Serikali yadai upatu wa PUFDIA ni mbaya kuliko Deci

Msindima

JF-Expert Member
Mar 30, 2009
1,018
33
WAKATI jamii ikiendelea kufikiria hatima ya wachama zaidi ya 300,000 wa taasisi ya Deci, serikali imesema athari za taasisi hiyo ni ndogo kuliko za taasisi ya People’s Unity for Development in Africa (PUFDIA).

Deci imesimamisha shughuli zake huku viongozi wake wanne wakiwa wamefunguliwa mashtaka ya kuendesha shughuli za ukusanyaji amana za watu kinyume cha sheria, wakati PUFDIA inaendelea na shughuli zake za kukusanya fedha kwa ajili ya shughuli mbalimbali.

Kwa mujibu wa masharti ya PUFDIA, mteja anayetaka kujengewa nyumba anatakiwa kutoa Sh470,000, wakati shule Sh670,000 na anayetaka kusomesha mtoto anatakiwa kutoa Sh100,000.

Baada ya kutoa fedha hiyo, kampuni inatakiwa kutoa ufadhili wa Sh1,140,000 kwa wanafunzi wa shule za msingi, Sh1,900,000 kwa sekondari kidato cha kwanza hadi cha nne, wakati kwa mradi wa ujenzi wa nyumba wanatoa ufadhili wa Sh6 milioni na shule Sh46 milioni.

Lakini jana Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo alisema uchunguzi mdogo uliofanywa na serikali umebaini kuwa athari za PUFDIA ni kubwa kuliko Deci.

Alifafanua kuwa wakati kuna wanachama wa Deci ambao wamekwishanufaika kwa kuvuna fedha mara mbili ya zile walizowekeza, hakuna mwanachama yeyote aliyewahi kunufaika na huduma za kampuni ya PUFDIA tangu ianze.

Alisema baada ya kubaini hilo, serikali imeanza kuifuatilia kampuni hiyo ambayo maelfu ya Watanzania wamejiunga.

“Nimezungumza na wakubwa na tayari wameanza kuifanyia kazi kikamilifu," alisema waziri huyo wa fedha.

"Ukiangalia athari za kampuni hii ni kubwa zaidi kuliko hata za Deci kwa sababu angalau watu wachache walifaidika Deci, lakini hii watu hawajapata chochote.”

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika baadhi ya matawi ya kampuni hiyo, umebaini kuwa shughuli za kuwahudumia wateja wanaotaka kujiunga, bado zinaendelea.

Tayari maelfu ya watu wamejiunga na kampuni hiyo yenye matawi karibu nchi nzima kwa matumaini ya kusomeshewa watoto wao, kujengewa nyumba, shule pamoja na kupata mikopo isiyokuwa na riba.

Uchunguzi wa Mwananchi ulibaini kuwa wanachama wengi waliojiunga na kampuni hiyo wameandikisha mtoto zaidi ya mmoja ikiwa ni pamoja na kujiandikisha wao wenyewe kwa zaidi ya jina moja ili wajengewe shule pamoja na nyumba za kuishi.

Kampuni hiyo ilianza kama taasisi ya kuwasaidia Wakristo na baadaye kutangazwa kuwa ni ya Watanzania wote.

Kwa mujibu wa kumbukumbu za Msajili wa Makampuni (Brela), PUFDIA ilisajiliwa rasmi Februari 18 mwaka 2008 na inamilikiwa na watu saba, wakiwemo raia watatu wa Uganda.

Moja ya masharti ya kujiunga na kampuni hiyo ni pamoja na mteja kuwa mvumilivu na mpole wakati fedha zinapochelewa.
“Wateja wetu wote mnatakiwa kuwa wavumilivu, wapole wakati njia za kufuatilia fedha zinapochelewa au kuchukua muda mrefu,” inasema sehemu ya maelezo yaliyo kwenye fomu ya kujiunga na kampuni hiyo.
 
Ama kweli Serikali imelala fofofo mpaka wananchi wake wanaibiwa fedhwa hivihivi.

Poleni sana
 
Back
Top Bottom