Na Muhibu Said
WAUMINI wa Msikiti wa Kwa Mtoro, jijini Dar es Salaam, wamefanya mapinduzi kwa kuuondoa uongozi wa aliyekuwa Imamu Msaidizi wa Msikiti huo, Sheikh Khalifa Khamisi na kuuweka madarakani uongozi mpya.
Mapinduzi hayo yalifanyika Ijumaa wiki iliyopita baada ya waumini wa msikiti huo kudai kuchoshwa na kile walichokiita "ubadhirifu wa mali za msikiti", ikiwamo michango ya sadaka za waumini, kunakodaiwa kufanywa na uongozi wa Sheikh Khalifa kwa kutumia msikiti huo.
Akizungumza na Mwananchi msikitini hapo jana, kiongozi wa mapinduzi hayo, Sheikh Ali Zilinde alisema waumini hao wanautuhumu pia uongozi wa Sheikh Khalifa kuwa kutoa kauli za kuwagawa waumini na kuwa na tabia za kuwahamasisha waumini kutekeleza jambo fulani, lakini muda wa kutekeleza unapowadia, wanakuwa 'ndumilakuwili'.
Kutokana na hali hiyo, Zilinde ambaye pia ni Naibu Imamu wa uongozi mpya wa msikiti huo, alisema baada ya waumini kuchoshwa na mwenendo huo ndipo wakaamua kuuondoa madarakani uongozi wa Sheikh Khalifa na kuteua uongozi mpya.
Alipoulizwa na Mwananchi jana, Sheikh Khalifa aliyaita mapinduzi hayo kuwa ni uvamizi na kusema kuwa wanayatafakari kwa kina na kwamba, watatoa maelezo yao baada ya kukutana na viongozi wenzake waliong'olewa madarakani.
"Kwa sasa hatujawa tayari kuzungumza lolote. Bado hatujakutana, tunataraji kukutana katika siku mbili-tatu zijazo. Tutazungumzia kuhusu huo uvamizi na tutatoa maelezo juu ya uhalali wetu wa kuwa viongozi wa msikiti," alisema Sheikh Khalifa.
Uongozi huo mpya uliotangazwa Jumatatu wiki hii, una wajumbe tisa wa kamati ya msikiti, wakiwamo maimamu saba.
Tangu uongozi mpya uingie madarakani, polisi wamekuwa wakifanya doria katika msikiti huo kila inapofika muda wa sala.
Mbali na Sheikh Khalifa, viongozi wengine waliong'olewa madarakani, ni Imamu Mkuu, Seif Gulu, Mwenyekiti wa kamati ya msikiti, aliyefahamika kwa jina moja la Mbelwa na Makamu wake wa kamati hiyo, aliyefahamika pia kwa jina moja la Kabunju.
Wengine, ni Katibu Mkuu, Rajabu Katimba na Naibu wake, aliyefahamika kwa jina moja la Kivura, Yasin Abeid (Mjumbe), Athumani Mkambaku (Mjumbe) na Bakari Malungulu (Mjumbe).
Maimamu walioteuliwa katika uongozi mpya wa msikiti huo, ni pamoja na Sheikh Zubeir Juma (Imamu Mkuu), Sheikh Juma Ngara "Mpakistan", Sheikh Abdallah Mohamed, Sheikh Abbas Ramadhani Abbas na Sheikh Zilinde.
Wengine, ni Katibu Mkuu, Ibrahim Khamis na Naibu wake, Nassir Hassan, Juma Chuli (Mjumbe), Ahmad Rashid Said (Mjumbe), Hamad Rashid (Askofu-Mjumbe) na Mgeni Bofu (Mweka Hazina).
Mimi sielewi huwa wanapinduana kwa sababu zipi? Ulaji,Mungu kawaagiza au sababu binafsi?Hawa kama wanasiasa tu
Source:http://www.mwananchi.co.tz/newsre.asp?id=3052
kahtaan,
Umetoka kufanya vurugu Misri hujaridhika umeanza kufanya mapinduzi kwenye misikiti ya bongo?