gilbert35
JF-Expert Member
- Nov 20, 2021
- 253
- 476
RIWAYA: HATARI
Imeandikwa na Halfani SUDY
SIMU 0629 360357
Hii ni sehemu ya kwanza.
MLANGO wa ofisi yake ulisukumwa kwa nguvu, kwa haraka, macho mawili ya Daniel Mwaseba yaliangalia pale mlangoni. Na kwa haraka ileile ya macho, mkono wake wa kuume ulikuwa umeshafika kiunoni kwake na kuichomoa bastola yake ndogo, nyeusi, mdomo wa bastola ulikuwa umeelekea pale mlangoni, huku kidole chake cha shahada kikiwa kimekigusa kibonyazio.
“Ni nani wewe?” Daniel Mwaseba aliuliza kwa pupa baada ya macho yake kumtazama mtu aliyeingia kwa ghafla ofisini kwake. Hakulipata jibu la swali lake, aliupata mshangao, kwa maana ghafla yule mtu alidondoka chini, huku akitoa mguno mkubwa kuonesha kwamba alikuwa anapitia katika maumivu makali sana.
Kwa umakini mkubwa, Daniel alikisukuma kiti alichokuwa amekikalia kwa kutumia paja lake la mguu wa kulia. Akapata nafasi ya kupita kuelekea pale mlangoni alipoangukia yule mtu. Huku mkono wake wa kulia ulioishika imara bastola yake ukielekea katika mlango, wakati macho yake yakimtazama yule mtu aliyelala kifudifudi mbele kidogo ya mlango.
Ndipo macho yake yalipoona, michirizi ya damu kutoka kwa yule mtu ilikuwa inaelekea chini ya meza yake. Daniel hakuamini kwamba lile anguko ndilo lililosababisha ile michirizi ya damu!
“Ni nini hiki kinatokea?” Daniel alijiuliza mwenyewe huku kwa umakini mkubwa akimsogelea yule mtu. Hakukuwa na wa kumjibu swali lake, kwa maana mle ndani alikuwa yeye na yule mtu aliyekuwa hajiwezi kwa lolote.
Hatua za Daniel zilimfikisha mahali alipolala yule mtu, kwa mkono wake wa kushoto alitoa vilinda mikono katika mfuko wake wa nyuma wa suruali na kuvivaa. Akainama taratibu na kumshika yule mtu, huku akiwa makini sana na mlango. Hisia zake zilimwambia kwamba ule ulikuwa mtego. Alifanikiwa kumgeuza yule mtu, sasa alikuwa anaitazama sura yake.
Kwa makadirio tu, alikuwa anatazamana na mzee wa zaidi ya miaka sitini. Ngozi ya sura yake, rangi ya nywele zake yalithibitisha makadirio ya umri ya Daniel Mwaseba. Wakati Daniel akitafakari cha kufanya, yule mzee alifumbua macho yake kwa shida sana, huku akijitahidi kusema maneno ambayo hayakueleweka na masikio ya Daniel, zaidi ya kushuhudia mabonge mazito ya damu yakimtoka mdomoni.
“Yanipasa kumpeleka hospitali huyu mzee” Daniel aliwaza kichwani kwake. Na kweli, hali ya yule mzee ilihitaji kitu kimoja tu, kupelekwa hospitali. Kwa maana sio tu hakuweza kusimama kwa miguu yake, bali pia hakuweza hata kuuinua ulimi wake mwenyewe na kuongea. Tatizo lilikuwa sasa, Daniel hakumjua yule mtu ni nani?
Hakujua kama yule mtu amekuja kwake kwa bahati mbaya au makusudi. Kama alifika pale kwa bahati mbaya hakukuwa na tatizo sana, lakini kama alifika pale kwa makusudi, basi kulikuwa na tatizo, na bila shaka ni tatizo lililoambatana na hatari kubwa sana.
Daniel alitoa simu yake mfukoni kwa mkono wa kushoto. Alibofyabofya kutafuta namba ya mtu, alipoipata, aliipiga.
“Hallo Dokta Tawakal?” Daniel aliita simuni.
“Hallo Daniel, habari za masiku?” Dokta Tawakal alijibu kwa kuchangamka na kuuliza swali.
“Salama Dokta Tawakal, nipo sehemu mbaya kidogo, ninaomba tukutane nyumbani kwangu baada ya nusu saa, nina dharura kubwa sana. Hakikisha hakuna anayejua kama unakuja kwangu” Daniel alisema harakaharaka.
“Kuna nini Daniel?” Dokta Tawakal aliuliza kwa sauti iliyoambatana na uwoga.
“Naomba tukutane nyumbani kwangu baada ya nusu saa, nitakueleza kila kitu, hapa nilipo sio sehemu sahihi kukueleza hayo maswali unayoniuliza” Daniel alisema tena kwa haraka.
“Ok sawa, tukutane nyumbani kwako baada ya hiyo nusu saa” Dokta Tawakal alikubali.
Simu ikakatwa.
“Sasa nitamtoaje nje huyu mtu?” Daniel alijiuliza mwenyewe. Ofisi ya Daniel Mwaseba ilikuwa maeneo ya Posta, katikati ya jiji la Dar es salaam. Katika jengo la Decade Tower, ghorofa ya kumi na nne, katika ofisi namba arobaini na tano. Haikuwa kazi ndogo hata kidogo kumtoa yule mtu akiwa katika hali ile, katika ghorofa namba kumi na nne hadi chini bila kuzua kasheshe!. Jengo la Decade Tower lilikuwa ulinzi mkali sana wa kutumia kamera za kisasa za CCTV, kamera zikizosaidiwa na walinzi wazoefu kutoka kampuni binafsi ya ulinzi, kwa idadi walikuwa zaidi ya hamsini, wao na kamera zao, kazi yao kuu ilikuwa ni kulinda usalama wa jengo la Decade tower.
“Yanipasa nimtoe huyu mtu bila mtu yeyote kujua” Daniel aliwaza huku akikuna kichwa kwa mkono wake wa kushoto. Alikuwa anawaza njia gani sahihi ya kumtoa yule mtu asiyemfahamu ndani ya ofisi yake na kwenda kumpatia matibabu. Baada kama dakika mbili za kuwaza mwenyewe, alipata jibu. Kwanza alianza kumpekua mifukoni yule mtu, hakuwa na kitu chochote kile katika mifuko yake. Alisogea hadi kabati lililokuwa limeegemezwa katika kona ya ofisi, akalifungua kwa kutumia funguo alioutoa mfukoni.
Akalitazama kabati kwa muda wa dakika tatu, akipiga mahesabu yake. Baada ya kuridhika, akarudi nyuma hadi katika meza yake, akafungua droo la upande wa kushoto, akatafutatafuta kwa sekunde kadhaa, lakini hakukiona kitu alichokuwa anakitafuta. Akarudi tena kwa yule mtu aliyekuwa bado amelala chini, akambeba huku akiruhusu damu nyingi zikichuruzikia sakafuni na kuchafua mandhari ya ofisi yake. Moja kwa moja akaelekea naye kwenye lile kabati lililokuwa wazi, akamkalisha hovyo ndani ya kabati, akalifunga kwa funguo kwa nje. Alielekea mlangoni na kutoka nje, akafunga mlango kwa kutumia kadi maalum.
Harakaharaka, alielekea katika chumba cha sita, ambacho kilikuwa ni stoo ndogo. Alichukua ndoo ya maji na skwiza. Alirejea navyo ofisini kwake. Alianza kusafisha ofisi yote, alihakikisha hayabaki mabaki ya damu hata kidogo. Akatoka tena nje akihakikisha amefunga mlango vizuri kwa kutumia ile kadi maalum, alienda kurudisha vile vifaa vya kudekia stoo, kisha alipanda lift na kumshusha hadi chini kabisa ya jengo. Moja kwa moja, alienda katika duka moja la zana za kilimo lilikuwa karibu na lile jengo la Decade Tower, akanunua mfuko mkubwa mweupe wa nailoni. Harakaharaka alirejea ofisini kwake kwa kutumia lift.
“Ili zile damu zake zisibubujike njiani lazima nimhifadhi kwenye huu mfuko” Daniel aliwaza wakati akiufungua mlango wa ofisi yake kwa ile kadi maalum. Akaingia ndani kuelekea katika kabati alilomweka yule mtu. Kwa kutumia mkono wa kushoto, alifungua mlango taratibu kwa kutumia funguo, wakati mkono wake wa kulia ukielekeza bastola kabatini.
Alichokutana nacho sasa….
Kwa mara ya kwanza tangu azaliwe Daniel Mwaseba hakuyaamini macho yake. Alibaki mdomo wazi, mkono wake wa kulia ulioshika bastola ulikuwa unatazamana na kabati tupu, amini usiamini, hakukuwa na mtu ndani ya lile kabati. Lilikuwa kabati tupu, tupu tupu tupu.
Haditi inaitwa Hatari, mwandishi wako anaitwa Halfani Sudy, tukutane tena kesho tuisome tena Hatari ndani ya riwaya hii ya aina yake.
Pia facebook tunapatikana kwa jina la Simulizi Za Gilbert. Tufollow
Imeandikwa na Halfani SUDY
SIMU 0629 360357
Hii ni sehemu ya kwanza.
MLANGO wa ofisi yake ulisukumwa kwa nguvu, kwa haraka, macho mawili ya Daniel Mwaseba yaliangalia pale mlangoni. Na kwa haraka ileile ya macho, mkono wake wa kuume ulikuwa umeshafika kiunoni kwake na kuichomoa bastola yake ndogo, nyeusi, mdomo wa bastola ulikuwa umeelekea pale mlangoni, huku kidole chake cha shahada kikiwa kimekigusa kibonyazio.
“Ni nani wewe?” Daniel Mwaseba aliuliza kwa pupa baada ya macho yake kumtazama mtu aliyeingia kwa ghafla ofisini kwake. Hakulipata jibu la swali lake, aliupata mshangao, kwa maana ghafla yule mtu alidondoka chini, huku akitoa mguno mkubwa kuonesha kwamba alikuwa anapitia katika maumivu makali sana.
Kwa umakini mkubwa, Daniel alikisukuma kiti alichokuwa amekikalia kwa kutumia paja lake la mguu wa kulia. Akapata nafasi ya kupita kuelekea pale mlangoni alipoangukia yule mtu. Huku mkono wake wa kulia ulioishika imara bastola yake ukielekea katika mlango, wakati macho yake yakimtazama yule mtu aliyelala kifudifudi mbele kidogo ya mlango.
Ndipo macho yake yalipoona, michirizi ya damu kutoka kwa yule mtu ilikuwa inaelekea chini ya meza yake. Daniel hakuamini kwamba lile anguko ndilo lililosababisha ile michirizi ya damu!
“Ni nini hiki kinatokea?” Daniel alijiuliza mwenyewe huku kwa umakini mkubwa akimsogelea yule mtu. Hakukuwa na wa kumjibu swali lake, kwa maana mle ndani alikuwa yeye na yule mtu aliyekuwa hajiwezi kwa lolote.
Hatua za Daniel zilimfikisha mahali alipolala yule mtu, kwa mkono wake wa kushoto alitoa vilinda mikono katika mfuko wake wa nyuma wa suruali na kuvivaa. Akainama taratibu na kumshika yule mtu, huku akiwa makini sana na mlango. Hisia zake zilimwambia kwamba ule ulikuwa mtego. Alifanikiwa kumgeuza yule mtu, sasa alikuwa anaitazama sura yake.
Kwa makadirio tu, alikuwa anatazamana na mzee wa zaidi ya miaka sitini. Ngozi ya sura yake, rangi ya nywele zake yalithibitisha makadirio ya umri ya Daniel Mwaseba. Wakati Daniel akitafakari cha kufanya, yule mzee alifumbua macho yake kwa shida sana, huku akijitahidi kusema maneno ambayo hayakueleweka na masikio ya Daniel, zaidi ya kushuhudia mabonge mazito ya damu yakimtoka mdomoni.
“Yanipasa kumpeleka hospitali huyu mzee” Daniel aliwaza kichwani kwake. Na kweli, hali ya yule mzee ilihitaji kitu kimoja tu, kupelekwa hospitali. Kwa maana sio tu hakuweza kusimama kwa miguu yake, bali pia hakuweza hata kuuinua ulimi wake mwenyewe na kuongea. Tatizo lilikuwa sasa, Daniel hakumjua yule mtu ni nani?
Hakujua kama yule mtu amekuja kwake kwa bahati mbaya au makusudi. Kama alifika pale kwa bahati mbaya hakukuwa na tatizo sana, lakini kama alifika pale kwa makusudi, basi kulikuwa na tatizo, na bila shaka ni tatizo lililoambatana na hatari kubwa sana.
Daniel alitoa simu yake mfukoni kwa mkono wa kushoto. Alibofyabofya kutafuta namba ya mtu, alipoipata, aliipiga.
“Hallo Dokta Tawakal?” Daniel aliita simuni.
“Hallo Daniel, habari za masiku?” Dokta Tawakal alijibu kwa kuchangamka na kuuliza swali.
“Salama Dokta Tawakal, nipo sehemu mbaya kidogo, ninaomba tukutane nyumbani kwangu baada ya nusu saa, nina dharura kubwa sana. Hakikisha hakuna anayejua kama unakuja kwangu” Daniel alisema harakaharaka.
“Kuna nini Daniel?” Dokta Tawakal aliuliza kwa sauti iliyoambatana na uwoga.
“Naomba tukutane nyumbani kwangu baada ya nusu saa, nitakueleza kila kitu, hapa nilipo sio sehemu sahihi kukueleza hayo maswali unayoniuliza” Daniel alisema tena kwa haraka.
“Ok sawa, tukutane nyumbani kwako baada ya hiyo nusu saa” Dokta Tawakal alikubali.
Simu ikakatwa.
“Sasa nitamtoaje nje huyu mtu?” Daniel alijiuliza mwenyewe. Ofisi ya Daniel Mwaseba ilikuwa maeneo ya Posta, katikati ya jiji la Dar es salaam. Katika jengo la Decade Tower, ghorofa ya kumi na nne, katika ofisi namba arobaini na tano. Haikuwa kazi ndogo hata kidogo kumtoa yule mtu akiwa katika hali ile, katika ghorofa namba kumi na nne hadi chini bila kuzua kasheshe!. Jengo la Decade Tower lilikuwa ulinzi mkali sana wa kutumia kamera za kisasa za CCTV, kamera zikizosaidiwa na walinzi wazoefu kutoka kampuni binafsi ya ulinzi, kwa idadi walikuwa zaidi ya hamsini, wao na kamera zao, kazi yao kuu ilikuwa ni kulinda usalama wa jengo la Decade tower.
“Yanipasa nimtoe huyu mtu bila mtu yeyote kujua” Daniel aliwaza huku akikuna kichwa kwa mkono wake wa kushoto. Alikuwa anawaza njia gani sahihi ya kumtoa yule mtu asiyemfahamu ndani ya ofisi yake na kwenda kumpatia matibabu. Baada kama dakika mbili za kuwaza mwenyewe, alipata jibu. Kwanza alianza kumpekua mifukoni yule mtu, hakuwa na kitu chochote kile katika mifuko yake. Alisogea hadi kabati lililokuwa limeegemezwa katika kona ya ofisi, akalifungua kwa kutumia funguo alioutoa mfukoni.
Akalitazama kabati kwa muda wa dakika tatu, akipiga mahesabu yake. Baada ya kuridhika, akarudi nyuma hadi katika meza yake, akafungua droo la upande wa kushoto, akatafutatafuta kwa sekunde kadhaa, lakini hakukiona kitu alichokuwa anakitafuta. Akarudi tena kwa yule mtu aliyekuwa bado amelala chini, akambeba huku akiruhusu damu nyingi zikichuruzikia sakafuni na kuchafua mandhari ya ofisi yake. Moja kwa moja akaelekea naye kwenye lile kabati lililokuwa wazi, akamkalisha hovyo ndani ya kabati, akalifunga kwa funguo kwa nje. Alielekea mlangoni na kutoka nje, akafunga mlango kwa kutumia kadi maalum.
Harakaharaka, alielekea katika chumba cha sita, ambacho kilikuwa ni stoo ndogo. Alichukua ndoo ya maji na skwiza. Alirejea navyo ofisini kwake. Alianza kusafisha ofisi yote, alihakikisha hayabaki mabaki ya damu hata kidogo. Akatoka tena nje akihakikisha amefunga mlango vizuri kwa kutumia ile kadi maalum, alienda kurudisha vile vifaa vya kudekia stoo, kisha alipanda lift na kumshusha hadi chini kabisa ya jengo. Moja kwa moja, alienda katika duka moja la zana za kilimo lilikuwa karibu na lile jengo la Decade Tower, akanunua mfuko mkubwa mweupe wa nailoni. Harakaharaka alirejea ofisini kwake kwa kutumia lift.
“Ili zile damu zake zisibubujike njiani lazima nimhifadhi kwenye huu mfuko” Daniel aliwaza wakati akiufungua mlango wa ofisi yake kwa ile kadi maalum. Akaingia ndani kuelekea katika kabati alilomweka yule mtu. Kwa kutumia mkono wa kushoto, alifungua mlango taratibu kwa kutumia funguo, wakati mkono wake wa kulia ukielekeza bastola kabatini.
Alichokutana nacho sasa….
Kwa mara ya kwanza tangu azaliwe Daniel Mwaseba hakuyaamini macho yake. Alibaki mdomo wazi, mkono wake wa kulia ulioshika bastola ulikuwa unatazamana na kabati tupu, amini usiamini, hakukuwa na mtu ndani ya lile kabati. Lilikuwa kabati tupu, tupu tupu tupu.
Haditi inaitwa Hatari, mwandishi wako anaitwa Halfani Sudy, tukutane tena kesho tuisome tena Hatari ndani ya riwaya hii ya aina yake.
Pia facebook tunapatikana kwa jina la Simulizi Za Gilbert. Tufollow
