizuri na kumwambia,
“Mimi naenda, nitakukumbuka sana mjukuu wangu
Ashura”
Baada ya kusema hayo alishangaa kumsikia mtoto
huyu akimsonya.
Huyu mama aliogopa na kumuweka mtoto pembeni
halafu aliwauliza wakina Mariam,
“Mmesikia jinsi alivyonisonya?”
Mariam akacheka na kusema,
“Hata hatujasikia, pole sana mama”
Juma alimuangalia mkewe na kumuuliza,
“Yani Mariam unacheka?”
“Jamani sijacheka kwa ubaya, kwani wewe umesikia
mtoto akisonya?”
Juma nae akakataa kuwa hajasikia halafu Mariam
akaongezea,
“Mtoto mdogo hivi na kusonya ni wapi na wapi
jamani? Hakuna kitu kama hicho”
Mama mkwe hakuongea zaidi bali alibeba begi lake
ikabidi wamsaidie tu kumsindikiza, wakati huo
Juma ndio alimbeba mtoto wao, ila walipofika
njiani tu, mama yao aliwataka warudi maana
hakuona sababu ya mtoto kutembezwa barabarani
ilihali akiwa mdogo bado.
Basi Juma na mkewe wakarudi nyumbani ambapo
waliweka mtoto pembeni halafu Juma alianza
kumsema mkewe,
“Unajua sijapenda kabisa, kilichokufanya kumcheka
mama yangu sasa ni nini?”
“Sijamcheka kwa ubaya, ila huyo mama yako
nilishamwambia kuwa mtoto huyu amelikataa hilo
jina la Ashura ila alisema sina adabu hadi nikaja
kumpigia magoti hapa kumuomba msamaha, yani
siku ile ndio kacharusha mashetani yangu kabisa,
muache tu asonywe”
“Mariam, chunga kauli zako. Kumbuka yule ni
mama yangu, pia kumbuka umeteseka na hii
mimba kwa miaka miwili ila yeye kahangaika
kukutafutia dawa hadi wewe umeweza kujifungua
salama, hivi kweli unaweza kumcheka?”
“Nisamehe mume wangu, haya tujadiliane huyu
mtoto tumuite jina gani kwasasa?”
“Mmmmh tusimpe jina ila tumuite tu mtoto halafu
hizo siku za mbeleni ndio tutampa jina”
“Jina gani unafikiri litamfaa?”
“Aaaah Mariam usiwe na haraka hivyo. Mambo
yanaenda taratibu haya”
“Kwahiyo kwasasa tumuite mtoto tu!!”
“Ndio, tumuite mtoto”
Mariam aliitikia tu ili wasiendelee kujadili ile mada
ya kuhusu mtoto ukizingatia kiukweli yeye alikuwa
hamtaki kabisa huyu mtoto wake.
Leo mapema kabisa, Juma alimuaga Mariam kuwa
anataka kutoka ila Mariam akang’aka na kusema,
“Kheeee unataka uniache na huyu mtoto peke
yangu!!”
“Kwahiyo Mariam kwasasa sitatoka kwenda kutafuta
hela wala nini, haya tutakula nini? Unataka niwe
masikini unikimbie”
Mariam akacheka kidogo na kumuuliza Juma,
“Kwani hapo ulipo una utajiri gani jamani! Mbona
sijakukimbia”
“Hivi Mariam, unaweza kuniweka mimi kwenye
kundi la masikini? Ni kweli sina gari la kifahari wala
gari la kawaida ila bado huwezi kuniweka kwenye
kundi la umasikini, kumbuka hapa tunapoishi ni
nyumba yangu mwenyewe kabisa, na hata kama
ningekuwa nimepanga, ilimradi ningeweza kulipa
kodi basi mimi sio masikini, hivi Mariam
unavyopenda kula wewe na kuvaa vizuri, ningekuwa
masikini ungekubali kuishi na mimi? Sina utajiri huo
ila mimi huwezi kuniita masikini, hapo ulipo unakula
unashiba tena chakula unachokitaka halafu upo
kujichekelesha eti unaniuliza kuwa mimi nina utajiri
gani!”
“Haya basi yamaisha Juma ila huwezi kutoka na
kuniacha mimi na mtoto huyu peke yangu”
“Ngoja nikuulize sasa, unatakaje?”
“Labda atafutwe msichana wa kazi, yani hapa ndani
tuwe tunaishi na msichana wa kazi ndio
nitakuelewa”
“Sasa Mariam, swala la msichana wa kazi mapema
hivyo itawezekanaje? Hayo ni maswala ya mchakato
mke wangu”
Walianza kubishana tu pale kwani Mariam hakutaka
kabisa mumewe kutoka pale nyumbani kwao, yani
hiko kitu hakukitaka kabisa. Kisha Juma akamuuliza
tena mke wake,
“Haya basi, sema tufanye nini kipindi hiki ambacho
bado hatujapata msichana wa kazi?”
“Labda mdogo wangu Zayana aje hapa”
“Mmmh, ngoja tumpigie simu”
Moja kwa moja Juma alimpigia simu mdogo wake
Mariam huku akimuahidi vitu vingi ili aweze kuja
hapo kukaa na dada yake,
“Mmmmh sawa shemeji, mwambieni kabisa mama
basi nitakuja kesho”
“Sawa, asante sana Zayana”
Basi moja kwa moja Juma alimpigia mama mkwe
wake kumwambia kuhusu hilo ambapo mama yake
Mariam alikubali kuhusu jambo hilo kuwa Zayana
afike hapo kumsaidia dada yake.
Ilbidi leo Juma asitoke maana Mariam alisema
hawezi kubaki hapo peke yake na mtoto basi Juma
hakuona tatizo zaidi ya kuendelea pia kubaki hapo
hapo ila akiwepo mdogo wake Mariam ndio aweze
kuendelea na shughuli zake.
Basi Juma alipika pale na siku ile walikula huku
akiongea na mke wake,
“Ila mke wangu wewe ni mvivu sana ndiomana
unahitaji mdada wa kazi”
“Sio sababu ya uvivu tu ila mdada wa kazi
namuhitaji sana sababu hata nikiwa nimeanza
shughuli zangu basi apatikane mtu wa kumuachia
mtoto”
“Mmmh haya bhana”
“Ila unajitahidi kupika mume wangu”
Juma alitabasamu tu na kuendelea kula, ila leo
hakuna kituko chochote kilichofanywa na mtoto wao
na waliishi nae vizuri tu hata usiku uliingia na
walienda kulala na hakuna lolote baya ambalo
lilitokea kati yao au kwa mtoto.
Kama kawaida usiku ule ni Juma ndio alilala na
mtoto maana Mariam alishakataa kabisa jambo la
yeye kulala na mtoto huyu.
Kulipokucha mapema kabisa, wote waliamka na
kuanza kufanya shughuli chache za pale, huku nguo
za mtoto zikiwa kwenye dishi, Juma akamwambia
mke wake,
“Mariam, si ufue tu hizo nguo za mtoto”
“Mmmmh hivi Juma huna huruma wewe! Mimi nina
mda gani toka nitoke kujifungua? Unawezaje
kuniambia nifue nguo kweli!”
“Khaaaa Mariam, ila kweli sema mimi kidole
kinaniuma sana”
“Atakuja kufua Zayana, unateseka na nini sasa”
Basi wakaacha zile nguo na kuendelea na mambo
mengine.
Muda wakiwa wanakula leo, ndio muda ambao
Zayana alifika na kuwasalimia, kisha walimkaribisha
kile chakula na yeye aliungana nao kula kile chakula,
ambapo Mariam akamwambia Zayana,
“Unaona mdogo wangu shemeji yako anavyoweza
kukorofisha mambo, yani anajua kupika balaa”
Zayana akasema kwa aibu aibu,
“Naona, chakula ni kitamu sana”
Juma nae akasema,
“Yani dada yako badala apike yeye ili mimi nisifie,
anabaki kila siku kusifia tu nikipika mimi”
Mariam akadakia,
“Na wewe Juma jamani! Ndio mahaba hayo”
Wakaendelea tu kula ambapo Juma aliinuka na
kwenda kujiandaa kwani alifurahi sana kwa leo
mdogo wake Mariam kufika ili na yeye aweze
kwenda kwenye shughuli zake.
Zayana alikaa na dada yake na kuanza kuongea nae
maana hata yeye hakupendezewa na ile kauli ya
dada yake na ile ya shemeji yake,
“Dada jamani hadi leo unamuachia tu shemeji apike
mwenyewe!”
“Tatizo liko wapi kwani? Anapenda kupika yule”
“Anapenda kupika ndio ila hadi analalamika kuwa
hajala chakula chako dada! Nilijua kipindi kile cha
mimba tu, yani hadi hapa umejifungua!”
“Hebu nitoleeni balaa na nyie, sijui sababu
nimejifungua toto kubwa hilo ndiomana mnaona
nipo sawa tu, sijui mnahisi toto limeshakuwa maana
lina meno yote mdomoni, mimi bado nipo kwenye
uzazi. Mdogo wangu wewe hujazaa bado kwahiyo
mambo ya uzazi huyajui, kwa kawaida mwanamke
anatakiwa kukaa miezi mitatu bila kufanya
chochote”
“Mmmmh dada!”
“Unaguana nini sasa? Huko makazini kwenyewe
huwa mwanamke akijifungua anapewa miezi mitatu
ya kukaa nyumbani kwani uzazi unajulikana bhana,
sasa mimi hata sina muda mrefu mnataka nianze
kuhangaika jikoni kweli!! Hebu muwe na huruma
basi, nimebeba mimba kwa miaka miwili jamani,
halafu nianze kuhangaika na majiko kweli!!”
“Dada, sina maana hiyo. Ila ngoja nikurekebishe,
unajua kwanini kazini huwa wanatoa miezi mitatu?”
“Kwanini?”
“Sababu mtoto anatakiwa kupata maziwa ya mama
kwa muda wote kwa miezi hii mitatu, haya kuhusu
kumpikia shemeji sina maana kuwa ndio uanze
kukukuruka na majungu kwasasa, ila dada wewe ni
mvivu jamani yani sijui kama ulikuwa ukimpikia
shemeji kabisa”
“Weeee nilikuwa nikimpikia zamani, hebu achana na
hizo habari kwanza. Kuna nguo za mtoto kwenye
dishi pale nenda kazifue”
Basi Zayana akainuka na kwenda kufua zile nguo za
mtoto wa dada yake.
Usiku wa leo, chakula kilipikwa na Zayana na
kumfanya Juma afurahie kula kile chakula huku
akisifia kuwa ni kizuri sana, basi waliongea mengi
pale na moja kwa moja kwenda kulala.
Kama kawaida huyu mtoto alilala na Juma, ila
Mariam alimuangalia sana mtoto wake na kuona
kuwa kama siku hizi ameanza kubadilika vile, kwa
kiasi Fulani aliacha kumuogopa yule mtoto wake.
Kulivyokucha asubuhi tu, Juma alifanya mambo
yake na kuondoka zake, basi Mariam alibaki na
mdogo wake wakisaidiana zile kazi ndogo ndogo za
pale nyumbani kwao.
Basi muda huu walikuwa wamekaa huku wakiongea
ambapo Zayana alimuuliza dada yake,
“Unajua dada, sijawahi kuona mtoto mdogo
mwenye meno, huyu wa kwako ni vipi dada?”
“Umeanza sasa Zayana, huyo mtoto ana meno ya
plastiki huwa wanaita hivyo, yatapotea yenyewe tu
hayo”
“Duh!! Halafu dada, huyu mtoto mkubwa hivi
hukujifungua kwa kisu kweli?”
“Mmmmh Zayana naomba usinikumbushe mambo
ya uzazi wa huyu mtoto, nimeshaanza kusahau mimi
haya mambo, tafadhari nakuomba usinikumbushe
Zayana”
“Mmmh haya dada”
Waliendelea tu na maongezi mengine, kwakweli kwa
kipinndi hiki kulikuwa na amani maana hakuna
jambo baya ambalo limetokea hata Juma alikuwa
akifurahi sana kila aliporudi na kukuta kuna amani
mahali hapo.
Siku hii Juma alipokuwa anaenda kwenye shughuli
zake akakutana na yule binti njiani ambapo yule
binti alimsalimia Juma na kumuuliza,
“Hivi huhitaji msichana wa kazi nyumbani kwako?”
“Mmmmh wewe unataka nini kwani?”
“Hapana sitaki kitu ila hata mimi nafaa kuwa
msichana wako wa kazi”
“Yani mimi nikuajiri mtu mwenye mambo ya ajabu
kama wewe!! Siwezi kufanya huo upuuzi”
“Mambo yangu ya ajabu ni yapi?”
“Hapana, siwezi kukuajiri tu”
“Kwanini usiweze kuniajiri?”
“Hayakuhusu”
“Sawa hakuna shida, mkataa pema pabaya
panamuita”
“Una maana gani?”
“Sina maana yoyote ila leo ukirudi nyumbani kwako
utaona kuna tukio la ajabu limetendeka”
“Kivipi?”
“Hayanihusu”
Kisha huyu binti akaondoka zake na kumuacha
Juma akiwa amesimama huku akimuangalia hadi
alipoelekea halafu Juma alienda kwenye shughuli
zake.
Mariam na mdogo wake wakiwa wamekaa
wakamsikia mtoto akilia ambapo alikuwa kwenye
kiti tu pale pale sebleni, basi Mariam akamwambia
mdogo wake,
“Hebu muangalie hapo ana tatizo gani?”
“Atakuwa amekunya dada maana nasikia harufu
hatari”
“Kheeee umenikumbusha kitu, hivi unajua kuwa
huyu mtoto hajawahi kutoa haja kubwa kabisa!”
“Kheeee unamaanisha hajawahi kunya dada?”
“Mmmh na wewe, hebu kuwa na tafsida basi,
najitahidi kuficha ukali wa neno hapa ila wewe hata
hujali unaniambia tu ujinga ujinga, mimi na mume
wangu humu ndani huwa hatutamki maneno ya
hovyo kama hayo”
“Mmmh dada, haya bhana”
“Haya nenda kamuangalie basi umtoe hiyo haja”
Basi Zayana akainuka na kwenda kumuangalia
mtoto ambapo aliamua kumuangalia kwanza kwa
kumtoa ile nguo, Zayana alipomtoa alishangaa sana
na kumwambia dada yake,
“Dada, njoo uone”
“Nione nini tena? Umenishtua loh!”
“Hapana, sina nia ya kukushtua ila njoo uone tu”
Mariam aliinuka na kusogea pale ambapo na yeye
alishangaa sana halafu Zayana akasema,
“Dada inawezekana vipi kwa mtoto kunya mavi
kama ya mbuzi!”
“Nimekwambia na wewe tumia tafsida basi jamani
khaaa!! Hapa unajua nashangaa pia, sijawahi kuona
kitu kama hiki, au sababu hajawahi kupata haja
tangu amezaliwa?”
“Mmmmh inawezekana, ila dada uliwezaje kukaa na
mtoto siku zote hizi bila kupata haja na bila
kumpeleka hospitali?”
“Mmmh mdogo wangu acha tu, huyu mtoto hakuna
hata huduma moja ya hospitali aliyoipata maana
wote walimkataa”
“Mmmmh nadhani ndiomana sababu mtoto
akizaliwa tu huwa wanamuangalia hivi vitu lazima
anye na kukojoa ila mtoto akae siku zote hizo bila
kunya jamani!”
“Hivi wewe Zayana una matatizo gani? Hebu acha
maneno yako machafu hayo, kamnawishe basi huyo
mtoto”
“Yananuka sana dada”
“Ndio hata mimi nasikia harufu, ila tutafanyaje sasa
zaidi ya kumnawisha tu!”
Basi Zayana ilibidi tu amchukue yule mtoto na
kwenda kumnawisha vile vile huku akiona kinyaa
sana ila alimnawisha na kurudi kumvalisha.
Juma aliporudi tu ule ujumbe ndio ulikuwa wa
kwanza kabisa kupewa kuhusu kujisaidia haja
kubwa kwa mtoto basi alibaki kushangaa tu,
“Kama ya mbuzi!!”
Zayana akadakia,
“Ndio, yale kama karanga karanga”
“Yani Zayana khaaaa mambo yako mdogo wangu
hadi unakera”
Juma alikuwa kimya tu ila alielewa maneno ya yule
binti kuwa kuna jambo la ajabu litatokea ila kwake
hili jambo hata halikuwa la ajabu sana kwani alihisi
labda kutokana na mtoto wake kutokujisaidia toka
siku amezaliwa ndio imepelekea kujisaidia kinyesi
cha aina ile.
Usiku ule walilala tu kama kawaida, na hata asubuhi
na mapema kabisa Juma aliamka na kujiandaa
kwenda katika shughuli zake kama kawaida.
Basi muda huu Mariam alikaa na mdogo wake
wakiongea ambapo mdogo wake aliamuuliza swali
dada yake,
“Hivi dada, shemeji kasemaje jana kuhusu mwanae
kutoa kinyesi kama cha mbuzi?”
“Kasema kuwa ni sababu mtoto hajapata choo toka
azaliwe ndiomana imekuwa hivi”
“Ila dada kwa hizi siku chache tu nilizoishi hapa,
namuona kama huyu mtoto hayupo sawa vile”
“Kivipi mdogo wangu?”
“Mmmmh namuona kama sio mtoto wa kawaida”
“Tatizo hujawahi kuzaa wewe mdogo wangu”
“Sio kutokuwahi kuzaa dada, ila nimewahi kuona
watoto kadhaa dada ila mtoto huyu naona kama ni
mtoto wa maajabu”
Mara mtoto alianza kullia kama ambavyo alikuwa
akilia jana, ikabidi Zayana aende kumuangalia na
kumkuta kajisaidia tena kama alivyojisaidia jana
yake, basi Zayana akamwambia dada yake,
“Dada, mtoto wako kafanya tena mambo huku.
Katoa kinyesi cha mbuzi”
“Mmmmh nenda kamnawishe tu Zayana”
Basi Zayana akambeba ili akamnawishe, alivyotaka
kumuweka wenye dishi alishangaa yule mtoto
akimwambia Zayana,
“Mimi sitaki kunawishwa na wewe, nataka
kunawishwa na mama”
Yani Zayana aliogopa na kujikuta akitetemeka na
kuwa kama ameganda vile alimuacha yule mtoto
kwenye dishi na kumuita dada yake, Mariam alitoka
hadi pale bila kujua kuwa kuna nini. Zayana
akamwambia dada yake,
“Mtoto wako huyo, mnawishe mwenyewe”
Zayana akaondoka zake, na moja kwa moja alienda
ndani kuchukua begi lake maana hakuona kama
angeweza kuendelea kukaa pale na yule mtoto.
Mariam na yeye aliogopa alimuangalia yule mtoto
aliyekalishwa kwenye dishi huku akimuangalia
mdogo wake, akashangaa yule mtoto akimwambia,
“Unashangaa nini mama? Njoo uninawishe”
Mariam alitetemeka kwa uoga, na vile alivyomuona
mdogo wake akitoka hata hakuuliza mara mbili bali
na yeye aliunganisha nyuma kwa mdogo wake na
wala hakubeba kitu.
Walipofika njiani ndipo walipoongea ambapo
Zayana alimuuliza dada yake,
“Dada, mbona umeondoka pia?”
“Siwezikkuishi na mtoto wa ajabu kiasi kile”
“Ila ni mtoto wako dada, mimi ndio siwezi kabisa.
Kitoto kidogo vile kinanisemesha, ila dada
umemuacha mule mule kwenye dishi, si ataanguka
kwenye maji yule? Atakufa dada”
“Aaaah siwezi, muache tu, yani hata nguo sichukui
tutaenda tu wote nyumbani”
“Kwahiyo na kwako hujafunga wala nini?”
“Sijafunga ndio, siwezi kwakweli, mimi mwenyewe
nimepatwa na uoga wa hali ya juu”
Walitembea hadi stendi, walikaa na kusubiria gari
ila pale stendi wote wawili walianza kusinzia.
Waliposhtuka walijikuta wakiwa ndani sebleni huku
mtoto akiwa kwenye kochi akiwaangalia.
 
MTOTO WA MAAJABU: 5
Walitembea hadi stendi, walikaa na kusubiria gari
ila pale stendi wote wawili walianza kusinzia.
Waliposhtuka walijikuta wakiwa ndani sebleni huku
mtoto akiwa kwenye kochi akiwaangalia.
Yani waliogopa sana na Zayana ndio aliyeanza
kumuuliza dada yake,
“Hivi dada si tulikuwa stendi sisi?”
Mariam akajibu,
“Ndio, na begi lako nlile pale”
Zayana akaangalia lile begi lake ambalo lilikuwa
mlangoni na kumfanya ashtuke sana halafu
akamuuliza dada yake,
“Sasa ni kitu gani kimeturudisha?”
“Au hatukuondoka mdogo wangu?”
“Nakumbuka kuwa tuliondoka na ulisema mtoto
umemuacha kwenye dishi, mbona ni yule kwenye
kochi anatuangalia?”
Walimuangalia mtoto huku wakijikuta wanamuogopa
zaidi ya walivyomuogopa mwanzoni, mtoto
akawauliza,
“Sasa mnaogopa nini?”
Hapo Mariam na Zayana walijikuta wakizimia kwa
uoga.
Leo Juma alichelewa kurudi nyumbani kwake kwani
alikuwa na mambo mengi sana ya kufanya,
alivyofika alifungua tu mlango na kutokukuta watu
pale sebleni akajua tu wote wamelala, basi alienda
chumbani kwake na kweli alimkuta mkewe na mtoto
wamelala, alitabasamu na kufurahi sana kuona vile
ukizingatia kila siku huyu mkewe alikuwa hataki
kulala na mtoto, basi Juma akaenda zake kujiandaa
kulala, na yeye alijilaza pembeni yao.
Kulipokucha, Juma ndio alikuwa wa kwanza kuamka
yani alitabasamu sana na kumuamsha mke wake,
“Mariam, Mariam”
Mkewe aliamka na kukaa yani alikuwa kama
akijitafakari hivi hadi Juma akamuuliza,
“Vipi kwani? Kuna nini?”
“Unajua najiuliza, nimekuja vipi kulala chumbani?”
“ivipi yani?”
“Ngoja kwanza”
Mariam aliinuka na kuanza kumuita mdogo wake
ambapo alipotoka nje alimkuta mdogo wake
ameshia tena begi, muda huu Juma na yeye alitoka
ila alikuwa haelewi ni kitu gani kinaendelea.
Mariam alimuuliza mdogo wake,
“Vipi Zayana?”
“Siwezi kuendelea kuishi humu ndani”
“Kwahiyo unataka kuniacha mwenyewe? Tunaenda
wote”
“Hapana dada, sitaki kuendelea kuishi hapa na
sitaki kuondoka na wewe”
Juma alikuwa hawaelewi kwakweli, na kuwauliza
kwa makini,
“Kwani kuna nini? Mimi sielewi?”
“Shemeji, siwezi kuendelea kuishi hapa, mtoto wako
anakunya mavi kama ya mbuzi halafu anaongea”
“Kivipi?”
“Anasema kuwa hataki kunawishwa na mimi,
anataka unawishwa na mama yake, kwakweli siwezi
kuendelea kuishi hapa shemeji, mtoto wako
ananitisha sana”
“Nakuomba shemeji yangu, usiondoke leo tufanye
utaratibu wa msichana wa kazi kwanza”
Mariam akadakia,
“Hata ukitafuta msichana wa kazi hata mimi siwezi
kuendelea kuishi hapa”
“Usinichanganye Mariam, kumbuka huyu mtoto
umebabe wewe mimba, uchungu umepata wewe na
kumzaa umemzaa wewe, unataka kunitisha mimi
kuwa humtaki? Msinichanganye jamani, angalieni
uwezekano wa kutafuta msichana wa kazi na sio
kuniletea mambo yasiyoeleweka”
Juma aliamua kutumia ukali maana aliona hawa
wanawake kama akiendelea kuwa mpole basi
watampanda kichwani.
Zayana akamuuliza shemeji yake,
“Na mimi nahusika na nini kwa huyu mtoto?
Naomba mimi niende shemeji?”
“Makubaliano yetu Zayana hayakuwa haya,
unatakiwa usubiri tupate msichana wa kazi ndio
uondoke”
“Duh!”
Zayana akapata wazo la kumpigia simu mama yao
ambapo alipoongea nae akamuahidi kuwa badae
ataenda na atawapelekea msichana wa kazi wa
ndugu yao mwingine ili waweze kukaa nae.
Juma leo hakutoka kwenda popote kwahiyo ni yeye
mwenyewe ndio aliyekuwa akishughulika na mtoto
wake na wala mtoto yule hakumfanyia Juma swala
lolote la kumshangaza zaidi ya Mariam na mdogo
wake.
Kwenye mida ya saa kumi na mbili jioni, mama
Mariam alifika akiwa ameambatana na mdada
mmoja ambapo aliwatambulisha kwao kuwa ndio
huyo mdada wa kazi aliyemchukua kwa ndugu yao,
“Anaitwa Dora huyu”
“Aaaah Dora, karibu sana Dora, jisikie kama upo
nyumbani”
“Asante”
Zayana hakutaka hata kupoteza muda, na alitaka
kuondoka siku hiyo hiyo ila mama yake alimuaomba
kuwa waondoke kesho yake maana alimuona
mwanae kuwa na haraka sana, ilionyesha wazi kuwa
Zayana hakutaka kabisa kuendelea kuwa mahali
hapo.
Kwa usiku huo walilalal tu hapo hapo na hakuna
chochote kile ambacho kilitokea.
Leo Juma alienda kwenye shughuli zake halafu
Zayana na mama Mariam nao waliondoka, kwahiyo
pale alibaki Mariam pamoja na Dora, basi Mariam
alianza kumuelekeza Dora kazi za mule ndani,
“Humu unataiwa kusafisha nyumba, kuosha vyombo,
kupika, kufua na kumuangalia mtoto. Hizo ndio kazi
zako, bila kusahau kuteka maji maana lazima
tuchote hapo nje kuyaweka ndani”
Dora akamuuliza Mariam,
“Kwani na wewe dada unakuwa kazini?”
“Hapana, mimi bado sijaanza kazi, nipo hapa hapa
nyumbani”
“Kwahiyo utakuwa ukinisaidia saidia hizo kazi eeeh!”
“Sasa kazi gani za kusaidiwa hapo? Kazi zote ni za
kawaida, tena ni kazi za kila mwanamke, halafu
humu ndani tupo mimi na wewe tu, na shemeji yako
akirudi, ni kazi gani hapo? Kama kupika unapika
chakula chetu tu, vyombo hapo hata vingapi havifiki
kuosha, haya tukija kwenye swala la kusafisha
nyumba, hii nyumba ina ukubwa gani wa kushindwa
kusafisha? Kwenye kuchota maji, je kwenu
mlikkuwa hamchoti maji? Tena usikute mlikuwa
mnachota mtoni huko, ila hapa utachota hapo nje
tu, sasa kuna kazi gani ya kusaidiwa hapo?”
“Hakuna dada, nimekuelewa dada yangu”
Basi Dora alikubali na kuanza kazi mbalimbali za
pale ndani ya nyumba.
Mtoto akilia, Mariam hakuwa na muda kabisa wa
kuishika mtoto wake kwanza kabisa ukizingatia
alikuwa akimuogopa, basi alikuwa akimuita Dora tu,
“Dora, hebu muangalie mtoto analia nini?”
“Itakuwa njaa inamuuma dada”
“Basi mkorogee maziwa yake umpe, njoo
nikuelekeze namna ya kumkorogea”
“Ila dada mimi napika”
“Acha kupika, njoo umkorogee kwanza maziwa
umpe”
Basi Dora aliacha na kwenda kuelekezwa namna ya
kukoroga maziwa ya mtoto kisha alienda kukoroga
na kwenda kumpa mtoto aweze kunywa yale
maziwa, na kweli mtoto alikunywa maziwa yote
aliyoyakoroga kwa wakati ule.
Kisha Dora sasa ndio akaenda kuendelea na swala
zima la kupika.
Leo Juma aliwahi kurudi na alifurahia jinsi Dora
anavyoonekana ni mchapakazi pale ndani na
kumsifia,
“Hongera sana binti”
Mariam aliguna na kusema,
“Unampa hongera ya bure tu, ni mvivu huyo balaa”
Dora akasema,
“Jamani dada, mbona kazi zote nafanya?”
“Unafanya ndio ila unfanya kivivu yani ukianza
kuosha vyombo unaosha wee, muda wote ni mvivu
wewe, jirekebishe”
Basi kwa muda huo waliweka tu chakula na kula
kisha kwenda kulala.
Usiku ule, Juma aliamua kumsema mkewe
chumbani kwa kauli ile aliyomwambia Dora pale
sebleni,
“Mariam sio vizuri hata kama ni mvivu basi
ungekuja kumsemea huku chumbani”
“Hivi unajua kuwa mimi siwezi kuficha ficha jambo!
Yule binti ni mvivu nakwambia, akianza kusafisha
ndani hadi kero, anatumia muda mrefu sana
kusafisha ndani, utakuta hadi mtoto analia, hapo
ananiambia dada si umbembeleze tu”
“Sasa mke wangu wewe kumbembeleza mtoto
unaona shida gani?”
“Kwanini tumeweka msichana wa kazi? Si
kwasababu ya huyu mtoto”
“Kama ni kwasababu ya mtoto basi kazi zingekuwa
zikifanywa kwa kusaidiana”
“Khaaaa huna huruma kabisa wewe mwanaume,
nimebeba mimba kwa miaka miwili, nimepata
uchungu huo sidhani kama wanawake wote
wamepata uchungu kama mimi, nimejifungua mtoto
wa ajabu ila bado huna huruma unataka
nikasaidiane na msichana wa kazi! Natakiwa
kupumzika, kwakweli nilifanya makosa sana
kukubali kuolewa na wewe”
“Kheee bado una kauli hiyo Mariam?”
“Ndio”
“Sasa unadhani ni nani ndio angekufaa kuolewa
nae?”
“Unamjua fika, nilimpenda sana huyu mwanaume.
Bora angenioa yeye”
“Khaaaa, tulale tu. Wewe mwanamke unaweza fanya
nikakuzaba vibao kwakweli”
Juma aliamua kulala zake na kumchukua mtoto
wake pembeni.
Mapema kabisa, Juma aliondoka zake na kumuacha
pale ndani Mariam na Dora pamoja na mtoto, muda
huu Dora alikuwa akisafisha ndani, basi Mariam
alitoka na kumwambia,
“Dora ukimaliza basi hapo, utaenda kufua zile nguo
za mtoto zipo kwenye dishi tokea jana”
“Sawa dada”
“Halafu uwanja nao hujafagia kabisa toka jana Dora
hata huwa sielewi unafanya nini jamani!”
“Nitafagia dada”
Mariam alikaa pale, Dora alimaliza kusafisha ndani
na kwenda kufua zile nguo za mtoto yani muda huu
Mariam alihisi njaa sana na kumuita Dora,
“Hivi bado hujapika chai tu Dora?”
“Mkate upo dada alileta shemeji jana, bado chai tu
sijabandika”
“Hivi ukoje wewe jamani, unachelewa sana kuamka,
hadi saa mbili hii hujabandika chai kweli!”
“Dada, nilianza kuosha vyombo kwanza kabla ya
kusafisha ndani”
“Yani wewe Dora ni mvivu jamani, kuna wasichana
wa kazi wenzio huwa wanaamka mapema sana,
wanaamka saa kumi na kufanya shughuli zote yani
kama muda huu alishamaliza kila kitu, ila wewe ni
uvivu namba moja.”
Kisha alienda mwenyewe kubandika chai na kunywa,
huku mtoto wake akimuangalia na kusema,
“Na mimi nataka chai leo”
Mariam alishtuka na kusema,
“Hata sijasikia kitu, sijasikia chochote”
Alitoka nje kwa muda huo na kwenda hadi ambapo
Dora anafagia, basi Dora akamuuliza,
“Naona umekuja kunisimamia dada, ila ndio
namalizia”
“Hapana sijaja kukusimamia ila nataka twendwe
kunywa chai”
“Khaaa dada jamani, naona leo ni ndoto, unataka
tukanywe chai pamoja?”
“Ndio mdogo wangu”
“Ngoja nimalizie”
Basi Dora alimalizia pale kufagia na kisha yeye na
Mariam wakaenda ndani kwaajili ya kunywa chai, ila
cha kushangaza pale ambapo Mariam aliacha
kikombe cha chai na mikate vyote alikuta vimeliwa
na kumfanya Mariam amuangalia yule mtoto wake
ambaye alikuwa amelala kwenye kochi kwa muda
huu.
Dora alikuwa akimshangaa Mariam alivyokuwa
akishangaa na kumuuliza,
“Sasa dada unashangaa nini?”
“Niliweka hapa chupa ya chai na mkate, nilikula
vipande viwili tu nikaja kukuita ila nashangaa kuona
hakuna mikate wala chai, vimeenda wapi?”
“Dada, una uhakika kuwa uliacha mikate na chai
kweli hapa?”
“Sasa unadhani naweza kula mkate mzima mimi?
Nilichukua wote mkate na kkuuweka hapa”
“Sasa itakuwa vimeenda wapi?”
“Sijui hata mimi nashangaa”
“Mmmmh”
Dora aliguna tu, kwahiyo aliamua kwa muda huo
aende tu akapike chakula cha mchana maana hata
yeye hakuelewa ila alihisi huenda huyu Mariam
amekula mkate wote ila kaamua tu kujigelesha,
ukizingatia hajawahi hata mara moja kumuita yeye
kuwa waende wote kunywa chai.
Dora akiwa jikoni anapika, Mariam alimfata Dora
jikoni na kuanza kuongea nae,
“Pika haraka Dora maana njaa zinauma hatari”
“Sawa dada”
Dora aliitikia tu ila alijua wazi kuwa mkate wote
umeliwa na Mariam, alipomaliza kupika aliweka
chakula na walianza kula sasa huku wakiongea
ambapo baada ya kumaliza kula ndio Dora
alikumbuka kuhusu mtoto,
“Kheeee dada, huyu mtoto leo hali?”
“Utamlisha bila kuamka? Si unamuona bado
amelala!”
“Unajua dada, mimi nimeshalea watoto wengi tu.
Kwa kawaida asubuhi mtoto unampa chakula,
unamuogesha na anaweza akalala, sasa huyu hajala
mpaka muda huu eti amelala tu”
“Haya nenda kamuamshe umlishe basi”
“Mmmmh hapana, acha tu aamke mwenyewe ndio
tumpe chakula”
Basi walimaliza pale na Dora alitoa vile vyombo na
muda huu alipata kupumzika sasa, ambapo Mariam
alimuuliza Dora,
“Ila Dora, hebu tuongee kirafiki muda huu. Asubuhi
ulishindwa nini kubandika chai leo? Wakati kila siku
huwa unabandika?”
“Dada, leo nakiri wazi kuwa nimechelewa kuamka
maana nimeamka saa kumi na mbili na nusu, na
hapo nilianza na kuchota maji kwanza, halafu ndio
nikaenda kuosha vyombo kisha ndio nikaja
kusafisha ndani, yani swala la kubandika chai
nikasahau kabisa dada yangu”
“Haya hapo nimekuelewa, ila ngoja nikwambie
ukiamka siku nyingine kabla ya vyote anza kwanza
kubandika chai”
“Ila dada mbona kubandika chai sio kazi? Ila usijali,
nitakuwa nabandika”
Waliongea pale ila Dora aliweza kuona jinsi gani
bosi wake huyu alikuwa ni mvivu maana alipenda
kukaa tu, ila huyu mtoto ndio alikuwa anamchosha
zaidi Mariam maana kila akimuangalia anajikuta
anakosa hata furaha kabisa.
Leo mume wa Mariam aliwahi kurudi na kuna nguo
zake aliomba ziweze kufuliwa maana yeye alikuwa
amechoka kuzifua, basi Mariam alizibeba na
kwenda nazo hadi kwa Dora,
“Dora, naomba uende kufua nguo za shemeji yako
hizi”
Dora alimuangalia Mariam ila alichukua zile nguo na
kwenda kufua halafu Mariam alirudi kuongea na
mume wake,
“Kwahiyo nguo umempa Dora akafue mke wangu?”
“Ndio, Dora atazifua”
“Ila nahitaji kuvaa zile nguo kesho”
“Nadhani ameenda kufua tayari, sasa ulitaka nikafue
mimi kweli wakati tuna msichana wa kazi humu
ndani!”
Juma akatikisa kichwa na kusema,
“Ila wewe Mariam ni bure kabisa”
“Bure kivipi? Huna huruma wewe mwanaume,
nimebeba mimba kwa miaka miwili mimi, tofauti na
wanawake wote duniani, haya nimepata uchungu
ambao hakuna mwanamke aliyewahi kupata,
nimejifungua mtoto wa ajabu halafu bado unakosa
huruma unataka nikafue kweli! Hebu kuwa na
huruma Juma japo kidogo”
“Sina maana kuwa sina huruma Mariam, ila siku hizi
naona ndio umekuwa msemo wako huo, sijui
nimebeba mimba kwa miaka miwili, yani kila kazi
ukiambiwa unasema kuwa umebeba mimba kwa
miaka miwili, sijui umezaa kwa uchungu yani kama
wimbo wa taifa vile. Ila ngoja nikuulize Mariam, lini
umefanya kazi wewe hata kipindi huna hiyo mimba
uliyobeba kwa miaka miwili! Tuongee tu ukweli, ila
sasa hivi umepata kitu cha kukutetea ndiomana”
“Mmmmh ila wanaume mna roho mbaya sana,
natamani siku moja Mungu apindue dunia halafu
nyie wanaume ndio mbebe mimba ndio mtajua kitu
gani huwa kinatokea kwetu tukibeba mimba”
“Ila si tayari umeshajifungua jamani Mariam!! Mada
za mimba ya miaka miwili bado zinaendelea tu loh!”
Juma aliamua kutoka nje ili akamuarakishe Dora
kumfulia ile nguo maana alilitaka kwa haraka sana
ili kesho yake aivae.
Alimkuta Dora ndio kwanza anaweka ile nguo
kwenye maji tena kwa kujivuta vuta sana, basi
alimsalimia pale na Dora alianza kufua sasa huku
akiongea nae,
“Dora mbona umenuna hivyo?”
“Huna ndani, dada na yeye yupo tu ila kila kazi
ananiachia mimi jamani!”
“Kheee Dora, huelewi maana ya msichana wa kazi
au?”
“Hata kama mimi ni msichana wa kazi ila inatakiwa
vitu vingine anisaidie, kila nguo nifuie mimi, za
kwake nifue, za kwako na mtoto zote nifue, kila
chakula nipike mimi, mtoto nimuhudumie mimi.
Nilijua atakuwa ananisaidia sababu yupo nyumbani”
“Mfano angekuwa anshinda kazini je?”
“Hiyo ya kushinda kazini huwa inajulikana, ila mtu
akiwa nyumbani jamani tena huyu mkeo anatuma
kama muhindi, utasikia mara niletee maji ya
kunywa, sijui chukua kikombe upeleke, angalia
mtoto analia nini, mpe maziwa, yeye amekaa tu
jamani khaaaa!! Chukua nguo umbadilishe, njoo
ufute hapa sijui nini kimeanguka, yani kwa muda
mfupi tu nimechoka, mama anatuma huyu sijapata
kuona”
“Aaah usijali, nitaongea nae. Chakula cha kesho
atapika yeye, tena huwa anapika chakula kitamu
sana. Kwahiyo usijali”
“Sawa, ila mambo mengine awe ananisaidia, kama
kubandika chai jamani kuna kazi gani sasa hadi
nibandike mimi kweli!!”
“Nimekuelewa Dora”
Basi Juma alimuacha hapo Dora na kurudi ndani
kwa mke wake.
Usiku ule Juma alimwambia Mariam ili tu kesho
apike na Dora aone kuwa mke wake amejirekebisha
ingawa hawezi kumwambia moja kwa moja kuwa
aache uvivu maana anamjua fika, Juma alimwambia
mkewe
“Kesho nitawahi kurudi Mariam, ila natamani sana
unipikie chakula, natamani sana nile chakula chako
mke wangu”
“Chakula gani sasa unataka?”
“Nataka ugali na samaki”
“Sawa, kuna kijana huwa anapita pita anauza
samaki, nitanunua kesho na nitapika mwenyewe
hakuna tatizo. Kwahiyo unarudi muda gani?”
“Mchana tu nitakuwa nimerudi ili tule pamoja”
“Sawa hakuna tatizo”
Basi kwa muda huu waliamua moja kwa moja
kulala tu, na kulipokucha tu Juma aliondoka
mapema na kumkumbusha mke wake kuhusu lile
swala la kumpikia.
Mchana wa siku hiyo ni kweli kabisa Mariam alipika
yeye ila bado Dora alikuwa akilalamika maana
kupika kapika Mariam ila Dora alikuwa akkitumwa
kwa kila kitu, sijui niletee mwiko, sufuria na kila kitu
yani hadi Mariam alipomaliza kupika basi Dora
alishukuru sana.
Muda huu Mariam na Dora waliandaa chakula huku
Mariam akimwambia dora kuwa wasubirie Juma
arudi ndio waweze kula nae.
Dora alikuwa anatamani sana kula kile chakula,
alijikuta akitoka nje kumsubiria huyo shemeji yake,
alipomuona akamuita Mariam,
“Dada, shemeji huyo anakuja”
Basi Mariam na yeye alitoka nje kumuangalia, yani
alijikuta tu siku hiyo yupo hivyo wakati siku zote
huwa hatoki kumuangalia mumewe anavyokuja wala
nini.
Mariam na Dora walimsubiria Juma hadi aliposogea
pale karibu ambapo hadi Juma aliwashangaa,
“Kwani kuna nini leo hadi kusubiriwa hivi?”
Dora akadakia,
“Dada kapika, chakula kinanukia nyumba nzima.
Tunakusubiria ili tuweze kula”
Juma akacheka na kusema,
“Ndiomana nilimuoa huyu mwanamke jamani”
Kisha wakaingia ndani sasa na kusogea mezani, ila
walishangaa sana kwani ugali wote ulishaliwa na
samaki wote walishaliwa.
 
MTOTO WA MAAJABU: 6
Kisha wakaingia ndani sasa na kusogea mezani, ila
walishangaa sana kwani ugali wote ulishaliwa na
samaki wote walishaliwa.
Yani kila mtu alibaki na mshangao wa hali ya juu,
Dora na Mariam walitazamana wakati huo Juma
aliuliza,
“Hiko chakula kiko wapi sasa?”
Mariam akamjibu,
“Hata sisi tunashangaa mume wangu ujue”
“Mnashangaa nini sasa?”
“Hivi huoni kama chakula kimeliwa hapa? Tena
kilikuwa ni kitamu hicho balaa”
“Sasa kimeliwa na nani?”
“Hata sisi tunashangaa”
Mariam akamtazama Dora na kumuuliza,
“Eti jamani Dora, si tuliandaa chakula mezani hapa!”
“Ndio dada”
“Itakuwa nani amekula jamani!”
Juma aliwaacha pale na kwenda chumbani kwani
moja kwa moja alihisi huyo mke wake Mariam na
Dora wamefanya jambo, yani alihisi kuwa wamekula
kile chakula maana hakuona kama ni kitu cha
kawaida kabisa kile.
Aliamua tu kujilaza, ila alikuwa akihisi njaa sana
maana tayari alishasema kuwa siku hii angekuja
kula nyumbani kwake.
Dora na Mariam wanaulizana tena kwa muda ila
Dora anahisi kitu kuwa huenda Mariam kamvizia
wakati yuko nje na amekula kile chakula ila
hakusema kwa muda huo, basi Mariam
akamwambia Dora,
“Hebu Dora tufanye hivi, songa ugali mwingine
niende hapo gengeni nikanunue hata tembele uje
upike tule”
“Dah!! Njaa inauma sana dada”
“Hata mimi njaa inaniuma ila sijui ni kitu gani
kimetokea jamani”
Basi Mariam akaondoka na kumuacha Dora
akisonga ugali mwingine huku akijiuliza mambo
mengi sana, kisha Mariam alirudi na mboga
ambapo Dora aliipika na Mariam akamuita mumewe
wakala kile chakula ila Juma hakuwa na furaha
kabisa kwani alihisi ni mchezo mchafu kafanyiwa na
mke wake ukizingatia mke wake ni mvivu sana.
Waliposhiba, moja kwa moja Mariam alienda kulala
maana alikuwa akishiba basi anashikwa na usingizi
sana, muda huo Dora alikuwa nje akiosha vyombo,
Juma aliamua kwenda kumuuliza Dora,
“Samahani Dora, hivi dada yako kweli alipika
chakula leo?”
“Kupika ni kweli alipika”
“Niambie ukweli Dora maana mke wangu kwa uvivu
namjua vizuri sana, ni mvivu sana huyu mwanamke.
Alipika kweli?”
“Hapo nakwambia ukweli shemeji, kupika alipika
ingawa wakati anapika anatuma huyo kama
muhindi, utasikia, nisogezee maji, hebu koroga
hapo, nisogezee mwiko, hebu nikatie kitunguu yani
yeye akikaa mahali basi habanduki ndio hapo hapo
ila kupika alipika shemeji”
“Sasa chakula kimeenda wapi?”
“Hapo hata mimi nashangaa kwakweli, chakula
kimeenda wapi? Tena alipika vizuri hadi mimi
nikawa natamani na kuamua kutoka nje kukusubiri
maana alisema tukusubiri kwanza ndio tuweze kula
kile chakula, nilipokuona unakuja nilimuita na
ndiomana na yeye alitoka nje kukuangalia kama
unakuja kweli, ila sasa aliyekula kile chakula ndani
hata sijui shemeji”
“Mmmmh!! Sawa, nitajua cha kufanya”
Basi Juma akaondoka zake na kumuacha Dora pale
akimalizia kuosha vyombo.
Usiku ule wakiwa sebleni waliweza kujadiliana sasa
kuhusu mtoto maana alionekana muda wote kuwa
ameshiba sana,
“Yani leo mtoto kanywa maziwa kidogo sana”
Juma akauliza,
“Au anaumwa?”
Mariam akasema,
“Sidhani kama anaumwa ila labda kabadili tu kipindi
maana kuna kipindi watoto huwa wanakula sana na
kuna kipindi huwa hawali sana”
Basi Dora akasema tena,
“Ila mbona analala sana?”
Juma hakutaka yale majadiliano zaidi kwani aliinuka
na kumbeba mtoto halafu akampeleka chumbani na
kumlaza, kisha yeye alibaki nae chumbani huku Dora
na Mariam wakiwa pale wanajadiliana.
“Ila dada mbona mtoto analala sana leo?”
“Mmmmh Dora, mambo ya mtoto huyu yaache tu,
yatakuumiza kichwa, fanya tu kazi zako maana
ukifikiria ya huyu mtoto unaweza kuwa kichaa”
Kisha Mariam aliinuka na kwenda kulala pia, ila
kiukweli Dora alikosa amani kabisa ya kuishi mule
ndani kwanza alianza hata kupatwa na uoga flani
hivi.
Asubuhi na mapema, Dora aliamka na kuandaa chai
kwanza na vitafunwa kisha akaiweka mezani na
kwenda kufanya sasa kazi zingine, alisafisha ndani,
alienda kuosha vyombo, kufagia nje na kujaza maji,
aliingia tena ndani kwenye mida ya saa tatu asubuhi
wakati huo Mariam nae alikuwa ndio anaamka, basi
akamsalimia na kitu cha kwanza kabisa Mariam
aliangalia mezani na kushangaa kuona Dora
alishatenga chai,
“Kheee leo mapema ushatenga chai?”
“Ndio dada, nimepika mapema kabisa”
“Sema leo sijaamka na njaa kabisa, sina njaa wala
nini. Ngoja nikae kae kwanza, au ngoja nikaoge
kwanza”
Basi Mariam alienda kuoga, wakati huo Dora na
yeye alitoka nje, shida ya Dora ni kuona kama ile
chai iliyoandaliwa itanywewa au ni vipi maana bado
hakuelewa kuhusu chakula cha jana.
Ila hadi badae anarudi ndani, na Mariam anakuja na
kunywa ile chai hawakukuta imenywewa hata
kidogo.
Walipomaliza ndipo mtoto alipoanza kulia njaa
ambapo Dora alienda kumuandalia maziwa na
kumpatia yale maziwa, kisha yule mtoto aliyanywa
na kulala, muda huu Dora aliendelea na mambo
mengine ila bado alikuwa akijiuliza kuwa chakula
kililiwa na nani.
Muda huu wakiwa wamekaa pamoja, Dora aliamua
kumuuliza swali Mariam kwani kuna kitu kilikuwa
kinamshangaza sana toka amefika mahali hapa,
“Dada, toka nimefika ni siku nyingi zishapita ila
mbona sijawahi kuona huyu mtoto akijisaidia haja
kubwa?”
“Kheee unapenda kufua nguo za haja eeeh!”
“Hapana sio hivyo ila kujisaidia haja kubwa ndio
uhai wenyewe huo, mtu yoyote lazima ujisaidie,
kumbuka mtu unakula chakula, je kinaenda wapi
kama mtu hujisaidii? Sasa huyu mtoto toka
nimefika sijakusikia hata mara moja kuwa
amejisaidia haja kubwa”
“Mmmmh Dora, acha tu habari za huyu mtoto
nakwambia, wala hata usizifatilie ukitaka kuishi kwa
amani”
“Halafu mbona anaonekana ni mtoto mkubwa tu ila
muda wote huwa unamlaza kwenye kochi? Kwani
haiwezekani akakaa huyu mtoto dada?”
“Wewe unavyomuona huyo mtoto unaweza
kumkadilia kwenye umri gani?”
“Yani anaonekana ni mtoto mwenye mwaka na kitu
hivi”
Mariam alimuangalia mtoto wake kisha
alimuangalia Dora na kumuuliza,
“Hivi umeshapika chakula cha mchana?”
“Bado sijapika”
“Basi nenda kapike kwanza tuje kula maana sidhani
kama nina majibu ya maswali yako”
Dora hakuwa na jinsi zaidi zaidi ya kwenda kupika tu
chakula cha mchana.
Muda huu Mariam aliinuka na kwenda kulala
chumbani kwani alikuwa akijihisi uvivu sana
kuendelea kukaa pale sebleni.
Dora alipomaliza kupika, aliandaa chakula mezani
na kukiacha hapo halafu yeye alitoka nje kwani
alitaka kusona kama na siku hiyo hiko chakula
kitaliwa au la, basi akakaa nje kwa muda sana hadi
pale alipoitwa na Mariam,
“Wewe Dora, kumbe umemaliza kupika hata husemi
jamani!”
“Samahani dada, nilitoka kupunga upepo nje”
“Haya basi, njoo tule”
Walienda na kukaa kula, ila chakula kilikuwa vile
vile, yani hakikuliwa wala nini kilikuwa vile vile
kama ambavyo Dora alikiandaa.
Basi walikula pale huku wakiongea mambo
mbalimbali tu kwa wakati huo.
Walipomaliza tu, Dora alitoka kwenda kuosha
vyombo ila kabla hajaanza kuosha yule mtoto
alijisaidia maana huwa akijisaidia ni harufu nyumba
nzima, Mariam alimuita Dora,
“Wewe Dora, hebu njoo. Msafishe mtoto hapo
amejisaidia”
“Mmmmh dada!!”
“Unaguna nini sasa?”
Dora hakujibu ila alienda kumchukua mtoto ili
akamsafishe, kwakweli hata yeye alishangaa na
kumwambia Mariam,
“Dada, mbona anajisaidia kama kinyesi cha mbuzi?”
“Aaah ni sababu ya kutokujisaidia kwa siku nyingi”
“Hapana dada, hii ni tatizo. Kikwetu nakumbuka
kuna dawa tulikuwa tukimpa mtoto kama akitoa
haja inayofanana na mbuzi, ila huyu ni kama ya
mbuzi kabisa”
“Dawa gani”
“Inapatikana polini, unataka nikamtafutie na huyu?”
“Ndio, itakuwa vizuri ukifanya hivyo”
“Sawa basi, kesho nitaenda kuiangalia kwenye kale
kapori”
“Sawa mdogo wangu, ila utaenda muda gani?”
“Itabidi niende jioni dada maana hiyo dawa itabidi
tumpatie asubuhi”
“Aaaah!! Basi sawa, hakuna tatizo mdogo wangu”
Wakajadiliana pale na kuendelea na mambo
mengine.
Usiku ule Mariam anamwambia mumewe kuhusu
dawa ambayo Dora ameisema, na Juma
anakubaliana na hiyo dawa,
“Kama dawa ipo basi ni vizuri sana, mtoto apatiwe
maana sio jambo la kawaida hata mliponiambia
kuwa mtoto anajisaidia kinyesi kama cha mbuzi
nilishangaa sana, ila kama kuna dawa ni vyema
mtoto akapatiwa”
“Sawa, kasema kuwa ataenda kuitafuta kesho jioni”
“Sasa mke wangu, itabidi chakula cha usiku upike
wewe au unaonaje hapo?”
“Kweli itabidi nipike mimi ila na wewe uwahi kurudi,
ili Dora akienda huko basi wewe uwepo hapa
nyumbani na mimi”
“Ila umpate mtu wa kumtuma muda wa kupika
eeeh!”
“Aaah jamani mume wangu, unaniona mimi ni
mvivu hatari. Sikia, kesho nitapika pilau, kwahiyo
nitakachokifanya ni kila kitu tutaandaa na Dora, yani
ataondoka hapa wakati mimi ndio naanza kupika.
Hapo atakuwa kanisaidia”
“Ila mke wangu huwa unaonaje kitu kama hiko
ukikifanya mwenyewe?”
“Jamani huwa naona uvivu hatari, mara nyingine sio
kwamba sitaki kufanya kazi ila naona uvivu”
“Punguza huo mwili mke wangu”
“Umeanza sasa, uvivu wangu na mwili vinauhusiano
gani? Mbona kuna watu wembamba wavivu? Na
kuna watu wanene wavivu pia. Kwanza mimi uvivu
nimeanza zamani kabla hata sijanenepa, umesahau
kuwa hii mimba ndio ilifanya ninenepe hivi?
Umesahau kipindi unanioa Juma?”
“Kweli, kipindi kile hukuwa mnene hivyo”
“Ndio hivyo, wale wenye miili yao ya asili wanaweza
kuendelea na kazi ila wengine sio asili yetu,
ukijumlisha na uvivu wa siku zote basi ndio balaa.
Ila nitapika hiyo kesho maana hata mimi nataka hiyo
dawa ya kumpa mtoto aache kutoa haja ya mbuzi,
halafu inanuka hiyo hatari”
Walijikuta wakiongelea hilo swala la dawa ya mtoto
sasa, walijadiliana kwa muda kisha ndio waliamua
kulala kwa muda huo.
Mapema kabisa leo, Dora alifanya vile vile kwa
kuandaa chai na mkate, kisha akaweka mezani na
kwenda kuendelea na shubhuli zingine, ila hadi
anarudi hakuna ambacho kilikuwa kimeliwa wala
nini yani kila kitu kilikuwa vile vile hadi muda
ambao yeye na Mariam walikaa na kunywa chai,
yani bado Dora alikuwa akijiuliza sana kuwa ni kitu
gani kinafanyika mule ndani? Mbona akiweka
chakula hakiliwi kama ambavyo wanakuta chakula
kilichotengwa na Mariam? Hapo hakuelewa
kwakweli.
Basi alifanya kazi zake na muda huu alikuwa
amekaa na dada yake Mariam na kuanza kuongea,
“Badae ndio nitaenda kuchuma ile dawa”
“Aaaah tena umenikumbusha, jioni napika pilau.
Haya kalete vitunguu swaumu umenye na utwange”
“Kheeee dada sio tumenye?”
“Sasa vitunguu tu navyo tumenye wote jamani!!
Kheeee Dora upoje wewe, kutaka kushindana na
mama mwenye nyumba!”
Hapo Dora hakuongea zaidi, basi akenda kuleta vile
vitunguu na kumenya huku Mariam akimwambia,
“Tena andaa kila kitu unachojua kinapaswa kupikwa
kwenye pilau, yani mimi nataka nikianza kupika basi
nipike moja kwa moja, kusiwe na kingine cha
kufata. Niwekee kabisa”
Basi Dora alifanya kazi ya kuchambua kila kitu na
kumuwekea jikoni Mariam ili akianza kupika kila
kitu kiwe tayari,
“Hivi na ile nyama imeiva eeeh Dora?”
“Ndio dada, nimeshaiepua”
“Sawa umefanya vizuri mdogo wangu ila msubirie
shemeji yako arudi ndio uende huko porini kuchuma
hiyo dawa”
Dora aliitikia pale na kuendelea na mambo mengine
pale.
Kweli Juma aliwahi kurudi na alipofika tu, Dora
alijiandaa kwaajili ya kwenda kuchuma dawa
kwahiyo pale alimuacha Mariam na mume wake.
Dora alienda kwenye pori ambalo halikuwa mbali
sana na pale kuangalia ile dawa ya kwao ambayo
huwa wanawapa watoto wadogo ila akiwa kule
alijiuliza sana,
“Mbona yule mtoto anaonekana mkubwa ila
ananyweshwa maziwa tu! Yule mtoto alitakiwa
kupata na vyakula vingine, kwanini anapewa maziwa
tupu? Nitamuuliza yule dada leo”
Basi akatafuta tafuta ile dawa na kuiona, hivyo basi
akaichuma ya kutosha tu na kuanza kurudi zake
nyumbani kwao.
Akiwa njiani kurudi kuna mdada alimuita Dora,
“Dora, Dora”
Dora aligeuka na kumuangalia aliyemuita, ila sura ya
yule mdada ilikuwa ni ngeni kabisa machoni
mwake, hata alishangaa imekuwaje yule mdada
kumfahamu yeye, ila yule mdada alitabasamu na
kumsogelea Dora kisha alimsalimia,
“Za siku Dora”
Yani Dora alikuwa akimjibu kinyonge maana
hakumkumbuka kabisa,
“Mbona unajibu kinyonge hivyo?”
“Unajua sikukumbuki kabisa, samahani. Kwani wewe
nani? Mimi na wewe tunafahamiana vipi?”
“Najua ni zamani sana, kunikumbuka itakuwa shida.
Ila Dora hubadiliki kabisa wewe, sura yako ipo vile
vile jamani. Vipi hayo majani unayapeleka wapi?”
“Ni dawa, nampelekea mtoto wa dada yangu”
“Kafanyaje kwani?”
“Aaaah ni dawa tu ya kumsaidia tumbo”
“Hivi unamjua vizuri mtoto unayemlea Dora?”
“Kumjua kivipi? Na wewe umenijuaje?”
“Mimi nakujua, na huyo mtoto unayemlea namjua
pia, nakuonea huruma sana”
“Jionee huruma na wewe, mimi nipo kazini sijui
mwenzangu unataka nini?”
“Ni bora nibaki sina kazi kuliko kufanya hiyo kazi
unayoifanya wewe, mama mwenye nyumba ni mvivu
haijapata kutokea, katoto kajabu hakuna mfano
halafu wewe umetulia tu”
Dora aliamua kuondoka zake, kwani kitu ambacho
alikuwa hakipendi kwneye maisha yake ni kuongea
mambo ya wengine, alikuwa anaona ni vyema
awaambie wahusika lakini sio kuongea na
yasiyomuhusu.
Dora alifika na kukuta chakula kinanukia hatari, yani
kile chakula kilikuwa kinavutia sana, wakakipakua na
kuweka mezani kwaajili ya kula, hapo Mariam
aliandaa na kachumbari nzuri kabisa ila Juma
akasema,
“Jamani, bila pilipili kweli! Chakula kitamu hivi
kikose pilipili! Ngoja nikachukue pilipili kwanza tuje
kula”
Basi Juma alienda kununua pilipili wakati huo
Mariam na Dora waliandaa chakula mezani, kisha
Dora alienda kuweka ile dawa vizuri halafu Mariam
alienda kuoga kwanza.
Muda kidogo Juma aliwaita maana alikuwa
amesharudi, basi Mariam na Dora walifika,
“Khaaaa jamani, mmeshindwa kunisubiri kweli
nimeenda kuchukua pilipili tu hapo”
“Kwani vipi?”
“Vipi nini? Huoni hapo mezani mlichokifanya”
Mariama aliangalia vizuri na kukuta chakula chote
cha mezani kimeliwa, ile kachumbari pia imeliwa,
“Khaaaa jamani, mambo gani haya?”
“Haya mambo ni ya ajabu sana jamani, kwahiyo na
leo chakula kimeliwa?”
Walijikuta wakijadiliana bila kupata jibu, na kwenye
sufuria kilibaki chakula kidogo tu, ikabidi
wakakichukue kile wale, wapike na chai wanywe
pamoja na mkate huku wakilalamika mwanzo
mwisho kwa hiko kilichotokea.
Yani siku hii hadi wanaenda kulala walikuwa
wakilalamika tu hakuna mfano yani, kila mmoja
alikuwa akilalamika kivyake.
Asubuhi na mapema, Juma aliondoka zake basi
Dora alimuamsha Mariam kisha walisaidiana kumpa
yule mtoto ile dawa ambapo alikunywa tu vizuri.
Ila baada ya kunywa ile dawa Dora alimuuliza
Mariam,
“Hivi dada, ni nani anayeweza kuwa anatufanyia
ujinga wa kula chakula humu ndani?”
“Hata sijui kwakweli”
Basi Dora akafikiria kitu na kumwambia Mariam,
“Dada, leo naomba ukapike chai halafu tuitenge
mezani, ili tuone huyo anayekula ni nani?”
“Kwanini nipike mimi?”
“Anayekula anaonekana anapenda kula chakula
unachopika wewe”
“Haya tutamjuaje sasa?”
“Tutaweka sumu ya panya kwenye hiko chakula,
halafu tutatulia tuone matokeo yake”
“Kwahiyo tutagunduaje huyo anayekula?”
“Sababu atakufa akila”
Mara mtoto alikohoa kidogo na kufanya wote
wageuke kumuangalia, kisha yule mtoto
akawaambia,
“Hata msijisumbue kuweka sumu ya panya maana
anayekula chakula ni mimi, napenda sana kula
chakula anachopika mama yangu”
Mariam na Dora walijikuta wameganda kama vile
wamechomwa sindano za kuwagandisha yani
hawawezi kwenda mbele wala kurudi nyuma.
 
MTOTO WA MAAJABU: 7
Mariam na Dora walijikuta wameganda kama vile
wamechomwa sindano za kuwagandisha yani
hawawezi kwenda mbele wala kurudi nyuma.
Tukio hili lilikuwa la ajabu sana kwa Dora na
lilimfanya aogope sana, cha kushangaza
walipokimbilia chumbani waliweza ila kwenda nje
ilishindikana, kwahiyo kila mmoja alikuwa chumbani
kwake kwa muda huu, Dora aliwaza sana,
“Hivi ni nini hiki? Kazi zote zipo hivi au ni hii hii
jamani! Mbona hii nyumba imeanza kunitisha?
Nitaweza kweli kuendeles kuishi hapa? Natakiwa
kufanya maamuzi kwakweli”
Akajikuta akikumbuka na maneno ya yule mdada
aliyekutana nae njiani hivyo akaogopa sana na
kuona kuwa hapo mahali hapafai kabisa ila mwisho
wa siku alilala tu mule chumbani.
Juma alirudi na kukuta kimya kabisa, alijiuliza mno
kuwa wameenda wapi? Ila akahisi tu lazima
wamelala ila alishangaa kuona ni mapema mno!
Akaamua kumuita Dora maana alikuwa amefika na
mboga ambayo alitaka waichemshe kabisa,
“Dora”
Dora akatoka chumbani ila kitu cha kwanza kabla ya
salamu alimwambia Juma,
“Shemeji, hii nyumba imenishinda, sidhani kama
naweza kuendelea kuishi hapa”
“Kwanini?”
“Mtoto wako anaongea shemeji”
“Khaaaa hivi una kichaa au ni kitu gani wewe? Sasa
ulitaka mtoto wangu awe bubu au ni kitu gani?”
“Kwahiyo shemeji ni kawaida hiyo?”
“Ndio ni kawaida, mtoto wangu lazima aongee
maana kazaliwa mzima kabisa”
“Na kula chakula chote je?”
“Kula chakula chote kivipi?”
“Mtu ambaye anakula chakula kila dada akitenga
mezani ni mtoto wako”
“Unajua wakati mwingine ukiwa unaongea unatakiwa
uttambue kuwa unaongea na nani na unaongea nae
kuhusu nini. Njoo uchukue hii mboga”
“Kiukweli shemeji mimi siwezi kuendelea kuishi
hapa, naondoka mimi. Muite dada tu”
Dora alienda ndani kupakia nguo zake maana aliona
watu wenyewe kwenye ile nyumba wanajifanya kama
hawaelewi vile.
Juma alimfata mke wake ambaye alimuhadithia kitu
kile kile cha mtoto kuongea na kula chote, kisha
Juma alimuuliza mke wake,
“Hivi unaona hiko kitu kina maana yoyote?”
“Sijui ila ni mtoto mwenyewe ndio kasema”
Kidogo Dora akawaita, walipotoka akawaambia,
“Jamani mimi naondoka, kwaherini”
“Kheeee msahahara wako je?”
“Dada, sitaki mshahara wala nini”
Juma akatikisa kichwa na kisha akaingiza mkono
mfukoni kwake na kutoa elfu thelathini akamkabidhi
Dora na kumwambia,
“Chukua hiyo, najua hujamaliza mwezi ila chukua
hiyo hela”
Dora alishukuru na kuchukua kisha akaondoka zake
yani hakutaka hata wamsindikize wala nini, kwahiyo
ndani alibaki Juma na Mariam ambapo Mariam na
yeye alimwambia mumewe,
“Na mimi naondoka”
“Sasa uondoke uende wapi?”
“Naenda kwetu”
“Na mtoto unamuacha na nani?”
“Na wewe baba yake”
“Hebu acha uchizi wako Mariam, hapa huendi
popote tutabaki wote kulea mtoto”
“Unadhani nipo tayari kubaki mwenyewe na huyu
mtoto!!”
“Ngoja, usipaniki”
Juma akachukua simu yake na kumpigia mama
yake kumuomba mdada wa kazi,
“Mama naomba utusaidie, unajua wazi kuwa mke
wangu hawezi peke yake halafu na mimi natakiwa
kwenye kazi zangu”
“Nimlete msichana wa kazi kwa huyo mtoto
anayesonya?”
“Aaah mama, usiseme hivyo jamani! Nisikilize
mtoto wako”
“Kesho, nitamuagiza mamako mdogo akuletee
mdada wake maana na yeye alisema kuwa hataki
tena msichana wa kazi”
“Dah!! Utakuwa umenisaidia sana mama”
Juma alifurahi sana kuongea vile na mama yake
kwahiyo alimpa mke wake ujumbe huo wa kuhusu
msichana wa kazi atakayeletwa.
Siku hii ni Juma mwenyewe ndio alipika na
wakapata kula na kulala ila kiukweli Mariam alikuwa
na mawazo sana na hata hakupenda kabisa mambo
haya yanayoendelea wala nini.
Kulipokucha, Mariam alimgomea Juma kuondoka
hadi hao ndugu zake wafike na kweli kwenye mida
ya saa nne asubuhi hivi, walifika ndugu wa Juma
yani mamamdogo wa Juma na huyo msichana wa
kazi, basi waliwasalimia pale huku mamamdogo wa
Juma akiwapa hongera kwa kupata mtoto,
“Hongereni sana, hebu mleteni mtoto nimshike
kidogo”
Basi Juma akampatia mamake mdogo mtoto huku
akitabasamu, yule mamake mdogo alimshika mtoto
na kumuangalia huku akisema,
“Tuseme ndio sijaja siku nyingi mpaka mtoto
amekuwa mkubwa jamani khaaa mimi mbaya loh!!
Ila hongereni sana, mmepata katoto kazuri hadi
raha, mmekapa jina gani?”
Mariam na Juma wakaangaliana kwani kiukweli
mtoto huyu hakuwa na jina, basi mama mdogo
akauliza tena,
“Kwani anaitwa nani mtoto”
“Aaaah mamdogo bado mtoto hajapewa jina”
“Jamani acheni masikhara, kinachowashinda kumpa
jina mtoto ni kitu gani? Ndio mnatafuta majina ya
kizungu? Si mmuite tu majina yetu ya Kiswahili?
Mnaweza hata kumpa jina langu la Nasra”
Mariam akamuangalia yule mama na kumwambia,
“Hebu muite hilo jina uone kama litaendana nae”
Juma akaingilia kati kwani alihisi tu kitakachotokea,
akamwambia mamake mdogo,
“Mama, mwanangu hawezi kuitwa Nasra lipo jina
lake makini kabisa, subiri tu utalisikia”
“Mmmmh jina gani hilo? Kwani Nasra sio jina?”
“Ni jina mamdogo ila huyu ana jina lake, hatupendi
kulitaja kwa watu kwasasa ila muda ukifika
utalisikia tu”
“Mmmmh makubwa, haya jamani huyu nimekuja
nae ndio mdada wa kazi ambaye mama yako Juma
kaniagizia, huyu dada anaitwa Lulu”
“Aaaah Lulu, karibu sana”
“Asante”
“Jamani ila mimi sikai sana maana si unajua tena
biashara zangu, alivyoniambia nikasema ngoja
niende kuwaona pia, kwahiyo mimi naondoka muda
sio mrefu”
Na kweli baada ya muda mfupi tu huyu mamdogo
akawaaga na kuondoka zake.
Mariam kama kawaida alianza kumuelekeza huyu
Lulu majukumu ya hapo nyumbani kwake,
alimuonyesha nyumba nzima ilivyo na kazi za
kufanya,
“Umeelewa kazi za humu?”
“Nimeelewa ndio, hizo kazi ni kila siku?”
“Ndio, kwani vyombo ni vya kuosha siku moja
moja? Hizi kazi ni kila siku”
Basi na hapo akampa kazi ya kupika chakula cha
siku hiyo, kwahiyo Lulu alipika na alivyomaliza
kupika waliandaa na kuweza kula, wakati wanakula
mtoto alilia ndipo Mariam alipomwambia Lulu,
“Mtoto yule chakula chake maziwa, kamtengenezee,
ngoja nikuelekeze ukamtengenezee”
Juma akainuka akasema,
“Ngoja nikamtengenezee mwenyewe”
Basi Juma alienda kumtengenezea mtoto wao
maziwa na kumpatia wakati wenyewe wakiendelea
kula ila Lulu alimwambia Mariam,
“Ila dada sio vizuri, mkianza kula pamoja halafu
mumeo akainuka kama hivyo unatakiwa kumsubiri
ili muendelee kula pamoja”
“Kheee wewe, kwahiyo njaa nayo huwa inasubiri au
ni nini unaongea? Haya mambo ya humu ndani
yaache kama yalivyo, yatakushinda ukianza
kuyapekenyua”
“Sawa dada, yameisha”
Basi walimalizia kula pale na kumuachia tu Juma
chakula chake ambapo aliendelea kula baada ya
kumaliza kumlisha mtoto wao.
Leo mapema kabisa, Juma aliondoka zake kwenda
kwenye shughuli zake ukizingatia jana yake
hakwenda popote pale, kwahiyo alibaki Mariam na
Lulu ambapo Mariam alipoamka alimfata Lulu na
kuanza kumwambia,
“Ukiamka asubuhi, cha kwanza kabisa unatakiwa
kubandika chai maana mimi huwa naamka na njaa
sana”
“Aaaah sawa dada”
Umeshachota maji?”
“Hapana, bado sijachota dada”
“Mmmmh mmh!”
Mariam alimuona Lulu ni mzembe zaidi ya Dora
maana Dora ingawa alikuwa anabishana ila alikuwa
sio mzembe kama Lulu.
Basi Mariam alikaa sebleni ambapo mtoto wake
alianza kulia njaa, akamuita Lulu,
“Njoo nikuelekeze umkorogee maziwa umpe”
Lulu alienda na kuelekezwa vile namna ya
kumkorogea huyu mtoto maziwa, alishangaa sana,
“Yani tunakoroga maziwa ndani ya maziwa?”
“Usishangae, ndio chakula nilichoamua kumpa
mtoto wangu”
Basi Lulu alienda kukoroga na kumnywesha yule
mtoto ambapo alikunywa yote aliyokorogewa, kisha
Mariam akamwambia Lulu,
“Inabidi uanze kupika chakula cha mchana tule
mapema maana hatujanywa chai”
“Ila dada bado namalizia kufagia nje”
“Acha, utamalizia badae. Kapike kwanza”
Lulu ilibidi aende kupika na baada ya kupika
walikula halafu ndio akaenda kumalizia kazi zake za
nje ila kiukweli alikuwa akichukia sana.
Jioni, Juma alirudi na mboga ambapo Mariam
alimuita Lulu aikatekate na kuibandika, basi Lulu
alienda kuandaa ile mboga vizuri tu huku Mariam
akiongea na Juma,
“Vipi umeshindaje na huyu mdada?”
“Vizuri tu”
“Ila ndio usiwe unamuachia kazi zote mke wangu”
“Kheeee analipwa mshahara, asiachiwe kazi zote
yeye kama nani?”
“Tutapoteza wasichana wa kazi sijui tutapata wapi
mwingine?”
“Wapo watu wengi tu wanatafuta kazi, akiondoka
huyu mmoja atakuja mwingine, sio kazi sana
kumpata msichana wa kazi si unaona tukisema tu
tunaletewa”
“Mmmmh kwa mtindo huu hata wanaotuletea
watachoka nakwambia”
Juma aliamua kuingia ndani huku Mariam akimfata
Lulu na kumwambia kuwa aandae chakula cha
usiku.
“Ukimaliza hapa, andaa chakula cha usiku Lulu”
“Sawa dada”
Chkula kilipokuwa tayari, wote walikaa na kuanza
kula huku wakiongea mambo mbalimbali na baada
ya chakula walianza maongezi mbalimbali ambapo
Lulu akawasimulia kitu,
“Nakumbuka bibi yangu aliwahi kunisimulia kuwa
kijijini kwao alizaliwa mtoto wa ajabu, maana
kuzaliwa tu akaanza kuongea”
Hapo Mariam alimkatisha Lulu kwa kumwambia,
“Humu ndani huwa hatusimuliani stori za kutisha,
kwasasa ni muda wa kulala”
Ukweli ni kuwa sio stori za kutisha ila tu aliogopa
pale mtoto wake angejibu kwahiyo aliamua
kumkatisha Lulu kwa namna hiyo.
Na kweli kwa muda huo, wote walienda zao kulala.
Leo mapema kabisa, Lulu aliandaa chai kama
ambavyo alipewa maagizo na mama mwenye
nyumba, kisha baada ya hapo ndio alianza kufanya
kazi zingine, na kweli Mariam alifurahi sana na
kwenda kunywa chai huku akifurahia ila badae Lulu
nae alienda kunywa chai ila Mariam akamwambia,
“Lulu ukimaliza hapo kunywa chai uende chumbani
kwangu kusafisha”
Lulu aliitikia tu ila hakupenda kabisa, na kweli
alipomaliza alienda kusafisha mule chumbani kwa
Mariam na baaada ya hapo akaitwa kwaajili ya
kuandaa chakula cha mtoto yani Lulu alikuwa
akichukia sana na siku zote alikuwa akifanya tu zile
kazi kimya kimya ila alijisemea kuwa kuna siku
ataamua kuongea tu.
Siku hii baada ya Lulu kumaliza kazi zake aliamua
kuongea na Mariam kwani aliona zile kazi anapewa
kama kuonewa hivi,
“Ila dada, mambo mengine ungekuwa unafanya
mwenyewe bhana”
“Unamaanisha nini?”
“Dada jamani, kweli wewe uamke uje kunywa chai
halafu mimi nikakutandikie kitanda na kusafisha
chumba ambacho unalala wewe na mumeo, unaona
hiyo ni sawa kabisa?”
“Unaongelea nini kwani?”
“Nasema kuwa kazi zingine uwe unafanya
mwenyewe, ni kweli mimi ni msichana wa kazi ila
kuna wakati nachoka. Na mimi ni binadamu, sio
mashine mimi, kazi zingine fanya mwenyewe”
“Kheeee usinisumbue, kama umechoka kazi
unaweza kwenda, ni wapi msichana wa kazi
anaambiwa kulipwa hela nzuri kama hapa? Mambo
ya mimi kutandika mwenyewe kitanda changu ni
pale nitakapojisikia lakini sio lazima kuwa kila siku
ninapoamka nitandike kitanda changu wakati wewe
msichana wa kazi upo! Haiwezekani hiyo”
“Mmmmh dada!!”
“Ndio hivyo, na ukimaliza kupumzika hapo kuna
nguo za kufua pale chumbani, utazichukua na
kwenda kuzifua”
“Duh!! Sijapata kuyona haya!!”
“Ndio uone sasa”
Lulu aliinuka na kwenda kuchukua hizo nguo na
kuzifua.
Ila leo usiku Lulu aliamua kuongea na Juma maana
aliona kamavile huyu Mariam hamuelewi, basi
aliongea nae,
“Shemeji, ni kweli nina shida na kazi, ni kweli
nimetafuta kazi hata nilipoambiwa kuwa naletwa
huku nilifurahi sana kwani ni kweli nina uhitaji wa
kazi sana. Ila shemeji kuna kazi zingine dada
angekuwa anazifanya mwenyewe”
“Kama kazi gani?”
“Mimi sio wa kutandika kitanda chenu shemeji,
mimi sio wa kusafisha chumba chenu shemeji. Bora
nifanye kazi zote za huku ila hizo za chumbani basi
mkeo angekuwa anafanya mwenyewe”
“Sawa nimekusikia”
Juma alipoenda kulala alimsema mke wake,
“Unajua Mariam nilikuwa najua tu wewe ni
msumbufu kwenye kazi za nje, hata kutandika
kitanda kweli kukushinde mke wangu?”
“Aaaaah na wewe usinitibue, kile kisichana ndio
kimekwambia ujinga sio? Yani visichana vingine vya
ajabu kweli, kufatilia maisha ya watu tu. Hivi
nikiondoka na kukuacha na kile kisichana
utajisikiaje?”
“Kwani mimi nimesema uondoke jamani Mariam?
Ila nimesema ujirekesbishe”
“Haya, mfano naumwa unadhani huko chumbani
atasafisha nani? Hiko kitanda atatandika nani?”
“Kuumwa ni swala lingine Mariam, hata mimi
nafanya kazi hizo lakini sio kumpa mtu ambaye
hahusiki, nishakwambia mke wangu, tutamfanya
huyu dada akimbie hapa nyumbani kwakweli”
“Akikimbia yeye tutapata mdada mwingine”
“Na hilo ndio tatizo lako, haya siongei sana ila
akikimbia usinisumbue kuwa nisiende kazini”
Mariam hakumjibu mume wake kwani kwa wakati
huo alishachukia na akaanza kuwaza mambo
mbalimbali ya kufanya ili na yeye aweze kupakimbia
hapo nyumbani kwake.
Kulipokucha Mariam alishtuka na kuona mtoto wao
kalala pembeni yake, yani alichukia sana, ambacho
hapendi Mariam ni kusogelewa na huyu mtoto yani
alikuwa hapendi kabisa kwahiyo siku hiyo alijikuta
amechukia sana.
Basi alipoondoka Juma, Mariam nae alijiandaa na
baadhi ya nguo zake akabeba kwenye rambo na
kumwambia Lulu kuwa anaenda kupeleka nguo kwa
fundi,
“Naenda hapo kwa fundi, nataka akaniwekee kiraka
kidogo kwenye nguo zangu”
“Sawa dada”
Kwahiyo Mariam alimuacha pale Lulu na mtoto na
kuondoka zake, akiwa njiani alijisemea,
“Ningemuaga yule mwanaume angekataa, ila
kwasasa naondoka zangu, siwezi yani siwezi
kuendelea kuishi na yule mtoto hata kama
nimemzaa mwenyewe ila siwezi kuishi nae
kwakweli”
Basi alienda hadi stendi ambapo hakukaa chini
kwani aliogopa kusinzia kama siku ile, moja kwa
moja alipanda gari ya kumpeleka nyumbani kwao.
Na kweli aliingia kwenye ile gari na hakulala kabisa,
aliwashuhudia abiria wote waliokuwa wakipanda na
kushuka kwenye lile gari.
Alifika hadi kwao na kushuka, alitembea huku
akiangalia mazingira ya nyumbani kwao hadi
kwenye nyumba yao na kugonga, kisha
akafunguliwa mlango ila aliyemfungulia mlango
alimshangaza sana kwani alikuwa ni Lulu.
 
MTOTO WA MAAJABU: 7
Mariam na Dora walijikuta wameganda kama vile
wamechomwa sindano za kuwagandisha yani
hawawezi kwenda mbele wala kurudi nyuma.
Tukio hili lilikuwa la ajabu sana kwa Dora na
lilimfanya aogope sana, cha kushangaza
walipokimbilia chumbani waliweza ila kwenda nje
ilishindikana, kwahiyo kila mmoja alikuwa chumbani
kwake kwa muda huu, Dora aliwaza sana,
“Hivi ni nini hiki? Kazi zote zipo hivi au ni hii hii
jamani! Mbona hii nyumba imeanza kunitisha?
Nitaweza kweli kuendeles kuishi hapa? Natakiwa
kufanya maamuzi kwakweli”
Akajikuta akikumbuka na maneno ya yule mdada
aliyekutana nae njiani hivyo akaogopa sana na
kuona kuwa hapo mahali hapafai kabisa ila mwisho
wa siku alilala tu mule chumbani.
Juma alirudi na kukuta kimya kabisa, alijiuliza mno
kuwa wameenda wapi? Ila akahisi tu lazima
wamelala ila alishangaa kuona ni mapema mno!
Akaamua kumuita Dora maana alikuwa amefika na
mboga ambayo alitaka waichemshe kabisa,
“Dora”
Dora akatoka chumbani ila kitu cha kwanza kabla ya
salamu alimwambia Juma,
“Shemeji, hii nyumba imenishinda, sidhani kama
naweza kuendelea kuishi hapa”
“Kwanini?”
“Mtoto wako anaongea shemeji”
“Khaaaa hivi una kichaa au ni kitu gani wewe? Sasa
ulitaka mtoto wangu awe bubu au ni kitu gani?”
“Kwahiyo shemeji ni kawaida hiyo?”
“Ndio ni kawaida, mtoto wangu lazima aongee
maana kazaliwa mzima kabisa”
“Na kula chakula chote je?”
“Kula chakula chote kivipi?”
“Mtu ambaye anakula chakula kila dada akitenga
mezani ni mtoto wako”
“Unajua wakati mwingine ukiwa unaongea unatakiwa
uttambue kuwa unaongea na nani na unaongea nae
kuhusu nini. Njoo uchukue hii mboga”
“Kiukweli shemeji mimi siwezi kuendelea kuishi
hapa, naondoka mimi. Muite dada tu”
Dora alienda ndani kupakia nguo zake maana aliona
watu wenyewe kwenye ile nyumba wanajifanya kama
hawaelewi vile.
Juma alimfata mke wake ambaye alimuhadithia kitu
kile kile cha mtoto kuongea na kula chote, kisha
Juma alimuuliza mke wake,
“Hivi unaona hiko kitu kina maana yoyote?”
“Sijui ila ni mtoto mwenyewe ndio kasema”
Kidogo Dora akawaita, walipotoka akawaambia,
“Jamani mimi naondoka, kwaherini”
“Kheeee msahahara wako je?”
“Dada, sitaki mshahara wala nini”
Juma akatikisa kichwa na kisha akaingiza mkono
mfukoni kwake na kutoa elfu thelathini akamkabidhi
Dora na kumwambia,
“Chukua hiyo, najua hujamaliza mwezi ila chukua
hiyo hela”
Dora alishukuru na kuchukua kisha akaondoka zake
yani hakutaka hata wamsindikize wala nini, kwahiyo
ndani alibaki Juma na Mariam ambapo Mariam na
yeye alimwambia mumewe,
“Na mimi naondoka”
“Sasa uondoke uende wapi?”
“Naenda kwetu”
“Na mtoto unamuacha na nani?”
“Na wewe baba yake”
“Hebu acha uchizi wako Mariam, hapa huendi
popote tutabaki wote kulea mtoto”
“Unadhani nipo tayari kubaki mwenyewe na huyu
mtoto!!”
“Ngoja, usipaniki”
Juma akachukua simu yake na kumpigia mama
yake kumuomba mdada wa kazi,
“Mama naomba utusaidie, unajua wazi kuwa mke
wangu hawezi peke yake halafu na mimi natakiwa
kwenye kazi zangu”
“Nimlete msichana wa kazi kwa huyo mtoto
anayesonya?”
“Aaah mama, usiseme hivyo jamani! Nisikilize
mtoto wako”
“Kesho, nitamuagiza mamako mdogo akuletee
mdada wake maana na yeye alisema kuwa hataki
tena msichana wa kazi”
“Dah!! Utakuwa umenisaidia sana mama”
Juma alifurahi sana kuongea vile na mama yake
kwahiyo alimpa mke wake ujumbe huo wa kuhusu
msichana wa kazi atakayeletwa.
Siku hii ni Juma mwenyewe ndio alipika na
wakapata kula na kulala ila kiukweli Mariam alikuwa
na mawazo sana na hata hakupenda kabisa mambo
haya yanayoendelea wala nini.
Kulipokucha, Mariam alimgomea Juma kuondoka
hadi hao ndugu zake wafike na kweli kwenye mida
ya saa nne asubuhi hivi, walifika ndugu wa Juma
yani mamamdogo wa Juma na huyo msichana wa
kazi, basi waliwasalimia pale huku mamamdogo wa
Juma akiwapa hongera kwa kupata mtoto,
“Hongereni sana, hebu mleteni mtoto nimshike
kidogo”
Basi Juma akampatia mamake mdogo mtoto huku
akitabasamu, yule mamake mdogo alimshika mtoto
na kumuangalia huku akisema,
“Tuseme ndio sijaja siku nyingi mpaka mtoto
amekuwa mkubwa jamani khaaa mimi mbaya loh!!
Ila hongereni sana, mmepata katoto kazuri hadi
raha, mmekapa jina gani?”
Mariam na Juma wakaangaliana kwani kiukweli
mtoto huyu hakuwa na jina, basi mama mdogo
akauliza tena,
“Kwani anaitwa nani mtoto”
“Aaaah mamdogo bado mtoto hajapewa jina”
“Jamani acheni masikhara, kinachowashinda kumpa
jina mtoto ni kitu gani? Ndio mnatafuta majina ya
kizungu? Si mmuite tu majina yetu ya Kiswahili?
Mnaweza hata kumpa jina langu la Nasra”
Mariam akamuangalia yule mama na kumwambia,
“Hebu muite hilo jina uone kama litaendana nae”
Juma akaingilia kati kwani alihisi tu kitakachotokea,
akamwambia mamake mdogo,
“Mama, mwanangu hawezi kuitwa Nasra lipo jina
lake makini kabisa, subiri tu utalisikia”
“Mmmmh jina gani hilo? Kwani Nasra sio jina?”
“Ni jina mamdogo ila huyu ana jina lake, hatupendi
kulitaja kwa watu kwasasa ila muda ukifika
utalisikia tu”
“Mmmmh makubwa, haya jamani huyu nimekuja
nae ndio mdada wa kazi ambaye mama yako Juma
kaniagizia, huyu dada anaitwa Lulu”
“Aaaah Lulu, karibu sana”
“Asante”
“Jamani ila mimi sikai sana maana si unajua tena
biashara zangu, alivyoniambia nikasema ngoja
niende kuwaona pia, kwahiyo mimi naondoka muda
sio mrefu”
Na kweli baada ya muda mfupi tu huyu mamdogo
akawaaga na kuondoka zake.
Mariam kama kawaida alianza kumuelekeza huyu
Lulu majukumu ya hapo nyumbani kwake,
alimuonyesha nyumba nzima ilivyo na kazi za
kufanya,
“Umeelewa kazi za humu?”
“Nimeelewa ndio, hizo kazi ni kila siku?”
“Ndio, kwani vyombo ni vya kuosha siku moja
moja? Hizi kazi ni kila siku”
Basi na hapo akampa kazi ya kupika chakula cha
siku hiyo, kwahiyo Lulu alipika na alivyomaliza
kupika waliandaa na kuweza kula, wakati wanakula
mtoto alilia ndipo Mariam alipomwambia Lulu,
“Mtoto yule chakula chake maziwa, kamtengenezee,
ngoja nikuelekeze ukamtengenezee”
Juma akainuka akasema,
“Ngoja nikamtengenezee mwenyewe”
Basi Juma alienda kumtengenezea mtoto wao
maziwa na kumpatia wakati wenyewe wakiendelea
kula ila Lulu alimwambia Mariam,
“Ila dada sio vizuri, mkianza kula pamoja halafu
mumeo akainuka kama hivyo unatakiwa kumsubiri
ili muendelee kula pamoja”
“Kheee wewe, kwahiyo njaa nayo huwa inasubiri au
ni nini unaongea? Haya mambo ya humu ndani
yaache kama yalivyo, yatakushinda ukianza
kuyapekenyua”
“Sawa dada, yameisha”
Basi walimalizia kula pale na kumuachia tu Juma
chakula chake ambapo aliendelea kula baada ya
kumaliza kumlisha mtoto wao.
Leo mapema kabisa, Juma aliondoka zake kwenda
kwenye shughuli zake ukizingatia jana yake
hakwenda popote pale, kwahiyo alibaki Mariam na
Lulu ambapo Mariam alipoamka alimfata Lulu na
kuanza kumwambia,
“Ukiamka asubuhi, cha kwanza kabisa unatakiwa
kubandika chai maana mimi huwa naamka na njaa
sana”
“Aaaah sawa dada”
Umeshachota maji?”
“Hapana, bado sijachota dada”
“Mmmmh mmh!”
Mariam alimuona Lulu ni mzembe zaidi ya Dora
maana Dora ingawa alikuwa anabishana ila alikuwa
sio mzembe kama Lulu.
Basi Mariam alikaa sebleni ambapo mtoto wake
alianza kulia njaa, akamuita Lulu,
“Njoo nikuelekeze umkorogee maziwa umpe”
Lulu alienda na kuelekezwa vile namna ya
kumkorogea huyu mtoto maziwa, alishangaa sana,
“Yani tunakoroga maziwa ndani ya maziwa?”
“Usishangae, ndio chakula nilichoamua kumpa
mtoto wangu”
Basi Lulu alienda kukoroga na kumnywesha yule
mtoto ambapo alikunywa yote aliyokorogewa, kisha
Mariam akamwambia Lulu,
“Inabidi uanze kupika chakula cha mchana tule
mapema maana hatujanywa chai”
“Ila dada bado namalizia kufagia nje”
“Acha, utamalizia badae. Kapike kwanza”
Lulu ilibidi aende kupika na baada ya kupika
walikula halafu ndio akaenda kumalizia kazi zake za
nje ila kiukweli alikuwa akichukia sana.
Jioni, Juma alirudi na mboga ambapo Mariam
alimuita Lulu aikatekate na kuibandika, basi Lulu
alienda kuandaa ile mboga vizuri tu huku Mariam
akiongea na Juma,
“Vipi umeshindaje na huyu mdada?”
“Vizuri tu”
“Ila ndio usiwe unamuachia kazi zote mke wangu”
“Kheeee analipwa mshahara, asiachiwe kazi zote
yeye kama nani?”
“Tutapoteza wasichana wa kazi sijui tutapata wapi
mwingine?”
“Wapo watu wengi tu wanatafuta kazi, akiondoka
huyu mmoja atakuja mwingine, sio kazi sana
kumpata msichana wa kazi si unaona tukisema tu
tunaletewa”
“Mmmmh kwa mtindo huu hata wanaotuletea
watachoka nakwambia”
Juma aliamua kuingia ndani huku Mariam akimfata
Lulu na kumwambia kuwa aandae chakula cha
usiku.
“Ukimaliza hapa, andaa chakula cha usiku Lulu”
“Sawa dada”
Chkula kilipokuwa tayari, wote walikaa na kuanza
kula huku wakiongea mambo mbalimbali na baada
ya chakula walianza maongezi mbalimbali ambapo
Lulu akawasimulia kitu,
“Nakumbuka bibi yangu aliwahi kunisimulia kuwa
kijijini kwao alizaliwa mtoto wa ajabu, maana
kuzaliwa tu akaanza kuongea”
Hapo Mariam alimkatisha Lulu kwa kumwambia,
“Humu ndani huwa hatusimuliani stori za kutisha,
kwasasa ni muda wa kulala”
Ukweli ni kuwa sio stori za kutisha ila tu aliogopa
pale mtoto wake angejibu kwahiyo aliamua
kumkatisha Lulu kwa namna hiyo.
Na kweli kwa muda huo, wote walienda zao kulala.
Leo mapema kabisa, Lulu aliandaa chai kama
ambavyo alipewa maagizo na mama mwenye
nyumba, kisha baada ya hapo ndio alianza kufanya
kazi zingine, na kweli Mariam alifurahi sana na
kwenda kunywa chai huku akifurahia ila badae Lulu
nae alienda kunywa chai ila Mariam akamwambia,
“Lulu ukimaliza hapo kunywa chai uende chumbani
kwangu kusafisha”
Lulu aliitikia tu ila hakupenda kabisa, na kweli
alipomaliza alienda kusafisha mule chumbani kwa
Mariam na baaada ya hapo akaitwa kwaajili ya
kuandaa chakula cha mtoto yani Lulu alikuwa
akichukia sana na siku zote alikuwa akifanya tu zile
kazi kimya kimya ila alijisemea kuwa kuna siku
ataamua kuongea tu.
Siku hii baada ya Lulu kumaliza kazi zake aliamua
kuongea na Mariam kwani aliona zile kazi anapewa
kama kuonewa hivi,
“Ila dada, mambo mengine ungekuwa unafanya
mwenyewe bhana”
“Unamaanisha nini?”
“Dada jamani, kweli wewe uamke uje kunywa chai
halafu mimi nikakutandikie kitanda na kusafisha
chumba ambacho unalala wewe na mumeo, unaona
hiyo ni sawa kabisa?”
“Unaongelea nini kwani?”
“Nasema kuwa kazi zingine uwe unafanya
mwenyewe, ni kweli mimi ni msichana wa kazi ila
kuna wakati nachoka. Na mimi ni binadamu, sio
mashine mimi, kazi zingine fanya mwenyewe”
“Kheeee usinisumbue, kama umechoka kazi
unaweza kwenda, ni wapi msichana wa kazi
anaambiwa kulipwa hela nzuri kama hapa? Mambo
ya mimi kutandika mwenyewe kitanda changu ni
pale nitakapojisikia lakini sio lazima kuwa kila siku
ninapoamka nitandike kitanda changu wakati wewe
msichana wa kazi upo! Haiwezekani hiyo”
“Mmmmh dada!!”
“Ndio hivyo, na ukimaliza kupumzika hapo kuna
nguo za kufua pale chumbani, utazichukua na
kwenda kuzifua”
“Duh!! Sijapata kuyona haya!!”
“Ndio uone sasa”
Lulu aliinuka na kwenda kuchukua hizo nguo na
kuzifua.
Ila leo usiku Lulu aliamua kuongea na Juma maana
aliona kamavile huyu Mariam hamuelewi, basi
aliongea nae,
“Shemeji, ni kweli nina shida na kazi, ni kweli
nimetafuta kazi hata nilipoambiwa kuwa naletwa
huku nilifurahi sana kwani ni kweli nina uhitaji wa
kazi sana. Ila shemeji kuna kazi zingine dada
angekuwa anazifanya mwenyewe”
“Kama kazi gani?”
“Mimi sio wa kutandika kitanda chenu shemeji,
mimi sio wa kusafisha chumba chenu shemeji. Bora
nifanye kazi zote za huku ila hizo za chumbani basi
mkeo angekuwa anafanya mwenyewe”
“Sawa nimekusikia”
Juma alipoenda kulala alimsema mke wake,
“Unajua Mariam nilikuwa najua tu wewe ni
msumbufu kwenye kazi za nje, hata kutandika
kitanda kweli kukushinde mke wangu?”
“Aaaaah na wewe usinitibue, kile kisichana ndio
kimekwambia ujinga sio? Yani visichana vingine vya
ajabu kweli, kufatilia maisha ya watu tu. Hivi
nikiondoka na kukuacha na kile kisichana
utajisikiaje?”
“Kwani mimi nimesema uondoke jamani Mariam?
Ila nimesema ujirekesbishe”
“Haya, mfano naumwa unadhani huko chumbani
atasafisha nani? Hiko kitanda atatandika nani?”
“Kuumwa ni swala lingine Mariam, hata mimi
nafanya kazi hizo lakini sio kumpa mtu ambaye
hahusiki, nishakwambia mke wangu, tutamfanya
huyu dada akimbie hapa nyumbani kwakweli”
“Akikimbia yeye tutapata mdada mwingine”
“Na hilo ndio tatizo lako, haya siongei sana ila
akikimbia usinisumbue kuwa nisiende kazini”
Mariam hakumjibu mume wake kwani kwa wakati
huo alishachukia na akaanza kuwaza mambo
mbalimbali ya kufanya ili na yeye aweze kupakimbia
hapo nyumbani kwake.
Kulipokucha Mariam alishtuka na kuona mtoto wao
kalala pembeni yake, yani alichukia sana, ambacho
hapendi Mariam ni kusogelewa na huyu mtoto yani
alikuwa hapendi kabisa kwahiyo siku hiyo alijikuta
amechukia sana.
Basi alipoondoka Juma, Mariam nae alijiandaa na
baadhi ya nguo zake akabeba kwenye rambo na
kumwambia Lulu kuwa anaenda kupeleka nguo kwa
fundi,
“Naenda hapo kwa fundi, nataka akaniwekee kiraka
kidogo kwenye nguo zangu”
“Sawa dada”
Kwahiyo Mariam alimuacha pale Lulu na mtoto na
kuondoka zake, akiwa njiani alijisemea,
“Ningemuaga yule mwanaume angekataa, ila
kwasasa naondoka zangu, siwezi yani siwezi
kuendelea kuishi na yule mtoto hata kama
nimemzaa mwenyewe ila siwezi kuishi nae
kwakweli”
Basi alienda hadi stendi ambapo hakukaa chini
kwani aliogopa kusinzia kama siku ile, moja kwa
moja alipanda gari ya kumpeleka nyumbani kwao.
Na kweli aliingia kwenye ile gari na hakulala kabisa,
aliwashuhudia abiria wote waliokuwa wakipanda na
kushuka kwenye lile gari.
Alifika hadi kwao na kushuka, alitembea huku
akiangalia mazingira ya nyumbani kwao hadi
kwenye nyumba yao na kugonga, kisha
akafunguliwa mlango ila aliyemfungulia mlango
alimshangaza sana kwani alikuwa ni Lulu.
 
MTOTO WA MAAJABU: 7
Mariam na Dora walijikuta wameganda kama vile
wamechomwa sindano za kuwagandisha yani
hawawezi kwenda mbele wala kurudi nyuma.
Tukio hili lilikuwa la ajabu sana kwa Dora na
lilimfanya aogope sana, cha kushangaza
walipokimbilia chumbani waliweza ila kwenda nje
ilishindikana, kwahiyo kila mmoja alikuwa chumbani
kwake kwa muda huu, Dora aliwaza sana,
“Hivi ni nini hiki? Kazi zote zipo hivi au ni hii hii
jamani! Mbona hii nyumba imeanza kunitisha?
Nitaweza kweli kuendeles kuishi hapa? Natakiwa
kufanya maamuzi kwakweli”
Akajikuta akikumbuka na maneno ya yule mdada
aliyekutana nae njiani hivyo akaogopa sana na
kuona kuwa hapo mahali hapafai kabisa ila mwisho
wa siku alilala tu mule chumbani.
Juma alirudi na kukuta kimya kabisa, alijiuliza mno
kuwa wameenda wapi? Ila akahisi tu lazima
wamelala ila alishangaa kuona ni mapema mno!
Akaamua kumuita Dora maana alikuwa amefika na
mboga ambayo alitaka waichemshe kabisa,
“Dora”
Dora akatoka chumbani ila kitu cha kwanza kabla ya
salamu alimwambia Juma,
“Shemeji, hii nyumba imenishinda, sidhani kama
naweza kuendelea kuishi hapa”
“Kwanini?”
“Mtoto wako anaongea shemeji”
“Khaaaa hivi una kichaa au ni kitu gani wewe? Sasa
ulitaka mtoto wangu awe bubu au ni kitu gani?”
“Kwahiyo shemeji ni kawaida hiyo?”
“Ndio ni kawaida, mtoto wangu lazima aongee
maana kazaliwa mzima kabisa”
“Na kula chakula chote je?”
“Kula chakula chote kivipi?”
“Mtu ambaye anakula chakula kila dada akitenga
mezani ni mtoto wako”
“Unajua wakati mwingine ukiwa unaongea unatakiwa
uttambue kuwa unaongea na nani na unaongea nae
kuhusu nini. Njoo uchukue hii mboga”
“Kiukweli shemeji mimi siwezi kuendelea kuishi
hapa, naondoka mimi. Muite dada tu”
Dora alienda ndani kupakia nguo zake maana aliona
watu wenyewe kwenye ile nyumba wanajifanya kama
hawaelewi vile.
Juma alimfata mke wake ambaye alimuhadithia kitu
kile kile cha mtoto kuongea na kula chote, kisha
Juma alimuuliza mke wake,
“Hivi unaona hiko kitu kina maana yoyote?”
“Sijui ila ni mtoto mwenyewe ndio kasema”
Kidogo Dora akawaita, walipotoka akawaambia,
“Jamani mimi naondoka, kwaherini”
“Kheeee msahahara wako je?”
“Dada, sitaki mshahara wala nini”
Juma akatikisa kichwa na kisha akaingiza mkono
mfukoni kwake na kutoa elfu thelathini akamkabidhi
Dora na kumwambia,
“Chukua hiyo, najua hujamaliza mwezi ila chukua
hiyo hela”
Dora alishukuru na kuchukua kisha akaondoka zake
yani hakutaka hata wamsindikize wala nini, kwahiyo
ndani alibaki Juma na Mariam ambapo Mariam na
yeye alimwambia mumewe,
“Na mimi naondoka”
“Sasa uondoke uende wapi?”
“Naenda kwetu”
“Na mtoto unamuacha na nani?”
“Na wewe baba yake”
“Hebu acha uchizi wako Mariam, hapa huendi
popote tutabaki wote kulea mtoto”
“Unadhani nipo tayari kubaki mwenyewe na huyu
mtoto!!”
“Ngoja, usipaniki”
Juma akachukua simu yake na kumpigia mama
yake kumuomba mdada wa kazi,
“Mama naomba utusaidie, unajua wazi kuwa mke
wangu hawezi peke yake halafu na mimi natakiwa
kwenye kazi zangu”
“Nimlete msichana wa kazi kwa huyo mtoto
anayesonya?”
“Aaah mama, usiseme hivyo jamani! Nisikilize
mtoto wako”
“Kesho, nitamuagiza mamako mdogo akuletee
mdada wake maana na yeye alisema kuwa hataki
tena msichana wa kazi”
“Dah!! Utakuwa umenisaidia sana mama”
Juma alifurahi sana kuongea vile na mama yake
kwahiyo alimpa mke wake ujumbe huo wa kuhusu
msichana wa kazi atakayeletwa.
Siku hii ni Juma mwenyewe ndio alipika na
wakapata kula na kulala ila kiukweli Mariam alikuwa
na mawazo sana na hata hakupenda kabisa mambo
haya yanayoendelea wala nini.
Kulipokucha, Mariam alimgomea Juma kuondoka
hadi hao ndugu zake wafike na kweli kwenye mida
ya saa nne asubuhi hivi, walifika ndugu wa Juma
yani mamamdogo wa Juma na huyo msichana wa
kazi, basi waliwasalimia pale huku mamamdogo wa
Juma akiwapa hongera kwa kupata mtoto,
“Hongereni sana, hebu mleteni mtoto nimshike
kidogo”
Basi Juma akampatia mamake mdogo mtoto huku
akitabasamu, yule mamake mdogo alimshika mtoto
na kumuangalia huku akisema,
“Tuseme ndio sijaja siku nyingi mpaka mtoto
amekuwa mkubwa jamani khaaa mimi mbaya loh!!
Ila hongereni sana, mmepata katoto kazuri hadi
raha, mmekapa jina gani?”
Mariam na Juma wakaangaliana kwani kiukweli
mtoto huyu hakuwa na jina, basi mama mdogo
akauliza tena,
“Kwani anaitwa nani mtoto”
“Aaaah mamdogo bado mtoto hajapewa jina”
“Jamani acheni masikhara, kinachowashinda kumpa
jina mtoto ni kitu gani? Ndio mnatafuta majina ya
kizungu? Si mmuite tu majina yetu ya Kiswahili?
Mnaweza hata kumpa jina langu la Nasra”
Mariam akamuangalia yule mama na kumwambia,
“Hebu muite hilo jina uone kama litaendana nae”
Juma akaingilia kati kwani alihisi tu kitakachotokea,
akamwambia mamake mdogo,
“Mama, mwanangu hawezi kuitwa Nasra lipo jina
lake makini kabisa, subiri tu utalisikia”
“Mmmmh jina gani hilo? Kwani Nasra sio jina?”
“Ni jina mamdogo ila huyu ana jina lake, hatupendi
kulitaja kwa watu kwasasa ila muda ukifika
utalisikia tu”
“Mmmmh makubwa, haya jamani huyu nimekuja
nae ndio mdada wa kazi ambaye mama yako Juma
kaniagizia, huyu dada anaitwa Lulu”
“Aaaah Lulu, karibu sana”
“Asante”
“Jamani ila mimi sikai sana maana si unajua tena
biashara zangu, alivyoniambia nikasema ngoja
niende kuwaona pia, kwahiyo mimi naondoka muda
sio mrefu”
Na kweli baada ya muda mfupi tu huyu mamdogo
akawaaga na kuondoka zake.
Mariam kama kawaida alianza kumuelekeza huyu
Lulu majukumu ya hapo nyumbani kwake,
alimuonyesha nyumba nzima ilivyo na kazi za
kufanya,
“Umeelewa kazi za humu?”
“Nimeelewa ndio, hizo kazi ni kila siku?”
“Ndio, kwani vyombo ni vya kuosha siku moja
moja? Hizi kazi ni kila siku”
Basi na hapo akampa kazi ya kupika chakula cha
siku hiyo, kwahiyo Lulu alipika na alivyomaliza
kupika waliandaa na kuweza kula, wakati wanakula
mtoto alilia ndipo Mariam alipomwambia Lulu,
“Mtoto yule chakula chake maziwa, kamtengenezee,
ngoja nikuelekeze ukamtengenezee”
Juma akainuka akasema,
“Ngoja nikamtengenezee mwenyewe”
Basi Juma alienda kumtengenezea mtoto wao
maziwa na kumpatia wakati wenyewe wakiendelea
kula ila Lulu alimwambia Mariam,
“Ila dada sio vizuri, mkianza kula pamoja halafu
mumeo akainuka kama hivyo unatakiwa kumsubiri
ili muendelee kula pamoja”
“Kheee wewe, kwahiyo njaa nayo huwa inasubiri au
ni nini unaongea? Haya mambo ya humu ndani
yaache kama yalivyo, yatakushinda ukianza
kuyapekenyua”
“Sawa dada, yameisha”
Basi walimalizia kula pale na kumuachia tu Juma
chakula chake ambapo aliendelea kula baada ya
kumaliza kumlisha mtoto wao.
Leo mapema kabisa, Juma aliondoka zake kwenda
kwenye shughuli zake ukizingatia jana yake
hakwenda popote pale, kwahiyo alibaki Mariam na
Lulu ambapo Mariam alipoamka alimfata Lulu na
kuanza kumwambia,
“Ukiamka asubuhi, cha kwanza kabisa unatakiwa
kubandika chai maana mimi huwa naamka na njaa
sana”
“Aaaah sawa dada”
Umeshachota maji?”
“Hapana, bado sijachota dada”
“Mmmmh mmh!”
Mariam alimuona Lulu ni mzembe zaidi ya Dora
maana Dora ingawa alikuwa anabishana ila alikuwa
sio mzembe kama Lulu.
Basi Mariam alikaa sebleni ambapo mtoto wake
alianza kulia njaa, akamuita Lulu,
“Njoo nikuelekeze umkorogee maziwa umpe”
Lulu alienda na kuelekezwa vile namna ya
kumkorogea huyu mtoto maziwa, alishangaa sana,
“Yani tunakoroga maziwa ndani ya maziwa?”
“Usishangae, ndio chakula nilichoamua kumpa
mtoto wangu”
Basi Lulu alienda kukoroga na kumnywesha yule
mtoto ambapo alikunywa yote aliyokorogewa, kisha
Mariam akamwambia Lulu,
“Inabidi uanze kupika chakula cha mchana tule
mapema maana hatujanywa chai”
“Ila dada bado namalizia kufagia nje”
“Acha, utamalizia badae. Kapike kwanza”
Lulu ilibidi aende kupika na baada ya kupika
walikula halafu ndio akaenda kumalizia kazi zake za
nje ila kiukweli alikuwa akichukia sana.
Jioni, Juma alirudi na mboga ambapo Mariam
alimuita Lulu aikatekate na kuibandika, basi Lulu
alienda kuandaa ile mboga vizuri tu huku Mariam
akiongea na Juma,
“Vipi umeshindaje na huyu mdada?”
“Vizuri tu”
“Ila ndio usiwe unamuachia kazi zote mke wangu”
“Kheeee analipwa mshahara, asiachiwe kazi zote
yeye kama nani?”
“Tutapoteza wasichana wa kazi sijui tutapata wapi
mwingine?”
“Wapo watu wengi tu wanatafuta kazi, akiondoka
huyu mmoja atakuja mwingine, sio kazi sana
kumpata msichana wa kazi si unaona tukisema tu
tunaletewa”
“Mmmmh kwa mtindo huu hata wanaotuletea
watachoka nakwambia”
Juma aliamua kuingia ndani huku Mariam akimfata
Lulu na kumwambia kuwa aandae chakula cha
usiku.
“Ukimaliza hapa, andaa chakula cha usiku Lulu”
“Sawa dada”
Chkula kilipokuwa tayari, wote walikaa na kuanza
kula huku wakiongea mambo mbalimbali na baada
ya chakula walianza maongezi mbalimbali ambapo
Lulu akawasimulia kitu,
“Nakumbuka bibi yangu aliwahi kunisimulia kuwa
kijijini kwao alizaliwa mtoto wa ajabu, maana
kuzaliwa tu akaanza kuongea”
Hapo Mariam alimkatisha Lulu kwa kumwambia,
“Humu ndani huwa hatusimuliani stori za kutisha,
kwasasa ni muda wa kulala”
Ukweli ni kuwa sio stori za kutisha ila tu aliogopa
pale mtoto wake angejibu kwahiyo aliamua
kumkatisha Lulu kwa namna hiyo.
Na kweli kwa muda huo, wote walienda zao kulala.
Leo mapema kabisa, Lulu aliandaa chai kama
ambavyo alipewa maagizo na mama mwenye
nyumba, kisha baada ya hapo ndio alianza kufanya
kazi zingine, na kweli Mariam alifurahi sana na
kwenda kunywa chai huku akifurahia ila badae Lulu
nae alienda kunywa chai ila Mariam akamwambia,
“Lulu ukimaliza hapo kunywa chai uende chumbani
kwangu kusafisha”
Lulu aliitikia tu ila hakupenda kabisa, na kweli
alipomaliza alienda kusafisha mule chumbani kwa
Mariam na baaada ya hapo akaitwa kwaajili ya
kuandaa chakula cha mtoto yani Lulu alikuwa
akichukia sana na siku zote alikuwa akifanya tu zile
kazi kimya kimya ila alijisemea kuwa kuna siku
ataamua kuongea tu.
Siku hii baada ya Lulu kumaliza kazi zake aliamua
kuongea na Mariam kwani aliona zile kazi anapewa
kama kuonewa hivi,
“Ila dada, mambo mengine ungekuwa unafanya
mwenyewe bhana”
“Unamaanisha nini?”
“Dada jamani, kweli wewe uamke uje kunywa chai
halafu mimi nikakutandikie kitanda na kusafisha
chumba ambacho unalala wewe na mumeo, unaona
hiyo ni sawa kabisa?”
“Unaongelea nini kwani?”
“Nasema kuwa kazi zingine uwe unafanya
mwenyewe, ni kweli mimi ni msichana wa kazi ila
kuna wakati nachoka. Na mimi ni binadamu, sio
mashine mimi, kazi zingine fanya mwenyewe”
“Kheeee usinisumbue, kama umechoka kazi
unaweza kwenda, ni wapi msichana wa kazi
anaambiwa kulipwa hela nzuri kama hapa? Mambo
ya mimi kutandika mwenyewe kitanda changu ni
pale nitakapojisikia lakini sio lazima kuwa kila siku
ninapoamka nitandike kitanda changu wakati wewe
msichana wa kazi upo! Haiwezekani hiyo”
“Mmmmh dada!!”
“Ndio hivyo, na ukimaliza kupumzika hapo kuna
nguo za kufua pale chumbani, utazichukua na
kwenda kuzifua”
“Duh!! Sijapata kuyona haya!!”
“Ndio uone sasa”
Lulu aliinuka na kwenda kuchukua hizo nguo na
kuzifua.
Ila leo usiku Lulu aliamua kuongea na Juma maana
aliona kamavile huyu Mariam hamuelewi, basi
aliongea nae,
“Shemeji, ni kweli nina shida na kazi, ni kweli
nimetafuta kazi hata nilipoambiwa kuwa naletwa
huku nilifurahi sana kwani ni kweli nina uhitaji wa
kazi sana. Ila shemeji kuna kazi zingine dada
angekuwa anazifanya mwenyewe”
“Kama kazi gani?”
“Mimi sio wa kutandika kitanda chenu shemeji,
mimi sio wa kusafisha chumba chenu shemeji. Bora
nifanye kazi zote za huku ila hizo za chumbani basi
mkeo angekuwa anafanya mwenyewe”
“Sawa nimekusikia”
Juma alipoenda kulala alimsema mke wake,
“Unajua Mariam nilikuwa najua tu wewe ni
msumbufu kwenye kazi za nje, hata kutandika
kitanda kweli kukushinde mke wangu?”
“Aaaaah na wewe usinitibue, kile kisichana ndio
kimekwambia ujinga sio? Yani visichana vingine vya
ajabu kweli, kufatilia maisha ya watu tu. Hivi
nikiondoka na kukuacha na kile kisichana
utajisikiaje?”
“Kwani mimi nimesema uondoke jamani Mariam?
Ila nimesema ujirekesbishe”
“Haya, mfano naumwa unadhani huko chumbani
atasafisha nani? Hiko kitanda atatandika nani?”
“Kuumwa ni swala lingine Mariam, hata mimi
nafanya kazi hizo lakini sio kumpa mtu ambaye
hahusiki, nishakwambia mke wangu, tutamfanya
huyu dada akimbie hapa nyumbani kwakweli”
“Akikimbia yeye tutapata mdada mwingine”
“Na hilo ndio tatizo lako, haya siongei sana ila
akikimbia usinisumbue kuwa nisiende kazini”
Mariam hakumjibu mume wake kwani kwa wakati
huo alishachukia na akaanza kuwaza mambo
mbalimbali ya kufanya ili na yeye aweze kupakimbia
hapo nyumbani kwake.
Kulipokucha Mariam alishtuka na kuona mtoto wao
kalala pembeni yake, yani alichukia sana, ambacho
hapendi Mariam ni kusogelewa na huyu mtoto yani
alikuwa hapendi kabisa kwahiyo siku hiyo alijikuta
amechukia sana.
Basi alipoondoka Juma, Mariam nae alijiandaa na
baadhi ya nguo zake akabeba kwenye rambo na
kumwambia Lulu kuwa anaenda kupeleka nguo kwa
fundi,
“Naenda hapo kwa fundi, nataka akaniwekee kiraka
kidogo kwenye nguo zangu”
“Sawa dada”
Kwahiyo Mariam alimuacha pale Lulu na mtoto na
kuondoka zake, akiwa njiani alijisemea,
“Ningemuaga yule mwanaume angekataa, ila
kwasasa naondoka zangu, siwezi yani siwezi
kuendelea kuishi na yule mtoto hata kama
nimemzaa mwenyewe ila siwezi kuishi nae
kwakweli”
Basi alienda hadi stendi ambapo hakukaa chini
kwani aliogopa kusinzia kama siku ile, moja kwa
moja alipanda gari ya kumpeleka nyumbani kwao.
Na kweli aliingia kwenye ile gari na hakulala kabisa,
aliwashuhudia abiria wote waliokuwa wakipanda na
kushuka kwenye lile gari.
Alifika hadi kwao na kushuka, alitembea huku
akiangalia mazingira ya nyumbani kwao hadi
kwenye nyumba yao na kugonga, kisha
akafunguliwa mlango ila aliyemfungulia mlango
alimshangaza sana kwani alikuwa ni Lulu.
 
MTOTO WA MAAJABU: 8

Alifika hadi kwao na kushuka, alitembea huku akiangalia mazingira ya nyumbani kwao hadi kwenye nyumba yao na kugonga, kisha akafunguliwa mlango ila aliyemfungulia mlango alimshangaza sana kwani alikuwa ni Lulu.
Yani Mariam ilikuwa bado kidogo akimbie ila Lulu alimdaka na kumuuliza,
“Kwani dada kuna nini?”
Mariam aliangalia vizuti yale mazingira, na Lulu alimshika mkono na kuingia ndani, ni kweli ilikuwa ni ndani kwake na sio nyumbani kwao wala nini, alijikuta akimuuliza Lulu kwa uhakika zaidi,
“Tupo wapi kwani hapa Lulu?”
“Si tupo nyumbani dada?”
“Nyumbani kivipi? Nyumbani kwangu?”
“Ndio, ni nyumbani kwako dada”
Mariam alikaa kimya yani hakuelewa kabisa aliona kamavile anaota basi moja kwa moja aliongoza hadi chumbani kwake na kwenda kulala yani hakujielewa kabisa.
Lulu alibaki tu kumshangaa ila aliamua tu kuendelea na kazi zake ambapo aliandaa chakula ila alipoenda kumuita Mariam aligoma kwenda kwahiyo ilibidi Lulu ale mwenyewe na bila kuelewa ni kitu gani kimempata bosi wake.

Muda huu Lulu alipigiwa simu na mama yake, kwahiyo alipokea na kuanza kuongea nayo ile simu, alimsalimia kwanza na kuanza kuongea habari za hapo,
“Vipi Lulu maisha ya hapo?”
“Si nilikwambia eeeh mama kuwa sipo tena kwa yule dada, amenileta kwa ndugu yake kuja kumsaidia kazi”
“Aaaah sawa, ila vipi maisha huko?”
“Jamani mama, huyu dada ni mvivu sijapata kuona mama yangu. Yani hakuna kazi anayofanya, zote nafanya mwenyewe”
“Kwani si anafanya kazi?”
“Hapana, yupo yeye na mumewe na mtoto ila mumewe ndio anafanya kazi, yeye huwa anashinda nyumbani ila ni mvivu mama balaa. Hebu fikiria hadi kitanda anacholala na mumewe nikatandike mimi kweli! Chumbani kwao nisafishe mimi jamani, na zaidi ya yote unajua nguo za ndani zake na mumewe nafua mimi!”
“Kheeee mbona makubwa, yani huyo sio uvivu tu bali atakuwa ni mchafu pia maana kusipokuwa na msichana wa kazi kwake inamaana hizo kazi hatozifanya?”
“Sijui mama, yani ni mvivu hatari”
“Ndiomana wanawake wengine wanaibiwaga waume zao!”
“Umeona mama eeeh! Sema kanikuta mtu mwenyewe sina tabia hiyo ila nilimwambia mume wake kuhusu swala la kutandika kitanda chao na kufagia ndani kwao kuwa mkewe ajitahidi awe anafanya mwenyewe”
“Alisemaje sasa?”
“Mmmh hata hakusema kitu, nadhani kazoea ila sikumwambia kuhusu mimi kufua nguo zao za ndani kwani najua bado hawezi kusema chochote anampenda sana mke wake ila mwanamke mwenyewe ni mvivu sana sijapata kuona jamani!”
Mara mlango ulifunguliwa, aliyeingia alikuwa ni Juma, hapo Lulu alishusha simu na kukata haraka haraka huku akimsalimia kwa uoga,
“Shikamoo shemeji!”
“Marahaba”
Juma hakusema neno zaidi ya kuitikia hiyo salamu tu, na moja kwa moja alienda chumbani kwake na kumkuta mke wake kajilaza, basi akamuamsha na kuanza kuongea nae,
“Hivi Mariam kweli kabisa hadi nguo zetu za ndani za kumpa msichana wa kazi afue jamani?”
“Kwani na zenyewe si nguo! Anafua kama anavyofua nguo zingine”
“Hivi Mariam mke wangu una nini? Hivi unajua nguo za ndani zilivyo? Mtu anaweza kukutendea jambo baya kwa kutumia nguo za ndani”
“Kama mtu akiamua kukutendea jambo baya anakutendea tu, iwe kwa nguo za ndani au la! Mambo mengine inategemea tu na moyo wa mtu, vipi kwani umemkuta Lulu ndio anazifua muda huu? Nimemuachia asubuhi kabisa ujue!”
“Hebu acha ujinga Mariam na acha kujipumbaza, unafanya ujinga tena ujinga haswaa, kinachokushinda kufua nguo a ndani ni nini? Kheri nguo zingine ila hadi za ndani jamani Mariam mbona ni mambo ya ajabu hayo lakini? Aaaarrgh sikujua yote haya, kama huwezi uwe unaziweka pembeni halafu mimi nikipumzika niwe nazifua mwenyewe”
“Ila ujue Juma nakushangaa sana, yani umefika hakuna cha salama, hakuna cha kuniuliza nimeshindaje, hakuna chochote umefika tu na swala lako la kufuliwa nguo za ndani utafikiri ni kitu cha ajabu sana kutokea kwenye maisha, mbona ni kawaida tu na wengi sana wanaishi maisha ya namna hii? Kuna wanawake ndani kwao hawashiki kitu chochote kile, kila kitu kinafanywa na mdada wa kazi, kwanini kunishangaa mimi sasa? Kwani nimefanya kitu ambacho hakijawahi kufanywa dunia nzima au ni kitu gani?”
“Hakuna siku ambayo nimewahi kukuelewesha ukaelewa Mariam hakuna kabisa, haya umeshindaje?”
“Sipo vizuri kiafya, kesho twende tu hospitali yani nina hali mbaya kwakweli”
“Sawa, tutaenda huko hospitali”
Kwahiyo ile mada ya uvivu tena ikaisha kwa namna hiyo maana hakuna kingine kilichoendelea kuzungumziwa zaidi ya Mariam kusema kuwa hana hali nzuri kumbe Mariam bado alikuwa na yale mawenge ya kwenda kwao na kujikuta akirudi hapo hapo.

Hata chakula cha usiku kwa siku hii Mariam hakula kama kawaida yake na kumfanya Juma ajue kuwa Mariam anaumwa kweli maana aliona amebadilika na wala hana furaha tena, basi akahisi huenda na swala la kumsema kwa uvivu limechangia hali ile na kumfanya Juma kuanza kumuomba msamaha kumbe Mariam alikuwa na swala lake lililomsumbua akili na kumtatiza zaidi ya hata swala la uvivu.
Usiku huu wakati wa kulala, Mariam alikataa kabisa kusogezewa mtoto wake karibu yake kwahiyo muda wote kama kawaida mtoto alibaki kulala na Juma tu hadi kulipokucha.
Basi Juma aliamua mwenyewe kwenda kuandaa kifungua kinywa ili wapate kwanza kifungua kinywa kabla ya kwenda hospitali na Mariam.
Ila hii chai Mariam alikunywa sana hadi alianza kuhisi usingizi ila bado alikazana kusisitiza swala la kwenda hospitali.
Baada ya kumaliza kunywa chai, Mariam aliinuka na kwenda kulala alisema kuwa atalala kidogo ila alivyoenda kulala ilibidi Juma pia ajiandae kwaajili ya kwenda kazini huku akimwambia Lulu,
“Iwapo akazidiwa basi utanipigia simu Lulu”
“Sawa shemeji, hakuna tatizo”
Basi Juma akamuachia Lulu namba zake halafu yeye aliondoka zake kwenda kwenye shughuli zake.

Kwenye mida ya saa nane mchana, Mariam alimka na kilichomuamsha ilikuwa ni njaa, basi alitoka chumbani kwake na kwenda sebleni ambapo alimkuta Lulu akiwa pale sebleni na kuanza kuongea nae kwa kumuuliza,
“Umeshapika Lulu?”
“Ndio dada”
“Nina njaa hapa hatari, weka hiko chakula tule maana nina njaa sana”
Basi Lulu aliandaa kile chakula na kuanza kula na Mariam huku akimwambia,
“Ila dada utanenepa sana ujue!”
“kwanini?”
“Yani asubuhi tu umekunywa chai na kwenda kulala yani tabia ya kula halafu kwenda kulala ndio tabia inayofanya wengi sana wanenepe hovyo”
“Sasa chakula kinavyolewesha vile haswa chai, kweli mtu unywe na uache kulala ufanye nini sasa?”
“Bora ufanye mambo mengine, halafu dada una eneo kubwa na zuri unaweza kuamua kulima lima huko na kupanda mboga”
“Khaaaa unaugua nini wewe, yani mimi nikalime lime na kupanda mboga kisa nini? Mume wangu kaishiwa hela au ni kitu gani? Mume wangu ana pesa, mambo mengine hajaamua tu, kama kununua gari ila mume wangu hela anayo, sina sababu mimi ya kuanza kulima lima wala nini”
“Kwani dada wote wanaolima lima waume zao hawana hela?”
“Ni umasikini tu huo, sasa mimi ukanishikishe jembe kweli!! Eti nalima mboga mboga, ili iweje sasa?”
“Ili usiwe unalala ukitoka kula tu, chakula kifanye kazi kwanza sio kukimbiziwa kwenda kulala”
“Nishazoea tayari, kwahiyo naona kama unanipigia kelele tu”
Lulu alinyamaza maana hakuona kama kuna kitu cha kumuelewesha huyu dada na akaelewa maana yeye huwa na kile anachokiamini yeye tu.
Kisha Mariam akamuuliza sasa,
“Halafu zile nguo nilikupa jana asubuhi, kuzifua jioni wakati shemeji yako anarudi ndio nini?”
“Nimezifua asubuhi dada”
“Haya huyo shemeji yako kajuaje kama nakupa ufue hadi nguo za ndani?”
Hapo Lulu alinyamaza kimya, kisha Mariam akamwmabia Lulu,
“Kama una mpango wa kuniroga mimi sababu eti nakupa nguo zangu za ndani, futa kabisa huo mpango wako maana mimi sirogeki mimi. Nione hivi hivi yani, mimi sirogeki na sitokuja kurogeka kamwe”
Lulu alimuangalia Mariam na kumuuliza,
“Kwani dada umenisikia muda gani kuwa nina mpango wa kukuroga?”
“Haijalishi nimekusikia au la ila mimi sirogeki kizembe namna hiyo”
Mtoto alianza kulia, ilibidi Lulu ainuke na kwenda kumpa maziwa maana hakuwa na mengi ya kuongea na Mariam.

Usiku wa leo, Mariam alifikiria jambo na jambo lenyewe ni swala la yeye kuondoka mahali hapo, yani alichokuwa akihisi yeye ni kuwa akiwa kwao kabisa atakuwa amefanikiwa kuondoka hapo ingawa hakujua ni kitu gani ambacho kimekuwa kikimrudisha hapo.
Basi muda huu alimpigia simu mama yake na kuongea nae,
“Mama, hivi mtu ukiwa unaenda mahali na kushangaa gafla umerudi kwako huwa ni kitu gani hicho?”
“Unaongelea nini Mariam?”
“Aaaah kuna tukio limenitokea hapa nyumbani kwangu”
“Tukio gani?”
“Mama sikia, nilipanga kuja huko nyumbani. Nimeenda hadi stendi na kupanda daladala halafu nimeshangaa badala ya kuja huko nyumbani eti nimerudi nyumbani kwangu”
“Mmmmh mmmh yani kama alivyonihadithia Zayana, mbona kuna maajabu huko kwako? Nimesahau tu kukuuliza, kwani huyo mtoto wako ana nini?”
“Hata mimi mwenyewe sielewi mama, huyu mtoto ana nini sijui”
“Zayana kaniambia kuwa huyo mtoto anatoa kinyesi kama cha mbuzi!”
“Ni kweli mama, halafu kuna muda anaongea”
“Duh!! Sasa Zayana aliniambia kuna siku mliamua kuondoka mkaenda hadi stendi na kujikuta mmerudi nyumbani sijui mlipitiwa na usingizi stendi”
“Ndio mama, kuna mambo ya ajabu sana. Haswa huyu mtoto mama huwa simuelewi kabisa. Ni kweli nimemzaa mwenyewe ila nashindwa kumuelewa, unajua huyu mtoto alimsonya mama yake Juma!”
“Kheeeee mbona makubwa”
“Ndio hivyo mama halafu Juma anaona kawaida tu, kila kinachotokea kwa huyu mtoto basi yeye anaona kawaida, sasa mimi nataka niondoke halafu huyu mtoto nimuachie yeye mwenyewe aendelee kumlea”
“Ila mwanangu mbona nahisi mtoto wako huyo atakuwa amerogwa! Maana unajua mtoto wako ni mzuri sana hata mambo unayoyasema ni yanashangaza sana, yani ni ngumu mtu kumjua kuwa ana mambo ya namna hiyo, mwanao ni mzuri sana mwanangu. Sasa sikia, njoo nyumbani ili tupange cha kufanya”
“Unadhani Juma anaweza kunipa ruhusa ya kuja? Hapa cha muhimu ni kutoroka tu, hebu niambie nitumie njia gani ili nisijikute nimerudi tena hapa nyumbani”
“Unajua hayo mambo ni kama mazingaombwe eeeh! Sikia Mariam, ukiondoka hapo kwako geuza viatu yani cha kulia vaa kushoto na cha kushoto vaa kulia maana naona hayo mambo kama mazingaombwe”
“Sawa mama yangu, ndiomana nimekupigia simu wewe ili unipe maujuzi”
Basi Mariam alifuirahi sana kupewa njia hii ya kufanya na mama yake, hapo sasa ndio aliweza kuendelea na mambo mengine huku mpango wake ukifanya kazi vilivyo kwenye akili yake.

Wakati wa kulala, Mariam alimsisitiza Juma kuwa anataka kesho waende hospitali maana hali yake sio nzuri ila alimwambia kuwa,
“Naomba tuondoke kabla hata ya kunywa chai”
“Duh!! Kwanini sasa?”
“Nimeamua, sitaki kulala kama leo maana huu ni ujinga, unapanga kwenda sehemu unakunywa chai unalala na huendi tena, sitaki huu ujinga kwakweli”
“Mmmmh!! Haya, nimekuelewa kwahiyo twende asubuhi kabisa?”
“Ndio, ni vizuri kwenda hospitali asubuhi”
Basi wakalala na kweli asubuhi na mapema, Juma alipoamka tu akamuamsha na mkewe kisha wakajiandaa na kumuachia mtoto Lulu, ila Juma hakuelewa kuwa mkewe alikuwa na mpango gani kwa siku hii ya leo.
Waliondoka pamoja hadi hospitali ambapo kabla ya kwenda kwa daktari, Juma alimuuliza kwanza mkewe,
“Hivi ni kitu gani kinachokuuma haswa?”
“Hata nikikwambia bado hutaelewa maana wewe si daktari”
“Ila mimi ni mume wako, napaswa kujua maana mimi na wewe ni mwili mmoja”
“Tungekuwa ni mwili mmoja hivyo basi kitu kinachonisumbua ungekuwa umeshakijua maana si mwili ni mmoja? Ila huo ni msemo tu, kila mtu na mwili wake Juma. Nikienda kwa daktari na kumueleza ndio nitakwambia ninachoumwa”
“Kwahiyo kwa daktari hatuendi wote?”
“Kwa leo hapana, itabidi unisubirie tu”
Yani kwa siku hii Mariam alikuwa ameshakamilisha vizuri kabisa mipango yake, wakati ndio anataka kwenda kwa daktari Juma alimuangalia miguuni na kumshangaa,
“Weeee Mariam mbona umegeuza viatu?”
Mariam alimuangalia mumewe bila ya kumjibu kisha akainuka na kwenda kwa daktari ila hakuingia kwa daktari yule bali alipitiliza halafu Juma hakuelewa kama Mariam hakuingia kwa daktari kwahiyo alikuwa akimngoja tu pale pale nje.

Juma alikaa sana pale nje na kuona kuwa kwasasa aende kuulizia kwa daktari, na alipoenda kuulizia kweli aliambiwa kuwa huyo mtu hakuingia pale kwa daktari, Juma alishangaa kuona kuwa mkewe kamchezea mchezo pale pale, wazo la haraka haraka lililomjia kichwani ni kuwa huenda Mariam kaenda kwao,
“Khaaaa mwanamke kichaa huyu, sasa angeniomba ruhusa angepungukiwa na nini? Si angeniambia tu na pengine ningemsindikiza na kurudi nae. Inabidi nikamfate tena jamani loh!!”
Kwanza Juma alitafuta tafuta pale hospitali, alipomkosa kabisa ikabidi tu aamue kwenda kumfata mke wake nyumbani kwao, hakumpigia simu sababu Mariam huwa hatembei na simu kwahiyo angejisumbua tu kumpigia.
Juma akiwa njiani kuelekea nyumbani kwakina Mariam, alikutana na yule binti ambaye alimsalimia Juma,
“Habari yako baba Mishi”
Juma alimuangalia yule binti na kumwambia,
“Una kichaa nini? Nishakwambia kuwa mwanangu hawezi kuitwa hilo jina”
“Haya yameisha, unaenda wapi?”
“Hayakuhusu”
Yule binti akacheka na kumwmabia Juma,
“Hata usihangaike kwenda kumfata mkeo nyumbani kwao, rudi tu nyumbani kwako utakutana nae njiani”
“Inamaana kaenda nyumbani!”
“Ndiomaana yake, mkeo kaamua arudi nyumbani sababu kaona hakuna anachoumwa ni kukusumbua tu”
“Khaaaa mwanamke ni kichaa sana huyu”
Juma aligeuza muda huo na kuondoka zake.

Mariam akiwa njiani, kwanza alikuwa na furaha sana kwani alikuwa amegeuza vile viatu bado ingawa watu walikuwa wakimshangaa ila yeye aliona ni sawa sawa tu kufanya vile huku akiwaza yale maneno ya mama yake kuwa hayo ni maswala ya mazingaombwe.
Ila aliposhuka kwenye gari kuelekea nyumbani kwao, alitokea mvuta bangi akiwa amebeba panga na kumwambia Mariam atoe kila alichokuwa nacho, yani Mariam alianza kulia tu na hakuwa na kitu cha kutoa kwakweli, yule mwizi akachukua nauli ya Mariam na viatu vya Mariam akaondoka navyo. Yani Mariam alihisi kuchanganyikiwa basi akaanza kukimbia kuelekea nyumbani kwao maana akili yake muda huo hadi imegoma kufanya kazi.
Ila wakati anakimbia, akashikwa bega, akaogopa sana kwani akajua ni kibaka mwingine, ila alipogeuka alimkuta ni Juma,
“Khaaaa mume wangu?”
“Mbona unakimbia jamani mke wangu, tena upo peku, umeanza kuchanganyikiwa?”
Mariam hakujibu ila alikuwa akiyaangalia yale mazingira sasa, alishangaa sana kwani yale mazingira yalikuwa ni mazingira ya kuelekea nyumbani kwake ambapo Juma alimshika tu mkono kumuongoza kuwa waende nyumbani.

Leo Lulu akiwa na yule mtoto ndipo akasikia harufu kali sana na kuhisi kuwa huenda yule mtoto amejisaidia haja kubwa, na kweli alipomtoa alikuta amejisaidia haja yenye muonekano ule ule wa kinyesi cha mbuzi, Lulu alishangaa sana na kuogopa hata kuendelea kumshika yule mtoto.
Ila badae alijipa ujasiri na kwenda kumnawisha kisha kumrudisha na kumvisha nguo vizuri halafu akajisemea sasa,
“Kwakweli hii nyumba itanishinda, mtoto anatoa kinyesi kinanuka hivi na kinafanana na kinyesi cha mbuzi halafu mama yake ni mvivu sijawahi ona dunia nzima. Mimi siwezi kuendelea kuishi hapa”
Mara yule mtoto akamwambia Lulu,
“Ulidhani kuwa utaweza?”
Lulu alijikuta akitetemeka mahali pale nakuanguka chini.
 
MTOTO WA MAAJABU: 9

Ila badae alijipa ujasiri na kwenda kumnawisha kisha kumrudisha na kumvisha nguo vizuri halafu akajisemea sasa,
“Kwakweli hii nyumba itanishinda, mtoto anatoa kinyesi kinanuka hivi na kinafanana na kinyesi cha mbuzi halafu mama yake ni mvivu sijawahi ona dunia nzima. Mimi siwezi kuendelea kuishi hapa”
Mara yule mtoto akamwambia Lulu,
“Ulidhani kuwa utaweza?”
Lulu alijikuta akitetemeka mahali pale nakuanguka chini.
Kwakweli Lulu hakujitambua kabisa yani ila alimsikia yule mtoto akiendelea kuongea pale pale,
“Hapa hapakufai Lulu, wewe hufai kukaa na mama yangu nilijua tu kuwa lazima pa kushinde hapa, unatakiwa kuondoka. Tena hata usiage, wewe ondoka tu waache na maisha yao humu ndani, hupawezi”
Yani Lulu alizidi kuogopa pale chini na kujikuta akizimia tu pale pale kwa uoga aliokuwa nao.

Juma na Mariam waliingia ndani na kumkuta Lulu akiwa chini, basi Juma akainama kumuinua ambapo lulu aliinuka bila hata ya kuongea kitu chochote kile kwani moja kwa moja alienda chumbani kwake, yani Mariam na Juma walijikuta wakiangaliana huku wakikaa pale sebleni na kujiuliza kuwa tatizo ni kitu gani mpaka imekuwa vile? Mbapo Juma alimuuliza mke wake,
“Unadhani ni kitu gani kimemsababisha kuwa vile alivyokuwa?”
“Mmmmh sijui ni kitu gani kwakweli maana kumbuka kuwa wote hatukuwepo hapa nyumbani”
“Haya tuachane na hayo, na wewe kwanini umeaniacha hospitali mwenyewe?”
“Aaaah kuna makubwa sana hapa, yani kila nikijitahidi nagonga mwamba”
“Kivipi?”
“Mama ameniambia kuwa mtoto wetu amerogwa, nikaongea nae na tulipatana nae kuwa leo niende nyumbani ili kwenda kuongea nae vizuri swala hilo, nikajua wazi kuwa nikikuomba ruhusa basi huwezi kukubali ndiomana nikaamua kutoroka pale hospitali”
“Khaaaa kumbe! Mbona mambo ya kawaida tu hayo, ungeniambia ningekataa vipi wakati ni kwaajili ya mtoto wetu Mariam? Haya, ila mbona badae umeamua kurudi nyumbani sasa? Na viatu viko wapi Mariam?”
“Kuwe na viatu wakati umetuma kibaka aje kuniibia hadi nauli yangu? Yani mambo vuluvulu, hapa nilipo sielewi kitu, nakuitikia tu. Ngoja na mimi niende nikapumzike kama Lulu labda akili itanikaa sawa maana naona kuwa akili haipo sawa kabisa”
Mariam aliinuka na kwenda chumbani kwao kwahiyo pale sebleni alibaki Juma na mtoto tu.

Juma alitikisa kichwa chake na kuamua kwenda kuangalia jikoni ila alikuta hakuna kitu chochote kilichopikwa ukizingatia huyu mdada wa kazi nae wamemkuta yupo chini na wamemshtua ila hajawajibu kitu zaidi ya kuinuka tu, basi Juma akajisemea,
“Au yule Lulu anajihisi vibaya kwa uvivu wa mke wangu? Maana mke wangu na yeye jamani ni shida sana”
Basi Juma aliamua yeye mwenyewe kuingia jikoni na kuanza kupika chakula cha kula usiku huo.
Juma alipomaliza kupika, alienda kumuamsha mke wake ambaye aliamka na moja kwa moja alianza kula, kisha Juma alienda kumuita Lulu, akamgongea mlango na kumwambia,
“Njoo ule Lulu”
“Hapana shemeji nimeshiba, asante”
“Mmmmh umekula nini?”
Mariam akadakia,
“Sasa na wewe mtu kakwambia ameshiba, mambo ya umekula nini yanatoka wapi? Alichokula anakijua mwenyewe ndiomana kakwambia kuwa ameshiba, muache tu.”
Juma akarudi zake kula na mke wake huku akimwambia,
“Ila mke wangu Mariam, mtu akikataa kula kama hivyo lazima ujue sababu”
“Sasa unataka kujua sababu ili iweje jamani? Mtu kakwambia ameshiba, sasa unataka sababu ya kushiba kwake ili ufanyeje? Halafu hayo maswala ya baba mwenye nyumba kumfatilia fatilia mdada wa kazi yameanza lini? Mkiambiwa mnatembea na wasichana wa kazi mnakataa”
“Jamani Mariam, kipindi chote hiko tumeishi pamoja sijawahi kutembea na msichana wa kazi, ndio iwe leo jamani! Hakuna kitu cha namna hiyo ila mimi ni baba kwahiyo lazima nijali hali ya watu wa kwenye familia yangu”
“Haya unatakiwa kuanza kunijali mimi kwanza”
“Nimekuelewa mke wangu”
Juma hakutaka mabisahano sana kwani aliendelea tu kula pale na mkewe na walipomaliza walimchukua mtoto wao na kwenda kupumzika ndani kwao, ila kama kawaida Mariam hakutaka kabisa kuwekwa karibu na mtoto huyo, hadi Juma aliamua kumuuliza leo,
“Sasa mke wangu ni lini utakubali kulala na mtoto wako?”
“Mimi!! Hapana kwakweli, siwezi kukubali yani ingekuwa inawezekana hata Lulu angekubali basi huyu mtoto angekuwa analala chumbani kwake”
“Kwahiyo wewe unaona ni vyema mtoto alale kwa mdada wa kazi kuliko kulala na wewe?”
“Ndio, tena ingekuwa vyema sana. Itabidi kesho nimebembeleze kama atakubali”
Juma hakusema neno zaidi na kuamua tu kulala kwa wakati huo kwani kuna muda alishindwa kabisa kumuelewa huyu mke wake.

Usiku ule ule, Lulu alipanga nguo zake vizuri yani hakutaka hata kupata mshahara wake wala nini kwani ilipofika saa kumi alfajiri aliamua kuondoka, na hakuona umuhimu wa yeye kuendelea kuwepo mahali hapo.
Lulu aliondoka zake kwa usiku ule hadi stendi huku akiwaza kama atapata usafiri au la, akiwa stendi kuna mdada alikutana nae na kusalimiana nae maana walikutana wawili tu stendi, yule mdada alimuuliza Lulu,
“Unatokea wapi?”
“Kuna nyumba huko nilikuwa nafanya kazi, ila kwakweli nimeshindwa kuendelea kuishi kwenye ile nyumba maana kuna mambo ya ajabu sijapata kuona”
“Mambo gani hayo?”
“Kwanza mama mwenye nyumba ni mvivu huyo balaa, anataka kila kitu afanyiwe”
“Ila unaelewa maana ya mdada wa kazi wewe?”
“Naelewa ndio, mdada wa kazi ni msaidizi wa kazi za nyumbani na msaidizi si kwamba ndio anatakiwa kufanya kazi zote peke yake, kuna kazi zingine zinatakiwa kufanywa na mwenye nyumba”
“Kama kazi gani?”
“Mfano, yule dada kaolewa ila anataka mimi ndio niwe namtandikia kitanda, mimi ndio niwe nasafisha chumba anacholala yeye na mumewe, mimi ndio niwafulie nguo zao za ndani yani yeye hafanyi kazi yoyote ile”
“Huyo dada ana ulemavu wowote?”
“Hamna, ni mzima kabisa yani. Hana ulemavu hata kwa mbali”
“Mmmmh unanishangaza maana walemavu wenyewe huwa kuna kazi wanafanya ila huyo nadhani ni zaidi hata ya walemavu, ila kuna ulemavu wa aina nyingi, na huyo ana ulemavu wa akili. Haiwezekani kabisa mtu mwenye akili timamu kuwa mvivu kiasi hiko! Hatukatai kusaidia, basi mtu uwe unafanya mara moja moja, ndio kila siku kweli?”
“Ndio yani kila siku ndio kazi zangu hizo, hata siku moja humkuti hata akisema leo namlisha mtoto yani”
“Sasa huwa anafanya nini kwasana?”
“Yeye anapenda kulala muda wote, yani akishiba tu basi analala”
“Pole sana, kingine kilichokuondoa hapo tofauti na huo uvivu wa mwenye nyumba?”
“Ni mtoto wa yule dada, ana maajabu sana, ana jisaidia kinyesi cha mbuzi halafu anaongea”
Huyu mdada mwingine akatabasamu na kumwambia Lulu,
“Naomba nipeleke huko tafadhari”
Lulu alimshangaa na kumwambia,
“Ila mimi nimetoroka na sitaki wanione”
“Hawatakuona, wewe nionyeshe tu kuwa nyumba yenyewe ndio hiyo hapo halafu mimi najua cha kufanya maana hata mimi nahitaji kazi za ndani”
“Ila hapo mbona utakimbia”
“Hapana, mimi siwezi kukimbia labda wakimbie wenye nyumba”
Huyu dada alikuwa akicheka tu huku akiongea hayo, basi Lulu aliongozana nae hadi kwenye nyumba ya wakina Mariam na kumuonyesha kuwa nyumba yenyewe ni hiyo hapo kisha Lulu aliondoka sasa na kurudi stendi ambapo alipanda gari na kuondoka zake.

Kulipokucha, wakati Juma amemaliza kujiandaa na kutaka kutoka, Mariam alimzuia kwanza na kumwambia,
“Ngoja kwanza, tuongee na Lulu kabisa kuhusu kulala na mtoto wetu”
“Khaaaa yani umedhamilia kabisa?”
“Ndio, kwa kifupi nimechoka kulala na huyu mtoto chumbani kwetu”
“Haya”
Basi Mariam alimuita Lulu ila Lulu hakuitika, alienda kuangalia chumbani kwa Lulu na kukutana na ujumbe tu, ambao alitoka nao na kumsomea mume wake,
“Dada na shemeji, mimi nimeamua kuondoka. Kazi hapo nyumbani kwenu sitaki tena, kila siku dada huwa unaniambia kama kuondoka na niondoke tu, unaniambia kuwa nisikusumbue wala kukubabaisha kuwa kazi ni nyingi. Kwakweli nimechoka yani dada unatuma kama muhindi vile! Nimechoka sana, na kikubwa ni mtoto wenu ameniogopesha sababu anaongea, kwaherini”
Juma na Mariam walitazamana basi Juma akamwambia mke wake,
“Ila nilikwambia Mariam, uvivu wako huo tutapoteza wafanyakazi wengi sana, kumbuka hata kipindi huna mimba ni wadada wangapi wa kazi walioondoka kwetu? Haya saivi una mtoto ndio mambo yamekuwa yale, yale. Mimi nilikwambia Mariam yakitokea haya usinizuie tena kwenda kazini”
“Kheee unadhani utaondoka uniache hapa peke yangu na huyu mtoto? Kwahiyo wewe unaona uovu wangu tu wa uvivu ila uovu wa mwanao anayeongea huuoni wala nini! Yani wewe huoni hata kama huyu mtoto ndio anayefanya wadada wa kazi waondoke humu!”
“Hata kama, ila sababu kubwa ni uvivu wako wewe, tena usikute hata huyu mtoto karogwa sababu ya uvivu wako, sijui ni mwanamke wa aina gani wewe!”
“Si unipe talaka yangu, kwanini unateseka sasa?”
“Talaka sikupi sababu nakupenda sana ila jirekebishe Mariam”
Juma akataka kutoka ila Mariam akamzuia kwa madai kuwa hawezi kubaki mwenyewe, Juma hakuwa na namna zaidi ya kuanza kupiga simu kuomba msaada wa kupata mdada wa kazi, kwanza Juma alimpigia mama yake simu ambapo alipomwambia tu mama yake alishangaa sana,
“Kheee huyo Lulu ni binti mstaarabu sana, mpole na mchapakazi, amewashinda huyo niwatafutie nani sasa?”
“Tusaidie mama yangu?”
“Kwakweli msitegemee kwangu maana sina msaada wowote”
Simu ilipokatika ilibidi Juma ampigie simu mama yake na Mariam ili amuombe msichana wa kazi pia, ambapo huyu mama alimwambia Juma,
“Mtoto wako ndio kikwazo hapo, hakuna msichana wa kazi atakayekubali kuishi na mtoto wa ajabu kiasi hiko”
“Ila mama sio mtoto tu ila wadada wengi wanaondoka kwasababu ya uvivu wa Mariam”
“Ila na wewe wakati unamuoa Mariam si nilikwambia lakini? Si nilikwambia kuwa mtoto wangu ni mvivu, kwani nilikuficha hilo jambo? Nilikuweka wazi kabisa kuwa Mariam wangu namjua mwenyewe, ya kwamba ni mvivu sana na siku zote alikuwa anatamani kuolewa ili aondoke nyumbani na kuachana na kazi za nyumbani, si nilikwambia wewe! Unalalamika nini sasa?”
“Basi mama yameisha, ila nahitaji mdada wa kazi”
“Tafuteni tu huko huko maana huku siwezi tena, Dora kashawatangazia sifa mbaya sana, siwezi kwakweli”
Mama Mariam akakata simu, kisha Juma akamuangalia Mariam na kumwambia,
“Unaona sasa Mariam, uvivu wako huo umefanya hadi tuwe na sifa mbaya”
“Uvivu wangu wapi, unadhani sijamsikia mama anachosema hapo? Ni mtoto ndio kafanya tuwe na sifa mbaya na sio uvivu wangu”
“Kwahiyo leo sitatoka?”
“Ndio, hakuna kutoka hadi tupate msichana wa kazi wa kuishi na mimi hapa”
Yani Juma alichukia sana, kwa mara ya kwanza alijikuta akijuta kumuoa huyu mwanamke kabisa.
Ila muda huo huo wakasikia mtu akibisha hodi, ikabidi Juma aende kufungua maana Mariam mara nyingi huwa na uvivu sana.
Akaingia binti ambaye kwa kumkadilia alikuwa kwenye miaka kumi na nane, basi aliwasalimia pale na kuwaambia,
“Samahanini naomba mnisaidie”
“Tukusaidie nini?”
“Natafuta kazi, kwahiyo kama kuna vikazi vya kufanya hapa mnaweza kunipatia au kama kuna mtu anahitaji msichana wa kazi mnaweza kunielekeza niende”
Mariam alimuangalia na kupumua kisha akasema,
“Yani mara nyingine ni kama bahati vile, sikia binti mimi na mume wangu hapa tulikuwa tukihitaji sana msichana wa kazi kwahiyo kuja kwako wewe imekuwa kama bahati”
“Jamani asanteni sana, nawashukuru sana”
Huyu binti alipiga magoti kama ishara ya kuwashukuru kwa hiki ambacho wamefanya kwake.
Hapo ndipo walipoanza kumuuliza maswali,
“Unaitwa nani kwani?”
“Naitwa Anna”
“Oooh Anna, karibu sana. Mimi dada yako naitwa Mariam, na huyu shemeji yako anaitwa Juma”
“Nashukuru sana kuwafahamu”
“Na sisi tunashukuru pia, karibu sana Anna”
“Asante”
Basi walimkaribisha pale Anna kuwa ni msichana wao wa kazi, na muda huo huo Juma aliweza sasa kumalizia kujiandaa na kuondoka zake kwenda kwenye shughuli zake.
Mariam alifurahi sana na kuanza kumuelekeza yule Anna baadhi ya mambo na kazi za pale nyumbani ikiwemo na kazi ya kumuhudumia mtoto wao, pia alitumia mwanya huo kumwambia Anna kuwa mtoto atakuwa analala na yeye sababu mtoto huyu huwa analala na wadada wa kazi.
“Aaaah kwahiyo halali na wazazi wake huyu?”
“Ndio, kashazoea kulala na mdada wa kazi huyu”
“Sawa mama hakuna tatizo”
“Nimefurahi sana Anna kuja kwenye maisha yetu”
Yani Mariam alikuwa na furaha kubwa sana kwa siku hii ya leo.

Kwa siku hii hii moja tu, Mariam alipenda kweli utendaji kazi wa Anna kwani alionekana ni msichana aliyekuwa anajishughulisha sana, basi Juma aliporudi wakati wa kulala alimuuliza kwanza mke wake,
“Mtoto je?”
“Kashachukuliwa na Anna huko amelala chumbani kwake”
“Duh!! Mke wangu, yani ushamwambia huyo binti alale na mtoto ikiwa huyo binti humjui vizuri wala nini”
“Sasa wewe unadhani kuwa huyo binti atamla mtoto wetu au ni kitu gani?”
“Hapana, mimi nimesemea tu. Vipi utendaji wake wa kazi?”
“Kwa leo tu nimempenda ila ngoja niendelee kumuangalia nitakupa jibu zuri mume wangu kadri atakavyoendelea kunifurahisha”
“Sawa, ila mimi binafsi sijapenda kwa mtoto kulala na msichana wa kazi”
“Ila mimi nimependa tena nimependa sana kwani yule mtoto alikuwa akizuia mambo yetu mengi sana”
“Lakini ni mtoto wetu”
“Hata kama ni mtoto wetu ila si haki yake kutufanya tusiwe na furaha, maisha yenyewe mafupi haya, tunatakiwa kufurahi, kweli tukawaze vioja vya mtoto kila siku! Kwanza nashukuru sana alivyopatikana huyu mdada wa kazi ambaye analala na mtoto wetu”
“Haya siongei zaidi”
Juma alikuwa sio mtu wa kubishana sana kwahiyo mara nyingi alimuachia ushindi tu mke wake ili mke wake afurahi ingawa ukweli hakupenda pia kuona kile ambacho kinaendelea pale nyumbani kwao.
Kulivyokucha tu, mapema kabisa akajiandaa na kwenda zake kwenye shughuli zake.

Kwakweli Mariam alipenda utendaji wa kazi wa Anna na alionekana kuwa ni mchapakazi sana hadi Mariam alimsifia Anna kwa mumewe Juma,
“Yani kwa siku hizi mbili tu, kwakweli nimempenda huyu binti hatari, unajua anafanya kazi sana tena sana”
“Basi cha uvivu umefurahi sana mke wangu kwa hilo”
“Kweli nimefurahi, unajua nakaa tu siku hizi na hiki ndio ninachokitaka. Yani mimi maswala ya kufanya fanya kazi kama mtumwa akuuu siyataki”
“Kwahiyo mtoto humuogopi tena?”
“Nitamuogopa wapi na muda wote huyo Anna ndio anashinda na mtoto! Yani anamuhudumia, anampenda hadi raha kama sio yule mtoto aliyekuwa akiniongelesha jamani, kwa Anna anatulia balaa”
“Basi ni vizuri kusikia hivyo mke wangu”
Juma alimjua mkewe kuwa ni mvivu kwahiyo alivyosikia yule msichana ni mchapakazi aliona ni jambo la kheri sana, basi kwa kipindi hiki walikuwa wakilala kwa furaha sana.

Leo Mariam alivyoamka alikuwa amechoka hatari, muda huu Anna alikuwa ameenda kumlaza mtoto chumbani kwake anapolala nae.
Basi Mariam alitoka sebleni na kumkuta Anna ndio anatoka chumbani pia,
“Hivi Anna ulifua na zile nguo za baba?”
“Ndio mama, na za kwako pia nimeshazifua”
“Oooh wewe ni binti makini sana Anna, ila leo nimechoka jamani, mgongo wote unauma”
“Pole sana dada”
“Naomba tu niletee chai niweze kunywa”
Anna akamuandalia Mariam ile chai ambapo Mariam alishangaa kwa vile vitafunwa alivyoweka Anna sababu alijua kutakuwa na mkate tu ila alishangaa kuona chapati,
“Kheee hizi chapati Anna umeenda kununua?”
“Hapana dada nimezipika”
“Kheee kweli wewe ni noma Anna, sasa chapati umepika saa ngapi? Nguo nazo umefua saa ngapi?”
“Unashangaa hilo tu dada, na maji nimejaza kila chombo”
“Kheee kwakweli nashukuru umekuja kwenye maisha yangu, hapa tu nimeamka na uchovu. Unajua kuchoka, yani nimechoka balaa”
Basi Mariam alikunywa ile chai huku akimsifia Anna kuwa anapika chapati vizuri sana.

Mariam alipitiwa na usingizi pale sebleni, alipokuja kushtuka alijikuta amechoka kushinda hata ya alivyokuwa amechoka asubuhi, alipotazama kwenye kochi aliona mtoto wake amekaa kwenye kochi pale, alishangaa sana na kujikuta akisema,
“Kheeee kumbe saivi wewe mtoto unakaa!”
Kisha alianza kujinyoosha nyoosha viungo vyake na kulalamika,
“Jamani nimechoka mimi, nimechoka sana. Viungo vyote vinauma jamani!”
Ila alishangaa kumuona kama mwanae akitabasamu kisha huyu mtoto akamwambia mama yake,
“Umepatikana sasa na uvivu wako”

Itaendelea…..!!!
Ka mawasiliano 0629980412
 
MTOTO WA MAAJABU: 10

Kisha alianza kujinyoosha nyoosha viungo vyake na kulalamika,
“Jamani nimechoka mimi, nimechoka sana. Viungo vyote vinauma jamani!”
Ila alishangaa kumuona kama mwanae akitabasamu kisha huyu mtoto akamwambia mama yake,
“Umepatikana sasa na uvivu wako”
Mariam alimuangalia huyu mtoto kwa makini sana leo kisha akasema,
“Jamani huyu sio mtoto wangu”
kisha yule mtoto akasema,
“Wakati unanizaa kuna mwingine alikuwa anazaa zaidi yako?”
Mariam akaogopa kujibishana na huyu mtoto basi akainuka na kwenda chumbani kwake ambapo alichukua nauli tu na kutoka ila mlango wa nje alikutana na Anna ambaye alimuuliza,
“Dada unaenda wapi?”
Mariam hakuwa na jibu la haraka haraka kwani safari ya leo hakujipanga nayo vizuri, kisha Anna akamwambia,
“Yani dada unataka kumtoroka mtoto wako?Hivi unajua kwenye maisha ya tu basi mama ana nafasi kubwa sana, kwanza anabeba mimba, pili anateseka na ile mimba na tatu anazaa kwa uchungu sana, yani mama ndiye anayejua mateso anayoyapata ili kumpata mtoto ndiomana wanasema uchungu wa mwana aujuaye mzazi, sasa wewe ni mama gani usiyeujua uchungu wa mwanao? Yani bila ya aibu unataka kumtoroka mwanao?”
Mariam alimuangalia Anna kisha hakusema chochote na kuondoka zake ila Anna alimuangalia tu na kucheka.

Mariam alienda hadi stendi na alikuwa amechoka sana, alisubiria daladala na kuona zinachelewa hivyobasi akaamua kukaa pale stendi na kujikuta akilala pale pale yani hakuwa na habari tena ya kitu gani kinaendelea kwake.
Muda huu Mariam alisikia mtu akimuamsha,
“Weee Mariam, weee Mariam weee”
Alipoamka alikutana macho na mumewe na kushangaa ila alikuwa chumbani basi mume wake akamwambia,
“Nimekuamsha ili nikuage kuwa ndio natoka muda huu”
Mariam alimshika mkono mume wake na kumuuliza,
“Umerudi muda gani na umenikuta wapi?”
“Jana nimechelewa kidogo kurudi ila nimekukuta umelala hoi basi ikabidi nisikusumbue, ndio asubuhi hii nimekuamsha ili nikuage inaonekana umechoka sana”
“Na kweli nimechoka sana mume wangu, ila ngoja niamke nikaoge ninywe chai ila kuna kitu sielewi jamani”
“Kitu gani tena?”
“Aaarrgh sijui kwanini imekuwa hivi, sielewi mimi”
“Huelewi nini mke wangu Mariam?”
Mariam aliinuka na kwenda kuoga, ila Juma alimsubiria hadi Mariam alipotoka kuoga na kumwambia,
“Mke wangu, kuna nguo zangu chafu nyingi sababu ya kazi ya jana, naomba unifulie basi”
“Kheee umeanza kuwa na wazimu wewe mwanaume? Toka lini mimi nikafua! Nitamwambia huyo Anna akazifue”
“Sawa hakuna tatizo, mimi nimekwambia tu wewe sababu wewe ni mke wangu”
Muda huo Juma aliondoka zake na kumuacha Mariam akiendelea kuvaa.

Mariam alipotoka chumbani, alikuta chai imeshatengwa mezani huku Anna akiwa sebleni akicheza na mtoto tu, alimsalimia pale halafu Anna alimkaribisha mezani kisha Mariam alimuuliza Anna,
“Hivi Anna kuna kitu chochote mimi na wewe tumeongea jana?”
“Kitu gani dada?”
“Sijui uliniambia kuwa namtoroka mwanangu?”
“Unamtoroka mwanao? Kivipi?”
Mariam akaona kamavile Anna hamuelewi basi alienda kukaa mezani na kumimina chai huku akifunua vitafunwa ila alishangaa sana,
“Kheee hivi vyote umepika wewe Anna?”
“Ndio dada”
“Jamani, umejuaje kama napenda hivi jama ni Anna! Wewe ni binti mzuri sana, yani bagia na sambusa huwa napenda sana”
Anna alitabasamu tu huku Mariam akianza kula na kusifia kuwa ni nzuri sana huku akimpongeza Anna kwa kupika vizuri ila alivyomaliza kula alirudi kukaa kidogo kisha akajikuta akilala pale kwenye kochi kwa muda kidogo aliposhtuka alimkuta Anna akiwa bado anacheza na mtoto alimuuliza,
“Anna, umesafisha chumbani kwangu?”
“Ndio dada, nimeshasafisha”
“Aaaah upo vizuri sana wewe, na nguo za shemeji yako zile umeenda kuzifua?”
“Nimeziloweka dada, nitazifua muda sio mrefu”
“Na zile nguo zangu?”
“Zote nimeloweka dada, nataka nikianza kufua basi zitakate kabisa”
“Dah ndiomana nakupenda Anna, wewe ni binti mchapakazi sana. Hongera, ngoja mimi nikapumzike kidogo maana nimechoka sana”
“Sawa dada”
Mariam muda huu alienda zake chumbani na kweli alikuta kumesafishwa vizuri sana hadi alipenda na zile nguo chafu zote zilikuwa zimetolewa, basi alijikuta akisema,
“Kwakweli huyu binti ndio mdada wa kazi niliyekuwa nahitaji, sio jitu unaliambia kasafishe chumba linaanza kusema oooh kazi zingimne ufanye mwenyewe dada wakati kumlipa namlipa vizuri aaarggh walikuwa wananikera wale basi tu, ila huyu ndio nimepata kwakweli, nadhani nitadumu nae”
Kisha kwa muda huu alilala sasa.

Mariam aliposhtuka alikuwa amechoka sana na kugundua kuwa hata chakula cha mchana kwa siku hiyo hakula wala nini, basi moja kwa moja alienda sebleni na kumkuta Anna akicheza na mtoto tu,
“Jamani Anna hata kunikumbusha kuhusu kula chakula cha mchana jamani!”
“Samahani dada nilijua ukilala hupendi kusumbuliwa”
“Yani mimi kwenye swala la kula uwe unaniamsha tu maana napenda sana kula na kulala”
“Sawa dada, nitakuwa nakuamsha”
“Yani kama saa hizi njaa inaniuma ile mbaya”
“Usijali dada, chakula tayari”
Anna alienda kupakua chakula na kuweka mezani ambapo Mariam alianza halafu Anna alipakua chakula kingine na kuanza kumlisha mtoto, hapo Mariam alishangaa sana na kuuliza,
“Mbona unamlisha mtoto chakula cha kikubwa?”
“Hata yeye ni mkubwa dada, sio mdogo huyu, kuna mambo kachelewa tu ila ni mkubwa?”
“Unajua ana umri gani huyo?”
“Ana miaka miwili”
“Miaka miwili ya wapi? Ni kweli mimba yake nimekaa nayo kwa miaka miwili ila yeye hana miaka miwili”
“Ila dada, chakula cha hivi ndio anapenda na anajisaidia choo kizuri sana tofauti na kule chakula chako cha kumchanganyia maziwa ya unga na ya ng’ombe”
“Kwani sababu ya maziwa ndio iliyopelekea kujisaidia choo cha aina ile?”
“Hapana sio sababu ya maziwa, ila kuna kitu kipo kwa mwanao halafu ulivyokuwa ukimpa maziwa yale ndio ulikuwa ukimuharibu huyu mtoto, kuna kitu ulikuwa hujagundua kuhusu huyu mtoto ila huyu ni mtoto mzuri sana. Si unaona anavyokula vizuri sana kwa muda huu”
Anna alimlisha mtoto na alipomaliza, Mariam nae alikuwa kamaliza kula huku bado akishangaa sana jinsi ambavyo Anna alionekana kumzoea yule mtoto tofauti na yeye ambaye amemzaa. Mariam akainuka kwanza ili arudi chumbani ila alimuuliza Anna,
“Vipi ulifua zile nguo?”
“Ndio dada, bado kuzianua tu”
“Vizuri sana Anna, ukizianua njoo nazo chumbani na uzipange vizuri kabatini”
“Sawa dada”
Basi Mariam akaingia chumbani kwake ila muda huu hakutaka kulala wala nini, alichukua simu ili ampigie mama yake na amueleze juu ya mdada wa kazi aliyempata ila alijikuta akilala huku ameshika ile simu mkononi.

Juma aliporudi leo nyumbani kwake, aliingia na kumkuta Anna akiwa ametoka kumlaza mtoto chumbani kwahiyo alimuuliza tu,
“Dada yako yuko wapi?”
“Amelala”
“Ooooh anawahi kulala sana siku hizi jamani”
“Anawahi kweli kulala”
Basi Juma aliingia chumbani kwao na alipenda kweli mpangilio wa chumba chao alioukuta, alikuta chumba kimesafishwa vizuri sana, nguo zimepangwa vizuri na alichopenda zaidi ni pale alipofungua kabati na kukuta nguo zimepangwa vizuri sana kabatini, akatabasamu na kumuamsha mke wake, Mariam aliamka huku Juma akitabasamu na kumwambia.
“Asante mke wangu?”
“Asante ya nini?”
“Najua hii ni kazi yako humu chumbani?”
“Kivipi? Ni Anna ndio nilimpa kazi ya kusafisha”
“Hata kama ila kafanya kwasababu yako, nashukuru mke wangu maana humu chumbani kulikuwa kunasafishwa juu juu tu ila leo ni kumesafishwa hadi raha jamani. Nafurahi sana mke wangu”
“Yani huyu Anna ni mchapakazi jamani mume wangu, hadi raha”
“Kweli ni raha, twende basi tukale”
“Mimi tayari nimeshakula, kwahiyo labda ukale wewe tu hata hivyo nimechoka jamani mume wangu nimechoka sana”
Yani Juma alikuwa akimshangaa mke wake kwa kauli ya kuchoka balaa ukizingatia kazi zote zilikuwa zinafanywa na mdada wa kazi, sasa yeye ni kitu gani kinachomfanya achoke kwa namna ambayo anailalamikia kila siku? Yani Juma alikuwa anachukia, ni basi tu alimpenda mke wake.
Juma alienda zake kula na kurudi zake kulala, mpaka asubuhi Mariam alikuwa amelala tu na muda wote alikuwa akilalamika kuwa amechoka sana.

Leo Juma kabla ya kuondoka kwenda kwenye shughuli zake, aliweza kukaa na mke wake kuwa chai kwa pamoja ambapo ilikuwa ni chai na chapati, basi Juma akamtania tu Mariam,
“Kheee huyu Anna anapika chapati kama wewe”
Mariama akatabasamu tu na kusema,
“Ila huyu anajua zaidi kupika”
“Hata wewe mke wangu kupika unajua sema tu ni mvivu, siku ukiacha uvivu wako mbona humu ndani tutakuwa tunajing’ata vidole kwa mapishi yako”
Mariam akatabasamu tu kisha akamwambia tena mumewe,
“Ila siku hizi ni tofauti na wale wasichana waliopita, kila chakula unachokula unakisifia mume wangu”
“Ni kweli, huyu binti naona huwa unamuelekeza kupika maana huwa chakula chake kama umepika wewe vile, kinanoga hatari. Ona kama hizi chapati, kwakweli leo nimefurahi sana mke wangu”
Juma alimaliza pale kunywa chai na kumuaga sasa Mariam kuwa anenda kwenye shughuli zake kwahiyo aliondoka zake.
Muda huu Mariam alienda kuongea kidogo na Anna kwani huwa hata hakai nae kuongea nae sababu ya kulala,
“Hebu Anna mdogo wangu nisaidie kitu, hivi ni kwanini nachoka sana ikiwa sifanyi kazi yoyote?”
“Kulala nako ni kazi dada, mtu gani muda wote unalala jamani! Lazima uchoke”
“Sasa mimi kama hivi nimemaliza kunywa chai najihisi usingizi balaa”
“Sasa huo usingizi ndio unakuchosha”
“Sasa nikae nifanye nini?”
“Unaweza hata ukaenda kulima lima pale nje, unajua dada una eneo zuri sana”
“Kheeee, na wewe usitake kuniudhi sasa, hivi kweli kabisa mimi niende kulima mimi? Kabisa mimi niinamishe mgongo kulima, nimepungukiwa na nini?”
“Kwani wanaolima dada wamepungukiwa na nini?”
“Ni umasikini ndio unaowafanya walime”
“Kheee dada, wakulima ni matajiri sana ujue, yani kilimo kina hera ni sababu tu unakidharau”
“Ila mimi siwezi kulima”
“Sawa dada, sijasema kuwa unaweza. Ni kweli nakuona huwezi kulima maana hata mikono yako ni laini sana dada yangu, ila mimi naweza leo nikalima lima kidogo pale ingawa kulima sio fani yangu pia”
“Bora ufanye wewe, upo vizuri sana wewe mtoto”
Kisha Mariam aliinuka na kwenda kulala ila kabla ya kulala leo alipigiwa simu na mama yake na kuanza kuongea nayo,
“Tena nilitaka kukupigia mama?”
“Mbona hukupiga?”
“Si nikapitiwa na usingizi”
“Yani wewe na huo usingizi umekuwa kama mjinga hadi unakera, haya mbona hukuja tena?”
“Mmmmh mama, wewe acha tu. Kuna makubwa yalinipata”
“Yapi tena hayo?”
“Acha tu mama yangu ila tumepata mdada wa kazi mzuri sana”
“Huyo atavumilia vituko vyenu humo ndani? Na yeye ataondoka tu”
“Hapana mama, yeye kampenda hadi mtoto wetu, anaishi nae vizuri sana halafu ni mchapakazi hatari”
“Ila mwanangu……”
Kabla hajaendelea simu ilikuwa imekatika, Mariam aliijaribisha lakini haikupatikana, basi Mariam aliiweka pembeni na muda huo akaamua kulala tu ingawa mama yake naye ameshamsema kuhusu swala la kupenda kulala kila wakati.

Mariam alipoamka muda huu, alijihisi kuchoka zaidi ya mwanzoni, alitoka kwenda kula na kukuta chakula kimeshawekwa mezani kwahiyo alifikia tu na kuanza kula huku akimsemesha Anna,
“Hivi wewe umeshakula?”
“Tayari dada, nimeshaanza hata kulima huko nje”
“Ooooh kazi nzuri sana, upo vizuri sana Anna. Wewe mtoto nikipata zawadi nitakuletea jamani zawadi yako”
“Asante sana dada, unataka tupande nini?”
“Sijui, kwani tupande nini?”
“Tupande mahindi na maharage”
“Inawezekana eeeh!!”
“Ndio dada, inawezekana. Shemeji akirudi mwagize hizo mbegu ili tuweze kupanda”
“Aaaah ngoja nimpigie simu tu aje nazo, halafu kesho upande hizo mbegu”
Mariam alipomaliza kula, moja kwa moja alichukua simu yake na kumpigia simu mumewe ambapo alimuagiza hizo mbegu za mahindi na maharage halafu alipomaliza hapo alienda kulala.

Juma aliporudi alimkuta mkewe kalala kwahiyo zile mbegu aliziacha sebleni na alimuona mkewe amechoka sana kwahiyo yeye alienda tu kula na kwenda kulala pia.
Kulipokucha tu Juma alianza kuongea na mke wake,
“Hongera mke wangu, hiyo ndio akili sasa tuna eneo kubwa ila hatujawahi kuwaza hata kupanda mahindi ya kula, hongera sana”
“Unafikiri ni wazo langu basi! Ni Anna huyo ndio kashauri hivyo”
“Ila kulima si unamsaidia?”
“Nani amsaidie bhana, mimi na kulima wapi na wapi Juma? Analima mwenyewe tu, halafu kulima anapenda yule mtoto”
“Basi twende tukaangalie alivyolima”
“Aaaah nimejichokea haswa, siwezi kwakweli”
Basi Juma alitoka nje na kuangalia palipolimwa ni kweli palilimwa sehemu kubwa sana na hata yeye alijisemea kuwa Anna ni binti ambaye anajiweza sana sababu kulima eneo kubwa vile sio mchezo.

Mariam hakutoka hata kula chakula cha asubuhi alitoka mchana tu ambapo alikula kidogo sana na kudai kuwa anaenda tena kulala, basi Anna alikuwa akimuangalia tu huku akitabasamu hadi Mariam alimuuliza,
“Mbona unatabasamu tu?”
“Hapana dada, yani swala lako la kulala kila wakati ndio ambalo linanifanya nibakiwe na tabasamu”
“Kwahiyo nakuchekesha eeeh ambavyo nasema kuwa naenda kulala kila muda? Nakushangaza eeeh!”
“Hapana, ila ndio maisha ambayo umeyachagua”
“Sawa, badae niamshe nile vizuri”
“Sawa dada”
Basi Mariam moja kwa moja alienda chumbani kwake na kulala, tena muda huu alijikuta akilala usingizi mzito sana.

Leo Juma aliwahi kurudi kutoka kwenye shughuli zake, alivyofika tu nyumbani moja kwa moja aliingia chumbani kwake na kumuona mke wake akiwa amelala na hajitambui kabisa.
Basi Juma aliamua kutoka nje ili kumuangalia Anna, alipozunguka kule nyuma karibu na lile eneo lililolimwa alishangaa kumuona mkewe akiwa yupo kupanda mahindi.

Itaendelea……!!!
Kwa mawasiliano 0629980412
 
MTOTO WA MAAJABU: 11

Basi Juma aliamua kutoka nje ili kumuangalia Anna, alipozunguka kule nyuma karibu na lile eneo lililolimwa alishangaa kumuona mkewe akiwa yupo kupanda mahindi.
Juma alishangaa sana ukizingatia mkewe alimuona chumbani tena akiwa hoi kabisa, basi Juma akaita,
“Mariam, Mariam…”
Na muda huo yule mke wake aligeuka ila akashangaa kuona kuwa ni Anna ndio aliyekuwa akipanda mahindi, yani Juma hakuelewa alifikicha macho yake sana ila hakuelewa kitu na hakusema kitu badala yake alirudi ndani na moja kwa moja alienda tena chumbani, nia yake ilikuwa ni kumuamsha Mariam ili aongee nae ila badala ya kumuamsha Mariam alijikuta na yeye akiwa amelala.
Juma akiwa kwenye usingizi alimuona mtoto wake akiwa anatembea ndani ya ndoto halafu yule mtoto wake alimwambia Juma,
“Mimi nakupenda sana wewe baba sababu unanipenda sana, hakuna kibaya cha kukupata wewe, ila huyu mama muache akome tu”
Juma alishtuka sana toka kwenye ile ndoto aliyoiota na kumuangalia mke wake ambaye alikuwa hoi ila baada ya muda mfupi na yeye alishtuka na alianza kulalamika kuchoka kama kawaida yake kwa kipindi hiki kulalamika kuwa amechoka sana,
“Nimechoka jamani, viungo vyote vinaniuma mimi jamani!”
“Pole mke wangu”
Ikawa ndio kama Mariam kashtuka vizuri maana mwanzoni hata hakujua kama mume yupo ndani, basi akamuangalia na kumuuliza,
“Umerudi muda gani Juma?”
“Nimerudi muda sio mrefu ila nimekukuta umelala hoi”
“Aaaah kumbe! Yani nachoka jamani siku hizi, nachoka sana au nina mimba tena!”
“Hiyo mimba tena uitoe wapi Mariam? Kumbuka kuwa ulikuwa ukinipa sababu ya mtoto kila siku kipindi kile tunalala na mtoto halafu kipindi hiki kila siku unadai kuwa umechoka haya hiyo mimba itatokea wapi?”
Mariam alitulia na kuona ni kweli hawezi kuwa na mimba nyingine ukizingatia hajashirikiana na mume wake toka alipojifungua huyo mtoto wake na amekuwa na sababu kila siku za kutokushirikiana nae, ila sababu tu Juma anampenda ndiomana alikuwa hamlazimishi.

Usiku wa siku ile, walienda tu kula na moja kwa moja kurudi kulala ila kwakweli Juma alikuwa na maswali sana katika akili yake hata hakujua ni wapi aanzie na majibu ya maswali yake ila aliamua tu kulala kwa usiku huo.
Kulipokucha tu, Juma alipoamka alikuta chai imeshaandaliwa mezani yani kwa kipindi hiki ilimbidi Juma awe anakunywa chai nyumbani kwake kabla hata ya kwenda kwenye mizunguko yake,basi alimuasha mkewe ili waweze kunywa chai pamoja,
“Twende tukanywe chai kwanza Mariam”
“Mmmmh niache nilale kwanza, nikiamka ndio nitakunywa chai”
Juma hakuwa na namna zaidi ya kumuacha alale halafu yeye kwenda kunywa chai na kumuaga Anna,
“Badae Anna”
“Na leo utawahi kurudi shemeji kama jana?”
“Mmmmh sijui lakini naweza kuwahi kurudi”
“Haya sawa”
Basi Juma akaondoka zake huku Anna akirudi kukaa sebleni na mtoto.

Kwenye mida ya saa nne asubuhi ndipo Mariam alipoamka tena alikuwa amechoka sana, yani alikuwa ajinyoosha tu na kupiga miyayo ya ucbhovu muda wote, basi alienda kuoga na kutoka sebleni huku akimwambia Anna,
“Umeshaandaa chai Anna?”
“Ndio dada, tena muda mrefu tu”
“Aaaah wewe ni binti mzuri sana, wewe ni mchapakazi sana yani mimi siwezi mwenzenu”
“Ila dada kila kiru ni maamuzi, hata wewe ukiamua unaweza”
“Hapana, mimi siwezi, yani mimi ni mvivu sana kufanya kazi”
Basi moja kwa moja alienda mezani na kuanza kunywa chai, huku akimuongelesha Anna,
“Halafu sikukuuliza, hivi ulishamaliza kulima na kupanda?”
“Ndio dada, yani hapa tunangoja mazao tu, tutakula sana mahindi. Kazi iliyobakki hapa ni kupalilia tu”
“Jamani haya mambo mwenzenu ndio siwezi kabisa, wanayaweza watu wa vijijini”
“Hivi dada unajua mimi sio wa kijijini”
“Sasa umewezaje kulima Anna?”
“Kila kitu ni kuamua dada yangu, kulima unashika jembe na kuliinua juu na kulishusha kwenye ardhi, yani ukiamua unaweza”
“Kwahiyo wewe Anna ni umekulia mjini kabisa?”
“Yani dada nikikuelezea historia ya maisha yangu unaweza kulia, maisha yanabadilika sana sio kama tunavyoyategemea. Maisha hayaeleweki”
Mariam alijikuta akitamani sana kujua historia ya Anna hivyobasi alikunywa chai kwa haraka na kwenda kukaa karibu na Anna ili Anna amuelezee historia ya maisha yake,
“Eeeeh niambie mdogo wangu”
“Ila nitakueleza kwa kifupi tu!”
“Ndio nielezee mdogo wangu”
“Yani dada, mimi nilizaliwa kwenye familia ya watoto wanne na mimi ndio nilikuwa kitinda mimba kwa mama yangu, ila wale wenzangu niliachangia nao mama tu, mimi baba yangu yupo. Sasa mama yetu alikufa, tena aliuwawa tu kikatili, yani unamuona mama yako muda huu halafu saa moja badae anauwawa kikatili, unapewa tu taarifa kuwa amekufa. Mimi wakati mdogo nimeishi maisha ya kitajiri sana, nilikuwa sifanyi kazi yoyote, mama alinidekeza na kunipenda sana, alinipa kila nilichokitaka ila tangu amekufa ndio mambo yalipobadilika kwangu. Baba yangu karogwa na mwanamke huko hanitaki na wale ndugu zangu wamechukua kila kitu hawataki kuishi na mimi wanasema niende kwa baba yangu, nimeishi kwa shida sana baada ya hapo, nikawa nahangaika tu, hakuna cha kusoma wala hakuna cha nini na ndio nahangaika tu na kazi za ndani, nashukuru hata nimefika hapa mmenipokea”
“Kheee pole sana, huyo mwanamke aliyemchanganya baba yako akili ataalaaniwa kabisa. Kwahiyo baba yako ana hela tu!”
“Ndio, baba yangu ana hela najua siku akili ikimrudia ndio atanikumbuka mtoto wake ila kwasasa hanitaki kabisa wala hata hanikumbuki”
“Pole sana, hao ndugu zako nao Mungu atawalaani mdogo wangu, yani kweli wakuache uhangaike wakati wenyewe wapo?”
“Yani dada angalia tu watu hivi hivi ila unathaminika ukiwa nacho, mimi walinipenda kumbe sababu ya mama ila kwasasa mama hayupo hawanipendi tena, hawanitaki tena yani mimi nipo tu kuhangaika na maisha”
“Pole sana mdogo wangu, kuanzia sasa jihesabie kuwa umempata ndugu yako maana mimi nitakupenda na kukuthamini, nitakuwa na wewe bega kwa bega yani mimi huwa roho inaniuma sana nikisikia kuwa kuna mtu ndugu zake wamemtenga, usijali Anna, kuanzia sasa mimi ndio ndugu yako”
Basi Anna alienda kumkumbatia Mariam huku akimwambia,
“Asante sana dada”
Mariam alizidi kumsisitiza Anna kuwa atamsaidia na atakuwa nae bega kwa bega ukizingatia ule ufanyaji kazi wa Anna ndio ulimfanya Mariam azidi kuvutiwa na Anna.
Basi baada ya kuongea ongea pale alijikuta akilala pale pale sebleni.

Mariam alipokuja kushtuka muda huu ilikuwa ni tayari mchana, basi akamuuliza Anna pale,
“Kwahiyo nililala hapa hapa”
“Ndio dada”
“Ila leo sijachoka sana wala nini, bado nina nguvu zangu ila siku hizi naamka asubuhi nikiwa nimechoka sana”
“Dada, unaonaje kila asubuhi tukianza zoezi la kukimbia!”
“Weeee, mimi hata mazoezi siwezi jamani, kujichosha tu. Siwezi kabisa”
Basi aliinuka na kwenda kula, ambapo Anna nae alienda kula basi Mariam akawa anakula na kumwambia Anna,
“Unajitahidi kusonga ugali mlaini sana”
“Sababu na mtoto nae anapenda ugali mlaini”
“Kwahiyo huwa anakula?”
“Ndio, huwa anakula. Anapenda sana, ila dada acha kumuogopa mtoto wako nahisi kuwa huwa unamuogopa maana hata siku moja hukai nae”
“Yani Anna mdogo wangu acha tu, ila kwasasa mimi na wewe tumekuwa kama ni ndugu, ngoja nikwambie kuhusu huyu mtoto”
“Eeeeh niambie”
Basi Mariam akamueleza Anna jinsi alivyohangaika na ile mimba kwa miaka miwili na jinsi mama mkwe wake alivyomletea dawa na jinsi alivyoitumia na yale aliyokutana nayo hospitali na jinsi mtoto walivyogoma kumuhudumia na jinsi ambavyo huwa akiongea, basi Mariam akamalizia kwa kumwambia Anna,
“Kiubinadamu lazima mtu uogope kwakweli, ndiomana mimi nimejikuta namuogopa sana mtoto ingawa ni mtoto wangu”
“Sasa unahisi kwanini mimi simuogopi?”
“Sijui, pengine sababu hujaona mambo yake ya ajabu”
“Sikia dada, mambo mengine ya ajabu ya huyu mtoto umeyataka mwenyewe dada yangu. Haya ulipewa dawa uoge kwa siku tatu, ni kitu gani ulichokuwa unakimbilia ukaoga kwa siku mbili? Ni kitu gani kimekushangaza kwa mtoto kutoka na meno, sasa mtoto akae tumboni kwa miaka miwili, akitoka si ameshakuwa mkubwa huyo! Hata kulia tena kitoto hawezi, na ndio kitu kilichotokea hapa, ilitakiwa ukubaliane na hali halisi, kwanza mmeyataka wenyewe, ulishaona mazingira ya mimba yamekuwa ya ajabu, ungevumilia tu na kujifungua nyumbani kisha ungemuhudumia vizuri mtoto wako na baada ya siku kadhaa ungempeleka hospitali na angepata huduma zote ila kule hospitali lazima waogope maana ni mtoto gani anazaliwa anatanguliza miguu? Kwa kawaida huwa mtoto anatanguliza kichwa, ila mtoto akitanguliza miguu basi huyo huwezi ukasema tena kuwa ni wa kawaida, lazima kuna uwalakini hapo, lazima hospitali waogope. Yani wewe mtoto umemnywea midawa kama yote halafu unashangaa kutokea na mambo ya ajabu jamani, sasa unashangaa nini?”
“Ila dawa nilikunywa baada ya kuona mimba imepitiliza?”
“Hivi hujawahi kunywa dawa kwa mganga wakati mimba changa wewe! Usije ukafikiri mimi ni mtabiri dada yangu, kuna vitu tu mimi huwa nikiviona nagundua mambo mengi. Jifikirie kuhusu hili nililolisema halafu utakuja kunipa jibu”
Mariam kidogo alikaa kimya na kumwambia Anna,
“Hebu niambie unachoelewa Anna?”
“Hapana dada, tuendelee tu na mambo mengine”
Basi waliendelea kula na baada ya kula sasa ndio Mariam alienda kulala ndani kabisa wala hakutaka kupata muda wa kutafakari wala nini.

Usiku huu Mariam akiwa anaongea na mume wake alikumbuka pia swala aliloongea na Anna mchana kuwa pengine aliwahi kunywa dawa kwa mganga, basi akamuuliza mume wake,
“Hivi kwenye kumbukumbu zako, wakati nina mimba changa nimewahi kwenda kwa mganga?”
“Kivipi mke wangu?”
“Sababu Anna kaniambia kuwa vitu vingine kwa mtoto wangu nimevisababisha mwenyewe”
“Kama vitu gani?”
Mariam alijikuta akiachana na hii habari na kuanza kumuelezea mumewe habari ya Anna,
“Halafu Juma, kumbe Anna ana shida sana usimuone hivyo”
“Kivipi?”
“Yani kumbe ni yatima halafu ndugu zake wamemfukuza na wamegawana mali zote, mama yake alikuwa na mali nyingi sana, tena mama yake alikuwa ni tajiri ila ndugu zake wamegawana kila kitu na kumuacha Anna patupu”
“Dah masikini, lakini ndio binadamu walivyo yani wanaonea sana watoto yatima”
“Yani nimemuhurumia Anna jamani, acha tu nikae nae hapa kama mdogo wangu, nitampenda na nitamtunza”
Juma aliitikia tu, na wote waliachana na kujadiliana habari ya mtoto tena kwani walijikuta wakijadiliana kuhusu Anna tu kwa wakati huo hadi muda wa kulala.

Kulipokucha tu kama kawaida Juma alijiandaa ila alipita kwanza kunywa chai maana ilishaandaliwa tayari ila kiukweli vingi vilivyokuwa vikipikwa alihisi kama ladha ya chakula ambacho mkewe huwa anapika akiamua kupika ila hakusema neno badala yake alimaliza na kuondoka zake kwenda kwenye shughuli zake, ila kabla ya kuondoka Anna alimuuliza tena na leo,
“Shemeji na leo utawahi kurudi?”
“Sijui inategemea, unataka kuniagiza nini?”
“Hamna kitu shemeji nilikuwa nakuuliza tu shemeji yangu”
“Sawa”
Ila kabla hajaondoka vizuri Anna alimwambia tena,
“Shemeji subiri kidogo”
Kisha Anna alikuja na mwamvuli na kumkabidhi Juma huku akimwambia,
“Hali ya hewa ya leo sio nzuri, uwezekano wa mvua kunyesha ni mkubwa sana, bora uende na mwamvuli shemeji”
“Sawa asante”
Juma alibeba ule mwamvuli na kuondoka zake kwenda kwenye shughuli zake.

Juma akiwa ametoka kwenye kazi zake, alifika muda huu nyumbani kwake na kukuta kila kitu kama kawaida kimeshaandaliwa mezani, sasa alienda chumbani na huko alishangaa sana kwani alikuta mkewe akiwa amelala chini halafu miguu yake ikiwa na tope, alishangaa sana ingawa mvua ilinyesha sana siku ile ila ni ngumu kwa mke wake kuwa na tope na ukizingatia huwa hafanyi kazi yoyote, sasa lile tope alitoe wapi? Basi akamshtua Mariam pale chini ila kabla hajamaliza kumshtua alimsikia Anna alimuita,
“Shemeji, shemeji”
Juma akahisi ni shida ya mtoto, hivyobasi alitoka kwa haraka na kwenda kusikiliza kuwa tatizo ni nini, alipofika sebleni alimuuliza Anna,
“Kwani kuna tatizo gani?”
“Hamna tatizo shemeji ila nilikuwa nakuuliza hivi samaki wa mchuzi unakula kweli wewe?”
“Ndio nakula, kwanini umeuliza?”
“Unajua leo tumepika tu samaki wa mchuzi bila mboga nyingine ndiomana nimekuuliza ili kama huli nikupikie mboga nyingine”
“Aaaah sawa, nakula”
Basi Juma aliachana nae na kurudi chumbani ila hakuona umuhimu wa yeye kuitwa na Anna sababu swali lile angemuuliza tu mke wake ambaye anajua kama anakula au hali, basi Juma aliingia chumbani na muda huu alimkuta mkewe amekaa moja kwa moja alimuangalia miguuni kama kuna matope ila alishangaa sana kuona miguu haina matope tena wala nini ila tu Mariam kama kawaida alikuwa akilalamika kuchoka yani hii hali ilianza kumtia mashaka Juma kwakweli, akaona ni vyema apange siku aende kumuuliza mama yake kwani huwa anamuona mama yake kuwa na uelewa wa mambo mengi sana.

Leo Juma alitoka mapema kwenye shughuli zake na moja kwa moja alienda kwao ili kwenda kuzungumza na mama yake kutokana na yale anayoyahisi yeye kwani alianza kumuhisi vibaya Anna, na lile swala la mkewe kuchoka muda wote ndio lililompa mashaka sana.
Basi alifika na kumkuta mama yake yupo kwake kama kawaida, basi alimsalimia na kuanza kuongea nae ambapo swali la kwanza kabisa yule mama alimuuliza Juma,
“Kwanza meshapata mdada wa kazi?”
“Ndio tumepata mama, na hiki ndio kilichofanya nije kwako mama”
“Vipi tena? Na huyo mdada wa kazi kaondoka?”
“Hapana hajaondoka ila kuna mambo sielewi toka yule mdada afike, kwanza yule mdada ni mchapakazi hatari yani anafanya kazi hadi raha, tatizo lipo sehemu moja tu”
“Sehemu gani hiyo tena?”
“Ni hivi, toka aje yule mdada basi mke wangu anachoka sana, mke wangu analalamika kuchoka usiku na mchana, kuna siku mke wangu alikuwa kama amelala ila badae nikamuona analima nje ila badae akageuka na kuwa yule mdada, sasa nahisi huenda yule mdada ni mchawi kwahiyo anamtumikisha mke wangu kwenye kazi za mule ndani”
Kwanza kabisa mama yake Juma akacheka sana na kumuuliza Juma
“Sasa unatakaje?’
“Ndio nimekuja kuomba ushauri kwako mama kuwa nimfukuze yule mdada au nifanye kitu gani, na kama nikimfukuza basi niandalie mdada wa kazi mwingine mama yangu”
Huyu mama alimuangalia kwa makini Juma na kumwambia,
“Hivi akili zako ni nzima kweli Juma? Kama huyo mdada anamtumikisha mkeo basi ni vizuri sana maana mkeo amezidi uvivu jamani, mwanamke gani mvivu kiasi kile? Muache tu akomeshwe, tena huyo mdada usimfukuze wala nini hata usiwaze kumfukuza, nilidhani anakutumikisha wewe kumbe anamtumikisha mke wako, acha tu mke wako atumikishwe maana amezidi sana, mtu gani hata hajielewi yule”
“Kwahiyo mama unaona ni sawa?”
“Kwanza huna ushahidi kama anamtumikisha kweli maana kusema amechoka sio ishara kuwa anatumikishwa na hata kama una ushahidi muache kwanza mkeo apate adabu jamani maana kazidi sana, tena mimi nikija namletea na huyo mdada wenu wa kazi zawadi kabisa, khaaa Mariam anachosha akili na uvivu wake jamani mtu kila kazi afanyiwe, kipindi kile eti sababu katoka kujifungua basi hadi akila vyombo nitoe mimi khaaaa muache tu afundishwe adabu kwanza.”
Juma akaona hakuna sapoti kwa mama yake kabisa ikabidi tu amuage ila mama yake alimkumbusha kitu,
“Hivi mmeshampa mtoto jina?”
“Bado mama”
“Maana jina langu la Ashura mmelikataa, haya mtampa jina gani siku zimeenda”
“Hata sijui tumpe jina gani mama?”
“Nakupa kazi mkajadiliane na mkeo mpate jina la kumpa huyo mtoto wenu”
“Sawa mama nimekuelewa”
Basi kwa muda huu ndio Juma akaondoka zake kuelekea nyumbani kwake.

Juma alivyofika tu nyumbani kwake, kama kawaida alimkuta mkewe akilalamika kuwa amechoka sana tena bila hata ya salamu yani kitu cha kwanza alichokisema Mariam ni kuwa amechoka sana.
Basi Juma alikaa kwanza ila leo alimshangaa mtoto wao kuwa anakaa maana hakuwahi kumuona akikaa, akauliza
“Kumbe mtoto wetu anakaa?”
Ila akashtuka sana baada ya kuona mtoto wao akishuka kwenye kiti na kumfata kwa kutembea.

Itaendelea.....!!!
Kwa mawasiliano 0629980412
 
MTOTO WA MAAJABU: 12

Basi Juma alikaa kwanza ila leo alimshangaa mtoto wao kuwa anakaa maana hakuwahi kumuona akikaa, akauliza
“Kumbe mtoto wetu anakaa?”
Ila akashtuka sana baada ya kuona mtoto wao akishuka kwenye kiti na kumfata kwa kutembea.
Juma alijikuta akisema kwa nguvu tena kwa hali ya uoga,
“Kheeee kumbe na kutembea anatembea!!”
Akatokea Anna pale na kusema,
“Ndio anatembea shemeji, unajua huyu mtoto ni mkubwa kama hivyo mnavyosema kuwa amekaa tumboni miaka miwili, kwahiyo ni mkubwa wa kutosha tu yani huyu ilitakiwa afanye hatua kwa haraka sana hata hivi amechelewa kutokana na chakula mlichokuwa mnampa ila mimi nimeanza kumpa chakula kinachotakiwa basi anakula vizuri na kuendelea na hatua zake na ndio mpaka sasa anatembea”
Juma akapumua kidogo na kuuliza,
“Kwahiyo siku hizi hanywi maziwa?”
“Maziwa anakunywa mara moja moja ila anakula zaidi chakula ambacho tunakula sisi, huyu sio mtoto mdogo shemeji”
Juma alimuangalia mke wake ambaye alikuwa amekaa kimya tu, basi akamuuliza,
“Ulikuwa unajua kama mwanetu anatembea?”
Mariam akajibu,
“Nijue wapi na muda wote nimechoka na kujisikia kulala tu. Yani na mimi nimemuona leo kama ambavyo wewe umemuona”
“Mbona hujashtuka?”
“Sasa unafikiri huko kutembea kunashtua sana? Ngoja siku akuongeleshe ndio utashtuka zaidi na kuamini maneno yangu”
Juma akauliza vizuri kamavile hajawahi kuambiwa swala hili, basi akauliza,
“Kwani anaongea?”
Hapo Anna akamwambia Juma,
“Shemeji, ni vyema uende kula halafu hayo mengine mtajadiliana badae”
Mariam nae akadakia,
“Kweli twende kula, yani nina njaa mimi balaa’
Mariam aliinuka pale, Juma nae alimfata mezani kwenda kula.

Wakati wanakula, Juma akamuuliza Mariam
“Unaonaje ladha ya chakula?”
“Ni kitamu sana”
“Yani mke wangu hiki chakula ni kama umepika wewe”
Mariam ndio kwanza akaanza kumpongeza Anna,
“Mambo ya Anna hayo, huyu mtoto ni hatari kwenye maposhi. Wasichana wangu wa kazi waliopita wote sikuwapenda ila huyu nampenda sana”
“Mmmh, haya bhana”
Yani Juma alimuona mke wake kutokugundua chochote kile, basi moja kwa moja walipomaliza kula aliamua kwenda kulala pamoja na mke wake ila kama kawaida ya Mariam ni kulalamika kuwa amechoka mwanzo mwisho, hadi Juma alitamani kumwambia ukweli kuwa yule msichana wao wa kazi sio mzuri na anamtumikisha ila tu alijikuta akishindwa kumwambia kwanza.
Kwahiyo walilala, na walipoamka asubuhi tu, Juma alijiandaa na kwenda sebleni ambapo chai ilishaandaliwa na leo ziliandaliwa chapati pale mezani pamoja na chai, Juma alikaa na kunywa ile chai ni kweli chapati zilikuwa ni nzuri sana ila bado Juma aliumia kwani aliona wazi kuwa mkewe ndiye ambaye anafanya kazi mule ndani kwa namna ya kutokujijua wala kugundua chochote.
Juma alikunywa chai na kurudi kumuaga mkewe,
“Ila na wewe Mariam punguza kulala basi mke wangu”
“Nachoka sana yani, nitapunguzaje kulala”
“Kwa stahili hiyo sidhani kama tutaweza kumtafuta mdogo wa mtoto wetu”
“Nikiwa sijachoka tutamtafuta tu, usijali mume wangu ila kwa kipindi hiki niache”
“Unajua umekuwa wa ajabu sana! Ni kweli huwa unachelewa kuamka ila siku hizi Mariam unachelewa sana mke wangu”
“Niache nilale bwana, kazi njema”
Juma hakuwa na namna zaidi ya kuondoka zake kwenda kazini.

Muda huu Mariam aliamka na yeye kuoga na kunywa ile chai aliyoandaliwa huku akiendelea kusifia upishi wa Anna kuwa ni wa kiwango kikubwa sana, kisha alikaa kwanza na kuanza kuongea nae,
“Anna mdogo wangu, una mchumba wewe?”
“Mchumba! Hapana dada mimi sina mchumba”
“Mpenzi je?”
“Hapana dada, hayo maswala ya mapenzi siyawezi nimejitenga nayo kabisa, wakati wa udogo wangu nimeshuhudia mambo mengi sana kwahiyo hata sina hamu na mapenzi”
“Umeshuhudia mambo gani?”
“Nina dada yangu, kipindi hiko alikuwa na mwanaume wake na walikuwa wakipendana sana ila kitu ambacho dada hakukijua ni kuwa yule mwanaume alikuwa akimtumia tu yeye, yani hakuwa na upendo wa dhati. Yule mwanaume alionekana kumpenda sana dada sababu kwetu kulikuwa na hela kwahiyo shilingi mbili tatu hazikumpiga chenga dada yangu na kujikuta akijitoa na kumuhudumia yule mwanaume vilivyo, kumbe yule mwanaume ana mwanamke wake, halafu kibaya zaidi mwanamke wa yule mwanaume akaja kuchanganya kaka zangu wawili kimapenzi, toka hapo nikasema mimi kwangu mapenzi hayana nafasi, ni uongo uongo mtupu, kumjua mtu anayekupenda ni kazi sana”
“Ila umesema ukweli mdogo wangu, kumjua mtu anayekupenda ni kazi sana. Halafu unaweza kumpenda mtu ila yeye asikupende na unaweza kupendwa na mtu ila wewe usimpende ndiomana mimi nilivyoona umri unaenda nikawa sina namna tena ni kuolewa tu na yeyote anayeonyesha kunipenda sana, uwiiiii huyu Juma hadi alikuwa analia sababu ya kunipenda mimi yani, ikabidi tu nimkubalie na kuamua kuishi nae. Ila sikumpenda wala nini, nimejifunza kumpenda ndani ya ndoa”
“Kwahiyo siku hizi unampenda?”
Mariam akatabasamu na kusema,
“Siku hizi nampenda maana hapo mwanzoni nilikuwa naona ni kitu gani tena hiki jamani! Kiukweli mwanzoni sikutulia ila saivi nimetulia na ninampenda tu mume wangu. Kwahiyo wewe Anna hutokuja kuolewa?”
“Sijui kama nitaolewa dada, leo hujachoka dada?”
“Kwanini?”
“Hadi muda huu hujaenda kulala?”
“Tena umenikumbusha mdogo wangu, ila leo ngoja nilale hapa hapa sebleni maana nikilala chumbani nalala sana hadi najisahau”
Na kweli kwa muda huo huo Mariam alivuta mto na kulala pale pale sebleni.

Juma akiwa anatoka kwenye shughuli zake alikutana na yule binti ambaye huwa anakutana nae mara kwa mara, yule binti akamsalimia Juma,
“Habari yako baba Mishi”
“Hivi una matatizo gani wewe! Mwanangu hawezi kuitwa Mishi hata iweje”
“Haya, hongera kwa kupata mdada wa kazi”
“Hivi wewe ni mchawi au ni kitu gani? Umejuaje kuwa nimepata mdada wa kazi?”
“Kwa uvivu ule wa mke wako? Mbona ni lazima mpate msaidizi pale kwenu, hongera sana”
“Wewe unajuaje kama mke wangu ni mvivu?”
“Asiyejua kama mkeo ni mvivu ni nani? Mkeo ni mvivu na jamii yote inamfahamu, nilitamani niwe mimi nafanya kazi kwako ila hata yule uleyemuweka nimemfurahia sana, atamnyoosha mke wako”
“Unamaana gani sasa?”
“Huelewi tu nina maana gani? Siku moja usiende kazini halafu utajua kuwa nina maana gani ila hakikisha mkeo unamuamsha mapema sana hata nenda nae nje ukafanye nae zoezi, hata akatae jitahidi umuweze kwa siku hiyo halafu ndio utajua kitu gani namaanisha”
“Mmmmmh au yule binti anamtumikisha mke wangu?”
“Usiniulize hivyo mimi ila nenda mwenyewe kafanye utafiti, mimi yangu nimemaliza sina mambo ya ziada hapa”
“Poa nimekuelewa”
“Haya kwaheri baba Mishi”
“Tena ukome, mimi sio baba Mishi”
Yule binti alicheka na kusema,
“Yani jina atakalokutajia mwanao utaona bora hata ya jina ninalolitaja mimi, utalia nakwambia”
Huyu binti aligeuka na kuondoka zake, yani Juma alimuangalia kwa hasira kidogo kisha na yeye akaondoka zake kurudi nyumbani kwake huku akiwaza kuwa ikiwezekana kesho ndio asiende kwenye shughuli zake ili aweze kubaki nyumbani kwaajili ya kumuangalia mke wake.

Usiku wa leo, Juma aliongea na Mariam kuwa kesho hatoenda kwenye shughuli zake ambapo Mariam alimuuliza,
“Kwanini huendi sasa?”
“Aaaah si nimeamua kupumzika tu”
“Kwanini upumzike kesho?”
“Jamani, kwani kupumzika kuna tatizo Mariam? Kupumzika ni kuamua tu”
“Mimi kesho kuna kitu nataka nikuagize, sasa ukibaki nyumbani ni nani ataenda kuniletea ninachokitaka?”
“Kwani unataka nini?”
“Yani unavyoniona jamani leo kutwa nzima nimejikuta nikitamani kula tende balaa, kwahiyo kesho nenda zako tu mjini ukaninunulie”
“Khaaaa Mariam jamani!”
“Ndio, fanya hivyo”
Juma hakusema kitu na waliamua kulala muda ule ila kama alivyoambiwa kuwa amuamshe mapema alijikuta akichelewa kuamka kwa siku hiyo, basi alipoamka tu aliamua kujiandaa kwaajili ya kwenda kwenye shughuli zake kwahiyo akamwambia tu,
“Nitakuletea hizo tende, niagize chochote kingine unachotaka Mariam”
“Mmmmh sijui na kitu gani kingine, ila niletee hizo hizo tu”
Basi Juma siku hii hata kunywa chai hakujisikia kwakweli, kwahiyo aliondoka zake na kwenda kwenye shughuli zake.

Mariam alipoamka, moja kwa moja alienda kunywa chai kama kawaida yake ila Anna akamwambia,
“Dada ukimaliza kunywa chai naomba twende nje kidogo”
“Sawa, hakuna tatizo”
Kwahiyo Mariam alipomaliza tu kunywa chai, moja kwa moja alitoka nje na Anna ambapo Anna alienda kumuonyesha pale alipokuwa akipanda mahindi kuwa yameanza kutokeza,
“Dada umeona mahindi yalivyoanza kutokeza! Kila kitu ni maamuzi katika maisha”
“Hongera sana Anna kwakweli”
“Na wewe hongera dada”
“Mimi hata sistahili kupewa hongera maana hata wazo hili sikuwa nalo, halafu hata kulima kidogo sijajishughulisha kabisa, kwahiyo mimi hata sistahili kupongezwa”
“Unastahili dada maana wewe ni mwenye nyumba, mahindi yakikua utaanza kula wewe dada”
Mariam alitabasamu na kusema,
“Na ninavyopenda kula yani, hapo hunibandui mbona, nitaanza kula hayo mahindi kama hata kushika jembe najua vile”
Anna na yeye alikuwa akicheka, kwahiyo walijikuta wakiongea na kufurahi kwa muda, kisha Mariam ndio akarudi ndani na kwenda kulala kama kawaida yake ya siku zote.

Juma akiwa antoka kwenye shughuli zake na leo alikutana tena na yule binti ambaye huwa anakutana nae mara kwa mara halafu yule binti akamwambia,
“Unajua nilijua leo ndio ungefanya nilichokwambia ili ujue ukweli”
“Yani leo nimeshindwa kwanza kabisa nimechelewa kuamka halafu mke wangu kaniagiza tende”
“Ulidhani utaweza? Mkeo akikuagiza kitu lazima umpelekee kwani? Mkeo ni mjamzito kusema akikosa atajihisi vibaya? Si anatamani tu, atakula hata siku nyingine. Sikia Juma, nilijua jana ungeomba usaidizi ila wewe ni hamna kitu kwakweli, tena hamna kitu kabisa”
“Kwahiyo ulitaka nikuombe wewe usaidizi? Wewe ni mganga au ni kitu gani?”
Kisha yule binti alitoa mbegu mbili na kumkabidhi Juma huku akimwambia,
“Leo mkienda kulala, weka hizi mbegu mbili chini ya mito yenu kitandani halafu utapata jibu”
“Mmmmh hizi mbegu umenipa mbona ni njegere na mbaazi?”
“Ndio, ni njegere na mbaazi ila kwangu vina maana kubwa sana”
“Maana yake ni nini?”
“Wewe nenda kaweke kama ninavyokwambia halafu ndio utapata jibu, nimetumia tu hizi mbegu ila nina maana kubwa zaidi ya hizi mbegu”
Juma alichukua zile mbegu na kuziweka mfukoni kisha huyu binti akaondoka na kumuacha Juma akimuangalia tu pale mpaka alipoishia ndipo Juma alipoondoka kwenda nyumbani kwake.

Muda wa chakula cha usiku Juma alikuwepo mezani pamoja na Mariam, na Anna wakila chakula cha usiku kwa pamoja huku wakiongea ongea baadhi ya mambo ambapo Anna aliwauliza,
“Jamani hapa hamna mazoea na majirani?”
Mariam akajibu,
“Majirani wa kazi gani? Kazi yao umbea umbea tu”
“Siku ukipatwa na matatizo je mtakimbilia wapi?”
“Tuna ndugu wa kutosha Anna, hatuna haja ya majirani au unasemaje mume wangu?”
Juma akajibu,
“Mimi sina usemi, ila mimi siwezi kufata fata majirani na kuweka ukaribu nao wakati mke wangu hafanyi hivyo, yeye ndiye anayeweza kuwa karibu na majirani, mimi ni mwanaume na yeye ni mwanamke”
Kisha Anna akasema sasa,
“Ila majirani nao mara nyingine hata sio wazuri, mambo yao ni umbea umbea tu kwenye majumba ya watu. Kuangalia watu wanaishi vipi, wanakula nini, kiukweli hata mimi majirani siwapendi, kwanza hawafai kabisa hao majirani jamani”
Mariam hapo ndio alipapenda zaidi na kusema,
“Ndiomana mimi nakupenda sana Anna, wewe mtoto huna mambo ya Kiswahili kabisa. Mimi nafurahi sana wewe umekuja kwetu”
Walitabasamu pale na kuendelea kula.

Wakati wa kulala, Juma alifanya kamavile ambavyo aliongea na yule binti kwani aliweka zile mbegu kwenye godoro lao na kisha kulala na mke wake.
Ila kiukweli ilikuwa ni tofauti sana leo kwani walifanya kazi ya kujigeuza tu na hakuna hata mmoja aliyelala kwa muda ule zaidi ya kujigeuza hadi mwisho wa siku waliamua kuamka na kuanza kuongea,
“Kheeee jamani kuna nini leo mbona siwezi kulala?”
“Hata mimi nashangaa mke wangu, yani kulala nimeshindwa kabisa, hakuna usingizi kabisa hapa”
Walijikuta wakiongea hadi saa kumi na moja alfajiri, basi Juma akamwambia mke wake,
“Unaonaje tukaenda nje kufanya zoezi labda tutaweza kuja kulala”
“Zoezi gani?”
“Twende tukakimbie kimbie mke wangu”
Kiukweli Mariam alichukia sana kwa yeye kushindwa kupata usingizi, kwahiyo alikubali na kwenda nje kufanya zoezi la kukimbia kimbia nje, yani walikuwa wakikimbia taratibu, Juma alifanya vile sababu hakutaka kumchosha sana mke wake.
Waliporudi ndani, walikuwa wamechoka kwahiyo moja kwa moja walienda kuoga ambapo Mariam alisema wakanuwe chai kwanza na ndio waende kulala tena.
Ila ilikuwa tofauti leo kwani walipofika sebleni walikuta Anna hajaandaa chai wala nini mpaka Mariam alimuuliza,
“Anna vipi leo? Hujaandaa chai halafu na usafi bado hujafanya?”
“Yani dada leo sipo vizuri sana, ngoja nikawaandalie chai”
Anna aliwaandalia chai na kuwatengea ila chai ya leo haikuwa na ladha kama chai wanayokunywaga siku zote.
Basi Juma alimuuliza mke wake,
“Unaionaje chai ya leo?”
Mariam akajibu,
“Sio nzuri kama ya siku zote ila nadhani ni sababu Anna anaumwa”
Basi Juma hakusema sana, yani alichotaka Juma ni mkewe kugundua mwenyewe kuwa huwa anatumikishwa na Anna.

Mariam alipotaka kulala sebleni, Juma alimlazimisha kwenda chumbani ili waongee asilale, ila walipokaa kitandani tu ni kweli usingizi wa Mariam ulikata kabisa kwahiyo hakuweza kulala hadi mchana ulifika wakiongea tu, wakatoka kwenda kula na wakakuta ndio Anna anaandaa chakula ila hadi Mariam alisikitika kwa kile chakula kwakweli na kumsema Anna,
“Jamani mdogo wangu, hata huu ugali haujaiva kwakweli”
“Dada, sipo vizuri hata chakula cha jioni itabidi unisaidie tu”
“Mmmmh mimi huyo na uvivu huu!! Hapana kwakweli, siwezi kupika Anna, jitahidi tu”
Juma akasema,
“Tena jioni naomba mniandalie pilau”
Mariam akamwangalia Anna na kumwambia,
“Umesikia ambacho baba amesema eeeh!!”
Anna akaitikia tu yani hakuwa na namna yoyote ile.

Jioni ilipofika, Juma alikuwa chumbani na mke wake alishangaa tu akipigiwa simu na mtu ambaye wanafahamiana sana, mtu yule alisema kuwa yupo stendi anataka kufika nyumbani kwao,
“Basi nakuja kukufata, nisubiri tu hapo hapo stendi”
Ikabidi Juma amuage mke wake na atoke kwa muda huo ila alitoka akiwa na mashaka sana.
Juma alifika stendi ila hakumuona yule mtu wala nini, alimpigia simu ila hakumpata hewani ikabidi tu aamue kurudi nyumbani ila alipofika tu nyumbani ni moja kwa moja alienda jikoni kwani alikuwa na mashaka sana, alishangaa sana kufika jikoni kumkuta mkewe wake akiendelea na mapishi ya chakula cha usiku.

Itaendelea…..!!!
Kwa mawasiliano 06229980412
 
MTOTO WA MAAJABU: 13

Juma alifika stendi ila hakumuona yule mtu wala nini, alimpigia simu ila hakumpata hewani ikabidi tu aamue kurudi nyumbani ila alipofika tu nyumbani ni moja kwa moja alienda jikoni kwani alikuwa na mashaka sana, alishangaa sana kufika jikoni kumkuta mkewe wake akiendelea na mapishi ya chakula cha usiku.
Kwakweli alishangaa sana ukizingatia mke wake alishasema kuwa hatopika chakula kwa siku hiyo, hapo ndio akajua ni muda wa kumkamata Anna na uchawi wake, basi hakwenda chumbani kuangalia kama mkewe kalala au la bali alimuongelesha pale pale alipokuwa anapika,
“Weee Mariam wewe”
Mkewe aligeuka na kumuangali, kisha Juma akataka kumuuliza ila kabla hajamuuliza kitu Mariam alimuagiza pale pale,
“Hebu niletee hotpot hapo nipakulie hiki chakula”
Juma alikuwa akishangaa tu, na kwenda kumpatia alichokuwa akihitaji, baada ya hapo Juma aliendelea kumuangalia Mariam ambaye alipakua kile chakula na kumtaka Juma mwenyewe ndio akakitenge kile chakula mezani ili waweze kula, yani kwakweli Juma alikuwa akishangaa sana basi akabeba na kupeleka mezani kisha Mariam nae akaenda na kumuita Anna, ila Anna alisogea pale na kupakua chakula kwenye sahani kwanza na kwenda kumlisha mtoto, yani Juma alijikuta akishangaa kila kitu na kuuliza,
“Inamaana siku hizi huyo mtoto anakula chakula ambacho kinaliwa na wakubwa?”
Mariam akajibu,
“Mbona nilishakwambia jamani Juma! Siku hizi mtoto wetu yupo vizuri, kumbe maziwa yale ndio yalimfanya azembee, saivi anakula hiki chakula anakuwa na nguvu unaona hata uliweza kumuona akiinuka na kutembea”
“Kheeee kumbe!!”
“Ndio hivyo, karibu mezani tule mume wangu”
Basi Juma alikaa pale na kuanza kula, ila kiukweli alikuwa na maswali mengi sana hadi hakujielewa kabisa, alijikuta akijiuliza mambo mengi sana na kukosa jibu kabisa kwa chochote alichokuwa akijiuliza.

Usiku ule walipolala Juma na Mariam, ilibidi Juma amuulize maswali mke wake maana bado alikuwa haelewi kitu,
“Nakumbuka mara ya mwisho wakati Anna anakwambia kuwa utapika chakula cha usiku ulimkatalia kabisa, imekuwaje ukapika?”
“Mmmh mume wangu, hata mimi ni binadamu eti lazima niwe na huruma. Mtu kasema kuwa anaumwa nikaona hakuna namna zaidi ya mimi kujitoa tu na kwenda kupika”
“Duh!! Halafu mbona mimi kwenda tu hapo stendi kumfata mgeni narudi nakuta umeshaivisha, hivi ndio pilau linaiva kwa muda mfupi hivyo?”
“Tena bora umenikumbusha, haya huyo mgeni uliyesema unamfata yuko wapi?”
“Sikumkuta halafu simu yake haipatikani, ila bado swali langu hujajibu Mariam, ndio pilau linaiva kwa muda mfupi hivyo?”
“Unajua Juma usitake kujigelesha, kama una mwanamke mwingine ni bora useme tu. Yani hapo huna hata aibu eti unauliza pilau linaiva kwa muda mfupi, hebu angalia muda, umeondoka muda gani na umerudi muda gani ndio uulize swala la pilau kuiva kwa muda mfupi”
“Kwani nilikawia kurudi?”
“Usiniulize mimi, hapo jiulize mwenyewe yani. Mimi nimeongea na Anna, tumeanza kupika na kumaliza eti wewe ndio unarudi halafu bila aibu muda huu unanijibu kuwa mgeni uliyemfata hukumkuta jamani!”
Juma akaona hapo atazua marumbano mengine yasiyokuwa na maana yoyote ile, basi akamuomba mke wake waache kurumbana kwa muda huo na waweze kulala.
Basi wakaamua kulala kwa muda huo ila kilichofanyika walijikuta wakijigeuza tu kitandani, hakuna hata mmoja aliyepatwa na usingizi hadi muda panakucha kabisa, walijigeuza tu hawakuweza kulala wala nini.
Kulipokucha, Mariam alilalamika mno,
“Nilikuwa nalala sana hapo awali, ila kwanini kwasasa siwezi kulala? Ni kitu gani kinatokea jamani kwenye usingizi wangu?”
“Hata na mimi sielewi jamani, sijui ni kitu gani ambacho kinatokea hadi kusababisha hali kama hiyo mke wangu”
Basi siku ya leo Juma hakwenda popote tena na alidhani kuwa itakuwa ndio siku nzuri ya kumbamba Anna maana na leo atafanyaje kazi? Wakati yeye yupo! Basi Juma akatulia nyumbani pia.

Mariam aliinuka na kutoka, alikuta Anna hajasafisha nyumba na hakuna chochote alichokifanya, vyombo vilikuwepo jikoni vichafu tu, basi Mariam alimfata Anna chumbani kwake ambapo alikuwa bado amelala,
“Anna vipi wewe?”
“Naumwa sana dada”
“Pole sana, kwahiyo itabidi kwenda hospitali?”
“Ni gharama nyingine hospitali dada, acha tu niangalie angalie hali yangu”
“Kumbe ndiomana hujaweza fanya chochote!”
“Ndio dada, naumwa sana”
Basi Mariam hakuwa na jinsi zaidi ya kwenda kubandika chai na kuja kunywa, ila kwenye swala la chai hapo, Anna na yeye alishiriki kunywa na vile vile alishiriki kumpatia mtoto wao ile chai, kisha Juma akauliza,
“Sasa itakuwaje maana hapa hakuna kinachofanyika?”
Mariam akamtazama Anna ambapo Anna akamwambia Mariam,
“Dada, nakuomba twende tukaongee kidogo”
Basi Mariam alitoka nje na Anna ili amsikilize ni kitu gani ambacho Anna alitaka kusema,
“Dada, kwakweli mimi sina hali nzuri toka jana nilikwambia ila kuna dawa nikiipata nitakuwa mzima kabisa”
“Dawa gani?”
“Natakiwa nipate mchicha wa kuchemsha halafu nitakunywa kwa mara tatu yani asubuhi hii, mchana na jioni”
Kisha Anna akataka kuendelea kuongea ila Mariam alimkatisha na kumwambia,
“Hapana Anna usiendelee, ngoja kwanza nikamuagize Juma ili akatupatie huo mchicha, sipendi uteseke mdogo wangu”
Muda ule ule Mariam alienda kuongea na Juma na kumwambia awaletee huo mchicha, Juma akamwambia mkewe,
“Yani hadi sasa hakuna ulichogundua Mariam?”
“Kugundua kitu gani? Kwani mchicha una nini? Ni mboga ya kawaida inayoshauriwa katika maisha ya kila siku”
Basi Juma akaondoka kwenda kununua hiyo mboga, kisha Mariam akarudi kuongea na Anna maana Anna alisema kuwa atakaa juani muda huo ili kupata jua la asubuhi pengine akapata hali nzuri,
“Haya mdogo wangu tuendelee”
“Dada, kama nilivyokueleza matatizo yangu. Hapa nilipo sina hata pa kwenda, hivi shemeji akinifukuza nitakimbilia wapi mimi!”
“Na kwanini akufukuze?”
“Sababu ataona sifanyi tena kazi kama mwanzoni”
“Mdogo wangu, huo ni ugonjwa tu na inajulikana. Kila mtu katika maisha lazima ataugua, kuumwa ni ibada mdogo wangu. Usijali, utapona tu”
“Ila dada hata kupika sitaweza na ninajua na wewe dada yangu kupika huwezi ndiomana nina mashaka kuwa shemeji anaweza nifukuza kazi”
“Usijali mdogo wangu, nitajitahidi mchana nipike chakula cha moja kwa moja hadi jioni ila kuhusu vyombo nadhani utaosha tu ukipona”
“Dah!! Nashukuru sana dada yangu, nakushukuru sana sana. Wewe umekuwa ni ndugu yangu sasa”
“Usijali Anna, mimi nakupenda sana mdogo wangu. Usiwe na wasiwasi wala tatizo lolote lile mdogo wangu”
“Nakupenda pia dada yangu”
Basi Anna alimkumbatia Mariam na kufurahi sana pamoja kwa muda ule.

Juma aliporudi na ule mchicha, ni mke wake ndio aliingia jikoni kuchemsha ule mchicha halafu ni mke wake ndiye aliyepika chakula cha siku hiyo, yani Juma alibaki akishangaa tu maana uvivu wa mke wake aliuelewa vizuri sana, akajiuliza kuwa uvivu wa mkewe umeenda wapi hakupata jibu ila walikaa pamoja na kula chakula huku Mariam akilalamika sana kushindwa kulala kabisa, na wala usingizi ulikuwa haumpati na muda huu akamwambia mume wake,
“Hivi unajua ni siku mbili hatujalala?”
Anna akauliza,
“Kwanini hamlali?”
“Yani usingizi hauji tu sijui kwanini”
Anna akasema tena,
“Labda kuna kitu chumbani kwenu, haswa kwenye godoro lenu, mnatakiwa kuchunguza ni kitu gani maana kutokulala nako ni ugonjwa mkubwa sana”
Juma akakumbuka kuhusu zile mbegu ambazo aliziweka chini ya godoro lao kwahiyo alipanga usiku wa siku hiyo akazitoe zile mbegu ili waweze kulala.

Na kweli usiku ulipofika, Juma alienda kutoa zile mbegu na kuzitupa nje kisha yeye na mkewe wakaenda kulala, yani hapo hawakuongea kitu chochote kwani ni moja kwa moja walijikuta wamelala tena walilala usingizi mzito sana.
Kuja kushtuka ilikuwa ni saa kumi jioni, yani waliamka wakiwa na uchovu wa usingizi bado, Juma alikaa na kuwaza sana,
“Yani toka jana ndio tumelala hadi muda huu!”
Mariam na yeye akaamka, huku akijinyoosha nyoosha na kumuuliza mume wake,
“Kwani saa ngapi saa hizi?”
“Saa kumi jioni”
“Au tuliamka halafu tukalala tena!”
“Sidhani kama tuliamka, hii inaonyesha ni tangia tulivyolala jana usiku”
Basi Mariam aliona waende kwanza kuoga ili kuondoa ule uchovu wa usingizi, na ndipo walipoenda sebleni ambapo Anna alikuwepo akimlisha mtoto, basi Anna aliwasalimia na Mariam alimuuliza Anna,
“Eti tuliamka asubuhi halafu tukaenda kulala tena?”
“Hapana dada, toka mlivyolala jana usiku ndio mmeamka muda huu”
Mariam alimuangalia mume wake na kumuuliza,
“Juma uliweka nini chumbani kwani?”
Juma hakujibu ila aliwaza sana, badala ya mchawi kuonekana ni Anna ila anaonekana ni yeye tena! Hakujibu kitu kwakweli, Anna aliwakaribisha mezani ili wapate kula na moja kwa moja Juma alihisi tu kuwa kile chakula kimepikwa na mke wake, ingawa hakuwa na cha kufanya zaidi ya kwenda kula tu.

Kabla ya kwenda kulala tena, Mariam aliamua kupitia nyumba yake na kukuta kote kumefanyiwa usafi vizuri kabisa, basi akasema,
“Kweli Anna ulikuwa unaumwa mdogo wangu, leo umefanya usafi mwenyewe wote kabisa. Chumbani kwangu utasafisha kesho Anna”
“Sawa dada, hakuna tatizo”
Basi moja kwa moja Mariam alienda na mume wake chumbani kwaajili ya kulala, hapa kabla ya kulala Juma alimuhoji kwanza mke wake ili kujua kuwa anaonaje kile kilichotokea,
“Mke wangu, hivi hili swala la sisi kulala jana na kuamka leo saa kumi jioni unalionaje?”
“Yani mimi hili halinishangazi sana sababu hatujalala kwa siku mbili, inawezekana ikawa ndio sababu ya sisi kulala usingizi mzito kiasi hiko. Ila tu najiuliza, ni kwanini tulishindwa kulala kwa siku mbili! Uliweka nini chumbani mume wangu, maana Anna aliposema ulikuja kutoa usiku wa jana na ndio kukafanya tuweze kulala. Ni kitu gani uliweka?”
“Sikuweka uchawi wala uganga ila tu nilitaka wewe ugundue”
“Nigundue nini?”
“Nilitaka ugundue kuwa kuna mtu anakuroga”
“Weee, sirogeki kizembe hivyo mimi. Umesahau kuwa mimi sirogeki? Hata wewe mwenyewe huwezi kuniroga mimi, mara ya mwisho nadhani ni hiyo mimba tu ndio walifanikiwa kuniroga ila mimi sirogeki kirahisi”
“Haya umeshinda Mariam, ila kiukweli huyu Anna mimi simpendi kabisa”
“Kama humpendi shauri yako, ila mimi nampenda sana”
Juma hakutaka marumbano na mke wake kwahiyo aliamua kulala tu kwa muda huo na walilala vizuri kabisa.

Kulipokucha, leo Juma alijiandaa na kwenda kwenye shughuli zake ambapo hakwenda kwa takribani siku tatu ili aweze kumbamba Anna, ila hakuweza maana Anna alifanikiwa kuwaambia kuwa yeye ni mgonjwa, hiko kitu kilimchukiza sana ila hakuwa na la kufanya.
Nyumbani kama kawaida alibaki Mariam na msichana wake wa kazi Anna pamoja na mtoto, na kama kawaida ile ratiba ya Mariam kulala sana ilijirudia na alipoamka alikula tu na kurudi tena kulala na mara nyingine alilala pale sebleni kwa kuona uvivu kwenda chumbani.
Jioni ya siku hii, Mariam alikaa na Anna na kuanza kuongea mambo mbalimbali ambapo Mariam alimuuliza Anna,
“Hivi unaamini kwenye swala la uchawi?”
Anna akashtuka na kusema,
“Uchawi?”
“Ndio uchawi”
“Mimi huwa nasikia tu kuwa kuna uchawi ila kiukweli huwa siamini kabisa mambo ya kichawi”
“Hujawahi kurogwa wewe?”
“Sijawahi ingawa nahisi baba yangu ndio amerogwa ili asinitake mtoto wake”
“Basi huo ndio uchawi Anna, ila mimi nilipewa kinga hiyo hatari na siwezi kurogwa kabisa”
“Kwahiyo na nyumba yenu mliweka kinga?”
“Ndio, kuna mganga alikuja hapa na tulifukia kichw acha mbuzi hapo mlangoni kwaajili ya kinga, basi hatuwezi kurogwa kabisa”
Anna akacheka, Mariam alimshangaa na kumuuliza,
“Mbona unacheka Anna?”
“Unajua nini dada, waganga wengi ni waongo sana. Na usipokuwa makini utakuwa mtumwa wao”
“Sasa unanishauri nini Anna? Maana maisha haya bila kujiganga jamani ni kazi bure”
“Mimi sijui ila sijawahi kujiganga, sema tu huwa naona waganga waongo. Sema inawezekana wa kwenu akawa mkweli”
“Ni mkweli ndio, tulifukia kichwa cha mbuzi mlangoni”
Hapa Anna hakuendelea tena na mada hii kwani alibadilisha mada na kuendelea na maongezi mengine.

Juma alirudi usiku maana siku hii alichelewa kurudi, kwahiyo moja kwa moja alienda kula na aliposhiba tu aliamua kwenda kulala sababu alikuwa amechoka na kazi zake, ila kama kawaida mkewe na yeye alimlalamikia kuwa amechoka sana siku hii ya leo yani Juma aliweza kutambua kuwa yale yale ya kipindi kile yamerudi tena.
Basi leo walilala tu huku Juma akiwaza sana kuwa ni kitu gani afanye maana nia yake kubwa ni kumuumbua Anna halafu mkewe amtambue na amfukuze mwenyewe, yeye binafsi ameshahisi kuwa kuna jambo sio jema linaloendelea kwa Anna kwenye nyumba yake basi aliwaza sana kwa usiku ule ila kuna mahali ambapo aliwaza kuwa atapata usaidizi wa haraka sana, akawaza kuwa mahali hapo aende kesho yake.
Kulipokucha, leo na Mariam na yeye aliamka ila chai ilikuwa tayari imeshatengwa mezani kwahiyo ilibidi Juma anywe kwanza chai kabla ya kuondoka nyumbani kwake.
Wakati anaondoka alimwambia mke wake,
“Unatakiwa kuwa mwangalifu sana humu ndani Mariam”
“Kwani mimi sio muangalifu jamani!”
“Hapana, nimekwambia maana wewe unapenda kulala sana”
“Au unahisi Anna anweza kutuibia? Aibie nini humu ndani? Kuna kipi cha kuibiwa?”
“Khaaaa ila mke wangu mara nyingine una dharau sana jamani”
“Sio dharau, au abebe hiyo friji? Anaweza kuibeba? Hebu tusitake kumtia dhambi mtoto wa watu kwa kumuwaza vibaya”
Basi Juma aliondoka zake tu kwa muda huo.

Moja kwa moja Juma alienda kwa mganga wa kienyeji kama ambavyo wazo lake lilikuwa likifanya kazi, alivyofika pale alisubiria na kwenda kuhudumiwa yeye ambapo yule mganga akkamwambia,
“Nimeshajua tatizo lako, umekuja hapa ili mkeo aweze kugundua kuwa mdada wa kazi mnayeishi nae ndani ni mchawi”
“Ndio yani hilo ndio lengo langu kubwa”
“Sijui nani kakuonyesha hapa?”
“Ni rafiki yangu, alishawahi kuniambia kuhusu wewe na ndiomana nimekuja moja kwa moja”
“Sawa, umefika kwenye suluhisho”
Kisha Juma alimuuliza yule mganga,
“Niambie kwanza, yule binti ni mchawi au sio mchawi?”
Yule mganga akacheka na kusema,
“Kumbe hata wewe huna uhakika na wazo lako?”
“Sina uhakika ndio ila kuna kila ishara kuwa ni mchawi”
“Sawa, mimi sitakujibu ila hii dawa ndio itakayowajibu wewe na mkeo kuwa mdada wenu wa kazi ni mchawi au sio mchawi”
Kisha yule mganga akamwambia Juma,
“Kwanza weka hapo salimia babu halafu nikupe dawa”
“Salimia babu ndio nini?”
“Ni hela, elfu ishirini ndio salimia babu”
Juma alitoa hizo hela na kuweka sehemu aliyoelekezwa, kisha yule mganga alitoa dawa kama ya unga unga hivi na kumwambia Juma,
“Subiri wote wakiwa wameenda kulala, halafu wewe utaamka na kwenda kwenye mlango wenu wa kutokea ndani kwenda nje yani hutoki nje ila utaweka hiyo dawa hapo utainyunyuzia ila kabla hujainyunyizia unatakiwa kunuizia maneno ambapo utasema kuwa mchawi yoyote humu ndani agande hapa, halafu asubuhi mtamkuta ameganda ila tu hakikisha wakati unaweka hiyo dawa hakuna mtu yoyote wa kukushika mguu”
Juma aliona sharti hilo ni rahisi sana maana mule ndani kwake ni nani wa kumshika kwenye huo muda wa usiku? Ukizingatia mkewe anapenda sana kulala kwahiyo lazima atakuwa amelala kwa muda huo.
Juma alimshukuru yule mganga na kuondoka zake na ile dawa kwenda nyumbani kwake.

Yani Juma alikuwepo nyumbani kwake ila alikuwa akingoja tu usiku ufike ili aweze kuifanya ile dawa yake, na walipomaliza kula chakula cha usiku kama kawaida wote waliinuka na kwenda kulala pamoja na yeye mwenyewe Juma.
Kwenye mida ya saa tano usiku, Juma alienda na ile dawa hadi mlangoni, kisha akanuiza maneno yake na kutaka kuinyunyizia ila alishangaa kushikwa mguuni, alishtuka sana na kuangalia ni nani kamshika! Alishangaa kuona ni mtoto wao ndio kamshika.

Itaendelea…..!!!
Kwa mawasiliano 0629980412
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom