NA MARY VICTOR
MBUNGE wa Maswa Magharibi (Chadema), John Shibuda, amekanusha madai ya kukihama chama hicho na kujigamba kwamba yeye ni sawa na Nyambizi ya kisiasa isiyozama.
Akizungumza na Raia Tanzania katika mahojiano kwa njia ya simu jana, Shibuda alisema tangu juzi amekuwa akipokea simu zikimuuliza kuhusiana na taarifa ya yeye kuchukua uamuzi wa kujiuzulu ubunge ndani ya chama hicho, taarifa alizosema zinasambazwa na wabaya wake.
Kwa mujibu wa uvumi ulionea katika baadhi ya mitandao ya kijamii juzi na jana, ilielezwa kwamba Shibuda ameandika barua Chadema kuomba kujiuzulu kutokana na chama hicho kumtenga na kushindwa kumpa ushirikiano katika shughuli za kichama .
Hata hivyo, katika mahojiano yake na gazeti hili, Shibuda alisema; Taarifa zote hizo zinazoenezwa dhidi yangu hazina mnyumbuliko wa upembuzi yakinifu bali ni taarifa ya mnyukano wa fikra mnyauko wa genge lenye mawazo yaliyopauka.
Napenda kuwaambia Watanzania kwamba waepukane na waumini wa kuabudu dini ya mapepo wa uongo ambao ni jiko la uzushi. Napenda kusisitiza kwamba uvumi huu ni fikra chakavu, mimi bado ni Mbunge wa Chadema.
Sijaandika barua ya kuomba kujiuzulu, watu wamekuwa wakipiga ramli ya maisha ya Shibuda na ni vema wanaotaka kujua waniulize mwenyewe. Shibuda ni nyambizi ya kisiasa, meli iliyo chini ya bahari isiyozama na ikiibuka inafanya operesheni tokomeza.
Wakati Shibuda akifafanua hayo, Ofisa Habari Mwandamizi wa Chadema, Tumaini Makene, amesema Hatujaona barua yoyote, kama watu wamevumisha kwamba Mabere Marando na John Mnyika wamejizulu itakuwa kwa Shibuda ?aliuliza Makene.
Mwingine aliyevumishiwa kuhama ndani ya chama hicho ni pamoja na mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Profesa Abdallah Safari, ambaye naye katika mahojiano na Raia Tanzania hivi karibuni alisema; Huo ni uongo mkubwa. Sina mpango wa kuondoka katika chama na sitegemei kuondoka na siku nikiamua kuondoka ndani ya Chadema, nitaamua kurudi kwetu Nyanguge kuchimba almasi.
Wakati huo huo, Shibuda amewataka baadhi ya wabunge kutonganania majimbo ya uchaguzi kutokana na kwamba hakuna mwenye hatimiliki; Mwenye kutaka kuja kugombea Maswa wakati ukifika, aje, sina hatimiliki, nawashangaa wabunge wanaolalamika kuingiliwa katika majimbo.
Hakuna mwenye hati miliki na jimbo lolote, mikataba yetu ya kuwatumikia wananchi ni miaka mitano, utumishi wa kibunge ni miaka mitano, hivyo kila mwananchi ali mradi awe ametimiza vigezo, ana haki ya kufanya kampeni katika jimbo lolote, wakati ukifika,alisema Shibuda.
Mwisho.