Sehemu ya 116
“Kivipi na wakati uliniambia huna mwanaume yeyote yule?” aliuliza John.
“Naomba unisamehe!”
“Amanda! Kama kweli uliweza kunidanganya kwa jambo hili, utaweza kuniambia ukweli kwa mengine? Leo ulipanga kwenda kulala kwa huyo Martin, hivi kuna kuachana hapa kweli? Amanda! Hapana kwa kweli!” alisema John, hapohapo akasimama, akamuita mhudumu na kuomba bili yake mezani.
Muda huo Amanda alikuwa akilia tu, hakuamini kama kweli rafiki yake huyo alimpotezea mpenzi wake aliyekuwa na mapenzi ya dhati kwake.
Christina hakujali, kwake kila kitu kilikuwa poa kabisa. Hakujiona kuwa na kosa kwani hata kama angeulizwa, angesema tu kuwa alikutana na mwanaume njiani, akamtongoza na ikawa hivyo, kosa la Amanda ni kwamba hakuwahi kumuonyesha mpenzi wake, hivyo hakujua.
John alikuwa kimya, alijizuia kutokupiga kelele, hoteli hiyo ilikuwa na watu wenye heshima zao, hivyo hataka kama angetiwa hasira kwa namna yoyote ile asingethubutu kupayuka.
Moyo wake ulimuuma mno, hakuamini mwanamke aliyekuwa akimuonyesha mapenzi yote, kumbe usiku huo alipanga kwenda kulala na mwanaume mwingine, moyo ulichoma kupita kawaida. Mhudumu akaleta bili yake, akaichukua, akaisoma na kumlipa.
“Twende nikurudishe nyumbani!” alisema John huku akisimama na kuelekea ndani ya gari lake, Amanda akafuata.
John hakuzungumza kitu, japokuwa msichana huyo alikuwa akiomba sana msamaha ndani ya gari lakini hakuongea chochote kile.
Alichokigundua msichana huyo hakumpenda, alikuwa na mwanaume mwingine, kama kweli alipanga kwenda kulala naye, basi mapenzi hayakuwa kwake kabisa.
Walitumia dakika kadhaa mpaka kufika kwao, akasimamisha gari na kumtaka ateremke.
“Naomba unisamehe John mpenzi! Najua nimeko....”
“Naomba uteremke garini! Tutaongea kesho!” alisema John, tayari macho yake yalikuwa mekundu mno.
Kwa upole, Amanda akateremka ndani ya gari! John hakutaka kubaki, akaondoka zake mahali hapo, Amanda akaanza kulia kama mtoto, hakuamini kama John aliamua kumuacha, lawama zake zote zikawa kwa rafiki yake, hata urafiki wenyewe ukawa na dalili ya kufa.