Riwaya: muuaji aliyebakia

Riwaya: muuaji aliyebakia

kidi kudi

JF-Expert Member
Joined
May 17, 2011
Posts
2,510
Reaction score
2,163
riwaya: MUUAJI ALIYEBAKIA

Mtunzi: RAYMOND MWALONGO

Sehemu ya 1
Ilikuwa Ijumaa ya tarehe kumi mwezi
Desemba ambayo hali yake ya hewa ilikuwa
tulivu kabisa. Nyakati hizo za asubuhi
mambo hayakuwa shwari katika nyumba ya
mzee Kibudo ambayo watu kadhaa
walikuwapo nje wakilia kwa huzuni juu ya
kifo cha mzee huyo aliyeuawa na watu
ambao hawakujulikana. Watu hao wa kijiji
cha Magugu wilaya ya Babati mkoani
Manyara waliungana na familia ya mzee huyo
katika tatizo hilo la msiba. Maswali mengi
yalikuwapo vichwani mwa watu juu ya mtu
aliyefanya mauaji hayo kwa mzee huyo
aliyekuwa mkarimu licha ya utajiri wake
aliokuwa nao kijijini hapo. Jeshi la polisi
lilifanya uchunguzi juu ya kifo cha mzee huyo
na mwishoe familia yake ilihurusiwa kufanya
mazishi wakati wahusika wa tukio hilo
wakiendelea kupelelezwa.
Hatimaye mzee Kibudo ambaye ilielezwa
kuwa aliuawa kwa mapanga alizikwa, tukio
hilo lilishuhudiwa na mkewe na watoto wake
watatu pamoja na ndugu na jamaa waliofika
msibani hapo. Mara baada ya msiba huo
familia ya marehemu Kibondo ilikuwa ikisubiri
maelezo yeyote kuhusiana na wauaji wa
mzee huyo lakini hakuna taarifa zozote
zilizopatikana kutoka jeshi la polisi. James
Kibudo ambaye alikuwa mtoto wa mwisho
wa marehemu ndiye pekee alifanikiwa kupata
nafasi ya kusoma katika shule moja mkoani
Arusha. Kaka yake mkubwa alikuwa
akiwasaidia wazazi wake kazi za shamba na
uchungaji wa ng’ombe vitu vilivyomfanya
mzee Kibudo kuwa na uwezo kifedha kijijini
hapo.
Baada ya msiba huo James aliondoka
nyumbani kwao kurudi shuleni mara baada
ya kuagana na familia yake akiwamo dada
yake aliyetarajiwa kuolewa. Kichwani alikuwa
na mawazo juu ya mtu aliyehusika na mauaji
ya baba yake jambo lililomkosesha raha mara
kadhaa. Alitamani jeshi la polisi lifanikishe
kukamatwa kwa watu hao na sheria kali juu
yao ichukuliwe. Katika nyakati tofauti
aliwasiliana na familia yake kwa njia ya simu
akiulizia jitihada zilizofanywa na jeshi la
polisi lakini jibu lilibaki kuwa watuhumiwa wa
mauaji hayo hawakupatikana.
Mwezi mmoja baadaye James akiwa
amebakiwa na siku chache ili shule yao
ifunge kwa ajili ya likizo fupi, alishtushwa na
ujio wa mjomba yake shuleni kwao. Jambo
lililompa hofu ni hali ya wazi aliyoionyesha
iliyompa hisia za tatizo nyumbani kwao.
Mjomba yake huyo hakumweleza kitu zaidi ya
kumwambia kuwa ajiandae kwa ajili ya safari
kuelekea kwao, baada ya kubisha kwa muda
mfupi akitaka kujua sababu ya kufanya hivyo
alikubali na kujiandaa. Safari ilianza kuelekea
kwao, muda wote wa safari James alikuwa
na mawazo akiwa haelewi jambo lililokuwa
limetokea hali iliyopelekea aanze tena
kumuuliza mjomba yake huyo. Baada ya
kuona usumbufu ulizidi alimjibu kwa ufupi
kuwa kulikuwa na matatizo nyumbani kwao
hivyo uwepo wake ulihitajika.
Baada ya safari hiyo ya masaa kadhaa
walifika kijijini kwao Magugu, walianza
kutembea taratibu kuelekea nyumbani kwao
muda wote alikuwa na hofu akiwa haelewi
kilichokuwa kinaendelea. Hofu hiyo ilimzidi na
kujikuta akianza kulia baada ya kuona kundi
la watu wakiwa wamezunguka eneo la
nyumba yao na kelele za vilio
zikiendelea.Alijitahitidi kutembea lakini miguu
yake ilimwishia nguvu na hatimaye alianguka
chini kabla ya kusaidiwa na watu
waliokuwapo eneo hilo la msiba. Alipelekwa
mpaka ndani na kuwakuta ndugu zake
kadhaa waliomtaka atulie na kujipa ujasiri
kama mwanamme. Walianza kwa kumweleza
kuwa familia yake yote ilikuwa imeuawa
usiku wa siku hiyo. Jambo hilo lilimfanya
James kulia kwa uchungu baada ya kuelewa
yeye pekee ndiye alikuwa amebakia katika
familia hiyo zaidi hakuelewa chanzo cha
mauaji hayo yaliyofanywa.
Kama kawaida polisi walifanya uchunguzi
wao juu ya tukio hilo na kuondoka na
vielelezo wakiahidi kufanya upelelezi zaidi.
Hatimaye miili ya wanafamilia hao
waliouawa kwa kukatwa na mapanga ilizikwa
kijijini hapo. James alijawa na mawazo juu
ya muuaji wa familia hiyo na wazo la
kuhakikisha muuaji anapatikana linamkaa
zaidi kichwani mwake. Akili yake ilikuwa
tayari kuua katika kulipiza kisasi kwa mtu
yeyote ambaye angethibitika kuhusika na
mauaji hayo. Wakati huo alikuwa kidato cha
nne akiwa amebakiwa na miezi kadhaa ya
kumaliza shule, baada ya likizo aliondoka
akirudi shule akitarajia kupata taarifa za
wauaji kutoka jeshi la polisi.
Mali za familia hiyo ya marehemu Kibudo
zilianza kusimamiwa na mdogo wake ambaye
hakubahatika kuwa na mtoto katika maisha
yake. Zaidi alikuwa ni mtu mlevi ambaye pia
hakuwahi kuoa. Alichaguliwa kusimamia mali
hizo wakati James akisubiriwa amalize shule
ili akabidhiwe, hiyo yote ilitokana na hofu
waliyokuwa nayo ndugu wa familia hiyo ya
kuuawa iwapo wangesimamia mali hizo.
Ndugu wengi waliogopa hata kulala katika
nyumba hiyo ya marehemu mzee Kibudo
wakihofia kuuawa.
George Kibudo alisimamia mali hizo katika
misingi mibovu kutokana na tabia yake ya
ulevi aliyokuwa nayo. Baada ya miezi mitatu
James alirudi kijijini hapo na kuungana na
baba yake mdogo huyo kusimamia mali hizo
akiwa ameshamaliza kidato cha nne. Tatizo
lililomsumbua kichwani mwake lilihusiana na
kutokamatwa kwa mtu aliyehusika na mauaji
ya familia yake. Pia aliingiwa na hofu juu ya
sababu ya mauaji hayo, lakini jambo
lililokuwa kichwani mwake siku zote aliamini
baba yake hakuwa na kosa lolote
alilomfanyia mtu. Aliamua kuanza upelelezi
wake kwa utulivu kumfuatilia mtu aliyehusika
na mauaji hayo kwani aliamini alikuwapo
kijijini hapo. Alianza tabia ya ulevi ambayo
awali hakuwa nayo lengo likiwa ni kuwa
karibu na watu ili kufanikisha upelelezi wake.
Baada ya kipindi kifupi alibaini baba yake
alishawahi kufanya biashara ya pamoja na
mzee mmoja aliyejulikana kwa jina la Samola
miaka mingi iliyokuwa imepita. Katika
biashara yao hiyo walimalizana kwa
kufikishana mahakamani baada ya
kushindana katika kugawana n`gombe
walizokuwa nazo. Baada ya mzozo huo wa
kugawana n`gombe kumalizwa na
mahakama, baba yake hakuwa na uhusiano
wa karibu na mzee huyo ambaye alifilisika
miaka kadhaa baada ya kugawana kwao.
Upelelezi huo uliompa shaka ndiyo ulimfanya
James amweleze baba yake mdogo aliyeishi
naye wakati huo ambaye alipinga kuhusishwa
kwa mzee huyo katika mauaji hayo ya familia
yao.
Waliendelea na shughuli zao za kila siku,
wakati upelelezi wa James dhidi ya muuaji
wa familia yake ukiendelea. Siku moja akiwa
amelewa akirudi nyumbani kwao akitokea
eneo lililouza pombe za kienyeji ikiwa yapata
saa saba usiku, James alishtushwa na kelele
zilizotoka nyumbani kwao za mtu
aliyeonekana alikuwa akipigwa. Kutokana na
hali ya kulewa aliyokuwa nayo hakuingiwa na
hofu zaidi ya hasira zilizompanda akiamini
kuna watu walikuwa wakifanya mauaji.
Alichomoa panga lake aliloliweka kwenye koti
ambalo siku zote alikuwa akitembea nalo
akihofia usalama wake, alianza kukimbia kwa
kasi akielekea nyumbani kwao huku akipiga
kwa sauti ya juu kelele ambazo
hazikueleweka.
Mara baada ya kuukaribia mlango wa
nyumba yao, aliwaona watu wawili wakitoka
kwa kasi, mmoja akiwa na shoka na
mwingine akiwa na panga. Alisimama
pembeni kidogo na mlango wao akiwa
anatafakari afanye nini, punde kidogo alitoka
mtu mwingine kwa kasi ndani kwao akiwa
amebeba panga mkononi. James alitoka
mbio akimfukuza mtu huyo aliyekimbia kwa
kasi ya ajabu, baada ya kuwa mita kadhaa
nyuma akimfukuza akiwa anahisi hawezi
kumkamata aliamua kurusha panga lake
lililompata sawasawa mtu huyo shingoni. Mtu
huyo alianza kukimbia kwa kupepesuka kabla
ya kuishia kuanguka, James alimsogelea na
kuanza kumpiga kwa mateke.
Mtu huyo alianza kujiviringisha chini akipiga
kelele baada ya panga lililompata kutoka
shingoni na damu nyingi ilikuwa ikimtoka.
“leo utasema anayewatuma kufanya
unyama…” alisikika James ambaye alikuwa
na hasira. Akiwa anaendelea kumpiga mtu
huyo katika eneo hilo la giza huku akili yake
ikiwa haijatulia kutokana na kulewa kwake
alishtushwa na kitu kizito kilichotua begani
kwake. Alianguka chini wakati mkono wake
wa kulia akielekeza kwenye bega lake la
kushoto na kushika panga lililomkata
sawasawa. Akiwa anapiga kelele kwa
maumivu aliwashuhudia watu wawili
wakimbeba mwenzao aliyemkata shingoni na
kuanza kuondoka naye kwa kasi eneo hilo
wakielekea katika vichaka vilivyokuwa karibu
na eneo hilo.

ITAENDELEA..
 
Sehemu ya 2


Akiwa anapiga kelele kwa maumivu
aliwashuhudia watu wawili wakimbeba
mwenzao aliyemkata shingoni na kuanza
kuondoka naye kwa kasi eneo hilo wakielekea
katika vichaka vilivyokuwa karibu na eneo
hilo.
James akiwa anaendelea kulia kwa maumivu
aliyoyapata, kundi la watu lilikuwa likielekea
kwa kasi eneo alilokuwapo baada ya watu
hao kusikia kelele zilizopigwa kwa muda
mrefu. Hatimaye walifika eneo hilo na
kumchukua kabla ya safari ya kumpeleka
hospitali kuanza, wakati huo James
aliendelea kulia pasipo kuelezea jambo lolote
lililokuwa limetokea. Watu hao waliomchukua
ambao walikuwa majirani walitoka kutoa
msaada baada ya kuamini kuna mauaji
yalikuwa yakifanyika katika nyumba ya
marehemu Kibudo. Walikuwa wamebeba zana
mbalimbali na zaidi kwa pamoja walikuwa na
shauku siku zote za kumfahamu mtu
aliyekuwa akifanya mauaji katika familia hiyo.
Waligawana kwa wengine kwenda kumpeleka
James hospitali wakati wachache walibaki
wakijadiliana juu ya matukio hayo yaliyokuwa
yakiongozana. Mmoja wao alimkumbuka
George Kibudo, baba yake mdogo na James
jambo lililowapa hisia za kuanza kumtafuta
kwa vile waliishi pamoja. Waliingia katika
eneo la sebule la nyumba hiyo wakiwa
wamebeba taa za mafuta kutokana na
ukosefu wa umeme eneo hilo. Walishtushwa
na mauaji yaliyokuwa yamefanyika sebuleni
hapo dhidi ya George, alikuwa ameuawa
kikatili na damu nyingi ilikuwa imemtoka
ikiwa imezunguka eneo alilokuwapo.
Wanawake walioshuhudia tukio hilo walianza
kulia kwa sauti huku wakitoka eneo hilo la
sebuleni ambalo mauaji hayo yalikuwa
yamefanyika dhidi ya George.
Watu waliokuwapo nje nao walipata shauku
ya kuona kilichokuwa kimetokea ambao nao
pia hawakuwa na hamu ya kumtazama
George mara mbili kwani alikatwa mapanga
kila eneo la mwili wake. Siku iliyofuata ndugu
na jamaa walifika nyumbani hapo kwa
marehemu mzee Kibudo wengi wakiwa na
mshtuko baada ya taarifa za mauaji hayo.
Ndugu wachache ambao awali
walipendekezwa kusimamia mali hiyo ya
marehemu mzee Kibudo walionekana
wakijisifu kwa kukataa kwao kutokana na
hofu ya kutokea kwa mauaji ambayo awali
walikuwa nayo. Bado kulikuwa na kitendawili
juu ya muuaji wa familia hiyo na wachache
walihisi huenda James alipata ufumbuzi
kidogo. Baada ya uchunguzi wa jeshi la polisi
mwili wa bwana George Kibudo ulihurusiwa
kuzikwa, siku iliyofuata zoezi hilo lilifanyika
ambalo pia lilihudhuliwa na James ambaye
alikuwa amepata matibabu ya awali.
Muda wote wa mazishi James alikuwa na
hasira juu ya mtu aliyehusika na mauaji hayo,
mkono wake wa kushoto ulikuwa ndani ya
koti lake baada ya kufungwa ili
usichezecheze. Bado hisia zake zilikuwa
zikimtuma na kuamini mzee Samola alihusika
na mauaji hayo. Mbali na mahudhurio ya
mzee huyo katika misiba ya ndugu zake bado
hisia zake zilibaki palepale. Jambo lililompa
taabu ni uwezo wake wa kufikiri alioufanya ili
kumkumbuka mtu aliyefanikiwa kumkata na
panga shingoni lakini hakufanikiwa
kumkumbuka. Aliamini hiyo yote ilitokana na
kulewa kwake siku hiyo ya tukio zaidi
alipanga kuhakikisha mtu aliyehusika na
mauaji hayo anagundulika na kufikishwa
katika vyombo vya sheria. Baada ya mazishi
hayo askari wa upelelezi walimwita James
kando na kuhitaji kujua mambo kadhaa
yaliyohusiana na tukio zima lililopelekea
kuuawa kwa baba yake mdogo.
James alitoa maelezo yake kwa askari hao
ingawaje hakuhusisha hisia zake juu ya mzee
Samola, alipanga kufanya upelelezi yeye
mwenyewe juu ya mzee huyo. Askari hao
ambao pia waliahidi kufanya upelelezi
walimweleza pia kuwa wangetoa taarifa
katika zahanati na hospitali ili mtu aliyeumia
shingo asipatiwe msaada wa matibabu
pasipo maelezo ya kutosha. Baada ya siku
tatu, katika kikao cha familia James
aliwaomba ndugu zake kadhaa wamsaidie
kusimamia mifugo na mashamba ambavyo
vyote vilikuwa vya marehemu baba yake.
Hakuna hata ndugu mmoja alithubutu
kukubali kumsaidia kusimamia mali hizo
kwani kila mmoja alihofia uhai wake akiamini
angeuawa. James alijitahidi kuwaeleza ndugu
zake juu ya mwenendo wa marehemu baba
yake akiwahakikishia kuwa alikuwa mtu
mwema lakini hakuna hata ndugu mmoja
aliyethubutu kuamini. Wengi walikuwa
wameiingiwa na hofu hata watu wazima
hawakuwa tayari kumsaidia.
Aliendelea kusimamia mwenyewe mali hizo
akiwatumia watu aliowaajiri kama vibarua.
Baada ya wiki moja akiwa katika matembezi
yake ya jioni, wakati ambao pia mkono wake
ulikuwa haujapona alimuona mzee Samola
kwa umbali katika eneo ambalo liliuzwa
pombe za kienyeji. Aliendelea kutembea
akiwa hana wazo la kumsalimia mzee huyo
ambaye alikuwa akimtazama kwa makini na
hatimaye alimwita James. Alitiii wito kwa
kuanza kutembea kuelekea eneo alilokuwa
amekaa mzee huyo, mara baada ya kumfikia
na kumsalimia, aliketi katika kiti kilichokuwa
upande wa pili uliotazamana na mzee huyo.
“Kijana pole sana kwa matatizo yaliyokukuta,
naomba ujipe moyo” Aliongea mzee Samola
akiwa ameinamisha kichwa chake chini.
“aah! mambo ya kawaida tu haya mzee,
mimi nimeshatulia” alijibu James akiwa
amemkazia macho mzee huyo. “Askari
wanaendeleaje na upelelezi?” Aliuliza tena
mzee huyo swali ambalo James hakuchelewa
kulijibu.
“upelelezi unaendelea vizuri na tunatarajia
watuhumiwa watafunguliwa mashtaka ndani
ya mwezi huu” alijibu swali hilo na
kumpandisha mzee Samola hofu ya waziwazi
aliyoigundua kutoka kwa mzee huyo. James
mara baada ya kumjibu aliaga na kuanza
kuondoka akimwacha mzee Samola akiwa
na nia ya kuwafahamu watuhumiwa wa tukio
hilo lakini James alimweleza alikuwa na
haraka wakati huo.
Akilini aliingiwa na hisia za kuamini ya kuwa
mzee Samola alihusika na mauaji ya familia
yake kwa namna moja au nyingine, zaidi
alihitaji ukweli juu ya hisia zake upatikane.
Aliamua kuanza kurudi nyumbani kwake ili
akapange jambo la kufanya kuhakikisha
anaupata ukweli unaomhusu mzee Samola.
Mara baada ya kufika nyumbani kwake alikaa
sebuleni akiwa anawaza jambo la kufanya,
punde alisikia sauti ya mwanamke akipiga
hodi jambo lililomfanya afungue mlango na
kumkaribisha. Alikuwa ni mwanamke
aliyemfahamu kwa sura lakini hakutambua
alikaa maeneo gani kijijini hapo.
Baada ya kuzungumza kwa muda mfupi,
mwanamke huyo ambaye alionekana
kutokuwa na furaha alimtaka James
waongozane naye nyumbani kwake.
Alimweleza kuwa kulikuwa na jambo muhimu
ambalo alipaswa kulitambua. James bila
uoga alikubali na mara baada ya kufunga
mlango wa nyumba yake walianza kutembea
na mwanamke huyo kuelekea nyumbani
kwake. Hatimaye walifika nyumbani kwa
mwanamke huyo baada ya nusu saa ya
kutembea, alikuwa akiishi katika nyumba
iliyokuwa eneo la peke yake, waliingia katika
nyumba hiyo na James alikaribishwa kiti na
kuketi.
Mwanamke huyo alianza kwa kuhitaji utulivu
wa James juu ya yote ambayo alidai
yangetokea siku hiyo, jambo ambalo aliahidi
kulitekeleza. Alianza kumwelezea juu ya
mume wake ambaye alidai alikuwa amefanya
mambo ya kusikitisha, wakati akieleza hayo
mwanamke huyo alikuwa akilia. Jambo hilo
lilimfanya James ahitaji kujua kuhusu mambo
ambayo mume wake huyo aliyafanya,
mwanamke huyo alisimama na kumwambia
amfuate. Alitimiza jambo hilo na walianza
kutembea kuelekea chumba cha pembeni
alichohisi kilikuwa chumba cha kulala,
alikuwa na shauku ya kujua jambo ambalo
lingetokea. Mara baada ya kuingia katika
chumba hicho James alimshuhudia
mwanamme mmoja aliyelala kitandani akiwa
amezungushiwa vitambaa shingoni mwake.
Kwa akili ya haraka aliamini mtu huyo ndiye
aliyefanikiwa kumdhuru kwa panga siku ya
mauaji ya baba yake mdogo.Alibaki na
shauku ya kutaka kujua mtu huyo alitaka
kumweleza nini. “Denis nimekuja na James
unayemhitaji” aliongea mwanamke
aliyeongozana naye mara baada ya kuingia
kwao. Mwanamme huyo aliyemgundua muda
huo kuwa aliitwa Denis alianza kunyanyuka
taratibu, “James karibu sana bwana” alisikika
akiongea kwa taabu mara baada ya kuketi
katika kitanda chake. Baada ya salamu
alianza kwa kumwambia kuwa alimwita ili
kumweleza mambo yaliyohusu mauaji ya
familia yake.Jambo hilo ambalo awali James
alilihisia lilimfanya moyo wake ulipuke kabla
ya kuanza kutokwa mishipa usoni iliyotokana
na hasira, hali hiyo haikugundulika na wenyeji
hao. “mtu anayehusika kwa aslimia zote ni
mzee Samola…..” alitulia kidogo wakati
mapigo ya moyo ya James yakiwa yameanza
kwenda mbio.
“yeye ndiye aliyemuua baba yako kwa mkono
wake akidai alidhulumiwa mali” Aliongea
mwanamme huyo kwa sauti ya chini na
polepole, alionekana alipatwa na tatizo
lililopelekea ashindwe kuongea vizuri.
 
Sehemu ya 3

“Yeye ndiye aliyemuua baba yako kwa mkono wake akidai alidhulumiwa mali” Aliongea mwanamme huyo kwa sauti ya chini na polepole, alionekana alipatwa na tatizo lililopelekea ashindwe kuongea vizuri.
Wakati huo James alikuwa ametoa macho
akimwangalia mwanamme huyo aliyesimulia
mauaji ya familia yake.
“nimeamua nikueleze kwani siamini kama
nitapona na zaidi nahitaji msamaha wako
kwani nilihusika katika mauaji ya mara ya pili ya familia ya…” kabla hajamalizia sentensi hiyo James alimvamia na kuanza kumpiga
ngumi mfululizo mwanamme huyo akitumia
mkono wa kulia ambao hakuumia.
“James usimpige, usimpige kama
nilivyokuomba kuwa mtulivu naomba utulie” alipiga kelele mwanamke aliyempeleka hadi eneo hilo jambo ambalo alitii. Alikuwa akitokwa na jasho kama alinyeshewa na mvua wakati huo mwanamme huyo alikuwa akikoroma mara baada ya kupigwa.
James aliondoka eneo hilo kwa kasi akiwa haelewi la kufanya hasira zilimpanda na aliweza kumuuwa mzee Samola kama angekutana naye njiani, alielekea nyumbani kwake ili kwenda kufikiri jambo ambalo alipaswa kulifanya. Aliamua kupiga simu
kituo cha polisi cha wilayani Babati, askari walimwahidi kufika katika kijiji hicho cha Magugu ndani ya nusu saa.. Baada ya dakika arobaini na tano gari la askari lilifika nyumbani kwake hapo na aliwaongoza mpaka nyumbani kwa bwana Denis baada ya kutoa maelezo ya muda mfupi. Walimkuta akiwa amezidiwa sana ingawaje aliweza kuwathibitishia kuhusika na mauaji ya familia
ya mzee Kibudo akiwa anatumwa na mzee
Samola.
Walimchukuwa na kuanza safari ya
kumpeleka hospitali ya wilaya ili akapatiwe matibabu, mara baada ya kufika katika hospitali hiyo madaktari walielezea uwezekano mdogo wa kupona kwake kwani kidonda chake kilichimbika sana. Hiyo yote ilitokana na aina ya dawa ya kienyeji aliyokuwa akiitumia, alikuwa akihofia kukamatwa kwake akienda hospitali jambo lililomfanya atumie dawa hizo. Askari mmoja
alielezwa amlinde mgonjwa huyo na gari hilo la polisi liliondoshwa kwa kasi na kuanza kurudi kijijini Magugu. Askari hao waliokuwa wameongozana na James, lengo lao kubwa lilikuwa ni kwenda kumkamata mzee Samola aliyehusishwa na mauji ya familia ya mzee Kibudo kwa kiasi kikubwa. Mara baada ya
kufika nyumbani kwake mzee huyo
alishtushwa na ujio wa askari hao jambo
lililowapa imani juu ya kuhusishwa kwa mzee huyo na mauaji hayo.
Askari hao walimkamata mzee Samola na
kumpakia kwenye gari la polisi, wakati hayo yakiendelea watoto wake pamoja na wajukuu kadhaa walikuwa wakilia kwa uchungu juu ya tukio hilo lililokuwa likiendelea. Hata majirani
walishtushwa na tukio hilo kwani
walimtambua mzee Samola kama mtu
mwema, vilio vyao hivyo havikuwazuia askari
kutekeleza kazi yao kwani waliondoka na
mzee huyo. Walimpeleka kituo cha polisi cha
wilaya hiyo ya Babati na mashtaka dhidi yake
yalitarajiwa kufunguliwa siku iliyofuata.
James aliruhusiwa kurudi nyumbani huku
moyoni akiwa na amani ambayo aliikosa
katika kipindi kirefu. Mawazo yake yalimtuma
kuhakikisha haki inatendeke katika kesi
ambayo ilitarajiwa kufunguliwa hakutaka aina
yeyote ya upendeleo. Alihitaji mzee Samola
ahukumiwe adhabu ya kunyogwa kwa vile
alifanya mauaji katika familia yake, alikuwa
tayari kuua endapo mahakama ingeshidwa
kufanya kazi.
Jioni ya siku hiyo James alipigiwa simu na
mtu ambaye namba yake haikuonekana
aliyemweleza awe mwangalifu kwani alikuwa
akitafuta matatizo. Alipuuzia kauli hiyo na
kuamini ilitoka katika familia ya mzee
Samola. Siku iliyofuata askari walimfuata
kijana Denis aliyekuwa amelazwa katika
hospitali ya wilaya wakihitaji maelezo zaidi,
lakini alikuwa amezidiwa na kushindwa
kuongezea jambo lolote. Masaa machache
baadaye hali yake ilizidi kuwa mbaya zaidi na
askari waliwaomba madaktari wajitahidi
kuokoa maisha ya kijana huyo ili atoe
maelezo yaliyohusiana na kesi ya mauaji.
Hiyo yote ilitokana na mahojiano ya awali
ambayo askari walifanya na mzee Samola
aliyekana kuhusika na mauaji ya familia ya
mzee Kibudo.
Hatimaye kesi iliyohusu mauaji ilifunguliwa
dhidi ya mzee Samola na kijana aliyeitwa
Denis ambaye pia alikuwa bado hajapona.
Wiki tatu baadaye kijana huyo alipata nafuu
baada ya jitihada kubwa zilizofanywa na
madaktari na alikuwa na uwezo wa kupanda
kizimbani. Jambo hilo lilikuwa faraja kwa
James ambaye muda wote alikuwapo na
askari hospitalini hapo ili kumlinda
mtuhumiwa huyo. Baada ya hali ya
mtuhumiwa huyo kuwa nzuri kiasi alimtaja
mtu mwingine ambaye alikuwa mtoto wa
mzee Samola kuwa alihusika pia na mauaji
ya familia ya mzee Kibudo. Kijana huyo
aliyeitwa Frank alikamatwa na kuongeza
orodha ya watumiwa waliobakiza siku chache
kupandishwa kizimbani.
* * * *
Jackson John Samola alikuwa mtoto wa nje
ya ndoa wa mzee Samola ambaye alikuwa
katika harakati za kutafuta maisha jijini
Nairobi nchini Kenya. Katika maisha yake
aliishi mkoani Shinyanga na mama yake na
hakuwahi kuishi pamoja na baba yake mzee
Samola. Alimheshimu baba yake huyo kwa
vile alikuwa akimtimizia mahitaji yote
aliyokuwa akiyahitaji wakati akiwa shule.
Jambo hilo lilimjengea tabia ya kumtembelea
mara kadhaa baba yake huyo mkoani
Manyara. Akiwa bado yuko jijini Nairobi
alishtushwa na taarifa alizopewa na ndugu
yake aliyemweleza kuwa baba na kaka yake
walikuwa wakishtakiwa kwa kosa la mauaji.
Jambo hilo lilimchanganya sana na
hakuamini kama ni kweli walikuwa
wakijihusisha na mambo kama hayo.
Aliwaeleza ndugu zake wajitahidi kufanya kila
waliwezalo kuhakikisha baba na kaka yake
wanashinda kesi hiyo. Kutokana na kubanwa
kwake na kazi aliamua kutuma fedha ili
ziwasaidie katika kutoa rushwa ikibidi ili
baba na kaka yake wasigandamizwe katika
kesi hiyo. Ndugu zake walijitahidi kufanya
jitihada mbalimbali ikiwamo ya kujaribu
kumuua kijana Denis aliyetarajiwa kuelezea
uovu huo lakini jitihada zao zilishindikana.
Hatimaye kesi hiyo iliposomwa kwa mara ya
kwanza watuhumiwa hao walionekana
kuhusika na mauaji ya familia ya mzee
Kibudo na hukumu ya kifo ilitolewa dhidi yao.
James alifurahishwa na tukio hilo lililofanywa
katika misingi ya haki, watu wengi
waliohudhulia kesi hiyo walihuzunika
ingawaje ukweli ulijieleza kuwa watu hao
walikuwa na hatia. Jambo kubwa ambalo
liliwafanya watu kuhuzunika ni imani
waliyokuwa nayo awali kuwa mzee Samola,
mwanaye pomoja na Denis walikuwa
wakionewa. Watu wa kijiji cha Magugu
waligawanyika pande mbili kwa wale
waliofurahia kutendeka kwa haki na wengine
wachache waliungana na familia ya mzee
Samola iliyokuwa na hasira juu ya hukumu
hiyo. James akiwa nyumbani kwake jioni ya
siku hiyo lilifika kundi la wazee na kuhitaji
kuongea naye, jambo ambalo alilitii.
Wazee hao waliokuwa upande wake
walimtaka ahame kijiji hicho haraka
iwezekanavyo ili kuokoa maisha yake, wazee
hao walimweleza juu ya mbinu za mauaji
ambazo lazima zingepangwa na familia ya
mzee Samola dhidi yake. Watu walizidi
kuongezeka katika kikao hicho cha ghafla na
zaidi ndugu zake waliungana na wazee hao
wakidai walichoka kushuhudia mauaji dhidi
ya familia yao. James alikubali ushauri huo na siku iliyofuata aliondoka akielekea mafichoni mkoani Arusha akiwa amewapa jukumu ndugu zake kuuza kila kitu alichokuwa nacho kijijini hapo. Alihitaji wamuuzie n`gombe zaidi ya mia aliokuwa nao na mashamba yote, fedha hizo alitaka
zimsaidie kwenda kuanza maisha sehemu
nyingine. Jambo hilo lilianza kutekelezwa na
vitu hivyo vilianza kuuzwa kijijini hapo na
sehemu nyingine tofauti.
Familia ya mzee Samola iliyokuwa na hasira
iliweka kikao juu ya jambo la kufanya wakati
watoto wa kiume wa mzee huyo walidai
walimsubiri mwenzao kutoka Nairobi nchini
Kenya ili wajue jambo la kufanya. Siku tatu
baadaye kijana Jackson John Samola
aliwasili kijijini hapo akiwa na hasira juu ya
tukio lililokuwa limetokea, alikaa na kaka
zake wengine ambao kwa pamoja
walijadiliana. Mtu aliyeonekana kusababisha
hukumu ya kaka na baba yao hakuwa
mwingine bali ni James Kibudo huku kaka
zake Jackson wakihitaji kulipiza kisasi.
Kilichowachanganya zaidi ni taarifa
walizozipata kuwa mtu huyo alikuwa
ameondoka kijijini hapo“msipate taabu kaka
zangu, kama mtu huyu yuko katika dunia hii
niachieni kazi, miaka hata kumi na tano
itapita lakini adhabu yake iko palepale”
alisikika akiongea Jackson akiwa na hasira.
Kupitia elimu yake aliwaeleza kaka zake
kuwa huo haukuwa muda muafaka wa kulipa
kisasi kwani ingekuwa rahisi kwa wao
kugundulika jambo ambalo walimwelewa.
 
mzee unatupoteza mzee!!! kwa nini usimalizie na uchu? milusi mingi siku zote humpoteza mbwa.
 
Sehemu ya 4

Kupitia elimu yake aliwaeleza kaka zake
kuwa huo haukuwa muda muafaka wa kulipa
kisasi kwani ingekuwa rahisi kwa wao
kugundulika jambo ambalo walimwelewa.
Baada ya kuuzwa kila kitu kilichokuwa chake kijijini kwao Magugu, James alielekea jijini Dar es salaam akiwa na lengo kubwa la kwenda kunzisha biashara hilo liliwezekana kwani alikuwa amepata kiasi kikubwa cha fedha. Ndugu zake aliwaeleza wagawane mashamba kadhaa ambayo hakuyauza na kichwani mwake hakuwa na wazo la kurudi kijijni hapo akihofia kuuawa kama aliyokuwa
amepewa ushauri. Moyoni alijiona hana kosa na alichoshukuru zaidi ni haki iliyokuwa imetendeka juu ya wauaji wa familia yake.
* * * *
Baada ya miaka kumi James alikuwa
miongoni mwa matajiri wakubwa jijini Dar es salaam kupitia biashara tofauti alizokuwa nazo. Hakuwahi kurudi kijini kwao hata siku moja ingawaje ndugu zake walimtembelea mara kadhaa. Tayari alikuwa ameowa na alibahatika kupata watoto wawili wakiume,
mambo yaliyojili miaka kumi iliyokuwa
imepita alianza kuyasahau na aliwaza
maendeleo zaidi. Wakati huo alikuwa na
marafiki zake kadhaa ambao baada ya
mikakati yao tofauti ya kujikwamua kimaisha waliamua kuanzisha kampuni ya utengenezaji wa vyombo vya ndani.
Taratibu zote zilifanyika na kampuni hiyo iliyosajiliwa kama JAJHO Company Limited ilianza kufanya kazi. Kampuni hiyo iliitwa hivyo ikitokana na kifupisho cha majina yao ambayo yalikuwa James,Amos,Jackson,Hamis na Onesmo. James ndiye alikuwa na hisa nyingi zaidi ya aslimia arobaini akifuatiwa na Jackson mwishoe wengine. Katika kipindi kifupi cha biashara kampuni hiyo ilionekana kukubalika
na watu walionyesha uzalendo kwa kununua bidhaa zake zilizotengenezwa hapahapa nchini. Jambo hilo lilikuwa faraja kwa James aliyekuwa kiongozi wa kampuni hiyo kutokana na hisa nyingi alizokuwa nazo,lakini pia wenzie walionyesha furaha juu yamafanikio hayo.Mafanikio yake ndiyo yalimfanya Jamesawapeleke mapema watoto wake nchini Marekani kwa ajili ya masomo. Walianza masomo katika shule iliyokuwa Chicago katika jimbo la Illinois iliyoitwa American Academy School iliyochukua watoto wa shule
ya msingi mpaka sekondari. Moyoni hakuwa na shaka akiamini alikuwa amefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika maisha yake.
Jackson wa kampuni hiyo ya JAJHO
Company Limited hakuwa mwingine bali ni
Jackson John Samola ambaye lengo lake
lilikuwa ni kulipiza kisasi kwa James.
Hakuwahi kukutana na James zaidi ya
kumuona kwenye picha kwa vile hakuishi
katika kijiji cha Magugu ambacho James
aliishi awali. Watu wote waliomiliki kampuni hiyo walikuwa rafiki zake na walikubaliana naye kuhakikisha wanamuua James. Lengo lao lilikuwa ni kusubiri kampuni hiyo ikue na James kuwa na kiasi kikubwa cha hisa na hatimaye kufanikisha zoezi la mauaji. Hakuna
mtu aliyekuwa akijua siri hiyo zaidi yao wanne, Jackson siku zote za maisha yake alikuwa akiamini James angekufa kizembe na tayari alinasa katika mtego wake.
Baada ya mwaka mmoja Jackson na
wenzake waliona ni muda muafaka wa
kuuawa kwa James wakati ambao walikuwa
na mafanikio makubwa katika kampuni yao. Walikuwa wakitafuta mbinu mbalimbali za kuhakikisha wanamuua James na mwishoe walipata jibu la kufanikisha zoezi hilo. Jackson alipendekeza kuwa waandae ziara
ya kufurahia mafanikio yao wakiwa na familia zao na mwishoe waiangamize familia ya James. Aliwataka ziara hiyo ifanyike nchini Kenya kwa vile aliifahamu vizuri nchi hiyo na
ingekuwa rahisi kufanikisha mauaji hayo. Wamiliki hao wa kampuni hiyo mbali na James walimheshimiana sana na Jackson na walikuwa tayari kumsaidia malipizi ya kisasi. Hawakuwa watu wema kwani walishawahi kufanya kazi za ujambazi na kwao kuuawa kwa James waliamini kungewapa kipato kikubwa kupitia hisa ambazo zingeongezeka.
Baada ya kikao chao hicho cha awali
walichokifanyia nyumbani kwa Jackson,
walipanga Amos ambaye alikuwa miongoni
mwa wamilikiwa kampuni hiyo atoe maoni ya ziara hiyo katika kikao chao cha kampuni kilichofanya kila mwisho wa wiki. Kama ilivyokuwa kawaida yao kuwa na kikao siku ya Ijumaa, James alijumuika na wamiliki wenzie wa kampuni hiyo katika kikao. Mara
baada ya mambo muhimu kuzungumziwa
Amos alitoa maoni ya kufanyika ziara nchini Kenya wakiwa na familia zao katika kumaliza mwaka huo na kufurahia mafanikio yao. Jambo hilo lilionekana kupokelewa vizuri ingawaje James hakulifikilia kabla alikubaliana na wenzake kufanyika ziara hiyo
mwishoni mwa mwaka. Wakati huo ilikuwa ni mwezi wa kumi na ziara yao ilipangwa
kuanza mwishoni mwa mwezi wa kumi na
mbili.
Makubaliano hayo yalionekana kuwa faraja kwa Jackson na wenzie walioamini kuwa mipango yao ilielekea kukamilika. Kila siku iliyokuwa ikienda walikuwa wakiendeleza vikao vyao vya siri vya kukamilisha mauaji hayo hiyo ilitokana na umaarufu aliokuwa nao James. Tayari alikuwa na jina kubwa hivyo mauaji dhidi yake yalihitaji usiri
mkubwa ili kushindikana kwa jitihada zozote za upelelezi. Jackson bado alijijengea tabia ya kuwaeleza kaka zake kuwa mambo mazuri yalikuwa hayahitaji haraka akiwahakikishia kukamilisha malipizi ya kifo
kama James alivyochangia kunyongwa kwa
baba na kaka yao.
Siku sita kabla ya ziara ya wamiliki wa
kampuni ya JAJHO Company Limited, James
alipokea taarifa za mwanae mmoja aliyekuwa akisoma American Academy School. Alielezwa mwanae huyo wa kwanza aliyekuwa na miaka tisa ambaye aliyeitwa Geofrey alikuwa akipatwa na homa za mara kwa mara jambo
lililowafanya walimu wa shule hiyo
wamshauri mwanae huyo arudishwe
Tanzania. James hakushangazwa sana na
taarifa hizo kwani alilitambua hilo kwa vile mwanae huyo alikuwa akipatwa na maradhi tofauti tokea utoto wake. Alikubaliana na walimu kuwa mwanaye huyo arudishwe Tanzania lakini mdogo wake aliyeitwa Robert alitakiwa kubaki nchini humo kuendelea na
masomo. Alielezwa mwanaye angefika
Tanzania baada ya wiki moja, hiyo ilitokana na ratiba ya ndege ambayo alikatiwa tiketi. James aliyaelewa maelezo hayo lakini aligundua mwanaye angefika yeye akiwa ziarani nchini Kenya, Alipanga kuacha taratibu zote za mapokezi ya mwanaye zikiwa sawa.
Hatimaye siku ambayo wamiliki wa kampuni ya JAJHO Company limited waliipanga kwa ziara ilifika na waliamua kutumia usafiri wa
gari lengo lao kubwa likiwa ni kupita katika vivutio tofauti vya nchi katika kanda ya kaskazini. Asubuhi ya siku hiyo James alifika na gari lake katika ofisi ya kampuni akiwa na mkewe ambaye walipendana sana tayari kwa ziara hiyo. Katika ofisi za kampuni yao
zilizokuwapo maeneo ya Posta tayari wamiliki hao walikuwa wamefika na alikuwa akisubiriwa Hamis na familia yake ambao walikuwa hawajafika. Lilikuwa limeandaliwa basi maalumu kwa ajili ya safari hiyo na
wamiliki hao walionyesha furaha wakisubiri safari hiyo ianze. “mzee hata mtoto tu,
inakuwaje?” aliongea Jackson akimuuliza
James katika hali ya utani kwani alielewa watoto hao walikuwa masomoni nchini Marekani.
“acha hizo bwana kwani hujui wako wapi?,ila mwanangu Geofrey yuko njiani akirudi tutapishana naye” aliongea James akijibu utani huo.
Baada ya dakika kadhaa Hamis alifika ofisini hapo akiwa na familia yake na safari ilionekana ilikuwa imesha kamilika. Waliingia
kwenye basi lililokuwa limeandaliwa na safari ilianza wakiwa wamepanga kupitia hifadhi ya taifa ya Serengeti na mwishoe walipanga wapitie mkoa wa Mara wakielekea nchini Kenya. Walimtumia dereva mmoja ambaye alikuwa akiaminika sana na kampuni hiyo,
James hakuwa na hofu kwani
alishamwandaa mtu wa kumpokea mwanaye
siku mbili zilizofuata hivyo aliamini mambo yote yangekuwa kama yalivyopangwa.Hawakuwa na haraka kwani siku hiyo walilala Moshi mjini wakiwa na lengo la kupata maelezo ya hifadhi ya mlima Kilimanjaro siku iliyofuata.
Walitekeleza zoezi la kutembelea hifadhi hiyo siku iliyofuata na baada ya maelezo mafupi yaliyohusu mlima huo waliendelea na safari wakipitia hifadhi ya Serengeti na siku tatu baadaye walikuwa nchini Kenya. Walitumia
siku mbili kutembelea maeneo tofauti ya jijini Nairobi na siku ya tatu walielekea Machakos kwa ajili ya kuendeleza ziara yao wakiwa na
furaha tele juu ya tukio hilo. Walifikia katika hoteli ya kifahari ambayo walikuwa wameikodi kwa ajili yao kwa siku kadhaa wakiwa sehemu hiyo. Kila familia ilipewa vyumba vyake na kila hitaji lilikuwa likitimizwa na wahudumu wa hoteli hiyo.
 
Sehemu ya 5

Kila familia ilipewa vyumba vyake na kila hitaji lilikuwa likitimizwa na wahudumu wa hoteli hiyo.
Jackson ndiye aliyefanya mipango yote na wakati huo aliona ulikuwa ni muda muafaka wa kuuawa kwa James na mkewe. Alikuwa ameongea na kundi la majambazi lililopaswa kuwasaidia kukamilisha mauaji hayo, majira ya saa tatu usiku watu hao walifika hotelini
hapo wakiwa na gari zao tatu. Mara baada ya kufika walimpigia simu Jackson ambaye aliwaahidi kutoka nje baada ya muda mfupi.
Baada ya kupigiwa simu Jackson alimuaga
mkewe na watoto wake akiwaambia kuwa
alikuwa na kikao kifupi na wamiliki wenzie wa kampuni yao. Alipotoka nje aliwapigia simu Amos, Hamis halikadhalika Onesmo akiwaeleza watoke nje. Walitekeleza jambo hilo kwani walielewa zoezi ambalo lilifuata,
nao waliaga familia zao wakieleza kuwa
walikuwa na kikao.Walipofika nje walipanda katika gari moja
lililokuwa la mwisho kati ya hayo matatu ya majambazi yaliyokuwa yamefuatana, Jackson alimpigia simu kiongozi wa kundi hilo aliyekuwa gari la mbele na kumweleza jambo
walilotakiwa kufanya. Mara baada ya zoezi hilo Jackson alichukua tena simu yake na kumpigia James na punde ilipopokelewa alianza kwa kusikika “haloo James, njoo nje hapa na mkeo ikibidi kuna tatizo limetokea”
“tatizo? tatizo gani tena!” aliuliza James kwa mshangao. “njooni tu jamani mtaliona tusipoteze muda”
“sawa tunakuja” alimaliza James akiwa
ameahidi kutoka na mkewe. Baada ya dakika tano James alitoka na mkewe wakiwa na nguo za kulalia, walisimama katika mlango wa kuingilia katika hoteli hiyo. Jackson na wenzie walishuhudia vizuri tukio hilo,
alichukua tena simu yake na kumweleza
James aende katika Range Rover iliyokuwa ya kwanza kati ya tatu zilizokuwa zimeegeshwa zikiwa zimeongozana. James alifanya hivyo na alianza kutembea akielekea
katika gari hilo na hakuonyesha hofu yeyote. Alikuwa amemwacha mkewe akimwangalia hatimaye James aliingia katika gari hiyo aina ya Range Rover.
Baada ya dakika tano Jackson alielewa
mpango alioufanya ulikuwa umefanikiwa
alichukua tena simu yake na kumpigia mkewe James ambaye walimwona vizuri akiwa katika mlango wa hoteli hiyo. Hatimaye walimshuhudia akipokea simu “shemeji vipi? mbona unakaa nje, kuna mgonjwa hapa tunashauriana cha kufanya njoo” alisikika Jackson akimweleza mkewe James. “hee! kumbe mgonjwa nakuja” alijibu kabla ya kuanza kutembea akielekea kwenye Range
Rover aliyoelekea mumewe. Hatimaye naye
alipanda gari hilo, Jackson na wenzie
walipiga kelele za kupongezana wakiamini kazi ilikuwa imeisha. Ziliwashwa gari zote tatu huku lao likiendeshwa na jambazi aliyekuwapo toka awali, mara baada ya kufunguliwa geti la hoteli walianza safari kwa
mwendo wa kasi wakiwa na lengo la kuelekea eneo la Garrissa lilokuwa kando ya mto Tana walikopanga mauaji ya James na mkewe yaende kufanyika.
Mr. Tyoso kama alivyofahamika kutokana na matukio yake tofauti haramu ndiye
aliyehusika katika mpango huo wa kutekwa kwa James na mkewe huku safari ikiendelea kuelekea eneo walilopanga kumfanyia mauaji.Mara baada ya James kupigiwa simu aelekee
kwenye gari aina ya Range Rover,
Walijiandaa na kijana wake mmoja wa kazi aliyekuwa kwenye gari hilo na punde alipoingia walimpiga na kitako cha bunduki na kumfanya azimie walimfanyia hivyohivyo mkewe ambaye pia alikuwa amezimia. Wakati
huo mr. Tyoso alipanga kufanikisha mauaji
hayo ili kutimiza matakwa ya wateja wake na
mwishoe alihitaji kuendelea na shughuli zake
akiwa na kundi lake hilo.
Walikimbiza gari zao na masaa mawili
baadaye walikuwa katika eneo la Garrissa
lililokuwa na giza nene kando ya mto Tana,
wakati huo ilikuwa yapata saa tano na nusu.
Waliegesha gari zao katika eneo hilo ambalo
pia halikuwa na njia ila vichaka na mti
kadhaa iliyokuwapo. Lilikuwa ni eneo lenye
giza nene ambalo mtu mwoga asingevumilia
kukaa. Gari moja kati ya hizo tatu
walizokuwa nazo liliwashwa taa zake na
kufanya eneo hilo liwe na mwanga kama
ilikuwa mchana. James na mkewe
walishushwa na kuwekwa eneo la mbele
ambalo taa hizo za gari zilielekezwa, kwa
umbali James alianza kurudiwa na fahamu ila
kichwa kilimuuma sana. Hali haikuwa hivyo
kwa mkewe ambaye bado alikuwa amezimia,
mr. Tyoso aliwaamuru vijana wake
wakachote maji katika mto Tana ambao
ulikuwa umbali mfupi toka hapo, lengo lao
likiwa ni kuwamwagia maji. Walitaka kufanya
hivyo ili kurudisha kumbukubu za James na
mkewe.
Baada ya dakika tano vijana wake hao
watatu ambao walikuwa na bunduki
mabegani mwao walirudi na madumu matatu
ya maji ambayo walianza kwa kuwamwagia
James na mkewe. Wakati hayo yote
yakiendelea Jackson alikuwapo eneo la tukio
na wenzie, alikuwa na hasira akihitaji kuuwa
lakini alitulizwa na mr Tyoso aliyemtaka
asiwe na haraka. Dakika kadhaa baada ya
kumwagiwa maji ambayo yalikuwa ya baridi
sana James na mkewe walishtuka na
kukutana na picha mbili zilizonekana vizuri.
Mkewe James hakuzitambua picha hizo ila
mumewe alionyesha kushtuka, wakati huo
walikuwa wako chini eneo walilokuwa
wamemwagiwa maji. Waliponyanyua vichwa
vyao walikutana na sura waliyoifahamua ya
mtu aliyekuwa ameshika picha hizo ambaye
alikuwa Jackson.
James na mkewe walishtushwa na hali halisi
iliyokuwapo eneo hilo, watu zaidi ya watano
walikuwa na bunduki, aliwashuhudia wamiliki
wenzie wa kampuni wakiwa eneo hilo mbali
na Jackson aliyekuwa ameshika picha. Tayari
alijua kulikuwa na shari kwani aliiona picha
ya mzee Samola na mwanaye Frank ambao
wote kwa pamoja walihukumiwa kunyogwa
kwa kosa la mauaji ya familia yake. Muda
huo wote hakuna mtu aliyekuwa akiongea
zaidi ya Jackson aliyeshika picha huku
akitetemeka.
“ulizani ungepona kwa kusababisha kunyonga
kwa baba na kaka yangu?” alisikika Jackson
baada ya kimya cha muda mrefu, kabla
hajajibiwa kitu wakati huo James na mkewe
wakitetemeka alikurupuka na kuchukua moja
ya bunduki ya kijana wa mr. Tyoso na
kimumiminia kifuani mkewe James risasi
zaidi ya saba.
James alipiga kelele juu ya tukio hilo, na kwa
kasi ya ajabu alikurupuka kumvamia Jackson
aliyekuwa na bunduki akiwa na lengo la
kumpiga, kabla hajafanikisha lengo hilo
alikamatwa na Amos aliyesaidiana na Hamis
kabla ya kususkumwa tena chini.
“wewe ni kama muuaji unadhani utatuweza”
Aliongea Onesmo aliyekuwa ameshika nondo
mkononi na alianza kumpiga nayo, Amos na
wenzie nao walijumuika naye kumpiga James
ambaye alilia kwa uchungu akiwa haelewi
kosa alilowafanyia wenzie hao waliomiliki
kampuni moja.
Baada ya dakika tano James alikuwa
ameumizwa sana na damu nyingi ilikuwa
imemtoka nguo zote alizokuwa amevaa
zilikuwa zimelowa damu.
“ mfungeni kamba huyu kinyago..” alisikika
Jackson baada ya kuwasitisha wenzie
wasiendelee kumpiga. Baada ya agizo hilo
vijana wa mr. Tyoso walitekeleza jambo hilo
na kuanza kumfunga kamba, muda wote
matukio hayo yakiendelea hawakuingilia kitu
kazi yao ilikuwa ni kuhakikisha usalama wa
wateja wao. Mara baada ya kufungwa kamba
kwa James aliyekuwa akilia kwa sauti ya
chini Jackson na wamiliki wa kampuni
wenzie waliopanga mauaji hayo walichukua
bunduki kila mmoja. Walianza kuzikoki tayari
kwa kufyatua risasi wakiwa wamezielekeza
eneo alilokuwa amelala James akiwa
hatazamiki mara baada ya kipigo. Jackson
aliwaeleza wenzie wakae tayari kwa kufyatua
risasi akihesabu mpaka tatu “ moja….!
mbili….! ta…”
* * * * *
George Johnson alikuwa ni kijana ambaye
alizaliwa nchini Kenya na baada ya masomo
yake ya shule ya msingi na sekondari alianza
kujishughulisha utengenezaji filamu. Mara
kadhaa alifanya kazi hiyo katika sherehe
mbalimbali jijini Nairobi zikiwamo harusi na
mahafali. Aliishi akitegemea kazi hiyo na
mara nyingine alikuwa akiwafanyia kazi ya
kuwapiga picha watalii kadhaa waliokuwa
wakitembelea nchini Kenya. Alikuwa
akiwaandalia filamu za ziara zao watalii
nchini humo na hatimaye walikuwa
wakimlipa pindi walipokuwa wakirudi katika
nchi zao.
Mwezi wa kumi na mbili wakati sikukuu
zikiwa zimekaribia alipigiwa simu na shirika
moja lililohusika na watalii. Alielezwa kuwa
kuna watalii walikuwa wakimhitaji awapigie
picha za filamu kwa ajili utafiti wa viumbe
vilivyoishi kando ya mto Tana. George alitaka kupuuza ombi hilo kutokana na sikukuu zilizokuwa zimekaribia lakini aligundua baadaye kazi hiyo ilikuwa muhimu zaidi.
Aliwajibu watu hao kuwa alikuwa tayari kwa kazi hiyo, na hatimaye utafiti huo ulienda kuanzia eneo la Kipini ambalo ndipo Mto Tana ulikuwa ukiishia kuingia bahari ya Hindi.
 
Sehemu ya 6

Aliwajibu watu hao kuwa alikuwa tayari kwa kazi hiyo, na hatimaye utafiti huo ulienda kuanzia eneo la Kipini ambalo ndipo Mto Tana ulikuwa ukiishia kuingia bahari ya Hindi.
Watalii hao wanne waliokuwa wazungu
wakitokea Norway walianza utafiti wao huo wakiwa na George aliyechukua picha kila jambo aliloambiwa kuchukua.
Alikuwa akipiga picha vyura wa aina tofauti waliokuwa kando ya mto huo na hilo lilikuwa ndilo lengo kubwa la watalii hao walitaka kujua aina za vyura waliopatikana kando ya mto huo. Walikuwa wakitumia gari aina ya
Land Cruiser na kila ilipofika jioni walikuwa wakiweka mahema na kulala. Maisha hayo yalimchukiza George lakini jambo hilo lilikuwa la kawaida kwa wazungu hao waliozoea kazi
hizo za utafiti. Siku iliyofuata walikuwa eneo la Burra wakiendelea na utafiti huo, hali kadahalika George alikuwa akipiga picha kwa ajili ya kuandaa filamu ya watafiti hao
waliokuwa wakitokea Norway.
Siku ya tatu walikuwa eneo la Garrissa na mara baada ya utafiti wao huo liliwekwa hema na walilala tena eneo hilo wakiwa na gari lao katika sehemu hiyo iliyokuwa na miti pamoja na vichaka, walikuwa wakiweza
kupita kutokana na uwezo mkubwa wa gari
walilokuwa nalo. Muda wote waliokuwa
wakilala George hakuwa na mazoea ya
kufanya hivyo kutokana na uoga aliokuwa
nao, lakini haikuwa hivyo kwa watafiti
aliokuwa ameongozana nao ambao walikuwa
wakilala pasipo hofu. Alikuwa na kamera
yake kifuani ambayo kamba ya kibegi chake ilikuwa imemkaa shingoni, alitamani kazi hiyo ikamilike ili waondoke maeneo hayo ya mto Tana.
Majira ya saa tano na nusu usiku alishtushwa na kelele za magari yaliyonguruma upande wa magharibi wa eneo walilokuwapo. Jambo hilo lilimshtusha kwani hakufikiria kama kuna gari lingeweza kufika eneo hilo aliamua kutoka nje na alishuhudia mwanga uliotokana na taa za gari na kufanya eneo hilo lililokuwa
na giza nene liwe kama mchana. Dakika
kadhaa akiwa hajagungua jambo la kufanya alishuhudia taa kadhaa za gari hizo zikizimwa na mwanga wa kawaida ulibaki katika eneo hilo.
Alipata ujasiri wa ghafla uliomtuma aende eneo hilo bila kijiuliza mara mbili alianza kutembea eneo la pembeni na mwanga huo akiwa anausogelea. Lengo lake lilikuwa asionwe na watu hao waliokuwa wamefika eneo hilo nyakati hizo za usiku, mara baada ya kukaribia eneo hilo na kuanza kuyaona
magari hayo vizuri alilala chini na kuanza kujiburuza kwa tumbo akisogea zaidi eneo hilo.Hatimaye alikuwa umbali wa kama mita nane na alishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea eneo hilo lililokuwa na mwanga kama wakati huo ilikuwa mchana.
Aliwashuhudia watu kadhaa wakiwa na
bunduki mabegani mwao na wengine wawili
mwanamke na mwanamume walikuwa chini
kama vile walikuwa wamepotelewa na
fahamu. Baada ya dakika chache
aliwashuhudia watu wengine watatu wenye
dunduki zao wakiwa na madumu aliyohisi
yalikuwa maji kwani walikuwa wametokea
eneo la mto Tana. Walianza kuwamwagia
watu hao maji ambao walishtuka baada ya
muda mfupi, George alihisi kuna jambo
lilitaka kutokea juu ya watu hao na aliamua kuwasha kamera yake ya filamu ili ajumuike nayo katika kushuhudia tukio hilo. Taratibu aliiegesha na ilianza kuchukua picha za kila
kitu kilichoendelea eneo hilo, alimshudia mtu mmoja akiwa anawaonyesha watu hao waliomwagiwa maji picha.Baada kimya cha muda mrefu mtu huyo aliongea kidogo kabla ya kukurupuka na kuchukua bunduki kisha kumumiminia mwanamke aliyekuwapo chini na mwanamume kwa risasi zaidi ya saba.
George alishtushwa na unyama huo uliokuwa ukiendelea hata hali ya hofu juu yake ilianza kumwingia lakini alijikaza akiamini alikuwa
mwanamme kamili. Aliigeukia kamera yake
na kushuhudia ikiendelea kuchukua kila tukio lililoendelea. Alimwona mwanamme
aliyekuwa chini na mwanamke huyo
aliyepigwa risasi akijaribu kumvamia mtu aliyekuwa amefanya tukio hilo. Hakufanikiwa zoezi hilo kwani alisukumwa chini na alianza
kupigwa na watu hao ambapo mmoja wao
alionekana alichukua kitu kizito kama chuma.
Dakika chache baadaye mtu huyo alikuwa
ameumizwa vibaya na aliamriwa afungwe
kamba, baada ya kufungwa kamba
aliwashuhudia wanaume wanne wakizikoki
bunduki zao wakiwa tayari kwa kumuua mtu huyo aliyefungwa kamba. Mmoja wao alianza kuhesabu akisikika “moja….! Mbili…! tatu…!”
mara baada ya kuhesabu mara tatu watu
hao walianza kummiminia risasi mtu huyo
kama vile walikuwa vitani walikuwa hawana huruma hata kidogo. Wakati tukio hilo likiendelea George aligeuza kichwa chache asishuhudie tukio hilo, aliiacha kamera yake ikipiga picha kila kilichoendelea. Katika
maisha yake alikuwa akidhani matukio kama hayo yalikuwa ya filamu za kuigiza lakini alishuhudia kwa macho yake na kubaini kuwa yalikuwa yakitokea.
Baada ya zoezi hilo watu hao waliwasha gari zao na kuondoa kwa kasi eneo hilo la tukio,George alijikuta akilia peke yake juu ya mauaji hayo yaliyokuwa yametokea.Aliikumbuka tochi aliyokuwa nayo baada ya giza nene kutanda eneo hilo ikiwa ni baada ya kuondoka kwa magari hayo, alichukua kamera yake na kuanza kusogea taratibu eneo la tukio. Mara baada ya kufika eneo hilo
alitumia tochi akiendelea kuwapiga picha watu hao waliokuwa wameuawa, moyo
ulimuuma sana na hakuelewa kosa
walililokuwa wamefanya.
Akiwa anaendelea kizichukua vizuri picha za sura za watu hao waliouawa alishtushwa na mngurumo wa gari lililokuwa likirudi kwa kasi
eneo la tukio. Alitoka mbio na kwenda
kufichama katika kichaka cha karibu,
aliwashuhudia watu sita wakishuka katika gari hilo na mmoja wao aliwaamuru wenzie wakaitupe miili hiyo katika maji ya mto Tana.
Walitii maagizo hayo na kuibeba miili hiyo,walianza kuelekea upande uliokuwa na mto huo. Baada muda mfupi walikuwa
wametimiza zoezi hilo waliwasha tena gari zao na kuondoka kwa kasi. George alikuwa amechanganyikiwa na katika maisha yake hakuwahi kushuhudia mauaji kama hayo,aliingiwa hofu juu ya uhai wake kuhusiana na picha hizo alizozipiga.Siku iliyofuta ambayo ilikuwa ya mwisho aliendelea kuchukua picha zilizohusiana na utafiti uliofanywa na raia wa Norway.
Hakujaribu kumwambia mtu juu ya tukio
alilokuwa amelishuhudia usiku wa siku
iliyopita, hakuwa na furaha sana jambo
lililofanya watafiti hao wamwulize mara
kadhaa kama alikuwa na tatizo. Hakuthubutu kutoa siri hiyo aliyokuwa ameishuhudia, mara baada ya utafiti huo aliandaa filamu ya watalii hao na hatimaye aliikabidhi na kupewa malipo yake. Tayari pia alikuwa ameandaa filamu ya dakika ishirini na tano
iliyohusiana na mauaji aliyoyashuhudia,
alikuwa akisubiri asikie tukio lolote
lililohusiana na mauaji hayo ili aipeleke filamu hiyo kituo cha polisi. Matukio ambayo yalikuwamo katika filamu hiyo ilikuwa na vigumu kwa mtu kuamini kama yalikuwa ni mauaji ya kweli, alifanikiwa kuzipata picha za watu ambao walionekana vizuri mwanzo mpaka mwisho.
Siku kadhaa zilipita pasipo kusikia jambo lolote lililohusiana na mauaji hayo, alipata wazo la kupeleka kituo cha polisi filamu hiyo lakini kabla hajafanya hivyo aliamua kuomba
ushauri kwa mjomba yake aliyekuwa
mwanajeshi mstaafu. Alisimulia tukio
lililoendana na lake na kujifanya akiomba ushauri wa tukio kama hilo, mjomba yake huyo alimtisha akimwambia matukio kama hayo ni hatari. Aliongezea kuwa angefanikisha kukamatwa kwa watu hao lakini mwisho wake lazima ungekuwa kifo.George jambo hilo halikumwingia akilini hata kidogo, moyoni aliumia juu ya mauaji aliyokuwa ameyashuhudia na alipanga kuifikisha filamu hiyo kituo cha polisi endapo angesikia mauaji yeyote yaliyohusina na tukio
alilolishudia. Suala la kutafutwa na wauaji hakuliogopa lakini mawazo yake yalimtuma kuhakikisha haki inatendeka juu ya wauaji.
* * * *
Mara baada ya kukamilisha mauaji ya James na mkewe, Jackson na wenzake pamoja na kundi la vijana wa mr. Tyoso waliondoka eneo la tukio na gari zao kwa kasi kubwa.
Wakiwa wametembea kilomita moja Tyoso
aliamua kutoa wazo la kutupwa miili ya watu hao waliokuwa wameuawa katika maji ya mto Tana na waliamua kutekeleza zoezi hilo.Gari moja liligeuzwa kurudi eneo la tukio likiwa na Jackson pamoja na vijana watano wa mr Tyoso, mara baada ya kufika eneo la tukio walifanikisha kutupwa kwa miili ya
James na mkewe katika maji ya mto Tana nahatimaye safari ilianza wakirudi eneo
walilowaacha wenzao.
 
Sehemu ya 7

Mara baada ya kufika eneo la tukio
walifanikisha kutupwa kwa miili ya James na
mkewe katika maji ya mto Tana na hatimaye
safari ilianza wakirudi eneo walilowaacha
wenzao.
Walipofika walianza safari ya kuelekea
Machakos eneo waliloziacha familia zao,
majira ya saa nane usiku walifika eneo hilo
na Jackson alichukuwa jukumu la kumlipa
mr. Tyoso alyesaidia kufanikisha mauaji hayo
akiwa na kundi lake. Mara baada ya tukio
hilo mr Tyoso aliondoka akiwa na kundi lake
katika hoteli hiyo waliokuwa wamefikia.
“sasa mmeona watu wangu kazi imeisha na
utajiri ule ni wetu” alisikika Jackson mara
baada Tyoso kuondoka na kundi lake.
“mwache aende kuzimu mtu gani anamikiki
nusu ya hisa za kampuni” aliongezea Hamis
jambo hilo, wote walikumbatiana na
kupongezana na walirudi katika vyumba vya
familia zao kama vile walitoka kwenye kikako
kirefu cha kampuni.
Siku iliyofuata kama ilivyopangwa ilikuwa na
siku ya kuanza safari ya kurudi nchini
Tanzania, asubuhi kilifanyika kikao cha
safari hiyo. Jackson aliwaeleza wanafamilia
hao kuwa James na mkewe walikuwa na
mambo ya ziada ya kufanya nchini humo
Kenya hivyo wangerudi Tanzania wiki moja
baadaye. Jambo hilo lilieleweka na safari
hiyo ilianza, siku tatu baadaye walikuwapo
nchini Tanzania.
* * * *
Robert ambaye alikuwa mtoto wa pili wa
James hakufurahishwa na safari iliyokuwa
imeandaliwa dhidi ya kaka yake Geofrey
aliyetakiwa kurudi nchini Tanzania kutokana
na homa za mara kwa mara alizokuwa nazo.
Baada ya maandalizi ya safari ilikuwa
ikisubiriwa siku hiyo wakati Robert akiwa
hayuko tayari kuachana na kaka yake huyo
ambaye pia hakupenda tukio hilo. Siku ya
safari ilipofika Robert akiwa na mwalimu
wake waliondoka shuleni hapo kuelekea
uwanja wa ndege wa Chicago kwa lengo la
kumsindikiza Geofrey. Walikuwa wakilia
wakiwa hawaamini kuwa wangetengana kwa
miezi kadhaa iliyokuwa imebakia kabla ya
likizo.
Hatimaye walifika katika uwanja huo wa
ndege na Robert aliagana na kaka yake na
kuishia kupanda ndege akiwa na mwalimu
wao. Walikuwa wakielekea jimbo la
Washington ambako safari ilitarajiwa kwenda
kuanzia. Robert alirudi shule akiwa na dereva
wa gari hilo la shule ila hakujisikia vizuri
muda wote kutokana na tukio hilo la kuagana
na kaka yake. Alijipa matumaini akiamini
angerudi Tanzania wakati wa likizo yake
ndefu jambo lililomfanya ajipe moyo wa
kubaki shuleni hapo kuendelea na masomo
yake.
Hatimaye majira ya saa moja jioni Geofrey
alikuwa akiagana na mwalimu wake tayari
kwa safari ya kurudi Tanzania. Ndege
aliyopanda ilikuwa ikitarajiwa kupita katika
bara la Amerika ya kusini katika jimbo la Rio
de Jeneiro nchini Brazil kabla ya kupita
Uingereza na mwishoe Afrika. Geofrey
alielezwa kuwa taratibu zote za mapokezi
yake zilikuwa zimeshakamilika na
angepokelewa mara baada ya kufika
Tanzania. Safari ya ndege hiyo ilianza mara
baada ya muda uliopangwa kutimia, Geofrey
mtoto wa miaka kumi alikuwa akiona mwisho
wa kuyaona maghorofa ya kifahari ya nchi
hiyo ulifika.
Aliamini angeikumbuka sana Marekani
hususani jimbo la Illinois ambalo alikuwa
akisoma, hiyo yote ilitokana na kuumwa
kwake mara kadhaa akaamua kukubaliana na
kila lililokuwa limetokea.
Mbali na mabegi yake ya nguo yaliyokuwa
yamehifadhiwa eneo la mizigo alikuwa
amebeba begi lake dogo alilokuwa akihifadhi
vitu vyake muhimu. Moja ya vitu alivyohifadhi
humo zilikuwa picha za familia yake ambayo
aliipenda sana, alikuwa na picha zidi ya
ishirini zikiwamo ambazo alikuwapo mdogo
wake Robert.Safari iliendelea kukiwa na kila
raha ambazo siku zote alitambua kuwa
zilikuwa za kawaida katika usafiri huo wa
ndege. Baada ya masaa kadhaa ya safari
hiyo alishtushwa na hali ya mtikisiko ambayo
ndege hiyo ilianza kukumbana nayo. Jambo
hilo pia liliwashtua hata abiria wenzie
waliohofia hali hiyo ya mtikisiko, hakuna
taarifa zozote zilizotolewa na dakika kadhaa
baada ya mtikisiko huo kuzidi. Walitoka
wahudumu wa ndege ambao pia walikuwa na
hofu na walianza kutoa maelezo ya hatari
ambayo ndege yao ilielekea kukumbana nayo.
Walieleza kuwa kila mtu asali kwa imani yake
kwani ndege ilikuwa imepoteza mwelekeo
kutokana na ukungu mzito uliokuwa
umetanda angani. Taarifa hizo ziliwashtua
abiria hao ambao kila mmoja alianza kufanya
jambo lake, wengine walikuwa wakilia, wapo
waliokuwa wakiomba pasipo kumaliza sala
zao kutokana na hofu iliyokuwa imetanda.
Kuna wengine walianza kuzunguka zunguka
katika ndege hiyo ambayo haikuwa na raha
tena kutokana na mtikisiko uliongezeka na
kuwafanya watu wengine washikilie vizuri viti
walivyokuwa wamekalia.
Marubani wa ndege hiyo walikuwa
wamechanganyikiwa baada ya ndege yao
kupoteza mwelekeo walikuwa hawaelewi
walichokuwa wakikifanya kutokana na
ukungu uliokuwa umetanda angani. Katika
harakati zao hizo za kujiokoa walishtushwa
na mlima uliokuwapo umbali mfupi toka eneo
walilokuwapo. Jambo hilo liliwaogopesha na
waliishia kufumba macho baada ya kuamini
haikuwezekana kuukwepa mlima huo wakiwa
tayari kwa lolote ambalo lingetokea.
* * * *
Hali haikuwa shwari katika milima iliyokuwa
eneo la jimbo la New Amsterdam nchini
Guyana bara la Amerika ya kusini kwani
kulikuwa na ajali mbaya ya ndege iliyokuwa
imetokea katika eneo hilo. Askari wa jimbo
hilo walitumia usafiri tofauti kufika katika
eneo hilo lililozungukwa na misitu ambalo
lilitumiwa zaidi na wawindaji. Hali
iliyokuwapo eneo hilo ndiyo iliyowakatisha
tamaa askari hao kwani kulikuwa na miili ya
watu saba tu ambao walikuwa wameokolewa
wakiwa wamejeruhiwa vibaya. Watu wengi
walikuwa wamepoteza maisha katika ajali
hiyo ya ndege iliyokuwa inabeba abiria zaidi
ya mia moja ishirini.
Askari waliwakimbiza hospitali watu
walikuwa wamejeruhiwa vibaya na walikuwa
wakiendelea kuwatafuta watu wengine na
tayari miili ya watu zaidi ya sabini ilikuwa
imepatikana. Ndege hiyo ilikuwa
imesambalatika katika vipande vidogo vidogo
na sehemu yake kubwa ilikuwa imelipuka
kwa kuwaka moto. Mpaka jioni ya siku
iliyofuata zoezi hilo liliendelea kuleta
matuamaini japo kuwa watu wengi walikuwa
wamepoteza maisha. Eneo ambalo ajali hiyo
ilitokea lilikuwa halipitiki kirahisi kutokana na
miti iliyokuwa imebanana sana jambo
lililowachosha sana askari na kuamini huenda
watu waliokuwa katika ndege hiyo tayari
walikuwa wameisha. Ndipo walipohitaji
orodha ya abiria waliokuwapo kwenye ndege
hiyo iliyoonyesha zaidi ya watu saba
walikuwa hawajapatikana. Taarifa za awali
zilizofanywa zilieleza ndege hiyo ilipata ajali
kutokana na ukungu ulikokuwa umetanda
angani siku ya tukio.
Siku tatu baadaye bado miili ya watu wawili
ilikuwa haijapatikana na askari baada ya
kuitafuta kwa muda mrefu walitoa tamko lao
la kuamini miili hiyo ilikuwa imelipuka na
sehemu kubwa ya ndege hiyo. Hatimaye
zoezi hilo lilisitishwa na ndugu wa marehemu
hao walianza kuwasili nchini Guyana ili
kuitambua miili ya ndugu zao waliopata ajali
katika tukio hilo lililojawa majonzi. Viongozi
mbalimbali wa nchini Guyana walitembelea
eneo la tukio lakini pia walikuwapo
waliotembelea mochuari ya hospitali ya mji
mkuu wa nchi hiyo wa Georgetown ambako
miili yote ilihifadhiwa.
Siku iliyofuata aliwasili mwanamke mmoja
mzungu ambaye mara baada ya
kujitambulisha aliongoza eneo ambalo
kulikuwa na watu waliojeruhiwa katika ajali
hiyo.Mara baada ya kumkosa mtu
aliyemtafuta kati ya hao waliokuwa
wamejeruhiwa alianza kutembea kwa haraka
akielekea mochuari huku akilia, alionekana
akiamini mtu huyo alikuwa miongoni mwa
wale waliokuwa wamefariki. Mkononi alikuwa
na picha ya ndugu yake huyo aliyekuwa
akimtafuta, mara baada ya kufika mochuari
alianza kuzunguka kila sehemu ambayo miili
ya watu hao ilikuwa imehifadhiwa.
Alizunguka kwa mara tatu lakini
hakufanikiwa kumwona ndugu yake huyo
jambo lililopelekea aanze kuonyesha picha ya
ndugu yake aliyemtafuta lakini hakuna
aliyemwona mtu huyo.
Baada ya kuona jitihada zake zikigonga
ukuta aliamua kuelekea katika kituo cha
polisi ili kukutana na mkuu wa kikosi
kilichotumika kutafuta miili ya watu hao
waliopatwa na janga hilo la ajali ya ndege.
Huko alijitambulisha kama Lashay na alieleza
kuwa alikuwa akitokea Marekani, alidai
alikuwa akimtafuta mwanafunzi wake
aliyeitwa Geofrey James ambaye alikuwa
safarini kuelekea Tanzania. Mara baada ya
maelezo hayo askari aliyeongoza kikosi cha
kuitafuta miili ya wahanga hao alitoa
masikitiko yake akidai mtu huyo ni mmoja
kati ya wawili ambao miili yao haikupatikana
eneo la tukio.
 
Sehemu ya 8

Mara baada ya maelezo hayo askari
aliyeongoza kikosi cha kuitafuta miili ya
wahanga hao alitoa masikitiko yake akidai
mtu huyo ni mmoja kati ya wawili ambao
miili yao haikupatikana eneo la tukio.
Hiyo ilitokana na taarifa ya majina
waliyopewa na shirika la ndege iliyopata ajali
na baada ya kufanya utambuzi wa miili
waligundua Geofrey ni mmoja ya watu hao
ambao hawakupatikana. Zaidi alitoa maelezo
ya imani yao kuwa Geofrey alikuwa
amepoteza maisha katika ajali hiyo ya
ndege.
Baada ya taarifa hiyo Lashay aliyeeleza kuwa
alitokea shule ya American Academic School
aliondoka katika kituo hicho cha polisi na
kurudi katika hoteli aliyofikia katika jimbo hilo
la Georgetown. Alikuwa na majonzi juu ya
tukio zima la mwanafunzi wake Geofrey
James aliyesoma katika shule yao ambaye
alikuwa akirudishwa Tanzania kutokana na
homa za mara kwa mara. Alikaa jimboni
hapo kwa siku tatu akiamini huenda
angepata taarifa za kupatikana kwa Geofrey
lakini haikuwa hivyo, baada ya kuona hakuna
dalili zozote za mafanikio aliamua kuanza
safari ya kurudi Marekani.
Mra baada ya kufika alitoa taarifa za kila
kitu kilichokuwa kimetokea katika uongozi wa
shule yao na taarifa za kuaminika alizozitoa
zilieleza Geofrey alikuwa amefariki katika ajali
hiyo ya ndege.
Robert James pia alielezwa taarifa hizo
alizozipokea kwa majonzi hali iliyopelekea
aanze kulia muda wote akiwa shuleni hapo.
Mwalimu wao Lashay ambaye awali James
aliwahi kumkabidhi watoto wake ndiye
aliyechukuwa jukumu la kumpeleka Robert
nyumbani kwake akimfariji juu ya tukio hilo.
Uongozi wa shule ulikuwa ukijaribu kufanya
mawasiliano na James ambaye hakupatikana
muda wote katika namba yake ya simu hali
kadharika mkewe alikuwa hapatikani.
Hatimaye waliamua Lashay aongozane na
Robert kurudi Tanzania ili kutoa taarifa
zilizohusiana na kifo cha Geofrey, mikakati
yote ilifanyika na safari hiyo iliandaliwa. Siku
husika ilipofika walianza safari ingawaje
Robert kwa kiasi kikubwa alikuwa
ametawaliwa na mawazo juu ya kifo cha
kaka yake.
Siku ya Jumatatu majira ya saa kumi na
moja jioni Lashay alikuwa ameongozana na
Robert wakitembea kutoka katika eneo la
uwanja wa ndege wa mwalimu Julius
Kambarage Nyerere. Lashay alikuwa na
mabegi kadhaa wakati Robert aliyeonekana
mchovu na alikuwa hajabeba kitu, waliongoza
hadi eneo la lililokuwa na teksi za
kukodishwa na kupata moja wapo. Safari
ilianza kuelekea nyumbani kwao maeneo ya
Masaki ambako Robert aliyekuwa na miaka
saba alikuwa akikukumbuka vizuri, wakati
huo Lashay alikuwa akitizama mandhari ya
Tanzania aliyokuwa akiisikia tu kupitia
vyombo vya habari juu ya utajiri wake wa
maliasili.
Baada ya saa moja walikuwa nje ya geti la
nyumba ya James ambalo lilifunguliwa baada
ya kupigwa honi ya gari hilo walilokuwa nalo.
Mara baada ya kuingia walishtushwa na
kundi la watu waliokuwapo eneo hilo ambao
walionekana walikuwa wakijadiliana jambo.
Robert alishtushwa na kelele za vilio
zilizompokea kutoka kwa majirani kadhaa na
ndugu zake wachache aliowatambua ambao
awali walikuwa wakiwatembelea nyumabni
kwao.
“jikaze mwanangu baba na mama
wamepotea na hivi zimepita wiki mbili”
aliongea mama mmoja aliyemtambua kama
shangazi yake. Taarifa hizo zilimshtusha
zaidi Robert ambaye alianza kulia kwa sauti
na mwishoe aliishia kupoteza fahamu
walimchukua na kumpeleka katika miti ya
kupumzika iliyokuwa na kivuli na kuanza
kumpepea. Mwalimu wake Lashay ambaye
alikuwa ameongozana naye hakutambua
chanzo cha kupoteza fahamu kwa Robert
kwani hakuelewa kitu. Alikaribishwa na
mwanamme wa makamo aliyejitambulisha
kwa jina la Jackson ambaye alidai awali
walimiliki pamoja na James kampuni ya
JAJHO Company Limited. Alimweleza Lashay
kila kitu kilichohusiana na mazingira ya
kupotea kwa James akiwa na mkewe nchini
Kenya. Zaidi alidai mchakato wa kutafutwa
kwao ulikuwa ukiendelea, Lashay naye
alieleza kuhusiana na kifo cha Geofrey
aliyekuwa mtoto wa James. Jackson
aliwatangazia watu wote waliokuwapo
nyumabni hapo kuwa James aliyeaminika
kuwa huenda alikuwa ameuawa na mkewe,
pia mwanaye alikuwa amefariki katika ajali
ya ndege iliyotokea nchini Guyana. Taarifa
hizo ziliangua vilio vya watu waliokuwapo
eneo hilo zaidi majirani ambao walimtambua
vizuri mwanae huyo wa James.
Siku tatu baadaye wakiwa wanaendelea
kusubiri jitihada za vyombo vya habari na
polisi ambao walikuwa na taarifa za kupotea
kwa James, ndugu zake waligundua jambo
lililowafanya waondoke nyumbani hapo
kimyakimya. Waligundua Jackson
aliyesimamia zoezi hilo la kutafutwa kwa
James na mkewe ambaye pia alikuwa mmoja
wa wamilikiwa JAJHO Company Limited
alikuwa ni mtoto wa marehemu Mzee Samola
aliyekufa kwa kunyongwa. Hisia za kulipizwa
kisasi ziliwajia na hofu zaidi ilitanda juu ya
uhai wao walimwacha Lashay aliyedai
alihitajika kurudi Marekani na Robert ambaye
ada aliyolipiwa ilikuwa ni ya miaka mitatu na
zaidi msimu wa masomo ulikuwa haujaisha.
Lashay alihisi jambo juu ya tukio hilo la
ndugu zake na James kuondoka wakati
taratibu za kumtafuta ndugu yao zikiwa bado
zinaendelea.
Siku iliyofuata hata majirani wachache
ambao walikuwapo nyumbani kwa James
kwa muda siku kadhaa wakisubiria taarifa
zozote zilizomhusu na mkewe waliamua
kuondoka. Jambo hilo lilimshangaza Lashay
ambaye alibaki na Robert sambamba na
wafanyakazi wawili waliokuwapo nyumbami
hapo. Majira ya saa saba mchana Jackson
alifika na watu kadhaa na kumwita Lashay
kando na kumweleza kuwa jambo lililokuwa
likifuata wakati huo ni uuzaji wa nyumba ya
James. Alimweleza kuwa James alikuwa
akidaiwa na kampuni yake ya JAJHO na
kulikuwa hakuna njia nyingine ya kulipa deni
hilo zaidi ya kuuza nyumba yake iliyokuwapo
baada ya kupotea kwake. Zaidi alidai kuwa
hata hati ya nyumba hiyo ilikuwa mikononi
mwao kama dhamana ya deni alilokuwa nalo.
Mnada wa nusu saa ulifanyika na nyumba
hiyo iliuzwa, waliamriwa wahakikishe
wametoka katika nyumba hiyo ndani ya
masaa matano.
Lashay alizidi kuchanganyikiwa na zaidi ni
Robert aliyemshangaa mr Jackson kwa
maamuzi yake, alikuwa akimtambua kama
mjomba kutokana na biashara aliyofanya na
baba yake lakini aligundua ukosefu wa utu
wa mjomba huyo. Hilo lilitokana na
kutowajalia kwani hakuzingatia ni wapi
wangelala siku hiyo zaidi aliondoka na watu
waliokuwa wamenunua nyumba hiyo wakiwa
wamepewa agizo la kuondoka kwao. Lashay
hakuwa na la kufanya zaidi ya kuchukuwa
mizigo yake hali kadharika Robert alichukuwa
mizigo yake. Aliamua kuwalipa wafanyakazi
ambao walikuwa wakifanya kazi nyumbani
hapo kwa James kwa vile walionekana
kutokuwa na mwelekeo na jambo lililofuata
hakujua kwani hakuwa na mawasiliano
yeyote na ndugu zake James.
Aliamua kupanga katika nyumba ya kulala
wageni akiwa na Robert aliyekuwa
amechanganyikiwa juu ya kila kitu
kilichokuwa kikiendelea katika familia yake.
Lengo kubwa la Lashay lilikuwa ni kuvuta
subira akiamini huenda James na mkewe
wangepatikana. Baada ya kutopatikana
mafanikio yeyote ndani ya siku tatu aliamua
kuanza safari ya kurudi Marekani akiwa na
Robert, hisia za mauaji dhidi ya James na
mkewe zilianza kumwingia. Nafsi yake ilikuwa
ikimtuma kuwa mtu ambaye huenda alihusika
na mauaji hayo ni Jackson hiyo ilitokana na
kukosa utu na kuonyesha ukatili wake
waziwazi. Tayari aliingiwa na hisia akiamini
alikuwa na kazi juu ya Robert ambaye
hakuwa na msaada kwa wakati huo.
* * * *
Jeshi la polisi nchini Kenya lilikuwa na taarifa
juu ya kupotea kwa watanzania wawili mtu
na mkewe wakati wakiwa katika ziara yao
binafsi. Taarifa hizo ndizo zilizowafanya
polisi kadhaa waanze upelelezi juu ya tukio
zima la kupotea kwa watu hao, wiki moja
baadaye kulikuwa hakuna dalili zozote za
kupatikana kwa watu hao jambo lililopelekea
askari hao waachane na upelelezi wao. Wiki
ya nne tangu kupotea kwa watu hao polisi
walipata taarifa za kupatikana miili ya watu
wawili kando ya mto Tana katika eneo la
Burra ikiwa imeharibika vibaya. Taarifa za
awali zilidai watu hao walikuwa ni
mwanamke na mwanamme ambao
walibakiwa na mifupa kwa kiasi kikubwa
kutokana na muda mrefu waliokuwapo
majini.
Miili hiyo ilichukuliwa mpaka jijini Nairobi
kwa uchunguzi zaidi, askari hao walituma
taarifa kwa askari wa Tanzania wakihitaji
vielelezo zaidi juu ya James na mkewe
ambao walikuwa wakitafutwa hadi muda
huo. Hiyo yote ilitokana na kutokuwa na
taarifa zozote za kupotea au kuuawa kwa
raia wa nchi hiyo, siku mbili baadaye
walipokea vielelezo zaidi vilivyomuhusu
James na mkewe na mwishoni uchunguzi
ulibainisha kuwa watu waliouawa walikuwa ni
wenyewe.
 
Sehemu ya 9

Siku mbili baadaye walipokea vielelezo zaidi
vilivyomuhusu James na mkewe na mwishoni
uchunguzi ulibainisha kuwa watu waliouawa
walikuwa ni wenyewe.
Taarifa hizo zilitumwa kwa jeshi la polisi
nchini Tanzania juu ya James na mkewe
waliopatika wakiwa wameuawa. Jeshi la
polisi lilitoa taarifa kwa kampuni ya JAJHO
juu ya kupatikana kwa mwili wa James na
mkewe na liliwahitaji wahusike na taratibu
zote za mazishi.
Jackson alitoa taarifa kwa wazazi wa mke
wa James akiwaeleza juu ya kupatikana kwa
maiti ya mwanao lakini hakufanya hivyo
katika familia ya James ambayo alielewa
ilijua juu ya kila kitu kilichoendelea. Kitendo
cha ndugu zake hao kuondoka bila kuaga
katika nyumba ya James aliamini kilitokana
na kugundua kwao ugomvi uliokuwapo baina
ya familia zao mbili za marehemu mzee
Kibudo na Samola ambaye alikuwa baba
yake. Aliondoka na wamiliki wenzie wa
kampuni sambamba na ndugu kadhaa wa
mkewe James kwa usafiri wa ndege
wakielekea jijini Nairobi. Lengo lake alihitaji
ahakikishe James na mkewe wanazikwa
nchini Kenya, japo kulikuwa na maswali
mengi juu ya vifo hivyo lakini aliamini hakuna
mtu ambaye angeliweza kutegua kitendawili
cha vifo hivyo.
Mara zote alionyesha huzuni juu ya tukio hilo
lakini moyoni alikuwa na furaha kupindukia,
alikuwa amefanikiwa kuwafukuza watu
waliokuwapo nyumbani kwa James akiwamo
mtoto wake. Alifanya hivyo akijifanya anaiuza
nyumba hiyo kwani aliamini hakuna ndugu
ambaye angethubutu kuifuatilia. Hilo
lilijidhihirisha wazi kwani hata vyombo vya
habari vilitangaza juu ya kupatikana mwili wa
James na mkewe lakini hofu ya ndugu zake
iliwafanya asijitokeze hata mmoja. Hatimaye
walifika nchini Kenya na mara baada ya
kuishuhudia miili ya James na mkewe
walipewa kibali cha kuizika. Amos ambaye
alikuwa miongoni mwa wamiliki ya kampuni
yao alijifanya akitoa wazo la kuizika miili hiyo
nchini humo. Alitoa mtazamo wake juu ya
mazishi ya watu hao ambayo yalipaswa
kufanyika katika kijiji cha James lakini
hakuna ndugu yeyote aliyefika kwa ajili ya
kufanikisha zoezi hilo.
Hilo lilikuwa ni wazo lao toka awali na
hawakutaka kurudi na miili hiyo nchini
Tanzania wakihofia maswali mengi na zaidi
uchunguzi ambao ungejitokeza. Waliwaeleza
ndugu zake na mkewe James kuwa kampuni
yao ilikuwa na matatizo ya kifedha wakati
huo hivyo kupunguza gharama katika miili
hiyo iliyokuwa ikizidi kuharibika waliomba
waizike hapohapo nchini Kenya. Jambo hilo
lilikubalika ingawaje kwa shingo upande na
miili hiyo ilizikwa katika eneo walilopewa
kibali cha kuzika. Jeshi la polisi lilidai kuwa
liliendelea na uchunguzi juu ya watu
waliokuwa wakihusika na mauaji hayo kwa
namna moja au nyingine. Jackson na wenzie
hawakuwa na hofu na walisisitiza kuwa
walihitaji jeshi la polisi lifanye kazi yake kadri
liwezavyo ili watuhumiwa wakamatwe.
Walieleza hayo kwa vile walielewa hakuna
mtu mabaye angeweza kutambua tukio zima
la mauaji ya James na mkewe.
Baada ya siku tano safari ya kurudi Tanzania
kwa usafiri wa ndege iliandaliwa na siku
iliyofuata walitakiwa kuwa safarini wakirudi.
Jackson na wenzie waliona huo ulikuwa
muda muafaka wa kumwachia kazi mr.
Tyoso ambaye walishirikiana kufanikisha
mauaji ya James na mkewe ili afuatilie zoezi
la upelelezi huo. Walifanya hivyo katika hali
ya kujihami lakini aslimia zote walizokuwa
nazo waliamini hakuna mtu aliyeshuhudia
mauaji hayo. Baada ya makubaliano hayo
hatimaye siku iliyofuata walianza safari
wakirudi Tanzania wakiamini hakuna jambo
lolote ambalo lingeweza kujitokeza. Mr.
Tyoso aliipokea kazi aliyopewa na wateja
wake na kuwahakikishia kuwa siri hiyo
isingeweza kuvuja.
Kwa vile mtandao wake wa ujambazi ulikuwa
mkubwa na alikuwa akishirikiana na askari
kwa kiasi kikubwa aliamua kuongea na askari
kadhaa ili wafuatilie kwa karibu kila
kilichoendelea katika upelelezi huo. Kila siku
nyakati za jioni alikuwa akiwapigia simu
askari aliyokuwa amewaachia kazi hiyo na
kuwauliza jambo lililokuwa likiendelea na
hakupata taarifa yeyote iliyotoa hofu ya
kuvuja kwa siri hiyo.Baada ya siku chache
wakati upelelezi huo ukiendelea alisikia simu
yake ikiita na aligundua mtu aliyepiga
alikuwa ni askari aliyempa jukumu la
kufuatilia kwa karibu upelelezi wa mauaji
ulioendelea. Wakati huo ilikuwa yapata saa
tano na nusu usiku “haloo mr. Tyoso kuna
jambo limejitokeza mkubwa” alisikika askari
huyo mara baada ya simu yake kupokelewa
“jambo gani hilo?” aliuliza Tyoso kwa
mshtuko
“kuna mtu anadai ana filamu ya mauaji ya
James na mkewe na ataileta kituo cha polisi
kesho”. Baada ya kusikia hayo Tyoso
alishtuka zaidi akiwa haamini juu ya jambo
hilo aliloelezwa, alimwomba askari huyo
afuatilie nyendo za mtu huyo haraka na zaidi
alihitaji jina na namba yake ya simu.
Alipatwa na mawazo ghafla na hakutaka
kuwaeleza wateja wake juu ya jambo hilo
lililokuwa linaendelea aliamini hakuna kitu
ambacho kingeweza kufanikiwa. Aliwaza
kuhakikisha filamu hiyo haifiki kituo cha
polisi na zaidi mtu aliyekuwa na filamu hiyo
alihitaji auawe kwa vile alikuwa na uwezo wa
kuitoa siri hiyo muda wowote. Dakika kumi
baadaye ujumbe mfupi wa maneno uliingia
katika simu yake na mara baada ya kuusoma
aligundua ulitoka kwa askari ambaye alikuwa
amempigia simu. Alikuwa amemtumia namba
ya simu na jina la mtu huyo aliyedai kuwa
alikuwa na filamu ya mauaji aliyeitwa George
Johnson.
Bila kupoteza muda Tyoso alichukua simu
yake na kumpigia mtu huyo akimweleza kuwa
alikuwa askari wa upelelezi aliyehusika na
uchunguzi wa mauaji ya James na mkewe.
Alimweleza aliihitaji filamu hiyo ya mauaji
usiku huo kwani ilikuwa ni muhimu sana
kutokana na maagizo waliyopewa na mkuu
wa upelelezi. Walielewana vizuri na baada ya
Tyoso kuelekezwa eneo ambalo George alishi
alianza kijiandaa kwa ajili ya kumfuata.
Jambo kubwa alilolihitaji kwa mtu huyo ni
uhai wake na kikubwa zaidi ni filamu
aliyoelezwa ilikuwa na mauaji ya James na
mkewe. Aliiandaa bunduki yake na kuweka
risasi za kutosha akiamini jambo lilofuata
lilikuwa ni mauaji, aliiweka katika koti lake
kubwa alilovaa na kufanya mtu asiweze
kugundua kirahisi kuwa alikuwa amebeba
bunduki. Alivaa miwani yake iliyopoteza
mwonekano wake wa sura na alipanda
pikipiki yake na kuanza safari kuelekea eneo
alilokuwa ameelekezwa.
George alikuwa amepata taarifa zilizohusiana
na kuokotwa kwa miili ya watu wawili
waliokuwa wameuawa ambao aliamini taarifa
zao alikuwa nazo kupitia filamu ya dakika
ishirini na tano aliyofanikiwa kuipata katika
mauaji hayo. Jambo lililomuogopesha ni
ushauri ambao awali alipewa na mjomba
yake kuwa asitoe siri kama hiyo akidai
lazima angefanyiwa jambo baya. Baada ya
kufikiria kwa siku kadhaa aliamua kufikia
uamuzi wa kutoa siri hiyo, kufanikisha hilo
siku moja majira ya saa nne usiku alipiga
simu kituo cha polisi na kueleza juu ya filamu
ya mauaji aliyokuwa nayo. Alielezwa aipeleke
siku iliyofuta na masaa kadhaa baadaye
aligiwa tena simu akielezwa filamu hiyo
ingefuatwa usiku huo na mtu aliyekuwa
askati wa upelelezi. Hakuwa na pingamizi juu
ya jambo hilo alikuwa akimsubiri mpelelezi
huyo aifuate filamu hiyo ya mauaji
aliyoyashuhudia.
Nusu saa baadaye mlango wa geti la nyumba
yake aliyoishi peke yake uligongwa ilikuwa
nyumba ambayo hata shughuli za uandaaji
wa filamu alizifanyia humo mara baada
kupiga picha sehemu tofauti. George
alisimama na kuanza kutembea taratibu
akielekea getini akiwa na imani kuwa mgeni
aliyekuwa amegonga geti lake alikuwa askari
mpelelezi. Mara baada ya kufungua geti mtu
huyo aliingia akiwa na pikipiki yake na
kuiegesha mbele ya nyumba hiyo ya George.
“samahani kwa muonekano wangu, kazi hii
inatuhitaji tuwe makini sana”aliongea
mpelelezi huyo kama alivyo jitambulisha
awali kwenye simu. “usijali karibu….” Ajibu
George ambaye kwa kiasi alianza kuonyesha
hofu na mgeni wake huyo. Mara baada ya
kuingua ndani walianza kuongea mambo
tofauti mbali na lile kubwa lililohusu filamu
ya mauaji. Wakati huo mgeni wake alikuwa
amevaa miwani ambayo haiku mwonyesha
vizuri sura yake, baada ya dakika kadhaa
mtu huyo alitoa miwani yake na sura yake
ndiyo ilimuongeza hofu zaidi na kuanza
kuingiwa na mawazo kuwa hakuwa askari.
Alimfananisha na mtu mmoja ambaye
alikuwapo kwenye tukio la mauaji ambayo
aliyashuhudia kwa macho yake. Jambo hilo
ndilo lilimfanya amuulize swali huku akiwa
na uoga. “samahani askari kabla ya yote,
naweza kukiona kitambulisho chako cha
kazi?” aliuliza George ambaye hakujiamini.

ITAENDELEA....
 
Sehemu ya 10

“Samahani askari kabla ya yote, naweza
kukiona kitambulisho chako cha kazi?”
aliuliza George ambaye hakujiamini.
Mtu huyo alisimama na kuelekeza mkono
wake kwenye koti lake kubwa alilokuwa
amevaa alitoa bunduki na kuielekeza kwenye
paji lake la uso wa George ambaye
alichanganyikiwa ghafla. “hiki ndiyo
kitambulisho changu, sasa mimi siyo askari
sihitaji chochote toka kwako zaidi ya kila kitu
kinachohusiana na mauaji uliyoyashuhudia”
alisikika mtu huyo akiwa ametoa macho. Kwa
uoga George alianza kutembea mpaka
kwenye chumba alichokuwa akiandalia filamu
hizo na alikuwa akifuatwa nyuma na mtu
huyo. Mara baada ya kuingia kwenye chumba
hicho aliitoa filamu iliyokuwa na mauaji
aliyoyashuhudia na kuikabidhi ikiwa
imeandikwa juu yake ‘MAUAJI’. “bado
sehemu gani nyingine kuna picha za hii
filamu” alisikika mtu huyo kwa ukali na
kumfanya George ampe kamera yake
aliyokuwa akipigia picha akidai picha hizo
hazikufutwa kwenye hiyo kamera.
Mara baada ya kuchukua vitu hivyo
alimumiminia risasi tatu George tumbomi na
kumfanya aangue huku damu nyingi
ikimtoka. Mtu huyo aliye jitambulisha kama
mpelelezi ambaye hakuwa mwingine bali ni
mr. Tyoso aliichukua kamera na filamu hiyo
na kuviweka katika boksi moja lililokuwa na
filamu nyingine. Mawazo yake yalimtuma
akiamini kuwa filamu hiyo ilikuwa
imehifadiwa sehemu nyingi hivyo ingekuwa ni
rahisi kupatikana tena. Alizipiga risasi
kompyuta tatu zote zilizokuwapo katika
chumba hicho akiamini zilitunza filamu hiyo.
Wakati akifanya hayo yote George alikuwa
akitupatupa mikono na miguu baada ya
kupigwa risasi, tayari damu nyingi ilikuwa
imemtoka.
Mr. Tyoso aliondoka kwa kasi eneo hilo la
nyumba ya George akiwa na boksi alilobebea
filamu zote alizoziona katika kile chumba
pamoja na kamera. Aliendesha pikipiki yake
akiamini alikuwa amefanikisha ushindi wa siri
hiyo iliyokuwa inataka kuvuja. Jambo ambalo
bado lilikuwa linamuumiza kichwa ni
kuhusiana na filamu hiyo alihisi ilikuwa
haihusiani na mauaji waliyokuwa
wameyafanya. Kumbukumbu zake zilimpa
aslimia chache na filamu hiyo jambo
alilokuwa akilisubiria kwa hamu lilikuwa ni
kuiona filamu hiyo kama ni kweli ilikuwa
ikihusiana na mauaji waliyokuwa
wameyafanya na wateja wake.
Saa nane kamili usiku aliwasili nyumbani
kwake na kabla ya yote alianza kuiangalia
filamu hiyo, baada ya dakika tatu tu za
kuiangalia alisikika akiongea peke yake
“Mungu wangu alituonaje mbwa huyu” .
Alishangazwa na filamu hiyo ambayo
aligundua ilionyesha kila kitu walichofanya
siku ya mauaji. Haraka aliamua kuanza
kuangalia filamu nyingine ambazo nazo
alikuwa amezichukua, alishuhudia sherehe za
harusi na nyingine ikiwamo misiba na filamu
moja ilikuwa ikionyesha vyura wa aina
tofauti. Baada ya muda mfupi wa kuziangalia
kwa haraka pasipo kumalizia aliigeukia
kamera ambayo aliweza kukutana na picha
nyingine za mauaji alizokuwa amezishuhudia.
Aliichukua filamu hiyo pamoja na kamera
kisha akavichoma usiku huohuo, hakutaka
kubakia na kumbukumbu za mauaji hayo
ambayo na yeye alihusika akihofia usalama
wake na wateja aliowafanyia kazi hizo.
Filamu nyingine aliziacha kwani aliona
zilikuwa hazina jambo lolote la hatari kwa
usalama wao mara baada ya zoezi hilo
alichukua simu na kumpigia Jackson. Ilikuwa
yapata saa tisa usiku lakini aliona umuhimu
wa mteja wake huyo kujua jambo ambalo
lilitaka kuwatokea. Alipongezwa sana kwa
kazi hiyo aliyokuwa ameifanya zaidi Jackson
alishtushwa na taarifa hizo za kuwa kulikuwa
na mtu aliyewafuatilia siku ya tukio la mauaji
waliokuwa wameyafanya. Alimuahidi Tyoso
kumtumia fedha siku iliyofuata kama pongezi
juu ya zoezi hilo alilokuwa amelifanya.
* * * *
Mzee Rogart alikuwa miongoni mwa raia
masikini walioishi nchini Guyana, alikuwa
mkazi a jimbo la New Amsterdam aliyefanya
shughuli kuu ya uwindaji pembezoni mwa
mlima ambao kulitokea ajali ya ndege. Katika
maisha yake mzee Rogart alikuwa na mke na
watoto wawili ambao walikuwa
wamemkimbia miaka kadhaa iliyokuwa
imepita, walimwacha porini huko kutokana na
ugumu wa maisha ambayo hawakuyaweza.
Mzee Rogart alikuwa wa kwanza kufika
katika eneo la ajali hiyo ya ndege na
kushuhudia ajali hiyo, jambo alilolifanya siku
hiyo ya tukio alimckukua mtoto mmoja
aliyekuwa amejeruhiwa vibaya kutokana na
ajali hiyo na alimpeleka mpaka nyumbani
kwake akiwa na lengo haswa la kumtibu na
hatimaye aanze kuishi naye.
Aliamini hilo lingewezekana kutokana na vifo
vya watu wengi vilivyokuwa vimetokea eneo
la tukio na aliamini mtoto huyo naye
angedhaniwa alifariki. Alikuwa akihitaji kuwa
na mtoto kwa vile mkewe na watoto wake
wawili waliokuwa wamemtoroka, walimpa
imani iliyomkaa kichwani kuwa hawangerudi
tena. Alianza kumtibu mtoto huyo kwa
majani ya porini ambayo aliyatambua kama
dawa kutokana na maisha ya miaka mingi
aliyokuwa akiishi porini huko. Wakati
akifanya hayo kila siku alikuwa akienda eneo
ambalo ajali ya ndege hiyo ilitokea na
kujumuika na askari waliotafuta miili ya watu
waliokuwa wamefariki. Hatimaye zoezi lao
lilikamilika pasipo kugundulika kuwa alimwiba
mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo. Alikuwa
akiishi umbali wa kilometa zaidi ya saba toka
eneo ambalo ajali ilitokea, muda wote
alikuwapo nyumbani kwake akisubiri kwa
hamu mtoto aliyekuwa amemwokota arudiwe
na fahamu.
Alikuwa amevunjika mkono na mguu akiwa
amepatiwa matibabu ya kufungwa vizuri na
miti midogo midogo iliyoenda sambamba na
maeneo aliyokuwa amevunjika. Mtoto huyo
pia alikuwa na majeraha mengi sehemu
tofauti za mwili wake, suala lililomuumiza
kichwa mzee Rogart lilihusiana na kuchelewa
kuzinduka kwa mtoto huyo aliyekuwa na
shauku ya kumfahamu. Alipunguza kasi yake
ya uwindaji na muda mwingi alikuwapo
nyumbani kwake hapo akihakisha mtoto huyo
anakuwa salama. Hakufanikiwa kupata
vielelezo vyovyote vilivyohusiana na mtoto
huyo zaidi ya picha akiwa na wazazi wake
ambazo alizipata kwenye begi pembeni
kidogo ya eneo ambalo alimchukua. Baada
ya siku nne tangu kuchukuliwa kwa mtoto
huyo toka eneo la ajali hatimaye alizinduka
akiwa anashangaa eneo alilokuwapo na mtu
aliyekuwa na ndevu na nywele nyingi zenye
mvi. Kilichomshangaza zaidi ni eneo hilo la
porini ambapo pia nyumba aliyokuwapo
ilijegwa kwa miti na kuezekwa kwa majani.
Hakuna jambo ambalo walielewana na mzee
Rogart aliyezungumza lugha ya Hindu zaidi
waliweza kutambuana majina.
Rogart alifurahishwa na kuzinduka kwa
mtoto huyo aliyebaini alikuwa raia wa
Tanzania ambaye pia aliitwa Geofrey,
aliendeleza matibabu yote aliyokuwa
akiyafanya kwa mtoto huyo na hatimaye
alipona baada ya miezi mitatu. Tayari alianza
kuifahamu lugha ya Hindu aliyokuwa
akiitumia, mara kadhaa Geofrey alionyesha
nia ya kutaka kurudi Tanzania ila alipoelezwa
nchi ambayo walikuwapo alikatishwa tamaa
kabisa. Hiyo ilitokana na imani aliyokuwa
nayo kuwa ingekuwa vigumu kwake kuondoka
eneo hilo na kumfanya aanze kujifariji kuwa
hayo yalikuwa makazi yake mapya. Suala la
shule lilikuwa limepotea kabisa kichwani
mwake, ingawaje hakuwahi kutembea na
kukutana na watu wengi zaidi ya wawindaji
wachache waliokuwa wakikutana mara
kadhaa porini. Chakula chao kikubwa ilikuwa
nyama na wakati huo alikuwa mwindaji mzuri
akishirikiana na mzee Rogart ambaye
alimpenda sana. Hakuthubutu kuisahau
familia yake na alikuwa akizitizama picha za
familia yake hiyo kila siku akiwa anaamini
miujiza pekee ndiyo iliweza kumkutanisha
tena na familia yake.
Baada ya miaka mitano akiwa tayari na
miaka kumi na tano alikuwa amepata mambo
tofauti kutoka kwa mzee Rogart aliyekuwa na
historia iliyojaa mikasa. Moja ya mambo
aliyoyatambua toka kwa mzee huyo ambaye
miaka ya nyuma alikuwa jambazi wa kutisha
lilihusiana na mauajia aliyowahi kuyafanya
dhidi ya mke wa rais wa nchi hiyo ya
Guyana. Alimweleza miaka kumi na tano
iliyokuwa imepita mzee Rogart akiwa jambazi
wa kutisha nchini humo alipewa jukumu na
chama cha upinzani cha nchi hiyo cha DPG
‘Democratic Part of Guyana’ la kumuuwa rais
wa nchi hiyo aliyeitwa Zakheem Pirjah.
Alikubaliana na kazi hiyo baada ya kupewa
fedha za kutosha na siku ya tukio
alisababisha ajali iliyomuua mke wa rais.
Msako mkali ulifanywa wa kutafutwa kwake
na rais huyo ambaye mpaka wakati huo
alikuwapo madarakani akitumia ubabe. Alidai
wakati huo alikuwa na umri wa miaka
arobaini na tano, hivyo baada ya kuona
mambo yalikuwa magumu aliamua kukimbilia
porini hapo akiwa na familia yake. Aliacha
mazoea aliyokuwa nayo ya kunyoa nywele na
muda wote alikuwa na nywele ndefu
zilizopoteza mwonekano wa sura yake.

ITAENDELEA...
 
Sehemu ya 11

Aliacha mazoea aliyokuwa nayo ya kunyoa
nywele na muda wote alikuwa na nywele
ndefu zilizopoteza mwonekano wa sura yake.
Aliishi na familia yake kwa muda mfupi porini
hapo wakiwa hawajui mauaji hayo
aliyoyafanya kwa mke wa rais zaidi ya vile
walivyomtambua kuwa alikuwa jambazi.
Baada ya kuona maisha ya porini yalikuwa
magumu mkewe na watoto wake waliamua
kuondoka na hawakuwahi kurudi tena porini
hapo. Geofrey alishtushwa na historia hiyo
ambayo mwishoe aliichukulia kama kitu cha
kawaida kutokana na heshima aliyokuwa
ameijenga kwa mzee Rogart akimchukulia
kama mzazi wake. Muda wote wakiwa porini
hapo katika shughuli za uwindaji walikuwa
wakitembea na bunduki ambayo waliitumia
siyo katika uwindaji tu bali ilitumika kama
tahadhari ya usalama wa mzee Rogart
aliyeamini rais wa nchi hiyo Zakheem
alikuwa akimtafuta. Mara kadhaa pia
walikuwa wakikumbana na wanyama wakali
kama Simba hivyo waliitumia kujiokoa.
Walikuwa wakipata risasi kwa kununua kwa
wawindaji wengine ambao walikuwa hawaishi
porini huko na hivyo ndivyo walivyoendeleza
maisha yao. Siku moja Geofrey aliondoka
peke yake akimwacha mzee Rogart aliyekuwa
na homa nyumbani hapo. Alikuwa akifuatilia
mitego waliyokuwa wameitega dhidi ya swala
na wanyama wengine hususani nguruwe pori
ambao haswa walikuwa nyama yao kubwa
wakiwa porini hapo. Akiwa ametembea
umbali wa kilometa kadhaa toka nyumbani
kwao alishtushwa na askari waliokuwapo
eneo hilo ambao mara baada ya kumwona
walianza kumfuata.
Alikuwa amevaa bukta pekee na kuacha eneo
la juu kuwa wazi zaidi alikuwa hajavaa hata
viatu, begani alikuwa na upinde sambamba
na mishale mingi aliyoishika katika mfuko
mdogo aliokuwa nao.
Alitaka kukimbia lakini alijipa ujasili,
mawazoni alihisi watu hao walitaka
kuwakamata kutokana na uwindaji waliokuwa
wakiufanya. Askari hao walianza
kumshangaa kwa jinsi alivyokuwa amevaa
lakini yeye kwake lilikuwa jambo la kawaida
kwa miaka yote aliyokuwapo porini hapo.
Mara baada ya kumfikia walimsalimia kwa
lugha ya Hindu na hatimaye walitoa picha
wakiashiria kuwa walitaka kumwuliza jambo.
Mara baada ya kumwonesha picha hiyo
ambayo aligundua ilikuwa ya mzee Rogart
moyo wake ulishtuka ingawaje hakuonyesha
hali yeyote ya mshtuko. Walimuuliza kama
alimfahamu mtu huyo au yeyote aliyefanana
naye lakini aliwajibu alikuwa hamfahamu na
hakuwahi kukutana naye porini hapo.
Picha hiyo ilionekana ilichukuliwa miaka
mingi wakati mzee Rogart akiwa hana nywele
nyingi kama alizokuwa nazo wakati huo.
Baada ya majibu hayo polisi hao waliokuwa
sita waliendelea na msako wao dhidi ya mtu
huyo, Geofrey aliamua kuacha zoezi lake la
kufuata mitego waliyokwa wameitega na
kuanza kurudi nyumbani. Mara baada ya
kufika katika nyumba waliokuwa wakiishi
alishtusha na moto mkubwa uliokuwa
ukiwaka ukiwa umeshia nyumba yao.
Pembeni kulikuwa na madumu ya mafuta
aina ya petroli ambayo yalionekana
kuteketeza nyumba hiyo. Alizunguka maeneo
yote ya sehemu hiyo waliokuwa wakiishi
akiwa naimani huenda mzee Rogart alikuwa
ameuawa lakini hakubahatika kuiona maiti
yeyote.
Hisia za kuwapo kwa kundi kubwa la polisi
msituni hapo zilimwingia na kuamini kuwa
mzee Rogart alikuwa amekamatwa. Aliongeza
mishale mingine na wakati huu aliamua
kuchukuwa dawa ambayo walikuwa
wakiipaka katika ncha ya mishale ambayo
ilikuwa ikiwafanya wanyama wapate usingizi
pindi wakiwa mawindoni. Dawa hiyo ya
majani ilikuwa katika kikopo kidogo na
ilikuwa ikiwasaidia kuwapata wanyama hata
kama walichubuliwa kidogo na mishale.
Hakuwa tayari kuishi porini bila mtu
aliyemheshimu kama mzazi wake na
mazingira aliyoyaona eneo la tukio aliamini
askari hao hawakuwa mbali na mzee Rogart.
Aliondoka kwa kasi ya ajabu ambayo ilikuwa
ya kawaida kwake kutokana na shughuli hiyo
ya uwindaji waliyofanya. Aliachana na njia
ambayo awali alikuwa ametokea na kuanza
kufuata njia nyingine na baada ya kukimbia
kwa muda mfupi alifanikiwa kuyaona
makanyagio ya viatu vya kiaskari na hapo
imani ya kukamatwa kwa mr. Rogart ilimkaa
zaidi kichwani.
Akili yake ilimtuma kufanikisha hata mauaji ili
kuhakikisha anampata mzee huyo, alikimbia
umbali wa zaidi ya kilometa thelathini pasipo
mafanikio ya kuwaona askari ambao aliamini
walikuwa wamemkamata mzee Rogart.
Alianza kuingia hofu ya kushindwa
kufanikisha lengo lake la kumuokoa mzee
huyo wakati huo ikiwa jioni, alianza kutembea
taratibu akiamini zoezi hilo lilielekea
kushindikana. Hofu ya kuuawa kwa mzee
Rogart ilizidi kumkaa kichwani na aliamini
rais Zakheem Pirjah wa nchi hiyo asingeweza
kumwacha hata kidogo. Tayari giza liliingia
na hakukuwa na dalili zozote za kuweza
kufanikisha kwake kumwokoa mzee huyo.
Akiwa bado anaendelea kutembea porini
humo huku akiwa amekata tamaa kwa kiasi
kikubwa alishtushwa na chanzo cha moto
kilichotoa moshi karibu na eneo alilokuwa
akitembea wakati huo.
Hisia zake zilimtuma akiamini kulikuwa na
jambo lililokuwa likiendela eneo hilo wakati
huo, japo hakuwashuhudia watu waliokuwapo
kwenye chanzo hicho cha moto lakini aliamini
kuwa ndiyo waliohusika na kukamatwa kwa
mzee Rogart. Alianza kusogelea taratibu eneo
ambalo moto huo ulikuwa ukiwaka huku
akijificha kwenye miti alitaka kuwaona watu
waliokuwapo eneo hilo. Hatimaye alitulia
sehemu na kuweza kuwaona vizuri lakini pia
akishuhudia kila kitu kilichokuwa kikiendelea
eneo hilo. Walikuwa askari wanne waliokuwa
wamezunguka chanzo cha moto kutokana na
baridi iliyokuwapo muda huo, akili yake kwa
haraka ilimpa jibu kuwa hao ndiyo walihusika
na kukamatwa kwa mzee Rogart. Jambo
lililomtatiza hakuweza kumwona mzee huyo
eneo hilo, akaanza kuzungusha macho kila
upande akiwa na lengo la kuhakikisha kama
alikuwapo eneo hilo.
Baada ya muda mfupi alimwona mzee Rogart
kwa umbali akiwa amefungwa kwenye
kwenye mti mkubwa uliokuwa pembeni na
eneo ambalo askari hao walikuwa wakiota
moto. Geofrey alianza kufikiri jambo la
kufanya baada ya kuamini kuwa huo ulikuwa
wakati muafaka wa kumuokoa mzee Rogart.
Alichuchumaa taratibu baada ya kugundua
jambo la kufanya na baada ya kufanya hivyo
alianza kutoa matawi ya miti ambayo
yalikuwa mengi chini ya miti iliyokuwa
imezuguka eneo hilo. Mara baada ya kuyatoa
alipata shimo lililomwezesha yeye kuingia
kwa kiasi kikubwa akiwa ameweka mishale
yake na upinde pembeni kidogo na eneo
alilokuwapo. Alikuwa amebakiwa na mishale
mitatu na dawa ambayo ilileta usingizi pindi
walipokuwa wakifanikiwa kuwadhuru
wanyama.
Mara baada ya kujihakikishia usalama wake
akiwa na mshale mmoja ambao tayari
ulikuwa na dawa kwenye ncha yake alianza
kupiga kelele kama za paka. Alizipiga kelele
hizo kwa sekunde kadhaa na kuwafanya
askari waliokuwapo kwenye chanzo cha moto
washtuke na kuanza kutazama eneo ambalo
kelele hizo zilitoka. Waliacha mazungumzo
yao waliyokuwa wakiyazungumza na kuanza
kuangalia eneo ambalo kelele hizo zilitoka.
Baada ya muda mfupi mmoja wao
aliwaondoa shaka akiwaambia kuwa hakuna
jambo lolote, walikaa tena chini na kuendelea
na mazungumzo yao. Dakika mbili baadaye
walizisikia kelele hizo zikiwa zimeanza tena
jambo lililomfanya mmoja wao achukue
bunduki yake na kuanza kutembea kuelekea
eneo ambalo alisikia kelele hizo. Ghafla
hakusikia tena kelele hizo lakini aliendelea
kutembea akielekea eneo ambalo alikuwa
amesikia kelele hizo zikitoka.
Alitembea mpaka eneo la ndani toka sehemu
iliyokuwa na chanzo chao cha moto lakini
hakuweza kuona kitu na alibaki amesimama
huku akiwa anacheka akiwaeleza wenzake
kuwa hapakuwa na kitu. Wakati huo Geofrey
alikuwa amejifukia chini katika matawi
ambayo askari huyo alikuwa pembeni yake
akiwaeleza wenzie, walikuwa katika eneo
lililokuwa na giza mbali na eneo lenye chanzo
cha moto. Alianza kwa kujitoa kichwa
taratibu na mara baada ya kutoka vizuri kwa
kasi alimchoma yule askari na mshale katika
mguu wake wa kulia, kabla ya kuuchomoa
mshale huo kwa haraka na kurudi tena katika
shimo alilokuwapo. Askari huyo alipiga kelele
akitupa bunduki yake pembeni na kuanza
kujiviringisha kwa maumivu aliyokuwa
akiyapata.
Wenzake walitoka mbio eneo walilokuwapo
na kwenda kumshuhudia damu zikimtoka
katika mguu wake wa kulia, hisia alizozipata
askari huyo alidhani ni nyoka jambo
lililowafanya askari wenzie wambebe mpaka
kwenye chanzo cha moto. Walianza kumpa
huduma ya kwanza kwa kumfunga kamba
eneo la juu na sehemu aliyokuwa amepata
jeraha hilo. Wakati huo kwa kasi akijiburuza
kama nyoka, Geofrey alitoka na kuelekea
eneo alilokuwa ameweka mishale yake na
upinde akiwa amebakiwa na mishale miwili
pamoja na dawa aliyitumia katika zoezi hilo.


ITAENDELEA..
 
Sehemu ya 12

Geofrey alitoka na kuelekea eneo alilokuwa
ameweka mishale yake na upinde akiwa
amebakiwa na mishale miwili pamoja na
dawa aliyitumia katika zoezi hilo.
Alikimbia upande mwingine wa pembeni na
kujilaza akiwa ameshaweka dawa ile
iliyosababisha usingizi katika mshale
mwingine na aliupachika kwenye upinde
tayari kwa kuuachia.
Alielewa kwa vyovyote vile watu hao
wangerudi eneo lile kuangalia nyoka ambaye
alikuwa amemdhuru askari mwenzao.
Aliwasikia wakijadiliana jambo la kufanya
huku wakiwa wamechanganyikiwa, hilo
lilifuata baada ya kuona askari mwenzao
akiwa amepatwa na usingizi wa ghafla.
Walishauriana waendelee na safari ili
wampeleke mwenzao hospitali, lakini umbali
wa kilometa zaidi ya arobaini zilizokuwa
zimebaki kuuacha msitu huo ndizo
ziliwakatisha taama. Mmoja wao aliwaeleza
wenzie kuwa rais Zakheem asingewaelewa
hata kidogo endapo mzee Rogart
angewakimbia, wakati huo mzee huyo
aliangalia kila kilichoendelea.Baada ya
makubaliano hayo waliona wabaki eneo hilo
kutokana na hofu kubwa juu ya mzee Rogart
waliyeamini hakuwa mtu wa kawaida kwa
vile alitafutwa kwa miaka mingi pasipo
kupatikana.
Askari hao waliendelea kumpa huduma
mwenzao aliyepatwa na usingizi wa ghafla
wakiamini alikuwa ameg`atwa na nyoka.
Baada ya muda mmoja wao alianza
kutembea kuelekea eneo lililokuwa limetokea
tukio hilo, mkono mmoja alibeba bunduki na
mwingine alikuwa amebeba ukuni uliokuwa
umeshika moto huku ukiendelea kuwaka.
Mara baada ya kufika eneo hilo aliziona
damu ambazo zilikuwa zimemtoka askari
mwenzao na aliamini eneo hilo alikuwapo
nyoka, aliendelea kuzungusha macho kila
upande wa eneo hilo akijaribu kumtafuta
nyoka huyo. Wakati huo kwa umbali mfupi
katika eneo lililokuwa na giza Geofrey
alimwona vizuri askari huyo aliyekuwa na
ukuni wenye moto ulioangaza vizuri sehemu
aliyokuwapo.
Bila kuchelewa aliivuta kamba ya upinde
wake iliyokuwa na mshale huku akiwa
ameupima sawasawa akielekeza katika mguu
mmoja wa askari huyo. Punde aliachia
upinde huo ulioenda kutua sawasawa kwenye
mguu wa kushoto wa askari huyo na ulizama
kiasi cha kutaka kutoka upande wa pili wa
mguu huo. Alitoka mbio na kuelekea upande
mwingine uliokuwa karibu kabisa na eneo
alilomwona mzee Rogart akiwa amefungwa.
Askari huyo alipiga kelele na kutupa bunduki
na ukuni uliokuwa na moto akiwa ameumia
mguu wake na kuushuhudia mshale
uliompata sawasawa. Kelele hizo ziliwashtua
askari wenzie waliokimbia kuelekea eneo
alilokuwapo na kumwona akiwa amedhuriwa
na mshale huo. Askari mmoja alianza
kumvuta kuelekea eneo ambalo lilikuwa na
chanzo cha moto na mwingine alimua kuzima
moto uliotaka kushika eneo hilo baada ya
ukuni wenye moto kutupwa chini na mara
baada ya kuzima alienda kuungana na
mwenzake. Hisia za nyoka tena ziliwatoka
kichwani mwao na walianza kuingiwa na hofu
kubwa kuwa eneo hilo kulikuwa na adui,
askari mmoja alianza kumpiga mzee Rogart
akimshutumu alihusika na matukio hayo.
Mara baada ya kumtoa mwenzao mshale na
kupunguza kasi ya damu iliyokuwa ikimtoka
wote wawili walishika bunduki zao wakiwa
tayari kwa shari hiyo iliyoendelea. Muda
mfupi mwenzao naye aliingia katika usingizi
mzito, jambo hilo liliwachanganya na kuamini
wenzao walikuwa wanakufa.
Mzee Rogart alionekana kupata faraja kidogo
moyoni akihisi huenda kuna mtu alikuwapo
eneo hilo kumwokoa lakini bado alikuwa
akihofia maadui zake kadhaa wa miaka mingi
iliyokuwa imepita na kuwahusisha na tukio
hilo lililokuwa likiendelea. Mawazo yake hata
kidogo hayakumweka akilini kijana wake
Geofrey aliyemchukulia kama mwanaye
kuhisika na jambo hilo. Askari mwingine
alimfuata kwa mara ya pili na kuanza
kumpiga tena ngumi za tumbo akimtaka
aseme mtu aliyehusika na tukio hilo. Wakati
huo askari mwenzie alikuwa kwa mbali
akizunguka eneo hilo akiwa na tahadhari
kubwa ya usalama wake. Akiwa anaendelea
kumpiga mzee huyo alishtushwa na mshale
uliotua kwa kasi na kupenya sawasawa
katika makalio yake na kumfanya aanze
kupiga kelele kutokana na maumivu
aliyoyapata.
Bunduki aliyokuwa ameishika aliitupa chini
na alianza kujivingisha kwa kelele za
maumivu. Askari mwenzie aliyebakia kwa
kasi alimfuata na kumvutia eneo
walilokuwapo wenzake, aliingiwa na hofu ya
ghafla na imani aliyoipata haraka
ilimbainishia alikuwa katika hatari ya
kupoteza maisha muda wowote.Akili yake
ilikuwa haijatulia hata kidogo akiwa bado
hajagundu jambo la kufanya askari huyo
aliyejeruhiwa aliingiwa na usingizi kama
wenzake. Jambo hilo lilimshtua askari huyo
aliyekuwa amebakia akamua kutoka kwa kasi
akikimbia kuondoka eneo hilo ambalo
wenzake aliamini walikaribia kufariki.
Aliongoza upande ambao walikuwa
wakielekea na mzee Rogart na aliondoka bila
hata kumsemesha jambo lolote akiwa na
hofu kubwa.
Mzee Rogart alikuwa bado katika mti
aliokuwa amefungwa kando kidogo na chanzo
cha moto huku hofu tele ikiwa imemjaa
baada ya askari pekee aliyebakia kukimbia.
Hofu yake ilitokana na mtu huyo
aliyemwokoa alikuwa na lengo gani, zaidi
aliamini hakuwa na mtu yeyote
waliyefahamiana wakati huo ambaye
angeweza kumsaidia. Kilichomtisha zaidi
alikaa dakika kama kumi pasipo kuona dalili
za mtu huyo akitokea, jambo hilo lilimtia hofu
zaidi na alihisi na yeye mwisho wake ulifika.
Akiwa na mawazo tele alishtushwa na mshale
ulitoka kwa kasi ya ajabu upande wa mbele
yake uliokuwa na giza na kutua juu kidogo na
kichwa chake katika mti huo aliokuwa
amefungwa. Hofu yake iliongezeka na hali ya
ketetemeka ilifuata alipogeuza kichwa chake
kuutazama mshale huo alishuhudia wote
ukiwa umezama kwenye mti.
Jambo hilo lilimfanya mzee huyo aanze kulia
peke yake, baada ya kuanza zoezi hilo la
uoga alishtushwa kumuona Geofrey akitoka
katika eneo hilo la miti lililokuwa na giza
huku akicheka juu ya hofu aliyoionyesha.
Mzee Rogart hakuamini macho yake baada
ya kugundua aliyekuwapo eneo hilo alikuwa
ni Geofrey, aliacha kulia akiwa tayari
ametokwa na machozi. Alimfungua haraka
kabla ya kukumbatiana kwao, akili yake
ilimrudia kichwani mzee Rogart na kuamini
kuwa kila kitu alichokiona kilifanywa na
mwanae huyo ambae alimtambua kwa
uhodari wa kutumia upinde na mishale.
Alikuwa hakosi pindi wakiwa katika shughuli
zao za uwindaji, kila mshale siku zote
ulikuwa lazima umpate mnyama. Walichukua
bunduki zote nne za askari hao ikiwamo na
ile ya askari aliyekimbia eneo hilo baada ya
kuingiwa na hofu ya kuuawa walianza
kukimbia kwa kasi kurudi eneo ambalo
lilikuwa na makazi yao. Lengo lao kubwa
lilikua ni kwenda kupanga na kujua jambo
ambalo lingefuata wakati huo.
Mzee Rogart ambaye alikuwa na umri wa
miaka sitini alikuwa akijitahidi kukimbia kama
vile alikuwa kijana mdogo ukimlinganisha na
Geofrey. Tayari ilikuwa imegundulika kwamba
waliishi porini na agizo la kukamatwa kwa
mzee Rogart lilikuwa limetoka kwa rais wa
nchi hiyo Zakheem Pirjah akiwa na
machungu juu ya kifo cha mkewe miaka
kadhaa iliyokuwa imepita. Rais huyo
alionekana alihitaji kwa hamu Rogart
akamatwe akiwa hai na lengo lake lilionekana
kuwa alihitaji kumuua ili kulipiza kisasi katika
kifo alichomsababishia mkewe. Majira ya saa
kumi usiku wakikuwa wamefika eneo
waliloishi huku wakiwa wamechoka sana na
eneo hilo lilikuwa limeungua lote kiasi cha
kukosekana kwa mabaki hata kidogo. Hiyo
yote ilitokana na miti iliyotumika kuijengea
nyumba hiyo na zaidi mafuta ya petroli
ambayo askari waliyatumia kuichoma.
Mzee Rogart alimweleza Geofrey kuwa
alihitaji waelekee jimbo la Linden lililokuwa
eneo la kusini mwa nchi hiyo ya Guyana.
Mawazo yake yalikuwa ni kwenda kutafuta
msitu mwingine katika jimbo hilo ili
wakaendeleze maisha yao kama ilivyokuwa
awali. Hakukuwa na pingamizi kutoka kwa
Geofrey ambaye muda wote alimsikiliza mzee
huyo aliyemchukulia kama mzazi na alikuwa
tayari kufanikisha lolote ili apone.
Kilichomuuma sana ni kuungua kwa
kumbukumbu ya picha zake za familia
alizokuwa akitembea nazo siku zote. Ila
alifarijiwa na mzee huyo aliyempa imani kuwa
siku moja lazima angerudi Tanzania kuwaona
wazazi wake. Waliamua kulala eneo hilo
ambalo lilikuwa na joto kutokana na moto
uliounguza nyumba yao wakiwa
wanapumzika baada ya kukimbia kwa muda
mrefu. Siku iliyofuata waliamka majira ya
saa tatu asubuhi na walikuwa na hofu
wakihisi muda wowote askari waliotumwa na
rais wangerudi tena eneo hilo.

ITAENDELEA..
 
kidi kudi tafadhali sana, wacha ukatili mzee, malizia riwaya ya uchu. au ulimind Willy Gamba na technian kukusaidia nn? kama una uwezo wa kutuandalia nyingine, si utumie uwezo huo kumaliza ya uchu halafu urudi kwenye hii?
 
kidi kudi tafadhali sana, wacha ukatili mzee, malizia riwaya ya uchu. au ulimind Willy Gamba na technian kukusaidia nn? kama una uwezo wa kutuandalia nyingine, si utumie uwezo huo kumaliza ya uchu halafu urudi kwenye hii?
Sijamaind mkuu ila naamini TECHMAN nae atatoa sapoti pale ninapokwama kama hivi sasa
 
Last edited by a moderator:
Sehemu ya 13

Siku iliyofuata waliamka majira ya saa tatu
asubuhi na walikuwa na hofu wakihisi muda
wowote askari waliotumwa na rais wangerudi
tena eneo hilo.
Walianza kujiandaa kama walivyokuwa
wamepanga kuondoka eneo hilo, kulikuwa na
shati moja ambalo lilikuwa la mzee Rogart
lililokuwa limechakaa sana ndilo alimpa
alivae Geofrey. Shati hilo lilikuwa nje ya
nyumba hiyo hivyo halikuungua katika janga
la moto, alimpa kwa vile hakuwa na mazoea
ya kuvaa shati akiwa porini hapo. Wote
walikuwa katika mavazi duni kwani hata
mzee Rogart alikuwa amevaa shati lililokuwa
limechakaa sana na suruali iliyojaa viraka
zaidi walikuwa hawavijui viatu. Mtu wa
kawaida angewachukulia kama watu
waliokuwa masikini wa kupindukia, walianza
kutembea kwa tahadhari kubwa wakielekea
eneo la kusini mwa eneo hilo walilokuwapo
ambapo walipanga kuelekea jimbo la Linden.
Mzee Rogart alikuwa amebeba bunduki tatu
zilizokuwa na risasi, wakati Geofrey alikuwa
amebeba upinde na mishale mingi iliyokuwa
kwenye mfuko wake lakini pia hakuacha
dawa aliyoitumia ambayo ilisababisha
usingizi. Moyoni kwa kiasi alikuwa na furaha
kwani alikuwa amelichoka eneo hilo alilokuwa
ameishi kwa miaka kadhaa. Walikuwa
wakiongea mambo tofauti ya hapa na pale
wakati wakiendelea kutembea kwa kasi lengo
likiwa ni kupunguza umbali wa msitu huo
uliokuwa mkubwa. Majira ya saa kumi na
mbili jioni walikuwa wametembea umbali wa
kilometa nyingi wakiwa wamekutana na
wawindaji wachache pasipo kuwaona askari.
Bunduki moja kati ya tatu walizokuwa nazo
walibadilisha na chakula kwa wawindaji
waliokutana nao ambao walikuwa wakitokea
makwao. Kubadilisha vitu wakiwa porini hapo
lilikuwa jambo la kawaida kwani wawindaji
wachache waliokuwa wakitokea vijiji vya
karibu walikuwa na mazoea ya kuweka kambi
porini kwa muda na baada ya kuwanasa
wanyama walikuwa wakirudi katika vijiji vyao.
Njiani walikuwa wanakutana na wanyama
ambao wengine walikuwa wakali ili kutokana
na uzoefu wao walikuwa wakiwafukuza
wasiwadhuru.
Hatimaye wakati wa nyakati za jioni walifika
katika eneo waliloamua kulala lilikuwa
pembezoni kidogo na mto mdogo wa maji,
walikuwa wamechoka sana na malengo yao
yalikuwa ni kuhakikisha siku iliyofuata
wanatoka katika msitu huo. Waliamua kukata
miti na kuikusanya sehemu moja lengo lao
likiwa ni kuzuia upepo na baridi
vilivyokuwapo eneo hilo. Mara baada ya
zoezi hilo walianza kula chakula walichokuwa
wamepata kwa wawindaji, walipokamilisha
zoezi hilo walilala wakisubiri safari yao
iendelee siku iliyofuata.
Muda wote wakati mzee Rogart akiwa
amelala Geofrey alikuwa hapati usingizi, mara
kadhaa alisinzia lakini alirudi katika hali
yake. Mkononi alikuwa na upinde na mshale
alivyoviweka sawa kwa shari muda wowote,
hakuwa na amani ya kulala na
hakumshangaa mzee Rogart kwani aliamini
mzee huyo alikuwa amezeeka baada ya
harakati kama hizo wakati wa ujana wake.
Majira ya saa sita usiku akiwa amesinzia
kwa muda mfupi alishtushwa na miale ya
tochi aliyoiona kwa mbali upande wa mbele
walikoelekea baada ya kuvuka mto mdogo
uliokuwapo. Jambo hilo lilimpa shauku ya
kutaka kujua mwanga huo ulikuwa ukitolewa
na nani. Wawindaji wachache aliwafahamu
hawakuwa na mazoea ya kutumia tochi
pasipo kumwamsha mzee Rogart alitoka
mbio akiwa na upinde sambamba na mishale
yake akielekea eneo alilouona mwanga huo.
Hatimaye aliukaribia mwanga huo na taratibu
alianza kusogea akijificha kwenye miti akiwa
na lengo la kuwona wau ambao walikuwapo
eneo hilo. Aliziona tochi kadhaa zikiwa
zimeegeshwa maeneo tofauti ya eneo hilo
lililokuwa na mahema lakini pia aliwaona
askari wakizunguka zunguka eneo hilo
wakiwa na bunduki zao. Hisia za msako
uliokuwa ukiendelea zilimjia kichwani na
aliamini askari hao walikuwa wengi. Akili
yake iliona huo ulikuwa muda muafaka wa
yeye na mzee Rogart kuondoka eneo hilo ili
kuokoa uhai wao, taratibu alianza kuondoka
eneo hilo na alipofiaka umbali mrefu alikimbia
kwa kasi akirudi eneo walilokuwa wamelala.
Alipofika eneo hilo alishtuka baada ya kuona
sehemu aliyokuwa amelala mzee Rogart
ikiwa wazi hata bunduki zake hazikuwapo,
hofu ilimwingia akiamini tayari mzee huyo
alikuwa amekamatwa. Alibaki ametulia akiwa
hana jambo la kufanya, baada ya dakika
kadhaa alishtushwa na sauti ya mzee Rogart
akimwita ambaye naye alionekana alitokea
sehemu ambayo ilikuwa na askari hai.
Alifurahi kumwona mzee huyo na
walikubaliana safari iendelee usiku huo kwani
eneo hilo lilikuwa tayari na matatizo.
Walibeba vitu vyao vichache na waliendelea
na safari yao wakiwa wamechoka lakini
waliamini kupona kwao kulikuwa bora zaidi
kuliko kitu kingine.
Siku iliyofuata majira ya saa sita mchana
waliweza kutoka katika barabara kuu
iliyoelekea jiji la New Amsterdam na mwishoe
jimbo la Georgetown. Walificha silaha zao
pembeni kidogo na barabara na walianza
kusimamisha magari tofauti yaliyopita eneo
hilo yaliyoelekea Linden walikopanga
kuelekea. Magari mengi yalisimama ila baada
ya kuwaona watu hao na hali zao kiujumla
madereva walikuwa wakiingiwa hofu na
kukataa kuwapa msaada. Hata magari ya
abiria yaliposimama yalikataa kuwachukuwa
wakiamini huenda walikuwa majambazi, watu
wengi walimshangaa zaidi Geofrey kwa vile
alikuwa mwafrika na zaidi katika mavazi
machafu. Hofu yao pia ilikuwa kwa mzungu
mwenzao mzee Rogart aliyekuwa na ndevu
pamoja na nywele nyingi vyote vikiwa na mvi
lakini pia sura yake ilikuwa haionekani vizuri
kutokana na nywele hizo.
Baada ya kukaa barabarani hapo pasipo
kupata msaada kwa zaidi ya saa zima huku
wakiwa na hofu ya kukamatwa wakiwa eneo
hilo, mzee Rogart alitoa ushauri wa kufanya
unyan`ganyi wa gari ili waweze kuondoka
eneo hilo. Alielekea katika kichaka
kilichokuwa pembeni kidogo ya barabara na
kutulia na bunduki yake akiwa amemwacha
Geofrey ajaribui kuendelea kusimamisha
magari ambayo yangepita eneo hilo. Magari
mengine yalikuwa hayasimami na baada ya
muda mfupi gari moja lilisimama lilokuwa la
kutembelea, teski aina ya Toyota. Alikuwamo
kijana mmoja ambaye baada ya kuelezwa
kuwa walihitaji msaada alipuuza akiimhofia
kwani hata kioo alishusha kidogo alianza
kulisogeza gari lake barabarani tayari kwa
kuendelea na safari. Geofrey alibweka kama
mbwa ishara iliyomtoa mzee Rogart kwa kasi
kichakani na kuelekezea bunduki yake eneo la
mbele la uskani ambapo dareva huyo
alikuwapo.
Alimuamru ashuke haraka jambo ambalo
alitekeleza, wakati huo Geofrey alianza
kupakia upinde na mishale yake na bunduki
nyingine aliyokuwa nayo mzee Rogart kwenye
gari hilo ambavyo walikuwa wamevificha
pembezoni mwa barabara. Mara baada ya
zoezi hilo mzee Rogart alimweleza kijana
aliyekuwa na gari hilo aanze kukimbia bila
kugeuka kurudi na barabara sehemu
aliyokuwa ametoka. Alitekeleza jambo hilo
akiwa na hofu huku akiamini watu hao
aliowachukulia kama majambazi wangemuua,
alitoka mbio akitekeleza masharti hayo.
Mzee Rogart aliamini kazi ilikuwa imeisha
aliingia kwenye gari na kulitoa kwa kasi eneo
hilo akielekea upande wa jimbo la Linden,
alikuwa na uzoefu mkubwa wa kuendesha
magari hiyo ilitokana na enzi za ujana wake
akiwa jambazi mkubwa. Geofrey alikuwa
haamini kilichoendelea zaidi alifurahishwa na
gari hilo, alikumbuka mara ya mwisho
kupanda gari ilikuwa wakati ambao
alisindikizwa na mwalimu wake wa American
Academic School katika uwanja wa ndege wa
Washington. Hakuwahi kupanda tena gari
kwa zaidi ya miaka sita aliyokuwepo porini
na mzee Rogart. Alikimbiza gari lao huku
wakiwa na imani ya kufika jimbo la Linden
baada ya masaa machache.
Muda wote wakiwa kwenye gari walikuwa
wakizungumza mambo tofauti zaidi walijisifia
kwa kuukwepa mkono wa askari
waliowafuata porini. Wakiwa wamebakiwa na
kilomita kadhaa ili wafike katika jimbo hilo,
walishtushwa na gari la askari lililokuwa likija
nyuma yao kwa kasi na hisia zote za
kukamatwa kwao zikawaingia. Furaha
waliyokuwa nayo iliwaishia ghafla na mzee
Rogart aliongeza kasi ya gari lao akiwa na
hofu. Dalili zote za kukamatwa kwao zilianza
kuonekana na tayari kulikuwa na vipaza
sauti vilivyotumiwa na askari hao
waliowataka wasimamishe gari lao.
Baada ya muda mfupi huku wakiwa hawatii
amri hiyo ya askari walifika aktika eneo la
mpaka lililotenganisha jimbo la Linden na lile
la New Amsterdam eneo ambalo lilikuwa na
askari wengi na geti lake lilifungwa
kutoruhusu gari lolote kupita kwa wakati huo.


ITAENDELEA...
 
Sehemu ya 14

Baada ya muda mfupi huku wakiwa hawatii
amri hiyo ya askari walifika aktika eneo la
mpaka lililotenganisha jimbo la Linden na lile
la New Amsterdam eneo ambalo lilikuwa na
askari wengi na geti lake lilifungwa
kutoruhusu gari lolote kupita kwa wakati huo.
Mzee Rogart alisikika akiongea kwa
machungu akimweleza Geofrey kuwa wakati
wake wa kuishi ulikuwa umeisha. Jambo hilo
lilimfanya Geofrey aanze kulia kwa uchungu
akiwa hayuko tayari kutenganishwa na mzee
huyo. Mwishoe aliamua kusimamisha gari
hilo wakiwa umbali mfupi na geti hilo, alianza
kwa kumshukuru Geofrey akiamini
asingepewa adhabu kama ambayo angepewa
yeye ambayo aliamini ilikuwa ni kifo.
Baada ya muda mfupi mzee Rogart akiwa
hajaongea mambo aliyotaka kumweleza
Geofrey, tayari kundi la askari walikuwa
wamelizunguka gari lao wakiwa
wamewaelekezea bunduki zao wakiwaambia
watoke. Mzee Rogart na Geofrey walitekeleza
amri hiyo na wote kwa pamoja walitoka
wakiwa wamenyoosha mikoni juu, askari
waliwafunga pingu kila mmoja na
walipakizwa katika gari tofauti kabla ya
kuanza kuondoka gari hizo za polisi eneo
hilo.
Siku iliyofuata vyombo vya habari nchini
Guyana vilitawaliwa na habari za kukamatwa
kwa jambazi sugu aliyetafutwa kwa zaidi ya
miaka kumi na tano pasipo kupatikana. Zaidi
vilielezea kuwa mtu huyo ndiye
aliyesababisha ajali iliyopelekea kifo cha mke
wa rais bwana Zakheem Pirjah. Magazeti
tofauti yalichapisha picha ya mzee Rogart
akiwa na kijana aliyeishi naye porini
aliyekuwa mwafrika. Mwonekano wa mavazi
yao na jinsi walivyokuwa vilikuwa kivutio kwa
raia wa nchi hiyo walionunua magazeti
wakihitaji kujua habari zao zaidi. Tayari kesi
dhidi yao ilifunguliwa wakati Geofrey akiwa
na kosa la kufanya unyan`ganyi wa gari
pamoja na kuishi na mtuhumiwa huyo.
Geofrey hakuwa na shaka sana juu ya
hukumu ambayo ingeenda kutolewa ila
alimwonea huruma mzee Rogart akiamini kesi
yake ilikuwa kubwa ambayo usalama wake
ulikuwa mdogo. Kilichompa shaka zaidi ni
vile muda akiwa anashikiliwa na askari katika
kituo cha New Amsterdam hakuelewa kituo
ambacho mzee Rogart alikuwapo. Siku yake
ya kesi alipelekwa mahakamani na baada ya
kukubali makosa yake alihukumiwa kwenda
jela kwa miaka mitatu. Geofrey aliumia
kufuatia adhabu hiyo na aliona mpango wa
kurudi Tanzania kuiona familia yake ulikuwa
unapotea kabisa. Kichwani aliingiwa na imani
ya kuwapo nchini Guyana kwa miaka mingine
zaidi ya mitano, kwani alielewa mara baada
ya kutoka jela alipaswa atafute fedha kwa
ajili ya nauli kurudi Tanzania.
Askari walimchukuwa tayari kwa safari
akiwa na wafungwa wenzie kuelekea katika
gereza kubwa lililokuwapo kusini mwa nchi
hiyo katika jimbo la Biloku. Safari ilianza
wakiondoka mahakamani hapo akiwa pia
haelewi mahali ambapo mzee Rogart
alikuwapo zaidi alikuwa hajui kesi yake
ilikuwa ikisomwa siku gani. Ndani ya gari hilo
la magereza alikuwa mwafrika peke yake na
alitulia pasipo kuongea na mtu ingawaje
wenzie wachache walikuwa katika maongezi.
Mawazo yake alikuwa ameyarudisha nchini
Tanzania akiwa anaikumbuka familia yake.
Siku zote alikuwa akiamini familia yake
ilimtambua kuwa alikufa katika ajali ya ndege
na hilo ndilo lililokuwa likimpa hamasa ya
kutaka kurudi nchini Tanzania.
Hatimaye walifika gerezani na aliweza
kukutana na wafungwa weusi kama yeye
kadhaa ambao walikuwa rafiki zake. Gereza
hilo lililokuwa na taabu nyingi lakini kwake
aliona kila kitu kilikuwa sawa kwa vile
maisha aliyokuwa akiishi porini yalikuwa
magumu zaidi. Baada ya wiki moja alipata
taarifa kutoka kwa wafungwa kadhaa
waliokuwa wakiingia gerezani hapo baada ya
hukumu zao ambao walimweleza kuwa mzee
Rogart alifariki kwa maradhi siku moja kabla
ya hukumu yake. Geofrey alilia kwa uchungu
juu ya taarifa hizo lakini pia hakuamini kama
ni maradhi yalipelekea kifo chake, kichwani
mwake aliaminii kifo hicho kilipangwa na rais
wa nchi hiyo bwana Zakheem Pirjah.
Wafungwa gereza hilo walikuwa
wanamwogopa sana Geofrey, kwani kwa
muda mfupi alifahamika kutokana na jitihada
zake za kuwasaidia wafungwa waliokuwa
wanaonewa. Alikuwa na mwili wa kawaida
lakini alikuwa tayari kupigana na mfungwa
yeyote aliyekuwa mkorofi na kumpiga.
Baada ya miezi sita Geofey alizoea zaidi
mazingira ya jela na hakuwa na imani kama
angemaliza muda wake na kuondoka eneo
hilo. Alijifunza kusahau kurudi Tanzania na
zaidi juu ya kifo cha mzee Rogart, siku moja
akiwa anaendelea na kazi za shambani
gerezani hapo alishtushwa na kauli ya askari
aliyemweleza kuwa alikuwa na mgeni.
Geofrey alimkabidhi mfungwa mwenzie jembe
alilokuwa akilitumia na aliongozana na askari
magereza kuelekea chumba cha wageni.
Hakupata picha juu ya mtu aliyefika gerezani
hapo akiwa na nia ya kutaka kumwona, hiyo
yote ilitokana na vile alivyokuwa akiamini
jambo hilo lilikuwa gumu akiwa gerezani
hapo.
Mara baada ya kufika katika chumba hicho
cha wageni alimwona msichana mmoja
mrembo aliyeonekana alikuwa na
mchanganyiko wa damu ya kiafrika na ya
kizungu akiwa amekaa katika mojawapo ya
kiti kilichokuwapo. Akili yake kwa haraka
ilimtuma akiamini mtu huyo hakumfuata yeye,
hata siku moja hakuwahi kuingiwa na fikra
juu ya ujio wa mtu kama huyo aliyevutia kwa
mwonekano. Alibaki kimya akimsikiliza askari
amwekekeze kuhusu mgeni wake na wakati
huo alihisi mgeni huyo alikuwa nje. Askari
huyo alimweleza Geofrey akimwonyesha kwa
kidole msichana aliyekuwa ameshangazwa
naye kuwa ndiye mgeni wake, alimpa dakika
kumi za maongezi.
Alianza kutembea kuelekea katika meza
ambayo msichana huyo alikuwa amekaa,
hatimaye alifika na kuketi katika kiti cha
upande wa pili akitazamana uso kwa uso na
msichana huyo huku wakitenganishwa na
meza ndogo.Kabla hajaongea kitu
alishangazwa kuona msichana huyo
akimsalimia kwa lugha ya kiswahili ambayo
hata askari aliyekuwapo pembeni kidogo
hakuielewa.
“Geofrey mambo, mzima?” alisikika msichana
huyo mara baada ya kuketi kwake “mimi
mzima sijui wewe” alijibu Geofrey akiwa
hajiamini na zaidi alikuwa hajaitumia lugha
hiyo toka aingie nchini hapo Guyana.
Msichana huyo alianza kwa kujitambulisha
kuwa aliitwa Magreth na alikuwa raia wa
nchini Tanzania, alimweleza kuwa alikuwapo
nchini humo Guyana kwa vile baba yake
alikuwa balozi wa Tanzania nchini humo.
Aliendelea kumweleza jinsi alivyomfahamu
Geofrey kupitia vyombo vya habari baada ya
kukamatwa kwake jambo lililomfanya apange
siku moja kumtembelea gerezani hapo.
Alihitaji kufahamu juu ya mkasa uliomfika
Geofrey mpaka alikuwa gerezani hapo akidai
kuwa aliwajali waafrika wote waliokuwapo
nchini humo. Muda wote wakati Magreth
akisimulia hayo kuna jambo alilokuwa
ameligundua ambalo tayari lilianza kuwa
kikwazo moyoni mwake.
Baada ya maelezo hayo mafupi ambayo
Geofrey aliyaelewa alianza kumsimulia mkasa
wa mambo yote aliyokutana nayo hadi wakati
huo akiielezea pia familia yake. Muda wote
akimsimulia, Magreth alipatwa na uchungu
akionyesha dalili zote za kutokwa na
machozi. Akiwa anaendelea kumwelezea,
askari magereza aliyekuwa kando ambaye pia
hakuelewa walichoongea alimweleza Geofrey
kuwa muda uliisha, alisimama tayari kwa
kurudi tena kwa wafungwa wenzie. “ahsante
dada Magreth kwa kunijali..” alisikika Geofrey
akiwa na anavutwa na askari huyo.
“usijali kuna chakula nimekuletea
watakupatia, lakini pia nitarudi siku nyingine
uumalizie mkasa wako” alisikika Magreth
akiwa na huzuni akimweleza Geofrey
aliyeanza kuondoaka eneo hilo na hakujibiwa.
Kichwani alipata hisia za ugumu wa maisha
ya Geofrey ingawaje alimsimulia mpaka
wakati anaokotwa kwenye ajali ya ndege na
kwenda kuishi na mzee Rogart.
Mbali na huzuni aliyokuwa nayo Magreth
alishtushwa na hisia zake za ghafla juu ya
Geofrey, alimhitaji awe mwanamme wake wa
ndoto. Alikuwa ameishi kwa miaka mingi
nchini humo Guyana lakini hakuwahi kuwapo
katika mahusiano, jambo hilo lilimshangaza
kuona alivutiwa na mtanzania mwenzake
aliyekuwa gerezani. Geofrey alikuwa tofauti
na yule aliyemwona kwenye vyombo vya
habari siku anakamatwa, kwa vile alikuwa
mwanamme aliyevutia. Baada ya kuelezwa
kuwa chakula alicho mpelekea angekipata
aliondoka gerezani hapo na kuelekea uwanja
wa ndege kwa safari ya kurudi jimbo la
Georgetown ambalo alikuwa akiishi na familia
yake. Mara baada ya kufika nyumbani kwao
hakumweleza mtu juu ya zoezi alilolifanya la
kumtembelea mfungwa wa kitanzania.
Jambo lililomkaa kichwani mwake na
kutawala mawazo yake lilikuwa juu ya
mfungwa huyo, hakuelewa sababu
iliyopelekea jambo hilo. Siku tatu baadaye
aliondoka nyumbani kwao na kusafiri tena
kurudi jimbo la Biloku lengo kuu likiwa
kwenda kukutana na Geofrey ili amumalizie
mkasa wake lakini zaidi alikuwa
amemkumbuka kupita kiasi.
Kama ilivyokuwa awali alifanikiwa kupata
nafasi ya kuongea naye ingawaje Geofrey
alishtushwa na bahati aliyoipata ya
kutembelewa tena zaidi alishukuru juu ya
chakula alichokipata. Hatimaye alimumalizia
mkasa wake na kumfanya Magreth akose
raha akiwa hana njia ya kumsaidia lakini
alimweleza kuwa angejaribu kwenda kufanya
jitihada za kuwatafuta wazazi wake Geofrey.
Alimweleza kuwa angempa mtu jukumu
kutoka Tanzania ili awatafute jambo ambalo
alifurahi kulisikia. Hatimaye Magreth
aliondoka na kuanza kurudi nyumbani kwao,
akiwa na furaha ya kumwona Geofrey wakati
lengo lake likizidi kujengeka zaidi moyoni.
Wakati huo alikuwa akisoma chuo kikuu cha
Guyana akisomea udaktari na alikuwa katika
likizo fupi. Tayari alikuwapo nchini humo na
wazazi wake kwa zaidi ya miaka saba, mama
yake alikuwa na asili ya Uingereza wakati
baba yake alikuwa mtanzania akiwa balozi
nchini humo kutoka Tanzania. Mara baada
ya kufika nyumbani kwao alimpigia simu
rafiki yake wa karibu aliyekuwapo nchini
Tanzania na kumwomba aulizie mtu aliyeitwa
James Kibudo kama Geofrey alivyolitaja jina
la baba yake.Baada ya kumpa rafiki yake
huyo kazi hiyo alianza kusubiri taarifa zozote
kutoka kwa mtu huyo ambaye mwishoni
alidai kulikuwa hakuna mtu aliyeitwa jina hilo.
Bila kuchelewa alimpa taarifa hizo Geofrey
ambaye alichukulia jambo hilo kama la
kawaida na aliamini siku ambayo angerudi
Tanzania mambo yote yangekuwa sawa.

ITAENDELEA....
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom