Shambulio la damu

NYEMO CHILONGANI
SHAMBULIO LA DAMU
0718069269

Sehemu ya Tisa.

HISTORIA YA MTU WA PILI KATI YA WALE WATANO ILIYOMFANYA KUWA NDANI YA NDEGE HIYO.

Mtu wa Pili Ndani ya Ndege.
“Guys, tell me what the hell is going on,” (jamani niambieni kitu gani kinaendelea) alisikika mwanaume mmoja aliyeitwa Sam Scott kutoka katika ofisi ya ndani kabisa katika jengo la makao makuu ya Shirika la Kijasusi nchini Marekani, CIA (Central Intelligence Agency) yaliyokuwa Langley, Virginia, McLean, Virginia nchini Marekani.
“The president calls the press,” (rais amewaita waandishi wa habari) alisema mwanaume mwingine kwenye simu.
“I want to get the feedback as soon as possible,” (nataka kupata kinachoendelea haraka iwezekanavyo) alisema Scott na kukata simu.
Dunia nzima ilikuwa bize kusikilizia kile kilichokuwa kikiendelea nchini Iraq. Watu walitega masikio yao, walihitaji kujua sababu ya rais wa nchi hiyo, Sharif Hamis kuwaita waandishi wa habari na kutaka kuzungumza nao.
Kila mmoja alimfahamu rais huyo, alikuwa miongoni mwa marais viburi waliowahi kutokea hapa duniani. Alikuwa mtu aliyependa fujo ambaye alitawala kibabe nchini mwake.
Watu hawakumpenda kwa sababu alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa ambaye alikuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile, wakati wowote pasipo kuogopa chochote.
Marekani walijitahidi kumuwekea vikwazo rais huyo, hakujali, kitu alichokijua ni kwamba alikusanya pesa nyingi kutokana na visima vya mafuta vilivyokuwa nchini mwake.
Nchi iliingiza pesa nyingi kupitia mafuta, ilijiendesha kama ilivyotakiwa kuwa kwa sababu tu biashara hiyo ilikuwa na pesa, aliziunganisha nchi nyingi na kuziuzia mafuta hayo ambayo yalimfanya kupata pesa nyingi.
Hakujali kuhusu Marekani, walimwambia wangeweza kuilipua nchi yake lakini hakutaka kujali, kwake, kelele zao zilikuwa ni sawa na muziki uliopigwa mbele ya mbuzi ili acheze lakini hakufanya hivyo.
Siku zikaendelea, baada ya Urusi kuona kulikuwa na maslahi makubwa nchini Iraq, rais wa nchi hiyo, Bwana Petrov Ludovick akampigia simu Rais Hamis na kumwambia kwamba hakutakiwa kuogopa kwa sababu alikuwa upande wake, kama kungekuwa na mtu yeyote ambaye angembabaisha basi angemsaidia kupambana na adui huyo.
Kwa Hamis akakenua, hakuamini kama angepata msaada kutoka kwa nchi kubwa kama Urusi, kitendo cha Rais Ludovick kusema angemtetea kwenye kila hatua, kwake ikaonekana kuwa ushindi mkubwa, akaongeza kiburi zaidi.
Alichokuwa akikiangalia Ludovick si kumlinda tu mwanaume huyo bali alihitaji kuingia kwenye biashara ya mafuta na nchi hiyo, aliamini kwamba Marekani alihitaji sana kupata mafuta kutoka nchini humo kibabe, yeye hakutaka kufanya hivyo na ndiyo maana kitu cha kwanza kabisa ambacho alihitaji kukipata ni kuchukua nafasi ya kufanya biashara na Iraq kwa kutengeneza urafiki.
Urafiki huo haukuwa siri, Marekani wakajua kwamba Urusi aliingilia kati, kulikuwa na mipango mingi ambayo nchi hiyo ilipanga, waligundua kwamba rais Ludovick aliahidi kumlinda Hamis, hata kama kungekuwa na wabaya walihitaji kupambana naye, mtu wa kwanza kabisa ambaye angejitokeza angekuwa Urusi.
Hilo liliwaumiza vichwa Wamarekani, walishindwa kujua nini cha kufanya. Urusi ilikuwa nchi kubwa na yenye silaha kubwa za kijeshi lakini kubwa zaidi ni kwamba walikuwa karibu na Marekani.
Kama ambavyo Marekani alivyokuwa mbabe, hata Urusi alikuwa hivyohivyo, hawakuwahi kupatana na kila siku walikuwa wakiangaliana kama maadui, yaani ni kama kila mmoja alikuwa akimsubiri mwenzake amchokoze.
Baada ya siku nyingi kupita hatimaye Rais Hamis akawaita waandishi wa habari na kutaka kuzungumza nao kitu, kila mtu alihitaji kusikia ni kitu gani kingezungumzwa mahali hapo mbele ya waandishi wa habari.
Waandishi hao walifika ikulu, waliweka kamera zao, waliujua ubabe wake, walijua kabisa kama siku hiyo mwanaume huyo alihitaji kuzungumza kitu cha kuigusa dunia kwa sababu tu hakuwa akipatana na mataifa mengi nje ya himaya ya Waarabu.
Baada ya dakika kadhaa, rais huyo akafika mbele ya waandishi wa habari. Alivalia kanzu nyeupe, iliyong’ara huku akiwa na kilemba kichwani mwake, kwa kumwangalia harakaharaka ilikuwa ni rahisi kusema mtu huyo alikuwa mtakatifu, mwenye moyo mzuri na wa kujishusha kama Mtume Muhammad kumbe haikuwa hivyo, alikuwa mwanaume aliyeishi katika dunia yake ya kibabe aliyependa kila mtu duniani amuogope.
Akakaa kwenye kiti chake, kabla ya kuzungumza kitu chochote kile, akaachia tabasamu pana, akachukua maji na kuanza kunywa, alihitaji kuzungumza kitu ambacho alijua kabisa dunia ingeshtuka na kuona hakukuwa na amani tena.
Hakutaka kupoteza muda wa waaandishi wa habari, akaanza kuzungumza kile kitu kilichomfanya kuwaita waandishi wa habari, aliwaambia kwamba alikuwa na mabomu ya nyuklia saba ambayo yalitengenezwa na watu wake, alikuwa na silaha nzito ambazo kila mtu alitakiwa kumuogopa.
Kila mtu aliyesikia hivyo, akashtuka, hapakuwa na mtu aliyeamini kama kweli mwanaume huyo alikuwa na mabomu ya nyuklia, Marekani wenyewe kwenye stoo ya mabomu yao kipindi hicho walikuwa na mabomu matatu tu ambayo walikuwa wakiringia nayo, cha ajabu Rais Hamis alikuwa na mabomu saba, alionekana kuwa mtu tishio.
Haraka sana Rais Ludovick wa Marekani akaitisha kikao ikulu na kutaka kuzungumza na viongozi wa juu wa CIA. Alihitaji kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea, walitakiwa kujipanga na kuhakikisha wanashinda kila kitu kilichokuwa mbele yao.
Simu ikapigwa na ndani ya nusu saa watu hao walikuwa ikulu na kufanya kikao hicho kidogo. Walizungumza mambo mengi ikiwemo lile la kuwamaliza watu waliokuwa wametengeneza mabomu hayo lakini kitu kikubwa zaidi kilikuwa ni kuhakikisha wanapata formula ambayo wataalamu wa Rais Hamis waliitumia kutengeneza mabomu hayo.
“Tuhakikisheni tunafanikiwa katika hilo, sawa?” alisema Rais Ludovick.
“Sawa.”
Wakaondoka, aliwaachia kazi ya kuhakikisha hilo linafanyika haraka pasipo kugundulika. Ili hilo lifanikiwe ilikuwa ni lazima kumtuma mtu kwenda nchini Iraq ambapo huko angefanya kila liwezekanalo kuhakikisha wanafanikiwa katika hilo.
Hawakutakiwa kumtuma jasusi wa Kizungu kwa kuwa walijua ingekuwa ni rahisi kugundulika, mtu ambaye alitakiwa kwenda huko ni jasusi mweusi ambaye angejifanya kama mfanyabiashara kutoka barani Afrika, ila baada ya kufika huko angefanya kila liwezekanalo kuhakikisha anagundua kila kitu kilichokuwa kikiendelea pamoja na kupata formula hiyo.
Walichokifanya ni kumchukua jasusi aliyeitwa kwa jina la Kennedy Edward ila kwenye kazi hiyo alitakiwa atumie jina la Ibrahim Munir ambaye angejifanya kuwa mfanyabiashara wa mafuta aliyekuwa na kampuni yake nchini Kenya.
Kabla ya yote, kitu cha kwanza walichokifanya ni kumtengenezea hati za kusafiria ambazo zilionyesha alikuwa akitokea nchini Kenya, hawakuishia hapo bali wakatengeneza tovuti yake binafsi ambayo ilionyesha shughuli mbalimbali za kijamii alizokuwa akizifanya nchini Kenya huku kukiwa na picha za kutengenezwa.
Kwa kuwa walikuwa na uhitaji wa kukamilisha kazi yao ilikuwa ni lazima Kennedy asafirishwe kuelekea nchini Kenya ambapo huko angetembelea vituo vya watoto yatima.
Hilo halikuwa tatizo kabisa lakini pia alitakiwa kubadilisha muonekano wake, haraka sana sura ya bandia ikaletwa na kuvalishwa, kila kitu ambacho kilikuwa kikienda kufanyika katika nchi za Kiarabu kilitakiwa kuwa siri kubwa, hakutakiwa mtu yeyote kufahamu kama alitumwa kwenda nchini humo kwa kazi maalumu.
Ilikuwa ni lazima kazi ifanyike, picha zipigwe huko Kenya na hatimaye kuingizwa kwenye tovuti hiyo na kwa sababu walikuwa siriazi na kazi hiyo, wakamtengenezea ukurasa wake wikipedia ambapo humo kulikuwa na stori yake ya uongo kuhusu maisha yake na mpaka alipoanza kufanya biashara ya mafuta huku akiwa ametokea katika familia ya kimasikini.
Mbali na yote hayo, pia walimtaka kupiga picha nyingi akiwa na kanzu, ilikuwa ni lazima aonekane kama alikuwa Muislamu hivyo alitakiwa kuuvaa uhusika na kupelekewa ustadhi ambaye alikuwa na kazi ya kumfundisha kuswali na kufanya mambo mengine katika dini hiyo.
Alikuwa makini kwa kila kitu, kichwa chake kilikuwa na uwezo mkubwa wa kukariri kila kitu alichokuwa akifundishwa, baada ya mwezi mmoja na kuonekana alikuwa tayari kwa kila kitu, akasafirishwa mpaka Dubai huku hati zake zote za kusafiria zikionekana kama alikuwa raia wa Kenya na kuanza kuelekea nchini Iraq.
Kabla ya kufika huko, tayari Wamarekani waliwasiliana na watu wao juu ya mtu huyo, waliwaambia watangaze kwamba mfanyabiashara mkubwa kutoka nchini Kenya alikuwa akienda nchini Iraq kufanya utalii wa kuzunguka sehemu mbalimbali ambazo mitume ya zamani ilikuwa imepitia.
Watu walitakiwa kujua ujio wake, si hilo tu bali pia watu walitakiwa kufahamu kwamba mtu ambaye alikuwa akija alikuwa bilionea mkubwa ambapo akaunti yake ilisoma kuwa na kiasi cha dola bilioni thelathini ambazo zilikuwa ni zaidi ya trilioni sitini, pesa hizo zote zilikuwa hewa lakini hilo hakukuwa na mtu aliyekuwa akilifahamu zaidi yake na watu waliokuwa wamemtuma.
Matangazo yakaanza kutolewa sehemu mbalimbali, kitendo cha bilionea kutoka Kenya kutangazwa kwamba alikuwa akienda nchini humo kutembelea sehemu mbalimbali za makumbusho na hata kutoa misaada, kila mmoja alichanganyikiwa, alikuwa Mwafrika lakini Waarabu hawakutaka kujali kuhusu ngozi, walichokuwa wakikijali ni kuona nchi yao ikinufaika na ujio wa mwanaume huyo.
Kila kona kulikuwa na stori kuhusu yeye, hakuwa amefika nchini humo lakini wale watu ambao walitumiwa kufikisha habari nchini humo walifanya kazi kwa uaminifu mkubwa mno kiasi kwamba ndani ya siku mbili tu, tayari alikuwa mwanaume maarufu sana.
Wale ambao hawakuwa wakimfahamu walikwenda kwenye tovuti mbalimbali na kulitafuta jina lake. Hawakupata tabu kumpata, ni ndani ya dakika chache tu walimuona akiwa sehemu mbalimbali Afrika huku akionekana kuwasaidia watu wengi waliokuwa kwenye matatizo.
Kwa jinsi alivyokuwa akijitoa, kila mmoja alifurahia, alionekana kuwa mwanaume mwenye roho nzuri ambaye alitamani kuona kila mtu akipata kile kidogo alichokuwanacho.
Uso wake ulikuwa wa huruma sana, alionekana kama malaika ambaye alitumwa duniani kwa ajili ya kuwasaidia watu waliokuwa wakiteseka kwa njaa kila siku.
Katika nakala zake alizobeba, aliandikiwa kwamba alitakiwa kufikia katika Hoteli ya Sultani Alwaqidr iliyokuwa pembezoni na Mji wa Baghdad.
Katika hoteli hiyo kulikuwa na msichana aliyeitwa kwa jina la Nurat ambaye alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha msichana huyo anakuwa na ukaribu naye kwa sababu baba wa msichana huyo aliyeitwa Shabir Kuwad alikuwa mfanyabiashara mkubwa wa matunda ndani ya jiji hilo.
“Sijaelewa, lengo hapa ni nini?” aliuliza Kennedy ambaye alijulikana kwa jina la Ibrahim Munir.
“Tunahitaji utengeneze ukaribu naye, umpende, umjali lakini mwisho wa siku tunataka uende mpaka nyumbani kwao, huko, tengeneza ukaribu na baba yake ambaye ni muhimu sana kwetu,” alisema mwanaume kwenye simu.
“Halafu?”
“Kwanza fanya hivyo, tutakwambia kazi kubwa ya baba yake. Hakikisha kwanza unaanza kumteka kimapenzi Nurat, halafu baada ya hapo tutakwambia ni kitu gani unatakiwa kufanya. Nakutumia picha ya Nurat ili isiwe vigumu kumpata,” alisema mwanaume huyo na kumtumia picha ya msichana huyo.
“Sawa. Nimemuona, nitakamilisha kila kitu na formula tutaipata tu,” alisema Kennedy na kisha kuzima simu ambayo ilikuwa ikitumia huduma ya wireless ndani ya ndege ile.

Je, nini kitaendelea kwa jamaa huyu wa pili?
Je, nini kitaepelekea kuingia ndani ya ndege ile?
Tukutane Alhamisi
 
Madameee santee
NYEMO CHILONGANI
SHAMBULIO LA DAMU
0718069269

Sehemu ya Kumi.

Hapakuwa hata na mtu aliyehisi kama ujio wa mwanaume huyo ndani ya nchi hiyo ulikuwa ni maalumu kwa ajili ya kuhakikisha anapata formula iliyotumika kutengeneza mabomu ya nyuklia nchini humo.
Kila mmoja alijua mwanaume huyo alikuwa rafiki mkubwa ambaye alikuja kutoa misaada kwa watu wasiojiweza, kufanya biashara ya mafuta lakini pia kutembelea sehemu mbalimbali ambazo mitume ilikuwa imepita.
Watu walimsubiri kwa mbwembwe, wale ambao walikusanyika katika uwanja wa ndege walikuwa wakiimba kwa shangwe kana kwamba kulikuwa na mtu mkubwa kutoka serikalini alikuwa akifika. Shamrashamra zote hizo ziliandaliwa na msikiti wa Al-Rahman ambao ulikuwa mkubwa katika Jiji la Baghdad.
Baada ya dakika kadhaa, ndege ya Shirika la Ndege la Qatar ikaanza kutua ndani ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Baghdad. Miongoni mwa abiria mia mbili na ishirini waliokuwa ndani ya ndege hiyo alikuwemo Kennedy.
Macho yake yalikuwa yakiangalia nje, jinsi Jiji la Baghdad lilivyojengwa, kila alivyokuwa akiliangalia, moyo wake ulimwambia kwamba hapo ndipo alipotakiwa kufanya kazi ya hatari ambayo kama tu angegundulika basi ilikuwa ni lazima auawe.
Katika maisha yake yaliyokuwa katika tovuti feki ilionyesha aliishi maisha ya kawaida sana na ndiyo maana hata usafiri wa ndege aliokuwa akiutumia ulikuwa ni wa jumuiya na hakutaka kabisa kununua ndege ambayo angeitumia yeye peke yake.
Alimuomba Mungu mpaka pale ambapo ndege ilisimama na kuanza kuteremka. Alipofika chini na abiria wenzake wakaanza kuelekea katika jengo la uwanja huo, walipokaguliwa, akaondoka na kutoka ndani.
Alishangaa kukuta watu wengi wakimsubiri kwa shangwe, moyo wake ulisikia furaha mno, hakuamini alichokuwa akikiona, kila mtu alimkaribisha huku akionekana kuufurahia ujio wake mahali pale.
Watu wakaanza kumpiga picha na kumuingiza ndani ya gari na kuondoka mahali hapo. Njiani, mashehe ambao walipanda naye garini wakaanza kuzungumza naye mambo mengi kuhusu maisha yake, alipotoka na hata kuhusu ushirika wake katika suala zima la dini.
Kwa jinsi alivyokuwa akijibu, ilionyesha kabisa mwanaume huyo aliishika dini na alijua mambo mengi kuhusu Uislamu kumbe hakuwa hivyo, ni mafunzo maalumu ambayo alipewa ndani ya wiki moja tu na kuyashika vilivyo.
Alionekana kuwa na furaha mno, hakutakiwa kuwaonyeshea watu hao kama alikuwa na kitu kingine moyoni mwake, ilikuwa ni lazima aonyeshe tabasamu pana ambalo lingemfanya kila mmoja aamini alikuwa mtu mwema kwa ajili ya maisha yao.
Hoteli iliandaliwa na Wamarekani lakini kwa kupitia jina lake. Akapelekwa huko na kutulia chumbani huku watu wale ambao walimpokea wakisema kwamba wangerudi siku inayofuata kwa ajili ya kumchukua na kumtembeza sehemu kadhaa kuangalia mazingira.
Ujio wake uliendelea kuwa gumzo nchi nzima, televisheni zilionyesha jinsi alivyopokelewa uwanja wa ndege, alionekana kama mtu fulani maarufu ambaye alifika nchini humo.
Maofisa wa CIA walipokuwa wakiangalia kwenye televisheni, walifurahia kwani waliona walifaulu kwa kile walichokuwa wamekifanya, walichotakiwa kusubiri ni utekelezaji tu.
Alitulia chumbani ndani ya Hoteli ya Sultani Alwaqidr, kazi yake ilikuwa ni kuwasiliana na wenzake na kuwaambia tayari alikuwa ameingia nchini humo na kitu pekee kilichobaki kilikuwa ni utekelezaji tu.
“Umekwishakutana na Nurat?” aliuliza mwanaume kutoka upande wa pili.
“Hapana! Ila nimekutana na wasichana wengi warembo, nahisi mmojawapo anaweza kuwa Nurat,” alisema na kuanza kucheka kwa kicheko cha chini.
“Sawa. Ila usikosee hesabu, hakikisha unakutana na huyo Nurat na kufanya tulichokwambia. Kuna pesa zimeingizwa katika akaunti yako, tumia unavyojua ila kumbuka kwamba ni lazima ufanikishe kujua formula iliyotumika kutengenezea mabomu hayo,” alisikika mwanaume huyo.
“Hakuna shida.”
Akakata simu na kuanza kupanga mikakati. Ilikuwa ni usiku wa saa tatu, alichoka kukaa chumbani hivyo akatoka na kuelekea kwenye mgahawa uliokuwa hotelini hapo kwa chini.
Hakutaka kugundulika kwani kila mmoja alijua kwamba alikuwa bilionea mkubwa, aliyejiamini kulindwa na Allah kwani hata walinzi hakuwa nao hata kidogo.
Alipofika chini huku akiwa na kilemba chake kiasi cha kutoweza kugundulika kwa urahisi, akaelekea kwenye mgahawa huo na kuagiza kahawa, akaletewa na kuanza kunywa.
Kule alipokaa kulikuwa na giza, ilikuwa ni vigumu kugundulika kwa kuangaliwa. Macho yake hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule kana kwamba alikuwa akitafuta kitu fulani.
Kwanza alihitaji kuonana na huyo Nurat, azungumze naye, amchangamkie na mwisho wa picha kabisa wawe wapenzi na kuambiwa ni kitu gani kilitakiwa kufuata baada ya hapo.
Hakutaka kuvumilia, alichokifanya ni kumuita kijana mmoja na kumuuliza kuhusu huyo Nurat, kwanza kijana huyo alishtuka, haikuwa ikiruhusiwa kwa mteja yeyote kwenda kwenye mgahawa na kumuulizia mhudumu fulani.
Hiyo ndiyo ilikuwa sheria ya Uarabuni, si Iraq tu bali kila kona huko. Kijana yule akahisi kabisa kwamba mtu aliyekuwa akizungumza naye alikuwa mgeni, hakufahamu kama kile alichokuwa alikifanya kilikuwa kosa kubwa.
“Who are you brother?” (wewe nani kaka?) aliuliza mhudumu huyo kwa lafudhi ya Kiarabu.
“A customer!” (mteja)
“Do you know the rules?” (unazijua sheria?)
“What rules?” (sheria zipi?)
Kijana yule akaanza kumwambia kuhusu kile kilichokuwa kikiendelea, Kennedy hakujua lolote lile, alimshukuru kijana yule lakini alimwambia kwamba alitamani sana kumuona msichana huyo kwa kuwa alikuwa na shida naye.
Aligundua kwamba kijana huyo alikuwa mgumu hivyo alichokifanya ni kuingiza mkono mfukoni na kutoa dola mia tatu na kumuwekea mezani kisiri ili watu wengine wasione.
“Nahitaji kumuona, nimemkumbuka sana. Kweli hutaki kunisaidia?” alisema Kennedy na kuuliza swali huku akizisogeza zile pesa upande wa kijana yule aliyekuwa amesimama mbele ya meza yake.
“Hakuna tatizo,” alisema kijana yule huku akizichukua.
“Nashukuru!”
“Ila sasa!”
“Kuna nini?”
“Amekwisharudi nyumbani! Kesho akija nitamwambia kwamba unamtafuta. Unaitwa nani?” aliuliza kijana yule.
“Ibrahim Munir.”
Kijana yule aliposikia jina hilo akashtuka, hakuamini kama mwanaume ambaye alikuwa mbele yake alikuwa Ibrahim. Alimfahamu mwanaume huyo, alikuwa bilionea mkubwa ambaye alikwenda kutembelea nchi hiyo huku akiahidi kutoa misaada mbalimbali.
Alimwangalia vizuri, Kennedy alikuwa kwenye mwanga hafifu hivyo kumgundua ilikuwa ni lazima umsogelee. Kitendo cha kumuona kijana huyo akiwa na ngozi nyeusi, aliamini moja kwa moja kwamba alikuwa mwanaume huyohuyo ambaye aliambiwa alifika nchini humo siku hiyo.
“Ibrahim!” alisema kijana huyo kwa kushtuka.
“Ndiyo! Naomba unisaidie!” alisema Kennedy huku akionekana kuomba sana.
“Hakuna shida. Nitakusaidia kwa gharama yoyote ile,” alisema huku akionekana kuwa na furaha mno.
“Nitashukuru!”
***
Siku iliyofuata asubuhi na mapema Nurat akaenda kazini kwake, alipofika tu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kufuatwa na kijana yule aliyeonana na Kennedy usiku uliopita na kuanza kuzungumza naye.
Kwanza kabisa akaanza kumpongeza kwa mbwembwe, Nurat hakujua sababu za kupongezwa huko, alibaki akimwangalia mwanaume huyo kwa macho ya mshangao.
Alihitaji kujua sababu za pongezi zile, kwake, kilionekana kuwa kitu cha ajabu kupongezwa huku akiambiwa kwamba alikuwa na bahati kubwa mno.
Alihisi inawezekana alipandishwa cheo hapo kazini lakini hilo likapotea kichwani mwake kwa sababu kitu cha kwanza kabisa ambacho kingetakiwa kufanywa ni kupewa barua ya kupandishwa hicho cheo.
Akamuuliza kijana yule, hapo ndipo alipoanza kufunguka kuhusu bilionea ambaye alikutana naye usiku uliopita na kuanza kumuulizia huku akionekana kuwa na uhitaji wa kuonana naye. Nurat alibaki kimya, ni kama alipigwa na mshangao, kile alichoambiwa hakukiamini hata kidogo.
Ilikuwaje mwanaume atoke huko barani Afrika halafu afike nchini Iraq na kumuulizia yeye? Alimjuaje na kulikuwa na kitu gani alichokihitaji kutoka kwake? Hiyo haikumuingia akilini lakini wakati mwingine alijiona kama alikuwa na bahati kubwa, kuuliziwa na mtu mwenye jina kubwa kama Ibrahim haikuwa kawaida, ni lazima kungekuwa na kitu.
“Wewe umehisi nini?” aliuliza Nurat huku akimwangalia kijana yule.
“Anataka akuoe!” alijibu.
“Anioe mimi?”
“Ndiyo! Kwani wewe siyo mzuri?”
“Sidhani! Labda kama kuna kitu kingine alikwambia halafu unanificha,” alisema msichana huyo.
Wakazungumza kwa dakika chache na kisha kuondoka. Kichwa cha Nurat hakikutulia, muda mwingi alifikiria kuhusu yale maneno aliyoambiwa, yalimchanganya kichwani mwake, alitoka kwenye familia ya kawaida sana ambayo haikuwa na uwezo mkubwa kipesa, baba yake alikuwa muuzaji wa matunda katika kambi ya jeshi, hakuona kama kulikuwa na sababu zilizomfanya mwanaume huyo kufika nchini humo na kumuulizia huku akitamani sana kuonana naye.
Hakutaka kujiuliza maswali mengi sana, kwa kuwa alisema alihitaji kumuona basi akasubiri, hata kama angemaliza kazi zake, alikuwa radhi kumsubiri na kuanza kuzungumza naye.
Wakati huo Kennedy alikuwa amekwishafuatwa na kupelekwa katika sehemu mbalimbali hapo Iraq. Alionyeshewa msikiti mkubwa wa Al-Rahman na sehemu nyingine nyingi.
Kila mtu aliyekuwa akimwangalia alimfurahia, kwa muonekano wake wa nje tu alionekana kuwa ustadhi mkubwa aliyeijua sana dini ya Kiislamu kumbe hakuwa huko kabisa, alikuwa Mkristo mzuri ambaye kila Jumapili alikuwa akienda kanisani kusali.
Siku hiyo ilikuwa ni ya kuzunguka huku na kule, waandishi wa habari walialikwa na hivyo kufuatilia na kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Wote walifurahia, uwepo wa mwanaume huyo ulionekana kuwa kama baraka kutoka kwa Mungu kumbe ukweli wa mambo walimkaribisha mwanaume hatari kuliko wote waliowahi kufika nchini humo.
Wakati hayo yakiendelea, walichokifanya Wamarekani ni kumtuma mwanaume mwingine mweusi aliyeitwa kwa jina la Backnon kwenda huko Iraq kwa ajili ya kufanya kazi nyingine ambayo waliamini ingewasaidia sana.
Walihitaji aelekee huko na kwenda kupanga nyumba fulani kubwa, walijua kabisa kwa namna moja ama nyingine ilikuwa ni lazima kutumika kama kweli walihitaji kuijua formula ya Waarabu ambayo waliitumia kutengeneza hayo mabomu ya nyuklia.
Backnon akaenda huko, naye alijifanya kuwa Muislamu mzuri kabisa, hakutakiwa kujulikana, kitu ambacho alitakiwa kufanya ni kuonyesha kwamba alikuwa na uhitaji wa kupanga nyumba kwa ajili ya matumizi yake binafsi.
Hilo halikuwa tatizo, akapewa nyumba moja iliyokuwa pembeni kabisa na Jiji la Baghdad ambapo kulikuwa na jangwa na kwa jinsi ilivyoonekana ilikuwa kama sehemu iliyotengwa kwani hakukuwa na watu wengine.
Baada ya kukabidhiwa nyumba hiyo, akaambiwa asubiri kitu chochote ambacho kingetokea kwani kwenye suala hilo, wao kama Wamarekani walikuwa wamejipanga kuhakikisha kila kitu kinakwenda kama kinavyotakiwa.
Kennedy alitumia saa kadhaa, ilipofika majira ya saa saba, akaenda msikitini kusali kisha kurudi hotelini kupumzika. Hakuhitaji mlinzi yeyote yule, aliwaambia Waarabu kwamba katika maisha yake yote alimwamini Mungu, unapokuwa na ulinzi wa Mungu hautakiwi kuhofia maisha yako kwa sababu huwa ni mkubwa kuliko hata ulinzi wa wanadamu.
Maneno hayo yakawafanya wampende zaidi pasipo kugundua kwamba mwenzao hakutaka kufuatiliwa, alihitaji kufanya mambo yake kimyakimya pasipo mtu yeyote yule kufahamu jambo lolote lililokuwa likiendelea.
Alipoingia hotelini, Nurat alikuwa akimwangalia tu, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini kama mwanaume huyo, bilionea alihitaji kuonana naye. Alitamani amuite na kumwambia alichotaka kumwambia lakini Kennedy alionekana kuwa bize mno, hivyo akaacha kwanza akapumzike.
“Ila mbona anaonekana hanijui?” aliuliza Nurat.
“Umejuaje?”
“Nimepishana naye, kama angekuwa ananijua basi angenisalimia,” alisema.
“Hapana! Unajua hawa mabilionea huwa wanakuwa na akili sana, ameamua tu kukupotezea ili usichanganyikiwe mtoto wa watu,” alisema kijana yuleyule aliyempa Nurat taarifa za kuuliziwa.
“Mmh!”
“Ndiyo hivyo! Ngoja giza liingie, nitakushtulia!”
“Sawa.”
Kazi hazikufanyika kama siku nyingine, kitu pekee kilichokuwa kichwani mwa Nurat ni mwanaume huyo tu. Alitokea kumpenda kwa sababu alikuwa bilionea, kwake, hakujali kuhusu ngozi yake, hakujali kitu chochote kile, alitamani sana amchukue, amuoe na kuondoka naye.
Ilipofika majira ya saa moja usiku, kama kawaida Kennedy akatoka chumbani kwake na kwenda kwenye ule mgahawa na kukaa palepale alipokuwa amekaa na kumuita yule kijana.
“Yupo wapi?” alimuuliza.
“Ngoja nikakuitie,” alisema na kuondoka.
Kennedy alisubiri mahali hapo, kichwa chake kilikuwa kikifikiria mambo mengi, alihitaji kuzungumza na msichana huyo kidogo, wazoeane na kuendelea na mambo mengine.
Baada ya dakika chache, kijana yule akarudi na Nurat kisha kukaa kwenye kiti na yeye kuondoka. Msichana huyo alimaliza kazi zake, alivalia nguo za nyumbani hivyo hakukuwa na tatizo lolote lile, kama alitaka kuongea naye, basi afanye hivyo kwa muda wowote aliohitaji.
“Nimesikia kwamba uliniulizia,” alisema Nurat huku akimwangalia Kennedy.
“Ndiyo! Nilihitaji sana kuzungumza na wewe,” alisema Kennedy.
“Kuhusu nini?”
“Mambo ya kawaida kuhusu maisha. Ila kubwa zaidi ni kujenga mazoea na urafiki,” alisema Kennedy huku akitabasamu.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli wa mambo, hakuhitaji awe mpenzi wake kwa sababu tageti yake haikuwa msichana huyo. Alitakiwa kujenga naye urafiki lakini lengo lake kubwa ni kuonana na baba yake Nurat na kuanza kupanga naye mikakati.
Njia nzuri ya kumuingia mzee huyo ilikuwa ni kupitia kwa binti yake, alitakiwa kujifanya kuwa marafiki wakubwa lakini mwisho wa siku apate kile alichokuwa akikihitaji.
Hilo halikuwa tatizo, hapo alipokuwa akaanza kuzungumza na Nurat, alimwambia alikuwa msichana mwenye akili sana ambaye muda mwingi alifikiria kumsaidia kwa kuwa uwezo wa akili yake ulikuwa mkubwa mno.
Maneno hayo yaliingia kichwani mwa Nurat, kwa kuwa Kennedy alionekana kuwa bilionea, akakubaliana naye na hivyo kuendelea kuzungumza kama kawaida.
Walicheka pamoja, walifurahi na ilikuwa ni vigumu kwa watu kugundua kama watu hao siku hiyo ndiyo ilikuwa ni ya kwanza kuonana na kuzungumza.
“Ni biashara gani kubwa unaweza kuifanya hapa?” aliuliza Kennedy aliyejulikana kwa jina la Ibrahim.
“Kuna biashara nyingi sana, tatizo mtaji tu!”
“Hilo si tatizo tena!”
“Basi sawa, ila zipo nyingi! Nitakwambia kama tutaendelea kuonana,” alisema Nurat.
“Usijali! Ninahitaji upanue mawazo yako, uniambie mchakato wake, faida na hata hasara zake, nitakusaidia, hakika wewe ni msichana wa mfano sana,” alisema Kennedy huku akimwangalia msichana huyo.
Hiyo ilikuwa siku ya kwanza tu, wakaagana na Nurat kuondoka. Japokuwa alionekana kuwa msichana mgumu lakini kwa Kennedy hakuwa lolote lile. Mwanaume huyo alijua kuongea, kumzoea mtu kwa haraka na hata kujenga uaminifu mkubwa kwake.
Kichwa cha Nurat kilikuwa kikifikiria mapenzi tu, kwa jinsi alivyozungumza na Kennedy kwa nusu saa tu aligundua wanaume wenye pesa walikuwa na mawazo tofauti, stori zao walizokuwa wakipiga walionekana kuwa tofauti na wao.
Alifurahia mno, alihisi kabisa maisha yake yalikuwa yakienda kubadilika na kuwa mtu mwenye pesa nyingi kwa kuwa hata mbinu alizopewa na mwanaume huyo namna ya kutafuta pesa zilikuwa kiboko na aliamini kabisa kwamba kama angezifanyia kazi, basi siku moja angekuwa na pesa nyingi kama alizokuwanazo mwanaume huyo.
“Nauona utajiri mbele yangu! Kama atanisaidia, au atataka kunioa, nipo tayari kwa lolote lile,” alijisemea Nurat huku akionekana kuwa na furaha tele, hakujua kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumapili.
 
Naash Nash
NYEMO CHILONGANI
SHAMBULIO LA DAMU
0718069269

Sehemu ya Kumi na Moja.

Urafiki wao ulitakiwa kuwa siri kubwa, hakukuwa na mtu yeyote ambaye alitakiwa kufahamu kile kilichokuwa kikiendelea kati ya watu hao wawili. Kila siku walikuwa wakionana hotelini hapo katika sehemu iliyokuwa na mwanga hafifu na kuanza kuzungumza.
Kennedy ambaye alijulikana kwa jina la Ibrahim alijifanya kuwa rafiki mkubwa, muda mwingi alimchangamkia msichana huyo kana kwamba walifahamiana kipindi kirefu kilichopita. Nurat akajisahau, kuchangamkiwa kule huku Kennedy akijifanya kuwa rafiki yake wa karibu ambaye baada ya hapo alitarajiwa kuingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, ukamchanganya zaidi na kuona kwamba tayari alikuwa mke wa mwanaume huyo.
Siku zikaendelea kukatika, kila kitu kiliendelea kuwa siri kubwa, baada ya wiki mbili za mazoea makubwa hatimaye Kennedy akamwambia msichana huyo kwamba alitamani sana kama angepata nafasi ya kuonana na familia yake kwa kuwa tu alikuwa na mipango mingi juu yake.
Nurat akafurahi, kwake, hiyo ilionekana kuwa nafasi kubwa, ukweli kutoka moyoni mwake alimpenda sana Kennedy, hakuona kama kulikuwa na mwanaume mwingine aliyestahili kuutoa usichana wake zaidi ya mwanaume huyo ambaye kwa kuongea tu ilikuwa ni rahisi kugundua alikuwa na akili nyingi.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, Nurat akakubaliana naye na hatimaye siku hiyo kumchukua na kuanza kuelekea naye nyumbani kwao. Walitembea huku Kennedy akijitahidi kujificha kwani hakutaka kugundulika kama alikuwa yeye, endapo tu angegundulika basi aliamini kila kitu kingekufa muda huo.
Baada ya dakika kadhaa wakafika nyumbani. Aliingia kikawaida sana lakini baada ya familia yake kumuona, kila mmoja alichanganyikiwa, hawakuamini kumuona mwanaume huyo mahali hapo. Alikuwa maarufu na tajiri mkubwa lakini mbali na hayo mawili, alipenda dini sana na kuswali
“Karibuni sana,” alisema mzee Shabir Kuwad huku akimwangalia Kennedy.
Bado aliona kama ndoto, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, kwake, Kennedy alikuwa mtu wa tofauti sana, maarufu ambaye alijizoelea sifa nyingi hapo Iraq. Aliheshimiwa kila kona alipopita kiasi kwamba watu wengi walikuwa wakimuhusudu kuonana naye lakini hakuwapa nafasi.
Mzee huyo aliona ni bahati ya kipekee kuonana na mtu huyo, alitafutwa kila kona, mpaka kufika nyumbani kwake ilimaanisha alizivuka nyumba nyingi, alitembea umbali mrefu mpaka kuthubutu kuingia humo ndani, hayo yote yakamfanya kuhisi kama alimkaribisha mtume nyumbani kwake.
Wakaanza kuzungumza, kila mmoja kwenye familia hiyo alionekana kuwa na furaha, waliongea mambo mengi, kwa kirefu na mwanaume huyo aliwaambia kuhusu mpango wake. Alihitaji kumsaidia sana Nurat lakini pia alihitaji kumsaidia mzee Shabir katika biashara zake alizokuwa akizifanya.
“Ninasambaza matunda serikalini,” alisema mzee huyo.
“Na ina faida?”
“Kiasi chake! Tatizo ni moja tu, usafiri, natumaini kama ningepata usafiri, ningefurahi zaidi,” alisema mzee huyo.
“Hilo si tatizo hata kidogo!”
Kennedy aliongea kwa kujiamini kupita kawaida. Kununua gari kwa ajili ya mzee huyo halikuwa tatizo lolote, alichohitaji ni kufanikiwa kwa kile kilichokuwa kimepangwa na hatimaye nchi ya Marekani kuwa na sifa kubwa kwa kila kitu kuhusu Rais Hamis ambaye mpaka kipindi hicho alijiona kuwa mjanja kuliko mtu yeyote yule.
Walizungumza mambo mengi na siku iliyofuatia, gari mpya aina ya Double Cabin likaingia nyumbani kwake na kuambiwa ilikuwa mali yake alinunuliwa na mtu mmoja kutoka nchini humo.
Mzee huyo hakuamini macho yake, akachukua kadi ya gari na kuangalia jina, liliandikwa jina lake, kulikuwa na vibali vyote na vililipiwa, hakutaka kujiuliza, aligundua kwamba alikuwa ni Kennedy ambaye alizungumza naye na kumwambia angemsaidia.
Hakutaka kuchelewa, haraka sana akachukua simu yake na kumpigia binti yake, Nurat na kumwambia kilichotokea. Msichana huyo hakuamini, alihitaji kuliona gari hilo hivyo siku hiyo haraka sana akarudi nyumbani, alipofika, akalikuta limepaki, huku machozi yakianza kumtoka, akamsogelea baba yake na kumkumbatia.
Familia nzima ilikuwa na furaha, wakampigia simu Kennedy na kumwambia siku hiyo walitakiwa kula wote chakula cha usiku, hilo halikuwa tatizo, akakubaliana nao na usiku huohuo kwenda nyumbani hapo.
Walipomuona, walimsogelea na kumkumbatia kwa furaha. Walimshukuru, mwanaume huyo alionekana kuwa na umuhimu mkubwa kuliko mtu yeyote yule katika dunia hii kwenye familia hiyo. Walizungumza naye mambo mengi, walimsifia pasipo kugundua kama mwanaume huyo alikuwa na mipango yake, gari halikuwa tatizo, walichokuwa wakihitaji ilikuwa ni lazima kifanyike.
“Tunashukuru sana, yaani sana,” alisema mzee Shabir huku akiikutanisha mikono yake.
“Hakuna shida. Allah amenigusa kufanya hivi,” alisema Kennedy huku akionekana kumaanisha alichokisema.
Wakaendelea na mazungumzo mengi, hapo ndipo Kennedy akatumia nafasi hiyo kumwambia mzee huyo kwamba alihitaji kuona sehemu aliyokuwa akipeleka matunda, kulikuwaje na kulikuwa na akina nani ambao kila siku ilikuwa ni lazima awapelekee matunda hayo.
Kwa kuwa alipewa gari, alikuwa na furaha kubwa hakusita kumwambia mambo mengi. Alisema kwamba matunda hayo alikuwa akiyapeleka jeshini kila siku usiku kwani kulikuwa na watu muhimu ambao walitakiwa kula matunda kwa kuwa kazi waliyokuwa wakiifanya ilikuwa kubwa na ya siri sana.
“Kazi gani?” aliuliza Kennedy, hakutaka kulitilia mkazo katika swali hilo, hivyo alikuwa akiuliza kama masihara kumbe alihitaji mzee huyo afunguke.
“Si wale wanaotengeneza nyuklia!” alisema mzee huyo.
“Nyuklia? Hivi kuna mtu anatengeneza nyuklia zaidi ya nchi za Magharibi?” alijifanya kuuliza, alihitaji kufahamu ukweli.
“Hujafuatilia habari?”
“Hapana! Huwa siangalii televisheni, muda mwingi nasoma Koran na kumuabudu Allah!” alijibu.
“Unapitwa,” alisema mzee Shabir na kuanza kumwambia Kennedy kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Hakutaka kumficha, utajiri wa uongo aliokuwanao ukamfanya mwanaume huyo kumwambia kila kitu, jinsi alivyokuwa akienda huko na kukutana na watu hao na kuwauzia matunda.
Walifichwa, walikuwa katika chumba cha siri na hakukutakiwa kuingia watu wengine wengi, ni yeye, viongozi wa serikali na wale ndugu wa karibu tu, tena wa damu.
“Daah! Kumbe napitwa, sasa na mimi naweza kuwaona? Nataka nijifunze mengi kuhusu wao,” aliuliza Kennedy.
“Kuwaona?”
“Ndiyo!”
“Sijajua!”
“Ila wewe si huwa unaingia?”
“Ndiyo!”
“Sasa kwa nini usinifanye mimi kama mfanyakazi wako halafu niingie na wewe?” aliuliza Kennedy.
Ilikuwa ni vigumu kukubaliana naye lakini kwa sababu alikuwa na ushawishi mkubwa kipesa na maneno matamu, mzee huyo akakubaliana naye na hivyo kupanga mipango ya kwenda huko.
Kwanza alitakiwa kubadilisha muonekano wake, hakutaka kuwa kama alivyokuwa, alitakiwa kutokugundulika na angekwenda naye huko kwa siku tatu tu kwani vinginevyo serikali ingegundua kilichokuwa kimetokea na hivyo kuingia kwenye matatizo na hata kupoteza kazi.
Kwa Kennedy halikuwa tatizo hata kidogo, alikubaliana naye na hivyo kuondoka kurudi hotelini huku wakiwa wamekubaliana kwamba siku hiyo wangekwenda katika nyumba hiyo huku akiwa na muonekano wa kimasikini na kuwaona watu hao.
Akarudi hotelini kwake. Kitu cha kwanza kilikuwa ni kuwasiliana na wenzake nchini Marekani na kuwaambia kila kitu kilichotokea, wao wakamwambia awasiliane na Backnon ambaye alikuwa mahali huko na kumwambia kile alichotakiwa kufanya.
“Nipeni mbinu, niwateke au niwamalize?” aliuliza Kennedy.
“Hapana! Wateke, tunahitaji kujua hizo formula ambazo wanazitumia kutengenezea mabomu hayo,” alijibu mwanaume kutoka upande wa pili.
“Ooh! Sawa haina shida! Basi nitahitaji dawa yenye nguvu ambayo inaweza kuwafanya watu kulala ndani ya dakika chache,” alisema.
“Haina shida. Backnon atakupa,” alisema mwanaume huyo na kukata simu.
Haraka sana Kennedy akawasiliana na Backnon na kumwambia kilichokuwa kimejadiliwa, kwa kuwa mwanaume huyo alikuwa hapohapo Baghdad, wakaonana hotelini na kuanza kuzungumza.
Alimwambia kwamba angempa dawa moja kali ya usingizi ambayo ilikaa katika chupa fulani na kama angeifungua, ingeanza kutoka na kusambaa chumbani na hatimaye watu wote hao kulala usingizi mzito na hivyo kufanya kile alichotaka kufanya.
“Mh! Na mimi si nitalala manake nitakuwa humo chumbani?” aliuliza Kennedy.
“Usijali! Hutoweza kulala! Yaani kuna dawa nitakupa ambayo itakuzuia wewe kulala kama wengine,” alisema Backnon.
Hicho ndicho alichomwambia, wakayapanga huko huku akimpa kamera iliyokuwa na muonekano wa kalamu ili kuitumia kuchukulia picha na kurusha moja kwa moja mpaka nchini Marekani na Backnon kuondoka hotelini hapo huku akimuacha Kennedy akiendelea kufanya mambo yake kama kawaida.
Kwa kuwa hakutaka kugundulika, aliendelea kuwasiliana na Nurat na kumwambia ni kwa jinsi gani alikuwa muhimu kwake, hakutaka kumtongoza lakini kitu alichokifanya ni kumtumia kiasi kikubwa cha pesa. Hakumtumia yeye tu bali hata mzee Shabir ambaye baada ya kuzipokea, alijikuta akichanganyikiwa na kumpenda Kennedy maradufu.
Siku iliyofuata usiku akaonana na mzee huyo na hatimaye kuanza kuelekea katika nyumba hiyo kubwa kwa ajili ya kupeleka matunda kwa kutumia gari yake mpya. Alipofika huko, kila mtu alishangaa, hawakuamini kama mwanaume huyo alikuwa na usafiri huo wa kifahari, kila mtu aliyekuwa akimuuliza, alimwambia alipewa zawadi na Mungu kwa kuwa alisaidia sana watu wenye matatizo mbalimbali.
“Na huyu nani?” aliuliza mlinzi.
“Huyu ni mfanyakazi wangu, nimenunua usafiri, sasa kwa nini nisiajiri mtu wa kunisaidia kazi zangu?” aliuliza mzee huyo huku akitoa tabasamu lililopokelewa kwa tabasamu pia kutoka kwa walinzi wa eneo hilo.
Walimwamini mzee huyo, alijiheshimu na hivyo kuliingiza gari hilo ndani huku akiwa na Kennedy ambaye alijifunga kilemba na ilikuwa vigumu kugundulika kwa sababu ilikuwa ni usiku sana.
Akaliingiza gari lake mpaka ndani. Kwenye uwanja wa nyumba hiyo kubwa hakukuwa na watu, walikuwa wachache sana ambao walikuwa wakilala humo. Wakateremka na kuondoka kuelekea ndani huku wakibeba makapu makubwa na kuingia mpaka kwenye chumba kile walichokuwa watu hao.
Macho ya Kennedy yakatua kwa watu hao waliokuwa mahali hapo. Walionekana kuwa na afya njema, walikuwa sehemu salama ambayo ilikuwa na ulinzi wa kutosha kwani mbali na wao, pia kulikuwa na askari waliokuwa wakilinda humohumo ndani huku wakiwa na bunduki zao, yaani watu hao walikuwa wakilindwa kupita kawaida na kila siku usiku ilikuwa ni lazima Rais Hamis kupiga simu na kujua maendeleo yao kama walikuwa chakula cha kutosha na matunda au la.
Walipoingia mule, macho ya Kennedy yalikuwa yakiangalia huku na kule, hiyo siku ya kwanza ilikuwa ni ya kuusoma mchezo, kulikuwa na nini na nini, watu gani walikuwa mahali gani.
Waliwaangalia watu hao, walikuwa watatu ambao walionekana kuwa wataalamu sana kwani muonekano wao tu ilikuwa ni vigumu kutokugundua kama walikuwa na akili kubwa.
Wakaanza kuwagawia matunda. Watu hao hawakuwa wakitoka, muda mwingi walitumia kuwa ndani ya nyumba hiyo na hawakutakiwa kupata taarifa yoyote kutoka nje na ndiyo maana hata huyo Kennedy alipoingia hawakugundua kama alikuwa Ibrahim kwa kuwa hata yeye mwenyewe hawakumjua.
Kamera ile ilikuwa ikiendelea kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali pale. Hakukuwa na mtu yeyote aliyegundua hilo, nchini Marekani walikuwa wakipata kila kitu, waliwaangalia wataalamu hao, hivyo wakajipanga kumwambia Kennedy kwamba siku nyingine ambayo wangeingia humo ilikuwa ni lazima ahakikishe kwamba anawateka watu hao na kuondoka nao.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumapili hapahapa
 
Kisukari wewe umenielewa sasa mana ilivyoanza na sasa tofauti
Unajua ukisoma mwanzo kabisa wa hadithi kuna maelezo yanasema. " ndanì ya ndege kuna watu 5 hawakujuana lakini walikuwa na mambo makubwa maishani mwao. Watu hao wangefika salama ilikuwa lazima dunia ichafuke. Oki dunia iendelee kuwa salama lazima kifanyike kile kilichofanyika." Maybe ndio maana unaona kuna new character. Nakisia tu
 
Inawezekana ngoja tuone
 
NYEMO CHILONGANI
SHAMBULIO LA DAMU
0718069269

Sehemu ya Kumi na Mbili.

Kila picha ambayo ilipigwa kwa kutumiwa kamera ndogo aliyokuwanayo Kennedy ikapelekwa mpaka nchini Marekani ambapo huko wakampongeza kwa kazi kubwa aliyoifanya na hivyo kumsisitizia kwamba ni lazima ashirikiane na Backnon kuhakikisha wanawateka watu hao na kuondoka nao.
Kilichokuwa kimepangwa kutumiwa ndani ya nyumba hiyo na kuwapata kilikuwa ni dawa ya usingizi lakini baada ya kufikiria sana wakagundua kitu kizuri ambacho kilitakiwa kutumika ni kuwawekea sumu kwenye matunda ambapo baada ya kula tu, walewe na kulala na kisha Kennedy awachukue na kuondoka nao.
Hilo lilionekana kuwa wazo zuri, akakubaliana nao na hivyo kuendelea na maisha ya huko nchini Iraq kama kawaida. Hakuacha kuonyesha mapenzi kwa Nurat, alijua kabisa kulikuwa na kazi ngumu, ilikuwa ni lazima akubalike kabla ya kufanya lile alilotaka kulifanya.
Hakuacha kufanya mambo na serikali ya nchi hiyo, alihakikisha anawafanyia kila kitu walichokuwa wakitaka, alifanya mambo mengi, alikutana na mawaziri mpaka Rais Hamis ambaye alimsifu kwa kuwa alifanya mambo mengi kwa ajili ya nchi yake.
Kwenye mazungumzo yao mengi na rais huyo alimwambia wazi kwamba katika maisha yake alikuwa akiichukua Marekani na nchi za Ulaya kwa sababu zilimtenganisha na familia yake.
Kwa stori yake ya uongo alimwambia kwamba familia yake iliuawa na Wamarekani baada ya kugundulika kwamba baba yake alikuwa akishirikiana na Waarabu katika mambo nyeti kabisa hivyo ili kumaliza ishu hiyo ilikuwa ni lazima waiteketeze familia yake pia.
“Wewe uliponaje?” aliuliza Rais Hamis huku akimwangalia Kennedy.
“Kipindi hicho nilikuwa nikisoma Urusi. Baba pia alikuwa na uhusiano mzuri na Warusi hivyo alizungumza na rais wa huko kwamba nilitakiwa kulindwa kwa kuwa ningeuawa muda wowote ule kwa sababu tayari kulikuwa na taarifa taifa la Marekani lilitaka kuimaliza familia yetu,” alisema Kennedy kwa huzuni kabisa, kwa jinsi alivyoonekana, ilikuwa ni rahisi kusema kile alichozungumza mahali hapo kilikuwa kweli kabisa.
Walizungumza mambo mengi na Rais Hamis pasipo kugundua kwamba mazungumzo yake yalikuwa yakinaswa na Wamarekani ambao walikuwa maadui zake wakubwa.
Walifurahia na kula pamoja huku wakipiga stori mbalimbali mahali hapo. Baada ya kumaliza, akaondoka zake kurudi hotelini.
Kesho, magazeti ya nchi hiyo yote yalikuwa na habari kuhusu Kennedy aliyekuwa akijulikana kwa jina la Ibrahim. Aliheshimika kila kona, alipendwa na wengi kuona kwamba alikuwa mtu muhimu sana ambaye Mungu alimtuma ndani ya nchi hiyo kwa ajili ya kuleta neema humo.
Hakukuwa na mtu yeyote aliyegundua kama mwanaume huyo alikuwa adui namba moja. Maofisa wa usalama wa taifa kutoka nchini humo walifuatilia kuujua undani wa mwanaume huyo lakini hawakugundua kitu zaidi ya kuonyesha alikuwa bilionea mkubwa nchini Kenya ambaye alifika humo kwa ajili ya kutembelea sehemu zilizokuwa na makumbusho ya mitume na kufanya mambo mengine ya biashara ya mafuta.
Hakutaka kuwaonyeshea kama alikuwa mtu hatari, aliwaambia nchini humo kulikuwa na mtu ambaye alikuwa rafiki yake, alikutana naye kupitia binti yake aliyeitwa Nurat.
Alimtambulisha mzee Shabir kwamba ndiye aliyekuwa mwenyeji wake, walizungumza mambo mengi na hivyo kila mmoja kumkubalia kwamba alikuwa mtu mzuri.
Hapo Baghdad akawasiliana na Backnon na kumwambia kwamba walitakiwa kutafuta dawa ambayo ingewekwa kwenye sindano na kuchomwa kwenye matunda ambayo watu hao walitakiwa kula.
Hilo halikuwa tatizo, dawa hiyo ikatafutwa na kupewa, akaambiwa kwamba ni lazima ayachome matunda hayo ambayo yangepelekwa huko na watu hao kulishwa.
Akapanga na Backnon kwamba siku hiyo achukue gari lake na kwenda kulipaki mbali kidogo na sehemu ambayo kulikuwa na nyumba hiyo kwa sababu wakati ambao angetoka na watu hao kwa kutumia gari la mzee Shabir basi aondoke nao na kuwaingiza ndani ya gari hilo na kwenda kwenye nyumba ambayo alikuwa akiishi.
Siku ambayo alipanga kufanya tukio hilo, kwanza yeye ndiye aliyehusika katika kuyanunua matunda hayo, aliagiza ya kutosha na yalipopelekwa kwa mzee Shabir, alihakikisha anachukua sindano yake na kuanza kuyachoma huku akijifanya kuendelea kufanya kazi nyingine.
Ilikuwa ni vigumu kugundua, kanzu ambayo aliivaa ilificha kila kitu, ilikuwa ni kwa siri kubwa, hakukuwa na yeyote ambaye aligundua na sehemu ambayo matunda hayo yalikuwa yakihifadhiwa ilikuwa ni kwenye kibanda kimoja.
Matunda hayo yakiwemo maembe, ndizi, matango, machungwa na mengine yalichomwa na hivyo usiku kuyachukua na kuanza kuelekea katika nyumba ile waliyokuwa wakiishi wale wataalamu wa kutengeneza mabomu ya nyuklia.
Njiani walikuwa wakizungumza mambo mengi, siku hiyo Kennedy alionekana kuwa mchangamfu mno, alizungumza mfululizo huku akimwambia mzee huyo ni kwa jinsi gani alitakiwa kufanya biashara zake na kufanikiwa. Aliaminika kwa sababu tu maisha yake yenyewe yalikuwa ni ya kifahari sana.
“Hutakiwi kudharau biashara ndogo,” alisema Kennedy huku akimwangalia mzee huyo aliyekuwa akiendesha gari.
“Kwani utajiri wako ulianzia huko?”
“Ndiyo! Nilianza kwa kuuza vitambaa vya suti, nakumbuka enzi hizo Waafrika hawakuwa wakivaa suti kabisa,” alisema.
“Sasa ilikuwaje mpaka kufanikiwa?”
“Ilikuwa ni vigumu mara ya kwanza lakini baada ya televisheni kuingia na watu kuona Wazungu wakivaa suti, wakapenda na hivyo kuja kununua kwangu,” alisema Kennedy.
“Oh! Kweli hatari! Ulivumilia sana!”
“Ndiyo! Kwenye biashara ni lazima uvumilie, kuna wakati unakutana na watu ambao wanajaribu kukukatisha tamaa kwa kusema kwamba huwezi, ukikubaliana nao, umepotea,” alisema Kennedy.
“Aisee kweli kabisa.”
Walizungumza kuhusu mafanikio, hayo yote alihitaji kuaminika na mzee huyo, hakutaka kumuonyesha kama kulikuwa na jambo lolote lililokuwa likiendelea.
Safari ilikuwa ikiendelea na baada ya dakika kadhaa wakafika katika nyumba hiyo na kuanza kuyashusha matunda hayo. Wakayaingiza ndani na kuwawekea watu hao, hilo halikuonekana kuwa jambo zuri kwa sababu Kennedy alitaka watu hao wale matunda hayo na kufanya mambo yake, akaanza kuwagawia.
Hilo lilikuwa jambo geni kwa mzee Shabir, si kwake tu bali hata kwa watu wale. Walimuona kuwa mtu wa ajabu, kwa Uarabuni kufanya tukio kama hilo ilikuwa ni nadra sana, ilionyesha ni kwa kiasi gani alikuwa na mnyenyekevu.
Walifurahia, wakayapokea na kuanza kula. Hakuishia hapo, aliwafuata walinzi na kuwapa matunda yale. Wote waliona kwamba alikuwa mtu mkarimu, hawakujua kama upande wa pili mwanaume huyo alikuwa na mipango yake.
Mzee Shabir akafurahi sana, kwake, kile alichokiona kikifanywa na mtu aliyekuwa na pesa kama Ibrahim ilikuwa ni kama muujiza. Alimwangalia mwanaume huyo, siku hiyo alidhihirisha hakuwa mtu wa majivuno, alikuwa mtu mpole na mkarimu ambaye kila mtu alitakiwa kuiga mfano kwake.
“Mbona wananishangaa?” aliuliza Kennedy huku akimwangalia mzee Shabir.
“Unavyowagawia matunda!” alijibu mzee huyo.
“Kwani kuna tatizo?”
“Ni heshima kubwa sana. Hilo wanatakiwa kufanya wanawake kwa wanaume, ila mwanaume kwa wanaume, unaonekana una heshima na mkarimu sana,” alisema mzee Shabir.
“Oh! Kumbe! Basi na wewe karibu,” alisema Kennedy huku akimpa ndizi mzee huyo.
Hakutaka kula lakini kwa sababu bilionea huyo alimuonyeshea heshima na ukaribu wa hali ya juu, naye akachukua na kuanza kula. Mpaka kufikia hapo tayari Kennedy aliona alifanikiwa kwani kila mtu aliyekuwa akimwangalia humo, alikuwa bize kula matunda.
Nchini Marekani walikuwa wakifuatilia kila kitu kupitia ile kamera aliyokuwanayo Kennedy, hawakuamini kama kazi ingekuwa nyepesi namna ile, kila mmoja akafurahi na kuona kwamba walifanikiwa kuwapata watu hao.
Ni ndani ya dakika kumi tu, kila mmoja akawa hoi, macho yakawa mazito, wakakaa chini na kulala, walinzi waliokuwa na bunduki zao, zikawaanguka na wao kulala, ile dawa ya usingizi iliyowekwa kwenye matunda yake ikaanza kufanya kazi kwa kasi.
“Mbona wanalala?” aliuliza Kennedy, alikuwa akimuuliza mzee Shabir ambaye naye macho yake yalianza kuwa mazito.
“Sijajua kwa nini! Hata mimi macho yangu yashaanza kuwa mazito, hebu subiri nikae hapa kwanza,” alisema mzee huyo, akakaa pembeni na kulala.
Yote yaliyokuwa yakitokea, Kennedy alikuwa akiangalia tu, kazi yake ilikuwa ni kuhesabu ni watu wangapi walikuwa wakiendelea kulala.
Humo kulikuwa na watu zaidi ya ishini, wote wakalala, hakutaka kuwa na presha, akachukua simu yake na kumpigia Backnon na kumwambia asogeze gari kwani tayari alifanikiwa kwa kila kitu.
Gari hilo likasogezwa na kuwachukua watalaamu hao, wakawapakiza ndani ya gari na kuondoka nao kuelekea kule alipokuwa amepanga Backnon kwani ilikuwa ni lazima sehemu hiyo itumiwe kwa ajili ya kuhakikisha wanapata formula hiyo.
Hawakuchukua muda mrefu, wakafika humo na kuwaingiza ndani, kila kitu kilikuwa kimeandaliwa, kulikuwa na watalaamu wanne, viti vyao vilikuwa tayari, wakakalishwa kisha kuvumiliwa nguo zote, wakawekewa nyaya za umeme mbavuni na sehemu za siri huku wakiwa usingizini.
Wakawafunga mikono na miguu, midomoni mwao wakawafunga gundi nzito ambayo isingekuwa rahisi kwao kufumbua midomo na kusema neno lolote lile.
Baada ya kila kitu kukamilika, wakapokea simu kutoka nchini Marekani ambapo huko walikuwa wakifuatilia kila kitu, wakawaambia kwamba walitakiwa kufanya lolote liwezekanalo kuhakikisha wanatoa siri zote vinginevyo basi wawamalize kwani hawakuwa na muda mrefu wa kukaa nchini humo.
“Hilo usijali! Ngoja wapate fahamu, watatuambia kila kitu, kwenye kazi zetu hamtakiwi kuwa na hofu hata kidogo,” alisema Kennedy, katika maisha yake yote hakuamini kama kungekuwa na mtu ambaye angejifanya kuwa mgumu kwake, alijiamini na kwa jinsi alivyowaangalia watalaamu wale, ilikuwa ni lazima wamwambie kile alichokuwa akikihitaji.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumanne.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…