Riwaya Mpya: Mpelelezi Ray Shaba katika

SURA YA KUMI NA MOJA (Inaendelea)

ZILIPITA WIKI KADHAA tangu Ray na Sofia waende kwa Padre Kiko kule Agape Center kutafuta ushauri katika matatizo yao ya ndoa. Siku ile ya Ijumaa Ray aliona kama ni ndefu isiyoisha; lakini hakuwa na haraka ya kurudi nyumbani kwani Sofia alipafanya nyumbani kuwa pachungu. Alijiuliza wanaume wangapi wako kwenye hali kama yake ambao hutafuta visingizio vya kutokwenda nyumbani mara moja ili kukwepa ugomvi.

Siku ile ilikuwa ni ya kawaida tu. Baada ya mazoezi yake ya asubuhi alijiandaa kuwahi kazini kama ilivyokuwa kawaida yake. Alipofika ofisini alikuta kuna ujumbe uliomtaka aende moja kwa moja ofisini kwa RPC. Aliingia ofisini kwake kwa dakika chache tu kuvua koti lake na kubaki na tai na moja kwa moja alielekea ofisini kwa RPC. Kufika huko alikuta ametanguliwa na maafisa wengine wa vikosi maalum vya jeshi hilo katika Kanda ya Dar na alikuwepo mmoja kutoka Makao Makuu ya Jeshi hilo.

Siku ilianzia hapo na kufika jioni Ray alikuwa hoi bin taabani. Tangu alipoingia ofisini kwa RPC hadi jioni alipotoka kazini Ray na wenzake walikuwa katika jukumu kubwa la kufuatilia kundi la majambazi ambalo lilidaiwa kuwa limeingia nchini Kenya. Taarifa za inteligensia ambazo zilipatikana kutoka Jeshi la Polisi la Kenya ni kuwa kundi hilo lilikuwa na lengo la kufanya matukio kadhaa ya ujambazi katika jiji la Dar-es-Salaam na Mwanza. Kutwa nzima siku ile Ray alikuwa na kazi ya kuratibu wapelelezi wa pale mkoani na wa mikoani katika kujiweka tayari kufuatilia kundi hilo na kuhakikisha taarifa zozote zinawasilishwa mara moja Jijini Dar. Kila mpelelezi aliviweka vyanzo vyake tayari tayari kwa fununu au tetesi zozote watakazozisikia.

Vyanzo vya wapelelezi hao vilikuwa ni vingi na hakuna aliyejua; walikuwepo wapiga kiwi viatu, wauza magazeti, madereva wa bajaji, dalala na hata vijana wanaoshinda vijiweni. Polisi waliwatumia watu hao kupata taarifa nyingi za siri na siyo wao tu hata watu wa Usalama wa Taifa nao walikuwa na watu kama hao nchi nzima. Mitego mbalimbali ya kipolisi ilianza kuwekwa sehemu mbalimbali nchini. Pamoja na juhudi zote za kutwa nzima kundi hilo la majambazi lilikuwa kama limegeuka upepo mara tu baada ya kuingia Tanzania.

Haikujulikana wamepotelea wapi, kwani magari mawili ambayo ilidaiwa walikuwa wameyatumia wakati wanatoka Kenya yalitoweka vile vile na hayakuonekana kwenye barabara yoyote ama kuelekea Moshi au mji mwingine. Jeshi la Upolisi lilikuwa na kamera kwenye baadhi ya barabara kuu ambazo zilikuwa zinarekodi magari yote yanayopita kila siku. Hisia ya viongozi wa polisi ni kuwa majambazi hayo yalikuwa yametulia mahali na kujificha kwa kimya kidogo kabla hawajaendelea. Hii ilimaanisha kuwa walikuwa na washirika wengine Tanzania ambao waliwapa hifadhi na labda hata usafiri mwingine.

Ilikuwa ni agizo la IGP kuhakikisha kuwa watu hao wanapatikana kwa namna yoyote na kwa mbinu yoyote kwani kiwango cha silaha ambazo kundi hilo lilidaiwa kuwa nacho lilimaanisha hawakuingia nchini kufanya ujambazi au uhalifu mdogo. Polisi na watu wa Usalama wa Taifa walitambua mara moja kuwa kundi hilo lilikuwa ni zaidi ya majambazi. Hivyo, kwa Ray ilikuwa ni siku ndefu kwani hakuweza hata kupata nafasi ya kula chakula cha mchana zaidi ya kunywa maji na juisi tu pale pale ofisini. Kutokana na kutokuwa na mafanikio makubwa siku hiyo Ray alitakiwa kuondoka na kuongoza kundi la wapelelezi waandamizi kuelekea Arusha mapema asubuhi kuongeza nguvu.

Alipokuwa akitafakari hayo alikuwa anaingia kwenye geti la nyumba yake funguo ya gari lake mkononi na mkoba uliobeba kompyuta na nyaraka mbalimbali mkono mwingine. Bastola yake ilikuwa upande wa kulia wa mkanda wake. Geti lilifunguliwa na mlinzi wake na taa za nje ndizo zilitoa mwanga pekee pale. Aliingia ndani lakini alikuta taa zote zilikuwa zimezimwa. Aliwasha taa ya pale sebuleni kwa kutumia mkono wenye bastola. Walinzi wake wawili walikuwa bado hawajafika, kwani kawaida walikuwa wanafika pale kwenye majira ya saa tatu hivi za usiku na kupishana na mlinzi wa mchana. Mara nyingi kama Ray yupo nyumbani huwa anamruhusu mlinzi wa mchana kuondoka mapema.

“Sofia!” Ray aliita kwa sauti kubwa. Hakukuwa na kuitikiwa. Alikuwa na uhakika kuwa alipoingia aliliona gari la Sofia likiwa limeegeshwa pembeni ya kibanda cha walinzi. Aliwasha taa ya kuelekea chumbani, na akaangalia jikoni ambako aliwasha taa pia na hakukuwa na mtu. Alienda moja kwa moja chumbani kwake akidhania labda Sofia alikuwa amelala. Hakukuwa na mtu. Kitanda kilikuwa kimetandikwa vizuri. Alianza kuingia na wasiwasi, akakumbuka bado ameshikilia mkoba na funguo yake, akarudi sebuleni na kuviweka juu ya meza. Akaenda bafuni, huko nako hakukuwa na mtu. Ray alikuwa na uhakika kuwa kuna kitu hakiko sawa.

Alirudi tena hadi sebuleni na kuangalia kila kitu kimepangwa vizuri, na inaonekana nyumba nzima ilikuwa imesafishwa vizuri. Hilo halikumshangaza sana kwani ndivyo alivyopenda sana nyumba yake kuonekana. Hata ofisini kwake kila kitu kilikuwa kinapangwa vizuri hadi kalamu za mezani. Kati ya vitu ambavyo hakuwa anavipenda sana ni kukuta vitu vyake vimevurugwa. Marafiki zake walikuwa wanamtania toka zamani kuwa kupenda kwake usafi na kupanga vitu vizuri kulitokana na malezi yake ya seminari. Alipoingia jikoni mara hii ya pili ndio aliona karatasi imebandikwa kwa gundi kwenye mlango wa friji lake kubwa la GE. Ilikuwa imekunjwa mara mbili tu.

Ray aliichukua na kuifungua. Alijikuta amemeza mate kwa ghafla yakampalia na kuanza kukohoa mfululizo kwa sekunde kadhaa. Aliamua kuchukua chupa ya maji ndani ya friji na kufungua na kunywa na mara kukohoa kukatulia. Pale pale jikoni akiwa amesimama bila kuegemea popote alianza kusoma karatasi ile akiwa ameishika kwa mikono miwili kama ilikuwa nzito mkononi.

Mpendwa Ray,

Naomba usishtuke sana kukuta nyumba imekupokea kwa ubaridi na upweke. Baada ya miaka yote ya kuishi nawe na maisha yote tuliyopitia pamoja nimejikuta sina ujasiri wa kuzungumza nawe ana kwa ana na najua mwisho wa siku tungeishia kugombana na tusizungumze kwa siku kadhaa kama ilivyo kawaida miezi hii mingi sasa.

Matamanio yangu yote tangu unioe ni kuwa ningeweza kupata mtoto na hata watoto wengi. Unajua jinsi gani kiu yangu hiyo imeshindwa kutulizwa katika maisha haya tuliyoishi pamoja. Miaka inaenda kwangu na sioni kama mwenzangu una kiu kama yangu kwani ni wazi umeamua kuweka kazi yako kwanza. Mazungumzo yote tuliyoyafanya inaonekana hatuendi popote zaidi ya kukosoana na kukosana.

Ni kwa sababu hiyo nimeamua kuondoka niende kutafuta maisha mahali pengine na Mungu akinijalia niweze kutimiza kiu yangu hiyo. Naomba usihuzunike sana na wala usinitafutea. Nitakuwa tayari kuzungumza nawe mara moja tu kwa simu kukuondoa hofu. Nakutakia mafanikio na maisha mema huko mbeleni.

Sofia.

Chini ya barua kulikuwa na sahihi ya sofia na tarehe ya siku ile. Ray Shaba, hakutaka kuamini kuwa ndoa yake ilikuwa imefikia kikomo kwa namna na mtindo ule. Alijihisi hasira zaidi kuliko uchungu. Lakini kitu kingine kilikuwa kimemshika moyoni nayo ni hisia ya hatia na kujiona kama mtu aliyeshindwa maisha. Hakutaka kuamini maisha ya useminari yalimshinda na sasa ndoa nayo imemshinda. Alijaribu kutafakari jinsi gani walifika hadi kuachana kwa namna ile hakuamini. Sofia alikuwa ni mpenzi wake wa pili lakini katika mapenzi ndiye alikuwa wa kwanza aliyemuingiza katika ulimwengu wa mapenzi na kumpagawisha. Hakuwahi kudhania kuwa maisha yake yangefikia mahali hapo, na kwa vile alikuwa ni Mkatoliki alijua hawezi tena kuoa mwanamke mwingine na wazo la kuishi kinyumba tu hivi hivi hakutaka hata kulipa nafasi.

Alichukua simu yake na kutaka kumpigia Sofia saa ile ile lakini alijikuta anajiuliza mara mbilimbili kama ampigie au vipi. Upande mmoja alitaka kuhakikisha kuwa yuko salama na ajaribu kumbembeleza kurudi lakini upande mwingine alikuwa na hasira na kiburi. Hata hivyo aliamua kukishinda kiburi chake.

“Hi Ray” Sofia alijibu mara baada tu ya simu kuita mara moja.

“Sofia, uko wapi?” Ray aliuliza huku sauti yake ikiwa kama ya mtu anayenong’ona lakini si kwa sababu ya kutaka kuficha jambo bali kutotaka kufichua hasira iliyokuwa inachemka kwenye damu yake.

“Ray usianze, umeisoma barua yangu?” Sofia alimjibu sauti yake ikiwa thabiti kabisa na isiyoonesha unyonge au huzuni au woga fulani mbele ya Ray.

“Ndio nimeisoma, kwanini usije tuzungumze Sofia?”

“Muda wa kuzungumza umepita Ray, tumezungumza sana na kwa kweli mimi ndio nimezungumza sana lakini sioni namna nyingine” Sofia alianza kutoa ya moyoni.

“Sasa kwanini usije unieleze vizuri mke wangu” Ray alijikuta anabembeleza. Hakujua kama anabembeleza kwa sababu kweli anataka arudi au anabembeleza kwa sababu alikuwa anatarajiwa kubembeleza. Sofia hakusogea hata nchi mmoja wala kuonesha dalili ya kumsikia Ray. Alikuwa ni mwanamke anayejua anachotaka na akishaamua kukipata hakukuwa na kitu cha kumbadilisha. Kwa dakika kama tano bila kumpa nafasi Ray kuzungumza Sofia alieleza tena aliyoyasema kwenye barua yake na kusema kuwa anaenda kukata simu na atabadilisha namba yake. Alichomuambia Ray ni kuwa tu asimtafute ampe muda kama atajikuta anataka kurudi basi atarudi mwenyewe. Alimuomba sana Ray asiwasumbue wazazi wake yeye Sofia kwani haendi kwao wala haendi kwa ndugu yeyote ambaye Ray anaweza kumpata.

Ray alijikuta hana la kusema zaidi ya kumwambia Sofia kuwa ule ulikuwa ni uamuzi wake na kuwa kama akitaka kurudi nyumba ile ni yake na ni pake na anaweza kurudi wakati wowote kwa sababu yeye hakumfukuza.

Walikata simu bila ya kwaheri wala kutakiana heri.

Aliamua saa ile ile kama kweli Sofia ameamua kuondoka basi hatokuja kuoa tena kwani hakutaka tena kuhangaika na wanawake. Aliona kuwa kama ndoa zipo duniani basi kwake ndoa yake pekee iliyobakia ni kazi na kazi peke yake. Aliamua kwenda tena kwenye friji safari hii hakutaka maji tena, alichukua chupa ya rangi ya dhahabu ya kinywaji kikali cha whiski ya Fyfe. Alichukua madonge matatu ya barafu na kuyaweka kwenye glasi na kumimina whiski ile hadi karibu ya kujaa. Bila kupumua aliiweka mdomoni na kuibugia kwa mafundo kama maji. Ray Shaba hakuwa mnywaji sana wa whiski lakini huwa anakunywa kwa mtindo huo kila anapokuwa katika msongo mkubwa wa mawazo na hisia kama ilivyokuwa usiku ule. Hakutaka hata kula.

Alielekea moja kwa moja chumbani, alibadilisha nguo zake za kutwa na kuvaa nguo za kulalia. Alitoka nje mara moja kuhakikisha walinzi wameshafika na aliwakuta hakuwaambia kitu aliwatakia tu usiku mwema yeye mwenyewe akarudi ndani. Alielekea moja kwa moja kulala kwani kesho yake kulikuwa na kazi ya kuwatafuta wale washukiwa walioingia nchini kutokea Kenya.

Hakutaka kumsikia Sofia, wala kumfikiria wala kuulizia mambo ya Sofia. Alitaka kujilalia tu; mambo ya Sofia aliamua kumuachia Sofia. Wakati anajiandaa kuzima taa kwenye meza ndogo ya pembeni ndio macho yake yakagongana na pete ya ndoa ambayo Sofia aliiacha pale. Aliiangalia kwa muda bila kutaka kuigusa kama kwa kuiangalia kule kungeifanya itoweke. Alijigeuza upande mwingine.

(Itaendelea)
Tupo pamoja mzeee
 
SURA YA 12
(Inaendelea)

TANGU MAPEMA ASUBUHI siku ile ya Jumatatu watu walianza kutiririka taratibu kuelekea Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza wakitokea katika viunga mbalimbali vya jiji hilo. Kina mama na watoto wao migongoni, huku wengine wakishikwa mikononi, wazee na fimbo zao za kutembelea na vijana na baskeli zao huku wengine wakitembea kwa miguu kila mmoja na simu mkononi walielekea Kirumba. Milango ya uwanja wa Kirumba ilifunguliwa tangu saa kumi na mbili asubuhi na watu walianza kuingia toka mida hiyo na ilipofika saa nne asubuhi, mzunguko wa uwanja ulikuwa tayari umejaa.

Watu waliruhusiwa siyo tu kukaa kwenye mzunguko bali pia kukaa katikati kabisa kwenye eneo la kuchezea mpira ambapo viti kwa maelfu vimepangwa vizuri kabisa kuelekea upande mmoja wa goli katika uwanja huo wa kabumbu. Upande ule ambapo viti vilielekezwa ndiko jukwaa kubwa lilikuwa limejengwa. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa mkutano mkubwa wa Injili kama ule kuruhusiwa kufanyika ndani ya uwanja wa CCM Kirumba. Uwanja ule ulichaguliwa kwa sababu ndio ulikuwa na eneo kubwa la kuweza kuchukua maelfu ya watu kwa wakati mmoja katika mazingira salama pale jijini Mwanza.

Watu walitoka nje ya Jiji la Mwanza kutoka mikoa ya Shinyanga, Mara, Geita, na Simiyu walikuwa wameingia mjini, wengi siku moja kabla. Kwa wakazi wa Mwanza ujio wa mkutano mkubwa wa Injili wa Askofu Mkuu Ndondo ulikuwa ni neema kubwa kwa wenye mahoteli, nyumba za kulala wageni, na biashara mbalimbali. Mkutano wa Kanisa la Mavuno ulileta mavuno ya neema kwa kila mtu mwenye akili ya kuchakarika.

Wale waliofika siku moja au mbili kabla waliweka kambi nje ya uwanja kama watu wanavyofanya huko Marekani wanaposubiria simu mpya za Iphone au kuwahi kufanya manunuzi yenye punguzo kubwa la bei wakati wa Krismasi. Polisi kutoka mikoa mitano jirani waliletwa jijini Mwanza kuongeza nguvu. Harufu ya ujio wa Nabii na Mtume Damien Ndondo ilikuwa imetanda kwa siku kadhaa katika anga zima la jiji la Mwanza, lenye maji baridi na samaki watamu waliosifiwa na Dkt. Remmy Ongala. Mkutano huo haukuvutia wenyeji tu bali hata raia wa kigeni ambao walikuwa wanatembelea Tanzania. Wageni wengi waliamua kutumia muda Jijini Mwanza kushuhudia mkutano huo mkubwa kama sehemu ya utalii pia.

Malori makubwa kumi ya aina ya Fuso Fighter yalikuwa yametangulia wiki moja kabla yakiwa na vifaa na vyombo vyote vitakavyohitajika kufanikisha mkutano. Malori yote yalikuwa yameandikwa pembeni kwa maandishi makubwa “Huduma ya Mavuno”. Magari mengine madogo yalibeba wafanyakazi mbalimbali na wahudumu wengine ambao jukumu lao ilikuwa ni kusimamia maandalizi ya mkutano, wote wakitoka makao makuu Dar-es-Salaam. Jukumu kubwa la timu hiyo iliyotangulia ilikuwa kuhakikisha kuwa dakika ambayo Askofu Mkuu, Nabii na Mtumishi wa Mungu Damien Ndondo anasimama jukwaani kila kitu kinaenda kwa ufanisi wa hali yajuu. Hakuna kitu ambacho Ndondo hakukipenda wala kukizoea kama watu kufanya kazi bila ufanisi wa hali ya juu. Kuanzia sauti, eneo, umeme na kila kitu ambacho kilihitajika kifanye kazi yake basi ilikuwa ni jukumu la timu hiyo kuhakikisha kinafanya hivyo. Wao walikuwa ni kwanza kufika na ni wa mwisho kuondoka.

Mazoezi ya vyombo na mitambo yote pamoja na kwaya zote yalifanyika siku ya Jumamosi siku moja kabla ya kuanza kwa mkutano. Pamoja na kuwa na genereta zao wenyewe kusimamia mifumo mikubwa ya utangazaji, huduma ya Ndondo ilitumia pia umeme wa nguvu za jua hasa kwenye matumizi ya taa pale uwanjani ambazo ziliongezwa kwani uwanja wa CCM Kirumba haukuwa na taa za kutosha za kisasa kuweza kumulika ndani na nje ya uwanja. Hii ilisaidia kupunguza kutegemea huduma ya umeme wa Tanesco na hawakutaka kutumia umeme huo sana kwani kama wangetumia basi kungekuwa na upungufu wa umeme kwa Jiji la Mwanza.

Uamuzi wa kuja na mtambo wao za kuzalisha umeme ulisaidia pia kuishawishi serikali kuruhusu kutumiwa kwa uwanja huo maarufu ambao huwa unatumiwa na timu za Pamba na Toto African za Jijini humo. Umeme wa ziada uliozalishwa uliingizwa kwenye maduka ya eneo lile na kuleta afueni kwa muda wa wiki nzima mkutano ulikuwa unafanyika. Hakuna mtu aliyetaka kupitwa na ujio wa Askofu Mkuu Ndondo. Kwa wakazi wa Mwanza iliwakumbushia ujio wa Mtakatifu Papa Yohani Paulo II mwaka 1990 kwenye kilima cha Kawekamo upande wa Magharibi wa jiji hilo kuelekea Uwanja wa Ndege. Wakatoliki kwa Wapentekoste, Walutheri kwa Waangalikana, Waislamu kwa Wahindu wote walitaka angalau kumuona mtu ambaye alitajwa kuwa ni miongoni mwa wachungaji maarufu zaidi katika Bara la Afrika lakini pia akiwa ni miongoni mwa wachungaji matajiri zaidi katika Afrika.

Ilipofika saa nane mchana hakukuwa na mahali pa kukaa pale uwanjani. Huduma ya Ndondo hata hivyo ilikuwa imejiandaa. Kulikuwa na TV kubwa zilizowekwa kuzunguka uwanja wa Kirumba kwa ajili ya watu waliokuwa nje ya eneo lile. Vile vile TV nyingine ziliwekwa kwenye viwanja vya Furahisha, pamoja na viwanja vya shule za Nyamanoro na Nyakabungo ambapo maelfu ya watu ambao hawakupata nafasi ya kwenda Kirumba walisubiria kufuatilia moja kwa moja mahubiri ya Askofu Ndondo. Mamilioni ya Watanzania wengine yalisubiri kwa hamu mahubiri kupitia televisheni ya ITV ambayo ilikuwa imenunua haki za kurusha matangazo yale moja kwa moja. Baadhi ya TV za Kenya na DRC maeneo ya Katanga.

Saa tisa kamili juu ya alama uwanja wa CCM Kirumba ulilipuka kwa shangwe baada ya helikopta iliyombeba Askofu Damien Ndondo kuibukia upande wa Magharibi wa uwanja ikitokea maeneo ya Pasiansi kiliko kiwanja cha ndege. Kelele na vigelele vilivyolipuka uwanjani hapo havikuweza kuzuia sauti ya ngurumo ya helikopta ile ambayo ilitumia dakika kadhaa kuuzunguka uwanja huku Askofu Ndondo.

Baada ya dakika chache za kuzunguka angani helikopta ya Askofu ilianza kushuka taratibu na kuchukua usawa wa sehemu iliyoandaliwa kwa ajili ya kutua. Sehemu ile ilikuwa imezungukwa na walinzi wa kanisa lake wakiwa katika sare zao nadhifu. Walinzi wale wapatao hamsini walikuwa wanahakikisha mtu hasogei karibu na sehemu ya helikopta kutua. Sehemu ile iliachwa wazi huku herufi kubwa ya “H” iliyoandikwa kwa chokaa ikionekana. Ilimaanisha ni eneo la kutulia helikopta.

Ngurumo ilibadilika na kuashilia taratibu za kuizima zimeanza. Baada ya mapangaboi kutulia mlango wa helikopta ulifunguliwa na wa kwanza kutoka alikuwa ni mpambe wa Askofu Mkuu Ndondo ambaye alikuwa kama yule askari wa Jeshi la Wananchi ambaye huwa anafuatana na Rais mahali popote anapokwenda. Mpambe wa Ndondo alikuwa amevaa sare za kampuni yake ya ulinzi ambayo ilikuwa ni ya rangi nyeupe, huku akivaa kofia kama ya kiaskari ikiwa na nembo yenye msalaba na maua. Alikuwa na nyota nne mabegani ziking’ara. Walifuatia walinzi wengine wawili kasha First Lady Grace na ndipo Askofu Ndondo mwenyewe aliteremka. Mpiga video wa kanisa ambaye alikuwa anarusha moja kwa moja safari ya Askofu Ndondo kuanzia wakiwa uwanja wa ndege. Alitua jijini Mwanza na ndege yake ya Gulfstream na kuchukua helikopta kuelekea uwanjani.

Sauti za vigelegele na shangwe za vijana zilizizima pale uwanjani wakati Askofu Mkuu Ndondo aliposimama na kupunga mikono. Askofu Ndondo alikuwa amevalia suti nyeupe, huku ndani akiwa amevaa shati la Kiaskofu la rangi nyekundu, msalaba wake haukuwa kifuani bali ulichomekwa kwenye mfuko wake wa kushoto wa shati lake. Mke wa Askofu Grace Ndondo naye alikuwa amevaa gauni zuri la rangi ya zambarau lililombana mwili kiasi. Mabinti wawili wa kanisa waliovalia suti za kike walikuwa ni wapambe maalum wa Grace Ndondo; wao walikuwa wanawasubiria pale uwanjani. Waliwapungia mkono watu na taratibu wakiongozwa na wapambe wao huku wakifuatiwa na ujumbe wao waliteremka jukwaa lile maalum la kutua helikopta. Viongozi wengine wa mkoa na wa makanisa mbalimbali walikuwepo pale kumpokea Askofu Mkuu Ndondo. Kiongozi pekee ambaye hakuweza kuhudhuria alikuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki la Mwanza, Mhashamu Yuda Ruwa’ichi O.F.M. Cap.

Alipomaliza kusalimiana nao tu aliingia kwenye gari la wazi la Bentley Bentayga la rangi nyeusi. Gari hilo lilikuwa ni miongoni mwa magari magari ya kifahari na ghali zaidi duniani. Mara baada ya Askofu, Grace na Mpambe wa Askofu kuingia kwenye gari lile, pikipiki kumi na mbili zilikuwa tayari kuanza msafara wa kuzunguka ndani ya uwanja kusalimia maelfu na makumi ya elfu ya watu waliojaa pale uwanjani. Pamoja na msafara wa pikipiki na magari mawili yaliyotangulia mbili Askofu alikuwa kama Rais akiwa tayari kuhudhuria sherehe za kitaifa. Alizunguka taratibu huku kwaya ikiendelea kupiga nyimbo mbalimbali za sifa kwenye jukwaa kuu. Ilichukua kama dakika kumi na tano kwa Askofu Ndondo kukamilisha mzunguko na alipofika pale walipoegesha Helikopta waliteremka na Askofu alitembea katikati ya uwanja akipita kama Musa alivyopita na wana wa Israeli kwenye bahari ya Shamu.

Wamama walirusha kanga zao kuzitandika chini wakati Askofu, mke wake na wapambe walipotembea kuelekea mwisho mwingine wa uwanja ambapo Jukwaa kuu kubwa lilikuwa limejengwa likitazama upande wa Magharibi. Watu walijaribu kumgusa, na wengine wakiomba baraka mbalimbali huku wakimpa vitu aviguse ili vipate upako wake. Alipofika jukwaa kuu viongozi wote na wageni waalikwa walisimama kumkaribisha tena na walikuwa tayari kwa ajili ya mkutano mkubwa kabisa wa Injili Tanzania.

Baada ya taratibu zote za kukaribishwa na kutambulisha wageni mbalimbali, kwaya mbalimbali zilianza kuhudumu huku watu wakiendelea kusubiri kwa hamu muda ufike Askofu Mkuu Ndondo apande jukwaani. Kulikuwa na upako wa aina ya pekee. Upako ambao maelfu ya watu waliamini upo, upako ambao hakuna aliyetaka kuukosa na wale ambao waliwahi kuupata hawakutaka kukosa upako mara mbili.

Saa kumi na moja na nusu Mtumishi wa Mungu, Askofu na Mjumbe wa Nyakati za Mwisho, Nabii na Balozi wa Serikali ya Mbinguni kama alivyokuwa ameanza kujiita wiki chache kabla alikuwa anapanda jukwaani. Alipopewa tu kipaza sauti na kukishika mkononi taa kubwa za uwanja ule zote ziliwashwa kama ishara kuwa mambo pale uwanjani yalikuwa yameiva. Hakuna aliyetaka kupitwa na lolote.

Askofu Ndondo aliuangalia umati ule, alinyosha mkono wake juu kuubariki, aliongoza kuimba wimbo maarufu wa Baba wa Mbinguni Nyosha Mkono Wako huku kwaya ikimsindikiza kwa muziki murua ukiwa na tarumbeta na magitaa yakicharazwa kiufundi. Umati uliitikia kwa shangwe kwani wimbo huo uliweza kuimbwa kwa lugha mbalimbali. Na walipoimba kwa Kisukuma vigelegele na kelele za shangwe zilipaa tena. Kwaya ambayo ilikuwa inaongoza ilikuwa ni ile ya Mavuno ikishirikiana na Bendi ya Hossana Life Ministry ya kutoka Entebbe Uganda ikiwa na mwimbaji Leona Mukasa.

Ujumbe wa Askofu Mkuu wiki ile ulijengwa kutoka kitabu cha Ufunuo wa Yohana 22:17 ambapo imeandikwa “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure”.

Mahubiri yalikuwa motomoto, Askofu alikuwa ni kama mwigizaji mahiri aliyeweza kumudu jukwaa lake vilivyo. Aliweza kupaza sauti na kuishusha kwa mbwembwe. Mifano yake iliendana na vichekesho na kila baada ya muda aliwahimiza watu wamshangilie Mfalme wa Serikali ya Mbinguni, huku akiwauliza watu waseme Amina, na kuwaambia warudie tena kusema Amina. Maelfu ya watu walifuatilia mahubiri yale, huku wakijihisi wanabarikiwa kwa kila namna. Michango ya watu kwenye kurasa za Facebook na Instagram zilikuwa zikitoa maneno mengi ya shukrani na kuonesha kuguswa na ujumbe.

Mtu pekee ambaye hakutaka kusikia habari za maji ya uzima wala chupa yake wala kuyaona yana rangi gani hakutaka kuwepo mahali popote alipo Askofu Ndondo. Mtu huyo alitoa udhuru wa kutokuweza kuongoza ibada licha ya kuahidiwa mamilioni ya shilingi na kuombwa kusahau yaliyotokea kwa sababu yalikuwa ni madhaifu ya kibinadamu. Jina la Askofu Ndondo kwake lilikuwa ni kama ubini wa shetani. Mtu huyo hakuwa tayari kuona watu wengine wanaingia kwenye mikono ya Askofu Ndondo. Alitambua kuwa Askofu alikuwa ni mtu hatari. Mtu huyo alikuwa ameapa kwa maisha yake kumuangusha Askofu Ndondo haraka iwezekanavyo, kwa namna yeyote inavyowezekana, na mahali popote itakapowezekana. Aliamini Askofu Ndondo alikuwa ni Mjumbe wa Shetani.

(Itaendelea)
 
SURA YA 12
(Inaendelea)

TANGU MAPEMA ASUBUHI siku ile ya Jumatatu watu walianza kutiririka taratibu kuelekea Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza wakitokea katika viunga mbalimbali vya jiji hilo. Kina mama na watoto wao migongoni, huku wengine wakishikwa mikononi, wazee na fimbo zao za kutembelea na vijana na baskeli zao huku wengine wakitembea kwa miguu kila mmoja na simu mkononi walielekea Kirumba. Milango ya uwanja wa Kirumba ilifunguliwa tangu saa kumi na mbili asubuhi na watu walianza kuingia toka mida hiyo na ilipofika saa nne asubuhi, mzunguko wa uwanja ulikuwa tayari umejaa.

Watu waliruhusiwa siyo tu kukaa kwenye mzunguko bali pia kukaa katikati kabisa kwenye eneo la kuchezea mpira ambapo viti kwa maelfu vimepangwa vizuri kabisa kuelekea upande mmoja wa goli katika uwanja huo wa kabumbu. Upande ule ambapo viti vilielekezwa ndiko jukwaa kubwa lilikuwa limejengwa. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa mkutano mkubwa wa Injili kama ule kuruhusiwa kufanyika ndani ya uwanja wa CCM Kirumba. Uwanja ule ulichaguliwa kwa sababu ndio ulikuwa na eneo kubwa la kuweza kuchukua maelfu ya watu kwa wakati mmoja katika mazingira salama pale jijini Mwanza.

Watu walitoka nje ya Jiji la Mwanza kutoka mikoa ya Shinyanga, Mara, Geita, na Simiyu walikuwa wameingia mjini, wengi siku moja kabla. Kwa wakazi wa Mwanza ujio wa mkutano mkubwa wa Injili wa Askofu Mkuu Ndondo ulikuwa ni neema kubwa kwa wenye mahoteli, nyumba za kulala wageni, na biashara mbalimbali. Mkutano wa Kanisa la Mavuno ulileta mavuno ya neema kwa kila mtu mwenye akili ya kuchakarika.

Wale waliofika siku moja au mbili kabla waliweka kambi nje ya uwanja kama watu wanavyofanya huko Marekani wanaposubiria simu mpya za Iphone au kuwahi kufanya manunuzi yenye punguzo kubwa la bei wakati wa Krismasi. Polisi kutoka mikoa mitano jirani waliletwa jijini Mwanza kuongeza nguvu. Harufu ya ujio wa Nabii na Mtume Damien Ndondo ilikuwa imetanda kwa siku kadhaa katika anga zima la jiji la Mwanza, lenye maji baridi na samaki watamu waliosifiwa na Dkt. Remmy Ongala. Mkutano huo haukuvutia wenyeji tu bali hata raia wa kigeni ambao walikuwa wanatembelea Tanzania. Wageni wengi waliamua kutumia muda Jijini Mwanza kushuhudia mkutano huo mkubwa kama sehemu ya utalii pia.

Malori makubwa kumi ya aina ya Fuso Fighter yalikuwa yametangulia wiki moja kabla yakiwa na vifaa na vyombo vyote vitakavyohitajika kufanikisha mkutano. Malori yote yalikuwa yameandikwa pembeni kwa maandishi makubwa “Huduma ya Mavuno”. Magari mengine madogo yalibeba wafanyakazi mbalimbali na wahudumu wengine ambao jukumu lao ilikuwa ni kusimamia maandalizi ya mkutano, wote wakitoka makao makuu Dar-es-Salaam. Jukumu kubwa la timu hiyo iliyotangulia ilikuwa kuhakikisha kuwa dakika ambayo Askofu Mkuu, Nabii na Mtumishi wa Mungu Damien Ndondo anasimama jukwaani kila kitu kinaenda kwa ufanisi wa hali yajuu. Hakuna kitu ambacho Ndondo hakukipenda wala kukizoea kama watu kufanya kazi bila ufanisi wa hali ya juu. Kuanzia sauti, eneo, umeme na kila kitu ambacho kilihitajika kifanye kazi yake basi ilikuwa ni jukumu la timu hiyo kuhakikisha kinafanya hivyo. Wao walikuwa ni kwanza kufika na ni wa mwisho kuondoka.

Mazoezi ya vyombo na mitambo yote pamoja na kwaya zote yalifanyika siku ya Jumamosi siku moja kabla ya kuanza kwa mkutano. Pamoja na kuwa na genereta zao wenyewe kusimamia mifumo mikubwa ya utangazaji, huduma ya Ndondo ilitumia pia umeme wa nguvu za jua hasa kwenye matumizi ya taa pale uwanjani ambazo ziliongezwa kwani uwanja wa CCM Kirumba haukuwa na taa za kutosha za kisasa kuweza kumulika ndani na nje ya uwanja. Hii ilisaidia kupunguza kutegemea huduma ya umeme wa Tanesco na hawakutaka kutumia umeme huo sana kwani kama wangetumia basi kungekuwa na upungufu wa umeme kwa Jiji la Mwanza.

Uamuzi wa kuja na mtambo wao za kuzalisha umeme ulisaidia pia kuishawishi serikali kuruhusu kutumiwa kwa uwanja huo maarufu ambao huwa unatumiwa na timu za Pamba na Toto African za Jijini humo. Umeme wa ziada uliozalishwa uliingizwa kwenye maduka ya eneo lile na kuleta afueni kwa muda wa wiki nzima mkutano ulikuwa unafanyika. Hakuna mtu aliyetaka kupitwa na ujio wa Askofu Mkuu Ndondo. Kwa wakazi wa Mwanza iliwakumbushia ujio wa Mtakatifu Papa Yohani Paulo II mwaka 1990 kwenye kilima cha Kawekamo upande wa Magharibi wa jiji hilo kuelekea Uwanja wa Ndege. Wakatoliki kwa Wapentekoste, Walutheri kwa Waangalikana, Waislamu kwa Wahindu wote walitaka angalau kumuona mtu ambaye alitajwa kuwa ni miongoni mwa wachungaji maarufu zaidi katika Bara la Afrika lakini pia akiwa ni miongoni mwa wachungaji matajiri zaidi katika Afrika.

Ilipofika saa nane mchana hakukuwa na mahali pa kukaa pale uwanjani. Huduma ya Ndondo hata hivyo ilikuwa imejiandaa. Kulikuwa na TV kubwa zilizowekwa kuzunguka uwanja wa Kirumba kwa ajili ya watu waliokuwa nje ya eneo lile. Vile vile TV nyingine ziliwekwa kwenye viwanja vya Furahisha, pamoja na viwanja vya shule za Nyamanoro na Nyakabungo ambapo maelfu ya watu ambao hawakupata nafasi ya kwenda Kirumba walisubiria kufuatilia moja kwa moja mahubiri ya Askofu Ndondo. Mamilioni ya Watanzania wengine yalisubiri kwa hamu mahubiri kupitia televisheni ya ITV ambayo ilikuwa imenunua haki za kurusha matangazo yale moja kwa moja. Baadhi ya TV za Kenya na DRC maeneo ya Katanga.

Saa tisa kamili juu ya alama uwanja wa CCM Kirumba ulilipuka kwa shangwe baada ya helikopta iliyombeba Askofu Damien Ndondo kuibukia upande wa Magharibi wa uwanja ikitokea maeneo ya Pasiansi kiliko kiwanja cha ndege. Kelele na vigelele vilivyolipuka uwanjani hapo havikuweza kuzuia sauti ya ngurumo ya helikopta ile ambayo ilitumia dakika kadhaa kuuzunguka uwanja huku Askofu Ndondo.

Baada ya dakika chache za kuzunguka angani helikopta ya Askofu ilianza kushuka taratibu na kuchukua usawa wa sehemu iliyoandaliwa kwa ajili ya kutua. Sehemu ile ilikuwa imezungukwa na walinzi wa kanisa lake wakiwa katika sare zao nadhifu. Walinzi wale wapatao hamsini walikuwa wanahakikisha mtu hasogei karibu na sehemu ya helikopta kutua. Sehemu ile iliachwa wazi huku herufi kubwa ya “H” iliyoandikwa kwa chokaa ikionekana. Ilimaanisha ni eneo la kutulia helikopta.

Ngurumo ilibadilika na kuashilia taratibu za kuizima zimeanza. Baada ya mapangaboi kutulia mlango wa helikopta ulifunguliwa na wa kwanza kutoka alikuwa ni mpambe wa Askofu Mkuu Ndondo ambaye alikuwa kama yule askari wa Jeshi la Wananchi ambaye huwa anafuatana na Rais mahali popote anapokwenda. Mpambe wa Ndondo alikuwa amevaa sare za kampuni yake ya ulinzi ambayo ilikuwa ni ya rangi nyeupe, huku akivaa kofia kama ya kiaskari ikiwa na nembo yenye msalaba na maua. Alikuwa na nyota nne mabegani ziking’ara. Walifuatia walinzi wengine wawili kasha First Lady Grace na ndipo Askofu Ndondo mwenyewe aliteremka. Mpiga video wa kanisa ambaye alikuwa anarusha moja kwa moja safari ya Askofu Ndondo kuanzia wakiwa uwanja wa ndege. Alitua jijini Mwanza na ndege yake ya Gulfstream na kuchukua helikopta kuelekea uwanjani.

Sauti za vigelegele na shangwe za vijana zilizizima pale uwanjani wakati Askofu Mkuu Ndondo aliposimama na kupunga mikono. Askofu Ndondo alikuwa amevalia suti nyeupe, huku ndani akiwa amevaa shati la Kiaskofu la rangi nyekundu, msalaba wake haukuwa kifuani bali ulichomekwa kwenye mfuko wake wa kushoto wa shati lake. Mke wa Askofu Grace Ndondo naye alikuwa amevaa gauni zuri la rangi ya zambarau lililombana mwili kiasi. Mabinti wawili wa kanisa waliovalia suti za kike walikuwa ni wapambe maalum wa Grace Ndondo; wao walikuwa wanawasubiria pale uwanjani. Waliwapungia mkono watu na taratibu wakiongozwa na wapambe wao huku wakifuatiwa na ujumbe wao waliteremka jukwaa lile maalum la kutua helikopta. Viongozi wengine wa mkoa na wa makanisa mbalimbali walikuwepo pale kumpokea Askofu Mkuu Ndondo. Kiongozi pekee ambaye hakuweza kuhudhuria alikuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki la Mwanza, Mhashamu Yuda Ruwa’ichi O.F.M. Cap.

Alipomaliza kusalimiana nao tu aliingia kwenye gari la wazi la Bentley Bentayga la rangi nyeusi. Gari hilo lilikuwa ni miongoni mwa magari magari ya kifahari na ghali zaidi duniani. Mara baada ya Askofu, Grace na Mpambe wa Askofu kuingia kwenye gari lile, pikipiki kumi na mbili zilikuwa tayari kuanza msafara wa kuzunguka ndani ya uwanja kusalimia maelfu na makumi ya elfu ya watu waliojaa pale uwanjani. Pamoja na msafara wa pikipiki na magari mawili yaliyotangulia mbili Askofu alikuwa kama Rais akiwa tayari kuhudhuria sherehe za kitaifa. Alizunguka taratibu huku kwaya ikiendelea kupiga nyimbo mbalimbali za sifa kwenye jukwaa kuu. Ilichukua kama dakika kumi na tano kwa Askofu Ndondo kukamilisha mzunguko na alipofika pale walipoegesha Helikopta waliteremka na Askofu alitembea katikati ya uwanja akipita kama Musa alivyopita na wana wa Israeli kwenye bahari ya Shamu.

Wamama walirusha kanga zao kuzitandika chini wakati Askofu, mke wake na wapambe walipotembea kuelekea mwisho mwingine wa uwanja ambapo Jukwaa kuu kubwa lilikuwa limejengwa likitazama upande wa Magharibi. Watu walijaribu kumgusa, na wengine wakiomba baraka mbalimbali huku wakimpa vitu aviguse ili vipate upako wake. Alipofika jukwaa kuu viongozi wote na wageni waalikwa walisimama kumkaribisha tena na walikuwa tayari kwa ajili ya mkutano mkubwa kabisa wa Injili Tanzania.

Baada ya taratibu zote za kukaribishwa na kutambulisha wageni mbalimbali, kwaya mbalimbali zilianza kuhudumu huku watu wakiendelea kusubiri kwa hamu muda ufike Askofu Mkuu Ndondo apande jukwaani. Kulikuwa na upako wa aina ya pekee. Upako ambao maelfu ya watu waliamini upo, upako ambao hakuna aliyetaka kuukosa na wale ambao waliwahi kuupata hawakutaka kukosa upako mara mbili.

Saa kumi na moja na nusu Mtumishi wa Mungu, Askofu na Mjumbe wa Nyakati za Mwisho, Nabii na Balozi wa Serikali ya Mbinguni kama alivyokuwa ameanza kujiita wiki chache kabla alikuwa anapanda jukwaani. Alipopewa tu kipaza sauti na kukishika mkononi taa kubwa za uwanja ule zote ziliwashwa kama ishara kuwa mambo pale uwanjani yalikuwa yameiva. Hakuna aliyetaka kupitwa na lolote.

Askofu Ndondo aliuangalia umati ule, alinyosha mkono wake juu kuubariki, aliongoza kuimba wimbo maarufu wa Baba wa Mbinguni Nyosha Mkono Wako huku kwaya ikimsindikiza kwa muziki murua ukiwa na tarumbeta na magitaa yakicharazwa kiufundi. Umati uliitikia kwa shangwe kwani wimbo huo uliweza kuimbwa kwa lugha mbalimbali. Na walipoimba kwa Kisukuma vigelegele na kelele za shangwe zilipaa tena. Kwaya ambayo ilikuwa inaongoza ilikuwa ni ile ya Mavuno ikishirikiana na Bendi ya Hossana Life Ministry ya kutoka Entebbe Uganda ikiwa na mwimbaji Leona Mukasa.

Ujumbe wa Askofu Mkuu wiki ile ulijengwa kutoka kitabu cha Ufunuo wa Yohana 22:17 ambapo imeandikwa “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure”.

Mahubiri yalikuwa motomoto, Askofu alikuwa ni kama mwigizaji mahiri aliyeweza kumudu jukwaa lake vilivyo. Aliweza kupaza sauti na kuishusha kwa mbwembwe. Mifano yake iliendana na vichekesho na kila baada ya muda aliwahimiza watu wamshangilie Mfalme wa Serikali ya Mbinguni, huku akiwauliza watu waseme Amina, na kuwaambia warudie tena kusema Amina. Maelfu ya watu walifuatilia mahubiri yale, huku wakijihisi wanabarikiwa kwa kila namna. Michango ya watu kwenye kurasa za Facebook na Instagram zilikuwa zikitoa maneno mengi ya shukrani na kuonesha kuguswa na ujumbe.

Mtu pekee ambaye hakutaka kusikia habari za maji ya uzima wala chupa yake wala kuyaona yana rangi gani hakutaka kuwepo mahali popote alipo Askofu Ndondo. Mtu huyo alitoa udhuru wa kutokuweza kuongoza ibada licha ya kuahidiwa mamilioni ya shilingi na kuombwa kusahau yaliyotokea kwa sababu yalikuwa ni madhaifu ya kibinadamu. Jina la Askofu Ndondo kwake lilikuwa ni kama ubini wa shetani. Mtu huyo hakuwa tayari kuona watu wengine wanaingia kwenye mikono ya Askofu Ndondo. Alitambua kuwa Askofu alikuwa ni mtu hatari. Mtu huyo alikuwa ameapa kwa maisha yake kumuangusha Askofu Ndondo haraka iwezekanavyo, kwa namna yeyote inavyowezekana, na mahali popote itakapowezekana. Aliamini Askofu Ndondo alikuwa ni Mjumbe wa Shetani.

(Itaendelea)
Twaisubir mkuu
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom