SEHEMU YA 18
“Kuna nini tena baby, kwanini mumeo anakuwa na swaga za kishamba namna hii, anakukoseshaje dili kubwa kama hivi?”Abdul Ally aliongea kwa lafudhi za vijana wa kileo.
Nilijisikia vibaya sana mtu yule kuniita mshamba mbele ya mke wangu, kwa kuwa simu ilikuwa imewekwa ‘loud speker’ niliichukua kisha tukaanza kutupiana maneno na mwanamuziki yule maarufu.
Tulitukanana matusi ya nguoni hadi simu ilipokatika kwa kuishiwa salio, kwa kweli siku hiyo iligeuka na kuwa siku mbaya mno. ***** Masiku yalikatika, angalau amani na furaha ikaendelea kudumu kwenye ndoa yangu. mawasiliano kati ya mke wangu na Abdul Ally yalikufa.
Mke wangu akazidi kuwa mwaminifu, akawa mchamungu, upendo na heshima dhidi yangu ilikuwa haina mafano, urembo wake ukabakia kuwa mali yangu, nilinenepa, dunia yote ikawa yangu. Miezi michache badaye, mke wangu alinasa ujauzito, jambo hilo lilizidisha furaha kubwa katika ndoa yangu.
Nilifuarahi kuona siku moja ningeitwa baba, sikujali ni mtoto gani angezaliwa, kwangu mtoto wa jinsia yeyote nilikuwa tayari kumpokea kwa mikono miwili.
Niliona siku zinakwenda taratibu, shauku ya kupata mtoto ilikuwa kubwa, mapenzi kwa mke wangu yalizidi maradufu.
Sikupenda hata mara moja kuona mwanamke yule anaingia kwenye mkanganyiko wowote katika nyakati zile za kulea mimba. Siku zilienda, waswahili wanasema ‘ndondo si chururu’ Baada ya kusubiri hatimaye miezi tisa ilitimia.
Usiku mmoja mke wangu alipatwa na uchungu, upesi mimi na mdogo wake Aisha tukamwingiza kwenye gari langu na kumwahisha Hospitali ya Regency.
Baada ya kuwasili, manesi walitupokea mbiombio, kwakuwa hali yake ilikuwa mbaya, alipelekwa moja kwa moja leba.
Mimi na Aisha tuliibakia nje kwenye benchi, mbele ya mlango wa kuingilia katika chumba ambacho mke wangu Nasra aliingizwa.
Tulisubiri pale kwa muda mrefu sana, nakumbuka karibu masaa matatu tulikuwa nje ya wodi ile.