RIWAYA: R i s a s i 4

RIWAYA: R i s a s i 4

Willy Gamba 1

JF-Expert Member
Joined
Jan 5, 2015
Posts
352
Reaction score
377

RISASI 4

na richard MWAMBE

Joseph Rutashobya anashuhudia mauaji
mabaya ya wazazi wake, hali hiyo inamwacha
yatima, anaishi maisha ya tabu mpaka
anakuwa mtu mzima.
Sasa Joseph Rutashobya 'JORU' analipiza
kisasi kwa wale waliofanya hayo. Kwa nini
Risasi 4?
fuatilia kisa hiki kinachokurudiaha nyuma.

SEHEMU YA 01
KAMBI YA JESHI MTUKULA-
August 1998
“Mguu pande! Mwiliiiiiiii legeza!”
ilikuwa ni sautinya amri kutoka kwa
kiongozi wa gwaride maalumu la
vijana wa JW lililokuwa likifanyika
katika kambi ya Mtukula, karibu
kabisa na mpaka wa Tanzania na Uganda.
Askari wote waliweka mguu pande na
kulegeza miili yao huku wakitazama mbele.
Jua kali lilikuwa likiwaka katika uwanja
huo, vumbi lilikuwa likitimuliwa na kaupepo
hafifu.
Wakiwa katika mistari minne yenye askari
kumi na mbili kila mmoja, James Rutashobya
alikuwa na mawazo lukuki, kijasho chepesi
kikitiririka kutoka katika katika kofia lake la
chuma na kuishia kidevuni.....
Upepo tulivu ulikuwa ukiendelea kuvuma,
kila mtu alikuwa ametulia katika uwanja
ule. Ndugu jamaa na marafiki walikuwa
wakitazama vijana wao wakakamavu wakiwa
uwanjani.
Joseph Rutashobya ‘Joru’ kama walivyokuwa
akiitwa na kuruta wenzake wa kombania moja
lakini service man wake alipenda kumwita
'Nyoka wa kijani' , alikuwa kijana mpole asiye na
maneno mengi lakini aliyejawa na vitendo zaidi,
alijiamini, aliamini uamuzi wowote uinaokuja
kichwani mwake, tangu aanze mafunzo ya
kijeshi katika kambi hiyo miezi sita iliyopita
wanaomjua wanadai alikuwa haongei maneno
zaidi ya hamsini kwa siku. Hakuna aliyekuwa
akijua kwa nini kijana huyu yuko hivyo, daima
alipenda kukaa peke yake kila apatapo nafasi
akyaruhusu mawazo yake kupita hapa na pale,
kujenga hili na lile. Daima alirudishwa mbali
kifikra na hali hii.
Akiwa mguu pande, aliinama kichwa chake na
kuangalia bunduki lake aliloliinamisha kwa
mbele, likimtazama kwa huruma, likitanguliwa
na singe linalong'aa kwa jua la saa nne asubuhi
huku kitako cha mti usiooza kikiwa kwenye
vumbi la ardhi hiyo kavu. Aliitazama kwa
uchungu na kukumbuka aina hiyo ya bunduki
ilipomuacha katika hali duni akiwa mtoto wa
miaka kumi tu, likambakisha yatima, bila
msaada wowote na kumsukuma katika maisha
magumu ambayo hakuyategemea wala
hakuwahi kuyafikiri, maisha ya shida na taabu,
maisha ya kutokuwa na baba wala mama.
Aliendelea kutazama singe lile ambalo nyuma
yake kulikuwa na tundu dogo lenye kutoa risasi
pindi tu liamurishwapo. Alilitazama tena na tena
bila kuchoka moyoni akliambia.
‘Ni wewe nakukumbuka sana kwa sura yako,
mdomo wako mdogo ulipiga kelele za kutisha
nikamshuhudia mama yangu akianguka chini
huku akilia kwa uchungu, ni wewe ambaye
baadae ulifanya vilevile na kumuacha baba
yangu akiwa hana uhai, sasa naelewa tukio
ulilofanya miaka ile, usihofu, hukuwa wewe ila
umefanana naye,’
Joru alijikuta ndani ya kumbukumbu nzito,
akiongea moyoni kwa uchungu huku akiitazama
ile 'rifle' bunduki aliyoishika mkononi mwake.
Alilolitarajia likatokea, uchungu ukatawala hisia
zake, hasira zikapanda kama moshi wa tanuru,
Joru akarudishwa kihisia katika kumbukumbu
mbaya iliyomrudisha miaka 21 nyuma, chozi
likatoka katika jicho lake na kuning'inia chini ya
kidevu chake, likajiachia na kudondoka ardhini,
kishindo kikubwa kilisikika moyoni mwa Joru,
vumbi lisilo la kawaida lilitimka na kumfanya
mapigo yake ya Moyo kuongeza kasi, damu
kwenda mbio, pumzi kutoka kwa nguvu.
‘Kesho na keshokutwa utakua kijana mwanangu,
hakikisha unalipa kisasi kwa damu hii
inayomwagika, damu ya familia yako, damu ya
wazazi wako,’
Sauti ya baba yake ilijirudia kwa mwangwi wa
ajabu kichwani mwake ikitanguliwa na kile
kishindo cha lile chozi kufika ardhini, yote hayo
hakuna aliyeyahisi wala kuyasikia isipokuwa
Joru peke yake.
“Gwarideeeeee!!!!” ilikuwa amri nyingine
iliyomgutusha kutoka katika ulimwengu wa
mbali, aliinua kichwa akatazama mbele.
“Silaha beganiiiiii weka!” amri iliendelea kutoka
kwa kiongozi wa gwaride. Kishindo kimoja
kikasikika, bunduki zile zikishikwa kwa
ukakamavu wa mikono ya wale wana wa jeshi,
wanaomaliza mafunzo, zikapandishwa begani na
miguu kuwekwa sawa kisha ukimya ukatawala.
Muziki maalumu wa tarumbeta ulisikika ukitoka
katika kikundi cha bendi ya jeshi kilichokuwa
kikisindikiza vijana hao, muziki huo uliashiria
kuwa mgeni wa siku hiyo alikuwa akiwasili.
Baada ya dakika chache mgeni yule alipanda
katika kibanda maalumu, alikuwa ni amiri jeshi
mkuu, mkuu wa nchi, juu ya kibanda kile
maalum alisimama akiwatazama wale vijana
waliokuwa ndani ya mavazi adhimu ya kijeshi
yaliokuwa na mabaka, yaliyowapamba
wakapambika, walikuwa ni vijana kutoka kambi
zote za mafunzo za kanda ya ziwa
wakihitimisha mafunzo yao kwa pamoja, hakika
ilikuwa sherehe kubwa. Wakati wengine
wakifikiria kukutana na ndugu na jamaa zao
baada ya gwaride hili, wakiwapongeza kwa
kuhitimisha mafunzo hayo magumu, haikuwa
hivyo kwa Joseph Rutashobya, hakuwa na mtu
wa kuja kumlaki wala kumwambia hongera
katika shughuli hiyo, hali hii ilimpa uchungu
sana lakini hakuweza kupingana na ukweli halisi
uliopo, hana ndugu, hata wale waliopo hawajui
kama siku hiyo anamaliza mafunzo yake ya
jeshi kwa maana ni miaka mingi imepita hata
hawakujua kijana huyo yuko wapi, walilia
wakanyamaza, wakajua kama hajafa basi
amepotea kimazingara.
Kiongozi wa gwaride akatoa amri nyingine, sasa
ilikuwa ya kutoa heshima kwa Amiri jeshi mkuu;
kama kawaida, zile bunduki zikatolewa
mabegani na kushikwa mikononi kwa umahiri
mkubwa.
Wimbo wa Taifa kombozi la Tanzania ulirindima,
wapigaji walipiga kwa umahiri mkubwa, wimbo
wa Taifa la Tanzania ambao kutokana na
maneno yenye ujumbe mzito na melodi ya
kupendeza mataifa kama Zambia na Afrika ya
kusini yaliufanya kuwa wimbo wao wa Taifa
vilevile, na ingependeza kama Africa nzima
ingekuwa na wimbo huu mmoja kwa kila Taifa
wenye maneno matamu ‘Mungu ibariki Afrika,
wabariki viongozi wake na watoto wake pia’.
Joru alitulia kwa ukakamavu hisia zake
zikatekwa tena na wimbo huo ambao alijifunza
alipokuwa shule ya vidudu na ile ya msingi
madarasa mawili tu aliyoyasoma, chozi lingine
likadondoka ardhini na kufanya kishindo kilekile
moyoni mwake, mara sauti ya kilio kikali ikapita
mawazoni mwake...
'Aaaaaaaaaagggggghhhhh, kimbia Jose kimbia,
usitazame nyuma,'
Aliikumbuka sauti hii ya mama yake kipenzi
ikimjia katika hisia kali na nzito, Joru alijikuta
akilia kwa kumbukumbu hizo. Alimtazama mgeni
rasmi, mkuu wa nchi aliyetulia juu ya kibanda
kile akiwa ndani ya suti safi ya kimaghalibi,
hakuwa mbali kutoka katika kibanda kile.
Joru alikuwa katika gadi ya pili ambayo kwa
mpangilio wao ilikuwa mbele kushoto ilikuwa
gadi ya kwanza na kulia ilikuwa gadi ya tatu,
katika gwaride hilo kulikuwa na gadi kumi na
tano.
Joru alimtazama kwa makini mgeni rasmi
moyoni akmwambia,
‘…Hujaubeba Uafrika, kama ungeubeba basi
ungevaa vazi nadhifu la kitenge ama cha
Sunguratex, Kilitex, au Mwatex.’
Wimbo wa Taifa bado ulikuwa ukiendelea,
‘Heshima umoja na amani, hizi ni ngao zetu,
Africa na watu wake,’ maneno haya yalimpa
uchungu Joru, akaitazama Africa kwa mapana
yake,
‘Afrika bara zuri, bara aliloishi mwanadamu wa
kale, lilokuwa na umoja mkubwa,
Afrika, kwa nini tunapigana Afrka?
Kwa nini tunakosa upendo Afrika?
Kwanini tumepoteza thamani ya maisha hadimu
ya kiafrika yenye tunu zisizo kifani? Umoja,
mshikamano, upendo na ujamaa, unapotea kati
ya Waafrika? Chuki, ubabe, ubinafsi vimeiteka
Afrika, vimeingia mioyoni mwa Waafrika na
viongozi wake. Watu wa kale waliita bara hili
bara la giza lakini sasa tunastahili kuliita bara
jekundu kutokana na damu inayomwagika siku
hadi siku.’
Wimbo ule mtukufu ulipotelea katika mawingu,
mawingu ya anga la Mtukula, mawingu safi
meupe yaliyopendezesha anga hilo, ndege aina
ya mbayuwayu waliokuwa wakiruka hapa na
pale walifanya nyimbo nyingine tamu mara tu
baada ya kuisha ule wimbo hadhimu. Joru
alikuwa bado katika hali ya ukakamavu mpaka
amri nyingine ilipotolewa.
Mgeni rasmi alishuka kutoka katika kibanda
chake na kuongozwa na askari maalum
alieandaliwa kwa shughuli hiyo ya ukaguzi wa
gwaride. Pamoja nae mkuu wa majeshi mkoa wa
Kagera aliomsindikiza, brigedia Shibagenda.
Walipita mbele ya mistari ya vikosi hivyo kwa
mwendo wa madaa wakiongozwa na wimbo
maarufu wa enzi zile,
‘Tanzania Tanzania, nakupenda kwa moyo wote,
Tanzania Tanzania jina lako ni tamu sana...’
Joru alitulia bila hata ya kutikisika, akisikiliza
muziki ule wa uliokuwa ukipigwa na bendi ileile
huku hisia zake zikiimba pamoja na melodi
hiyo.
'Nilalapo na kuota wewe, niamkapo ni heri
mama we...'
Ni siku hii Joru alipogundua umaana na uzito
wa wimbo huo, picha za mauaji ya wazazi wake
zilimrudia na kumsumbua kichwa. Machozi
yalimtoka kijana huyu mkakamavu mwenye
tambo la mtu anayenyanyua vyuma au kufanya
mazoezi ya vitu vizito.
Mgeni rasmi alipomfikia alisimama na
kumtazama Joru ambaye alisimama
kiukakamavu; ukiacha machozi yaliyokuwa
yakitoka machoni pake na kumwagika kwa fujo
huku kelele nyingi za vilio zikimrudia, akiwaona
askari wa Uganda chini ya kiongozi wao Mali ya
Mungu wakitesa na kuua wanakijiji ndani ya
mpaka wa Tanzania na Uganda, kipande cha
ardhi ambacho Uganda ilidai kuwa ni chao,
ubabe na utemi vilitawala.


ITAENDELEA
 
RISASI 4
Ilipoishia...
Mgeni rasmi alipomfikia alisimama na
kumtazama Joru ambaye alisimama
kiukakamavu; ukiacha machozi yaliyokuwa
yakitoka machoni pake na kumwagika kwa fujo
huku kelele nyingi za vilio zikimrudia, akiwaona
askari wa Uganda chini ya kiongozi wao Mali
ya Mungu wakitesa na kuua wanakijiji ndani ya
mpaka wa Tanzania na Uganda, kipande cha
ardhi ambacho Uganda ilidai kuwa ni chao,
ubabe na utemi vilitawala.

CHAPISHO LA 02
MASAKA – UGANDA, 1976 February 20, saa 5 as.
LAND ROVER 109 ziliingia katika uwanja wa
shule ya sekondari Masaka kwa fujo za aina
yake, vumbi jekundu ‘ngunja’ lilitimka huku na
kule, kelele za wana Uganda waliojazana katika
uwanja huo zilisikika zikishangilia tukio hilo huku
akina mama wakipepeza matawi ya miti
kunogesha tukio. Vikundi vya ngoma vilianza
kurindimisha midundo ya Kiganda na vijana wa
kike na kiume wakionesha umahiri wao katika
kusakata mirindimo hiyo. Yote hayo yakiendelea,
zile gari zikasimama na wanajeshi wenye
bunduki wakateremka kuweka ulinzi eneo hilo
wakishirikiana na wale waliowakuta pale.
Ndani ya benzi moja nyeusi ya kijerumani
iliyokuwa ikipepea bendera ya Uganda
aliteremka binadamu mwenye tambo kubwa,
mweusi ti; aliyependezeshwa kwa mavazi ya
jeshi la Uganda yaliyochafuka tepe na vyeo
anuai, hakuwa mwingine, bali ni yule ambaye
wewe ulimdhani kuwa ni katili, asiyecheka na
mtu, la, huyu alikuwa mcheshi aliyesalimiana na
watu wa kila rika, aligusika na kila mmoja, japo
alikuwa akitawala nchi kwa mabavu baada ya
kumtoa Rais aliye madarakani mwaka '62,
Milton Obote. Huyu alijulikana kwa majina mengi
ya kibabe ndani na nje ya Uganda, huwezi
kuamini, aliwapenda watu wake na kila
alilofanya alilifanya kwa manufaa ya watu wake
ijapokuwa katika macho ya wengine ilikuwa ni
ukatili, uonevu, udikteta na mengineyo, alikuwa
Idd Amin Dada, aka The butcher of Africa, aka
The Conqueror of England Empire , aka The Lord
of all beasts, alikuwa na majina mengi na huku
kwetu tulimwita 'Nduli'...
“Uganda oyeeeeeeee” alianza namna hiyo pale
tu alipopanda katika jukwaa lililoandaliwa.
“Oyeeeeeeeeeee” aliitiliwa kwa nderemo na vifijo.
“Habari...!” aliwasalimu watu wake kwa lugha
ya kiswahili, akaendelea; “Leo nipo hapa Masaka
nimekuja kuwasalimu ninyi watu wangu, najua
kila mtu anapenda Uganda sio? ‘Ndiyooooooo’,
Basi na kama ni hivyo lazima tuilinde nchi yetu,
tuipende na kuipigania, serikali yenu inawapenda
japokuwa mataifa mengine hayatupendi lakini ni
kwa sababu ya wivu, wanatuonea wivu kwa
maendeleo yetu, msihofu hakuna wa kutupiga
bali tutawapiga, na katika hili nitataka wote
muungane nami atakayebisha, atakayesaliti
juhudi mnajua nitakachomfanya.
Sasa tuna mpango wa kwenda kukomboa
kipande chetu cha ardhi huko Tanzania, kwa
maana ni mali yetu pale Mtukula, ni mali yetu
mto wa Kagera, tuogope nn? Tuogope nn?
Uganda oyeeeeeeeee!!!!!!"
Ilikuwa hotuba fupi ambayo ilishangiliwa kwa
hamasa kubwa, ngoma zikaanza kurindima tena,
sasa ilipigwa ngoma ya kwao, alikozaliwa, Idd
Amin, akashuka na kuungana na wanachi
kucheza ngoma hiyo kwa ustadi mkubwa sana,
watu walimsahangilia huku wakimrushia maua
kuonesha wamemkubali kiongozi wao.
Sura ya kutisha kiumbe huyu haikusahaulika
kwa wengi waliodhurumiwa roho za ndugu au
marafiki zao, walimtazama na walitamani wamle
nyama lakini haikuwezekana, ilikuwa
ukizungumza vibaya juu yake unaamka hauna
kichwa au umepambwa kwa matundu ya risasi,
hali ilikuwa mbaya, mtu huyu aliogopwa na kila
mtu lakini amini usimini alikuwa na marafiki
wakubwa waliompenda na kumpa misaada mingi
kwa ajili ya watu wake. Baada ya shughuli hiyo
hapa Masaka akaendelea na kazi zingine za
kujenga taifa lake.
§§§§§

Mgeni rasmi wa gwaride lile alifika pale
aliposimama Joru, aliyashuhudia machozi
yaliyokuwa yakimtiririka usoni, alionekana wazi
ana uchungu na kitu, akasimama mbele ya
kuruta huyu, akamtazama tena na tena, mkuu
wa majeshi aliyekuwa pamoja na mgeni rasmi
ndiyo kwanza alimtambua kijana huyo Joseph
Rutashobya 'Joru', mkuu wa majeshi alibaki
katumbua macho hakutegemea kabisa kama
angemuona kijana huyo, akakumbuka miaka
mitatu nyuma, jinsi alivyokutana na kijana
mtukutu, mpole, Joru, katika mazingira ya
kutatanisha.

MIAKA MITATU ILIOPITA
MISITU YA BIHARAMURO

TAARIFA ya duru za usalama ilisema kuwa idadi
ya vitendo vya ujambazi imekuwa kubwa, kila
uchwao, mabasi yanatekwa, watu wanaporwa,
wengine kuuawa na kubakwa, polisi walifanya
kazi kubwa ya kupambana na majambazi hayo
lakini walijikuta wakizidiwa kwani majambazi
yalikuwa na silaha kubwa za kivita walizozipata
kutoka nchi jirani, wakifanya ujambazi na baadhi
ya wanajeshi wa nchi hizo sio tu kuteka mabasi
bali hata kuvamia maduka na kupora.
Siku moja kulifanyika uhalifu mkubwa, mabasi
sita na malori ya mizigo yaliyokuwa yakienda
Kagera na Ngala yalitekwa na majambazi hao
walipora mali nyingi za thamani, wakawavua
nguo abiria na kuwaacha uchi kisha kuwaamuru
waimbe wimbo
‘Mtaji wa masikini ni nguvu zake’
Ilikuwa ni aibu ma fedheha kwa watu hao.
Joru akiwa kajificha msituni, juu ya mti,
aliyashuhudia hayo yote yaliyokuwa yakitukia
kwa kupitia darubini aliyokuwa nayo, aliumia
sana lakini hakuwa na msaada. Alitazama kwa
uchungu na alijua wazi kuwa akileta tabu lazima
watamuua, alijibana palepale na kuendelea
kutazama.
Wale majambazi wakamaliza kazi yao
wakakusanya kila kitu, wakikung'uta nguo
walizowavua wale abiria na kuchukua kila kilicho
katika mifuko kisha wakatokomea msituni.
Joru alitulia kulekule juu ya mti akihofia kushuka
akijua kwa vyovyote watafikiri kuwa yeye ni
mmoja wao. Baada kama ya nusu saa tangu
wale majambazi waondoke, polisi walifika na
landrover zao aina ya 110, kwa ajili ya
kuwalinda raia hao. Waliwahoji juu ya tukio zima
jinsi lilivyokuwa, wakasimulia. Baada ya kila kitu
kuwa sawa, yale mabasi na malori yaliondolewa
eneo lile.
§§§§§

Usiku wa siku ile ya tukio, polisi wakishirikiana
na JW, waliuvamia msitu na kufanya msako wa
haja, walipekua kila kichaka na vichaka kusaka
mali na majambazi hao.
Wimbi la utekaji mabasi lilikuwa kubwa katika
mkoa wa Kagera, askari wa jeshi wa nchi jirani
walikuwa wakishirikiana na majambazi katika
uporaji huo. Wasafiri na wananchi waliilalamikia
serikali kwa hali hiyo. Wahusika walisikiliza kilio
hicho, wakakaa kikao na kuamua kulivalia njuga
swala la ujambazi katika mkoa huo.
Joru alikuwa ndani ya kichaka usiku huo akiwa
kajipumzisha, mara akasikia kelele za mbwa na
watu wanaoongea, hakufanikiwa kuchomoka
kwani mbwa wa polisi walifika katika kichaka
hicho, alipojaribu kujiokoa alichelewa, kwa amri
moja walimvamia na amri nyingine walimwacha
akiwa hoi, wale polisi na wanajeshi wakamtia
pingu kijana huyo kisha msako ukaendelea.
Usiku huo walifanikiwa kuwakamata watu 12
akiwemo Joru, wakawakusanya na kuwatembeza
kwa miguu kuelekea barabarani walikoacha
magari. Kati ya hao 12 kuna walioleta ujeuri
njiani, walipigwa risasi na kuuawa kisha
kutelekezwa msituni, ilikuwa ni hali ya kuogofya
sana kwa Joru, hakutamani kuangalia nyuma.
Mwendo kama wa nusu saa hivi wakafika
barabarani na kuwakuta askari wengine,
wakawapokea kwa kichapo cha haja kisha
wakawaamuru wote kuchuchumaa chini.
Kiongozi wa operesheni hiyo akasogea na
kumtazama mmoja mmoja kwa sura akimmulika
kwa kurunzi yenye mwanga mkali, akafika kwa
Joru, akasimama na kumwangalia sana kijana
huyu kwa makini.
“Yaani hata wewe ni jambazi?” akamuuliza Joru.
“Hapana afande,” Joru akajibu.
“Sasa unafanya nini huku?” yule kiongozi wa
msako alimuuliza Joru,
“Ni stori ndefu sana mzee,” yule kiongozi wa
operesheni ambaye alikuwa ni mtu wa makamo
alimtazama tena Joru.
“Unaitwa nani?” akamuuliza
“Joseph Rutashobya,” akajibu.
“Haya nambie kwa nini umekuja huku msituni?
Ukinambia ukweli nakuachia ukinidanganya
nakufunga jela,” yule askari alimkaripia. Joru
alitulia kimya kisha akaanza kulia.
“Unalia nini?” Yule askari akauliza kwa
ukali.
“Afande ni stori ndefu nay a kusikitisha
sana, huwa siipendi kuikumbuka kwa maana
inanitia uchungu” Joru alisema huku bado akilia
kwa vikwifukwifu. Yule askari akamtazama Joru
kwa jicho la huruma sana, moyo wake ukaingia
ganzi akashindwa kuvumilia, chozi likamdondoka
hata kabla Joru hajaweza kuongea chochote
katika hilo.
Baada ya kujifikiria mara kadhaa, Joru aliinua
kichwa na kumtazama Yule askari jeshi,
Shibagenda, kisha Joru akajaribu kukumb uka
lile tukio la kutisha katika maisha yake
akamueleza kisa na mksa way eye kuwa msituni
siku hiyo.

1977
Kijiji Fulani huko Mtukula

“Hatuwezi kukubali kunyang’anywa ardhi hivi
hivi, ye nani? Kama ninyi mnamuogopa basi
mimi simuogopi,” ilikuwa sauti ya mzee
Rutashobya katika mkutano wa kijiji uliotishwa
siku moja na mwenyekiti wa kijiji hicho.
Suala la Idd Amin kuvamia Tanzania na kudai
maeneo Fulani ni ya Uganda huko pande za
Kagera lilichukua kasi, ilikuwa haipiti wiki
wanakijiji hawa walisikia sehemu Fulani Amin
amevamia na kuteka kijiji Fulani, ilikuwa hali ya
kuogofya sana iliyokuwa ikifanywa na hao
vibaraka wake ambao wakati mwingine
walivamia sit u kwa madai hayo bali kupora mali
za wanakijiji na hata kufanya unyanyasaji wa
kijinsia kama kubaka na kuwapa wananchi
mateso makali mwishoe kuwaua. Mzee
Rutashobya, hakuipenda sana hali hiyo, alikuwa
akiumia sana kila aliposikia taarifa hizo hasa
kupitia redio idhaa ya taifa. Alitamani siku moja
apambane na watu hao awaoneshe kama kweli
yeye alikuwa ni mmoja wa askari wa KR, jeshi la
mkoloni, aliyepigana vita ya pili ya dunia kwa
upande wa Ujerumani.
“Mzee Rutashobya unasema tu wewe, wakija
hapa sijui hata kama utaweza kukimbia,” mzee
mwingine alimpinga Rutashobya.
“Sikia wewe mimi si muoga kama kuku, niko
tayari kufa, kama kufa nimeshaona wengi
waliokufa siwezi kuogopa kufa, nitajisikia furaha
kufa kwa ajili ya nchi yangu na si kwa lingine,”
alibisha. Mkutano ulikuwa mrefu sana katika
kijiji hicho, hoja ikiwa ni jinsi gani ya kukilinda
kijiji chao dhidi ya askari wa nduli Amin ambao
waliteka na kunyang’anya ardhi ya wananchi
kila kukicha.
Si kwamba viongozi wa chama na serikali kwa
ujumla walikuwa hawalijui hilo lakini bado roho
ya subira ilikuwa ikitawala roho za viongozi hao
waliokuwa wakisikiliza kila agizo kutoka kwa
Mwl J.K Nyerere, ambaye ndiye alikuwa Rais na
Amiri jeshi mkuu mwaka huo. Baada ya mkutano
huo kwisha na kila mtu kurudi katika kaya yake
iliadhimiwa kuanzisha ulinzi wa kulinda kijiji
chao.
Usiku wa siku hiyo, mzee Rutashobya na familia
yake ya mtoto mmoja, Joseph, walikuwa
wameketi nje, mkekani, wakiangaziwa na taa ya
kandili iliyokuwa kati yao. Mkewe alikuwa
akiendelea kuchambua buni alizokuwa
amezivuna kutoka shambani wakati Mzee
Rutashobya aliketi kwenye kiti chake cha uzee,
macho yake yakiangaza huku na huko katika
migomba iliyozunguka eneo hilo lote, pembeni
yake alikuwa amelaza bunduki kubwa aina ya
gobole na risasi kadhaa zikiwa kwenye mfuko
wa suruali yake aliyokuwa amevaa, mdomoni
mwake alikuwa akivuta kiko huku akimsimulia
hadithi mbalimbali za kale na kumfundisha stadi
za maisha mwanae pekee Joseph.
“Na wewe siku moja utakuwa mkubwa,”
alimwambia mwanawe.
“Na mi nikiwa mkubwa nitakuwa kama wewe?”
Joseph aliuliza.
“Ndiyo, tena itabidi uwe mkakamavu sana, uwe
mwanaume asiyeogpa kitu kama mimi baba
yako, sikiliza mwanangu, mimi baba yako tangu
nikiwa mdogo wakati wa ukoloni, nilikuwa
najifunza kila kitu kutoka kwa baba yangu,
kuwinda, kulima na kila kitu.” Akavuta kiko
chake na kupuliza moshi kwenda angani kisha
akaendelea kumueleza mwanae, “Na wewe
ujifunze kutoka kwangu, usikubali mtu akuonee
hata siku moja, uwe Mtanzania imara, mwana
TANU thabiti, hakikisha unaitetea nchi yako
katika lolote lile ikiwa hata kufa, kufa, huo ndio
uzalendo mwanangu,” Mzee Ruta alikuwa
akimwambia mwanane ambaye alikuwa
ameduwaa kwa maneno hayo makali.
“Baba, mi mbona naogopa kufa?” aliuliza.
“Kwa sasa utaogopa kwa sababu hujui, lakini ipo
siku hautaogopa kufa, mazingira yatakufanya
usiogope kufa hata kidogo, lazima uwe
mwanaume kweli kweli, hata mi nikikuachia mji
huu basi uweze kuutunza na kuulinda maana
ndio utakuwa wajibu wako, wewe huna dada
huna kaka, upo peke yako kwa hiyo uwe
mkakamavu katika kila kitu, usijione mdogo”
Mzee Ruta aliongea huku akimpigapiga
mgongoni mwanawe huyo, hata baadaye
aligundua kuwa tayari amekwishalala muda
mrefu, na maneno yale yalikuwa yakiingia katika
ubongo wake kama ndoto ya kutisha sana yenye
matukio ya ajabu ambayo Joseph hakuwahi
kuyaona maishani mwake.

ITAENDELEA
 
ili niisome kwa ukamilifu, ngoja niachane nayo ila ntakuwa nachungulia. siku nikiona SEHEMU YA MWISHO hapo ndo nitaanza kusoma.

sina imani na hawa majembe yetu. mpaka sasa wameninyima raha sana kwenye UCHU
 
ili niisome kwa ukamilifu, ngoja niachane nayo ila ntakuwa nachungulia. siku nikiona SEHEMU YA MWISHO hapo ndo nitaanza kusoma.
sina imani na hawa majembe yetu. mpaka sasa wameninyima raha sana kwenye UCHU
Naunga mkono hoja!
 
ili niisome kwa ukamilifu, ngoja niachane nayo ila ntakuwa nachungulia. siku nikiona SEHEMU YA MWISHO hapo ndo nitaanza kusoma.

sina imani na hawa majembe yetu. mpaka sasa wameninyima raha sana kwenye UCHU

Usiwe na wasiwasi hii itakuja mwanzo mwisho bila chenga
 
RISASI 4
ILIPOISHIA...
“Kwa sasa utaogopa kwa sababu hujui, lakini
ipo siku hautaogopa kufa, mazingira
yatakufanya usiogope kufa hata kidogo, lazima
uwe mwanaume kweli kweli, hata mi
nikikuachia mji huu basi uweze kuutunza na
kuulinda maana ndio utakuwa wajibu wako,
wewe huna dada huna kaka, upo peke yako kwa
hiyo uwe mkakamavu katika kila kitu, usijione
mdogo” Mzee Ruta aliongea huku akimpigapiga
mgongoni mwanawe huyo, hata baadaye
aligundua kuwa tayari amekwishalala muda
mrefu, na maneno yale yalikuwa yakiingia
katika ubongo wake kama ndoto ya kutisha
sana yenye matukio ya ajabu ambayo Joseph
hakuwahi kuyaona maishani mwake .

[COLOR=6]SEHEMU YA 03[/COLOR]
§§§§§
Joseph Rutashobya, mtoto pekee wa mzee
Rutashobya alikuwa na umri wa miaka tisa
wakati alipokuwa akiambiwa hayo yote na baba
yake ambaye tayari umri ulikuwa umekwenda,
lakini pamoja na umri wake mkubwa alikuwa ni
mkorofi na hakuna mwanakijiji aliyekuwa hamjui
mzee huyo. Joseph hata shuleni ilikuwa ni
vigumu kupewa adhabu kutokana na ukorofi wa
baba yake, ijapokuwa yeye alikuwa ni mpole
sana asiyependa kuongea na watu, wengi
walisema ni tabia ya mama yake, shuleni
hakuwa akichangamana na marafiki, daima
alikuwa akiambatana na mtoto wa shangazi
yake tu, Kemilembe. Daima utawakuta pamoja
hata kama si muda wa masomo, ilikuwa ni
vigumu wawili hawa kuwatenganisha kiasi
kwamba walionekana kama mapacha
wanapoambatana. Si Joseph wala Kemilembe
aliyewahi kufikiri kuwa siku moja watakuja
kutengana au kutenganishwa, daima katika
maongezi yao ya kitoto waliweka ahadi za kuwa
wakiwa wakubwa wataishi kama wazazi wao
wanavyoishi, kuishi nyumba moja, kulala
pamoja, wao kwao ilikuwa ni kama sehemu ya
maisha ya ukubwa ambayo walijua wazi kuwa
siku moja watayafikia.
Hata wakati Kemilembe alipoanza kuota matiti,
alimwambia Joseph kuwa kifua chake kinavimba
huku na huku, Joseph alitazama uvimbe huo na
kubonyezabonyeza lakini alikutana na vitu
vigumu, kwa kuwa Kemilembe aliamini kuwa
Joseph anajua mengi kwa kuwa ni mwanaume,
alifurahi sana alipoambiwa na Joseph kuwa
“Sasa utakuwa kama mama, utakuwa na
maziwa makubwa, tukiwa na motto
atanyonyamo.”
Joseph mara nyingi alikuwa akimsikia baba yake
anavyosikitika hasa asikilizapo redio yake ndogo
ya mbao aina ya Phillips iliyokuwa ikimpa habari
kila saa nne, saba na kumi ya kila siku.
Mzee Rutashobya alichukizwa wazi na yale
anayaoyasikia kutoka kwenye chombo hicho
kidogo ambacho Joseph aliaamini kabisa kuwa
kuna watu ndani wanaoongea.
“Baba kila ukisikiliza humu unakasirika, kwa
nini?” Joseph alimuuliza baba yake.
“Mwanangu, dunia hii sijui tunakwenda wapi,
kila siku watu wankufa lakini wenye nguvu
wanafumba macho,” akamjibu kana kwamba
anamjibu mtu mzima mwenye uelewa mpana.
Joseph akamkazia macho baba yake
akimaanisha hajamuelewa alichomwambia.
“Umeshawahi kumsikia Idd Amin?” Rutashobya
akamuuliza mwanawe.
“Ndio, mwalimu ametuambia kuwa ni mtu
mbaya sana, anaua watu,” Joseph akajibu huku
akionesha huzuni ya wazi usoni mwake. “Sasa
kwa nini polisi wasimkamate?” akauliza.
“Aaah Jose, polisi wote wako chini yake,
wanamsikiliza yeye,” Rutashobya akajibu.
“Mi ningekuwa polisi ningempiga bastola,” Jose
akajibu akiwa hajui anachokiongea.
Siku iliyofuata….
“…Idd Amin akifa, mimi siwezi kulia, nitamtupa
Kagera awe chakula cha Mamba…” zilikuwa
sauti za watu wakiimba kutoka mbali sana.
Joseph akiwa na Kemilembe walikuwa njiani
kuelekea shuleni alfajiri ya siku hiyo, mikononi
mwao walikuwa na fagio pamoja na vidumu vya
kuchotea maji kwa ajili ya kumwagili bustani
zao za mbogamboga.
“Kemi, unasikia hao wanaoimba?” Jose
alimuuliza Kemilembe.
“Ndiyo, kwani ni akina nani?” Kemilembe aliuliza.
Joseph akatulia kwanza bila kujibu akisikiliza
zile sauti za ule wimbo ulioonekana kumpa
faraja kubwa masikioni mwake.
“Unataka kuwajua?” Joseph aliuliza.
“Ndiyo,” Kemi akajibu. Joseph akamshika mkono
Kemilembe na kumvutia kwenye majani,
wakajificha huku zile sauti zikikaribia pale
walipo. Punde si punde kundi kubwa la watu
waliogawanyika katika makundi makubwa
manne walipita wakikimbia mchaka mchaka.
Walikuwa wanajeshi wengi wenye silaha
mikononi, wakiwa wamevaa magwanda yao
yenye mabaka mabaka yaliyowafanya
waonekane kama wadudu, kofia za chuma
zilikuwa zimezungushiwa majani mengi na
kufanya kama wamebeba vichaka, walikuwa
wakiimba kwa jazba na wakipiga mbinja nyingi.
Walipokwisha pita, Joseph na Kemilembe
wakajitokeza kutoka kwenye lile chaka
walilojificha.
“Wanaenda wapi?” Kemilembe akauliza.
“Watakuwa wanakwenda kumkamata Idd Amin,”
Joseph alijibu kwa kujiamini kisha wakavuka
barabara na kuelekea shuleni.
Watu wa eneo hilo ilikuwa ni kawaida kwao
kuona wanajeshi wakipita na kuimba au wakiwa
wamejificha machakani wakiwa katika mazoezi
ya kivita kutokana na hali halisi iliyopo.
Walikuwa katika hali ya utayari muda wote hasa
wale wa mpakani, Mtukula.
Mashuleni nako kulikuwa na ulinzi mkali,
tahadhari kabla ya hatari.
Mchana wa siku hiyo, masomo yalipokwisha,
Joseph na Kemilembe waliwahi kurudi nyumbani
tofauti na siku nyingine. Siku hiyo Joseph alifika
nyumbani na kumkuta mama yake akiwa ndio
kwanza ametoka shambani lakini hakumkuta
baba yake. Alimuuliza mama yake kuwa baba
yake amekwenda wapi akajibiwa tu amekwenda
kijiji jirani hatochelewa kurudi. Joseph alipitiwa
na usingizi baada ya shibe ya mchana, akajilaza
kwenye kijitanda kidogo kilicokuwapo sebuleni.
Alishtuliwa na sauti ya baba yake aliyekuwa
akimsimulia mama yake habari mbaya na ya
kutisha kuwa wameokota maiti za watu katika
mto Kagera. Mzee Rutashobya alikuwa akiongea
kwa huzuni sana na uchungu juu ya hali hiyo.
Joseph aliyekuwa amelala kisungura alikuwa
akisikiliza yote. Baadae alipoamka hakusita
kumueleza baba yake kuwa amekutana na
wanajeshi wakienda kumkamata Idd Amin ili
wmtupe Kagera aliwe na Mamba. Joseph
akamuuliza baba yake kama katika hizo maiti
ilikuwepo ya Idd Amin. Baba yake akamtazama
kwa mshangao lakini akajua kuwa ni akili za
kitoto tu.
Usiku wa siku hiyo wazee wa kijiji kile
walikutana pamoja kujadiliana juu ya hali halisi
ilivyo kwa usalama wao kwa mara nyingine,
ikiwa pia kuweka zamu ya kulinda. Siku hiyo
mzee Rutashobya na wengine tisa walikuwa
zamu ya kuweka ulinzi. Mzee Rutashobya
kutokana na uzoefu wake wa medani za kivita
alipokuwa huko ughaibuni katika vita ya pili ya
dunia.
“Mnajua tukiwa wazi watatuona kirahisi, hapa ni
kujificha kwenye migomba na wengine kwenye
mibuni,” alitoa maelekezo kwa wengine,
yakaeleweka. Kila mtu akajificha kama
alivyoambiwa, hakuna aliyekuwa hamuamini
mzee huyo kwa mipango bahati mbaya tu
hakuwa kiongozi katika kijiji hicho.
Usiku wa manane…
Kutoka pale alipojificha mzee Rutashobya,
alisikia mlio wa gari lililokuwa likielekea kule
kijijini kwao, likishuka mlima wa karibu.
Alijitokeza kwa hadhari kubwa na gobole lake
mkononi akiwa keshaliweka tayari kwa
mashambulizi endapo anayekuja ni adui.
Akawapa alama wenzake ishara ya mruzi kama
mlio wa ndege akiwaweka tayari kwa lolote.
Yalikuwa malori mawili makubwa, moja lilikuwa
na askari na linguine lilikuwa tupu, wakatelemka
kuanza kuvamia mazizi ya mifugo, wakaanza
kuswaga ng’ombe na mbuzi kupakia katika lori
lililo tupu, huku wengine wakianza kuvunja
milango ya nyumba. Askari mmoja aliyekuwa
akivunja mlango kwa teke alichomwa mshale wa
mgongo na kupiga yowe la nguvu, hapo
waligundua kuwa kuna watu nje wenye silaha,
wale wavamizi wakavamia machaka ya
migomba kuanza kusaka huku wakipiga risasi
kila wanayemkamata. Mzee Rutashobya
alimlenga mmoja aliyeonekana kimbelembele
kwa kutoa amri hizo, akamlega na gobole lake
akafyatua shabaha safi, ikapasua kichwa cha
Yule mtu, kisha akahama kile kichaka na kwenda
kichaka kingine ikiwa ni moja ya kuwapoteza
wale wavamizi. Mara risasi kama mvua zikakata
na kutengeneza uwanja katika lile eneo ambalo
risasi ya Rutashobya ilitokea.
“Atakuwa ameshakufa huyo!” mmoja wa askari
akasema, lakini kabla hajatoka eneo lile, gobole
la Rutashobya lilifanya kazi nyingine
likamtungua Yule aliyekuwa akisema hayo,
akajibwaga akiwa kifua chote hakitamaniki. Hali
ikawa mbaya, kiongozi wa wavamizi
aliyejulikana kama Mali ya Mungu ambaye muda
wote huo alikuwa ndani ya lori akivuta bangi
alimua kuteremka na kumsaka huyo anayejifanya
mdunguaji. Mpaka yeye aliposhuka tayari vijana
wake wanne walikuwa chini bila uhai, wakiwa
wamelazwana gobole la Rutashobya. Mali ya
Mungu akajua wazi kuwa wanapambana na mtu
anayejua anachokifanya.
Kelele za akina mama na watoto ziligubika anga
la kijiji hicho, ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia
vilitendwa hadharani kwenye mbalamwezi
nyeupe.
Mzee Rutashobya bado alikuwa akiwaumiza
vichwa wale wavamizi huku akiangalia kila
linaloendelea, ijapokuwa roho ilimuuma sana,
lakini haikuwezekana yeye kujificha muda wote
huku akiwasumbua wale wavamizi, risasi
zilimwishia akabaki na gobole tu. Wakiwa bado
wanamsaka kwenye migomba, mzee Rutashobya
sasa alikuwa amejificha kwenye kichuguu.
Mmoja wa wavamizi alikuwa akija huku
akifuatiwa na wenzake kuelekea nyumba ya
Rutashobya, walipofika walivunja mlango na
kumtoa mke wa Rutashobya, Joseph naye
alishtuka usingizini, akatoka nje kasi ili
kumsaidia mama yake lakini teke kali lilimtupa
upande wa pili, kitendo hicho kilimfanya
Rutashobya kutoka mwenyewe kwa kasi
kumkabili Yule askari aliyefanya hivyo,
wakakutana ana kwa ana, Yule mvamizi
alimuona Rutashobya akija kasi wakati
akijipanga na bunduki yake kumlipua alichelewa
kwani kitako cha gobole kilitua shavuni na
kuvunja taya la jamaa huyo, Rutashobya
akavamiwa na askari kama watano na kuanza
kupigwa vibaya, wakati huo kiongozi wao Mali
ya Mungu akija taratibu kumuona mtu huyo
aliyekuwa akiwanyanyasa na tayari alikuwa
ameua askari wane kwa risasi zake nne.
“Muacheni!” sauti ya Mali ya Mungu iliwafanya
vijana hao wenye hasira kumuacha Rutashobya
akiwa hoi kwa kipigo, wakati huo mkewe akilia
kwa kwikwi na Jose ndio hatamaniki.
Mali ya Mungu akamsogelea Rutashobya,
akamtazama kwa tuo, “Wewe ndio unajifanya
kujua siyo?”alimwuliza huku akimzunguka, kisha
akasimama na kugeuka upande mwingine,
“Mleteni mkewe hapa, lazima niwaue wote
wawili kwa mkono wangu huu uliolaaniwa,”
alizungumza kwa sauti yake mbaya huku
akiupunga hewani mkono wake wa kuume.
“Aaaaaaaaiiiigghhh!!!!” ilikuwa sauti ya mke wa
Rutashobya alipokuwa akiburuzwa kuja kwa
mumewe. Joseph alikuwa akitazama huku
machozi yakimtoka, alitamani kuwaokoa wazazi
wake lakini haikuwezekana hakuwa na nguvu za
kufanya hivyo, alibaki kajikunyata na kutazama
ukatili huo wanaotendewa wazazi wake. Askari
mmoja alimuona Joseph pale alipojikunyata
akatoka kwenda kumfuata.
“Kimbia Joseph, usirudi nyuma!” mama yake
alimgutusha na Joseph alinyanyuka na kukimbia
bila kutazama nyuma akipita katika machaka ya
migomba, akilini mwake alihisi kuna mtu
anayemfuata nyuma kumbe ulikuwa ni mwangwi
wa nyayo zake kila zinapotua ardhini, alipogeuka
nyuma kuangali huku akiwa kwenye mbio hizo
alijibamiza kwenye mti na kuanguka vibaya,
damu zilikuwa zikitiririka kwenye jeraha
lililotokea pembeni mwa paji la uso wake,
akadondoka chini na kupoteza fahamu.
Giza nene lilimchukua Joseph kusikojulikana,
alikuwa akisikia sauti za watu ambao walikuwa
hawaeleweki wanachokiongea, hakuweza kuona
kitu isipokuwa giza lililomzunguka, giza nene
kuliko unavyofikiria, mara akaona watu wa
kutisha wenye mapembe na ndimi zinazowaka
moto kila waachamapo vinywa vyao, zile kelele
zikanyamaza, kukawa na kimya kikuu, sasa
Joseph alikuwa akisikia sauti ndogo ya tone la
maji lililokuwa likianguka kutoka juu na kutua
katika dimbwi kubwa la maji, sauti ile ilijirudia
rudia, akahisi kiu kikali kimeshika, akainuka
kutoka pale alipolala, mbele yake alisimama mtu
mwanaume ambaye mkono wake wa kuume
alimshika mwanamke, wote wawili walikuwa
wakionekana kwa tabu kutokana na giza lile.
Mara mwanga mwembamba ukawamulika,
walikuwa wamevaa maguo meupe yaliyokuwa
yamewafunika hata nyuso zao zisionekane. Yule
mwanaume alijifunua uso wake, alikuwa ni
binadamu asiye na sura, sura yote ilikuwa
imeliwa kama si wadudu basi sijui ni kitu gani.
“Joseph, hivi ndivyo tulivyofanywa wazazi
wako,” ilikuwa sauti ile ile ya baba yke
ikimwambia maneno hayo, kisha ikaendelea,
“Sasa unabaki kwenye ulimwengu wa peke yako,
utateseka sana mwanangu lakini roho za babu
zako hazitakuacha, lipa kisasi cha damu hii,
damu ya mzimu wa Rutashobya haiendi bila
malipo”. Mara tone la maji baridi sana
likamdondokea Joseph, akakurupuka kutoka
katika mzimio huo, na kujikuta peke yake porini.
Ilikuwa ndoto kama ndoto ya kutisha ndoto ya
kuogofya sana, Joseph alikuwa akibubujikwa na
machozi, kijua kitamu cha asubuhi kilikuwa
kikimchoma akiwa juu ya umande wa asubuhi,
akajinyanyua na kutazama huku na huko,
hakuna alichokishuhudia, ni moshi mkubwa
uliotapakaa angani, Joseph akashikwa na
uchungu akaanza kutimua mbio kurudi kijijini
kwao. Baada ya mwendo wa dakika kumi na
tano hivi bila kusimama alitoke upande wa
nyuma wa kijiji hicho, akakutana na kibao
kikubwa kilichoandikwa, “ENEO HILI LIKO CHINI
YA SERIKALI YA UGANDA, USIKATISHE.”
Joseph akasimama ghafla akatazama na
kusoma kibao hicho lakini hakuelelwa sawasawa
kilichoandikwa, alitembea taratibu ndani ya
machaka ya migomba, akitazama nyumba
zilizokuwa zikifuka moshi kwa kuchomwa moto,
miili ya watu bado ilikuwa imelala chini na
wengine hawakujulikana walipo, aliendelea
kuvuta hatua ndogondogo akitazama vizuri,
akafika usawa wa ilipokuwa nyumba yao, moto
ulikuwa ukimalizia kuangusha mti wa mwisho
uliokuwa umeshikilia nyumba hiyo, yote ikalala
chini, jivu. Joseph akajitokeza na kuvunja sheria
asiyoijua, akasimama mbele ya nyumba hiyo,
alipogeuka, mara akasikia kama mtu akikohoa,
akageuka huku moyo wake ukifanya paaaaa!
Alikuwa ni mtu aliyelala chini kwenye vumbi na
jivu, Joseph akamwendea kwa uoga na kumfikia,
aliitambua nguo ya mtu huyo, alikuwa baba
yake, aliyekuwa na majeraha na damu kila kona
ya mwili wake, sura yake ilikuwa imechafuka na
kugandwa na damu nzito ambayo ilificha kabisa
sura yake.
“Baba!” Joseph aliita. Mzee Rutashobya aliisikia
sauti ya mwanane lakini hakuwa na uwezo wa
kumuona kwani alikuwa ametobolewa macho,
kabla ya kupigwa risasi mbaya ya kifuani,
alikuwa akihangaika kupigania roho yake
iliyokuwa ikimuacha taratibu.
“Jose! Hauna wazazi, utabaki Yatima, nilikuwa
napigania nchi yangu, lakini haikuwa hivyo,
utakuwa mtu mzima, tafadhali damu ya
Rutashobya isipotee bila malipo, malipo
yanayoistahili,” alipokuwa akisema hayo alikuwa
akimwagikwa damu nyingi, akijaribu kuinua
mkono wake kuonesha kitu Fulani lakini
hakuweza.
“Nini baba?” Joseph aliuliza huku akilia kwa
uchungu, “Nyuma ya shimo la ch….o…..
chiiiooooo,” Mzee Rutashobya, akarudi ardhini,
Roho ikamuacha akatulia tuli, kwa utulivu
mkubwa. Upepo mkali ukaanza kuvuma katika
eneo lile, vumbi la moto na jivu likasambaa kila
mahali.
“Joseeeeeee kimbiaaaaaaa!!!!!!!!!!” alihisi sauti ya
mama yake ikimwambia kwa kelele kubwa,
Joseph akatimua mbio na kukimbilia
kusikojulikana.
WAZAZI WA JOSEPH WANAUAWA.... NINI

KITAENDELEA?
 
RISASI 4
ILIPOISHIA..
“Nini baba?” Joseph aliuliza huku akilia kwa
uchungu, “Nyuma ya shimo la ch….o…..
chiiiooooo,” Mzee Rutashobya, akarudi ardhini,
Roho ikamuacha akatulia tuli, kwa utulivu
mkubwa. Upepo mkali ukaanza kuvuma katika
eneo lile, vumbi la moto na jivu likasambaa kila
mahali.
“Joseeeeeee kimbiaaaaaaa!!!!!!!!!!” alihisi sauti ya
mama yake ikimwambia kwa kelele kubwa,
Joseph akatimua mbio na kukimbilia
kusikojulikana.

CHAPISHO LA 4

Vijana wa Jeshi la Wananchi kutoka Mtukula
walifika eneo hilo kwa kuchelewa, walikuta tayari
mauaji mabaya yameshafanyika na kijiji kizima
kipo chini kwa moto, hakuna hata jiwe lililosalia
juu ya jiwe. Kiongozi wa vijana hao Kepteni
Tibaijuka, hakuwa na la kufanya, alitazama
maafa hayo akabaki kimya, hakuna aliyeongea
na mwingine, kila mmoja alitoa kofia yake
kichwani kuonesha ishara ya majonzi.
Taarifa ya uvamizi huo mbaya kuliko iliyowahi
kutokea katika eneo hilo ilifika makao makuu
kwenye kitengo chake. Amiri jeshi mkuu
alishikwa na masikitiko makubwa juu ya hali
hiyo. Alijishika mikono shavuni akiegemeza
viwiko vya mikono hiyo mezani huku kifimbo
chake akiwa kakibana kwapani, alionekana wazi
kuchoshwa na taarifa hizo za kila siku,
aliyafunika macho yake kwa viganja vyake kisha
akayafikicha kiasi na kutoa ile mikono na sasa
akaiweka mezani na kuwatazama wale walioketi
mbele yake. Mkuu wa majeshi, Musuguli na
wasaidizi wake, wote walibaki kimya hakuna
aliyeongea katika mkutano huo wa dharula.
“Mzee, sisi tulishakwambia kabisa kabisa huyu
si mtu wa kumwacha hivi, tazama sasa
anavyonyanyasa watu wetu!” Yule mkuu wa
jeshi akamwambia Mwalimu.
“Nimekuelewa kijana, hata mimi hapa nafikiri
nini cha kufanya, maana hii inatisha,
anatudharau huyu, anaingia mpaka ndani kwetu
akidai ardhi ni yake, anavunja mikataba ya
kimataifa juu ya mipaka ya nchi,” Mwalimu
alijibu kwa uchungu, akakiweka kifimbo chake
mezani na kujiegemeza kwenye kiti chake cha
enzi, kiti kilichoibeba nembo ya taifa, akatafakari
jamabo, jamabo la kuamua juu ya usalama wa
raia wake.
Wakati Mwalimu akivuta muda kwa busara zake
huku akitumia mazungumzo kumsihi Nduli huyo
aache anachokifanya, wananchi walikuwa tayari
wamechoshwa na hali hiyo, kila mmoja
alitamanai kumkamata mtu huyo na kumtafuna
nyama lakini wote walikuwa wakisubiri amri ya
mkuu wan chi, majeshi yalikwishajipanga kwa
vita, yalikuwa yakisubiri amri ili yaanze kazi
ambayo kwayo ndio maana wamekuwa
wanajeshi.
§§§§§
3
J oseph Rutashobya alianza maisha
mapya, maisha pa sin a baba wala mama,
hakumuamini mtu, kila aliyemuona kwake
alimuona kama mnyama, kitendo walichofanyiwa
wazazi wake kilimuuma sana na kilimuachia
kumbukumbu mbaya moyoni mwake. Aliamua
kuishi peke yake, kila kukicha alikuwa akitembea
mwendo mrefu kwenda asikokujua, matunda ya
mwitu na vyakula vya kuomba, wakati mwingine
vyakula vya jalalani vilimsitiri na adha ya njaa.
Kutokana na umri wa Joseph ilikuwa vigumu
kutafuta ndugu aliamini kama wazazi wake
wameuawa basi kila binadamu mwenye
uhusiano na yeye ameuawa, hali hii ilimfanya
mara akimbie mara atembee kwenye barabara
ndefu za vumbi na machaka ya kutisha.
Baada ya mwendo wa siku nyingi wa mvua na
jua hatimaye Joseph alifika Bukoba Mjini, kwa
jinsi alivyokuwa alihitaji kitu japo cha kula au
kunywa ili aweze kupoza njaa kali iliyokuwa
imemletea udhoofu. Kila duka aliloingia na
kujaribu kuomba chochote alifukuzwa kama
mbwa, Joseph akaona maisha hayo hayawezi
bora kama angekufa pamoja na wazazi wake,
akaamua kwenda kwenye magari mabovu ili
kujistiri kwa siku hiyo akiwa amekata tama
kabisa ya kupata hata chakula, kichwani mwake
mawazo mengi yalikuwa yakipita ‘Au nikaibe
tu?’ alijiuliza, lakini kila alipotaka kupitisha
uamuzi huo alikumbuka maneno ya mama yake
siku nyingi nyuma yaliyokuwa yakimwambia
‘Mwanangu hakuna kitu kibaya kama wizi, ni
bora ukaomba kama unahitaji kitu, lakini si
kuiba, ukiiba watakupiga na kukuua,’ maneno
hayo yalimjengea ukuta katika maamuzi yake,
‘Nikiiba nitapigwa na kuuawa,’ aliyaelewa
maneno hayo lakini alibaki njia panda kwa
sababu hata akiomba alikuwa hapewi wala
hapati.
Akiwa njiani kutafuta maeneo ya kujitiri
alikutana na watoto ‘wakora’ waliokuwa
wakigombana, Joseph akasimama kuwatazama,
akagundua kulikuwa na makundi mawili
yasiyopatana na kila kundi lilikuwa na kiongozi
wake, hakujua ni nini wanachogombea,
aliwatazama kwa dakika kadhaa na alipoona
sasa wameanza kupigana, Joseph hakuifurahia
hali ile, kwa nini wapigane, akawaendea na
kusimama katikati yao.
“Kwa nini mnapina nanyi ni marafiki?”
akawauliza.
“Toka hapa kwanza we nani hata uingilie ugomvi
wetu, nenda zako ukalelewe na mama yako
huko, hapa tunaishi nmanunda tupu,
tutakumaliza sisi!” walipiga kelele zilizopishana
na haikueleweka nani kasema lipi na lipi kasema
nani. Joseph akaamua kuondoka na kuwaacha
watoto hao, mmoja kati yao akatukana tusi
lililomtaja mama, Joseph akashikwa na hasira,
akageuka na kurudi akamkamata Yule
aliyetukana, ngumi vichwa na mateke vilitawala,
mara wenzake wakaingia kumsaidia Joseph
hakujali kwani hasira zilimfanya kama kichaa,
akawapiga vibaya wote watano, wakakimbia na
kumuacha peke yake. ‘Kumbe na mi najua
kupigana!’ alijisemea moyoni kisha akavuta
hatua fupifupi na kwenda kuketi karibu na jumba
bovu moja ambalo lilikuwa hapo jirani na
barabara. Usingizi ukampitia, akalala.
Aliposhtuka usingizini, akajikuta hayupo peke
yake, kuna watoto wa rika lake, wako watatu.
Akawatazama kwa zamu.
“Mnataka nini?” akawauliza.
“Sisi tunataka ujiunge kwenye chama chetu,”
wakajibu. Jose aliielewa kauli hiyo kwani hata
shuleni alikotoka alisikia mara nyingi watoto
wenye mtazamo mmoja kujisema kuwa wana
chama chao. Akakubaliana nao, wakafurahi
sana. Mmoja wao akajitolea kwenda kuleta
chakula, Jose hakujua ni vipi na ni wapi, baada
ya nusu saa wote walikuwa wamesinzia tena
kwa shibe ya chakula hicho mchanganyiko
kilichokuja kwenye mfuko wa plastiki.
Joseph Rutashobya akajitambulisha kwa vijana
hao kama ‘Joru’ akaingia rasmi kwenye maisha
ya ukora , akawa hakamatiki, mhindi gani
asiyemjua Joru, kila uchwao watoto wa Kihindi
wanarudi nyumbani wakilia, Joru kawapora,
hela, chakula chao cha shule na wakileta ukaidi
wanapigwa makwenzi. Akimaliza kupora vitu
hivyo moja kwa moja alikuwa anavileta maskani
na kula na wenzake, lakini pesa alikuwa akificha
daima. Hakuna chama chochote cha watoto wa
mtaani kilichokuwa hakimjui Joru, kila
wanachama wake wakipigwa yeye ndiye
anaenda kama mtetezi na kupiga wote
atakaowakuta huko. Maisha hayo yalimjenga
usugu Joru akawa haogopi mtu wala watu, mara
kadhaa alikurupushwa na polisi lakini alikuwa
mjanja sana kwani alikuwa akihamisha chama
chake kila baada ya siku mbili na kuwaficha
mahali pengine, hiyo iliwafanya polisi au
wanaomtafuta washindwe kujua yuko wapi.
Siku moja jioni kama kawaida alikuwa katika
harakati zake za kutafuta windo, ndipo
alipopambana na mtoto wa mwarabu maarufu
sana hapo Bukoba mjini. Wakati Joru na
wenzake hawana kitu, wameteseka kwa njaa
mchana kutwa yeye alikuwa akirusha maandazi
kuwapiga njiwa. Hali hiyo Joru ilimuumiza sana,
alimtazama sana Yule motto na kisha
akawaambia wenzake wamsubiri akamwende,
makofi matatu ya mashavuni yalimtia akili Yule
motto akampa joru mfuko wa maandazi
yaliyobaki na pesa kidogo alizokuwa nazo
mfukoni, bahati mbaya alipofanya hayo kulikuwa
na polisi aliyekuwa akimuona. Joru na wenzake
wakaondoka kwenda maskani kama kawaida.
Usiku wa siku hiyo Josru akiwa na watu wake
ndani ya magari mabovu walikuwa wakisikiliza
redio, redio ndogo ambayo Josu alimpora mmoja
wa watoto wa kihindi hapo mjini. Ilikuwa kipindi
cha majira, saa tatu usiku, hotuba ya kihistoria
ya Mwalimu Nyerere ilikuwa ikirudiwa redioni,
hotuba hii ilimkuna sana akajikuta akishangilia
na kupiga makelele ovyo mpaka wenzake
wakaamka.
“Joru vipi una kichaa wewe?” wakamuuliza,
lakini Joru aliendelea kushangilia na kupiga
mbinja, hii haikuwa tabia ya Joru hata kidogo.
Lakini siku hiyo alikuwa kama mtu aliyewehuka
akili.
“Sikilizeni, Rais Nyerere anaongea,” akawaweke
kale karedio katikati yao.
“….nia ya kumpiga tunayo, uwezo wa kumpiga
tunao, nguvu za kumpiga tunazo…” maneno
hayo wenzake hawakuyaelewa ila Joru alielewa
kwa sababu alikuwa akisikiliza mara kwa m,ara
redio, akawaeleza wenzake.
“Rais Nyerere anaenda kumpiga Idd Amin,”
aliwaambia na wote wakaungana katika furaha
yake. Wakiwa katikati ya furaha yao, mara
wakavamiwa na kundi la watu, wakakamatwa na
kufungwa kamba wakapelekwa kituo cha polisi.
Joru alikuwa akilia njia nzima kwa kitendo hicho
mpaka alipofikishwa polisi, pale alimkuta Yule
mtoto wa kiarabu akiwa na baba yake, Joru
alitokwa na macho kukutana na mtoto.
“Huyu ndiye aliyeninyang’anya maandazi yangu,”
Yule motto wa Kiaarabu alizungumza huku
machozi yakimtoka. Joru alimkazia macho ya
hasira. Wale polisi wakamwambia Joru lazima
apate adhabu kwa lile alilolifanya. Joru
akagoma, akakataa katakata kwamba yeye
hakumnyang’anya maandazi. Lakini mabishano
kati ya watoto hawa yalikuwa makali mpaka
mmoja wa polisi alipoingilia kati. Joru
akachapwa viboko nane na wale askari na
wenzake wakachapwa viboko vine vine kila
mmoja kisha wakaambiwa wasionekane kabisa
mtaani.
Tangu hapo Joru akaona maisha hayo si mazuri
maana siku nyingine anaweza hata kuuawa.
Mchana wa siku iliyofuata, mji ulikuwa na
hekaheka sana, kila kona kulikuwa na askari na
wanajeshi, ndegevita nazo zilikuwa zikipita huku
na kule na kufanya kelele zisizo na mwisho. Joru
aliutazama mji wa Bukoba na kuona haumfai
hivyo aliamua kutafuta mahali pengine ambapo
angeweza kuendesha maisha yake. Jioni ya siku
hiyo hakuwaaga wenzake, wote walijua tu kuwa
amekwenda kutafuta chochoite kama kawaida
lakini sivyo, mguu na njia, malazi yakawa porini.
Baada ya kupata vibarua hapa na pale akapata
nauli kidogo akapanda basi na kushukia
Bihalamuro, huko hakuwa na mtu anayemjua,
kama kawaida yake alijikuta mitaani tu akizurula
hapa na pale na kuangalia hiki na kile, siku ya
kwanza ilimuishia katika mgahawa fualani
ambapo kwa kuwa hakuwa na chochote aliomba
mmiliki wa mgahawa huo ampe japo kazi ya
kusafisha vyombo ili apate kula, ikawa hivyo.
Siku zikaenda na miaka ikapita, Joru akaanza
kuwa kijana mkubwa, kifua kilianza kutanuka,
sauti ikawa nzito ya kutosha, Joru alibalehe na
kuwa rijali, hakuona tena umaana wa kufanya
kazi ya ile ya kuosha mabakuli kila siku, maana
tangu alipoianza mpaka siku hiyo ilikuwa ni tabu
tu, pa kulala ilikuwa tabu, aliwekewa kilago
katika banda la kuku hivyo yeye na kuku waliishi
pamoja.
Hali ya utulivu ilirudi nchini ijapokuwa kiuchumi
maisha yalikuwa magumu sana, Joru alikaa
mpaka miezi mine hajalipwa chochote kila
akimwambia tajiri wake alicojibiwa
hakikumridhisha. Majibu mabovu ya dharau
yalikuwa ndiyo apewayo kila uchwao.
‘Nitamvumilia mpaka lini?’ alijiuliza mara nyingi,
pale anapomuona akiwanunulia watoto wake
vitu mbalimbali vingine ikiwa ni vya kuchezea tu
wakati yeye hana chochote hana hata hela ya
kununua dawa ya mswaki. Joru aliwakwa na
hasira, akaamua kumfanyizia bosi huyo kitu
ambacho hatokisahau maishani mwake.
Siku moja ilikuwa jioni ya jumamosi, Joru
alijifanya anaumwa sana, Yule bosi wake
hakumjali sanasana alimpangia kazi nyingi za
kufanya siku yote. Ilipotimu mida ya saa kumi
jioni yeye na watoto wake wakatoka lakini
walimuacha binti mkubwa wa yapata miaka 20
hivi ili aangalie kinachoendelea katika mgahawa
huo. Joru alianza kulaghai binti huyu kwa neno
hili na lile, ijapokuwa binti Yule alikuwa hataki
kusikioliza maneno matamu ya mapenzi
aliyokuwa akiambiwa na Joru, kijana huyo
hakukata tama, kila alipomkuta kasimama
alimshika maziwa, mara kumtomasa kiunoni
ilimradi tu amuamshe nyege lakini Yule binti
alikuwa akikasirika sana hata wakati Fulani
alimpiga Joru kwa chupa ya chai. Joru
alitafakari sana, ijapokuwa pamoja na umri wake
huo yeye kama kijana hakuwahi kufanya
mapenzi na mwanamke ila katika mazunguzmo
yao ya vijiweni alipata raha ya tendo hilo kihisia
zaidi.
Akaachana na msichana huyo na kwenda zake
bandani anakolala, alikusanya kila kilicho chake
na kutia katika kijibegi chake cha mgongoni
alichojinunulia siku za karibuni, ‘Sasa naondoa
nyodo za huyu binti na hilo litakuwa pigo kwa
baba yake, mi ndio Joru motto wa kikopo, motto
asiye na wazazi, baba yake Jua mama yake
mwezi kaka na dada zake nyota, maadu zake
Mvua na jua,’ alijisemea huku akijipigapiga
kifuani.
Jioni hiyo kabla bosi wake hajarudi, akiwa bado
yupo yeye na binti huyo Kokusima, Joru
alijibanza katika mlango wa banda alilokuwa
akilala, akimwangalia binti huyo akienda kuoga,
Joru aliifurahia bahati hiyo kwa kuwa binti huyo
alivaa kanga ya Mombasa kwa mtindo wa
lubega na nyingine akajifunga kiunoni, alipoingia
tu Joru alimpa kama sekunde 25 nhivi akijua
tayari kwa kuda huo atakuwa kabaki kama
alivyozaliwa, akanyata taratibu kwa mwendo wa
kinyonga mpaka pale mlango wa bafuni, mlango
wa bati ulioshikizwa kwa kamba tu kwa upande
wa ndani. Joru kwa mara ya kwanza aliliona
umbo la mwanamke asiye na nguo, kwa
kuchungulia katika pachipachi za mlango ule,
mara akaona damu inachemka, moyo
unamuenda mbio, akasukuma mlango na kuingia
baada ya ile kamba kukatika kisha akaurudishia.
“Jamani nani huyo?” Kokusima aliuliza huku
sabuni ikiwa imemtapakaa mwilini hakuweza
kufumbua macho.
“Utamjua baadae,” Joru akajibu.
“Ha! Joru, yaani unanifuata bafu…” kabla haja
maliza, Joru akamkamata na kumbana mdomo
asitoa sauti, kisha kukuru kakara zikaanza,
kutokana na nguvu za Joru alifanikiwa
kumdhibiti Koku, kofi moja kali, Koku akawa
mpole.
“Ukipiga kelele nakumaliza,” Joru alimuonesha
kisu ambacho Koku alikiona kwa tabu sana
kutokana na sabuni iliyokuwa ikimuwasha
machoni, Joru akaanza shughuli yake mara
baada ya kuitoa dhana yake iliyosimama vyema,
japokuwa Koku alileta upinzani wa kimyakimya
lakini nay eye hakuwahi kujaribu mchezo huo,
hivyo mambo yakaenda japo kwa shida, huku
Koku akilia, Joru hakujari yeye aliendelea na
shughuli yake mpaka alipoona inatosha,
akamuwacha Koku bafuni akiwa anajililia yeye
akatoka na kubeba kibegi chake na kuondoka
zake, akapita kwenye mgahawa, akakuta
wafanyakazi wakiendelea na kazi zao, akapita
kaunta kwa sababu walikuwa wakimjua
hawakuwa na shida naye, Joru akavuta droo na
kubeba mauzo yote kisha akaondoka zake.
Mlangoni alikutana na bosi wake akirudi na
familia wakirudi. Ilikuwa kama saa mbili usiku
hivi wakasalimiana kama kawaida, Joru akaficha
kibegi chake, ile gari ya bosi wake ilipoingia tu
katika uwanja wa ile nyumba, Joru akapotelea
mitaani, moyoni mwake roho yake kwatu, pesa
kapata na binti wa bosi kamnanihii.

JORU ANALELEWA NA 'MTAA', KUTOKUWA NA
WAZAZI SASA KUNAMPELEKEA KUWA SUGU NA
KUPAMBANA NA MAISHA.....
ANAMBAKA BINTI WA BOSI WAKE KAMA KISASI
CHA KUNYIMWA MSHAHARA...
JE NINI KITAFUTA?
 
RISASI 4

ILIPOISHIA...
“Ukipiga kelele nakumaliza,” Joru alimuonesha
kisu ambacho Koku alikiona kwa tabu sana
kutokana na sabuni iliyokuwa ikimuwasha
machoni, Joru akaanza shughuli yake mara
baada ya kuitoa dhana yake iliyosimama vyema,
japokuwa Koku alileta upinzani wa kimyakimya
lakini nay eye hakuwahi kujaribu mchezo huo,
hivyo mambo yakaenda japo kwa shida, huku
Koku akilia, Joru hakujari yeye aliendelea na
shughuli yake mpaka alipoona inatosha,
akamuwacha Koku bafuni akiwa anajililia yeye
akatoka na kubeba kibegi chake na kuondoka
zake, akapita kwenye mgahawa, akakuta
wafanyakazi wakiendelea na kazi zao, akapita
kaunta kwa sababu walikuwa wakimjua
hawakuwa na shida naye, Joru akavuta droo na
kubeba mauzo yote kisha akaondoka zake.
Mlangoni alikutana na bosi wake akirudi na
familia wakirudi. Ilikuwa kama saa mbili usiku
hivi wakasalimiana kama kawaida, Joru akaficha
kibegi chake, ile gari ya bosi wake ilipoingia tu
katika uwanja wa ile nyumba, Joru akapotelea
mitaani, moyoni mwake roho yake kwatu, pesa
kapata na binti wa bosi kamnanihii.

CHAPISHO LA 05

Baba wa Koku alikaribishwa na kilio cha binti
yake, alichokisikia kutoka bafuni.
“Mama Koku, huyo si Koku anayelia, hebu nenda
kamwangalie,” akamwagiza mkewe akamwangalie
binti yao kule bafuni. Lo, mama alimkuta bintiye
akiwa chini sakafuni, hana nguo, mwili bado
umejaa povu la sabuni, kilio kinatawala, hapa na
pale palikuwa na damu zilizochanganyika na
damu.
“Nini mwanangu?” mama akauliza.
“Joru, Joru kanibaka!” alijibu Koku. Mama Koku
akatoka na kumpa taarifa mumewe, hasira
ikawaka, ‘Namuua Joru,’ alijiwazia, akaingia ndani
akachukua kisu chake kikubwa na kupotelea
mtaani kumsaka Joru, aliposhindwa, akaripoti
polisi, polisi wakaingia kumsaka Joru kila kona,
Joru hakuonekana, kila walipouliza, vijiweni kote
Joru hakuonekana.
Ilikuwa ni fadhaha kwa familia, aibu kwa Koku,
Mama wa Koku alibaki hana la kusema,
alikwenda bandani alikokuwa akilala Joru na
kukuta kijikaratasi juu ya godoro, akakiokota.
Ilikuwa ni ngumu kusoma maandishi hayo
yaliyoandikwa kwa mwandiko mbaya kama kapita
bata, na hii ilichangia kwa Joru kuwa na kisomo
cha madarasa matatu tu.
“…Nimefanya kazi sana, hamtaki kunilipa
mshahara, nilichokifanya ndicho shukrani na
malipo yangu, asanteni kwa kila kitu. Mimi ni
mtoto wa mtaa, na mtaa utaendelea kunilea
mpaka siku utakaponichoka wenyewe…”
Baada ya kusoma kijikaratasi kile Mama Koku
akaangusha chozi, akalia sana lakini hana la
kufanya. Alimpenda sana Joru lakini hakuamini
alichokifanya na hakuamini alichofanyiwa. Baada
ya Joru kukosekana kila mahali, hasira za mzee
huyo zilipungua ijapokua alihapa kuwa popote
atakapokutana naye lazima amtoe uhai kijana
huyo asiye na faida.
§§§§§

Joru pamoja na upole wake, sasa aliingia katika
magenge ya kihuni, wavuta bangi na wacheza
kamali katika viunga vya mji mdogo wa
Biharamulo, kwa kuwa alihofia siku yoyote
kukamatwa na polisi, Joru alikuwa kila usiku
akilala porini, akikwea juu ya mti na
kujipumzisha, hayo ndiyo yalikuwa maisha ya
Joru.
Siku moja akiwa katika malalo yake huko porini
alijikuta akiota ndoto mbaya sana, watu
wakimchoma moto na kumpiga kwa magongo na
mawe, alishtuka kutoka usingizini na kudondoka
kutoka katika lile tawi mpaka chini, akaumia
kiuno, Joru akawa hawezi kutembea isipokuwa ni
kutambaa tu, hakuwa na ujanja, alijikaza na
kutambaa kwa mwendo wa kitambo mpaka
barabarani, hapo alipata msaada wa kijana
mmoja ambaye alimfikisha katika hospitali ya
jeshi la wananchi, pale akapata matibabu na
kupumzishwa kwa wiki kadhaa.
…Joseph mwanangu…. Najua unateseka sana,
lakini maisha unayoyaishi hayakustahili, achana
na tabia za uhuni, rudi uwe Joseph yuleyule
niliyemuacha, roho ya Rutashobya haitakuacha
mpaka utimize lile inalotaka,…
Sauti hiyo ya mama yake ilimjia katika mawazo
kama radi kali, Joru alianza kutetemeka kwa hofu,
akiwa pale kitandani, akazama katika wimbi la
mawazo, akamkumbuka mama yake na baba
yake, akayakumbuka mateso makali waliyoyapata
mpaka kifo chao, akakumbuka kauli ya baba yake
ya mwisho ambayo haikuisha iliyomwambia
‘nyuma ya choo’ , Joru akajiuliza mara kadhaa,
nyuma ya choo, hakujua baba yake alitaka
kumwambia nini, akatulia na kuruhusu machozi
yamtiririke. Mara pembeni yake akasimama
daktari mwanamke, aliyevalia kijeshi na juu yake
alikuwa na koti jeupe, Joru akamtazama kwa
kumhusudu mwanadada huyu aliyependeza katika
nguo zake hizo.
“Samahani daktari,” Joru aliuliomba. Yule daktari
mwanadada akageuka na kumtazama Joru kwa
jicho kali, kisha akavuta hatua kumfuata pale
alipolala.
“Naomba kukuuliza, hivi Idd Amin
alishakamatwa?” Joru aliuliza. Swali hilo kwa
askari huyu lilikuwa swali la kipumbavu sana,
akacheka kwa dharau.
“Hakukamatwa, alitoroka,” Yule daktari akajibu
huku akiondoka. Joru alikaza macho kumwangalia
daktari Yule mpaka alipopotelea katika vyumba
vingine vya wodi hiyo. Joru akakumbwa na
usingizi na kulala fofofo, ndoto nyingi nzuri na
mbaya zilimjia kichwani mwake, aliweweseka
sana, “Nitalipa kisasi, baba usihofu nitalipa
kisasi,” alikuwa akisema kwa sauti ya chini
ambayo ilisikiwa na mtu aliye jirani yake tu. Joru
alihisi anaguswa na kutikiswa mguu wake kuwa
aamke, akapambana na hali hiyo mpaka mwisho
akaamka na kufumbua macho yake. Pembeni
yake alisimama mwanaume mmoja, si kijana
sana wala si mzee sana, walitazamana macho.
“Nimekusikia ulipokuwa ukujitambulisha kwa
daktari mara ile ya kwanza,” Yule mwanaume
alimsemesha Joru, akakohoa kidogo akavuta kiti
na kuketi karibu na kitanda alicholala Joru,
akaendelea kumtazama kijana huyo, “Joseph
Rutashobya, nimekuwa nikilisikia jina hili kwa
muda mrefu sana, mpaka nikawa na hamu ya
kukuona,” akaendelea kusema.
“Wewe ni nani?” Joru aliuliza.
“Usiogope, kwanza kwa nini umemuuliza daktari
kama Idd Amin amekamatwa?” akamuuliza.
“Nimeuliza kwa sababu nataka kujua,” Joru
akajibu.
“Ina maana wewe hujui lolote juu ya Idd Amin?”
Yule mtu akmuuliza tena.
“Aaah! Ndio sijui lolote, mi naishi nje ya
ulimwengu, siwezi kujua ya ulimwengu, nilitoka
zamani sana,” Joru alijibu. Maneno haya
yalimuweka Yule mtu njia panda, hakuelewa Joru
alikuwa akimaanisha nini kwa kauli yake hiyo,
akabaki akimtazama tu.
“Mbona unaniangalia?” Joru alimuuliza Yule
mwanaume.
“Nakushangaa kwa kile unachoniambia, unaishi
wapi?” Yule mwanaume alimwuliza tena.
“Sijui nikujibu nini, ninapoonekana ndipo
ninapoishi, linaponikuta giza ndipo ninapolala,”
akajibu Joru.
“Ok, nimekuelewa, nitahitaji tuonane mara ukitoka
hospitali,” Yule mwanaume akamwambia. Joru
alimtazama kwa kitambo, hakummaliza yule mtu,
kisha akafungua kinywa chake na kumuuliza.
“Nitakupataje, nikuulizie wapi na kwa jina gani?”
“Captain Shibagenda, ukitoka tu hapa ulizia hata
hapo getini watakuleta kwangu,” Yule mwanaume
akajibu na kuondoka kutoka nje ya wodi ile.
“Captain Shibagenda,” Joru alijisemea kwa sauti
ya chini na kuvuta shuka kujifunika gubigubi.
Joseph Rutashobya, aliendelea kulala palepale,
ilikuwa wiki kadhaa zimepita tangu afike katika
hospitali ile ya jeshi. Bila kutegemea jioni ya siku
hiyo aliruhusiwa kutoka hospitali. Joru alitoka
katika jengo la wodi ile na polepole alikuwa
akivuta hatua ndogondogo kuelekea getini mwa
kambi hiyo, alifikiria kumuulizia Yule mtu lakini
moyo wake ulisita, akaamua kutoka na kuondoka.
Joru alikuwa hajui hata ni wapi akielekea,
akafuata njia iliyokuwa ikielekea madukani.
“Joseph!” mara alisikia sauti ya kike ikiita. Joru
akasimama kwa mshtuko na kugeuka, ilikuwa ni
giza kidogo hakuweza kumuona vyema Yule
anayemwita, alipomsogelea akamfahamu, dakatari
wa kike aliyekuwa akimtibia pale hospitali,
“Unaenda wapi?” akamuuliza.
“Nimeruhusiwa, naenda kulala,” akajibu Joru,
huku akimtazama daktari Yule.
“Unaenda kulala wapi? Mbona mi nimeambiwa
kuwa wewe umeokotwa tu barabarani? Joru hebu
nambie ukweli,” Yule dada akamwambia Joru.
Joru akainama chini kwa aibu kidogo, kisha
akamtazama mwanadada Yule ambaye
ukimtazama huwezi kufikiri kama ni ‘binti jeshi’ .
Joru akashikwa mkono, akashtuka na kumtazama
Yule daktari, “Twende ukale, kisha nitakuruhusu
uende kutafuta pa kulala.”
Joru akaongozana na yule dada ‘binti jeshi’
wakarudi tena jeshini katika kota za wafanyakazi.
Joru aliona watoto wengi waliokuwa wakicheza
michezo mbalimbali kwa furaha sana huku mama
na baba zao wakiwa vibarazani wameketi
wakibadilishana mawazo. Hali hiyo ilimhzunisha
sana Joru alikumbuka miaka kadhaa nyuma kijijini
kwao, alimkumbuka Kemilembe wake kwa mara
yakwanza, lakini mpaka muda huo hakujua binti
huyo yuko wapi, sanasana alijua atakua amekufa
kama walivyokufa wengine, Joru aliamini kuwa ni
yeye tu aliyepona kutoka katika kijiji kile.
Mwenyeji wa Joru aliandaa chakula na kuweka
mezani, akamkaribisha Joru nao wote pamoja
wakaanza kula huku mazungumzo ya hapa na
pale yakiendelea.
“Hebu nambie Joru, kwa nini siku ile uliniuliza juu
ya Idd Amin? Kiukweli mtu huyo hakukamatwa na
wala hajafa, alitoroka baada ya majeshi ya
Tanzania kufika kabisa jirani na pale alipo,”
alimwambia kwa kifupi.
“Na Mali ya Mungu, alikufa au amekamatwa?”
Joru akamuuliza tena swali geni kabisa. Yule
daktari akanyamaza kimya kwa sekunde kadhaa,
akamtazama Joru usoni.
“We unamjua Mali ya Mungu?” akamwuliza Joru.
“Ndiyo namjua sana, sana tu, na kama yuko hai
nina shida naye,” Joru alimwambia Yule dada.
“Yupo, katika vita ile hakufa, lakini sijui sasa
atakua wapi, we umemjuaje na una shida gani
naye?” Joru alipokea swali linguine.
“Kiukweli, siwezi kukwambia ni nina shida naye
gani, lakini siwezi kumpata, basi,” Joru akajibu na
kuinua kikombe chake cha chai, akapiga funda
kadhaa kwa mtindo wa mruzi.
“Ulale hapa Joru,” Yule dada alimuomba Joru
alale pale.
“Hapa, kwangu si mahali salama, sijazoea kuishi
na binadamu,” Joru akajibu. Baada ya muda
mfupi Joru aliandaliwa maji ya kuoga katika bafu
la nje na kutakiwa kwenda kuoga. Joru
akashukuru akanyanyuka na kuonesha chumba
atakachotumia kulala, akakitazama na kwenda
zake bafuni kuoga.
Joru, kutokana na aina ya maisha aliyokuiwa
anaishi hakuona usalama wowote wa kuishi na
watu kama hawa, baadae aligundua kuwa
unaweza kuwa ni mtego ili akamatwe na wabaya
wake, hakuwa tayari, aliliacha taulo juu katika
msumari nay eye kupotelea nje akimuacha Yule
dada bintijeshi akimsubiri, Joru alitoka nje ya
kambi ya jeshi na kupotelea anakokujua yeye.

4….
rejea MTUKULA
JESHINI

MKUU wa majeshi Shibagenda aliondoka eneo lile
na mgeni rasmi na kuendelea kukagua gwaride
hilo. Walipomaliza ukaguzi huo wakarudi jukwaani
kuungana na wageni wengine ili kupisha gwaride
hilo kufanya utaratibu mwingine wa maadhimisho
hayo.
“Gwarideeeee!!!! Kulia geuka!” amri ilitolewa
wanajeshi wote wakageuka kulia na kupiga mguu
chini, kisha viongozi wa gadi mbalimbali
wakaondoka katika maeneo yao kwa mwendo wa
haraka na aina yake na kusimama mmbele ya
vikosi vyao wakisubiri amri nyingine ya kiongozi
wao.
“Gwaride litapita mbele ya mgeni kwa mwendo
wa pole, na kisha mwendo wa haraka,
mbeleeeeeeee tembea!” amri ikatoka, na ngoma
laini kutoka kwa kikosi cha bendi ya tarumbeta
cha jeshi ikaanzisha wimbo mtamu na kuwafanya
vijana hao waanze kutembea kwa madaha na
maringo, kila aliyekuwa hapo alitazama miguu ya
vijana hao iliyokuwa ikienda kwa ufundi mkubwa,
hakika walipendeza, hakika walivutia, hakika
waliipamba sherehe hiyo.
…Wazazi wangu wangekuwepo, siku hii
wangeifurahia sana, mama angenikumbnatia na
kunibeba kama nilivyokuwa mchanga,
angenitemea mate kwenye paji la uso ili safari hii
iwe ya Baraka na mafanikio….
Joru alikuwa akisema moyoni maneno hayo,
akiwa anapita mbele ya jukwaa la mgeni rasmi
akiwa amegeukia kulia kama ishara ya heshima
kwa mgeni rasmi gwaride linapokuwa katika
mwendo wa pole. Mawazo ya Joru yalikuwa ni
juu ya wazazi wake siku nzima ya sherehe hiyo.
Baada ya dakika thelathini gwaride lilikuwa
limejipanga tena mbele ya wageni baada ya
kumaliza sehemu hiyo ya kutoa heshima.
Watu walikuwa wamefurika katika uwanja huo
wakishangilia na kupiga makofi kila vijana hao
wanapoonekana kufanya jambo Fulani la
ukakamavu, Joru alikuwa akisumbuliwa na kelele
za mashangilio hayo kwa maana alijua wazi kuwa
hazimhusu yeye.
Gwaride lilikwisha, tayari ilikuwa ni saa saba
mchana, mawingu yalilifunika jua na kufanya hali
ya hewa kuwa ya kaupepo kidogo uwanja ulibaki
kimya na hakukuwa na mtu katikati isipokuwa
wageni na raia waliokuja kuwapongeza ndugu zao
kwa kuhitimu mafunzo. Muongoza sherehe
alitangaza kuwa sasa ni wakati wa vijana hao
kuonesha umahiri wa mafunzo waliyoyapata.
Walianza kuonesha aina mbalimbali za mapigano
ya silaha baada ya kumaliza hapo yalifuata
mapigano ya mikono, umahiri uliooneshwa wa
kucheza mitindo ya kungfu na karate iliwakosha
watazamaji, muda wote walikuwa
wakiwashangilia vijana hao waliokuwa ndani ya
mavazi rasmi ya kijeshi.
Baada ya hapo lilifuata onesho la mtu mmoja jinsi
anavyoweza kuwakabili watu zaidi ya watano,
Joru alikuwa ni huyo mtu mmoja, kazi ikaanza,
akavamiwa na wenzake wasiopungua watano,
Jorun akaonesha umahiri wa kuwapa kipigo kwa
mtindo wa Karate, akipangua na kupiga,
akijijengea umakini ili asipatwe na shambulizi
lolote, mara kwa mara alionekana jinsi
anavyobadili miondoko ya mikono na miguu yake
na kutoa aina ya ukelele iliyokuwa
ikipendezewsha mchezo huo, dakika tatu alikuwa
tayari kawalaza wote chini, makofi na nderemo
vikatawala. Likaja onesho la tatu, kijana yuleyule,
sasa alitakiwa kupambana na watu wane wenye
visu na mapanga hali yeye hana chochote, Joru
alitunisha misuli yake kuonesha jinsi mwili wake
sasa ulivyokakamaa kimazoezi, akaonesha
umahiri wa kukwepa na kupiga kiufundi kisha
akawashinda wote wane na kuwalaza chini,
akakusanya mikono yake kifuani na kuinama kwa
heshima, makofi yalisikika kila kona. Brigedia
Shibagenda hakuamini anachokiona kutoka kwa
huyui motto wa mtaani, mtoto aliyesumbua mitaa
ya Bukoba mpaka Biharamulo, aliyeonekena
takataka, aliyelazwa kwenye mabanda ya kuku
lakini leo hii alionekana wazi kuwa ni hazina ya
JW, Shibagenda aling’amua wazi kuwa mitaani
kuna hazina nyingi zinazozurula ovyo bila
kuwekewa mkakati, alijikuta akisimama na kupiga
makofi ya kumpongeza.
Joru alirudi nyuma na kupisha onesho linguine
ambalo liliwasilishwa na wengine kwa umahiri
mkubwa na wa kisasa. Baada ya maonesho
kadhaa kupita, pale mbele pakawekwa tofali na
ilitakiwa mtu mmoja aje kulivunja kwa mikono pia
kulikuwa na miti iliyowekwa kma magoli ya mpira
yote hayo ilitakiwa mtu ayavunje kwa umahiri,
mbele ya wote akasimama Joseph Rutashobya,
alipoonekana tu mbele ya watu, wote wakaanza
kushangilia huku vijana wakipiga mbinja na
kutamka Joru, Joru, Joru Joru. Joru akasimama
katika msimamo wa mashambulizi huku
akibadilisha mwendo wa mikono yake katika
mtindo wa kupendeza, akavuta hatua na kuruka
hewani kwa mtindo wa aina yake akapiga kile
kigogo kwa mguu wake kikapaa juu, Joru alipotua
chini akajirusha tena kwa ufundi na kukizabu kwa
mguu wake mwingine na kukipasua vipande
viwili, alipotua chini moja kwa moja mkono wake
wa kulia ulipiga pigo moja juu ya tofali na
kulitawanya vipande vipande, Joru aliuma meno
mkono wake ukatetemeka, “Yuko wapi Mali ya
Mungu?” aliongea kwa sauti ya chini huku chozi
likimtoka kwa hasira. Makofi, vigelegele, nderemo
na vifijo vilimfanya Joru ajue kuwa wapo
wanaompenda, wapo wanaomhitaji, wapo
wanaomthamini katika jamii, alitikisa kichwa kwa
masikitiko, akamuomboleza baba na mama yake,
akasimama na kutoa ishara ile ile ya heshima na
kurudi kukaa walipokuwa wamekaa wenzake.
Ilipotimu saa nane na nusu sherehe ile ilikuwa
ikifika ukingoni, ilikuwa ni wakati wa kutoa
zawadi maalum kwa wahitimu.
Miongoni mwa wageni waliohudhuri alikuwepo Dr
Janeth Ishengoma, huyu aliposikia jina la Joseph
Rutashobya likitamkwa kuwa amepata zawadi ya
utii, mlenga shabaha mahiri na ukakamavu,
alijikuta anashidwa kujizuia, alikuwa
akimfananisha kijana huyu na Yule aliyemtoroka
nyumbani kwake siku ile alipomkaribisha na
kumuwekea maji bafuni maji ya kuoga na
aliporudi hakumkuta. Dr. Janeth alimtafakari Joru
hakummaliza alimtazama jinsi anavyotembea kwa
ukakamavu akipewa zawadi yake huku
mashangilio yakiongezeka, Joru, Joru, Joru, Joru…

NINI KITAENDELEA?
 
RISASI 4
ILIPOISHIA
Miongoni mwa wageni waliohudhuri alikuwepo
Dr Janeth Ishengoma, huyu aliposikia jina la
Joseph Rutashobya likitamkwa kuwa amepata
zawadi ya utii, mlenga shabaha mahiri na
ukakamavu, alijikuta anashidwa kujizuia,
alikuwa akimfananisha kijana huyu na Yule
aliyemtoroka nyumbani kwake siku ile
alipomkaribisha na kumuwekea maji bafuni
maji ya kuoga na aliporudi hakumkuta. Dr.
Janeth alimtafakari Joru hakummaliza
alimtazama jinsi anavyotembea kwa ukakamavu
akipewa zawadi yake huku mashangilio
yakiongezeka, Joru, Joru, Joru, Joru…

CHAPISHO LA 06

Turudi nyuma nyumbani kwa Dr
Janeth…
JORU alitazama huku na kule hakuona mtu
maana usiku ulikuwa mwingi, akaingia mitaani
na kutafuta sehemu yenye kichaka na kujipatia
usingizi wake hapo huku bado mguu wake ukiwa
haujakaa sawa kwa shuruba nyingine.
Joru alitamani kurudi kuishi na watu lakini
aliona wazi kuwa siku akipambana na polisi
lazima atafungwa kwa maana alikumbuka
madhambi mengi aliyoyafanya na zaidi kumbaka
binti wa bosi wake hili lilimuumiza kichwa.
Alitamani kurudio kwao kijijini lakini bado alipata
kumbukumbu mbaya ya matukio yaliyopita,
hakutaka kurudi kule kwanza aliamini kuwa kila
mtu atakuwa amekwishakufa kama ilivokuwa
kwa wazazi wake, ilimpa shida.
Kulipopambazuka hakutaka kuonekana mitaa ile
kabisa, alijivuta taratibu huku mguu mmoja bado
ukionekana wazi kuwa kuwa haukuwa
sawasawa. Alipokuwa akiifuata barabara kubwa
pembezoni tu mwa ile kambi ya jeshi ambako
alikuwa akitibwa, akaona gari moja ambayo
anaijua fika ikipita kwa kasi na mbele yake
ikapunguza mwendo, Joru akasimama
kuitazama, akaikumbuka, gari ya bosi wake
aliyekuwa akimlaza katika banda la kuku, Joru
akatabasamu, ‘Watakoma mama zao,’
akajisemea neno hilo la kashfa, kisha akatoa
sonyo refu. Akaendelea kuitazama ile gari
ikikata kona kuingia mle jeshini, Joru akashtuka,
‘lo, ningelala kwa Yule mwanamke
ningekamatika leo, asante Mungu,’ akajisemea
kisha akingia zake mtaani kwa upande
mwingine, alipokuwa katika kutembeatembea
akitafuta wapi anaweza kupata kifungua kinywa,
akahisi mtu akimshika bega, Joru akashtuka,
moyo wake ukafanya paaaa!
“Joru,” sauti nzito ya kiume ikayafikia masikio
yake. Alipogeuka hakuamini macho yake,
Kalokola, rafiki yake wa siku nyingi, aliyekuwa
naye katika chama kimoja cha mitaani, sasa
walikutana baada ya muda mrefu sana kupita,
kila mmoja alikuwa baba tosha kwa kupevuka.
“Kalo, upo? Leo imekuwa bahati sana aisee,
tangu tuachane sijaonana na mtu yeyote katika
chama chetu, vipi jamaa wanaendeleaje?” Joru
aliuliza kwa furaha sana.
“Aaaaa siku ile wewe ulipoondoka, na chama
kikaishia palepale, mimi siku hizi sipo kule kaka,
nafanya kazi ya ufundi magari,” Kalokola
akamwambia Joru.
“Aaaaa mwenzangu umeula! Mimi bado
natangatanga na mtaa maisha yananisukuma
huku na kule lakini naendelea vyema,
nilipowaacha nikaja huku Biharamulo na kufanya
vibarua lakini waliniuzi nikawafanyia mbaya,
yaani hapa mda wowote nitakuwa mikononi
mwa polisi,” Joru alimweleza rafikiye kwa kifupi.
“Aaaa Joru, haujaacha tu fujo zako? Nyoka wa
kijani, Joru,” Kalokola aliongea huku
akimpigapiga mgongoni kisha wote wakaangua
kicheko.
“Sasa Kalo, mwenzio hapa hata chai sijapata
halafu naumwa si unaona nachechemea mguu
huu,” Joru akajieleza.
“Joru, hilo lisikuumize kichwa, wewe ni rafiki
yangu sana, unakumbuka uliniokoa kwenye yale
mapigano pale Bukoba na wale watoto wakora,
siku yetu ya kwanza kukutana na tukakutawaza
kuwa mkubwa wetu,” wakacheka tena na
kugonganisha viganja vyao.
Kalokola na Joru wakajivuta mpaka kwenye
mgahawa wa jirani na kuingia kisha wakaagiza
chain a maandazi kila mmoja, wakanywa huku
wakiongea mambo mengi yaliyopita,
wakibadilishana mawazo ya kila mmoja
alivyofika hapo. Joru alivutiwa sana na
mapambano aliyopambana Kalokola katika
safari yake.
“Yaani Joru, bora uliondoka, haikupita siku mbili,
lilitokea vurugu pale mjini tukakusanywa wote,
mi nilifungwa miaka miwili ndipo nilipojifunzia
ufundi magari huko magereza, nimetoka jela
hata miezi saita sijamaliza bado, nimejishikiza
ufundi kwenye gereji ya mwarabu mmoja hivi,”
Kalokola alimweleza Joru.
“Safi sana Kalo, umefanya jambo jema sana,
sasa utafute pesa, upange au ujenge uoe mke
uzae watoto na ujenge familia yako,” Joru
alimwambia Kalokola maneno hayo mazito huku
mkono wake ukiwa umetua juu ya bega la
rafikiye nay eye machozi yakimdondoka taratibu.
“Joru, kwa nini unalia rafiki?” Kalokola
akamuuliza.
“Siijui kesho yangu, nasubiri kufa kwangu,
sidhani kama nina thamani duniani tena, hata
nikifa ni manispaa itakayonizika endapo
itagundua maiti yangu, kama la, basi nitabaki
niliko na mwili wangu kuliwa na fisi au tumbusi,”
Joru aliyasema hayo huku machozi yakimtiririka.
“Joru, acha kulia, umesema vyema kuwa kesho
yako huijui name nakuhakikishia kesho yako
anaijua Mungu, we tulia, sasa una mpango
gani?” kalokola alimtuliza Joru na kisha
kumtupia swali.
“Nafikiri kwenda kufia Uganda, nataka nikalipize
kisasi cha mauaji ya wazazi wangu,” Joru
alijibu.
“Joru, unamjua aliyeuwa wazazi wako?” Kalo
aktupa swali linguine.
“Namjua na nimemuona, anaitwa Mali ya
Mungu, kama yuko hai lazima nikamuue kama
amekufa basi nikalikojolee kaburi lake,” Joru
alijibu kisha akatikisa kichwa chake, akata
andazi na kujimiminia chai yote iliyobaki
kikombeni, “Aaaaaaaaaggghhhhh! Tanzania Tea
Blenders, aisee asante sana kwa kifungua
kinywa, sasa mi nafikiri tuagane, nahitaji
kupumzika,” Joru akamalizia kusema.
“Joru huna pa kupumzika, nifuate, pale gereji
kuna magari mengi mabovu nitakutafutia
mojwapo upumzike na hatokusumbua mtu,” Joru
alikubaliana na nrafiki yake, wakatoka nje ya
mgahawa huo.
“Una shilingi mia tano hapo?” Joru akauliza.
“Ipo, vipi?”
“Ninunulie kofia, nijisitiri pia sura yangu
isionekane na wabaya wangu,” Joru akamjibu
Kalo.
“Ok, kofia gani inakufaa, balaghashia, pama,
kapelo, balleti au ipi?” Kalo akauliza kwa kutaja
mlolongo wa kofia.
“Haujaitaja kati ya zote, ninunulie ‘Mungu
usinione,’ cap,” Joru akajibu.
Joru na Kalokola waliwasili kaytika gereji
anayofanyia kazi kalokola, na kama
alivyomuahidi akamfungulia mlango wa hiace
moja iliyokuwa hapo muda mrefu na kumuweke
kiti kwa kulala, Joru akashukuru na
kujipumzisha hapo. Joru alibebwa na usingizi
mzito ambao hakupata kwa siku nyingi.
“…Umekuwa sasa Joseph, ni wakati wako wa
kuanza kile niichokwambia, usione unafanikiwa
kukwepa hatari nyingi, ni baba na babu zako
wanaofanya hio kwa kuwa wanakulinda ili uilipie
damu yao iliyomwagika…”
Joru alikuwa akiota na kuyasikia maneno hayo
aliyokuwa akiambia na baba yake katika ndoto
hiyo.
“Sawa baba, nitatimiza,” naye alijibu akiwa
usingizini.
“….Usikate tamaa Joseph, usiyachukie maisha,
njia yako itafunguka muda si mrefu nawe
utaliona jua katikati ya giza, latakaloondosha
kwako nuru hafifu ya mbala mwezi na
kukuangazia kwa mwanga mpya….”
Joru aliitikia tena lakini bado alikuwa katika
usingizi mzito sana, akaendelea kuota ndoto
mbayambaya na nzuri nzuri, Joru aliota
akitembea juu ya daraja kubwa sana mara
akawa anasikia mtoto analia, sauti ya kuomba
msaada, sauti ya mtoto mchanga, Joru
akasimama na na kutafuta wapi mtoto huyo,
mara akamuona motto akilia akiwa amelazwa
pembeni tu mwa barabara aliyokuwa akipita,
karibu kabisa na daraja lile, alimtazama na
kutetemeka sana. Akavuta hatua kumsogelea
maana huruma iliukamata moyo wake
akamfuata motto Yule taratibu na kumyanyua
akamkumbatia kifuani mwake, mara akasikia
sauti za vicheko zenye mwangwi wa kutisha
zikafuatiwa na makofi ya pongezi.
“….Umekuwa mkubwa Joru, sasa una motto
mchanga aliyezaliwa muda huu, hakikisha
unamtafutana kumpata huyo ndiye atakuwa
faraja yako maishani….”
Joru alikurupuka kama mtu aliyegutushwa ghafla
akawa anahema kwa nguvu zote kama mbwa
aliyekimbia mwendo mrefu. Akashuka kutoka
katika ile gari aliyokuwa amelala, akaliendea
bomba na kunawa maji na mengine akanywa
kisha akajishika kiuno na kutafakari jambo.
Alitazama huku na kule hakumuona Kalokola
akauliza kwa jamaa waliokuwa pale
wakamwambia Kalokola ametoka kuna gari
wamekwenda kulichukua lakini hawakujua
atarudi saa ngapi. Joru akaamua kuondoka
akawaachia ujumbe kuwa atarudi siku ya pili
yake.
§§§§§

Mauaji ya kimbari ya Rwanda na Burundi 1994
Taarifa ya kudunguliwa kwa Rais wa Burundi na
Rwanda mwaka 1994 zilimfikia Joru akiwa
kajipumzisha kwenye makazi yake ya muda
ambayo hakuna aliyekuwa akiyajua. Alikuwa
akionekana mjini mara tu akiwa na mahitaji ya
muhimu lakini wakati mwingine hakuwa na
muda wala haja ya kuja mjini. Mjini kwake
aliona hakumfai kabisa kabisa kwa maana kila
akitua huko lazima kutokee janga ambalo kama
si kuhusishwa basi mara kadhaa lilala katika
votuo vya polisi, akaona haina haja, akaamua
kuhamia porini kabisa huko Biharamulo. Daima
aliowaona huko ni majambazi tu kutoka nchi za
jirani.
Baada ya vita vya Rwanda na Burundi, wananchi
wengi walikuwa wakijimilikia silaha bila ya
mpango maalumu, na baadhi ya wanajeshi
kutoka nchi hizo walikimbili katika mpaka wa
Tanzania na kufanikiwa kupenya na kuingia na
silaha nzito za kivita. Polisi wa Tanzania ilikuwa
ni kazi kubwa sana kwao kuwakabili majahili
hao kwani walikuwa wamekwishachoka maisha.
Joru alikuwa akiwaona mara nyingi walivyokuwa
wakijificha huko maporini na kuteka magari
makubwa au yale ya abiria ilitegemea, walikuwa
hawana mzaha ukiwasogelea kwenye 18 zao
wanakumaliza, wao kuua ilikuwa ni kama
kukanyaga mende tu. Mwanzoni Joru alikuwa
akiogopa sana, hasa pale aliposhuhudia
wakimuua mmoja wao waliedai kuwa
amewasaliti na kuwachongea kwa polisi. Lakini
basi, Joru aliamini kuwa huo ndiyo ulimwengu
wao.
Wizi wa utekaji mabasi na malori ukashamili, na
hapo alipokuwa Joru kapafanya kama makazi
yake ndio haswa palikuwa njia yao ya kupitisha
mali kuzikimbizia porini, hapakuwa mbali na
barabarani ni kama kilomita moja hivi. Siku moja
walipokuwa wakipita hapo Joru alikuwa
kapumzika juu ya mti mkubwa ambao matawi
yake yalimfanya hasionekane na yeyote
anayepita chini. Siku hiyo ilikuwa tofauti kabisa,
wale majambazi walikuja wakaketi chini ya ule
mti wakivuta bangi zao na wengine kubwia
unga, vifaa vyao walikuwa wameviweka chini
mara akasikia mruzi toka mbali na wale jamaa
wakakurupuka na kuondoka eneo lile kwa kasi,
wakabeba vifaa vyao lakini walisahau pale chini
darubini, Joru alipohakikisha wameondoka,
akashuka mpaka chini na kuichukua ile darubini
kisha akapanda nayo tena juu ya mti. Mara
akaona polisi wakija pamoja na wanajeshi
wakikagua kila chaka wkapita mpaka pale alipo
alikuwa akiwa tazama tu, wakasaka huku na
kule lakini hawakuona mtu wakaondoka zao.
Mara nyingine tena, Joru alishuhudia wale jamaa
wakiteka malori na mabasi kwa wakati mmoja
wakiwavua nguo wasafiri na kuwapora kila kitu
mwisho wakawaacha wakiwa uchi wa mnyama.
Koru alikuwa akiumia sana juu ya jamaa hawa
na alikuwa akipata uchungu sana lakini alikuwa
hajui nini atafanya. Usiku wa siku hiyo alikuwa
ameshuka chini ya ule mti ili apate matunda
mwitu, alipokuwa ameketi chini usiku ule
akapitiwa na usingizi palepale. Na siku hiyo
ndiyo ilikuwa siku ya msakao mkali wa usiku
kwa usiku ndipo walipomkamata joru pamoja na
majambazi wengine na kuja nao mpaka
barabarani.

JORU AMEPAMBANA NA MAJANGA KATIKA
MAISHA YAKE... NINI HATIMA YA KISA HIKI?
 
nikiona neno tamati, ndo naanza kuisoma. sitaki kuwa mtumwa tena kama kule kwenye uchu
 
CHAPISHO LA 07

5… rejea JORU NA
MAJAMBAZI

Joru alipomaliza kumsimuliamkisa hicho
Captain Shibagenda, akaanza kulia. Shibagenda
akamtazama kwa jicho la huruma, akawauliza
wote majina yao, akagundua kuwa ni Joru peke
yake ambaye ni Mtanzania. Joru hakumkumbuka
mtu huyu lakini Shibagenda alimkubuka Joru
ndiyo maana akamuulia ‘Hata wewe jambazi?
Alijua ugumu wa maisha ya Joru, mara ya
kwanza alimuona Joru wakati alipokwenda na
kikosi kutoka Mtukula katika kijiji cha akina Joru
mara baada ya yel mauaji. Wakati Joru anarudi
kijijini asubuhi ile, wanajeshi hao walikuwa
wamejificha katika machaka ya migomba wakitaka kuona kama kuna mwanajeshi wa
Uganda atakayekuja hapo ili wamshughulikie
lakini alikuja Joru tena kwa kunyata na kwa
hadhari ya hali ya juu. Alipokuwa akisikiliza hiyo
simulizi kutoka kwa Joru akamkumbuka kijana
huyu na tukio lile.
Mara ya pili alimuona kijana huyu katika hospitali ya jeshi hapo Shibagenda aakiwa na
cheo cha Captain, alizungumza machache na Joru, akamtaka kumtafuta lakini Joru alipotea
katika mazingira ya kutatanisha. Sasa
wanakutana katika mazingira yasiyo rafiki hata
kidogo.Shubagenda akamtazama Joru, akamwita kwa ukali.
“Njoo hapa!”….
Joru akamsogelea mwanajeshi huyu kwa utulivu
sana, hakumtazama usoni kwa woga aliokuwa
nao maana alijua ukishaingia mikononi mwa
mjeshi basi ujue kinachofuata kama si kifo basi
ni kipigo cha mbwa mwizi. Joru alisimama
mbele ya kapteni Shibagenda.
“Nitazame usoni!” Shibagenda alimuamuru joru,
Joru akafanya hivyo, “Sasa nakuamuru uondoke,
ukimbie kutoka eneo hili bila kusimama wala
kugeuka nyuma, sawa?!”
“Sawa afande,” Joru akajibu kwa utii huku akiwa
anatetemeka. Shibagenda akamnong’oneza Joru,
“Kesho uje kambini na unione mimi,” Joru
akajibu kwa kutikisa kichwa na kisha akaanza
kutimua mbio. Joru alikimbia kama mtu
aliyepatwa na kichaa, hakutazama nyuma bali
alikimbia bila kusimama kimbio kama la saa
moja hivi.
Kitu kama radi kilipiga kwa nguvu, Joru aliusikia
ukelele huo wa nguvu na kuhisi vumbi likitimka
mbele yake,
“…..Kimbia mwanangu, kimbia bila kuchoka….”
Joru aliisikia sauti ya baba yake ikimwambia
kwa mwangwi mwingi uliotoka huku na huko.
Kila aliyemuona Joru katika mbio hizo alifikiri
kuwa nkijana huyu kwa vyovyote
kachanganyikiwa, walimtazama wakamuacha.
Joru akasimama katika duka moja dogo,
akatazama alikotoka, hakika ni mbali, alikuwa
akihema kama aliyekuwa anakimbizwa,
akainama na kufuta jasho, kisha akaliendea
bomba la karibu, kulikuwa na akinamama
waliokuwa wakichota maji, walipomuona Joru
akija hapo bombani walimpisha maana walimjua
kijana huyo mtukutu, Joru akanywa maji na
mengine akajimwagia kichwani kisha akapotelea
mitaani.

Baada ya mwaka mmoja…
JORU baada ya misukosuko mingi ya maisha
akipambana na hili na lile, alikumbuka kauli ya
Shibagenda kuwa amtafute, ingawa Joru
hakupenda kukutana na mtu huyu akijuwa kuwa
kwa vyovyote atakuwa kawekewa mtego wa
kukamtwa, alikaa akatafakari, “Kama
kunikamata si siku ile ile angenikamata, kwa nini
aliniachia?” alijisemea moyoni, akakta shauri
akaamua kwenda kuonana na mtu huyo ili ajue
kile alichokua akimuitia ni kipi, akaanza safari.
§§§§§

Joru alikuwa ameketi katika nyumba ya
Shibagenda, akifungua gazeti kurasa hii na ile,
akijaribu kusoma hapa na pale.
“Joru!” alistuliwa na sauti ya Shibagenda
aliyekuwa ndio kwanza ameingia nyumbani
kwake, akiiweka kofia yake juu ya meza. Alipewa
taarifa ya ugeni huo akiwa ofisini, Shibagenda
alikuwa mkuu wa kambi hiyo baada ya
kupandishwa cheo. Joru alimuona jinsi
alivyobadilika kwa kuchafuka kwa tepe za
kung’aa na vitu vingine visivyoeleweka.
“Ulikuwa wapi siku zote Joru, nilijua hutoweza
kuja kama ulivyofanya awali, hata hivyo ni
mwka sasa,” Shibagenda alimwambia Joru.
“Ni kweli, nimekuwa nikiogopa sana kukutana na
watu wanaofanya kazi za usalama nikihofia
kuwa nitakamatwa na wabaya wangu,” Joru
alieleza, kisha akamsimulia mabaya yote
ambayo kayafanya na watu wanamtafuta.
Shibagenda alisikitika sana lakini aliipenda hiyo
simulizi kwa kuwa aliona jinsi gani kijana huyu
alivyokuwa si mtu wa kukata tamaa na kuiacha
haki yake iende, mtu wa kutimiza alilolipanga
kwa njia yoyote. Shibagenda hakuwa na kitu cha
kufanya Na Joru kwa wakati huo lakini
hakupenda kumuacha kijana huyu aendelee
kuzagaa mitaani ilhali alimuaona akiwa tangu na
miaka kumi mpaka sasa mbaba wa kutosha.
Alifikiri kitu kisha akamtazama tena kijana huyu.
“Sikia Joru, nilikuwa nakutafuta sana, wewe
hunijui mimi ila mimi nakujua wewe,”
Shibagenda alianza kumueleza jinsi alivyomjua.
Simulizi hiyo ilimrudishia uchungu Joru, akaanza
kulia kiume bila kutoa machozi.
“Nikuulize swali Joru, unamjua aliyemuua baba
yako au unamkumbuka?” Shibagenda aliuliza.
“Anaitwa Malyamungu,” Joru akajibu mara moja,
jina hilo lilionesha wazi mshtuko wake.
Shibagenda alimkumbuka vizuri Mali ya Mungu,
alimkumbuka jinsi walivyopambana huko
Masaka wakati wa vita vya kumng’oa Nduli,
Mali ya Mungu alikuwa ndio kiongozi wa kikosi
cha mwisho kabla hujamfikia Idd Amin,
aliyeaminika na mtu huyo kwa asilimia zaidi ya
mia. Alikumbuka jinsi walivyopambana kwa
takribani dakika arobaini na tano, Mali ya Mungu
alionesha umahiri mkubwa sana wa kupanga
vijana wake katika pambano hilo ambalo
almanusura liwamalize Watanzania, lakini vijana
wa JW nao walikuwa ngangari, wakijua
wanachokifanya, waliweza kuwadhibiti lakini
Mali ya Mungu alitoroka na hakuonekana tena.
“Ni mtu hatari sana,” Shibagenda akasema.
“Lazima nimuue kama bado yuko hai,” Joru
alijikuta akiropoka.
Shibagenda alimtazama Joru kwa jicho kali, Hivi
huyu haelewi maana ya ‘mtu hatari’ ?
Shibagenda alijiwazie kisha akatikisa kichwa na
kujiweka vizuri kitini, akashusha pumzi na
kumwambia Joru, “Vipi, bado unataka kuishi
mtaani kufukuzana na polisi na kuwakimbia
wabaya wako?”
“Sina jinsi, sina maisha mengine, hapa nataka
kutafuta pesa kwa njia yoyote ile niende Uganda,
nina shida huko,” Joru alijibu. Shibagenda
alielewa kile anachokimaanisha Joru.
“Sawa, sasa kama upo tayari, mimi nina nyumba
kule Mtukula, shambani kwangu, kama unaweza
kuishi na kunitunzia nyumba ile, nitakuwa
nakulipa kila mwezi, ili ukae mbali na mji, utulize
akili na kupanga mipango yako mpaka
utakapoona upo tayari kwa jambo lingine,”
Shibagenda akamwambia Joru. Joru aliitika na
kukubali jambo hilo.
Jioni ya siku hiyo waliondoka na gari ya jeshi
kuelekea Mtukula, huko Joru alianza maisha
mapya, alikuwa akikaa kwenye nyumba kubwa
ya Shibagenda, pamoja nae alikuwa akiishi na
mke wa Shibagenda na watoto wake wawili.
Yeye alipewa nyumba ya uani yenye kila kitu,
kitanda, seti ya makochi, jiko na kadhalika wa
kadhalika. Joru hakuamini, alitazama nyumba
hiyo iliyoonekana haikukaliwa na watu kwa
kipindi kirefu, alijitupa kitini na kufungua redio
ndogo iliyokuwa hapo, imeunganishwa na
umeme. Akasikiliza kipindi cha michezo kupitia
RTD.
Siku ilofuata, Joru alikuwa akitembea tembea
kuangalia mandali ya shamba la Shibagenda
lililojaa Migomba iliyozaa vizuri na mazao
mengine, akifuatana na watoto wa Shibagenda
walioonekana kumpenda sana. Nyumba hiyo
haikujengwa mbali na kambi ya Mtukula, na
wala haikuwa mbali sana na mpaka wa Uganda
na Tanzania, Joru alijua Shibagenda kamsogeza
karibu na azma yake. Alihakikisha anaishi kwa
amani na familia hiyo, akiwatumikia kwa upendo
mkubwa, akfanya kazi mbalimbali za shambani
bila kinyongo, alijua kupanga ratiba zake za kazi
hivyo aliweza kupata nafasi ya kutembea hapa
na pale akitazama hili na lile.
Ni miaka mingi sana ilikuwa imepita tangu Joru
aondoke Mtukula baada ya vifo vya wazazi wake
na kuteketezwa kijiji chake, ilikuwa ni zaidi ya
miaka 15. Siku hii Joru alikuwa amekwenda
sokoni kununua hiki na kile. Maisha kwa ujumla
yalikuwa ya fuaraha hayakuwa yale ya hekaheka
tena, yale ya kulala juu ya miti tena, hapana,
haya yalikuwa ya utulivu, yalikuwa yale ya
kulala kwenye kitanda safi, ya kula chakula safi,
Joru alianza kubadilika, alianza kunawili, kwa
kuwa sasa alikuwa ametulia, Joru alikuwa
akifanya mazoezi kila siku asubuhi na jioni, ya
kukimbia, kunyanyua vitu vizito, baada ya Muda
Joru akawa katika hali nzuri, akawa na siha
bomba ya kiume, kila aliyemuona alimhofia.
Joru aliunga na kikundi cha Karate kilichopo
maeneo ya Mtukula sokoni, Shibagenda na
mkewe hawakuwa na kinyongo na hilo.
Mwaka ulipita Joru alikuwa na uwezo wa
kujilinda kimapambano, ijapokuwa hakuwa na
renki yoyote katika mchezo huo lakini alijikuta
anaweza japo kupambana na kibaka na
kumdhibiti kwa makofi kadhaa. Kutokana na
familia hii kumpenda sana Joru, hawakutaka
kabisa kijana huyu aondoke hapo, kila alipoaga
kuwa atarudi baada ya siku tatu, ilikuwa ngumu
kumuachia na wakati mwingine walikuwa
wakimuachia kwa shingo upande tu.
Mwishoni mwa juma Shibagenda alikuwa akija
kupumzika shambani kwake, siku hiyo alikuja na
kukutana na Joru wakawa katika mazungumzo
ya hapa na pale.
“Sasa kaka, mi naona muda umefika, uniruhusu
nikatafute maisha mahali pengine,” Joru
alimwambia Shibagenda.
“Yah, naelewa unachosema Joru, ni kweli sasa
unastahili hata kuwa na mke, lakini Joru,
unaonaje ukisubiri japo mwaka mmoja tu ili
nipate mtu wa kukaa hapa nawe nikuruhusu,”
Shibagenda alimwamba Joru, Joru hakukataa.
Mara nyingi aliombwa hivyo nye hakuwa na
kinyongo kwa maana hakuwa na shida ya pesa,
kama pesa alikuwa akipewa nyingi na
Shibagenda, mpaka hapo alikuwa na kitabu
katika benki ya posta, hivyo haikuwa tatizo.
Akaendelea kuishi hapo na kuendelea na
shughuli zake kama kawaida.
“….Maisha ni uvumilivu, mvumilivu hula mbivu,
usilazimishe tunda kuiva, subiri wakati wake,
likiiva litaanguka lenyewe, siku yako inakuja ….”
Ilikuwa ni kama sauti ya mtu iliyokuwa ikipita
masikioni mwa Joru alipokuwa amesinzia katika
kibaraza cha nyumba anayoishi.

6 rejea MTUKULA JESHINI
HILI ni jambo ambalo Joru hakulitegemea hata
kidogo, alibaki mdomo wazi hakujua ni nini
kinatukia mbele yake, kama ilivyo ada kuwa kila
aliyepata zawadi alilakiwa na ndugu zake na
kupewa zawadi mbalimbali, Joru alijua kuwa
akipokea zawadi hakutakuwa na yeyote kwake
wa kumpa zawadi. Alipopokea zawadi ya vyeti
vyake vilivyomstahili, machozi yalikuwa dhahiri,
shahiri katika macho yake, Shibagenda alilielewa
hilo alipokuwa akimtazama Joru na kumkabidhi
mgeni rasmi vyeti hivyo vinavyomstahili kijana
huyo, Joru alivipokea, akapeana mkono na
wakuu hao, akarudi nyuma hatua moja akapiga
mguu chini na kutoa saluti kisha akageuka kwa
ukakamavu alipokuwa akitoka eneo lile kurudi
katika mstari wake, alimuona mke wa
Shibagenda na watoto wake wawili wakija kasi
huku wakipiga vigelegele. Joru alitabasamu na
kuifungua mikono yake akawakumbatia watu
hao waliopendana sana, huko nje kila mtu
alikuwa akishangilia Joru! Joru! Joru! Joru!...
“…Usiseme kuwa katika dunia hii hauna ndugu,
ndugu ni wale wote uliowatendea mema, tenda
mema uende zako usingoje shukrani, kesho
utaona makandokando yake…”
Joru alikuwa akijiwazia moyoni, akiikumbatia
familia hiyo kwa furaha, akiwanyanyua wale
watoto wa Shibagenda kwa furaha, miruzi
ilitwala uwanja mzima.
Walipokuwa wakitoka pale uwanjani, Joru
alimuona binti mmoja aliyekuwa akipenyapenya
kwa shida kwenye kundi la watu, Joru
akamtazama, sura haikuwa ngeni sana. Binti
Yule alikuwa na motto katika bega lake,
alipopata nafasi akatembea kwa mwendo wa
haraka kumuwahi Joru kabla hajafika katika
mstari wake, Joru akasimama akimtazama, Joru
akavuta hatua kumuwendea msichana huyo,
vifijo na nderemo viliongezeka uwanjani. Yule
binti akamkumbatia Joru kwa nguvu huku akilia
machozi, Joru alimbembeleza, akamtazama Yule
motto pale begani, Yule mtoto akacheka,
alikuwa na meno manne tu kinywani mwake.
“Hii ndiyo zawadi yako, huyu ni mtoto wako….”
Yule binti akamwambia Joru, Joru alimtazama
kwa tuo.
“Nione mara baada ya shughuli hii,” akamjibu
kisha akawaacha na kurudi kwenye ule mstari.
Baada ya tukio hilo sherehe ile ilifikia tamati
awamu ya kwanza, sasa ilibaki ni burudani na
mazungumzo na marafiki, ndugu na jamaa.
Watu wote walimwagika uwanjani wakiserebuka
na muziki mzito uloiokuwa ukipigwa katka eneo
lililoandaliwa, kama unavyojua, ndugui, wazazi
na marafiki walikuwa mekuja na mpochopocho
mbalimbali ili kushereheka na wahitimu wao,
ndugu zao, watoto wao.
“Hongera sana Joru!” mke wa Shibagenda
alimpongeza huku wakipeana mikono, na watoto
wake wakafanya vivyo hivyo. Joru alikuwa na
furaha sana kwa kumaliza mafunzo yake. Akiwa
katika mazungumzo hayo mara askari mmoja
akamfuata.
“Joru, unaitwa ofisini,” aliambiwa. Joru
alishtushwa na wito huo, akaagana na mama
Shibagenda na kuelekea alikoitwa.

MWANMKE HUYO ANAYEMPA ZAWADI YA
MTOTO NI NANI?
JORU AMEITWA OFISINI, KUNA NINI?
 
CHAPISHO LA 08
Kilikuwa chumba nadhifu chenye samani za bei
mbaya, lakini zilizochongwa na vijana wa jeshi
wenyewe. Alikaribishwa na binti mmoja
aliyevalia nadhifu kabisa, Joru akapita ndani na
moja kwa moja akakutana na brigedia
Shibagenda.
“Karibu kiti Joru, karibu sana,” Joru
alikaribishwa na Shibagenda, akaketi kiti
kinachotazamana mara tu baada ya kupeana
mikono. Kabla Shibagenda hajaongea lolote,
Joru akaanza na yake.
“Kwanza samahni sana mkuu, nilitoka nyumbani
bila kuaga na kujiunga na jeshi katika mazingira
ya kutatanisha, wakati wewe ulipoondoka
nilipata fununu za ajira jeshini, nikajua wazi
nikimuaga mama naye atakushirikisha wewe
hivyo nilikuwa nafanya utaratibu mwenyewe
kimyakimya…
Rejea Mtukula kwa
Shibagenda

JORU akiwa bado anaishi kwa Shibagenda,
alipata tetesi za ajira za vijana kujiunga na
jeshi, alijaribu kuzifuatilia bila ya kumshirikisha
mtu. Kwake haikuwa tabu sana kwani wakati
huo bosi wake Shibagenda alikuwa amesafiri
kikazi kwenda nchi ya ng’ambo kwa miezi
miwili, Joru alifanikiwa zoezi la kujiandikisha jina
lake. Lakini wakati wa kukaguliwa vyeti vya
shule, Joru hakupata nafasi kwa kuwa elimu
yake ilikuwa ni ya shule ya msingi tena darasa
la nne ila tu alijua kusoma na kuandika vyema.
Joru alisikitika sana kuikosa nafasi hiyo, lakini
moyoni mwake hakukubali kushindwa.
“Sasa wewe hauna hata cheti kimoja, hapa
umekuja kufanya nini?” mmoja wa wakaguzi
alisema.
“Samahani afande, sikujua kama jeshio linahitaji
watu waliosoma, mi nilidhani upiganaji na
ufyatuaji risasi ni uwezo wa mtu yeyote, lakini
sina uhakika kama vyeti vinaweza kuonesha
umahiri wa mtu kuilinda nchi yake,” Joru alijibu.
Yule mkaguzi aliyekuwa na cheo cha luteni usu
alikasirishwa na majibu hayo, akamwita MP
amkamate Joru na kumpa adhabu kali. Ilikuwa
ni siku mbaya kwa Joru, alaitumbukizwa kwenye
bwawa la maji machafu na kuambiwa aogelee
kwa kupiga mbizi na kuibuka, baada ya adhabu
hiyo iliyochukua takribani dakika thelathini, Joru
akiwa ametota kwa tope na uchafu aliambiwa
akimbie uwanja wa gwaride huku akipigwa
bakora za nguvu. Kisha akaamuriwa kulala
chini, chali wakati wa jua kali mpaka wenzake
watakaporuhusiwa kuondoka, baada ya zoezi
lote kukamilika Joru alitakiwa kuondoka eneo lile
na asirudi tena. Joru akaondoka kwa unyonge
kurudi nyumbani, alifika na kulala, mama
Shibagenda alimletea chakula na kumuuliza
kilichomsibu, Joru hakumwambia kitu alijifanya
tu anaumwa.
Baada ya wiki moja, wale wote waliotakiwa
kurudi, walikuwa kama vijana hamsini hivi,
walifika tena pale kikosini kwa ajili ya awamu
nyingine ya usahili. Siku hiyo jopo la wakaguzi
liliongezeka, alikuwepo msaidizi wa mkuu wa
jeshi mkoa wa Kagera, daktari wa jeshi mkoa Dr
Janeth Ishengoma alikuwapo kwa ajili ya
kuhakikisha afya za walengwa hazina mgogoro.
Wakiwa tayari katika mstari maalum nje ya
hema lililoandaliwa tayari kwa ajili ya kazi hiyo,
Joru aliibukan tena siku hiyo, Joru hakukubali
kushindwa katika zoezi hilo alidhamilia tangu
moyoni, ‘kama kuniua waniue tu’, alikwenda
mpaka pale lakini hakujipanga kwenye ule
mstari, alisimama mbali kidogo.
Ilikuwa siku ya vipimo vya afya, MP mmoja
alipita eneo lile na kumuona Joru kasimama
pembeni akiwa kavalia fulana yake nyeusi na
jeans ya bluu ‘LEE’
“Wewe,” akaita Yule MP, akamtazama Joru juu
mapaka chini, “Mbona umekaa mbali na
wenzako, hutaki jeshi ee?” akauliza kwa ukali,
Joru akasimama akimkazia macho, “Nakuuliza
hutaki jeshi?” Joru aliona swali hili linalorudiwa
mara mbili lina maana sana kwake.
“Nataka afande,” akajibu.
“Haya kwenda kwa wenzako pale, simama
mstari ala!” Yule MP aling’aka. Joru akajiunga
katika mstari akawa nafasi ya mwisho. Moyoni
mwake aliwaza, waliochaguliwa ni mia moja vipi wakikata mstari mpaka mtu wa mia moja nayeye ni wa miamoja na moja? hakupata jibu,
‘liwalo na liwe’ akajipa moyo na kupiga moyo
konde. Mstari ule ukazidi kwenda, alipata moyo
pale alipoona siku hiyo hakuna maswali ya vyeti
wala elimu wala kuitwa majina. Joru alisimama
mbele ya meza yenye vifaa tiba lukuki kwa ajili
ya zoezi hilo.
“Kaa kitini,” muuguzi aliyekuwepo alimwambia
Joru, naye akaketi akiwa ana hofu yasije kutokea
yale ya wiki iliyopita, “Tulia mwanaume, mbona
una hofu sana, au hujiamini?” Yule muuguzi
akamuuliza. Akampima Joru kifua na presha
akaandika kwenye kijitabu chake, kisha akachukua sindano na kumtoa damu kwenye mshipa akaibandika kikadi Fulani kisha akamwuliza jina, akalizndika kwenye kile kijikadi na kitabu chake, akamruhusu aende kwa wengine. Hatua ya upimaji ikakamilika. Baada
ya hapo wakaja MP wane wakawachukua wale
vijana na kuwagawanya makundi manne ya
watu ishirini na tano kila moja, mchakamchaka ukaanza. Walitakiwa kukimbia mchakamchaka
wa kilomita sita kwenda na sita kurudi bila
kupumzika. Zoezi hilo kw Joru lilikuwa kama
kumpiga chura teke. Nyuma wakifuatwa na gari
moja ya jeshi, maalumu kwa kubeba wote
watakaozimia njiani. Wakiwa njiani kwenda huku
wakiimba nyimbo, vijana wengi walionesha udhaifu na kuanguka ovyo wengine wakilalamika vichomi, mmoja wa vijana hao aliyekuwa akikimbia sambaba na Joru alianza kujishika
mbavu na mara akapunguza mwendo akaanguka
chini akiwa hana uwezo hata wa kupumua, MP
akaamuru Joru na mwingine wambebe kumpeleka garini huku wenzao wakiendelea na
mchakamchaka. Walipofika kwenye ile gari na
kufunguwa mlango walimpakia kijana huyo
ndani kulikuwa na wengine wawili. Joru wakati
anatoka, alipita karibu na dirisha la mbele
upande wa kushoto wa gari hilo. Dr Janeth
Ishengoma alimuona Joru, akashtuka kidogo,
‘Huyu sio Joru?’ akajiuliza lakini akatulia akiendelea kumwangalia kijana huyu aliyekuwa akikimbia huku akiimba kila wimbo unaoanzishwa na MP hao.
§§§§§

Vijana kumi na mbili walionekana kushindwa
kabisa, walirudishwa na kufikia hoapitali ya jeshi
hapohapo Mtukula. Mistari mine iliyo sawa
ikapangwa mbele ya lile hema la kupimia afya
kwa ajili ya matangazo machache. Mara hii Joru
alimuona Dr Janeth katika ya wale wanajeshi
waliokuwa wakiongea pale mbele, alijisikia
vibaya kidogo kwa kuwa alikumbuka alipotoroka
nyumbani kwa daktari huyo. Baada ya matangazo hayo ya kutakiwa kurudi baada ya
siku saba tena kwa ajili ya majibu ya afya na
kujua nani kachaguliwa na nani la, Yule mkuu
wa jeshi msaidizi alimwita tena Joru mbele
yake, akiwa na waambata wengine wa jeshi.
“Hivi wewe kijana, siku ile si nilikufukuza, sasa
leo umekuja kufanya nini?” aliuliza.
“Nimekuja jeshini afande,” Joru alijibu bila
kuogopa maana alikwishajua kitakachofuata.
Yule mkuu akawaeleza wale wengine
alichomfanya kijana huyo wiki moja iliyopita na
leo karudi tena. Dr Janeth alisikitika sana kwa
adhabu aliyoisikia kuwa Joru alipewa na MP
siku hiyo.
“Mtazame huyu kijana mkuu, ana umbo la
mazoezi, amejengeka vyema, umempa adhabu
na leo kaja tena, unaonaje kama huyu akiwa
mwanajeshi wako jasiri atayekuwa mstari wa
mbele katika mapambano na adui, ana kiu na
nchi yake labda ndio maana karudi tena,
anahitaji, mpe nafasi akashindwe mwenyewe,”
Dr Janeth alizungumza. Joru alifarijika kwa
maneno hayo.
“Una wazazi wewe?” Yule mkuu aliuliza, lakini
alichokishuhudia ni uso wa Joru uliobadilika
ghafla.
“Sina wazazi,” akajibu.
“Sawa, kaa pale juani nitakuita, inaonekana una
kichaa wewe, sio bure,” Yule mkuu akamwambia
Joru kisha akaondoka na jopo lake. Dr. Janeth
alimtazama Joru kwa huruma akiwa anaketi
pale juani kisha akageuka na kuondoka kurudi
hemani, akapekua vipimo vyote na kupata vile
vya Joru, akacheki majibu yake ya awali alikuwa
amzima wa afya, hii ilimpa faraja kidogo lakini
kwa kuwa alijua kuwa kijana huyu hakufaulu
upande wa elimu, na alijua wazi utata wa mkuu
wake hivyo alishikwa na hofu juu ya hatima ya
Joru.Siku hiyo Joru alipewa adhabu nyingine ya
kuchimba mashimo ya takataka katika nyumba
za jeshi, mashimo mawili makubwa, Joru
aliifanya kazi hiyo na kuimaliza saa kumi nambili
jioni akiwa hoi kwelikweli. Joru aliendelea kuvumilia yote moyoni akiwa na moja tu kuingia jeshini. Baada ya kumaliza aliruhusiwa kuondoka
na hakuambiwa kitu chochote na afande aliyekuwa akimsimamia. Joru alitafakari hatima yake hakujua ni nini kinaendele, aliamua kutokata tama. Alirudi nyumbani akiwa hoi,akaoga na kulala, siku iliyofuata akaendelea na
kazi zake kama kawaida za hapo nyumbani kwa
Shibagenda.
Baada ya wiki moja, ilifika siku ya kwenda tena
jeshini, Joru hakujali kitu aliaga kwa mama
Shibagenda lakini hakumwambia anakwenda
wapi. Alifika pale na kuwakuta vijana wengine
wameshafika. Baada ya mudamfupi ikapigwa
filimbi na wote wakatakiwa kujipanga, mara
akaja Yule mkuu wa jeshi msaidizi na waambata
wengine wawili, siku hiyo Dr. Janeth hakuwepo,
wakaanza kuita majina ya wote waliofaulu,
vijana sabini na sita walipata nafasi, lakini
katika majina yote hayo jina la Joseph
Rutashobya halikuwapo. Joru aliumia sana na
hali hiyo, alimtazama Yule mkuu wa jeshi kwa
jicho bay asana lakini afanyeje, wakatakiwa
kuondoka lakini wale waliofaulu wakatakiwa
kuripoti siku ya tatu ili kambi ianze rasmi. Joru
akaondoka, hakutaka kuongea na yeyote jambo
lolote.
Siku ya tatu,Joru alikuja, mkononi akawa na
mfuko mdogo wa Rambo wenye surari moja ya
jeans na fulana moja pamoja na vitu vidogodogo
vya usafi wa mwili wake, alifika na kubaki nje ya
geti kwa muda akiangalia mazingira, baada ya
muda kidogo aliingia getini na kuripoti katika
kibanda alichokuwa ameketi mlinzi, akaambiwa
akae chini asubiri wengine. Ndani ya masaa
mawili vijana wote walikuwa wmefika, ilikuwa
tayari saa kumi jioni, jina la mmoja mmoja
likaanza kuitwa, kama kawaida Joru hakuwapo
kwenye orodha, Yule mlinzi akamwita.
“We mbona jina lako halipo?” akauliza Yule MP
“Sijui kwa nini, lakini mpaka jana lilikuwepo,”
Joru akajibu kwa kujiamini. Wale MP wakaongea
paembeni kisha mmoja akachukua ile orodha na
kuondoka nayo na kuwaacha vijana kwa Yule
Mp mmoja.
“Haya panga mistari mitatu hapa, weka na
mzigo wako kichwani” Mp akatoa amri, vijana
wakajibanga, kila mmoa alikuwa na mzigo wa
ukubwa wake, walitakiwa kujitwisha kichwani,
kama una sanduku haya, kama ni box haya. Joru
pekee alikuwa na kijimfuko hicho cha plastiki
akajitwisha kichwani, wakaanza kukimbizwa
jogging, Mp akipiga filimbi mnakwenda mbele
akipiga tena mnageuka na kurudi na mizigo yenu
kichwani.
Lilikuwa ni zoezi gumu la masaa mawili, baadae
waliongozwa mpaka mbele ya ofisi moja
iliyotengenezwa kwa mabati, wakapangwa pale
mbele mistari mitatu kila mmoja akiwa bado na
furushi lake kichwani, majina yakaanza kuitwa,
likiitwa askari mwingine anasikiliza sauti
ilipotokea anakurushia buti mpya, chombo cha
chakula ‘ Mess tin’ , unatakiwa uvidake bila
kuangusha mzigo wako kichwani, ukiangusha tu
adhabu kali. Watu wakaitwa, lakini hakuna
aliyefaulu kudaka bila kuangusha wote
wakaangusha mizigo yao na kusubiri adhabu.
Joru hakuamini aliposikia jina lake likiitwa la
mwisho, alitabasamu kiasi kwamba aliona kama
mbiongu zimefunguka, zikarushwa buti
akazidaka kwa kidole kwa kuinasa kamba
iliyoziunganisha huku mkono huohuo akikamata
mess tin iliyofika sekunde chache tu nyuma ya
buti hizo, mzigo wake haukuanguka.
“Safi sana, Joseph,” alitamka Mp mmoja kisha
akawageukia wale wengine, “Hivi ninyi mnafikiri
mnakuja nhapa pikniki, mabegi makubwa ya nini,
hakuna fashion show hapa, angalieni mwenzenu,
huyu ndiye mwanajeshi wa kweli, anajua
analofanya, tazameni alivyodaka hivyo vitu
hakuna kilichomuanguka, sasa yeye ataendelea
na utaratibu mwingine na nyie kwanza mnakwenda pond kuongea na watoto wqa
kambale, haya weka vitu vyenu hapo chini,”
akawaamrisha, wakavibwaga na wote kupelekwa
kwenye adhabu ya kuoga matope. Joru
alichukuliwa mpaka kwenye ofisi ya msajili,
akasajiliwa kwa mara ya mwisho kisha
akapewqa, nguo zake za mafunzo, begi la
kijeshi, kofia ya chuma na vitu vingine
akaoneshwa bweni, akaenda na kujichagulia
kitanda cha kona.
Joru alianza mafunzo makali ya jeshi na vijana
wengine kwa muda wa miezi tisa katika mvua
na jua, vumbi na umande, alionesha umahiri
mkubwa katika kila Nyanja, kutumia silaha,
shabaha, Joru alionesha umahiri mkubwa katika
kulenga shabaha, mpaka anamaliza kozi ile
hakuwahi kukosa hata risasi moja, katika
michezo ya mapigano, Joru alikuwa tayari ana
uwezo mkubwa tangu mitaani hivyo ilimchukua
muda mfupi tu kuweza kuwa juu ya wengine
katika hilo, alikuwa akicheza karate na kungfu
kama mtu aliyepatwa kichaa.

ITAENDELEA....
 
CHAPISHO LA 09
… rejea Mtukula
Jeshini

“Joru, umenidhihirishia msemo wa wahenga,
atafutaye hachoki na akichoka keshapata,”
Shibagenda alimwambia Joru huku akimpa mkono, “Hongera kwa kuhitimu mafunzo,nimeona umahiri wako wa hali ya juu, nimesikia
sifa zako mara tu nilipofika ijapokuwa sikujua ni
Joseph gani lakini leo ndiyo nimejua kuwa ni
wewe, wewe ni jasiri, mwanaume anatakiwa
kuwa hivyo kama ulivyo wewe, nilimwambia mke
wangu wiki moja iliyopita kuwa upo jeshini
alishangaa sana kwa sababu niliporudi
waliniambia umetoroka nyumbani hukuaga,
niliumia sana lakini sikuwa na la kufanya,”
Shibagenda aliongezea.
“Asante Mkuu, nilijua wazi usingeniruhusu kuja
jeshini ndio maana sikuaga mtu, samahani kwa
hilo,” Joru aliomba msamaha.
“Usijali Joru, wewe ni mwanangu, nakujua kuliko
wote hawa, sasa ile nyumba pale nyumbani ipo
kwa ajili yako, muda wowote, ukitaka kuja uje
pale, upumzike pale, hata kama utataka kuoa
basi muweke mke pale wakati wewe uko
kambini kwa sababu sheria unazijua, sivyo?”
Shibagenda akaendelea kuzungumza na Joru.
“Ndiyo mkuu, asante kwa moyo wako wa pekee,”
Joru alishukuru, akasimama na kupiga saluti
kisha akatoka nje na kuwakuta watu wakiendelea na sherehe, alipokuwa akitoka tu
mlangoni akakutana na Dr. Janeth Ishengoma.
“Hongera sana Joru, nimeona kazi, hakika jeshi
lilikuwa linahitaji mtu kama wewe, sina muda
wa kukaa hapa, nafikiri unanikumbuka, na
unakumbuka ninapoishi, Biharamulo kikosi
namba KJ 756Y, naoma uje, naenda kuandaa
zawadi yako nzuri sana, utaikuta pale, niambie
utakuja lini?” Dr Janeth alimpongeza na kuomba
miadi.
“Dr, kwa kuwa kuanzia kesho tutakuwa na mapumziko ya wiki mbili kabla ya kupangiwa
kazi na kikosi cha kwenda, nitakuja mwisho wa
juma hili,” alijibu.
“Karibu sana,” Dr janeth akamalizia na kumbania
jicho kisha akaingia kwenye jeep ya jeshi tayari
kwa safari. Joru akaja kuungana na familia ya
Shibagenda kwa chakula cha mchana
kilichoandaliwa na familia hiyo. Joru akawa
kama ameshtuka hivi, akaacha kwanza kula.
“Joru vipi?” aliuliza mke wa Shibagenda.
“Subiri, kuna kitu nimekumbuka,” akainuka na
kuondoka, Joru alipita hapa na pale katika
makundi ya watu, hakufanikiwa kumuona Yule
binti. Ikabidi aulize, kila mtu akamwambia
hajamuona. Joru akiwa amekata tama ya
kumuona akarudi alikowaacha Mama Shibagenda na watoto wake, wakaungana tena.
“Ulienda wapi?” mama Shibagenda akauliza.
“Nilikuwa namwangalia Yule msichana aliyenifata na motto, nahisi motto Yule ni
wangu, bila shaka,” Joru alimueleza mama
Shibagenda.
“Kumbe Joru ulikuwa Simba mwenda pole ee?”
mama Shibagenda alizungumza huku akitikisa
kichwa chake.
“Aaaa mama ni stori ndefu, siku tukitulia
nitakusimulia” Joru alieleza.
“Ok, basi uwe unauliza kwanza, yuko pale ndani
ya gari ananyonyesha motto, atakuja,” mama
Shibagenda alimwambia Joru. Joru akamtazama
na kucheka, akainua chupa ya sodana
kujimiminia. Japokuwa Joru alikuwa na wenyeji
wake hao bado pongezi nyingi zilikuwa
zikimiminika kutoka kwa kila aliyepita na
kumuona hapo. Dakika chache baadae Yule binti
akaja pale walipo, Joru akainuka na kuwahi
kumpokea mtoto, akambusu na kisha kumbeba
begani, akamkumbatia na Yule binti naye akambusu.
“Koku!” akaita, “Samahani kwa kila kitu, zilikuwa
ni silka za ujana na mambo yake,” Joru aliomba
msamaha kwa Koku kwa lile alilolifanya takribani
mwaka mmoja uliopita.
“Usijari Joru, nilikwishakusamehe muda mrefu
sana na kila siku nilikuwa naomba Mungu
nikutane nawe nikupe mtoto wako, mi
nimeshazaa inatosha,” Koku alijibu.
“Una maana gani unaposema hayo?” Joru
aliuliza.
“Mimi nimeshachumbiwa na mtu mwanaume
ninayempenda, hivyo siwezi kuwa nawe tena,
mchukue mwanao na mi nikaanze maisha
mapya,” Koku alijibu huku akiondoka. Joru
alimtazama Koku akiondoka na kumuwacha na
mtoto mikononi mwake, Joru akarudi na
kumkabidhi mama Shibagenda Yule mtoto.
“Vipi?” mama Shibagenda akauliza huku
akimpokea Yule mtoto.
“Ameniachia mtoto yeye ameondoka,” Joru
akajibu huku akiangusha machozi.
“Usijali mwanangu, tutamlea tu, atakuwa bila
tabu, nitatafuta binti atamwangalia mtoto,”
mama Shibagenda alimfariji Joru na kumtuliza.
Shughuli zote zilikamilka na watu
wakatawanyika. Mama Shibagenda akaondoka
na Yule mtoto, Joru akabaki kambini kwa siku
mbili zaidi kabla ya kurudi nyumbani.

7 … baada ya
siku mbili.

WAHITIMU wote wa mafunzo walipangiwa vituo
vyao vya kazi, walitakiwa kuripoti baada ya wiki
mbili za mapumziko. Haikuwa hivyo kwa Joru,
yeye hakupata taarifa yoyote ya kuripoti kazini.
Alibaki kama alivyo, ‘Labda nitabaki hapa hapa,’
alijiambia mwenyewe. Siku hiyo alikuwa
akifungafunga begi lake tayari kwa safari ya
kurudi nyumbani kwa Shibagenda, kichwa chake
kilikuwa kina mambop mengi kiasi yaliyokuwa
yanakinzana, mojawapo lilikuwa ni juu ya Yule
mtoto aliyeachiwa, jinsi gani ya kumlea, lakini
aliamini kuwa kama yeye alibaki bila mlezi tangu
umri wa miaka kumi mpaka siku hiyo basi vivyo
hivyo na mtoto huyo ataleleka. Joru alitoka nje
na begi lake mkononi, akakutana na MP mmoja
akija kwenye bweni lao.
“Joru, unatakiwa ofisini mara moja,” Yule MP
alimpa ujumbe kisha naye kuondoka zake, Joru
alielekea ofisini kama alivyoambiwa, aligonga na
kuingia katika ofisi hiyo nadhifu, ofisi ya mkuu
wa kikosi. Akasimama imara na begi lake
mgongoni akapiga mguu chini na kutoa heshima
ya kiaskari.
Yule mkuu naye akajibu.
“Nimeitika wito mkuu,” Joru aliongea huku akiwa
kasimama kikakamavu, kiaskari kwelikweli.
“Joseph Rutashobya, najua umejiuliza kwa nini
hujapangiwa kituo kama wengine, usijali, kwanza
kabisa jeshi limekutazama kwa jicho la pekee
sana, kama askari mkakamavu, mpiganaji,
mvumilivu asiyekubali kuishindwa, hivyo
umependekezwa kuendelea na mafunzo zaidi.
Hapa tunavyoongea unatakiwa kuondoka leo hii
kuelekea Chukwani, Zanzibar kwa mafunzo
mengine ya miezi sita katika medani za kivita
katika ngazi kubwa zaidi. Huna muda wa
kupumzika wala huna wa kumuaga, nimemaliza,
unaweza kwenda,” Yule mkuu wa jeshi alimaliza.
Joru alirudi nyuma hatua moja na kuptoa
heshima ileile akageuka na kutoka nje, pale
akakutana na askari mwingine.
“Samahani we ndio Joseph Rutashobya?”
akauliza.
“Ndio afande,” Joru akajibu.
“Ingia kwenye gari tuondoke haraka,
tumechelewa,” akaambiwa. Ukiwa jeshini hakuna
lele mama lazima kuwa tayari muda waote. Joru
akakwea gari na ile gari ikaondoka katika kikosi
cha Mtukula.
Ndani ya masaa mawili Joru alikuwa katika
dege la jeshi Buffalo akielekea Dar es salaam.
Ilikuwa ni mara ya kwanza Joru kupanda ndege,
mara ya kwanza Joru kutoka nje ya mkoa wa
Kagera, kwake ilikuwa kama anayeota ndoto,
lakini hili hakika ndilo alilokuwa akilitaka siku
zote.
Joru alikuwa mwanajeshi, mwanajeshi
aliyeonekana kati ya wote aliokuwa nao,
waliochaguliwa kwa vyeti vyao, lakini yeye
ukakamavu na uvumilivu wake ulimpeleka mbele
zaidi.
§§§§

Nyumbani kwa Shibagenda walipigiwa simu tu
kuwa Joru hatorudi nyumban mpka baada ya
miezi sita, mama Shibagenda alisikitika sana
ukizingatia alikuwa ameandaa chakula kizuri
kwa ajili ya kijana wao waliyempenda sana,
Joru.
Maisha yaliendelea, mama Shibagenda alipata
msichana wa kumlea Yule mtoto, hakuwa
msichana mdogo bali mwanamke mwenye umri
kama miaka 28 na 32 hivi lakini alikuwa bado
kuolewa, walikutana sokoni ndipo alipoongea
nae baada ya kutambulishwa na mwanamama
mwingine.
Msichana Yule alijitambulisha kwa jina la
Kemilembe, na moja kwamoja alikuja kuishi kwa
mama Shibagenda, naye alipotambulishwa
mtoto jina lake Joseph Rutashobya, moyo wake
ulipaa kwa mshtuko, akamkumbuka Joseph
wake waliepoteana zaidi ya miaka ishirini ilopita.
Kemi alimlea kwa upendo mkubwa sana mtoto
Yule, kwani alikuwa akimkumbusha mbali sana.
Kemilembe wakati yakitokea yale mauaji pale
kijijini kwao, yeye na wazazi wake walitoroka
usiku ule ule na kwenda kijiji kingine, hilo ndilo
liliwaweka hai. Daima alimkumbuka rafiki yake
Joseph waliekuwa wakienda pamoja shuleni,
wakicheza njiani, wakiwekeana ahadi mbalimbali
za maisha ya baadae, lakini mawazo hayo yote
alijaribu kuyafukuza na kusema ‘ulikuwa utoto,’
Siku zikapita, miezi ikayoyoma, Kemilembe
akawa mlezi mzuri sana kwa mtoto Joseph,
mtoto huyo akakua kwa kimo na akili, akajifunza
kutembea, akajifunza kuita ‘mama’ akimwita
Kemilembe kwa jina hilo, naye Kemi alikuwa
akiitika na kufurahia kuitwa hivyo, kwani ni
Baraka ya pekee ambayo wengine wachache
hawaipendi ndio maana hutupa watoto,
wakisahau kuwa hilo ni tendo la dhambi, tena
dhambi kubwa.
§§§§

…. Miezi sita
Baadaye

Joseph Rutashobya ‘Joru’, alimaliza awamu ya
kwanza ya kozi ngumu kuliko maelezo.
Walikwenda vijana sitini lakini waliomaliza
salama walikuwa arobaini na tano, watano kati
yao walipoteza maisha, wengine waliishia njiani
kwa sababu mbalimbali, lakini bado Joru
alionekana kuwa mahiri katika mafunzo hayo, ya
kuruka kwa miamvuli na kutua katikati ya
bahari, kuogelea umbali mrefu na kukaa ndani
ya maji kwa muda mrefu ikiwa ni mbinu ya
kujikinga na maadui inapobidi.
Joru alisifiwa na kila mkufunzi hasa wale
waliotoka nje ya nchi kama Urusi na Umarekani,
walimpenda kijana huyo na wenzake wawili
ambao walionekana pia kuwa mahiri kwa namna
Fulani. Baada ya miezi hiyo sita, walitakiwa
kurudi mapumziko ili wasubiri taarifa nyingine
kutoka kambini. Joru na wenzake walirudi
mpaka Dar es salaam na kufikishwa moja kwa
moja katika kambi ya Makongo (Lugalo
Barracks).
Baada ya siku nyingine tatu Joru alipata ruhusa
ya kwenda kusalimia kwao Mtukula. Aliamua
kwenda bila kutoa taarifa kwa mtu yeyote, kesho
yake tu tayari alikuwa Kagera kwani alifanikiwa
kupata ndege ya jeshi inayokwenda huko. Jioni
ya siku ya tano alikuwa akielekea Mtukula,
nyumbani kwa jenerali Shibagenda, maana huko
ndiko kumekuwa nyumbani kwake sasa.

NINI KITAENDELEA?
 
CHAPISHO LA 10
HODI iliyogongwa katika mlango wa mbele wa
nyumba ya Shibagenda iliwagutusha wote
waliokuwa sebuleni wakiangalia TV, aliyetoka
kwenda kufungua mlango alikuwa ni mama
Shibagenda mwenyewe, hakuamini anchokiona
mbele yake, hakuamini kama Joru ndiye
aliyesimama mbele yake, alimkumbatia kwa
bashasha, akampokea begi lake na kumkaribisha
ndani, watoto wa shibagenda waliokuwa hapo
sebuleni nao walikuwa na furaha ya ajabu
kumkaribisha kaka yao waliyemzoea kwa miaka
mingi, walimkaribisha sebuleni, naye akaketi
kitini.
“Mwanangu yuko wapi?” lilikuwa swali la
kwanza kuuliza.
“Aaaa jamani Joru hata hujapumzika?” Mama
Shibagenda akajibu.
“Hapana, yeye ndiye hasa nilikuwa namfikiria
katika safari yangu yote,” Joru akajibu. Mama
shibagenda akamwita Kemi kwa sauti ili aje
kumleta mtoto amsalimie baba yake. Joru akiwa
anafungua kamba za buti zake alihisi nywele
zikimsisimka akatazama chini akaona kuna mtu
aliyesimama, akamtazama, mtoto wa kiume.
“Waoh!” Joru akamnyanyua, “Sikujua hata kama
ni wa kiume au wa kike, sasa mnamwita nani?”
akauliza.
“Joseph Rutashobya, junior,” mmoja wa watoto
wa Shibagenda akajibu. Mara Joru akainua
macho kumtazama dada anayemlea mwanawe,
lo! Akagongana macho na Kemilembe,
Kemilembe yuleyule aliyekluwa akishikana nae
mikono kwenda na kurudi shule, Joru alibaki
kama aliyenaswa kwa umeme. Walibaki
wakitazamana, nyumba yote ikawa kimya, Kemi
akamkumbatia Joru kwa nguvu, Joru
akaonekana kufurahi bila kuficha.
“Kwani nyi mnafahamiana?” mama Shibagenda
akauliza.
“Mama, sisi tumetoka mbali sana, mimi nilijua
Kemi inawezekana hata alishakufa, maana
nilipoondoka pale kijijini miaka ile ndipo
sikumwona tena!,” Joru alimwambia mama
Shibagenda, alirudisha kumbukumbu yake mbali
sana, Kemilembe aliangusha machozi kwa
maana hakutegemea kabisa kama angemuona
tena mwanaume huyo aliyeahidiana nnaye kuishi
kama wazazi wao wakiishi, sasa wamekutana
tena katika umri wa utu uzima.
“Kemi, ulikuwa wapi siku zote hizi?” Joru
alimuuliza Kemi, Kemi akamtazama Joru, jicho
lake lilizungumza lugha iliyojificha ‘nakupenda
Joru’ . Joru alimtazama mwanawe kisha
akamtazama Kemi, hakika katika siku zote hizo
Joru aliishia kulia tu kila alipomuwaza Kemi.
§§§§§

rejea 1977
≈
Kijijini kwa kina JORU
na KEMI
USIKU HUO wa uvamizi, Kemi alikuwa amelala
ndani ya nyumba yao, akiwa hana hili wala lile,
ndoto tamu za maisha zilikuwa zimeugubika
usingizi huo ambao siku hiyo haukuwa na
mang’amung’amu bali ulikuwa ni usingizi mzito,
Kemi alilala fofofo.
Ngurumo za magari ziliposikika, wazazi wa Kemi
hasa baba yake , alishtuka kutoka usingizini,
aksikiliza mlio huo, akahisi ukija upande huo,
baba wa Kemi akamuamsha mkewe,
akamwambia asikilize gari hilo, mlio ulizidi
kuongezeka.
“Baba Kemi, hapa sio pa kukaa tena,” Mama
Kemi akamwambia mumewe.
“Umeona ee?” Baba wa Kemi akajibu, akavuta
kapazia na kuchungulia nje, akaona mwanga wa
magari hayo ukisogea pale kijijini.
“Muamshe Kemi, muamshe haraka!” Baba Kemi
alimwambia mkewe. Mama Kemi hakusubiri hata
kauli ya mumewe ifike mwisho, tayari alikuwa
katoka chumbani na kumuendea binti yake.
“Kemi, Kemi, Kemi,” alimuamsha kwa kumtikisa,
Kemi ndio kwanza alijigeuza upande wa pili.
Ilikuwa taabu kidogo kumuamsha Kemi,
hakukuwa na jinsi alimtikisa kwa nguvu na
kufanikiwa kumuasha.
“Mama nini jamani, mbona hakujakucha?” Kemi
aliongea kwa sauti ya uchovu uliojaa usingizi,
mama yake akamnawisha maji usoni, fahamu
zikamjia sawasawa.
“Wamekuja kutuvamia watatuua, tuondoke”
mama yake alimwambia huku akimvuta mkono
binti yake na kumtoa chumbani, kisha
wakasubiri kwenye kikorido. Baba wa kemi
akatangulia mlango wa kutokea nyuma akiwa na
kurunzi yake mkononi, akausukuma taratibu na
kutazama nje huku na kule, ni mbala mwezi tu
iliyokuwa iking’aa kila upande, akamvuta
mwanawe na mkewe na kuvuka upenuni mwa ua
wa nyumba yake, hakujali hata kama alikuwa
akisikia sauti za wavamizi ambao tayari
walikuwa wameshuka katika magari yao na
kuanza vurugu zao. Kemi na wazazi wake
walifanikiwa kujificha katika mapori ya migomba
na kupiga jicho kinachoendelea, walishuhudia
watu hao wakifungua mazizi ya mifugo yao na
kuiswaga kwenda garini. Baba wa Kemi aliumia
sana kwa hilo mara kadhaa alishikwa na hasira
akataka kujitokeza kwenda kupambana na watu
hao, lakini mkewe alimkataza, akimuhasa kuwa
atauawa ni bora aache. Mara kelele za akina
mama na watoto zikawa zinasikika.
“Mama Joru yuko wapi?” Kemi akauliza.
“Joru yuko kwao!” mama yake alimjibu kwa
kifupi tu.
“Mama nendeni mkamchukue Joru, masikini
watampiga,” Kemi akaanza kulia kwa uchungu.
Alikuwa ni binti mdogo wa miaka kumi tu, lakini
mapenzi aliyoyaonesha kwa mtoto mwenzie,
Joseph Rutashobya, yalikuwa ni mapenzi
mazito. Mama yake akambembeleza
akimwambia kuwa Joru ni mtundu kwa vyovyote
atafanikiwa kutoroka. Kemi alitulia, akiamini
kabisa yote aliyoambiwa na mama yake yana
ukweli mwingi. Mara wakaanza kusikia milio ya
risasi ikitokea upande wa pili na kelele za watu
zikisikika. Baba wa Kemi akamshika mwanae na
mkewe akaanza kuwavutia maporini ili
wasionekane, akawapeleka umbali kidogo na
kuwaficha kwenye vichaka, kisha yeye akarudi
kushuhudia nini kinaendelea, ndipo alipokuwata
nyumba yake ikiteketea kwa moto, vilio vya huku
na kule, akashuhudia wavamizi haop wakiwapiga
wananchi na wengine wakibaka wanawake.
Aliumia sana lakini hakuwa na la kufanya,
akaamua kuondoka na kwenda alikoiachafamilia
yake, akawachukua na kupotelea msituni.
Baada ya siku mbili tangu yale yatokee, mzee
Yule alirudi kutazama hali ya kijiji kile, alilia
sana, hakukuwa na nyumba iliyobaki, majivu
yalitapakaa kila mahali, aliwaona kwa mbali
vijana wa JW waliokuwa wakihifadhi miili ya
marehemu huku eneo lile limefungwa utepe
maalumu wa kuzuia kuingia. Baba wa Kemi
akageuza alikotoka, akatembea hatua chache na
kusimama akageuka na kuangalia kijiji chao
walichokipenda, hakujua nani na nani waliokufa
katika sakata hilo wala hakujua nani na nani
waliopona, akaendelea na safari yake.
Siku zilikwenda na wiki zikapita, Kemi alitamani
sana kumuona Joru lakini haikuwa hivyo, kila
siku alikuwa akiomba kumuona Joru lakini wapi.
Kutokana na umbali wa makao mapya, Kemi
alianza shule nyingine na kuendelea na masomo
yake, hakuwa na raha kila alipokuwa akienda
shuleni. Wakati vita ya Tanzania na Uganda
ilipopamba moto miaka ya 1978 mpaka 1979
Kemi alitamani siku hizo angemuona Joru. Kwa
kuwa alijua wazi Joru alikuwa hampendi kabisa
Idd Amin tangu wakiwa shuleni, na marakadhaa
alipokuwa akiwaona wanajeshi siku zile wakiwa
mazoezini Joru alikuwa akishangilia sana.
Hakukuwa na jinsi, wazazi ilibidi wamuelekeze
Kemi kuwa Joru atakuwa amekufa katika siku ile
ya uvamizi, Kemi alilia sana kwa habari hiyo,
alimlilia sana Joru lakini kwake ilikuwa ngumu
kuamini, yeye kwa umri wake alijuwa wazi kuwa
wanaokufa daima ni wakubwa tu na si watoto.
Mwaka 1984, baba wa Kemi akafariki baada ya
kuumwa sana, alifariki kwa maradhi ya UKIMWI;
Kemi akabaki na mama yake tu, ijapokuwa
maisha yalikuwa ya tabu kidogo lakini waliweza
kusonga mbele. Bado moyoni mwa Kemi aliamini
kabisa kuwa ipo siku Joru ataonekana mbele ya
macho yake. Kemi akawa msichana mkubwa na
mrembo sana, kila mwanaume alimtamani
msichana huyo kwa jinsi alivyoumbika, sura,
rangi, umbile, vyote vilimfanya Kemi kuonekana
msichana mrembo pote kijijini. Wazee wenye
watoto wa kiume walio tayari kuoa walikuja
kuongea na mama Kemi na ndugu wengine wa
familia hiyo ili kumposa binti huyo kwa vijana
wao, lakini kila ilipoamuriwa hivyo, Kemi
alitoroka nyumbani. Aliapa kuwa penzi lake si
kwa mwanaume mwingine ila Joru tu, awe hai
au amekufa, Kemi alijiwekea hilo moyoni na
alishawahi kumweleza mama yake kuwa yeye
alipenda kuolewa na Joru pekee, hivyo atabaki
kuwa hivyohivyo mpaka mwisho wa maisha
wake, hakika Kemi alijitunza na akatunza kila
alichonacho kama nadhiri yake ilivyokuwa. Kemi
alifanikiwa kufika kidato cha nne, lakini hapo
hakuweza kuendelea kutokana na hali ya afya ya
mama yake. Mama yake alikuwa akiumwa sana,
alikonda sana na hakukaa muda mrefu alifariki
mikononi mwa Kemi mwaka 1987. Baada ya
msiba huo kumalizika, Kemi hakuona haja ya
kuishi kwa ndugu yeyote, aliamua kuchukua
maisha yake mikononi mwake, akaondoka kijijini
hapo na kuhamia mjini ambako hakuwa na
ndugu yoyote, akatafuta kazi akapata kwenye
familia ya kiarabu iliokuwa ikiishi Bukoba mjini,
mji ambao Joru alishafanya fujo zake na
kuondoka miaka kenda nyuma na kutorokea
mahali pengine.
Kemi alifanya kazi na vibarua mbalimbali kwa
miaka kadhaa mpaka alipoamua kurudi tena
Mtukula, huko akawa akiishi kwa mama Fulani
na kumsaidia kuuza mboga katika soko la
Mtukula. Maish aliyokuwa akiishi yalikuwa ya
taabu sana, wakati mwingine alikuwa akishinda
bila kula, lakini kwake haikuwa na jinsi angeenda
wapi, uzuri Kemi ulichujuka sana kutokana na
lishe duni ya hapo alipokuwa akiishi, mama
aliyekuwa akiishi nae alikuwa hamjali, alipenda
amfanyie kazi tu, maana tangu ampate Kemi
alikuwa na soko kubwa sana la mboga zake
kwani watu wengi walipenda kununua mboga
kwa Kemi kutokana na lugha safi kwa wateja
wake. Hata mama Shibagenda daima alikuwa
akiishia kwa binti huyo kununua mboga.
Baada ya miaka kadhaa
kupita
§§§§§

Nyumba aliyokuwa akiishi Kemi, kwa mama
mboga kulikuwa na kijana wa kiume aliyekuwa
akimpenda sana Kemi, kila mara alimtongoza,
alimshawishi kufanya naye mapenzi lakini Kemi
alikuwa mgumu haswa. Yule kijana hakukata
tama kwa maana alikuwa akienda mtaani vijana
wenzie wakimcheka kwa kuwa alikuwa na
msichana ndani na alishindwa kufanya chochote,
hii ilimtia hasira sana, siku moja akapania
kumbaka Kemi ikiwa atakataa kumtimizia haja
yake.
Ilikuwa purukushani usiku huo katika chumba
cha Kemi, Kemi hakukubali kijana huyo amfanyie
hilo atakalo, katika vuta nikuvute hiyo Kemi
alimgonga kichwani kijana huyo kwa kutumia
mfuniko wa chungu, Yule kijana akaanguka na
kupoteza fahamu, kisha Kemi akaona hapo sio
pa kukaa tena, alitoka nje usiku huo na
kutoroka. Usiku huo mama mboga alikuwa
akisika fujo zote hizo lakini hakufanya lolote
kwani kijana wake alishamwambia kuwa yeye
lazima ampate Kemi hata kwa kumbaka na
mama yaek alimruhusu kufanya hivyo kwa binti
huyo yatima. Lakini baada ya kama dakika kumi
na tano alisikia kitu kikianguka na ukimya
ukatawala isipokuwa mlango wan je
uliofunguliwa na kufungwa. Wasiwasi ukamjaa
mama mboga ikabidi aende kutazama akijua
labda tayari shughuli inaendelea, chakushangaza
hakusikia hata miguno ya mahaba ambayo
alikuwa akiisubiri kwa hamu. Lo, kusukuma
mlango tu anakutana na mwili wa mwanae
ukiwa chini uchi wa mnyama, hakujua kama
kazimia au kapoteza maisha, akaanza kulia kwa
sauti na kuita majirani.
Dakika tano tu zilitosha majirani kujaa, balozo
wa nyumba kumi akafika na kuona hali hiyo,
wakaita polisi wakatazama na kuandika ripoti
zao, kijana alikuwa amekufa kwa kuwa
amechelewa kupata huduma ya haraka.
RB ikatolewa, Kemi atafutwe popote alipo ili
sheria ichukue mkondo wake. Mkono wa dola ni
mrefu, Kemi alikamatwa baada ya siku tatu,
akarudishwa Mtukula, kesi yake ikaunguruma na
kuwavuta karibu watu wengi wa Mtukula, Kemi
alipata mashahidi wengi sana kumtetea. Baada
ya miezi miwili jaji aliyekuwa akiendesha kesi
hiyo akaridhika na ushahidi uliotolewa, maana
ilionekana wazi kuwa marehemu amefia katioka
chumba cha binti tena akiwa mtupu, usiku wa
manane, kelele za fujo hiyo kwa vyovyote
ingemuamsha mama mboga lakini kwa nini
hakuamka, ilikuwa njama. Hukumu ikatolewa
Kemi akafungwa miaka miwili kwa kosa la kuua
bila kukusudia, japokuwa alifungwa lakini
wanakijiji waliona ni heri miaka hiyo miwili
kuliko kufungwa maisha. Msamaha wa Rais
ulipotoka, Kemi akaangukukiwa na bahati hiyo
akatoka gerezani baada ya kukaa miezi sita tu.
Kemi akarudi na kuanza maisha mapya kabisa,
bado moyoni mwake alikuwa akiomba japo hata
kwa ndoto Joru aje atoe usichana wake kwanza
hapo labda angemfikiria mwanaume mwingine,
daima alishinda akilia, hakupenda
kuchangamana na watu.
Siku moja katika usingizi wake akamuota Joru,
akaota kuwa kakutana na Joru sokoni, na
kupeana ahadi zao zilezile za tangu utoto,
‘ tutaishi kama baba na mama wanavyoishi’ .
Aliamka mwenye furaha sana, alipojiswafi
asubuhi hiyo aliamini kabisa kuwa atakutana na
Joru sokoni, aliokwenda sokoni asubuhi na
kushinda huko akizungukazunguka mara
akiongea na huyu mara na yule, kila aliyemjua
binti huyo mwenye huzuni siku hiyo alishangaa
kumuona akiwa na furaha ya ajabu. Saa
zilikwenda lakini Kemi hakumuona Joru, ilikuwa
ni ndoto tu, ndipo alipotoka na kuketi pembeni
mwa soko hilo karibu kabisa na barabara. Mara
akasikia sauti ikimwita, akageuyka na kumuona
mwanamke aliyemzoea, mama Shibagenda,
wakafanya mazungumzo mawili matatu,
akamchukua na kuja naye nyumbani ili amsaidie
kulea mtoto wa Joru. Kemi alipigwa na butwaa
aliposikia kuwa mtoto huyo anaitwa Joseph
Rutashobya, alimlea kwa upendo mkubwa akilala
nae kitanda kimoja kana kwamba ni mtoto wa
kuzaa mwenyewe.

JOSEPH RUTASHOBYA (JORU) ANAKUTANA NA
MSICHANA WA UTOTO WAKE (KEMI)...
MZPENZI YANACHUKUA NAFASI YAKE....
NINI KITAENDELEA KATI YA WAWILI HAWA?
 
CHAPISHO LA 11
§§§§§

Rejea JORU na KEMI
JORU alimkumbati Kemi kwa nguvu, wote wawili
waliangusha machozi. Mama Shibagenda alibaki
kuwaangalia vijana hao. Wakati wakiwa katika
kukumbatiana huko Kemi alihisi mwili
ukimtekenya sana, alihisi raha ya ajabu, alizidi
kumkumbatia Joru. Baada ya dakika kama tano
za kumatiano hilo, Joru alimuachia Kemi,
akamfuata machozi.
“Ina maana ninyi mnafahamiana?” Mama
Shibagenda akauliza.
“Mama tunafahamiana tangu utoto wetui,
tumelelewa kijiji kimoja na tulikuwa marafiki wa
kweli, sikutegemea kama mrembo wangu yuko
hai,” Joru akaeleza, ndipo mama Shibagenda
alipopata kujua mkasa mzima wa Joru na Kemi
kila mtu kwa upande wake.
“Poleni, sana sasa mmeamini kuwa milima
haikutani ee? Haya basi Joru, kama kawaida
nyumba yako ipo daima inakusubiri,
ukajipumzishe kidogo,” mama Shibagenda
akamwambia Joru, kisha akamgeukia Kemi
aliyekua akionekana na aibu kidogo, “Nani, Kemi!
Mchukulie mzigo umuongoze, usijali ni siku
nyingi hamjaonana basi mkaongee vizuri na
kusalimiana, kazi za huku mi nitafanya tu,”
alimaliza mama Shibagenda, Kemi akamchukua
begi la Joru na kuelekea kule kunako nyumba ya
uani, wakimuacha mtoto akirudishwa kulala.
Kama kuna kitu ambacho Kemi alikuwa
akikifikiria kitafika lini na vipi ni hicho, tangu
avunje ungo hakuwahi kukutana na mwanaume.
Upendo wake wa kweli kwa Joru ulimfanya Kemi
kuuhifadhi usichana wake mpaka huyo
aliyetamani kumpa afike, ijapokuwa alikuwa
hajui kama yupo hai au amekwishakufa, lakini
upendo wa kweli ulimwongoza katika hili. Kemi
alikuwa mtu wa kuweka ahadi bila kuvunja,
alimpenda Joru, alimpaenda sana, siku zote
alikuwa akimfikiria kijana huyo, haja yake hata
kama asipoolewa na Joru lakini Joru awe wa
kwanza kufungua njia hiyo inayotamaniwa na
wengi.
Walifika kwenye nyumba ambayo Joru alikuwa
akiitumia tangu kwanza, akakuta kila kitu kipo
kama kilivyo.
“Hapa ndio kwako?” akauliza Kemi.
“Ndiyo, nyumba hii nilikabidhiwa na baba
mwenye nyumba, mzee Shibagenda, niishi muda
wote wa maisha yangu, wamekuwa kama
wazazi kwangu, wamenipenda kwa upendo wote.
Kemi nalikutafuta sana katika nafsi na moyo
wangu nisikuone, hakika nilijuwa kuwa labda
umekufa miaka ile ya mauaji yaliyotokea pale
kijijini,” Joru alimjibu Kemi na kuongezea na
mazungumzo mengine. Kemi akatua begi chini,
akamtazama kijana Yule aliyekuwa ndani ya
sare nadhifu ya jeshi, aliyejaa katika umbo la
kiuwanaume haswa, kemi akainamisha uso wake
hakupenda kumwangalia usoni.
“Joru siamini kama ni wewe, siamini kabisa,
sikujua kama mtoto Yule ni wako, lakini jina lake
lilinifanya nimpende kama mwanangu, kwangu
nilimuona kama mume, hata nilipolala naye
kitandani nilihisi niko na Joru wangu, nakupenda
sana Joru,” Kemi alimweleza Joru kisha machozi
yakafuata na kutiririka juu ya mashavu yake
meusi, yanayopendeza kwa rangi hiyo
aliyojaliwa na Mungu, akamtazama Joru usoni,
huku akiwa amejawa na uchungu, “Joru,
nimekutunzia usichana wangu mpaka sasa
ingawaje sikujua kama upo hai au umekufa,
niliapa sintompa mwanaume yoyote penzi langu
isipokuwa wewe, nilitaka kubkwa lakini
nikapigania mwili wangu mpaka nikajinasua
mikononi mwa nunda, ijapokuwa nilimuua bila
kukusudia na kufungwa jela miaka miwili, bado
nilikukumbuka Joru, sasa moyo wangu unauma
sana kuona kuwa mtoto Yule ni wako, najua
huwezi kupata mtoto bila mwanamke, ijapokuwa
hautakuwa tayari kunioa lakini kabla sijampa
penzi mwanaume mwingine nilitaka wewe uwe
wa kwanza, wewe uondoe kizinda cha uke
wangu, niko tayari hata kama umepata ugonjwa
huko ulikopita,” Kemi akaangusha chozi.
Joru akamsika mbega na kumvutia kwake,
akamkumbatia katika kifua chake kipana,
akamsaidia kulia kwa sekunde kadhaa, kisha
akamtoa, mikono yake ikiwa katika mabega ya
Kemi alimtazama usoni.
“Kemilembe, daima umekuwa ndani ya moyo
wangu, kiukweli kabisa siwezi kubishana na
moyo, ninakupenda kipepeo, nimekuwa nikikulilia
daima, nikikuomboleza kama umekufa lakini
bado Mungu alikuwa na mpango na sisi.
Nimeishi kwa taabu sana Kemi, porini na katika
maeneo hatarishi, nimefanya kazi kwa bwana
mmoja nikidhulumiwa ujira karibu mwaka
mzima, kwa hasira ili kulipiza kisasi kwa bwana
huyo aliyekuwa akinilaza pamoja na kuku ndani
ya banda lililojaa utitiri, nikaamua kumbaka binti
yake, Koku, kumbe siku hiyo inaoneka alikuwa
katika siku za uzazi, akashika mimba pa si mi
kujua, siku ya mwisho ya kuhitimu kozi yangu
ya jeshi ndipo aliponilete mtoto huyu, akanambia
kuwa yeye amechumbiwa na bwana mwingine
hivyo mimi nilee mwanangu, nikamchukua.” Joru
akaeleza, akameza mate kisha akaendelea,
“Hakuna mwanamke nampenda kama Kemi,
daima sikuona thamani ya maisha bila wewe,
daima nilikuwa naomba Mungu kama upo hai
tukutane tena na sasa limetimia, nisamehe
mpenzi, nisamehe sana, lakini elewa kuwa wewe
si ubavu wangu bali ni moyo wangu, nakupenda
Kemi, uwe mama wa watoto wangu, tuishi,
tutulie, tujenge familia,” Joru akamaliza na
kumtaza Kemi usoni. Machozi ya Kemi
yalikauka, tabasamu likachanua kama ua la
yugiyugi.
Kemi akamsogelea Joru, akashika kifungo cha
gwanda lake na kukifungua, kisha cha pili, mara
cha tatu mpaka vyote vikaisha, akamvua
gwanda lile na kuliweka kochini, Kemi hakuishia
hapo, akaufyatua mkanda mnene wa suruari ya
Joru, akalegeza zipu, jicho lake likapenya ndani
ya eneo nyeti la Joru, akaona jinsi gani kijana
huyo alikuwa kwenye hari, kwani alituna
kiukweli. Kemi akamkalisha Joru kochini,
akamvua buti zake na kuziweka kando akamtoa
na suruali akaiweka kando na kumuacha akiwa
na vesti na boxer pekee, kifua chake kilichokuwa
kikipanda na kushuka kilimhamasisha Kemi,
akawa akikaukiwa mate kila sekunde,
akasimama. Joru akaelewa nini maana ya Kemi
kusimama, naye akasimama na kumkumbatia
akambusu kwa bashasha, kama alivyokuwa
akiona kwenye sinema, akaupitisha ulimi wake
kinywani mwa binti huyo, Kemi nae hakuwa
nyuma akakubaliana na hilo, ndimi zao
zikaogelea katika kinywa cha kila mmoja. Joru
akaishusha zipu ya blauzi ya Kemi kabla
hajaitupa pembeani na kukutana na kifua mororo
cha binti huyo, matiti mawili ya ukubwa wa
wastani yalikipamba kifua hicho kilichopendeza,
kilikuwa kikipanda na kushuka kikionesha ni jinsi
gani kilitamani. Joru akacheza na mtiti hayo,
akiyaminya kwa ustadi na kuyanyonyanyonya,
akaona Kemi akilalamika kwa raha,
akamnyanyua na kuingia naye chumbani,
akambwaga kitandani kisha akamalizia kuitoa
sketi ya binti huyo.
Baada ya dakika kama kumi na tano za
kuliwazana kwa kushikana hapa na pale kimya
bila yeyote kuongea, sasa kila mtu akawa kama
alivyozaliwa akishuhudia umbo la mwenzie,
wawili hao wakazama katika mapenzi mazito,
Kemi alikuwa akilalamika hasa kwa kusikia
maumivu kwa kuwa ilikuwa ni mara yake ya
kwanza, shughuli ilikuwa pevu, Joru akiwa ni
mara moja katika maisha yake kufanya tendo
hilo, hapo kwa Kemi alifurahia, kila mtu akawa
anaongea lugha yake, lugha iliyojulikana na wao
wenyewe.
Baada ya saa nzima ya mapenzi mazito, tayari
Joru alikuwa ameshafungua njia kama Kemi
alivyomuahidi, usingizi ukawapitia wote wawili,
waliposhtuka ilikuwa saa nane mchana, kila
mmoja akakimbilia bafuni kujiswafi, lakini bado
kila mmoja alikuwa na hamu na mwenzake,
hivyo wakatumia muda mwingine kujuliana hali
ndani ya bafu hilo lililojengwa kwa ndani ya
nyumba hiyo. Ilikuwa ni furaha ya watu wawili
kukutana tena.
Baada ya wiki moja
“Joru mpenzi, ijapokuwa tumeonana baada ya
miaka mingi, lakini unaonekana huna furaha”
Kemi alimwuliza Joru, wakiwa wameketi kwenye
jiwe nje ya nyumba ya Shibagenda pamoja na
mtoto wao.
“Ni kweli usemalo mpenzi, sina raha hata kidogo,
kuna jambo natakiwa kulifanya lakini sijajua ni
wapi pa kuanzia,” Joru akajibu.
“Niambie nitakusaidia, kama tumekutana tena
na jambo hilo hujaweza kulitatua basi amini
kwamba ni mimi wa kukusaidia ili ulitatue sasa,”
Kemi aliongea kwa lugha ya ushawishi.
“Kemi, kabla baba yangu hajafa aliniambia
maneno machache lakini pia hakuyamaliza,
akakata roho,” Joru akamwambia Kemi.
“Maneno gani?” Kemi akahoji.
“Aliniambia nilipize kisasi kwa mtu aliyemwaga
damu ya wanakijiji na damu ya Rutashobya,
sasa hili ni deni ambnalo liko moyoni mwangu
kwa miongo miwili sasa, nitaaniza wapi, sijajua,
kabla hajafa ilionekana kuna kitu anataka
kuniambia, aliishia tu kusema neno ‘nyuma ya
choo’ lakini hakunambia nini alimaanisha,” Joru
akamueleza Kemi kile kinachomsumbua akilini
mwake.
“Nyuma ya choo?” Kemi akauliza.
“Ndiyo, nyuma ya choo,” Joru akajibu. Kemi
akatulia kimya akitafakari jambo, kisha
akamtazama Joru aliyekuwa akicheza na
mwanawe, akatabasamu kuwaona hao Joru
wawili wakicheza kwa furaha.
“Joru, huna budi kufanya uloambiwa, kuna kitu
nakumbuka sasa, nafikiri kitakuwa na maana
kwako, nafikiri, labda ni jibu la swala lako,” Kemi
alimweleza Joru, akaketi vizuri na kumtazama.

1977
kijijini kwa JORU na
KEMI

JIONI ya siku moja, mzee Rutashobya, aliingia
chumbani mwake na kufungua mkoba ambao
una kitu alichokihifadhi kwa miaka mingi sana,
akakitoa na kukitia katika mfuko wa plastiki
kisha akatoka nacho nje, nyuma ya nyumba
akihakikisha hakuna anayemwona katika kufanya
hilo. Akachukua jembe na kuzunguka nyuma ya
choo, akachimba shimo la kina cha nusu mita na
kutumbukiza ule mfuko, kisha akafukia vizuri na
kutandaza nyasi juu yake. Akaangalia sana
kama kuna mtu aliyemuona hakuona kitu.
Wakati huo mzee Rutashobya akafanya hayo,
Kemilembe alikuwa akitoka kuteka maji,
akamuona baba wa Joseph akifukia kitu chini.
Kemi akasimama kwenye nyasi ndefu ili kuona
nini kinatukia, alishuhudia kila kitu mpaka Yule
mzee alipomaliza. Kwa kuwa Kemi alijuwa kuwa
hayamhusu, alaiendelea na safari ya kuingia
nyumbani. Mzee Rutashobwa akamuona Kemi,
akajiuliza kama atakuwa amemuona wakati
akilifanya hilo, akamwita Kemi, akimtaka kwanza
aweke ndoo ya maji nyumbani kwao. Baada ya
hapoi Kemi alikuja mpaka pale nyuma ya choo.
“Kemi, ulikuwa unatoka wapi?” akauliza
Rutashobya.
“Kuteka maji,” Kemi akajibu kwa lafudhi ya
Kihaya.
“Umeniona hapa nilikuwa nafanya nini?”
akauliza tena.
“Ndiyo babu nimekuona, umefukia mufuko,”
akamjibu kwa ustadi sana.
“Sasa sikiliza, hapa nimefukia sumu, sumu
mbaya kabisa ambayo ukiishika lazima ufe, usije
kucheza hapa na wenzako, sawa?” Rutashobya
akatoa onyo.
“Sawa babu!” Kemi akajibu. Watoto wa kijiji
hicho walizoea kumwita mzee Rutashobya
‘babu’ kutokana na uchezhi wake kwa watoto,
akiwatania kila kukicha, hivyo daima
walimpenda sana mzee huyu.
“Usimwambie mchumba wako Jose, sawa?”
akamsisitizia. Kemi akaitikia na kukiri kuwa
hatomwambia mtu. Kemi alipoondoka mzee
Rutashobya nae akatoka eneo lile, alijua wazi
kuwa baada ya siku chache tu Kemi atasahau
juu ya tukio lile na ndivyo ilivyokuwa.
Kemi hakukumbuka tena hata kama alimuona
mzee huyo akiwa pale, siku, miezi ikapita. Lakini
yeye tu Rutashobya aliyejua kuwa amefukia kitu
gani, malengo yake si kumpa mtu yeyote kitu
hicho bali aliamua kukitupa kwa kuwa ni sumu
mbaya kabisa, alikitupa kwa mtindo huo kwani
aliona wazi kama akitupa kwa njia ya kawaida,
watoto na watu wengine wangezurika nacho.
Siku alipokuwa anakufa baada ya mateso makali
ya vibaraka wa nduli Idd Amin, aliona kuwa ni
wakati wa kumwambia mwanawe, japokuwa
haikuwa dhamira yake tangu kwanza, kabla
hajamwambia ni nini kipo mzee Rutashobya
akakata roho, Joru akabaki gizani, hakujua ni
nini baba yake alitaka kumwambia.
Rejea Joru na KEMI
JORU alisisimkwa mwili kwa habari hiyo ya
Kemi, hakuwahi kuisikia hata mara moja katika
maisha yake, alimkumbatia Kemi kwa nguvu.
“Kemi, twende kijijini, nikachimbe hapo nione
kuna nini!” joru alisisitiza. Kemi akamtazama
Joru, akatikisa kichwa.
“Joru, hakuna kijiji kule ni mapori na machaka
ya kutisha!” Kemi akamwambia Joru.

KEMI NA JORU MAPENZINI..... KEMI
ANAMSIMULIA JORU JUU YA TUKIO LA ZAMANI
SANA AMBALO YEYE ALILISHUHUDIA KIJIJINI
KWAO..... JE LITAKUWA NA MATIKI KATIK
MKASA HUU?
 
Back
Top Bottom