Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,299
- 33,082
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Balozi Herbert Mrango
Wizara ya Ujenzi, imesema kuwa miradi sugu ya ujenzi wa barabara iliyokuwa imekwama kutokana na madeni tayari ujenzi umeanza kwa kuwa wameshawalipa wakandarasi fedha zao.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Balozi Herbert Mrango, katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam ambapo alieleza kuwa fedha walizopatiwa ni Sh. bilion 200 kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi na kwamba zoezi la ulipaji lilimalizika mwishoni mwa mwaka jana.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, serikali imewalipa wakandarasi mbalimbali nchini na kuongeza kuwa kwa sasa miradi ya ujenzi wa barabara inaendelea vizuri.
Alieleza kuwa malipo ya madeni ya wakandarasi yanafanyika kwa kutumia hati za madai iliyoidhinishwa na Mhandisi Mshauri anayesimamia mradi husika na hati hizo huwasilishwa kwa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) ili kuzipitia hati hizo.
Baada ya kuziangalia hati hizo huwasilishwa wizarani kwa ajili ya kuombea fedha za malipo kutoka Hazina, alisema.
Kadhalika, taarifa hiyo ilieleza kuwa mkandarasi M/S CHICO-CRSG JV anayejenga barabara ya Kagoma -Lusahunga iliyoko mkoa wa Kagera kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilometa 154 kwa gharama ya Sh. bilioni 191.4 ameshalipwa fedha zake kwa asilimia 59 ya gharama za mradi huo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mradi huo umefikia asilimia 60 ambapo jumla ya kilometa 88 tayari zimewekwa lami kati ya kilometa 154.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa malipo ya wakandarasi yamefuata taratibu za kisheria ambazo zinatakiwa kufuatwa na hakuna malipo hewa ambayo yamefanyika kwa mkandarasi CHICO-CRSG JV kama inavyodaiwa.
Akitolea ufafanuzi kuhusiana na mabadiliko yaliyofanywa ndani ya wizara, Tanroads pamoja na taasisi nyingine iliyoka katika wizara hiyo, Balozi Mrango alieleza kuwa suala hilo limefanywa kwa lengo la kuongeza ufanisi wa kazi na pia walifuata taratibu za kisheria katika suala hilo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mabadiliko hayo yamesaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufanisi wa kazi katika utendaji wa majukumu yao.
Hata hivyo, taarifa ya Balozi Mrango haikueleza kiasi cha deni lililobaki, lakini kwa mujibu wa taarifa zilizoko zinaonyesha kuwa wakandarasi walikuwa wanaidai serikali Sh. bilioni 425. Kwa mana hiyo, wakandarasi hao kwa sasa wanaidai serikali Sh. bilioni 225.
CHANZO: NIPASHE