Rushwa ya wazi katika majimbo-Rais uko wapi?

Regia Mtema

R I P
Nov 21, 2009
2,970
863
MATUMIZI ya fedha kwa ajili ya kujiweka katika nafasi nzuri kuteuliwa kugombea ubunge katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) yameshika kasi miezi minne kabla ya uteuzi rasmi utakaodhibitiwa kwa Sheria ya Gharama za Uchaguzi ambayo imepitishwa na Bunge hivi karibuni, badala ya kanuni za chama hicho zisizoheshimika tena miongoni mwa vigogo wake, Raia Mwema imefahamishwa.
Uchunguzi wa Raia Mwema na taarifa za ndani ya CCM na vyombo vya dola, vimethibitisha kuwa kuna majimbo katika mikoa zaidi ya 14 ya Tanzania Bara na Visiwani, ambako tayari fedha zimekwisha kuanza kutolewa kufanikisha ushindi, kila mwanasiasa kwa staili yake, baadhi wakiwa ni viongozi waandamizi wa serikali wakiwamo mawaziri, makatibu wakuu na hata maofisa wa ofisi nyeti za umma walio karibu na ‘wakubwa.’
Hali hiyo inaendelea wakati tayari utafiti wa wasomi Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) ukibainisha kuwa CCM ambayo miongoni mwa ahadi kwa wanachama wake ni kutambua kuwa “rushwa ni adui wa haki,” kinaongoza katika masuala ya utoaji rushwa wakati wa michakato ya uchaguzi, na uchaguzi uliopita wa serikali za mitaa umedhihirisha usugu wa chama hicho katika vitendo vya rushwa.
Utafiti huo wa UDSM, ulitolewa mwishoni mwa wiki iliyopita, jijini Dare es Salaam, ukipewa jina la Mapambano ya Rushwa kwenye Serikali za Mitaa, ukigusa vijiji, vitongoji, mitaa na kata. Katika utafiti huo, CCM inaongoza katika kujihusisha kwenye vitendo vya rushwa kwa kupata asilimia 49.5, Chadema kikipata asilimia saba, CUF 2.7, NCCR-Mageuzi kikipata asilimia 0.5 kama ilivyo pia kwa TLP.
Kutokana na mkanganyiko huo, CCM makao makuu kupitia kwa Katibu wake wa Uenezi, John Chiligati imetangaza rasmi kuwa yeyote mwenye malalamiko ya viongozi kutaka ubunge kwa kutoa rushwa wakaripoti (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa) TAKUKURU moja kwa moja kwa kuwa hayo ni makosa ya jinai, yaliyo nje ya chama.
Uchunguzi wa Raia Mwema kwa miezi kadhaa sasa umebaini kuwa majimbo kadhaa katika mikoa hiyo yameingia katika pilikapilika zinazohusisha baadhi ya wagombea watarajiwa na wabunge wa sasa kuwamo katika mikakati ya kujiimarisha kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho hasa ngazi wilaya na kata katika jimbo husika kwa kutumia nguvu ya fedha, katika kile kinachoelezwa kuwa “kujipanga kabla ya Sheria ya Gharama za Uchaguzi kuanza kutumika na kabla TAKUKURU hawajazinduka”.
Miongoni mwa wanaotuhumiwa kutoa fedha kwa baadhi ya viongozi wakiwamo wa ngazi ya majimbo ni pamoja na baadhi ya mawaziri wanaotetea nafasi zao, mawaziri wanawake wanaolenga kuwania ubunge katika majimbo ili kujiengua kwenye ubunge wa viti maalumu; viongozi waandamizi wa CCM baadhi wakiwa makao makuu ya chama hicho; pamoja na makada wengine wanaofanya kazi katika ofisi za serikali na hata taasisi binafsi.
Kwa upande mwingine, imebainika kuwa hata baadhi ya wabunge wa sasa wamelazimika kutumia mbinu hizo zinazotumiwa na washindani wao huku baadhi yao wakiripotiwa kutoendelea na mbinu hizo wakitegemea kuokolewa na Sheria ya Gharama za Uchaguzi, pindi itakapoanza kutumika, baadhi wakikusanya ushahidi utakaowawezesha kuwashughulikia wapinzani wao.
Hali hiyo inajitokeza katika wakati ambao tayari Bunge limepitisha Muswada wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi ambao bila shaka utaisiniwa na Rais, sheria ambayo itatumika kuanza kudhibiti matumizi ya fedha kuanzia mchakato wa uteuzi wa wagombea ndani ya vyama. Lakini hali halisi inaonyesha kuwa ni kama vile wagombea watarajiwa wameiwahi sheria hiyo inayotarajiwa, wakianza kumwaga fedha tangu miezi kadhaa iliyopita, mchakato ambao unaendelea hadi sasa.
Mwanzo ni wabunge wachache tu waliokuwa wakitoa kilio cha fedha kupenyezwa majimboni mwao, hasa Spika wa Bunge, Samuel Sitta na Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe. Leo idadi hiyo ya majimbo yenye kupokea fedha yameongezeka.
Yanayotajwa sasa ni pamoja na ya Mikoa ya Morogoro, Tanga, Arusha, Kigoma, Shinyanga, Mara, Mwanza, Tabora, Mbeya, Ruvuma, Dar es Salaam, Pwani, Kilimanjaro na Kagera. Mkoani Morogoro, majimbo yenye utata ni pamoja na Mvomero ambalo Mbunge wake ni Suleiman Sadiq; Morogoro Mjini linaloongozwa na Dk. Mzeru Nibuka; Morogoro Kusini Mashariki linaloongozwa na Sameer Lotto, Kilombero linaloongozwa na Castor Ligallama na Mikumi linaloongozwa na Clement Lyamba.
Mkoani Tanga, mvutano na madai ya kuwapo kwa matumizi ya fedha kwa njia ya siri yanajitokeza zaidi katika Jimbo la Kilindi linaloongozwa na Beatrice Shellukindo, Lushoto linaloongozwa na Balozi Abdi Mshangama; Mkinga linaloongozwa na Mbaruk Mwandoro; Muheza linaloongozwa kwa sasa na Herbert Mtangi; Korogwe Vijijini linaloongozwa na Laus Mhina na Handeni linaloongozwa na Dk. Abdallah Kigoda.
Mkoani Arusha, matumizi ya fedha yameanza kwa miezi kadhaa sasa katika Jimbo la Arusha Mjini linaloongozwa na Felix Mrema, Arumeru Magharibi kwa Elisa Mollel; Simanjiro kwa Christopher ole Sendeka; Monduli linaloongozwa na Edward Lowassa; Longido kwa Michael Laizer na Ngorongoro kwa Kaika Telele.
Kigoma kasi ya matumizi ya fedha imejitokeza katika Jimbo la Muhambwe linaloongozwa na Felix Kijiko ambaye hivi karibuni amehutubia mkutano jimboni humo akidai kuwa baadhi ya wanaogawa fedha hizo wamezipata kwa kufanya ujambazi na inawezekana wengine kwa kuuza viungo vya albino.
Jimbo jingine ni Kigoma Kaskazini ambalo licha ya kuongozwa na Kabwe Zitto wa Chadema, CCM wanachuana wakiamini chama chao kitashinda.
Mbali na Muhambwe pamoja na Kigoma Kaskazini, jimbo jingine ambalo fedha inatumika kuandaa ushindi wa baadhi ya wagombea ni Kigoma Mjini, ambalo kwa sasa Mbunge wake ni Peter Serukamba, ambaye anatarajiwa kutetea nafasi yake hiyo katika uchaguzi ujao.
Kutoka Shinyanga, majimbo ya Kishapu linaloongozwa na Fred Mpendazoe, Shinyanga Mjini linaloongozwa na Dk. Charles Mlingwa, Maswa linaloongozwa na John Shibuda, Bariadi Mashariki kwa John Cheyo ambako wana-CCM wanaamini watalitwaa jimbo hilo na Kahama kwa James Lembeli nako matumizi ya fedha yako wazi . Majimbo hayo yanahusishwa na mgawo wa fedha kwa lengo hilo la kusaidia ushindi wa baadhi ya wagombea. Fedha hizo inaaminka zinatoka kwa wafanyabiashara wakubwa.
Jimbo la Bunda mkoani Mara linaloongozwa na Steven Wassira ambaye ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika hali si swari kwa upande wa matumizi ya fedha, viongozi wa CCM wakitajwa kugawanyika chanzo kimojawapo kikitajwa kuwa ni nguvu ya fedha, chanzo kinachofichwa nyuma ya pazia la utendaji unaodaiwa hauridhishi wa mbunge huyo. Musoma Mjini linaloongozwa na Vedasto Manyinyi, matumizi ya fedha yameripotiwa.
Jijini Mwanza, Jimbo la Nyamagana linaloongozwa na Lawrance Masha ambaye ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Busega kwa Dk. Raphael Chegeni, Sumve kwa Richard Ndassa, Busanda kwa Lolensia Bukwimba, Buchosa kwa Samuel Chitalilo, Magu Mjini kwa Dk. Festus Limbu na Geita kwa Ernest Mabina kote kunatajwa kuwa fedha nyingi.
Mkoani Tabora kiwewe cha kujiweka sawa kiushindi kwa kutumia nguvu ya fedha kimehamia Tabora Mjini, jimbo linaloongozwa na Siraju Kaboyonga, baada ya hali hiyo kuanza kupoa katika majimbo ya Urambo Mashariki kwa Samuel Sitta na Nzega kwa Lucas Selelii ikilinganishwa na awali. Majimbo mengine ni Igalula kwa Tatu Ntimizi na Tabora Kaskazini kwa Dk. James Msekela ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.
Mbeya baada ya kelele za muda mrefu katika Jimbo la Kyela, ushindani wa kujiimarisha kwa nguvu ya fedha umebisha hodi katika Jimbo la Mbeya Mjini linaloongozwa na Benson Mpesya, Lupa linaloongozwa na Victor Mwambalaswa na Mbeya Vijijini ambalo kwa sasa mbunge wake ni Mchungaji Lakson Mwanjale.
Kutoka Ruvuma majimbo yaliyoingia katika orodha ya kugawa fedha ni pamoja na Songea Mjini kwa Dk. Emmanuel Nchimbi, Mbinga Magharibi kwa Kapteni John Komba huku Jimbo la Mbinga Magharibi kwa Gaudence Kayombo, likitajwa kuwindwa.
Jijini Dar es Salaam, ushindani wa kujiimarisha ili kupata ushindi ni mkubwa karibu katika majimbo yote. Jimbo la Ubungo, ambalo kwa lugha ya wana-CCM linatajwa kuwa wazi viongozi wa kata mbalimbali za jimbo hilo wamekuwa wakipata fedha za mmoja wa wagombea watarajiwa. Majimbo mengine ya Ilala, Temeke, Kawe, Ukonga na Kinondoni hali ya ushindani ni kubwa na hasa ushindani wa kujiweka karibu na viongozi wa kata kwa kuhusisha fedha.
Kutoka mkoani Pwani, Jimbo la Mkuranga kwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Malima, Kisarawe kwa Othman Janguo na Kibaha mjini kwa Dk. Zainab Gama ambako wasomi wengi wanalenga kutwaa jimbo hilo linalochangamshwa na Shirika la Elimu Kibaha, hakuna usalama katika matumizi ya fedha.
Kilimanjaro tayari timu za baadhi ya wagombea watarajiwa ziko kazini kuwang’oa wabunge wa sasa na katika majimbo ya upinzani na hasa Moshi Mjini kwa Philemon Ndesamburo, nguvu zaidi imeongezwa ikihusisha vijana kutoka Umoja wa Vijana wa CCM. Hata hivyo, hali ya ushindani mkoani Kilimanjaro ni kubwa zaidi nje ya CCM ambako wagombea wa vyama vya upinzani wanaonekana kukubalika.
Kati ya viongozi wanaotajwa kutaka kuhujumiwa kwa kutumia fedha chafu ni pamoja na Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Cyril Chami wa Moshi Vijijini ambako inaelezwa kwamba mmoja wa watu wenye uhusiano na watuhumiwa katika makosa mbalimbali ya jinai, ameelezwa kuwekeza fedha nyingi katika jimbo hilo akisukumwa zaidi na baadhi ya watuhumiwa hao.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe anaelekea kuwa katika wakati mgumu baada ya wazee waliomsimamia alipoingia katika siasa kumtupa mkono na sasa wanaelezwa kumpigia chapuo mwanasheria, Joseph Tadayo, ambaye ameelezwa kumchanganya waziri huyo kiasi cha yeye naye kuanza kuingia katika harakati za kujinasua.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Dk. Mathayo David Mathayo katika jimbo la Same Magharibi amepata wapinzani wanaonyemelea jimbo huku na Mbunge wa Hai, Fuya Kimbita, akipata kiwewe baada ya kuibuka tena kwa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, ambaye ndiye anayetajwa kuwa ‘mmiliki’ wa jimbo hilo.
Mkoani Kagera matumizi ya fedha kusaka ushindi katika uteuzi yanaripotiwa katika majimbo yote ya Muleba, ambayo ni Muleba Kusini kwa Wilson Masilingi, Muleba Kaskazini kwa Ruth Msafiri. Majimbo mengine yaliyoingia katika kashfa ya mapema ya matumizi ya fedha kwa mujibu wa taarifa zilizotufikia ni Karagwe kwa Gosbert Blandes, Ngara kwa Profesa Feethan Banyikwa na Kyerwa kwa Eustace Katagira.
Katika mazungumzo yake na Raia Mwema, Chiligati alisema CCM tayari kimekataza masuala ya rushwa na kwamba kama kuna mwanachama au kiongozi anajihusisha na rushwa afikishwe moja kwa moja katika Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Alipoulizwa kuhusu msimamo wa chama hicho kwamba matatizo au migogoro miongoni mwa wanachama au viongozi wake humalizwa kwenye vikao, Chiligati alisema; “Suala la rushwa ni kosa la jinai, si suala la kisiasa. Matumizi ya fedha kupata uongozi ni uvunjaji wa sheria, wanaofanya hivyo wanatia aibu. Kwa hiyo yeyote mwenye ushahidi aende moja kwa moja TAKUKURU si kusubiri chama.”


Hoja zangu!
Kama rushwa ndio zimeanza kwa fujo kiasi hiki na Rais amekaa kimya eti anasubiri mpaka sheria ya matumizi ya fedha ya uchguzi ianze kufanya kazi,hivi kweli atafanikiwa?Hivi rushwa inatambulika mpaka uchaguzi mkuu uanze?na je kwenye kura za wali ambako nako kuna rushwa za kutisha itadhibitiwaje? Rais anasemaje katika hili?Hizo double standards till when? Kikwete be serious hebu dhibiti na huku basi.

hs3.gif
 
Muheshimiwa Mkuu amekuwa kaka simba dume aliyeng'ofolewa makucha na kung'olewa meno....... ni wale zamani tulikuwa tunawaita...."simba wa kibisa"
 
Back
Top Bottom