Riwaya:Mfuasi

Riwaya:Mfuasi

winston20

JF-Expert Member
Joined
Jun 21, 2020
Posts
1,116
Reaction score
2,320
MFUASI
01

* *

Usiku ni rafiki wa giza! Naam. Giza hupambwa na nyota! Ndivyo. Lakini usiku huu haupo hivyo! Giza limenuna hakuna pambo za nyota wala nuru ya mwezi. Wingu zito limeteka utawala wa anga. Mvua kubwa inazidi kuichapa ardhi kibabe. Ngurumo za radi zinarindima kishari. Vijiji vyote kimya…!

Ingawa ni kawaida kunyesha mvua kipindi cha majira ya masika, lakini mvua ya usiku huu imekuwa zaidi ya kawaida. Mvua ya radi zisizokoma. Kila miale mikali ya mwangaza wa radi ilipochanua, giza lilichanika kwa sekunde chache kabla ya ngurumo kali kutoa kishindo kama bomu.

Kila kiumbe kilijituliza mahala pake. Zaidi ya kelele za radi na mvua, hakukusikika sauti ya mtu, mnyama wala ndege. Kwa kifupi usiku huu ulikuwa wa kuogofya mno.

Katikati ya barabara anaonekana mtu mmoja akitembea kwa kupepesuka. Mwanaume wa makamo, mrefu mweusi. Amevaa nguo chakavu zilizoacha baadhi ya sehemu za mwili wake nje. Suruali kuu-kuu, shati limechanika, amelowa chapachapa, miguuni anapekua. Mvua ikizidi kumchapa bila huruma radi zikimkea kwa hasira.

Miguu yake ikakosa stamala ikaanza kugongana mwili ukamtetema. Ingawa alijitahidi kujilazimisha kwenda lakini mwishowe akajikuta anashindwa na kuanguka kama mzigo.

“Aaaagh!” Sauti ya hamaki ikamtoka. Damu zilikuwa zikimvuja magotini, hakujali. Akasimama tena mkononi amekumbatia kwa umakini mkoba mdogo. Kwa mwendo wa kujilazimisha akainyanyua miguu kwenda lakini ikamsaliti tena, akaanguka kama mzigo kwa mara nyengine, Puu..!

“Aaaahh…! Oooophhuuh!” Akaugua na kuhema kwa nguvu akiwa amelala chali pembezoni mwa ile barabara. Mkoba wake akaukumbatia kwa mikono miwili kifuani mwake. Mvua nayo haikumwonea haya, ikamchalaza hadi machoni na kujikuta akifumba macho na kuachama mdomo.

Usoni anaonekana kama bondia aliyetoka kupokea kichapo kikali. Macho yamemvimba mdomo umechanika!

Kulikoni…? Nini kimempata….! Yeye ni nani?

Hakuna alichokuwa anakumbuka wala hakuonesha kama ni mtu mwenye akili timamu. Kucha ndefu mikono yote! Nywele zake msitu hazitamaniki! Ndevu zimemwota ovyo na kumpa mwonekano wa mwehu.

Baada ya muda akajitahidi kukusanya nguvu ili anyanyuke kwa mara nyengine tena. Lool! Safari hii akashindwa kabisa hata kusimama, akaangukia ubavu palepale chini. Akajisonya na kutukana kwa sauti ya shida huku akijitahidi kukaa kitako, akafanikiwa.

Baada ya kukaa na kuvuta pumzi, ndipo alipochana kipande cha shati lake na kujifunga kwa nguvu mkono wa kushoto. Alipojiridhisha akafungua zipu ya ule mkoba wake wenye umbo la kisanduku. Akaanza kutafuta kitu mkobani kwa shida huku akitetemeka mikono. Mwangaza wa radi ukamsaidia kuona alichokuwa anahitaji.

La haula! Mkoba ulikuwa na mabomba kadhaa ya sindano zilizobanwa vyema. Akachomoa moja na kuufunga kabla hajajituliza kwa umakini na kuanza kujidunga kwenye mshipa wa ule mkono aliojifunga kwa kipande cha shati.

Hakujali mvua, kelele za radi wala pale alipokaa pembezoni mwa barabara. Taratibu akaanza kujikamulia dawa iliyokuwa ndani ya lile bomba huku akivuta hisia za kujisikia vizuri.

“IZANI…!”

Ghafla sauti ya mwanamke ikasikika na kumfanya asite kujikamulia dawa na kutega sikio. Akatazama kushoto kulia, Giza nene halikumpa nafasi ya kuona chochote. Akapuuza na kumalizia kujidunga kabla hajatupa pembeni bomba la sindano huku akipumua kama mtu aliyejitua mzigo uliomuelemea.

“IZANI..!”

Kwa mara ya pili sauti ikasikika tena kwa ukaribu zaidi. Ni wazi aliuhisi ukaribu wa sauti ya mwanamke huyo aliyemwita. Mwangaza wa radi ukatanda tena kwa sekunde chache hakuona kitu. Ngurumo kubwa ikafatia na kumfanya atulie zaidi na kujikunja pale chini akisikilizia dawa aliyojidunga ikitembea mwilini mwake na kumliwaza. Hakuzingatia chochote zaidi umakini wake ukawa kwenye mkoba aliouweka katikati ya miguu yake. Lakini mara sauti ya mwanamke ikaanza kumsumbua tena kichwani mwake naye hakutaka kuisikia wala kuiitika.

Akaanza kujipigapiga kichwani kama anayewashwa na nywele huku akiunguruma kama beberu lililoasiwa akibishana na hisia zake.

“Ni mimi Mfuasi wako Izani!” Sauti ya mwanamke ikasikika vyema kwa mara nyengine. Akataharuki zaidi baada ya kuzihisi hatua za mtu akitembea kumuelekea. Ndipo akanyanyua uso kutazama. Laa! Hakuona kitu ingawa mbele yake kulitokea nuru ya ajabu.
Mwanamke mrembo akaonekana ndani ya mwanga wa ile nuru akimsogelea karibu yake.

“Ina maana nawe pia hunioni Izani? Ni mimi Izani! Mimi Mfuasi wako.” Taswira ya mwanamke ikaongea tena na kumfanya yule bwana azidi kutaharuki.

“Mfuasi? Naniii Izaa-ani! Hahahah” Akauliza mara akajichekesha mwenyewe kama mwehu. Sauti yake ilibobea uraibu wa madawa ya kulevya. Mdomo wake ulizidiwa uzito na ulimi. Akazidi kubwabwaja yule kijana.. Akatumbua macho kama mjusi aliyebanwa na mlango, huku akipapasa kumtafuta mwanamke aliyemsemesha bila mafanikio.

“Pole sana Izani! Nisamehe Izani!…Nisamehe mimi Mfuasi wako!” Safari hii sauti ya yule mwanamke ikasikika kwa huzuni sana na kusindikizwa na kilio cha kwikwi. Mara Nuru ikaanza kufifia na mwangaza kupotea.

Giza nene likatawala tena eneo lote kama awali ingawa mvua ilipungua sasa. Yule kijana akajikuta amepata nguvu ya kusimama tena na kuanza kuchechemea kuendelea na safari yake isiyoeleweka usiku ule wa manane.

***

MIKOCHENI | DAR ES SALAAM

Katika jumba la kifahari la Mchungaji maarufu aliyeheshimika nchini, NDIMBO MASIZI, sala maalum ilikuwa inaendelea usiku wa manane.

Akiwa amesimama sebuleni sambamba na familia yake, mke na watoto wawili, Mchungaji Ndimbo Masizi akazidi kuwaongoza kuomba huku wote wamefumba macho kwa hisia.

“Baba! siku ya tatu leo tunakesha kukushukuru na kutaka ulinzi wako uinuke, tunakuomba bwana usiikaribishe tena halufu ya mauti ndani ya nyumba hii….! Nakemea na kulifungia pepo la mauti lisimguse yeyote kati yetu…! Tunasema asante kwa kumnyakua binti yetu Eeeh yehova! Japo tulimpenda lakini tunajua mapenzi yako ni makuu sana. Mfungulie mlango wako na utulinde na shari zote. Oooh! Katika jina la mwanao Yesu Kristo tunaomba na kuamini….Ooooh Yehova”

“AMEEEN!” Familia ikaitikia kwa imani kila alivyokuwa anaomba.

Ilikuwa ni wiki moja imepita tangia wampumzishe binti yao kipenzi ANITA kwenye makazi ya milele. Anita alifariki baada ya kuugua kwa muda mfupi. Hakika ulikuwa msiba mkubwa kwa familia na wote waliokuwa karibu na Mchungaji Ndimbo, ndugu na marafiki wa Anita.

Kanisani walifanya ibada maalum baada ya maziko kwa kukesha siku tatu. Na baada ya hapo mkesha ukawa umehamia nyumbani kwake akiongoza maombi mwenyewe.

Usiku huu ulikuwa ndio wa mwisho kukamilisha siku sita za mkesha wa kumuombea Anita na kuibariki upya nyumba yao baada ya msiba.

Wakati wanaendelea na maombi mara umeme ukazimika ghafla. Jumba zima likawa giza lakini hakuna aliyehisi chochote. Dakika chache mara mwangaza mkali ukamulika katikati yao lakini ajabu pia hakuna aliyegutuka wala kufumbua macho. Wote walizama kwenye kina cha maombi. Kwa sekunde chache mwangaza ule ukaanza kufifia na mara umeme ukawaka tena.

Ajabu! Katikati ya duara waliposimama akaonekana binti mrembo akilia kwa uchungu na kuzungumza kwa fadhaa.

“Oooh! Hapana…! Mama fumbua macho. Doris, Papii, fumbueni macho! Niko hapa. Niko hapa mama nisikieniii.” Licha ya kuongea kwa sauti yule binti hakusikiwa na yeyote kati yao wala kumuhisi. Ndipo akajaribu kupiga hatua kuwashika ili awatingishe lakini akapitiliza asifanikiwe.

“Haaah!” Akafadhaika na kuishia kuwatazama kwa hadaiko asijue cha kufanya.

Lakini mara akamshuhudia mchungaji Ndimbo akifumbua macho huku akiendelea kunena kwa lugha isiyoeleweka. Macho ya binti yalipoutazama uso wa mchungaji, akajikuta anapoteza furaha na kukunja sura, ghadhabu zikimjaa kifuani.

“Shetani! Unaniona?” Binti akauliza huku akimtazama kwa hasira mchungaji Ndimbo Masizi.

“Wewe Shetani mwenye sura ya Malaika!” Binti akaipaza tena sauti huku akimsogelea Mchungaji Ndimbo kwa hasira. Akamnyanyulia mkono na kumnasa kofi kwa nguvu lakini mkono wake ukapitiliza hakumgusa. Hamaniko likamvaa upya binti akajikuta akijililia kwa maumivu ya kuhakiki ukweli wa hali yake.

Anita! Wewe ni Nafsi isiyo na mwili sasa.

Sauti ikasikika ndani yake na kuziumiza hisia zake. Mwanaume aliyeamini ni baba yake kipenzi sasa anaamini ni Shetani mwenye sura ya Malaika.

Akamshuhudia mchungaji akizidisha sauti ya maombi yaliyomchefua Anita ambaye sasa ni nafsi isiyo na mwili.

“Asante bwana! Asante najua unanisikia. Haaaa! Mpokee binti yetu Anita kwenye makazi yako tulivu umpe raha za milele ee bwana..”

“NYAMAZAA!” Anita akafoka kwa sauti kali kumkatisha lakini haikusaidia chochote. Hasikiki na yeyote! Akabaki kushuhudia maombi yakiendelea huku akiwatazama kwa huruma waikitikiaji wasiojua chochote. Akajisogeza pembeni kwa huzuni na kuitazama picha yake kubwa iliyotundikwa ukutani akiwa ametabasamu.

Yeye ndiye Anita Ndimbo Masizi ambaye sasa inajulikana amefariki. Hakuwa na uwezo wa kuuishi tena ulimwengu aliouzoea japo bado anauona na kuusikia.

Siri ya kifo chake si siri tena kwake. Anaujua ukweli wa yote yaliyojificha nyuma ya ulimwengu aliotoka. Na sasa ana siku arobaini tu za kuushuhudia ulimwengu aliokatishwa maisha yake kabla hajawa mgeni ndani ya ulimwengu wa mauti.

“IZANI”

Akatamka huku akiitazama ile picha ambayo uhalisia wake ilichorwa kwa mkono. Tena ilichorwa kwa ustadi wa hali ya juu, na pembeni yake kuliandikwa tarehe na jina la mchoraji.

31 July 2018 Izani Nteze

“Nisamehe Izani!” Anita akajisemea kwa huzuni na hadaa. Kumbukumbu zikamchoma akiwa katika hali ya nafsi akiutazama ule mchoro na kuyaona yale ambayo yalijificha kwenye fahamu zake nyakati zile akiwa hai kimwili.

ITAENDELEA.....
 
MFUASI
02

Anita! Wewe ni Nafsi isiyo na mwili sasa.

Sauti ikasikika ndani yake na kuziumiza hisia zake. Mwanaume aliyeamini ni baba yake kipenzi sasa anaamini ni Shetani mwenye sura ya Malaika.

Akamshuhudia mchungaji akizidisha sauti ya maombi yaliyomchefua Anita ambaye sasa ni nafsi isiyo na mwili.

“Asante bwana! Asante najua unanisikia. Haaaa! Mpokee binti yetu Anita kwenye makazi yako tulivu umpe raha za milele ee bwana..”
“NYAMAZAA!” Anita akafoka kwa sauti kali kumkatisha lakini haikusaidia chochote. Hasikiki na yeyote! Akabaki kushuhudia maombi yakiendelea huku akiwatazama kwa huruma waikitikiaji wasiojua chochote. Akajisogeza pembeni kwa huzuni na kuitazama picha yake kubwa iliyotundikwa ukutani akiwa ametabasamu.

Yeye ndiye Anita Ndimbo Masizi ambaye sasa inajulikana amefariki. Hakuwa na uwezo wa kuuishi tena ulimwengu aliouzoea japo bado anauona na kuusikia.

Siri ya kifo chake si siri tena kwake. Anaujua ukweli wa yote yaliyojificha nyuma ya ulimwengu aliotoka. Na sasa ana siku arobaini tu za kuushuhudia ulimwengu aliokatishwa maisha yake kabla hajawa mgeni ndani ya ulimwengu wa mauti.

“IZANI”

Akatamka huku akiitazama ile picha ambayo uhalisia wake ilichorwa kwa mkono. Tena ilichorwa kwa ustadi wa hali ya juu, na pembeni yake kuliandikwa tarehe na jina la mchoraji.

31 July 2018 Izani Nteze

“Nisamehe Izani!” Anita akajisemea kwa huzuni na hadaa. Kumbukumbu zikamchoma akiwa katika hali ya nafsi akiutazama ule mchoro na kuyaona yale ambayo yalijificha kwenye fahamu zake nyakati zile akiwa hai kimwili.

_____***_____

31 JULAI 2018

Ilikuwa ni asubuhi ya siku ya kumbukizi ya kuzaliwa mtoto wa kwanza wa Mchungaji Ndimbo na Mkewe ambaye walibahatika kupata watoto watatu, mabinti wawili na wa kiume mmoja.

Anita Ndimbo Masizi, ndiye mkubwa akifuatiwa na mdogo wake wa kiume aliyeitwa PAPII, na kizuwanda chao aliitwa DORIS ambaye mwaka huo alitimiza miaka nane.

Siku hii ilikuwa maalum na ya kipekee sana kwa Anita. Si tu kwakuwa alikuwa anasherehekea kuzaliwa kwake, bali ni kwa kile alichokuwa anatimiziwa na mtu aliyempenda. Mwanaume aliyegusa hisia zake haswa na kuukonga moyo wake. Mwanaume huyu aliitwa Izani Nteze.

“Nakuahidi nitakuchora siku ya kuzaliwa kwako na picha hiyo itabaki kuwa alama muhimu ya upendo wangu kwako ewe mfuasi wangu.” Yalikuwa maneno ya Izani wiki moja kabla yaliyoutekenya moyo wa Anita na kumfanya acheke kizembe.

“Acha utani Izani! Hivi unajua kuchora kweli?” Anita akauliza kwa sauti ya kudeka.

“Siku ya ahadi ikifika nitatimiza ahadi yangu nawe utashuhudia.” Izani akajibu kwa uhakika wa kile asemacho huku akimtazama Anita usoni. Wakajikuta wote wanatabasamu na kutazamana kwa aibu. Walikuwa wamesimama nje ya geti la Kanisa walipoahidiana hayo.
Na kweli siku ya ahadi ikawadia, wakakutana asubuhi ndani ya ofisi ya kupiga picha iliyomilikiwa na mpiga kinanda wa kanisa.

Katika hali ambayo Anita hakuitarajia Izani akamchora kwa
ustadi mkubwa akamtoa kama alivyokuwa ameweka pose!
Masaa matatu tu! yalitosha Anita kutokea kwenye karatasi ya A3 kama alivyo. Hakuamini punde alipooneshwa mchoro wake.
“Woow! Izani haaaa! Jamani kumbe hodari hivi! Siamini.”

“Amini mfuasi wangu. Sasa unaweza kwenda kujiandaa na ratiba nyengine. Zawadi hii nitakuja nayo jioni ukumbini ikishakuwa imekamilika asilimia mia moja.” Izani akasema huku akimtazama Anita. Macho yao yakasema mengi kuliko midomo yao.

“Jamani asante sana Izani. Milele nitabaki kuwa mfuasi wako.” Anita akashukuru na kumkumbatia Izani kabla hajatoka akimuacha amalizie kuupamba mchoro wake.

Na kweli aliupamba kwa umaridadi mkubwa kabla hajauweka kwenye flemu nzuri ya kioo iliyovutia kutazama. Na hiyo ndiyo ikawa zawadi maalum iliyokonga moyo wa Anita Ndimbo ambaye alikuwa anatimiza miaka ishirini ya kuzaliwa kwake siku hiyo ya tarehe 31/07/2018

* *
IZANI NTEZE,

Ni Kijana aliyeapa na kujitolea maisha yake kupigana vita dhidi ya uraibu wa mihadarati na dawa za kulevya.

Alizaliwa Dar es salaam maeneo ya Tandale, na kukulia mitaa ya Uwanja wa fisi kwenye familia duni ambayo ilizamishwa na uraibu wa mihadarati.

Izani akajikuta akipitia nyakati ngumu ya makuzi yake yaliyobeba historia ya kuumiza. Makuzi yake ndiyo yakapelekea kujiapiza kusimama kwa imani kupambana na vile ambavyo aliamini ndivyo vyanzo vilivyomfanya apite kwenye mateso mazito akiwa angali mdogo.

“Baba yangu alikuwa sadali maarufu mtaani pia alikuwa mlevi sana. Mama yangu naye alikuwa muuza gongo. Mimi na kaka hatukuwahi kushuhudia mapenzi ya wazazi zaidi ya ugomvi wa mara kwa mara. Maisha yao ya kufukuzwa na Polisi mitaani yalitufanya hata tusiende shule. Nilishuhudia siku moja baba akimpiga mama kama mwizi nikaumia sana. Na siku nyengine sitoisahau mama alivyomvizia baba akampiga na chuma kichwani na kusababisha kifo chake baada ya damu nyingi kumvuja. Tokea hapo sikufanikiwa kumuona mama kwa zaidi ya miaka minne baada ya kutukimbia na kutuacha wenyewe.

Nilishuhudia maisha yetu yakizama tukiwa bado wadogo sana. Kaka yangu aliyebaki kama tegemezi aliuawa kwenye maandamano ya vurugu za Mitaa na Polisi. Nimeishi maisha ya kujilea mwenyewe tangia nina miaka kumi na tano. Nilikuja kupata taarifa mahala alipo mama yangu nikiwa na miaka kumi na saba. Nilifanikiwa kukutana naye tena lakini safari hii alikuwa si mama niliyemtambua. Alikuwa teja kabisa kwa matumizi yaliyokithiri ya dawa za kulevya.

Nasikitika kusema mama yangu madawa yalimuathiri sana na kumkaribishia magonjwa sugu kutokana na mtindo wa maisha aliyoanza kuyaishi tokea ametukimbia. Kifo chake kilitokea siku chache baada ya kumuona kwa mara nyengine. Mama yangu alikutwa amekufa kama mnyama kwenye jumba bovu.

Hili ndio tukio la mwisho lililoniliza na kunitoa hofu ya kukaa kimya. Hakika nilijiapiza siku ile nitayatumia maisha yangu yote yaliyosalia kupigana vita na mihadarati ambayo inasababisha vijana kama mimi na mitaa yetu kuzidi kufa ingali tukiwa hai. Na ndivyo nilivyoanza kampeni zangu za kuzunguka mitaani nikiwasihi wenzangu kutojitumbukiza kwenye shimo la mihadarati huku nikiitumia hadithi yangu kama mfano ulio hai kwa wengine wanaodhani mihadarati ni starehe. Hapana! Starehe ya kweli ni furaha iliyo ndani ya mtu.

Na furaha huchanua pindi mwili unapokuwa na afya njema. Na hivyo ndivyo nilivyoanza mpaka sasa namshukuru Mungu sauti yangu imeanza kusikika kwenye jamii. Nafurahi kwa kiasi chake kuishuhudia jamii mpya kwenye mitaa niliyokulia ambayo awali ilikithiri utumiaji wa mihadarati mpaka kwa watoto wa chini ya miaka kumi na mbili.

Hivi sasa vijana wanaelewa na hata wazee wanaamini kama inawezekana kwa kuzungumza tu. Hatuwezi kuwa watumwa wa mihadarati ndani ya falme zetu wenyewe. Mitaa bila dawa za kulevya inawezekana. Tukiamini tunaweza. Sihitaji shabiki wa kushabikia hili akaishia tu kushangilia…!

Bali nahitaji MFUASI wa kuungana nami bega kwa bega nyakati zote ili kwa pamoja tuzipaze sauti za ushindi na kuikomboa mitaa yetu kwenye shimo la mihadarati na dawa za kulevya. Tuitengeneze jamii mpya tukilinde kizazi chetu. Wakikosekana watumiaji hao wauzaji wataacha biashara yao hii haramu.“

Sauti ya Izani Nteze Ilisikika akizungumza huko mitaani alipohojiwa kwenye kipindi cha Habari za Kitaa na mtangazaji MARKUS MAKATA.

Haikuwa rahisi wala kutegemewa kwa wakazi wa jiji la Dar, hususani aliyeifahamu Tandale na uwanja wa fisi kama angeweza kutokea kijana mzawa wa maeneo hayo akaibuka kuwa shujaa wa kuwakomboa vijana katika utumiaji wa mihadarati kwa kuzungumza tu.

Hakika mwanzoni kilionekana kichekesho lakini mwishoni kikawa lulu na muujiza wa ajabu kwa Izani na waliomfahamu. Sauti yake na hadithi ya madhila yaliyomkuta ikageuka kuwa dawa kwa kila aliyemsikia .

Izani Nteze akiwa na miaka kumi na tisa tu, akafanikiwa kuwa kivutio kwa kila aliyesikia habari zake na vitendo vyake. Wengi wakasadiki kuwa maneno aliyokuwa anatamka hayakuendana na umri wake wala hakufanana nayo.

“Amini kwanza wewe ni bora kuliko chochote! Usiiweke imani yako iongozwe na vitu iwe vyakula, mavazi, ama chochote kilicho nje nawe. Amini starehe kubwa kwenye maisha ni furaha ambayo iko ndani yako na si kwenye vitu ambavyo matokeo yake vinakuja kuwa maumivu makubwa. Tandale bila madawa inawezekana….!

Vijana hatuwezi tena kukubali kuwa watumwa wa mihadarati ikiwa tunafahamu sasa sisi ndio Wafalme wa Kitaa! Kila anayekubali kitaa chake awe wa kwanza kukilinda. Na ili ukilinde kitaa chako linda Afya yako kwanza. Na madawa ya kulevya ama uraibu wowote uliokithiri unabomoa afya zetu za mwili na akili.

Nakuomba kaka yangu, dada yangu, kijana mwenzangu amka sasa na ukinge ngumi moja hewani uungane nasi kutokomeza madawa ya kulevya kitaani kwetu. Kila kitu kinaanza na sisi wenyewe. Vifo vya mihadarati na uraibu sasa vimekoma. Tusimame kama washindi hakika inawezekanaaaaa! Sihitaji mashabiki nahitaji wafuasi wa kusimama nami na kupaza sauti pamoja. Hakika inawezekanaaa!”

Kila aliposimama kuzungumza Izani aliikuna mioyo ya wengi na kuwashangaza. Watu wengi waliobahatika kumuona akizungumza walitumia simu zao kumrekodi na kumposti kwenye mitandao ya kijamii. Video zake zikasambaa.

Kila mtu akatoa mawazo yake kwa maono yake. Wapo waliomcheka kwa kumuona hajui akisemacho. Wengine walimhurumia kwa kuona anapoteza muda. Na baadhi walimuunga mkono kwa pongezi na kutamani waibuke vijana majasiri na wenye maono kama yeye. Na Kupitia mitandaoni huko ndipo Anita Ndimbo alipobahatika kumuona Izani Nteze kwa mara ya kwanza akavutiwa naye, akaanza kufatilia video zake.

Mwaka 2017 Izani akafungua akaunti yake ya kwanza facebook na kupost matukio yake mwenyewe ya harakati zake, huku mara nyingi alipokuwa anaandika alisisitiza hatafuti mashabiki bali anahitaji wafuasi wa kusimama naye pamoja.

Na huo ndio ukawa mlango kwa Anita Ndimbo kuingia katika mawasiliano na Izani Nteze kwa kutumia akaunti mpya iliyomtambulisha kwa jina la MFUASI.

Hakuweka picha yoyote kwenye akaunti hiyo wala hakuwa anapost vitu zaidi aliitumia kutumiana ujumbe na Izani akimpongeza na kumuuliza maswali tofauti ili apate kumfahamu kiundani.

Izani, wewe ni kijana wa ajabu sana. Umesema hujawahi kwenda shule! Sasa umejuaje kusoma na kuandika?

Ulikuwa moja ya jumbe za Anita alizomuandikia Izani facebook.
Maarifa huja kwa maamuzi. Niliamua kujua kusoma na nikajifunza kwa wanaojua na sasa najua kuandika hata kama kweli sikuwahi kwenda shule.

Majibu ya Izani yalizidi kumfurahisha Anita akaamini kijana yule ni tunu ya taifa. Ndipo siku moja majira ya jioni mwanzoni mwa mwaka 2018 Anita akiwa ameketi na baba yake sebuleni alianza kumpasha habari kuhusu Izani Nteze.

“Baba! Katika maisha yangu kuna mtu nimebahatika kumfahamu facebook ambaye amekuwa gumzo kwa kile anachokipigania mitaani, hakika naamini baba yangu kwa namna Mungu anavyokutumia utafurahi sana kumjua mtu huyu.” Anita akasema na kumfanya mchungaji Ndimbo akae kwa umakini kumsikiliza.

“.….Anaitwa Izani Nteze. Ni kijana mwenye imani sana baba.”

akaendelea huku akimpa simu baba yake baada ya kuweka moja ya video za Izani alizopakua mtandaoni.

Mchungaji Ndimbo akatabasamu alivyokuwa anatazama ile video na kumsikiliza kwa umakini Izani. Akajikuta anatingisha kichwa juu chini kukubaliana na maneno aliyokuwa anasikia Izani akitamka. Jambo hilo likamfurahisha Anita.

Lazima nimshawishi baba amfadhili Izani na kumuweka karibu yangu. Huyu ndiye mwanaume anayestahili kuwa nami maishani. Nami nimechagua kuwa Mfuasi wake.

Anita akawaza moyoni mwake. Na mara baba yake alipomaliza kuitazama ile video na kumrudishia simu, kabla hajafumbua kinywa kusema chochote akamuwahi tena. “Tazama na hii baba!” huku akimuwekea video nyengine na kumrejeshea simu janja yake. Mchungaji Ndimbo akazidi kutabasamu na kustaajabu maneno na ujasiri wa Izani.

“Halelluyah! Hakika bwana ana majeshi mengi na roho wake hajawahi kusinzia kufanya kazi ndani ya watu! Yaaashatarabusa-busina ghara-mashika buswaa!”

Baba Anita akajikuta mpaka ananena kwa lugha. Kisha Akamgeukia binti yake kumtazama kwa kumstaajabia.

“Mbona hukunambia mapema kuhusu huyu kijana?” akamuuliza
“Sikutaka niharakishe kukufikishia habari zake kabla sijajua kama ni tapeli au kweli anachokifanya anakiamini. Nimemchunguza tokea nikiwa chuo, huyu si tapeli ana imani hakika naamini anafaa kuwezeshwa huduma yake iwafikie wengi ambao wanadidimizwa na mihadarati huko mitaani.”

Anita akafafanua jibu lake. Baba yake akamkubalia.

Siku hiyo ndiyo akatumia kumshawishi baba yake awekeze kwenye mawazo ya kijana huyo ili iwe faida kwake na kwao mbele ya jamii.
“Naamini baba! Ukimpa hata kipindi kwenye TV yetu na akiwa anajumuika nasi kanisani itaongeza ushawishi mkubwa kwa watu na hamasa ya kumtumikia Mungu.”

Anita akapigilia msumali wa mwisho uliomfanya baba yake akose namna zaidi ya kukubaliana naye kwa dhati huku akimtaka afanye mawasiliano na Izani Nteze.

Na ndivyo ilivyokuwa!

Kwa mara ya kwanza Izani akapokea simu ya Anita akiwa hajui kama ndiye mtu aliyekuwa anachatigi naye kwa jina la Mfuasi. Kwenye mazungumzo yao, wakakubaliana kukutana uwanja wa fisi siku inayofata majira ya saa tisa alasiri.

Kama utani ikawa kweli, kesho yake saa tisa alasiri gari ya kifahari Mercedise Benz - New Model iliyokoza weusi ikakanyaga ardhi ya Tandale uwanja wa fisi kwa mara ya kwanza. Izani akiwa na rafiki zake nje ya saluni ya Zomboko, akaiona ile gari lakini hakuitilia maanani kama ndio usafiri wa Mfuasi wake. Lakini simu yake ilipoita na kupokea akajikuta moyo ukimdunda na kuisogelea ile Benz pale ilipoegeshwa.

“Waoo! Izani panda twende sehemu tulivu tukazungumze.”

Anita akazungumza akiwa amechanua tabasamu baada ya kushusha kioo punde Izani alipofika. Izani alijikuta kinywa kikiwa kizito kwa mshangao. Akaingia garini huku kichwani akimtafakari Mfuasi wake yule. Hata jamaa aliokaa nao pale saluni wakabaki wanakodoa wasimini kama gari ile ilimfata Izani. Wakaisindikiza kwa macho wakati ikiondoka baada ya Izani kupanda.

“Naitwa Anita Ndimbo Masizi. Mimi ndiye Mfuasi wako tuliokuwa tunachati facebook. Nafurahi leo imekuwa siku ya kipekee nimefurahi kukuona Izani.” Anita akajitambulisha na kumgeukia Izani kabla hajamakinika na barabara huku akiendelea kuzungumza.

“Kuwa na amani kwa suprise zote utazokutana nazo leo…. Mimi ni Mfuasi wako Izani.” akatua na kumeza mate wakati huo gari ilikuwa barabara kuu kuelekea mitaa ya Mikocheni.

Na kweli siku hiyo Izani akakutana na shangazo nyingi asizotarajia. Safari yao ikatua mbele ya jumba la kifahari lililozungushiwa ukuta wa kibabe. Gari ilipofika getini geti lilifunguliwa na mlinzi wa kampuni maarufu jijini. Anita akaisogea gari eneo la maegesho kulipokuwa na magari mengine mazuri ya bei mbaya.

“...Leo utaenda kuzungumza na baba yangu pia ambaye amekubali kukuunga mkono kuwezesha kile ulichokianzisha kiwafikie wengi zaidi. Bila shaka ushawahi kumsikia mchungaji Ndimbo Masizi.” Anita akampasha Izani baada ya kuzima gari kabla hawajashuka kuelekea ndani ya mjengo. Izani hakuwa na la kupinga zaidi ya kuitika na kushusha pumzi za kuondoa kitete.

Kweli Alikuwa analijua jina la mchungaji Ndimbo Masizi na sifa zake aliwahi kuzisikia. Lakini yeye hakuwa mtu wa kanisa ingawa mara chache aliwahi kutazama mahubiri ya mchungaji huyo aliyemiliki kituo cha televisheni na redio.

Huo ndio ukawa mwanzo wa maisha mapya ya Izani baada ya kuzungumza kwa mapana na marefu na mchungaji Ndimbo aliyemuahidi kumwezesha kwenye vita aliyoianzisha.

Heshima ya Izani ikainuka baada ya kupewa kipindi cha televisheni katika luninga iliyomilikiwa na Mchungaji Ndimbo, pia akapangiwa nyumba nzuri ya kuishi mitaa ya Tabata Bima. Urafiki wake na Anita ukazidi kukomaa huku hisia za mapenzi zikifukuta ndani ya kila mmoja ingawa midomo yao ilikuwa mizito kutamkiana.

Na ndipo miezi michache mbele ikawa kumbukizi ya kuzaliwa kwa Anita. Na hiyo ikawa nafasi ya kipekee kwa Izani kumfanyia Anita jambo kubwa kwa kumchora kama alivyo.

Na kwa hakika picha ile ikawa ndiyo funguo iliyolegeza nta za papi ya midomo yao na kutamkiana hadithi ya mapenzi kwa mara ya kwanza.

Ilikuwa ni usiku wa siku ileile kwenye tafrija ya kumpongeza Anita kutimiza miaka 20 ya kuishi duniani toka azaliwe.

ITAENDELEA....
 
MFUASI
03

Nafsi ya Anita ikazidi kujililia baada ya kukumbuka hadithi yake na Izani ambaye muda mfupi uliopita ametoka kumuona akiwa na hali mbaya amewehuka hajitambui. Izani aliyejitoa kupigana vita vinavyompiga sasa. Vita ya uraibu wa mihadarati na madawa ya kulevya. Alipolikumbuka hili Anita aliumia zaidi na kumsikitikia Izani.

Ni yeye ndiye aliyemtokea kule Morogoro usiku huu na kumshuhudia akijidunga na kuthamini mkoba uliojaa sindano za madawa kuliko afya ya mwili wake. Hakika alimshudia Izani wa tofauti na yule aliyemfahamu akiwa hai.

Kwa kuwa Anita alikuwa nafsi bila mwili alikuwa na uwezo wa kusafiri kwa haraka kuliko mwanadamu mwenye mwili. Ndipo hapo alipokata shauri na kuona hakuwa na muda wa kupoteza tena pale kwao. Aligeuka kwa mara nyengine na kumsogelea baba yake aliyekuwa bado anaongoza maombi bila kuchoka. Ghadhabu zilimvaa tena Anita kila alipokuwa anamtazama baba yake.
Kwa uchungu akajisogeza karibu na sikio la Mchungaji Ndimbo Masizi na kusema kwa sauti ya kunong’ona huku uso ukifasiri hasira zake.

“Baba umeniua halafu unaniombea, Kweli? Hakika wewe ni Shetani mwenye Sura ya Malaika….! Ila nakuhakikishia nawe siku ya majuto yako inakuja.” Aliposema maneno hayo akapotea mazima mule ndani. Lakini cha ajabu safari hii mchungaji Ndimbo alihisi kitu cha tofauti na kujikuta anastuka na hata kunyamaza kuomba. Akafumbua macho yake na kuangaza kona zote kama anayemtafuta mtu. Jasho likamchemka na mapigo ya moyo yakaongeza mwendo wa mbio. Akaitazama familia yake wote wamefumba macho wametulia tuli wakimsikiliza.

Akageuza shingo kutazama saa kubwa iliyotundikwa ukutani na kugundua ilishatimua saa kumi alfajiri. Akiwa anageuza macho ndipo akaiona ile picha ya mchoro wa Anita pale ukutani. Mchungaji akauma meno na kujiinamia huku akifumba macho kwa uchungu akaamua kufunga maombi na kuwataka watoto wakalale.

“Papii inatosha baba. Wewe ndiye mkubwa nakutegemea sasa umsimamie mdogo wako. Doris mwanangu usiwaze kila kitu Mungu amekiweka sawa. Haya kalaleni sasa wanangu wapendwa dada yenu naye amelala kwa Mungu sehemu nzuri na salama kabisa msiwaze wala msilie tena.”

Akawafariji watoto kwa maneno ya upendo wakamtii na kuelekea ghorofa ya juu kwenye vyumba vyao.

“Mama Papii. Naomba ile picha uihamishe pale inawaongezea huzuni na simanzi watoto hata sisi wenyewe. Tafadhali fanya hivyo sasa mke wangu.”

Akatoa maelekezo kwa mkewe huku yeye akitangulia chumbani akiwa hoi kwa uchovu na huzuni kubwa baada ya kusimama kwa zaidi ya masaa sita wakiomba na kushukuru.

_______***_______
|MOROGORO VIJIJINI|

KOKORIIIIKOOOO!!

Majogoo yakapiga mbinja kuikaribisha alfajiri. Hali ya hewa sasa imetulia na safari ya hayawani inaendelea. Izani Nteze akiwa kama kichaa anajikongoja huku amekumbata begi lake mikononi.

Kumbukumbu zimemuhama hajikumbuki. Wapi anatoka wapi anaenda haijulikani. Vita alivyoapa kuvipiga sasa vinampiga. Si wa kuchovya si wa kulumagia! Mwendo wa kuchechema unamchosha zaidi mwili unakufa ganzi alipofika kijiji cha Kisanzala akajikuta hana jinsi zaidi ya kuchepuka na kujilaza kwenye shamba la miwa lililokuwa pembezoni mwa barabara. Hakuchukua hata dakika tano usingizi wa njaa na maumivu ya safari ukamteka. Muda huo huo Nafsi ya Anita ikatokea tena mahala pale na kubaki akimtazama kwa masikitiko asiwe na namna ya kumsaidia.

Oooh! Masikini Izani…! Nini kimekupata?

Kwa uchungu akabaki kujiuliza Anita na kujaribu kumgusa Izani lakini hakuweza. Kitu kimoja kilimpa tumaini ni pale alipokumbuka kuwa Izani alikuwa anamsikia mara ile alipomtokea kwa mara ya kwanza ingawa alihisi haonekani vyema mbele yake.

“Muumba wangu nipe kibali niupate mwili wa kunifanikisha kulipa kadhaa hii niliyofanyiwa ee Mungu. Usinifungulie Mlango huo wa mauti kabla sijauanika ukweli wa Izani na baba yangu kwa jamii ipate kufahamu. Nakuomba Mungu nihurumie mja wako nikubalie ombi langu.”

Anita akapiga goti kwa uchungu na kutazama juu akibaki anaelea asiweze hata kuikanyaga ardhi. Akiwa katikati ya masikitiko makubwa mara akaiona Nuru ikitokea angani na kuja mbele yake. Akamshuhudia kiumbe mkubwa anayeng’aa akiwa na mbawa sita akitua na kusogea mbele yake jirani kabisa na alipolala Izani.

“Salamu Anita! Amani iwe nawe. Hongera nimekuletea habari njema kutoka kwa Mola wako. Ombi lako limekubaliwa na umepewa kibali cha kuishi tena ndani ya mwili. Lakini kwa kuwa mwili wako umeshakufa! Hauna roho tena, hivyo huwezi kuurudia mwili huo kwa sasa. Mwili pekee unaoweza kuuingia kwa mwanadamu ni wa mtoto asiyehesabiwa dhambi ama mkubwa mwenye akili timamu ambaye ana roho safi. Budi sasa kuutafuta mwili wa namna hiyo ambao upo upande wa kaskazini ndiko pekee utaukuta mlango wake uko wazi. Pia umefunguliwa mlango wa kuingia kwa ndege na wanyama wote kasoro wenye mimba. Na kibali chako kitaisha baada ya siku zako arobaini ulizopewa kukamilika kabla ya kufunguliwa mlango wa ulimwengu utapoishi mpaka siku ya kufufuliwa miili yenu itapotimu..”

Baada ya kusema hayo yule kiumbe alifunua mbawa zake mbili na ndipo Nuru kubwa ikamuangazia Anita. Punde akamshuhudia kiumbe yule akifungua mbawa zote sita na kupaa kwa kasi ya ajabu akatoweka.

“Asante Mungu. Asante malaika mtakatifu.” Akafurahi Anita na kushukuru kwa sauti. Ndipo palepale akaanza kujishangaa kuona mwili wa Izani ukiwa na mlango katikati ya kifua. Akaushika kutaka kuufungua lakini mara sauti ikamkataza nyuma yake.

“Acha Anita! Malaika amekwambia uingie kwenye mwili wa mtu mwenye akili timamu mwenye roho safi. Na mtu huyo yupo Kaskazini utaukuta mlango wake uko wazi. Zingatia hilo Anita.”

Anita akageuka kuitazama sauti ilipotokea na kushangaa kumuona Izani amesimama akiwa na sura ile aliyozoea kumuona kipindi cha uhai wake duniani.

“Izani?” Akaita na kumtazama kwa makini. Akamsogelea kumgusa akafanikiwa.

“Haaa!…” Anita akastaajabu

“Izani? Ni wewe au ni….” Akageuka kumtazama Izani aliyelala pale chini na kugundua kiunganishi cha miale ya ajabu kutokea kichwani kwa Izani aliyelala kwenda kichwani kwa Izani aliyesimama.

“Ni yeye ni mimi Nafsi yake. Anajiona na kukuona kwa sasa lakini hatojikumbuka akiamka kwa kuwa hana akili timamu. Ila angekuwa na akili timamu angesema kwa roho iliyo hai ndani ya mwili kuwa amekuota na ungezungumza naye kwa vile angejiruhusu. Nenda Anita acha nishangae kidogo mji huu ulivyo.” Ikasema nafsi ya Izani na kunyanyuka juu ikielea huku ikifurahia mandhali.

Anita akaitazama nafsi ya Izani huku akitabasamu. Ndipo kwa juu akamuona ndege mkubwa akielea kwa furaha ya alfajiri. Alikuwa mwewe! Bila kuchelea Anita akaelea kumfata na kushuhudia mlango ukiwa wazi. Akatamani kuuingia ajaribu kuona inakuwaje anapokuwa ndege. Kufumba na kufumbua Anita akafanikiwa kuingia ndani ya ule mlango wa Mwewe na palepale akajishangaa kujiona amekuwa ndege mwenye mawazo ya binadamu. Akachapa mbawa na kuzunguka anga mara tatu na kujikuta akitabasamu.
“Uuuuuww! Asante Munguuu!” Akapiga ukonga wa furaha wakati nafsi ya Izani ikimshuhudia na kutabasamu.

“Usiende mbali rudi mwilini mwako na usiache mlango wazi. Kumbuka mimi ni mfuasi wako naenda kutafuta mwili wa mtu mwenye roho safi nitakuja kukusaidia Izani.” Akasema Anita akiwa ndani ya Mwewe na Nafsi ya Izani ikatii kurudi mwilini. Safari ikaanza, Mwewe aliyebeba nafsi ya Anita akachanua mbawa angani kuelekea upande wa kaskazini kumtafuta huyo mtu mwenye roho safi.

Kipindi safari ikiendelea angani mawazo ya Anita yakamrudisha kwenye maisha yake na Izani kabla hawajatengana. Aliikumbuka siku ile iliyofunua sura mpya baada ya kutamkiana kilichojificha kwenye mioyo yao. Siku ile ya sherehe ya kuzaliwa kwake akitimiza miaka 20 mwaka 2018 ndani ya ukumbi wa Ramada Resort.

______***______

Ilikuwa ni tafrija ya gharama iliyohudhuriwa na watu wachache walioalikwa ndani ya ukumbi wa Ramada Resort jijini Dar Es Salaam.
Anita Ndimbo akiwa amevaa gauni jekundu lililompendeza mno akinakshiwa na mtindo wa nywele aliopambwa siku hiyo hakika alivutia macho ya kila aliyemtazama. Tabasamu halikumkauka machoni kila alipomtazama Izani, wazazi wake, wadogo zake na marafiki wa karibu walioalikwa kujumuika pamoja kufurahia siku hii.

Baada ya kukata Keki na kuwalisha wahudhuliaji ndipo mshereheshaji alipotangaza muda wa zawadi kabla hawajajumuika kwa chakula kilichoandaliwa kwaajili ya wote waliohudhuria.
Huu ndio ulikuwa muda uliosubiriwa kwa hamu na Anita. Licha ya wazazi wake kumfanyia shangazo kwa kumnunulia gari mpya ya kifahari lakini haikumshtua sana kama picha yake aliyochorwa na Izani. Hata mama na baba mchungaji Ndimbo Masizi walistaajabia kipaji cha Izani kupitia mchoro ule muruwa.

Mshereheshaji akamtaka Izani aseme chochote kuhusu zawadi yake kwa Anita na kumkabidhi kipaza sauti. Ukumbi wote ulinyamaza kimya huku kila mmoja akiwa ametabasamu aliyatuliza macho na masikio kwa Izani.

“Mtanisamehe wapendwa kwa kuwa moyo una mengi ya kusema lakini mdomo unakosa sentesi sahihi ya kufupisha. Huenda kutokana na furaha niliyo nayo kutimiza ahadi yangu ama shauku ya kuongea imenikaba. Ila ninachoweza kumwambia Anita kuhusu zawadi hii ya picha ambayo nimemchora, ajue ni maalum. Nimefanya hivi ibaki kuwa kama alama ya shukrani kwake na ishara ya upendo wangu kwa mfuasi aliyenionesha thamani bila kutazama mipaka ya uwiano wa kitabaka uliokuwa baina yetu. Nakushukuru sana Anita nakuombea Mungu akulinde na kukutimizia kila hitaji la moyo wako. Asante.”

Ukumbi ulisisimka kwa makofi ya wahudhuriaji baada ya kumsikia Izani akizungumza maneno machache yaliyojaa hekima na busara. Chozi la furaha lilimdondoka Anita na kujikuta anamkumbatia kwa nguvu Izani baada ya kupokea picha yake.

“Nakupenda sana Izani. Hakika nakupenda mno. Asante kwa upendo huu.” Kwa hisia kali Anita akatamka maneno haya ambayo yalipenya ndani ya moyo wa Izani na kumchanulia ujasiri wa kutamka neno lililomkaba tokea siku ya kwanza kumuona binti yule.
“Nakupenda pia Anita. Tena natamani uwe wangu wa maisha.” Kauli hii ya Izani ikamuongezea tabasamu zaidi Anita Ndimbo na kuzidi kumkumbatia kwa furaha.

“Nami pia natamani iwe hivyo.” Anita akajibu na kushangaza hisia za Izani na kujikuta wakiachiana na kutazamana kwa sekunde kadhaa. Kila mtu mzima aliyekuwa ukumbini pale aliweza kuyasoma macho ya Anita na Izani kwa vile walivyotazamana. Mshereheshaji akajikohoza na kuchomekea maneno ya kufurahisha yaliyowavunja mbavu ukumbi mzima na kuzidisha tabasamu kwa kila aliyehudhuria.

ITAENDELEA..........
 
MFUASI
05

|MOROGORO VIJIJINI|

“BABAAA! BABAAA!” Mtoto akaita kwa sauti akiwa haamini anachokiona. Baba yake aliyekuwa upande wa pili anakimbilia upande aliokuwepo mwanae haraka.

“Wee Koba nini tena kunistua?” Akauliza kwa taharuki baba wa mtoto huku akilikamatia vyema panga lake mkononi. Koba akaonesha kwa kidole kumuelekeza baba yake alichokiona. Mzee akageuza macho kutazama naye akastaajabu.

MTU!

Akashangaa na kuanza kumchunguza kwa makini na tahadhari. Hakujua mwanaume aliyekuwa amelala pale chini ni mzima au amekufa.

“kimbia nenda nyumbani kamwite mjomba Banzi haraka uje nae.” Akampa maagizo mwanae huku yeye akijaribu kumgusa gusa kwa ubapa wa panga yule mtu kuona kama ataamka.

Kimya! Hajitingishi hatingishiki. Halufu ya mikojo inapwiyuka alipomuinamia na kumfanya anyanyuke na kutema mate.

“Huyu kichaa kaacha kufia kote anakuja kuangukia shambani kwangu?”

Akajikuta akiongea peke yake baada ya kuhisi mtu yule aliyelala kwenye shamba lake la miwa si mtu mwenye akili timamu.
Muonekano tu ulitosha kumuaminisha hivyo.

Dakika chache mbele mara yule mtoto akafika akiwa bwana mmoja mnene mfupi akiwa ameshika Mundu mkononi.

“Baba Koba kunaki?” Akauliza yule bwana kibonge akiwa anahema baada ya kufika pale shambani. Lakini kabla hajajibiwa alipotazama chini akastaajabu.

“KHA! Mwiyangu si munu huyu?”

“Sasa Banzi chouza choni? Tena anaonekana Mditwi bure huyu!” Akajibu baba Koba akimwambie mwenzie kile anachohisi kuwa yule mtu ni chizi.

“Koba! Genda kamwita mjumbe haraka Kimbiaa!” Bwana kibonge akamtuma tena yule mtoto aliyetoka mbio kuelekea kwa mjumbe. Wakabaki wanajadiliana kwa kilugha baada ya kugundua mtu yule alikuwa mzima ila hali yake ilionesha anaweza kufa muda wowote. Kalala fofofo hajitambui mwili unanuka vidonda vimemtapakaa na majeraha ya ajabu.

Ndipo yule kibonge alipomgusa na Mundu yake yule bwana na ghafla akageuka kama aliyekurupushwa. Cha kwanza akawahi kuukumbatia mkoba wake uliokuwa pembeni. Wale wakulima wakashtuka na kumkemea.

“Tuliaa! Weee nani? Tutakuchinja mwizi wee! tulia” Wakamtisha na kushangaa mtu yule hatishiki zaidi ya kuwashangaa. Alitazama pembeni kushoto kulia na kujikuta akivunja muwa bila kusema kitu akaanza kuutafuna kwa fujo na kuwafanya wale wakulima kutazamana kwa taharuki wasijue wamfanye nini.

“Si nilikwambia huyu mwehu!” Baba Koba akasema na wakati huo mjumbe akafika akiwa na yule mtoto na vijana wengine wawili.
Wote wakashangaa walichokikuta na hakukuwa na mjadala zaidi wakajua yule mtu alikuwa ni kichaa lakini ni mgeni hawakujua alipotokea. Lakini kilichowatisha zaidi ni vile alivyoonekana ana majeraha kama ya kupigwa na kukatwa na vitu vya ncha kali.

“Huyu atakuwa kichaa lakini pia mwizi. Vijana mkamateni mumfunge kamba kwanza tufanye utaratibu wa kumpeleka serekali ya kijiji kutakuwa na maamuzi sahihi.” Mjumbe alizungumza kuwaambia vijana aliokuja nao wakati huo yule kichaa akiendelea kufakamia muwa bila kujali watu waliomzunguka na kumuongelesha. Mkoba wake aliubana kwenye miguu sawia. Na ndipo wale vijana walipomvizia na kumkamata. Akajitahidi kufurukuta lakini hakuwa na ubavu zidi ya kupiga kelele.

“Niacheniiii! Heeee! Sitakiiii…! Nyieee” Kwa sauti iliyokosa nguvu akajitahidi kupiga kelele lakini hakufua dafu. Vijana waliokuja na mjumbe wakamtuliza na kumfunga kamba mikono na miguu. Wakambeba msobe-msobe kumpeleka ofisi ya serikali ya kijiji huku mjumbe akiwa ameubeba ule mkoba waliomkuta nao na kipande cha muwa aliouvunja shambani.

Msafara wa wale wakulima na yule mtoto ukaongoza barabara na kila walipopita wanakijiji hawakuacha kushangaa na kuuliza kulikoni!

Ilikuwa yapata saa tatu asubuhi, mwehu yule ambaye alikuwa ni Izani Nteze akafikishwa serikali ya kijiji akiwa kabebwa msobemsobe akipiga kelele na kuzungumza maneno yasiyoeleweka.

* *

Wakati Izani Nteze akikutwa na masahibu yale kule shambani, upande mwengine safari ya Mwewe aliyebeba nafsi ya Anita Ndimbo bado inaendelea. Ingawa kweli alikuwa anaruka kwa kasi lakini haikuzidi kasi anapokuwa kama nafsi bila mwili. Alichofurahi akiwa ndani ya mwili ni kuweza kuugusa ulimwengu ambao kwa wiki moja alikata mawasiliano nao. Ndege wenzake aliokuwa anakutana nao yule Mwewe walimshangaa na wengine wakajaribu kumsemesha lakini Anita hakuwaelewa kwakuwa hakuwa na asili ya ndege moja kwa moja ingawa alimsikia yule Mwewe akiwajibu.
Hali hii ikaanza kumchosha na kujikumbuka siku ile alipokuwa anatoweka kwenye ulimwengu aliouzoea akiwa na mwili wake alioupenda na kuuthamini.

Anko Chika na Baba hakika mtayalipia maisha yangu mashetani nyie!

Akasema ndani yake akiwa haamini ingawa alishakubaliana na ukweli kama yeye si yule wa mwanzo tena na hajui hiyo siku ya ufufuo kuurejea mwili wake wa asili itakuwa lini. Kutumia mwili wa ndege asiyemjua atokapo ilimuumiza. Muda mwengine alijikuta akishindana maamuzi na nafsi ya yule ndege alipohisi kuchoshwa na safari asiyoielewa. Mwishowe akaamua kutoka na kuelea kama nafsi huru huku kumbukizi zikimrudisha wiki moja nyuma siku ile ya mwisho kabla na baada ya kutolewa kwa nguvu ndani ya mwili aliouzoea.

***
|WIKI MOJA NYUMA|

“Leo ndio siku yako ya mwisho Anita tumekuja kuchukua damu yote ya mwili wako tukaifanye kazi ya baba yako. Na hiki ni kibali cha kazi na tazama makubaliano yetu yalivyokuwa.”

Sauti mbaya ya kutisha ikasikika toka kwa Jitu kubwa la ajabu likiwa limesimama mbele yake. Anita akaogopa na kupiga kelele lakini sauti haikumtoka wala mdomo kufunguka. Jitu lile lenye jicho moja na pembe kama kifaru likanyoosha kono lake na kumuelekezea kiganja Anita atazame. Hapo ndipo Anita akaanza kushuhudia video kupitia kiganja kile kikubwa cha lile jitu na kumshuhudia baba yake akifanya makubaliano na mtu mmoja mwenye ndevu nyingi, juu ya kifo chake.

“Ni mtoto wako wa kwanza ndiye tunahitaji damu yake ikasafishe nuksi iliyoanza kuvamia nyota yako ili upako wetu ukafanye kazi juu yako na asitokee yeyote wa kukutilia mashaka. Usipofanya hivyo tarajia anguko kubwa na kifo cha kudharirika sana maana upepo wako umeanza kuingiwa vumbi la mauti huduma yako itazama na siri zako zitamwagika.” Akasikika yule bwana mwenye ndevu.

“Siko tayari yatokee yote hayo. Niko tayari kumtoa Anita ila mnihakikishie mnawaacha salama watoto wangu wawili niliosalia nao.” Macho yakamtoka Anita asiamini kama kweli baba yake ndiye alikuwa anaongea maneno yale akikubali yeye afe na damu yake ikatumike kumsafisha nuksi zake.

Akamshuhudia yule bwana mwenye ndevu akiangua kicheko cha ajabu na kumpongeza baba yake aliyepiga magoti mbele yake. Hapohapo lile jitu likafunga kiganja chake na kuzidi kumuongelesha Anita ambaye muda huo alikuwa anajishangaa hawezi kusema chochote kila alipojaribu kunyanyua kinywa.

“Sisi ni watendaji tu Anita! Baba yako ndiye ametoa kibali na sasa jiandae nimekuja kuchukua damu ya mwili wako nawe hutoweza kuishi tena ndani ya mwili huu. Hivyo namaanisha sasa unaenda kufa! Haahahahahaaaa!”

Likasema lile jitu na kuanza kuachama mdomo wake mkubwa na hapo akashahudia ulimi wa lile jitu wenye ncha nyembamba ukirefuka kama mrija wa ajabu na kuanza kumuelekea mwilini hususani upande ule wa miguuni.

Anita akaogopa sana na kupiga kelele za msaada huku akilalamika aachiwe lakini haikuzaa matunda. Ingawa safari hii alijisikia sauti ikitoka lakini akashangaa kuona watu wengine waliokuwa chumbani alipolala wakiamuriwa na baba yake watoke.

Akashangaa kwanini lile jitu lenye ulimi mrefu hawalioni. Akaumia zaidi miguuni kushikwa na dereva wa baba yake aliyemfahamu vyema na kumuheshimo kama Anko wake. Lile jitu likapeleka ulimi wake mpaka sehemu zake nyeti na hapo ulimi ukanata kama sumaku juu ya kufuli lake. Anita akajitahidi kufurukuta lakini hakufua dafu. Kushoto akamshuhudia baba yake akizungumza maneno yasiyoeleweka huku ameshika biblia.

Maumivu makali akaanza kuyahisi kupitia chini ya maumbile yake uliponatia ule ulimi na hapo akaanza kushuhudia ulimi wa jitu ukizidi kuwa mwekundu naye maumivu yakizidi kuongezeka. Nguvu zikazidi kumuisha na sauti ya kumkauka huku wingu la giza nene likitanda machoni mwake.

Akiwa haamini kinachomkuta fahamu zake zikaanza kufunga polepole akaanza kujiona akipotea kwenye ulimwengu wake.
Mwanga wa ajabu ukamulika mbele yake, akamshuhudia kiumbe mwenye nuru inayong’aa na mbawa zinazomeremeta akiwa anamnyooshea mkono pembeni ya kitanda. Hakuliona lile jitu muda huo wala hakuhisi maumivu yoyote.

Malaika!

Akajisemea na akitabasamu, akajikuta ananyoosha mkono na kushikana na yule kiumbe mwenye mbawa zinazong’aa. Hapo ndipo alishangaa kujiona mwepesi akinyanyuka pale kitandani huku akishangaa zaidi kujiona amelala. Pembeni yake akamuona baba yake akitoa nguo ya ndani na kumkabidhi mtu aliyezoea kumwita ANKO CHIKA.

“Sasa timiza wajibu wako. Mvue aliyovaa mvishe hii haraka na ufunge mdomo wako.” Akamsikia baba yake akisema na kumshangaza zaidi! Akastaajabu kuona Anko Chika akimvua nguo pale alipolala huku akijishangaa yeye amevaa nguo nyeupe na alipojitazama mwili wake unang’aa tofauti na yule aliyelala pale. Akataka kumzuia Anko Chika asimdhalilishe lakini akajikuta mkono ukipitiliza bila kumgusa.

“Anita wewe si Mwanadamu mwenye mwili tena! Wewe ni nafsi tu kwasasa nami nimekuja kukupokea na kukupa maelekezo ya awali kabla hujafunguliwa mlango wa makazi yako ya milele. Kwasasa unahesabika ni mfu lakini mwili wako umedhurumiwa na roho yako ishapokelewa Mbinguni.”

Akazungungumza kwa mara ya kwanza yule kiumbe mwenye mbawa ambaye alikuwa ni Malaika mpokezi wa nafsi iliyotenganishwa na mwili.

“WHAAAT! INA MAANA NIMEKUFA?” Anita akauliza kwa taharuki asiamini anachokisikia na anachokiona. Akamsogelea baba yake lakini alijikuta anapitiliza. Kila alichotaka kukishika hakikushikika naye. Hata alipojisogelea pale kitandani akajikuta anajililia asiamini kama kweli kafa na hatoweza kunyanyuka tena akiwa na mwili wake alioupenda.

“Anita Ndimbo! Baba yako amekubali kutumia damu yako kwa maslahi yake ya dunia. Lakini Mungu wako ni mwingi wa rehema na amekurehemu. Kila kiumbe atalipwa kwa alichokichuma. Usihuzunike kwasasa huna cha kubadili hali iliyotokea. Unachotakiwa kujua utakuwa na siku arobaini tu za kuuona ulimwengu uliotoka kabla hujafunguliwa mlango wa ulimwengu wa nafsi zilizoonja mauti.”

Baada ya kusema hayo yule Malaika akapotea na kuiacha nafsi ya Anita kwenye huzuni kubwa asiamini anachokiona na kusikia.

Aliweza kutoka kila hatua na kushangazwa na kauli za baba yake kwa kile alichokuwa anakifanya bila familia kujua.

“Mungu ni Mwema mke wangu. Anita ametulia kwa sasa muacheni apumzike walau kwa saa tatu hali ikiwa bado itabidi tumuhamishie kanisani kwa maombi ya jumuiya.” Akamsikia baba yake akimuongopea mama yake pindi alipomuuliza Chikala kuhusu hali yake. Aliumia na kujitahidi kuzungumza lakini hakuna aliyesikia.

“Babaaa weee ni shetaniii! Shetaniii! Mamaa nimekufa mimiii! Baba ameniuaaaa” Kelele zake na kilio cha kwikwi hakikuzaa matunda.

Alizunguka zunguka nyumba nzima kujaribu kuzungumza na yeyote wa kumsikia hakumuona. Mpaka yanapita masaa matatu mama yake akaingia chumbani ulipolala mwili wake kumtazama. Na hapo ndipo taharuki mpya ikazaliwa. Yule mama akastuka baada ya kumgusa pale kitandani na kuhisi hali isiyo ya kawaida.

“Wee Anita! Anita mwanangu! UUUWIIIIH MUME WANGUUU!” Mama yake akapiga ukonga huku akigusa mapigo ya moyo ya Anita na kujikuta wasiwasi ukimvaa macho yakamtoka. Mchungaji Ndimbo akakimbilia ndani akiwa ametaharuki pamoja na watoto wake wengine waliokuwa sebuleni.

“VIPI?” Akauliza kwa taharuki macho yamemtoka asiamini kuona mkewe akilia huku anamtingisha Anita pale kitandani. Nafsi ya Anita ikaghadhibika na kumrukia baba yake kishari lakini ikapitiliza asimguse.

“Hebu nyie tokeni kwanza!” Akawafukuza watoto wake na kujisogeza kwenye kitanda alicholala Anita akijifanya haelewi mabadiliko ya hali ya Anita. Akamgusa mwili umeshapoa chozi la kinafki likamdondoka Mchungaji Ndimbo Masizi.

Wakati huo mkewe akajikuta ananyong’onyea nguvu zikimwisha asiamini anachokiona.

“Usilie mke wangu! Dokta anakuja nishaongea nae lakini bado Bwana wa majeshi ana nguvu..! Haa Naamuru nguvu ya uzima inyanyuke kwa binti yetu…! Anitaaa…” Akaanza kuangusha maombi lakini akajikuta anashindwa kuendelea na kuanza kumwita binti yake akimtingisha bila mafanikio. Wakati huo huo daktari wa familia akafika kama ilivyopangwa na kushangaa kukuta nyumba imetawaliwa vilio. Watoto walianza kulia baada ya kumsikia mama yao na kuhisi dada yao hayuko salama. Daktari akaingia chumba alichokuwa mgonjwa na kuwataka wampishe kwanza afanye uthibitisho wa kitaalam zaidi. Na ndipo alipohakiki na kumwita faragha mchungaji Ndimbo Masizi.

“Mzee nasikitika kusema huyu binti amelala usingizi wa mauti. Hayuko hai tena.” Alitamka Daktari wakati nafsi ya Anita ikiwa pembeni inasikia na kushuhudia baba yake akiangua kilio baada ya kupewa uhakika wa kifo chake.

Jambo hili lilizidi kumuuma Anita kupitia msiba wake akafanikiwa kuujua moyo wa baba yake. Baba ambaye miaka yote kuishi kwake aliamini ni mwema kwake na kwa jamii nzima. Alijua Mungu anamtumia katika huduma za kiroho lakini kumbe sivyo. Msiba wake ukatangazwa na taratibu za mazishi zikaanza. Kila aliyesikia hakuamini. Aliumia kuona marafiki walivyokuwa wanamlilia.

Wadogo zake na ndugu waliohudhuria kutoka ndani na nje ya nchi.
Jambo lililomuumiza zaidi kumuona yule mtu mwenye ndevu siku ya mazishi yake ambaye baba yake alimtambulisha kwa mama yake kuwa ni Mtumishi kutoka Kenya. Aliumia kuona anapokelewa kama mgeni wa heshima wa familia na ndiye aliyetoa mchango wa hela nyingi kwenye kitabu cha rambirambi kuliko mtu yeyote.

Mpaka anaenda kuzikwa Anita alisimama pembeni akijishuhudia mwili wake ukiingizwa kaburini. Baada ya mazishi kukatangazwa siku tatu za mkesha kanisani wa kumuombea kwa Mungu. Anita alijililia sana lakini hakuwa na namna yha kubadili hali.

Malaika wawili wakamtokea tena siku hii na kumfariji kwa kumpa maneno ya matumaini ya kuzoea hali mpya aliyokuwa nayo huku akikumbushwa baada ya siku arobaini hatokuwa na uwezo wa kuyaona tena maisha ya dunia aliyotoka bali atafunguliwa mlango wa ulimwengu wa nafsi zilizoonja mauti. Huko ndipo ataishi kwa daraja ya maisha aliyoyaishi duniani kama yalimpendeza Mungu ataishi vyema kama sivyo ataishi kwa taabu na mateso mpaka siku ya ufufuo ambayo haikujulikana itakuwa lini.

ITAENDELEA.........
 
MFUASI
06

| DAR ES SALAAM |
Mpaka kunakucha usingizi haukumshika mchungaji Ndimbo Masizi. Ilipotimu saa tatu asubuhi mkewe akaamka na kushangaa kumkuta mumewe akiwa ameketi kitandani akisoma kitabu cha biblia lakini usoni huzuni iliuzonga uso wake.
“Tumsifu Yesu Kristo Mume wangu.” Mkewe akamsalimu huku akimhurumia mume wake ingawa hata naye alikuwa na machungu ya kumpoteza binti yake.

“Milele Amina! Pole na uchovu.” Mchungaji Ndimbo akajibu huku akiiweka biblia pembeni na kumbusu shavuni mkewe. Faraja ikamuinuka yule mama na kumtazama mumewe kwa upendo.

“Mama Papii! Leo nina safari ya Nairobi mchana. Hivyo naomba niandalie nguo utazopenda nivae na mbili za ziada uniwekee kwenye begi.” Aliposema hivyo akamshtua mkewe na kumfanya aketi kitako pale kitandani.

“Jamani mume wangu! Kwanini usipumzike kwanza. Wiki nzima tunakesha wima na tupo kwenye wakati mgumu ni heri tunavyokuona tunapata nguvu. Tafadhali baba Anita siku moja sasa naiona ndefu sana mume wangu kuniacha na watoto.” Mama Anita akasema kwa unyonge huku machozi yakimlenga. Alichokifanya mchungaji Ndimbo ni kumkumbatia na kumsisitiza umuhimu wa yeye kufika Nairobi pia akimtoa hofu ya upweke.

“Bwana wa majeshi yupo na Malaika zake wametanda kila kona. Funga mkanda mke wangu hatuwezi kuibadili hali zaidi ya kuipokea na kuyaacha maisha mengine yaendelee.” Akamsisitiza na mkewe akakubali kishingo upande.

Ndimbo Mchungaji alipochukua rununu yake na kuingia sehemu ya kuhifadhi majina na alipolifika jina la mtu aliyemkusudia akaipiga namba yake na kuipeleka simu sikioni ambapo haikuchelewa kupokewa baada ya kuita mara mbili.

“Hallow!… Milele Amina. Sasa hebu niandalie tiketi mbili za Nairobi. Yaah Mchana….! Ok Asante….. Kazi njema.”

Alipomaliza kuongea na mtu aliyempigia akamgeukia mkewe ambaye muda wote alikuwa anamtazama kwa huzuni na upendo.
“Safari itakuwa saa nane na nusu.” Akamwambia.

“Utaenda na Chikala?” Mkewe akamuuliza naye akamuitika kwa kichwa kumkubalia huku akisimama na kuuelekea mlango wa chooni.

Upande wa jikoni dada wa kazi alikuwa anaendelea na mapishi baada ya kumaliza maandalizi ya chai meza kuu ya chakula ingawa mpaka muda huo wenyeji wake wote hawakuamka.

Papii anaonekana chumbani kwake akicheza tv game huku Doris akiwa amejiinamia chumbani kwake akisoma kitabu cha biblia.
Ilipotimu saa nne ndipo mchungaji na mkewe wakatoka chumbani na kuungana mezani kwa chakula cha asubuhi.

“Angelina! Kawaamshe kina Dori mwanangu.” Mama mchungaji akaipaza sauti kumuagiza dada wa kazi baada ya kufika meza ya chakula na kuhisi watoto wake hawajaamka kunywa chai. Mfanyakazi akatii na kutimiza agizo. Aliposhuka akaenda kuwasalimia mabosi zake na kurudi jikoni kuendelea na kazi. Muda mfupi baadae Papii na Doris wakajiunga na wazazi wao mezani.

“Wanangu! Nawaomba kuanzia leo muanze kuchangamka na kuacha kuwaza sawa! Tunawapenda na Mungu anawapenda sana. Leo nitasafiri kwenda Nairobi lakini naomba mkae tayari nitaporudi tutaenda sote Dubai.”

Mchungaji Ndimbo akazungumza huku akiwatazama kwa zamu watoto wake. Nafsi yake ilimsuta macho yake yakamng’ong’a kila alipoiona huzuni aliyoitengeneza mwenyewe kwa familia yake.
Maji ukiyavulia nguo sharti uyaoge.

Akili ikamwambia na ujasiri ukamuinuka ndani yake.

Kama yapitavyo mawimbi baharini na hili nalo litapita.

Akajisemea moyoni ingawa kila alivyoitazama familia yake moyo ulimuuma lakini hakuwa na namna zaidi ya kuwafariji na kuhakikisha sasa wanamsahau Anita na wanatazama maisha mengine.

Mkewe naye hakuwa nyuma kuwaliwaza watoto kwa maneno ya faraja na mifano ya maisha ya watakatifu kupitia biblia. Ingawa naye alikuwa na huzuni kuu lakini alijitahidi kuhakikisha furaha inarejea upya kwa watoto wao ambao tangia dada yao afariki hawakuwa na hamu ya kula wala kucheza. Huzuni iliyokuwa kwa watoto haikujificha hasa kwa Doris ambaye licha ya umri wake mdogo lakini yeye alikuwa na pigo kubwa moyoni mwake kwa kuwa alimzoea sana dada yake na ndiye alikuwa rafiki yake mkubwa.

Baada ya kumaliza kufungua kinywa Mchungaji Ndimbo akawa wa kwanza kunyanyuka na kuelekea chumbani kwake. Alifika na kujiinamia kitandani kwa dakika chache kisha akavuta pumzi ndefu na kuzitoa polepole akajiweka sawa. Akatazama muda kwa saa ya ukutani iliyokuwa chumbani na kugundua tayari imetimu saa nne asubuhi. Akachukua simu yake kumpigia Chikala Gumbo, kijana wake wa kazi aliyetumaini kusafiri naye.

* *

Simu ya Chikala ikaita wakati akiegesha gari mbele ya mgahawa mmoja uliokuwa maeneo ya Kinondoni. Akaitazama namba ya anayepiga na kuipokea.

“Ndiyo Boss!” Akaitika baada ya kuipokea, sauti ya Mchungaji Ndimbo Masizi ikasikika upande wa pili.

“Safari saa nane na nusu! Saa saba nipitie Kanisani usisahau na ile…..” Anasita kumalizia upande wa pili.

“Naelewa Boss…! Lakini….!”

“Lakini nini tena Chikala?”

“Samahani bosi najikuta hali yangu inabadilika kadili muda unavyosogea sijisikii vizuri nahisi nina homa kali sidhani kama nitaweza kusafiri.” Chikala akadanganya na kumshtua vibaya Mchungaji Ndimbo upande wa pili. Simu ikakatwa bila bosi wake kuongeza neno. Chika akashusha pumzi na kushuka garini kuelekea ndani ya ule mgahawa.

Ulikuwa ni mgahawa wa kisasa ambao aliumiliki mwenyewe ingawa ulisimamiwa na binti aliyeitwa Kisa Kabeby ambaye alikuwa mpishi mkuu.

Alipofika akakaa upande wa ndani v.i.p na kumtumia ujumbe Kisa kumtaarifu ameshafika. Dakika chache mbele akafikishiwa supu ya kuku na ndizi za kuchemsha mezani.

“Karibu Bosi!” Muhudumu akamkarimu huku akijitolea kumnawisha ingawa ilikuwepo sehemu ya kunawa wateja pembeni ya mlango wa kuingilia.

Alipomaliza kunawa na kuanza kupata kifungua kinywa mara akafika Kisa Kabeby. Msichana mwenye umbo tashtiti lililonogeshwa na makalio makubwa yanayostusha macho ya wanaume wakwale.

“Boss Chika! Mambo..!” Kisa akamsalimu huku akiwa mwingi wa tabasamu, akavuta kiti na kukaa mbele yake.

“Nambie Kisa kishundu, mabwana zako hawajambo?” Chika akajibu kwa sauti cheshi na kumtazama Kisa aliyeishia kubenua midomo na kurembua macho.

“Bwana Bosi Chika mi sipendi utani huo mwenzio!” Kwa sauti ya puani akajibu huku akimtazama Chikala anavyokula.

Chikala Gumbo na Kisa Kabeby ni watu waliozoena kwa muda mrefu. Mbali ya kuwa mtu na bosi wake lakini waliwahi kuwa wapenzi miaka ya nyuma kipindi wakiwa shule. Kipindi hiko Chikala akiwa kidato cha nne na Kisa kidato cha kwanza. Wakapoteana na walipokuja kukutana tena ukubwani ilikuwa miaka mitano imepita tangia Chika aanze kufanya kazi kwa mchungaji Ndimbo Masizi, huku Kisa akiwa anafanya kazi hotelini.

Na huo ukawa mwanzo wa mazoea mapya mpaka pale Chika alipoamua kufungua mgahawa huo wa kisasa na kumkabidhi Kisa ausimamie huku yeye akiwa anaendelea na mambo yake kwa mchungaji Ndimbo ambayo Kisa hakuwa anayajua zaidi ya kujua Chikala alikuwa dereva tu wa mchungaji.

“Vipi mwezi huu mahesabu yapoje?” Akauliza Chika baada ya kumaliza kunywa supu, muhudumu akafika kuondoa vyombo na kumnawisha.

“Haya hapa na nishapeleka benki.” Kisa anajibu huku akifungua mkoba mdogo aliokuwa ameupakatia na kumkabidhi Chikala karatasi zilizokuwa na maelezo ya mapato na matumizi ya mwezi mzima.

“Vyema! Nafikiria tufungue matawi mengine wilaya ya temeke na Kigamboni au unaonaje zilipendwa wangu.”

“Wazo zuri lakini sipendi unavyonita zilipendwa ujue. Mbona unakuwa hivyo Chika au ndio ushakuwa bosi unaniona takataka miaka hii. Umesahau shule eeh!” Kisa akaongea huku akijinunisha kwa kudeka na kumfanya Chikala acheke na kunyanyuka huku akiikunja ile karatasi aliyopewa na kuitia mfukoni.

“Any way tuache masihara Kisa! Kuwa makini na biashara nakuhakikishia tukifungua matawi mengine mawili moja litakuwa lako kwa asilimia mia.” Akasema kwa sauti ya kumaanisha huku akivaa miwani yake usoni. Kisa akatabasamu na furaha kumlipuka moyoni mwake. Wakaagana, Chikala akatoka kuielekea gari yake huku Kisa akiishia kumtazama bila kuongeza neno ingawa moyoni alikuwa ana mengi ya kumwambia mwanaume yule ambaye hakuwahi kufikiria kama siku moja atakuwa na maisha mazuri jijini hata kuwa mfanyakazi wake mbali ya kumzidi elimu ya darasani.

Alipoingia garini akampigia simu bosi wake kabla hajaondoa gari. Simu ikaita lakini haikupokewa. Akawasha gari kuondoka mara ukaingia ujumbe wa maneno kwenye simu yake. Akaichukua kuusoma ulikuwa unatoka kwa bosi wake.

Nifikishie huo mzigo wa msingi kanisani muda huu na uendelee na kujiuguza kwako.

Ujumbe ukasomeka na akahisi bosi wake hajaridhika kusafiri peke yake. Akamjibu kwa kumuitika kisha akaielekeza gari kuitafuta Upanga kulipokuwa na Kanisa la mchungaji Ndimbo Masizi.

______***_______
| MOROGORO VIJIJINI |

Baraza la kijiji lilikusanyika muda mfupi baada ya mtu waliyeamini ni kichaa kufikishwa. Kundi la wanakijiji lilikusanyika nje ya ofisi ya kijiji. Baada ya kuteta na mjumbe mwenyekiti akasimama kuzungumza.

“Jamani wanakijiji wenzangu kama mnavyoona hali ya huyu bwana mditwi habule! Na kijiji chetu hakina hata kituo cha polisi pia serikali yetu haina hukumu kwa mtu kichaa ingawa inajali usalama wa raia zake. Mtu huyu anaonesha ni chizi lakini pia tuna wasiwasi anaweza kuwa mkorofi au mwizi. Kwenye mkoba wako tumekuta sindano na tuna mashaka inaweza kuwa mtu huyu ni mtumiaji madawa ya kulevya. Basi napendekeza kuwatuma vijana wetu shupavu wambebe kumfikisha kituo cha polisi MTAMBA huko watajua cha kumfanya. Au mnaonaje wenzangu?”

Mjumbe na wanakijiji wakaunga mkono wazo la mwenyekiti. Vijana wanne ambao ni mgambo wa kijiji wakachaguliwa kufanya hivyo. Izani akabebwa tena msobemsobe na kuanza kupelekwa kijiji cha Mtamba kilichokuwa nje ya kijiji cha Kisanzala. Walitembea kuifata barabara ambayo Izani alikuwa ametokea jana yake. Njiani.

Msafara wao ulikuwa sambamba na yule bwana aliyemkuta shambani na mwenyekiti wa kijiji pia na mjumbe akawa miongoni mwao.

Wakiwa njiani mara wanakutana na gari ndogo Suzuki Vitara nyeusi inayosimama ghafla baada ya dereva kuuona msafara wao.

“Hey! Samahani kidogo mzee wangu!” Dereva akaita huku akishusha kioo baada ya kukutanisha macho na mjumbe.

“Mimi?” Mjumbe akauliza huku akijielekezea kidole kifuani.

“Ndio mzee wangu samahani lakini.” Kijana aliyekuwa mbele ya usukani akasema kwa heshima. Mzee akasogea wakati wenzake wakiendelea na safari ya kumpeleka Izani mtamba.

“Naona msobemsobe mmembeba mtu juu amefungwa vipi ni kwema huku?” Akauliza yule bwana.

“Aaah! Yule chizi amevamia shambani huko tunampeleka polisi ila kwema tu.”

“Wapi Mtamba?”

“Ndio.”

“Duh! Aisee nashukuru kunijuza maana nilikuwa na mashaka labda kaua mtu huko.”

“Hapana chizi tu hata sisi hatumjui vizuri anaweza kuwa muuaji kweli.” Mjumbe akakazia na ndipo yule bwana akaagana naye na kutia gia kuendelea na safari yake na mujmbe akaanza kuwakimbilia wenzake.

Kwa mwendo wa masaa mawili hatimaye wakafika kituo kidogo cha polisi Mtamba.

“Halloo vipi tena? Hebu mshusheni hapo kafanya nini huyu?” Askari aliyevaa kiraia akiwa amekaa nje ya kituo akahamaki alipoliona kundi la watu wakifika kituona wamebeba mtu juujuu.

Mara akatoka afande mwengine mwenye sare akiwa na bunduki mkononi. Huyo alikuwa Koplo Ponda, askari mpya kwenye kituo hiko baada ya kuhamishwa akitokea Dar es salaam ambapo awali alikuwa Sajini wa polisi Mtongani, kabla hajashushwa cheo kutokana na masahibu ya mkasa wa Mitaa na Polisi.

“Vipi tena hapa! Kafanya nini huyu kichaa kabaka?” Naye akauliza swali lilelile alilouliza yule wa kwanza. Mwenyekiti ikabidi ajitambulishe na kuanza kutoa maelezo.

“Lifungueni kamba, Afande, nenda kalifungie sero! Mzee njoo utolee maelezo huku.” Afande ambaye hakuvaa sare akamkatisha mwenyekiti na kutoa amri kwa Koplo Ponda. Kituo kilikuwa na askari wawili tu na sero ilikuwa na mtu mmoja ndani. Izani akaingizwa huku mwenyekiti akielekea kaunta na kuanza kutoa maelezo na yule afande akawa anaandika.

“Uko wapi huo mkoba?” Afande akauliza baada ya mwenyekiti kutoa maelezo juu ya kile walichomkuta nacho mtu yule. Mwenyekiti akamkabidhi naye alipoufungua ndani yake akashangaa na kutikisa kichwa kwa masikitiko.

“Hili sio chizi! Hili ni teja la madawa ya kulevya. Enhee baada ya hapo mkachukua hatua gani? Mbona ana majeraha mlimpiga?”
“Hapana Afande! Hakupigwa ila amekutwa hivyo. Nami nikaamuru kumfikisha sehemu hii salama ili asije akaleta madhala kijijini kwetu nanyi mnaweza kujua mengi zaidi kuhusu mtu huyu.” Mwenyekiti akazungumza kwa adabu. Baada ya yule afande kumchukua maelezo mwenyekiti akamruhusu aende na watu wake.

Wakatoka na safari ya kurudi Kisanzala ikachukua nafasi. Wakiwa njiani walienda wakizungumza njia nzima huku mada kubwa ikiwa kuhusu mtu yule. Njiani wakakutana tena na ile gari ndogo, Vitara nyeusi ikawapigia honi nao wakaipungia mkono hususani mjumbe ambaye alizungumza na dereva wa ile gari wakati walipokuwa wanaenda Mtamba. Mwenyekiti akaitazama ile gari kwa mashaka.

“Kwani nani yule?” Mwenyekiti akamuuliza mjumbe.

“Hata simfahamu aliniita tu kuniuliza tulipokuwa tunampeleka yule chizi kituoni.” Mjumbe akajibu na hadithi nyengine zikaendelea.

Upande wa pili ndani ya ile gari dereva aambaye alikuwa peke yake garini akatoa simu na kupiga huku mkono mmoja akimakinika na usukani.

“Hallow kiongozi! Nimejua alipo lakini bado hayupo kwenye mikono yetu.” Akaongea baada ya simu kupokewa upande wa pili.

“Unamaanisha yupo kwenye mikono gani?” Sauti ya aliyempigia ikamuuliza.

“Polisi.” Akajibu na kukaa kimya.

“Nisikilize kwa makini Chox…..Hakikisha unamtoa hapo! Usikibweteshe kichwa chako. Kuna polisi gani wa kusumbua huko porini? Tumia ujanja wako atoke na usipende kunipigia simu kwa kazi nyepesi.” Sauti ikamfokea kiasi na kumfanya akunje uso na kushusha pumzi huku akiilazimisha sauti yake kuongea kwa utii.
“Lakini kumbuka mkuu ana mzigo yule? Wanaweza kunibananisha hapo!” Akasema lakini upande wa pili simu ikakatwa. Akatukana tusi la nguoni wakati huo gari ilikuwa inapanda mwinuko wa kuingia kijiji cha Mtamba. Akaigesha upande wa kushoto na kutulia akifikiri kwa kina nini afanye.

Huyo alikuwa ni CHOX kijana wa Chikala Gumbo aliyepewa jukumu la kumfatilia Izani na kumpa huduma za madawa. Kwenye gari alikuwa na mzigo mwengine wa sindano sita na Mikate mikubwa mitatu, pia juisi kubwa kopo mbili na maji. Vyote ilikuwa kwa niaba ya Izani, lakini kuingia mikononi mwa polisi akaanza kutia shaka kiasi.

Bora ningewalaghai wale wanakijiji pale ningemchukua kirahisi
Akajisemea na kuwaza moyoni. Akafungua zipu ya mkoba wake mdogo uliokuwa kiti cha pili na kutabasamu baada ya kumjia wazo kichwani. Akachukua vibunda viwili vya noti vilivyojaa na kuvitia mfukoni. Kisha akashuka na kufunga milango ya gari, akaanza kuzichanga hatua kuelekea kilipo kituo kidogo cha polisi Mtamba.

_____***_____
| KILIMANJARO |

Ukungu umefunika kilele cha mlima mkubwa barani Afrika. Baridi limeshamiri licha ya majira kusoma saa saba mchana. Malaika mwenye mbawa sita akamtokea Anita kwa mara nyengine punde alipoigusa anga ya mkoa huu wa Kaskazini.

“Sasa umefika kwenye eneo husika Anita! Anza kuufata usawa wa mashariki wa eneo hili. Utamkuta mtu mwenye roho safi na akili timamu akiwa nyumbani kwake amelala. Mola wako amempa kibali cha kuzungumza nawe punde utapoingia ndani yake. Hakikisha unamshawishi na kumwambia ukweli wa ombi lako hakika yeye ni mwenye imani na mwalimu wa sheria anayefata haki.”

“Nitajuaje kama ni yeye! Nambie ishara ya upekee wake tafadhali?” Anita akauliza.

“Utapoliona paa la nyumba iwakayo Nuru ya kumetameta ndimo humo alipo. Mlango wake utakuwa wazi na nafsi yake itakukarimu ikikuona.” Malaika akasema na kupotea mbele ya Anita kwa kasi ya ajabu. Anita akatuama kuufata uelekeo wa mashariki. Na kweli baada ya mwendo mfupi kwa mbali akaweza kuiona nyumba moja katikati ya nyumba nyingi ikiwa inawaka na kumetameta Nuru.

Nafsi ya Anita ikatabasamu na kujawa na matumaini ya mwanzo mzuri wa kufanikisha adhma yake aliyoomba ridhaa kwa Mola wake.

* *
Ndani ya nyumba hiyo iliyokuwa katikati ya mji anaonekana bwana mmoja akiwa anasinzia kwenye kiti huku mbele yake kukiwa na meza yenye vitabu kadhaa juu yake na pembeni kulikuwa na laptop iliyokuwa imewashwa. Usingizi wa mchana ukamshinda nguvu na kujikuta ananyanyuka kukielekea kitanda na kujibwaga.

“Neema mke wangu….” Akaita yule bwana akiwa kitandani, mwitikio ukasikika upande wa pili. “Abee Mume wangu.” Msichana mrembo akaitika akiwa jikoni akiaandaa mahanjumati.

“Napumzika kwa masaa mawili naomba usiniamshe labda kwa dharura kubwa.” Akasema yule bwana huku akiitegesha alarm kwenye simu yake na kujilaza kitandani.

“Sawa mume wangu.” Mkewe akamuitika bila kuhoji. Alipoulaza ubavu haikumchukua hata dakika kumi usingizi ukawa umemteka yule bwana. Haukupita muda tangu usingizi umpambe akajikuta anapatwa ndoto ya ajabu mchana ule asiyowahi kuifikiria.

Akawa anajiona anasafiri na gari kuelekea kwao Dutumi Morogoro. Akiwa njiani katikati ya msitu gari yake ikaharibika. Mara akiwa anatafakari namna ya kuita msaada ndipo akamuona mtu mmoja akiwa ameegama kwenye mti akijidunga sindano ya madawa mkononi huku udenda ukimchuruza. Akiwa bado anashangaa mara akastushwa na sauti kutokea nyuma yake.

“Ni yeye huyo. Mtu mwema kama wewe aliyeponzwa na wema wake.” Akageuka kumtazama msemaji alikuwa ni mwanamke. Msichana mrembo aliyeonesha wazi anatoka kwenye familia inayojiweza. Lakini machoni anaonesha mwenye huzuni kubwa. Akiwa ametaharuki, msichana akazidi kuzungumza.

“Naomba msaada wako wa kumuokoa mtu huyo mwema. Hakika ameharibiwa akili na kuingizwa kwenye huo mkumbo aliopambana kuwatoa wenzake. Anaitwa Izani Nteze. Naomba umtafute na kumpa msaada wa kweli. Yote yaliyosemwa na kuandikwa juu yake ni uongo. Ila ukweli wake ni vile alivyokuwa hapo kabla. Yule mchungaji anayejiita mtu wa Mungu ndiye mnafki aliyetengeneza mchezo wote kwa Izani. Hebu muone sasa alivyo! Anateseka nawe ni mtu pekee unayeweza msaidia.”

“Wewe ni nani?” Akauliza kwa mashaka huku akigeuka tena kumtazama yule bwana akashangaa kuona anajidunga sindano nyengine tena.

“Mimi ni Anita Ndimbo! Mfuasi wa harakati za Izani Nteze. Mungu amekuchagua wewe mtu wa haki itumie sheria ya kuufichua uhalifu wa mchungaji Ndimbo Masizi. Yeye ni baba yangu lakini si mtu mwema kama anavyojitangaza. Yeye ni Shetani mwenye sura ya Malaika.” Baada ya kusema hayo yule binti akapotea machoni mwake kimuujiza. Akahamaki na kugeuka upande wa yule teja aliyekuwa anajidunga naye hakumuona. Akiwa mwingi wa wasiwasi akageuka kuitazama gari yake nayo haipo! Hofu ikamvamia na kujikuta anataka kupiga yowe la hamaniko lakini Mara…….! NGRRRRRIIII NGGGRRRRRIIIII

Sauti ya alam aliyoitegesha ikazirudisha fahamu zake na kumwamsha usingizini. Anatazama kushoto alipokuwa awali anamuona mkewe akiwa anaperuzi kwenye laptop yake. Wanakutanisha macho ila wasiwasi haukujifichi machoni mwake. Mkewe anamstukia na kumuuliza.

“Vipi mbona hivyo mume wangu! Uko sawa?”

“Ni ndoto tu ya mchana, usihofu.” Akajibu na kunyanyuka kitandani akakaa kitako akiitafakari ile ndoto.

“Pole baby! Vipi utakula au nikuwekee maji ukaoge kwanza?”

“Yap! Kuoga kwanza.” Akamjibu mkewe huku akiwasha internet kwenye simu yake na kuingia google. Akaandika jina Izani Nteze na kuruhusu kitufe kitafute habari zake. Akashangaa kukutana na habari za Izani na muunganiko wa kile alichokiota.

Akaanza kusoma hata pale mkewe aliporejea na kumwambia maji tayari hakumsikia. Mapigo ya moyo wake yakawa yanaongeza kasi kila alivyopitia habari za Izani Nteze hasa alipofika kipande kilichoandikwa .…..mwishowe kijana huyo akaiba pesa za kanisa na kutokomea kusipojulikana. Lakini Mungu akampa maono mchungaji wake Ndimbo Masizi na kutabiri adhabu ya kudhalilishwa kijana Izani Nteze kwa kile alichokifanya na unafki wake.

Ndipo mwezi mmoja mbele akaonekana Izani akiwa amerukwa na akili na amekuwa teja wa dawa za kulevya ambazo siku za nyuma alisimama kidete kuzipinga hata akamvutia mchungaji Ndimbo kuitangaza kampeni yake na kumpangia nyumba ya kuishi na kumpa kipindi cha televisheni lakini yote ikawa kazi bure kwa kijana Izani akaona haitoshi akamuibia mtu mwema aliyemtoa mtaani.
Akashusha pumzi yule bwana na kukuna kichwa. Mkewe akabaki anamtazama kwa fadhaa akamuuliza.

“Bado unaitafakari hiyo ndoto au kuna jipya mume?”

“Hamna mke wangu, Niko sawa tu.” Akajibu huku akisimama na kuiacha simu kitandani. Akaelekea bafuni kuoga huku akiwa anashangaa maajabu ya ndoto ile ya mchana na uhalisia wa mambo yanavyoenda.

Jina lake ni ZUBERI MWANAHAKI. Yeye ni mzaliwa wa Morogoro aliyekulia Arusha. Wazazi wake walifariki akiwa mdogo na alilelewa na mjombaake aliyekuwa mwalimu wa shule ya sekondari Ngarenaro. Kama lilivyo jina la ubini wake ndivyo alivyo.

Mwanahaki alipenda haki siku zote tokea shuleni. Alikuwa mtu wa kudadisi mambo na mwenye imani ya kweli. Hakuwa muongo wala hakuwa mtu wa kukata tamaa. Alisomea sheria na alipasi vyema mpaka elimu ya juu. Aliamua kuwa mwanasheria wa kujitegemea, na mara zote toka aanze kazi zake hakuwahi kushindwa kesi.

Amekuwa miongoni mwa wanasheria wachache wenye mioyo ya ajabu nchini. Na aliipenda kazi yake, mara nyingi hakuisha kujifunza kwa kupitia kesi mbalimbali za nchi tofauti zilizomuongezea umakini na uzoefu.

Bwana Zuberi Mwanahaki alikuwa na mke mmoja ila bado hakuwa amebahatika kupata naye mtoto baada ya kufunga ndoa miezi michache iliyopita. Na kilichomvuta kumpenda mwanamke huyo si tu kwakuwa naye alikuwa mwanasheria kama yeye, ila kutokana na imani ya ujasiri wa mwanasheria huyo aliyevuma kwa kuwafichua Polisi walioenda kinyume na haki za Mitaa, baada ya kifo cha dereva bajaji aliyepigwa risasi miaka michache Mtoni kwa Azizi Ally jijini Dar es salaam.

Mwanasheria huyo aitwaye NEEMA HUSSEIN kabla hajahamia Arusha walifahamiana kupitia chama chao cha wanasheria (TLS) na alipoamia Arusha mahusiano yao yakakomaa na mwishowe wakawa mke na mume wakiishi kwa furaha na amani.

Bwana Zuberi Mwanahaki siku zote aliamini ndoto ni habari za siri ambazo Mungu huwaonesha waja wake. Na aliziamini sana ndoto zake ingawa hii aliyoota mchana ilikuwa ya kipekee na tofauti kabisa na ndoto alizozizoea za mafumbo.

Aliifikiria ndoto ile na kile alichokiona hata alipokuwa bafuni. Alipomaliza kuoga alijumuika na mkewe sebuleni kula chakula huku akimsimulia kwa ufupi kile alichokiota na maajabu aliyoyaona baada ya kuingiza jina la yule teja mtandaoni.

“He! Mbona miujiza mume wangu. Lakini naomba usiumize kichwa ni ndoto tu.” Neema akasema huku akimtazama usoni. Zuberi hakumjibu kitu akaendelea kula. Alipomaliza akarejea kitini na kuketi mbele ya laptop yake. Aliamua kuunganisha mtandao na kuanza kusoma tena habari za Izani Nteze na mchungaji Ndimbo Masizi. Na hapo ndipo akashtuka zaidi baada ya kuiona picha ya mtoto mkubwa wa mchungaji ambaye aliandikwa amefariki wiki moja iliyopita. Akashangaa na macho yake yakaganda kumtazama yule binti Anita Ndimbo na kubaki kinywa wazi.

“Ndiye yeye kabisa huyu! Neema mke wangu..! Hakika sikupata ndoto tu bali huyu binti amenitokea na nina mashaka na alichonambia kina ukweli ndani yake. Mungu wangu!” Akahamaki na kumshirikisha mkewe aliyebaki kushangazwa na taarifa zile. Akamtazama usoni mumewe akaishiwa maneno.

“Kwahiyo utafanyaje sasa?” Neema akauliza

“Sijui.” Zuberi akajibu na kushusha pumzi ndefu.

ITAENDELEA......
 
MFUASI
07
_____***______
| DAR ES SALAAM |
Saa saba mchana anaonekana mchungaji Ndimbo Masizi akiwa anatoka kwenye ofisi yake kanisani akiwa na Chikala. Usoni alijitahidi kuificha hasira yake asifanikiwe. Akaingia garini na Chikala akapanda mlango wa dereva.

“Unajua fika nakutegemea kwenye nyakati kama hizi lakini sasa naona dalili za kunisaliti.” Mchungaji akaongea kwa sauti ya chini yenye kumaanisha. Chikala akawasha gari huku akimtazama bosi wake.

“Hapana bosi! Kwanini niwe hivyo? Mangapi nimekuwa mtii kwako na hata hili sikupinga, ila najikaza tu lakini ukweli naumwa tokea usiku wa jana na sikutarajia kama nitaendelea kujihisi vibaya mpaka muda huu.” Chikala akajitetea huku akiendeesha gari taratibu.

“Inatosha! Endesha niwahishe Airpot.” Mchungaji Ndimbo akasema huku uso wake akiugeuzia pembeni. Akafikiria muda mfupi alipomuona Chikala anaingia ofisini mwake hakuona kama ana dalili za kuumwa chochote. Hata alipopatiwa gazeti lenye ile nguo ya ndani akamuuliza kuhusu vyeti vya hospitali lakini hakuridhishwa na majibu ya dereva wake aliyemuamini.

“Nimeviacha nyumbani kabla sijaja hapa.” Akalikumbuka jibu la Chikala na alipomsoma machoni akagundua alikuwa anamuongopea. Aliihakikisha ile nguo ya ndani ya Anita na kuitia kwenye begi lake ndipo akazungumza kwa njia ya simu na mtu wa uwanja wa ndege kubatilisha tiketi moja ya kwenda na aigeuze iwe ya kurudi. Kila kitu kilipokuwa sawa ndipo ikambidi amwambie Chika amfikishe uwanja wa ndege na sasa atakuwa anasafiri peke yake kuelekea Nairobi ingawa nafsi yake haikuridhika kutoongozana na Chikala.

Njiani hawakuwa na maongezi yoyote mpaka wanafika uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere. Chikala akamuaga bosi wake kwa kumuomba msamaha kwa mara nyengine kisha akageuza gari na kuondoka.

Lisaa limoja baadae Mchungaji Ndimbo na abiria wengine wakaingia ndani ya ndege baada ya ukaguzi. Kupitia ndege ya shirika la usafirishaji wa anga, Kenya airways, safari ya Nairobi ikaanza kwa raha mustarehe. Kwa mwendo wa lisaa limoja na dakika arobaini angani, mwishowe ndege ilitua salama kwenye uwanja wa Jomo Kenyata Nairobi, wasafiri wakaanza kushuka. Mchungaji Ndimbo hakuwa mgeni na jiji hili hivyo haikumpa usumbufu kutoka na kuzielekea Taxi zilizokuwa nje ya uwanja wa ndege. Akaingia kwenye Taxi moja wapo na kumtaka dereva amfikishe Mitaa ya Mashimoni

______***_______
| MOROGORO VIJIJINI |

“Habari ya kazi afande.” Chox akamsalimia bwana aliyekaa nje ya kituo baada ya kumfikia.

“Njema karibu!” Akaitika huku akimtazama kwa makini mtu yule ambaye hakuonesha kama ni mwenyeji wa pale kwa lafudhi zake tu.

“Samahani sana kiongozi naomba tuzungumze kidogo.” Chox akasema huku akitazama kushoto kulia. Alipoona hakuna anayewatazama akampatia kibunda kimoja yule polisi na kumstusha moyo na macho.

“Ya nini hii?” akauliza kwa hamaki huku akisita kuipokea.

“Pokea tu, ni sehemu ya ususm bufu wa kukupotezea muda kwa maongezi yangu mafupi.” Chox akajibu huku ametabasamu. Yule bwana ambaye ndiye alikuwa mkuu wa kituo kile, alichungulia kwa mlangoni kuona kama Koplo Ponda anamuona, hakuwepo.

Akakipokea kile kibunda na hakuwa na muda wa kuhesabu akakiweka mfukoni moja kwa moja. Mapigo ya moyo yalishaanza kumwenda kasi lakini alijipa ujasiri wa kipolisi. Akamruhusu Chox kuketi kwenye kiti cha plastiki kilichokuwa pembeni yake. Akawa tayari kumsikiliza hata kwa siku nzima kutokana na kibunda alichopewa ni zaidi ya mshahara wake wa miezi miwili.

“Kuna ndugu yangu akili zake si nzuri ametoroka siku ya pili sasa.”Chox akazungumza huku akitoa simu yake na kumuonesha yule afande picha ya Izani.

“Aaaah! Si huyu teja aliyeletwa na wanakijiji?” Mkuu wa kituo akauliza kwa mshangao huku akiitazama ile picha.

“Na ndio tunapambana naye ameanza kliniki mjini lakini nashangaa kafikaje huko. Naomba nisaidie niende naye tafadhali.” Chox akazungumza kwa adabu. Wakati huo Koplo Ponda alikuwa anatoka ndani ya kituo.

“Koplo hebu muachie tu huyo chizi amefatwa na ndugu yake hapa.” Mkuu wa kituo akazungumza kwa amri. Koplo Ponda hakutaka kuhoji akarudi selo na kumfungulia Izani.

“Je, mkoba aliokutwa nao wenye sindano nao unahusikaje?” Mkuu wa kituo akamuuliza Chox.

“Kwakweli sifahamu kuhusu hilo huenda ameuokota huko majalalani si unajua mtu huyu hana akili?” Chox akajibu, ingawa maelezo yake hayakujenga sababu ya msingi kwa mkuu wa kituo, ila pesa alizotanguliza kama takrima zilimfanya bwana yule asimuwekee uzito. Muda mfupi baadae Izani akatolewa na kukabidhiwa kwake.

“Hee! Niacheee! Niacheee!” Izani akapiga kelele lakini sauti yake haikuwa na nguvu. Labda kutokana na njaa ya kutwa kucha au ni alosto ya madawa. Chox akamshukuru mkuu wa kituo na kutoka na Izani akiwa amemshika mkono kwa nguvu akimvuta mpaka barabarani alipoegesha gari yake. Akamsukumia mlango wa nyuma na kufunga mlango, kisha naye akapanda sehemu ya dereva na kuiwasha gari akatokomea eneo lile akiwa haamini kama amefanikiwa kumtia tena mikononi mwake Izani kutoka kwenye mikono ya polisi.

“Kula Mikate chizi wewe, Nani kakwambia utoroke kule.” Chox akawaka huku akimtupia mkate Izani ambaye ikamlazimu kutulia na kuanza kufakamia mikate kwa pupa ya njaa. Wakati huo ndipo Chox aliamua kuchukua simu na kumpigia bisi wake huku mkono mmoja akimakinika na usukani, na miguu ilizidi kukanyaga mafuta.

***
|MASHIMONI - KENYA|

Mashimoni ni moja ya mtaa wa mafukara uliokuwa katikati ya Jiji la Nairobi nchini Kenya. Na hapo ndipo kulikuwa na nyumba ya kazi iliyotumika na mchawi hatari MR. ZONGO.

Yeye ni mtaalamu wa kutoa utajiri kwa njia za mazingara. Waliomfahamu walipenda kumwita Gwiji au Mtumishi.

Mr. Zongo alikuwa na makazi ya kifahari katika kata ya Muthaiga walipoishi matajiri, lakini mara nyingi yeye alilala Mashimoni kwenye nyumba maalum iliyokuwa vichochoroni ambapo wateja wake wazito kutoka sehemu mbalimbali walifika kupata huduma yake. Na wateja wake wakubwa walikuwa ni wachungaji wa makanisa wenye tamaa na wasanii waliokuwa wanatafuta umaarufu wa haraka. Ingekuwa si rahisi mtu kumjua Mr Zongo kwa sura, ingawa tetesi za uwepo wake zilikuwa kubwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki.

Kwa mwendo wa dakika nane hatimaye taxi aliyopanda Mchungaji Ndimbo ikafika mitaa ya Mashimoni. Ndimbo akashuka baada ya kumlipa dereva, alipiga hatua mpaka kwenye mti mmoja uliokuwa njia panda akasimama kisha akampigia simu mwenyeji wake.

“Nimefika Mtaalamu wangu.” Akazungumza baada ya simu kupokewa upande wa pili.

“Bila shaka unafahamu taratibu zetu Ndimbo! na unajua namna ya kufanya. Lululu yuko hapo.” Sauti nzito ikampa maelekezo kabla simu haijakatwa upande wa pili.

Ndipo Mchungaji Ndimbo alipofungua zipu ndogo ya mkoba wake na kutoa kichupa kidogo cha marashi akajidondoshea tone moja mdomoni na kujitemea mate yake mkono wa kushoto akajipaka usoni huku akisema maneno kwa sauti ya chini akirudiarudia kwa mara saba. Baada ya hapo mbele yake akatokea binti aliyekuwa mtupu. Akamsogelea huku akiwa ametabasamu.

“Vua twende! Bado una mashaka Ndimbo?” Binti yule akasema huku akimfungua vifungo vya shati Mchungaji Ndimbo.

“Ha-hapana Lululu ni sawa tu! Naelewa.” Ndimbo akazungumza huku akimeza mate na kuanza kuvua nguo zake eneo lile la wazi ambalo sasa alijua kuwa haonekani na mtu yeyote wa kawaida.

Baada ya Ndimbo kusaula naye kuwa mtupu kama alivyozaliwa ndipo kila alichokuja nacho akakiacha pale kwenye shina la mti kasoro ile nguo ya ndani ya Anita tu, ndiyo aliitoa kwenye begi na kuishikilia.

Binti aliyetokea kimazingara akamuongoza kukata vichochoro kuelekea kwenye nyumba husika ambamo Mr Zongo alikuwamo.

Mchungaji Ndimbo alimfahamu Mr. Zongo miaka mingi kiasi kupitia rafiki yake wa Kenya aliyemuunganisha naye baada ya kuijua kiu yake ya kuvuna utajiri kupitia Kanisa. Siku ya kwanza ilikuwa ngumu sana kwa Ndimbo kufika kwa mganga huyo wa ajabu kutokana na masharti ya kumtaka avue nguo zote pale kwenye mti baada ya kunywa tone la marashi maalum na kujipaka mate usoni. Hilo halikuwa jambo jepesi. Hata alipozoea bado ilimtatiza kama ambavyo Chikala ilimtatiza siku alipofika naye kwa Mr. Zongo.

Lakini hiyo ndiyo ilikuwa njia pekee ya kumfikia Mr Zongo pindi unapofata huduma zake za kichawi. Na kila utachokiacha pale mtini hakuna awezaye kukiona wala kukichukua. Binti Lululu ni msaidizi pekee wa Mr. Zongo kwaajili ya kupokea na kusindikiza wageni. Naye alikuwa kama kiburudisho cha tiba ya wenye matatizo ya nguvu za kiume na kismati kwa wenye kutaka wanawake. Lakini yote hayo yalifanyika kwa namna ya siri za kichawi ambazo mtu wa kawaida asingeweza kuzifahamu kirahisi.

“Bwana Ndimbo Masizi. Nafsi ya binti yako inataka kulipa kisasi na kama hatukuifunga naiona jinsi itavyokuadhili na kukuumbua. Ni vyema umefika mapema.” Mr. Zongo akazungumza kwa sauti nzito mara baada ya Mchungaji Ndimbo kufika kilingeni kwake.

“Ndio mkuu! Tumaini langu ni kwenu. Nifanyeje sasa?” Mchungaji akazungumza akiwa amepiga magoti mbele ya Mr. Zongo aliyekaa kwenye kigoda kilichotengenezwa kwa mafuvu na mifupa ya mtu.

“Vaa hizo twende kwenye chumba cha Sita.” Zongo akasema huku akimuonesha kwa kidole nguo maalum alizotakiwa kuvaa Ndimbo, ambazo wakati huo zilikuwa mikononi mwa Lululu, binti aliyeongozana naye kutoka pale mtini. Mchungaji akageuka na kupokea shuka mbili nyekundu na kuvaa kama masai.

Mr. Zongo akasimama na kuanza kupuliza kibuyu chake huku akitembea kukielekea chumba husika na nyuma yake Mchungaji Ndimbo akafatia.

______***_______
| DAR ES SALAAM |

Alipotoka uwanja wa ndege baada ya kumsindikiza bosi wake, Chikala akaelekeza moja kwa moja mpaka Tandale mitaa ya uwanja wa fisi ambapo Izani alitokea. Aliegesha gari na kushuka akiwa ametinga miwani yake meusi, akatazama kushoto kulia na kuvutiwa na saluni ya kinyozi iliyokuwa mbele yake karibu na uwanja.
ZOMBOKO HAIR CUTING SALOON! Akayasoma maandishi ya utambulisho wa ofisi aliyokusudia kabla hajaingia ndani.

“Karibu sana bro!” Kijana aliyekuwa ameketi sofani akitazama luninga akamkaribisha. Hakukuwa na mtu yeyote wa ziada.

“Wewe ndiye Kine mtoto wa Zomboko?” Chikala akauliza huku akikaa kwenye kiti cha kunyolewa.

“Yaaah kaka ndiye mimi.” Kine akajibu huku akitabasamu akimfunika kitambaa maalum cha kuzuia nywele kumchafua mteja.
“Umeacha kuimba siku hizi?” Chikala akauliza.

“Unanyoaje bro!” Kine akabadili mada badala ya kujibu.

“Oooh! Nikwangue ndevu tu.” Chikala akasema huku akikaa vizuri.

Kilichomfikisha kunyoa hapo si kwasababu alikuwa anamfahamu Zomboko tu, bali pia alikuwa anajenga mazoea ya kupata taarifa za Izani kama zimevuja. Mahala walipomficha hakutaka mtu wa uwanja wa fisi apajue. Kine akaanza kumnyoa ndevu, baada ya muda mfupi akawa amemaliza.

“Hivi, yule dogo aliyekuwa anatembea na spika akipiga vita matumizi ya madawa bado yupo?” Chikala akauliza kama mwenyeweji aliyesafiri nje kwa muda. Kine akafikiria na kumkumbuka mtu aliyeuliziwa.

“Unamaanisha Izani?”

“Haswaa! Ndiye huyo.”

“Aaah yule sidhani kama mzima au vipi. Mara ya mwisho naye alikuwa teja sijui chizi baada ya kumuibia mchungaji huko alipofadhiliwa.” Kine akafunguka alichokijua akiwa hana wasi na mteja yule asiyemjua. Lakini maneno yake aliamini huenda akawa rafiki wa zamani wa baba yake.

Baada ya Chikala kuona hakuna tetesi za kuvuja mahala alipo Izani akasimama na kumuaga Kine baada ya kumpa noti ya shilingi Elfu tano huku akimtaka chenji abaki nayo.

“Asante sana kaka. Karibu tena.” Kine akashukuru na kufurahi.

Chikala akatoka na kuzunguka maeneo machache ya uwanja ule wenye sifa nyingi za ajabu. Baada ya kuona hali ya utulivu ni kubwa na hakuna anayezungumzia habari za Izani, akafarijika Chikala na kuingia garini akawasha ili aondoke. Lakini mara simu yake ikaita. Alipoitoa kuitazama alikuwa ni Chox Moro, akaipokea haraka.

“Nipe mpya Chox.”

“Tayari boss niko naye.”

“Safi sana, hakikisha hakupotei tena mpaka nikupe amri aidha ya kummaliza au kama kuna mabadiliko basi usichukue hatua yoyote kabla hujanitaarifu.” Chikala akamsisitiza Chox kwa njia ya simu.

“Nimekuelewa kiongozi.” Chox akajibu, wakaagana na kukata simu.

______***_______
| ARUSHA |

Dakika na masaa yakasonga tokea Zuberi Mwanahaki aote ndoto ya ajabu iliyo sawa na ukweli wa dunia yao. Kwakuwa alikuwa mtu wa imani tena mwislamu safi aliyeshika swala tano, Zuberi siku hiyo aliswali rakaa mbili maalum kabla ya swala ya usiku akamuomba Mola wake kujua maana ya kile alichokiota na namna ya kufanya.
Kitu ambacho hakukijua wala kukiona yeye na mkewe, ni uwepo wa nafsi ya Anita kwenye nyumba yao.

Anita alikuwa huru akitembea hapa na pale na kila alichokuwa anafanya Zuberi alikiona na kilimvutia. Alipenda namna watu wale wanavyoishi kwa upendo na furaha. Alichokuwa anasubiri sasa ni matokeo ya kile alichofanikiwa kumshawishi Zuberi katika nafsi yake.

“Mke wangu, Allah atatuonesha njia na namna ya hii ndoto na hiki kilichotokea.” Zuberi akazungumza alipotoka kuswali na kukaa sebuleni na mkewe wakila matunda huku wakitazama filamu ya watu wa pangoni.

“Naamini mume wangu usemacho na pia nakuombea kwa Mungu akuzidishie wepesi na maarifa.” Neema akasema huku akikiegemeza kichwa chake kwenye kifua cha Zuberi.

Wakati huo nafsi ya Anita ilikuwa pembeni ikishuhudia. Na mara ndipo akatokea yule Malaika mwenye mbawa sita. Zaidi ya Anita hakuna aliyemsikia wala kumuona.

“Anita! Adui yako sasa yupo mlangoni. Huruhusiwi kutoka nje ya nyumba hii mwenyewe. Ngome pekee ya kujificha ni ndani ya Mwanahaki. Vita iliyo mbele yako ni kubwa kwakuwa adui yako amejua nia yako.” Akazungumza yule Malaika huku akifungua mbawa yake moja iliyotoa mwangaza na kujitengeneza luninga ya ajabu.

Mara akaonekana Mchungaji Ndimbo akiwa kwa yule bwana aliyemuona siku ya mazishi yake. Bwana mwenye madevu. Mganga wa Kienyeji kutoka Kenya anayejiita Mtumishi au Dokta Zongo.

“Wanachotaka sasa kukufunga katika ulimwengu huu pia usiwe huru. Na salio lako la kuishi hapa ni la muda tu! Mola wako kwa utukufu wake amekupa neema kupitia Mwanahaki utakuwa salama iwapo utakumbuka kuzingatia. Kumbuka pia uadui unaokuandama una nguvu ya kukudhuru kwa mara ya pili ingawa hauwezi kukuua tena.” Malaika akazungumza zaidi wakati Nafsi ya Anita ikibutwaika na vile baba yake alivyokuwa anaelekezwa cha kufanya akiwa kwenye chumba cha ajabu kilichojengwa kwa pembe tatu na kila pande kukiwa na mchoro mkubwa wa namba sita. Kilichomstua zaidi Anita kuona Mgomba ukiwa katikati ya kile chumba kilichozungushiwa mishumaa iliyokuwa inawaka. Akamsikia yule bwana akimuamuru baba yake kuuvalisha ile nguo yake ya ndani ule mgomba.

“Ni nini hiki kwanini bado wanayo nguo yangu?”

“Huo ni mwili wako wa kichawi ambao baba yako anauona kwa sasa. Ingawa uhalisia si mwili wako uliozikwa. Wanahitaji sasa kuunganisha mawasiliano ya kuona ulipo kupitia kivuli cha nafsi.”

“Je, Na Izani atakuwa salama?” Anita akauliza kwa mashaka zaidi.

“Usalama wa Izani upo kwenye mafanikio ya Mwanahaki vile utavyoweza kumshawishi ndivyo utajiongezea kibali cha kumtoa haraka na kumfatilia. Kumbuka, wewe ni nafsi tu na bado hujaingia rasmi kwenye ulimwengu wa mauti. Endapo utakamatwa na nguvu za adui zako hakika pia hata Izani hatokuwa salama.”

“Ina maana nguvu zao ni kubwa kiasi hata nilipo wananiona?” Anita akauliza huku akikumbuka mbona hakuonekana kwa yoyote aliye hai tokea amefariki!

“Huku wanakuona kwa alama maalum ambayo waliichukua wakati unatolewa kwenye mwili.”

“Alama ipi hiyo? Je, haiwezekani muifute?”

“Anita, damu iliyotoka eneo lako nyeti ni damu yenye nguvu ya kunasa mawimbi yako katika maisha haya mpaka zipite siku arobaini. Hivyo ndivyo wanavyoweza kukunasa kwa mawimbi na kukufungia kwenye kifungo cha Nafsi mpaka utapofunguliwa mlango wa ulimwengu wa mauti ndipo kifungoni utapotea.”

“Lakini kwanini usiwazuie ewe Malaika Mtakatifu?”

“Anita….! Sisi ni tofauti na nyinyi Wanaadamu. Sisi tunafanya kile tunachoamrishwa tu! Na ndivyo tulivyoumbwa. Hata haya nikwambiayo ni ujumbe nilioamriwa nikufikishie kutoka kwa Muumba wetu. Yeye ni mwenye Nguvu na ametukuka lakini kazi zake zinafanyika kwa rehema na inapaswa imani na subira katika kuzitazama. Angeweza kuzuia yote lakini kwakuwa amewapa chaguo kwenye matendo yenu ndio maana amewaacha adui zako watende kile wakitendacho nawe unapaswa kutenda hiki nikwambiacho ili uweze kuwa salama kwenye vita hii ambayo pia unaweza kushindwa ikiwa utachagua kwenda kinyume.”

Baada ya kusema hayo Malaka akapotea na ile video ya ajabu ikayeyuka. Nafsi ya Anita ikaingiwa na hofu kubwa baada ya kusikia maneno ya Malaika yule ambaye hakujua anaitwa nani na ana mamlaka gani.

Akatazama mlango wa nafsi ya Zuberi Mwanahaki na kuuona ukiwa wazi. Akaamua kuingia ndani yake ili abaki salama asinase kwenye mtego wa adui zake ambao ulikuwa umeanza kutegwa katika
ulimwengu alipo.

ITAENDELEA.......
 
MFUASI
08
|MASHIMONI - KENYA|

Ndani ya chumba cha SITA ndimo walipokuwa Mr. Zongo na Mchungaji Ndimbo Masizi ambaye mkononi alikamata ile nguo ya ndani aliyovaa Anita siku ya mwisho.

“Mvishe!” Mr. Zongo akazungumza akimuonesha Ndimbo mwili wa binti uliokuwa umelazwa utupu katikati ya mishumaa mingi kwenye kile chumba.

Mchungaji Ndimbo akastushwa kuona ni mwili wa Anita ambaye walishamzika wiki moja nyuma. Akataka kusita kwa taharuki akatamani kuuliza kujua.

“Mvisheee Ndimbo!” Zongo akapaza zaidi sauti na Ndimbo Mchungaji Ndimbo alipopiga magoti na kuanza kuuvisha ule mwili ile nguo. Moyo ulimwenda puta na hofu kumtanda. Hakujua kama akionacho ni mazingara. Katika uhalisia alichokuwa anakivisha ile nguo ni mgomba wa kichawi ambao Mr Zongo aliutengeneza.

“HA HA HA HAAA! Usiogopee Ndimbo ndivyo kazi inavyotaka uwe na moyo wa ujasiri.” Mchawi akasema huku akiuzunguka ule mwili na kuumwagia maji ya ajabu kutoka kwenye kibuyu alichoshika. Mara ule mwili wa mazingara ukapotea.

Mr. Zongo akatazama pale ulipopotelea mwili zaidi ya dakika tatu bila kupepesa kama mtu aliyeganda. Baada ya hapo akaimba nyimbo zake kwa lugha isiyoeleweka kwa zaidi ya nusu saa. Wakati huo wote, Mchungaji Ndimbo alisimama eneo lilelile hakukaa wala kupiga hatua kwenda popote.

Chumba kile kilikuwa na mambo kadha wa kadha ya kuogofya. Mchoro ya namba 6 kubwa kwenye kila pembe haikutisha kama yalivyotisha mafuvu ya watu yalyokuwa yananing’inia juu ya dali kama vibuyu. Pia kulikuwa na Pembe za wanyama kwenye kila V ya chumba. Chini waliposimama pia kulikuwa na mchoro wa Jicho na pale ulipopotelea mwili ndipo kulikuwa na mboni ya jicho hilo kubwa lililochorwa kwa gharama na stadi mkubwa.

“Ilipaswa tumuone kwa dakika tatu tu! Lakini sasa haonekani.” Mwishowe Zongo akaacha kuimba na kumgeukia Mchungaji Ndimbo akamuhabarisha kile kilichokuwa kinaendelea.

“Una maana gani Mtumishi.” Mchungaji akauliza kwa wahka.

“Namaanisha kuna nguvu inayosababisha asionekane au mlikosea masharti ya utunzaji wa nguo yake siku alipovuliwa. Una hakika haikuonwa na zaidi ya watu sita?” Zongo akauliza huku akitambuka tambuka eneo lile ulipopotelea mwili.

“Nina hakika kwa hilo.” Mchungaji akajibu huku akimfikiria Chikala kama angeweza kuvujisha kumuonesha mtu mwengine ile nguo ya ndani. Hakuona kama Chika angweza kuwa mzembe kiasi hiko.

“Basi kama ndivyo, itakuwa kuna nguvu nyengine inayozuia kuonekana Anita! Shika hii…Usiiachie wala usitishwe na utachokiona tunasafiri kuchungulia ulimwengu wa majibu!” Zongo akasema na kuchukua pembe moja akamkabidhi Ndimbo akaipokea.

Kilichofatia hapo kilizidi kumuweka kinywa wazi Ndimbo Masizi. Hakika siku hii aliviona vituko vingi vya kichawi kutoka kwa Mr. Zongo au kwa jina lengine Mtumishi.

Akashangaa kuona kile chumba kikizunguka ingawa wao hawakuzunguka. Na mara likatokea jitu la ajabu katikati yao, laiti isingekuwa tahadhari ya kutohofia aliyopewa na mwenyeji wake basi huenda Mchungaji Ndimbo angetimua mbio kwa vile jitu lilivyotisha.

“Wapi unanusa harufu yake?” Mr Zongo akaliuliza lile jitu.

“Mashariki ya Kwetu iliyo Kaskazini ya kwao ananukia.” Likasema Jitu huku likinyoosha mkono wake uliokuwa na kiganja kikubwa kama beseni la kuogea watoto.

Zongo na ndimbo wakamkinika kutazama kilichoanza kuonekana kwenye mkono wa lile jitu. Lilikuwa ni jitu lile lile lililomtokea Anita siku ile ya mwisho na kumnyonya damu.

Kupitia kiganja chake ikaonekna nyumba ya Zuberi Mwanahaki iliyokuwa jijini Arusha.

“Nioneshe Ndani yake, onesha chakula pia baada ya harufu. Ndimbo tazamaa!” Zongo akanena zaidi huku akizidisha mzuka wa kuimba wimbo uliolihamasisha jitu lake kufanya kazi kwa umakini.
Lakini kadili jitu lilivyojitahidi kunasa mawasiliano ya kumuonesha Anita liliishiwa ujanja na mwishowe akafanikiwa kumwonesha Zuberi Mwanahaki.

Ndipo Mr Zongo akang’amua jambo.

“Oooooh! Ni huyu kumbe! Ni huyu ndiye anaishi sasa. Umechelewa bwana Ndimbo na ili usichelewe zaidi imeibuka kazi mpya hapa.” Maneno ya Zongo yakamtia tumbo joto Ndimbo akatumbua macho kwenye kiganja cha jitu kumshangaa mwanaume aliyekuwa anaonekana wenye tv ya maajabu.

“Ni mwanaume lakini…!” Ndimbo akazungumza huku akihisi huenda Zongo hakuitazama vizuri ile picha.

“Ni mwanaume ndiyo, lakini ndiye mwenye nafsi ya binti yako kwa sasa. Na hii sasa inatulazimu tupate nafsi ndani ya nafsi ili kushinda vita yetu itayokuacha ubaki kuwa salama.” Akasema Zongo na mara chumba kikaacha kuzunguka. Lile jtu likafunika kiganja na kupotea.

Wakajikuta wamerejea kwenye chumba kilekile cha awali lakini safari hii kukawa na hali mpya ambayo ilimshangaza hata Mr. Zongo mwenyewe mbali ya uchawi wake wa kukubuhu aliokuwa nao.

Wakashangazwa kukuta mgomba katikati ya eneo ulipokuwa ule mwili waliouvisha nguo ya ndani. Lakini pia mgomba ule haukuwa na nguo ya ndani, na jambo hili hata Zongo lilimstua japo alijua maana yake lakini hakuitegemea.

“Huu mgomba?” Ndimbo akajikuta anauliza bila kutegemea. Zongo hakumjibu kitu ingawa naye alisstushwa ila akaishia kuimba nyimbo zake za kichawi.

Hakumwambia Ndimbo ambaye kwa muda huo alibaki kufunga kinywa kila aliposhuhudia mauzauza alIyojitakia kuyaona ili aishi maisha bora.

“Turudi kwenye yai Ndimbo! Turudi sasa..” Mr Zongo akasema wakati akiuelekea mlango wa kutoka kwenye kile chumba cha Sita. Mchungaji Ndipo akafatia nyuma yake kwa tahadhali akifatisha kukanyaga nyayo za mwenyeji wake.

“Nafsi ya binti yako ipo ndani ya Nafsi ya Mwanaume uliyemuona. Na ili tuweze kumfungia kwenye kifungo cha Nafsi lazima tupate nafsi inayoweza kuzama ndani ya Mwili wenye Nafsi ili tuweze kumtoa na kumnasa Kinafsi. Jambo hili linahitaji Masaa Kumi na Nane mara tatu. Ufike hapa baada ya masaa hamsini na nne, yaani kesho kutwa jioni majibu tutakuwa tumeyapata.“ Mr. Zongo akamwambia Mchungaji baada ya kuketi kwenye kile chumba cha awali. Ndimbo akashusha pumzi ndefu na hali ya mashaka ikaanza kumjia nafsini.

Ina maana itabidi kuua tena?
Akajisemea moyoni Ndimbo huku akimtazama Zongo bila kusema kitu.

“Sio kuua tena! Zipo nafsi zetu za kutengeneza kichawi zinaweza kufanya kazi hiyo. Usiogopeeee!” Zongo akajibu baada ya kulisikia swali la Ndimbo ambalo hajalitamka kinywani. Ndimbo akainama na kusujudu mbele ya Zongo akaanza kuomba kwa uchungu.

“Naomba nisaidie tafadhaliii Mkuu. Nakuomba fanya nisiumbuke katika hili.”

“Hutaumbuka Ndimbooooo! Niamini mimi tutaimaliza salama kafara yetu. Mimi ndio Zongo Mwanazongwe Mzongoaji Mwenye Zongo Zongolotubwi. Usiogopeee!” Mr. Zongo akangurumisha tambo zake kwa sauti ya chini yenye mwangwi mzito. Ndimbo akanyanyua kichwa na kukubali huku akiilazimisha nafsi yake kuamini hakuna tatizo litalompata.

“Shika hii, paka miguuni nenda kaoshe nyayo zako kwenye beseni la nyota… Hakikisha ndani ya siku zote mbili hukanyagi mchanga wa bahari ukiwa peku. Tunamfatilia Anita kupitia wewe. Ambrrrrr…” Zongo akampa Ndimbo sabuni nyekundu na kumuelekeza upande wa kushoto kulipokuwa na beseni la ajabu lililotengenezwa kwa mifupa ya watu.

Mchungaji ndimbo akafanya kama alivyoelekezwa na alipomaliza akarejea na kuketi mbele ya Mr. Zongo.

“Vyemaa! Unaweza kwenda sasaaaa” Mchawi akasema na kumfanya Mchungaji asimame mbele ya Lululu na kuanza kuvua zile nguo alizopewa akamkabidhi mikononi. Safari ya kurejea mtini ikaanza akiongozwa na msichana wa kichawi Lululu.

***
|ARUSHA|

Ulikuwa ni muda wao kulala Zuberi na Neema. Wakiwa kitandani Zuberi bila kujua kama ndani ya nafsi yake ana nafsi ya mwanamke.
Akajikuta anazama kwenye kina cha kumfikiria sana mwanamke aliyezungumza naye ndotoni. Akaanza kuyajibu maswali yaliyokuwa yanajigonga yenyewe kichwani mwake bila kujua yanachochewa na nini…

Lazima itakuwa na maana kubwa hii. Kupaota Nyumbani? Kumuota mtoto wa yule mchungaji? Kumuona yule kijana! Lazima kuna kitu Mungu ananionesha nifanye…!

Akazidi kufikiri Mwanahaki wakati Anita akiwa ndani yake anazidi kuisemesha nafsi ya Zuberi na kumtahadharisha na vishindo vilivyokuwa vinasikika nje ya nyumba. Zuberi akajikuta anasimama bila kutaraji akaanza kuuelekea mlango wa kutoka.

“Vipi mume wangu?” Neema akamuuliza akiwa kitandani.

“Nakuja usijali ngoja nicheki mazingira.” Zuberi akajibu na kumshangaza Neema.

“Mazingira?” Neema akauliza huku akitafakari maana ya jibu la mumewe. Lakini dhima ya Anita ilikuwa Zuberi afungue tu mlango ili aweze kumshuhudia adui aliyesimama mlangoni kwa Mwanahaki ambaye Malaika amemtahadharisha usalama wake ni kutotoka nje akiwa nje ya mwili wa Zuberi.

Hamadi! Nafsi ya Anita ikahofia baada ya kuliona lile lile jitu ambalo lilimnyonya damu siku ya mwisho mpaka anatenganishwa na mwili wake.

Zuberi nywele zikamsisimka alipotoka nje na kutazama hali ya usalama.

“Audhu billahi mina sheitwaani Rajyim!” Zuberi akatamka kwa imani ya kumlaani shetani baada ya kusisimka vile kwa nywele zake na kuhisi hali ya hofu kumvaa. Hakuishia hapo, akasoma dua zaidi moyoni mwake na pale pale Anita akalishuhudia lile jitu likipotea na Zuberi akarudi ndani na kufunga mlango.

“Uko sawa kweli? Bado ndoto inakusumbua!” Neema akamuuliza tena mumewe akiwa mwenye mashaka na mabadiliko ya Zuberi tokea aote ndoto ya mchana iliyofanana na maisha halisi.

“Niko sawa tu mke wangu ondoa shaka!” Zuberi akamtuliza mtima Neema na kumkumbatia. Baada ya michezo ya hapa na pale usingizi ukawapitia.

Na hapo ndipo Anita akapata wasaa mzuri wa kuzungumza tena na Zuberi katika hali ya wote kama nafsi bila kuusumbua mwili zaidi ya kuupa taarifa za kindoto

______***_______
| DAR ES SALAAM |

Wakati Chikala akikunja kona ya kutoka uwanja wa fisi, akapishana na bodaboda iliyombeba mtangazaji wa Habari za Kitaa, bwana Markus Makata.

Mark akaitazama mara mbili mbili gari aliyokuwa anaendeesha Chikala na kuifahamu.

Mchungaji leo kaja uwanja wa fisi?

Akajiuliza mwenyewe wakati huo wakawa wamefika nje ya saluni kama alivyomuelekeza mwendesha bodaboda aliyemkodi.

Akashuka na kumlipa kabla hajajitoma ndani ya saluni.

“Karibu bro!” Kine akamkaribisha Mark na wakati huo Zomboko akawa anaingia. Akamtazama Mark vile alivyo akahisi wazi hakufika kama mteja wa kunyoa.

“Mjomba Zomboko mzima wewe?” Mark akamsalimu Zomboko kwa bashasha.

“Kama unavyoniona. Nani mwenzangu.” Zomboko akazungumza huku akimtazama vizuri Mark apate kumkumbuka. Hakumkumbuka kwa haraka.

“Mimi naitwa Mark! Mzee wa habari za Kitaa. Tulikuwa wote kwenye misukosuko iliyomkuta binti yako mwaka juzi.” Mark akamkumbusha Zomboko.

“Oooh! Wewe ndiye mtangazaji aliyekupigia simu Wakili Neema?” Zomboko akauliza.

“Naam, ndiye mimi mjomba Zomboko!” Mark akajibu huku akifurahi moyoni kuona Zomboko amemkumbuka mbali ya kuwahi kuonana mara moja tu mahakamani naye hakwenda tena kutoa ushahidi wowote siku ya hukumu.

“Karibu saluni kwetu, Naona upo kikazi…?” Zomboko akazungumza huku akimtazama Mark ambaye mkononi alikuwa amebeba mtambo mdogo sambamba na kipaza sauti chenye nembo ya radio yao.

“Kweli mjomba. Nimekuja tu kuchukua taarifa za Izani Nteze baada ya kuwehuka kapotelea wapi? Maana muda mrefu sasa hajaonekana jjini.” Mark akaongea huku akikaa vyema kwenye Sofa la Saluni. Kine akashangaa.

“He! Leo mbona imekuwa kismati kila sura mpya inayokuja anauliziwa Izani.” Kine akasema, Zomboko na Mark wakamtazama kwa swali la kutaka amtaje mwengine aliyefika kumuulizia
“Kuna jamaa nimetoka kumnyoa muda si mrefu alikuja na pira moja jeusi la gharama akamuulizia, tena mmepishana kidogo tu.” Kine alipofafanua Mark akaikumbuka ile gari ya Mchungaji Ndimbo ambapo ndiko naye kulikuwa kanisani kwake.

“Yupoje mtu mwenyewe.” Mark akauliza, Kine akaelekeza mwonekano wa mtu huyo.

Ni yeye Chikala, dereva wa Pastor! Kafata nini sasa, kwanini amuulizie Izani?

Akajiuliza Mark kichwani mwake.

“Amesema anaitwa nani? Naye mtangazaji au..?” Zomboko akauliza huku akimtazama Kine. Mark akameza mate kusikia jina ambalo Chikala amejitambulsha kwa Kine.

“Hakusema ila inaweza kuwa unamfahamu labda.” Kine akajibu Zomboko akamgeukia Mark.

“Enhee kwa hiyo umekuja kutuhoji nini?” kisha akamuuliza.

“Nahitaji kujua kwanza kama Izani yupo huku, na je kwasasa mnamtazamaje wakazi wa Tandale.” Mark akazungumza huku akitazama saa yake ya mkononi na kugundua zimebaki dakika chache anatakiwa kuwa hewani redioni.

Na kwakuwa kipindi chake siku hiyo kilikuwa kinaenda mubashara akiwa mitaani, ikabidi auwashe mtambo wake mdogo na kuchomeka mike ya kuzungumza kabla hajapokea simu na fundi mitambo aliyekuwa studioni kwao kumtaka awe tayari baada ya dakika kumi ataunganishwa kwenda hewani.

“Nitafurahi kama tukifanya kipindi kabisa mjomba Zomboko umzungumzie Izani kuwawakilisha watu wa kitaa hiki ambacho katokea.” Mark akazungumza na kumfanya Zomboko amtazame kwa makini kabla hajamjibu.

“Sawa, ila usikawie si unajua tupo kazini!” Zomboko akajibu.

“Haina shida mjomba.” Mark akasema na kujiweka tayari.

Haukupita muda mrefu akajulishwa na fundi mitambo kuwa anaweza kuendelea. Akachomeka airphone sikioni iliyomuwezesha kujisikia na kuanza kufanya mahojiano na Zomboko kuhusu mtazamo wa watu wa uwanja wa fisi toka Izani Nteze alaanike na madawa je nini wamejifunza.

“Mpenzi msikilizaji, kwa mara nyengine leo tena nakukaribisha katika kipindi chako pendwa cha Habari za Kitaa. Kama nilivyokutonya wiki iliyopita baada ya kupokea simu nyingi zikitaka kujua wapi alipo Izani Nteze baada ya kulaaniwa kutokana na wizi alioufanya kanisani. Sasa leo mtu wako niko mitaa ya Tandale uwanja wa Fisi, kuzungumza na wenyeji wa hapa ambapo ndipo Izani ametokea. Hivi sasa nipo kwenye saluni maarufu ya Zombi Zomboko ambapo pia ndipo Izani Nteze alikuwa anapatikana kirahisi. Mambo vipi kaka Zomboko?”

“Poa mdogo wangu Mark karibu.” Zomboko akazungumza huku akikohoa kidogo. Kine akakaa vyema na kupachika earphones naye akaweka kituo kilichokuwa kinarusha yale matangazo ambayo alikuwa anayaona mubashara.

“Asante sana, hebu tuambie Zomboko unamfahamu vipi Izani Nteze?”

“Izani namfahamu kama mtoto wangu wa kitaa, pia ni shujaa wa kweli wa kupambana na madawa ya kulevya .”

“Na uliposikia amefanya tukio na kutoweka ulilipokeaje suala lake? Je ulibahatika kuonana naye?”

“Hapana, sijabahatika kuonana naye ingawa nilijisikia vibaya sana kusikia wanasema eti Izani kaiba tena kanisani..?”

“Mh! Unaposema eti kaiba.. hebu tufafanulie ina maana huamini kama kweli?”

“Kabisa ndugu mtangazaji. Siamini kama Izani alikuwa mwizi ingawa watu hubadilika, ila kwa yule dogo hapana.” Zomboko akasema kwa kumaanisha. Mark akatamani akatishe mahojiano kwanza lakini akapiga moyo konde na kuendelea kumuhoji.

“Hahahaa! Sawa kwa maoni yako, je unajua kwa sasa Izani yuko wapi na anaendeleaje?”

“Hapana! kwasasa sijui alipo na huku kwetu hakuonekana tangia isemekane amemuibia huyo mchungaji. Ila naamini kwa ninavyomjua Izani hawezi kuiba. Na hata kama angekuwa ndio anaanza basi asingeanzia Kanisani kwa imani aliyokuwa nayo” Zomboko akazidi kusimamia dukuduku lake.

Ndiyo tabia yake Zomboko. Si mtu wa kukubali kuzipinga hisia zake.

“Unataka kusema hata video hujaiona mjomba Zomboko?” Mark akauliza huku akicheka kwa kuona hisia za Zomboko sawa na mzaha.

“Kwani unadhani wewe na mimi nani anamfahamu vyema Izani?” Zomboko akauliza kwa sauti yake nzito akimaanisha.

“Bila shaka wewe.” Mark akajibu huku akinyamaza kucheka.

“Sikia ndugu mtangazaji. Sitaki kujisingizia nafsini kusema siufahamu moyo wa Izani. Yule kijana hakuwa na tamaa hata theluthi. Na angekuwa na tabia hiyo hata chembe mimi ningemtambua. Maisha yangu nishakuwa mwizi na nazijua dalili zote za wezi weu anachipukia au amekubuhu. Naamini Izani hakuiba hizo pesa za Kanisa.”

Zomboko akazungumza kwa hisia zilizomfanya Mark aanze kufikiria upya hisia zake. Ikabidi ayarejeshe mawasiliano studio kwa matangazo kabla hawajaendelea na kipindi.

“Samahani mjomba Zomboko, tuko live naomba usiongee kwa kukana maneno ya mchungaji si unajua redio yetu inasikilizwa na watu wengi. Isije ikaingia kasoro.” Mark akazungumza wakiwa Off-air

“Basi jihoji mwenyewe au kamtafute mtu muongo umuhoji.” Zomboko akajibu kwa kukereka. Wakati huo studio walikuwa tayari wameyarudisha matangazo kwa Mark na ikabidi aendelee kuzungumza na Zomboko hivyo hivyo akimuhoji kwa kujitoa lawamani asionekane kama wamepanga kumkanusha mchungaji kwa kile ambacho kilishatokea.

“Mpenzi msikilazaji kama ndio unajiunga nasi, hizi ni habari za Kitaa na kwasasa tuko uwanja wa fisi tunazungumza na Zombi Zomboko kuhusu yule kijana aliyelaanika kwa wizi Kanisani, Izani Nteze….! Enhee Zomboko umesema huamini kama Izani aliiba, ina maana hata maneno ya mchungaji Ndimbo huyaamini?” Mark akauliza huku moyo ukimwenda kasi kwa shauku ya kusikia jibu la Zomboko.

“Mi namuamini Mungu na hisia zangu tu. Ingekuwa simjui Izani labda ningesadiki. Ila nakuhakikishia mtangazaji zunguka mitaa yetu uliza kwa anayemjua vyema Izani kama atasema anaamini eti kaiba.” Zomboko akazidi kuzungumza maneno yaliyomshangaza Mark.

“Na je unazungumziaje laana iliyompata mpaka awehuke na kutumia madawa ambayo awali alisimama kuyapinga?” Mark akabadili mlolongo wa maswali.

“Kuhusu kilichotokea naona kama kuna mambo yanaendelea chini ya kapeti ambayo sisi hatuyajui. Kwa maana hatujui wapi alikuwa zaidi tumestukia tayari amekuwa teja tena asiye na akili kana kwamba katumia madawa kwa miaka ishirini. Sidhani kama Mungu ndiye kamlaani.” Zomboko akajibu na kumfanya Mark amshangae kwa mashaka yake.

“Kwa hiyo umejifunza nini mjomba Zomboko.”

“Nimejifunza kuwa dunia ina siri nyingi na si kila nikisikiacho na kukiona nikipokee kama kilivyo. Hebu jiulize kwanini Izani apotee na aonekane kisha apotee tena? Kwanini Mungu asingekuja kumdhalilisha huku alipokuwa anapigania vita ili sote tumcheke? Kwani chizi ana aibu? Mi nimejifunza kuwa makini tu na maneno ya watu haijalishi wapoje.”

“Ina maana mjomba Zomboko….” Mark akataka kusema kitu lakini hakujua akiwasilishe vipi. Akajikuta anamezea ndani na kunyanyuka kwenye sofa.

“Sawa…! Huo ni Mtazamo wa Zomboko kuhusu Izani nadhani mmemsikia. Nakurudisha Studio kwa matangazo na tukirejea tutazungumza na mwenyeji mwengine wa Uwanja wa Fisi atuambie amejifunza nini kwa kile kilichompata Izani Nteze. Nakusihi ubaki nasi.” Mark akasema na kuyarudisha matangazo studio.

Akamtazama Zomboko na Kine aliyekaa kitini ametabasamu akifurahishwa na vile baba yake alivyozungumza kwa ujasiri.
“Kwa maneno yako unaonesha unaunga mkono kuwa Izani si mwizi, Fikiria tena mjomba kumbuka hata Mchungaji Ndimbo alimuamini sana Izani lakini mwisho wa siku mwenyewe kathibitisha kwa uchungu na kazi ya Mungu tumeiona. Mi naenda!” Mark akaaga.

“Huyo mchungaji mimi hanichungi. Sasa kama wewe imani yako inachungwa na Ndimbo Masizi basi kichwa chako kitakuwa hakina jambo jipya. Izani angekuwa mtumiaji wa madawa angeanzia hapa. Na kilichompata siamini kama kimetokana na ndoto ya mchungaji wenu. We nenda ila siku nyengine ukija usije na majibu yako kichwani ili utuhoji tujibu utakavyo. Ebo!” Zomboko akazungumza kwa jazba kiasi wakati Mark akitoka.

* *

Baada ya kutoka Uwanja wa Fisi, Chikala akaelekea moja kwa moja Kinondoni kwenye mgahawa wake uliosimamiwa na Kisa Kabeby. Aliposhuka na kuingia mgahawani alistushwa na kile alichokuwa anakisikia redioni kupitia spika zilizofungwa kwenye kona mbili za mgahawa.

“Kisa hebu ongeza kidogo sauti.” Chika akazungumza wakati akikaa. Kisa naye akampa kazi ile muhudumu mwengine kisha yeye akajiunga mezani na Chikala.

“Mbona mapema leo, enhee nambie!” Kisa akasema lakini Chikala akabaki kimya masikio yake akiwa ameyatega redioni kusikiliza mahojiano yaliyokuwa yanaendelea. Kisa akajikuta anashusha pumzi na kunyamaza. Ikamlazimu naye asikilize kile ambacho bosi wake kimemgandisha hata asiseme naye.

Kilikuwa ni kipindi cha Habari za Kitaa na kwa muda huo Zomboko ndiye alikuwa anazungumza. Chikala akajikuta anaachia sonyo la sauti akichukizwa na maneno ya Zombi Zomboko.

Mara Chikala akasimama na kuanza kuondoka kabla kipindi kwisha, na bila kuzungumza chochote kwa Kisa aliyekuwa amemuongelesha muda mfupi.

“Vipi bosi Chika! Uko sawa?” Kisa akauliza.

“Kuna kitu muhimu nimesahau. Nitakucheki baadae.” Chikala akajibu na kutoka. Akaingia kwenye gari na kuiwasha kabla hajageuza akafungulia redio na kuweka kituo kile kilichokuwa kinarusha kipindi cha habari za kItaa.

Kisha akaondoa gari na kufata mwelekeo wa njia ya kurejea alipotoka muda mfupi. Akili zake zikamtuma arudi tena Tandale kule kwa Zomboko aidha kukutana na huyo mtangazaji au Zomboko mwenyewe ambaye hisia zake zilitishia uhai wa siri ya yale aliyomfanyia Izani.

Lakini akiwa njiani kwa mawazo akajikuta ananyoosha mpaka Magomeni mataa na kuacha kuikunja njia ya Tandale. Hapo akajikuta katikati ya foleni kubwa iliyomchelewesha mpaka kipindi kikaisha akiwa hajafika. Ndipo akabadili mbinu katika mawazo yake yaleyale.

“Anhaa! Huyu bwege si ana binti yake pale Grocery Manzese. Acha nianzie hapo kwanza nimuingize binti yake kwenye himaya yangu.” Chikala akazungumza kwa sauti ndani ya gari akiwa bado kwenye foleni.

Alijikuta anaganda hapo kwa zaidi ya lisaa na kuichukia siku hiyo kutokana na foleni ambayo ilisababishwa na msafara wa kiongozi wa nchi. Mpaka gari zinaruhusiwa tayari kigiza kilishabisha hodi kwenye anga la jiji lakini hakuivunja safari yake, akaongoza barabara mpaka Manzese mbele ya grocery ya Zomboko ambayo ilisimamiwa na Mkewe pamoja na binti yake aitwaye Zinduna.

Akaegesha gari na kushuka akaongoza mpaka sehemu vilipopangwa viti kwaajili ya wateja.

“Karibu.” Zinduna akazungumza baada ya kusogea alipoketi Chikala.

“Niletee Pepsi baridi nawe chukua kinywaji utakacho.” Akasema Chikala huku akitoa noti ya shilingi elfu kumi akamkabidhi Zinduna.

Baada ya dakika Zinduna akarejea na kumfungulia soda aliyoagizwa, huku yeye akiwa amechukua bia.

“Usijali keep change mrembo. Pia kama hutojali naomba uketi hapa tuzungumze.” Chikala akasema punde Zinduna alipotaka kumpa chenji yake. Zinduna naye hakujivunga, akaweka pesa kwenye mfuko wake wa suruali aliyovaa na kuvuta kiti akaketi pamoja na mteja wake asiyemfahamu.

ITAENDELEA.........
 
SYAGA JAMES
09

______***_______

| NAIROBI |



Mchungaji Ndimbo Masizi akiwa nyuma ya Lululu wakatembea hadi pale kwenye mti na kuvaa nguo zake kabla hajamuaga Lululu na kushika njia mpaka kwenye maegesho ya Taxi.

“Nipeleke hotelini Fairview.” Akamuelekeza dereva mara baada ya kuingia kwenye taxi. Safari ya kutoka Mashimoni kwenda hotelini ikachukua mwendo wa dakika zisizozidi kumi wakipita barabara ya Ngong.

FAIRVIEW HOTEL Ndipo alipokuwa anapenda kufikia Mchungaji Ndimbo kila awapo Nairobi. Baada ya kufika hotelini akamlipa mwenye taxi kabla hajashuka na kuingia mapokezi mwa hoteli hiyo ya gharama ambayo kulala tu kwa siku moja ni shilingi laki tatu na ushee.

Akapokewa kwa heshima na kuandikisha chumba. Lakini alipomaliza kujaza taarifa zake na kukabidhiwa funguo, mara Mchungaji Ndimbo akashangaa kusikia anaitwa kwa jina na mtu asiyemfahamu akamkimbilia aliposimama.

“Baba Mchungaji… Mtume Ndimbo Masizi…Bwana Yesu asifiwe”

“Milele Amina!” Ndimbo akaitika huku akimtazama mwanamke aliyesimama mbele yake akiwa mwingi wa furaha.

“Siamini kwakweli bwana amenitendea muujiza. Naomba nibariki mimi ni Mfuasi wa kanisa lako, huwa nasali na familia yangu kwa njia ya TV kila jumapili. Imekuwa bahati leo nimekuona mchungaji nibariki.” Akasema yule mama huku akipiga goti mbele ya Ndimbo Masizi.

“Pokea baraka. Umebarikiwa.” Ndimbo akazungumza huku akimsihi yule mama kunyanyuka. Akamuacha na kuongozana na muhudumu mpaka ghorofa ya pili kwenye chumba namba 106.

Akaingia ndani na kufunga mlango kabla hajajitupa kitandani na mawazo tele kumteka kichwani. Akawazia sana hatima yake kwa kuukumbuka mwanzo wake. Akajikuta anamkumbuka binti yake wa kwanza ambaye tangia mtoto alimsifu kuwa amepata mtoto mwema na aliahidi kumlinda. Lakini leo ndiye kasababisha kifo chake na sasa nafsi ya bintiye imeanza kuwa hatari ya mafanikio yake ambayo yalianza baada ya kuzaliwa kwake Anita. Mawazo yakamfunulia vyema kurasa za kumbukumbu tokea ile siku Anita anazaliwa, kabla Ndimbo Masizi hajawa Mchungaji wala hajatajirika kwa kivuli cha Kanisa.

***

1998 | DSM

Ilikuwa siku ya Ijumaa alfajiri ya tarehe thelathini na moja mwezi wa saba, Ndimbo Masizi akaamshwa na mwito wa simu yake iliyokuwa pembeni ya kitanda alipolala. Simu hiyo ndiyo ilimjuza kuwa mkewe amejifungua mtoto wa kike muda mfupi.

“Ooooh! Asante Yehova kwa zawadi hii ya faraja uliyotupatia ee bwana. Nami nitatimiza ahadi yangu kama nilivyokuomba utubariki mtoto awe chachu na faraja ya maisha yetu ya mafanikio. Naamini kwakuwa umetenda vile nilivyotaka na iwe utakavyo. Nasema asante baba naomba umfanye binti huyu awe wa kipekee kwenye mamlaka yako nami naahidi kumlinda katika maisha yangu yote nitamtunza.”

Ndipo akasimama akiwa mwingi wa furaha akazungumza na kumtukuza Mungu. Aliendelea kusema zaidi moyoni mwake mpaka anafika Mwananyamala hospitali ambapo jana yake mkewe alimfikisha baada ya kuanza kusikia uchungu wa uzazi.

Mwaka huo 1998, Ndimbo na mkewe walikuwa wanaishi Makumbusho kwenye nyumba ya kupanga ambayo ilimilikiwa na Mchungaji wa Kanisa walilokuwa wanasali.

Kanisani Ndimbo alikuwa msomaji mzuri wa biblia pindi Mchungaji alipozungumza alimchagua asome kwa niaba ya wengine kifungu cha andiko alilosimamia kwenye mahubiri. Ndimbo alikuwa mwepesi kuelewa na alikariri vifungu vingi vya biblia kuliko kitabu chochote.

Baada ya mkewe kuruhusiwa wakarejea nyumbani kwao na mgeni wao aliyewafungulia dimba la uzazi.

ANITA….! Ndiyo jina walilompatia, ikiwa na maana sawa na BAHATI.

Kuzaliwa kwa Anita kukachochea juhudi na tamaa ya kufanikiwa kwa Ndimbo na familia yake ili nao waishi kifahari. Wakajitahidi kutunza wanachokipata na kuongeza juhudi ya kutafuta kipato kwa kazi za kuunga unga ambazo Ndimbo alifanikiwa kuzipata.

Lakini kabla hawajatimiza lengo, miaka miwili mbele ugonjwa wa ajabu ukampata Anita. Kuugua kwa mtoto kukamaliza akiba zote za fedha walizokuwa wanatunza. Pesa zilipokwisha na mtoto akapona. Hali ya maisha ikazidi kuwa tete ingawa Ndimbo alijitahidi kusimama kidete kuhakikisha familia yake inakuwa salama.

Siku moja aliamua kumtembelea rafiki yake ambaye alikuwa na uwezo kiasi, shida za milioni mbili tatu hazikumsumbua.

“Unajua mimi ningejua biblia kama wewe ningeanzisha kanisa langu nianze kupiga pesa.” Prospa, rafiki wa Ndimbo akasema mara baada ya Ndimbo kuzungumza shida yake ya kumkopesha kiasi fulani cha pesa ili akizungushe kwenye biashara zake.

“Kwani kufungua Kanisa ni biashara?” Ndimbo akamuuliza Prospa.

“Ni zaidi ya biashara kwa mjanja! Ila hailipi kama utajifanya mtu wa Mungu kweli. Ila kama utaamua kutumia kama kazi…. Unaweza kuwa maarufu na tajiri kupitia sadaka za waumini wa Kanisa na michango mbalimbali inayotoka kwenye taasisi. Ha ha ha Anzisha Kanisa mzee huo ndio mchongo.” Prospa akazungumza huku akicheka kama mzaha lakini alimaanisha. Ndimbo akabaki kinywa wazi siku hiyo hakukubaliana na Prospa pia akakosa mkopo alioutaka baada ya kukumbushiwa deni ambalo alishakopa siku za nyuma akawa hajalipa.

Lakini miezi michache mbele mambo yakazidi kuwa magumu baada ya Mchungaji wa kanisa lao kufariki. Nyumba ya Makumbuho waliyokuwa wanaishi hatimaye ikauzwa na watoto wa marehemu mchungaji huyo.

Nyumba ilipouzwa hawakuwa na jinsi zaidi ya kuomba hifadhi kwenye stoo ya kanisa walipokuwa wanasali kutokana na kukosa fedha ya kukimu kodi.

Maisha yakauumiza moyo wa Ndimbo kipindi mkewe akitumika kama mfanya usafi mkuu wa kanisa naye akitumika kama mlinzi wa kanisa. Wakati huo Anita akiwa na miaka miwili Ndimbo akaukumbuka ushauri wa Prospa.

Maisha ya kumtumaini Mungu na kuendelea kuwa fukara yalimuuma mno moyoni mwake na kumtia uchungu Ndimbo, ingawa machoni alipomtazama binti yake aliipata faraja na nguvu ya kupambana upya iliamka.

Ndipo nyakati hizo akakumbuka maneno ya Prospa na kujitafakari upya uwezo aliokuwa nao kibiblia na kuzungumza kwake kwanini asijitumie kufanya mageuzi ndani ya kanisa lile alilozoeleka kabla hajafungua la kwake?

Akajiuliza swali likafunguka kichwani mwake kwa mlango wa jibu.

Shida zikamfanya atamani kuvuna pesa za sadaka kanisani. Na kila alivyomsikiliza Mchungaji mpya hakuona kinachomshinda na yeye kuwa Mchungaji.

Siku hiyo akakutana tena na Prospa, safari hii wakazungumzia namna gani Ndimbo anaweza kufanya awe mchungaji tajiri.

“Mbona rahisi hiyo.” Prospa akasema bila wasi.

“Urahisi wake unakujaje Papii, nielekeze basi..” Ndimbo akataka kujua.

“Siku ya ibada nyoosha mkono kwenye kutoa ushuhuda ukipewa nafasi usiseme kama walivyozoea kusikia. Tumia dakika hizo kuwapigisha bonge la stori la uongo ambalo litawashika na kuamini usemacho.”

“Mh…! Pipii..sasa stori gani unadhani?”

“Aaah Ndimbo we si unavijua vifungu kibao vya biblia…! Au Waambie tu Yesu kakutokea na ametaka uanze kumtumikia kwa kuwachunga kondoo wake. Halafu unaanza kushusha nondo zako… Mbona wataelewa tu! Ukifanikiwa hilo nakuahidi kuwa pamoja nawe mpaka ujenge kanisa lako tuanze kutengeneza pesa. Hapa mjini ishi kwa akili Ndimbo usiwe mjinga ushakuwa baba sasa.” Prospa akazungumza na kumjaza sumu, Ndimbo akalewa na kukubaliana naye.

Ndipo siku moja aliomba kuzungumza mbele ya kanisa mara baada ya Mchungaji mpya kutaka yeyote aliyekuwa na shuhuda mbele ya Kanisa azungumze.

Ndimbo Masizi akasimama na kupiga hatua mpaka mbele ya kanisa. Akapewa kinasa sauti na kuzungumza kama walivyojadiliana na Prospa akitumia uongo ule ule wa kutokewa na Yesu.

“Kanisa…! Kwa mara ya kwanza nina shuhuda na taarifa ya kuwambia kuwa bwana amenitokea wiki hii zaidi ya mara mbili na kusema nami akinitaka niwe Mchungaji mbele ya kondoo. Amenipa kibali cha kuwarudisha zizini kondoo waliopotea. Na huu ndio ukweli wangu kwenu. Kwa yule atayeng’ong’a kwa mashaka namkumbusha katika Kristo kuwa hupaswi kuwa na mashaka. Kwani umesahau hata Mtume Paulo kipindi akiwa bado Sauli bwana alimtokea njiani alipokuwa anaenda Damaski! Je, kama bwana alikuwa tayari kumtumia Sauli aliyekuwa mwovu vipi ashindwe kunitokea na kutaka kunitumia mimi nyakati hii? Hakika maneno haya ni baraka nami najisikia vyema leo kuyatamka hadharani na tokea sasa nitasimama kufanya kazi ya baba kama alivyonitaka…! Halleluyaaa.”

Shuhuda yake ilisababisha kanisa libaki kimya kumtafakari. Kila aliyemsikia Ndimbo akajikuta anapambana na hisia zake zilizomlazimisha kumkanusha. Lakini maneno yake hayo wengine yakawalegeza, wakamuamini kweli na hilo likamuhakikishia kuwa anaweza kuwa mchungaji mwenye wafuasi wengi.

Alianza kama mchezo baada ya kuitwa kwenye uongozi wa kanisa kulizungumza kwa kina hilo alisemalo. Huko nako akasimamia uongo wake uleule. Uongo uliowalegeza wazee wa kanisa ukizingatia walimfahamu tangia siku za nyuma alivyokuwa anamsomea biblia mchungaji aliyefariki. Hilo likawaaminisha huenda kweli bwana Ndimbo Masizi ametokewa na Yesu na na sasa ana upako wa kulisema neno la Mungu.

“Kuanzia sasa inabidi uanze kuhudhuria vikao vya kiutumishi na kanuni za Kanisa ili siku zengine uongoze ibada wewe.” Kiongozi mzee wa Kanisa akasema na Ndimbo akafurahi sana. Hiyo ilikuwa mwaka 2000.

* *

- 2002 -

Miaka miwili mbele ilitosha kumuwezesha Ndimbo kumpindua Mchungaji mpya na kufanikiwa kuwa mchungaji mkuu kwenye Kanisa alilokuwa anasali. Kipindi hiko Neema akiwa na miaka Minne.

Watu wengi wakaanza kumuelewa vile alivyokuwa anahubiri Injili yake aliyoiita Injili ya ukombozi.

“Leo ni siku ya kubariki kipato na kuwarudisha watumwa kwenye ufalme wao. Bwana amesema nami kwa yeyote atayetoa nusu ya kipato chake cha mwezi kwa siku moja. Basi naye atakibariki kipato hiko cha mwezi kiwe cha kila siku…Halleluyaaaaa…! Njoo ujazwe kipato na Yesu mahala hapa. Nakusihi sasa sogea mbele chukua bahasha yako muoneshe Mungu kama wewe ni mwaminifu naye atakuonesha uaminifu wake kwako….!”

Ndivyo Mchungaji Ndimbo alipoanza kupitisha nia yake ya kukomba pesa za waumini waliokuwa na imani ya kweli kwa kusikia maneno yake ya uongo. Na taratibu hali ya maisha yake ikaanza kuchukua sura mpya kila uchwao.

Mara nyengi aliposimama alisisitiza sana watu kutoa sadaka zilizonona ili Mungu apate kuwapa maisha yaliyonona pia.

“Sasa wewe unataka umtolee Mungu vichenji chenji ukitaraji akupe noti noti? Huoni haya…? Kanisaaaa inabidi tuambiane ukweli na ndivyo bwana anavyotaka tuwe. Huwezi kupanda mbegu kidogo ukatarajia mavuno mengi. Lazima tuwe wepesi kwenye utoaji ili Mungu atupe baraka zake. Na Mungu anawapenda sana watoaji… Haya sasa shika sadaka yako iliyonona leo nitapita mwenyewe kwa mtu mmoja mmoja ili baraka zikushukie kiwepesi zaidiii haleluyaaa…” Akazungungumza Ndimbo siku hiyo ambayo mama mmoja aliweka sarafu za shilingi mia nane kwenye kapu la sadaka kipindi cha matoleo. Jambo hilo likamfanya asitishe matoleo na alipomaliza kuzungumza akaanza kupita upya kuchangisha hata kwa wale ambao walishatoa.

Siku hiyo akakusanya pesa nyingi zaidi ya siku zote. Akaipenda mbinu hiyo na mwishowe ikawa tabia. Na mwaka huo huo Mchungaji Ndimbo Masizi akanunua gari yake ya kwanza ya kutembelea kabla hakujazuka ugomvi mkubwa kati yake na wazee ya Kanisa siku ya kikao cha maendeleo ya Kanisa mwisho wa mwaka.

“Mtumishi, tumepata malalamiko kwa muhasibu kuwa unamlazimisha mara kwa mara kutoa pesa kwenye akaunti ya Kanisa kwa matumizi yako binafsi……”

“Simlazimishi ila namtaarifu.” Nimbo akamkatiza mzee wa kanisa mwenye heshima kubwa ambaye ndiye aliwezesha kumpa nafasi ya utumishi.

“Sasa kwanini Mchungaji unafanya hivyo bila kututaarifu? Inakuwaje matumizi yako yawe makubwa kuliko ya Kanisa?” Mzee mwengine akaongea na kumlaumu Ndimbo aliyebaki anawatazama kwa hasira.

“Kwani niwaulize wazee. Kabla yangu kusimamia suala la sadaka, mliweza kukusanya walau milioni kwa jumapili moja?” Ndimbo akauliza swali lililowaudhi wazee na kumkemea.

“Bila shaka mtumishi una pepo haiwezekani leo hii uwe unazungumza nasi hivyo.” Muhasibu ambaye alikuwa mke wa mzee mkuu wa Kanisa akazungumza na hapo ndipo Ndimbo akasimama akiwa mwenye hasira.

“Sasa kuanzia muda huu, nitawaacha na kanisa lenu kwa maana si nyinyi mlionipa upako wa kulijua neno ila Mungu amenichagua. Na wewe malaya ukome siku nyengine kunambia nina pepo.”

“MALAYA?” Wazee wote wakahamaki. Zogo likaibuka katika kikao kila mtu akamlaani Ndimbo hata alipotoka akiwa kafura hasia akaingia kwenye gari yake na kuondoka. Na hiyo ikawa mara yake ya mwisho kujumuika kwenye kanisa hilo na ukawa mwanzo wa kufungua kanisa lake akianza kwa kukodi ukumbi mitaa ya urafiki.

Rafiki yake Prospa akamfanya kuwa mzee wa Kanisa na mkewe akawa muhasibu. Lakini mambo yakawa mazito kwake kupata waumini mbali ya kulipia matangazo redioni na kubandika mabango barabarani.

“Twende Sumbawanga tukasafishe nyota Ndimbo, mambo haya hayaendi hivi hivi lazima itakuwa wale wazee wamekufunga tu.” Prospa akamshauri siku moja walipokuwa wenyewe wakizungumza. Ndimbo akafikiri na kusema.

“Lakini mke wangu ujue ana imani ya kweli na hataki kabisa kusikia habari za waganga.”

“Hilo sio tatizo Ndimbo. Tunaweza kuanya yetu na mkeo asijue. Tumia jina la vikao vya kanisa au safari ya kiutumishi. We mdanganye tufanye yetu tusije kuchekwa mzee.” Prospa akazidi kumtia ushawishi Ndimbo ambaye hakuwa na pingamizi zaidi ya kufata ushauri huo. Na huo ukawa mwanzo wake wa kuanza kwenda kwa waganga kutumia dawa za kuwavuta watu kimazingara. Na huo ukawa mwanzo mwengine wa kujaza kanisa lake na kuzidi kufurahia maisha na familia yake ambayo haikujua nyayo zake nyuma ya pazia.



* *

-2006 -

Miaka minne mbele, wakati huo Anita akiwa na miaka nane akisoma darasa la tatu. Maisha ya Ndimbo yakazidi kupanda hadhi na umaarufu wa kanisa lake ukazidi kuongezeka. Sasa hakuwa amepanga ukumbi kama awali. Ila alijenga kabisa Kanisa lake lilioitwa, Kanisa la Ukombozi.

Na mwaka huo ndipo akazidi kuzisoma akili za binti yake na kuugundua moyo wa dhahabu aliokuwa nao Anita. Moyo wa kusaidia wengine japo alikuwa mtoto lakini aliliona kwenye michezo yake na watoto wenzake iwe shule, kanisani, hata nyumbani. Anita alimpenda sana baba yake na kumwelezea shida mbali mbali za rafiki zake na alifurahi punde baba yake alipotatua shida hizo.

“Baba…baba…waone waleee” Siku moja Anita alimwonesha baba yake watoto wenzake ambao walisimama barabarani wakiomba msaada. Walipolifikia gari yao Anita aliwahurumia vile walivyo walionesha wenye shida.

“Wape pesa baba.” Anita akasema na kumfanya Ndimbo atabasamu akiwa kwenye usukani akashusha kioo na kuwapa noti ya shilingi elfu kumi.

“Wape nyengine baba.” Anita kazungumza tena. Ndimbo akamtazama binti yake na kucheka kabla hajawapa noti nyengine ya thamani ileile.

“Tena baba…” Anita akakazania, Ndimbo akamshangaa bintiye lakini hakutaka kumpinga. Akawageukia wale watoto waliokuwa watatu na kuwapa Elfu kumi nyengine ikiwa jumla ya shilingi elfu thelathini. Kisha akamtazama Anita akamuona amefurahi. Taa zilipowaruhusu Ndimbo akaendeesha gari na kumfikiria binti yake kwa kupenda haki na usawa baada ya kugundua maana yake kuwa alitaka kila mtoto ampe pesa yake na si kuwapa moja wakagawane. Akafurahia na uwezo wa hesabu aliokuwa nao binti yake. Mapenzi baina yao yakazidi ongezeka.

* *

- 2008 -

Miaka miwili tena Ndimbo akawa Masizi kweli kweli. Hiyo ni baada ya miaka kumi ya kuzaliwa Anita. Mtandao wa Mchungaji Masizi ukawa mkubwa na kanisa lake likaanza kuwa gumzo. Wakati huo alikuwa tayari amejenga nyumba ya kifahari Mikocheni.

Yote hayo alifanikisha baada ya kukutana na mtaalamu wake kutoka Nairobi ambaye aliunganishwa na mchungaji mwenzake mpigaji kama yeye aliyekuwa na mahusiano ya karibu na Prospa.

Mwaka huo pia ukawa wa huzuni kwa upande mwengine baada ya Prospa kufariki ghafla, lakini pia ukawa wa Neema baada ya mkewe Ndimbo kujifungua mtoto wa kiume ambaye Ndimbo akampa jina la PAPII ambalo alipenda kumwita Prospa enzi za uhai wake.

Mwaka huo pia ndio alijuana na Chikala Gumbo na kumpa kazi zake za siri kabla hajaamua kumuweka jirani kama dereva wake baada ya kuuona umuhimu na uhodari wa Chikala kwenye kazi zake.

Mbali na kanisa, Mchungaji Ndimbo alikuwa mwingizaji mzuri wa dawa za kulevya nchini. Kivuli cha Kanisa alikitumia vyema kujificha. Biashara zake za madawa ya kulevya ndizo zilizomzidishia kipato na jeuri ya kuhubiri kwa kujiamini hata akafanikisha kufungua kituo chake cha luninga na redio.



* *

- 2016 -

Miaka 18 toka kuzaliwa Anita ilitosha kubadilisha kabisa historia ya Ndimbo kutoka kwenye ufukara mpaka ubilionea. Sasa akawa na miradi mingi mikubwa ya siri na dhahili. Kanisa lake likawa maarufu huenda kuliko makanisa yote Tanzania. Nani hakumjua,…! Nani mwenye shida ambaye hakufika kufanyiwa muujiza na Yesu wa Ndimbo. Jiji zima kila ifikapo jumapili ibada yake ilifatiliwa na wengi kupitia luninga na wengine kwenye redio.

Mwaka huo binti yake alikuwa anatimiza miaka ya kuuacha utoto na kuingia ukubwani. Kwa furaha, mapenzi na jeuri ya pesa Mchungaji Ndimbo siku hiyo alimtunza binti yake zawadi ya gari New Marcedise Benzi baada ya kutimiza vigezo vya kumiliki leseni.

Mbali na hilo aliweka gumzo kubwa kwa kuwakutanisha mahasimu watatu wa muziki wa Bongo Fleva, Diamond, Alikiba na Hamornize kwenye jukwaa moja ili kumpongeza na kuwaburudisha wote waliohudhuria sherehe hiyo iliyofanyika ndani ya ukumbi wa KILIMANJARO HOTEL (KEMPISKI).

Waliohudhuria tukio hilo kila mmoja aliondoka ametabasamu baada ya kuwashuhudia mahasimu hao wakubwa wakiimba pamoja wimbo maarufu wa kumpongeza mtu anapoadhimisha kumbukumbu ya kuzaliwa.\

Hiyo ikazidisha heshima na imani kwa wattu kuwa upako aliobarikiwa Ndimbo na Mungu ulikuwa wa daraja la juu sana. Lakini nyuma ya pazia Ndimbo alitambua vyema siri ya mafanikio yake ya kushangaza.

“Shika hivi vijiti vinaitwa Mtwanatumwa….! Yeyote utayemtaka ukimwita ataitika na taarifa zako hatozipinga. Tafuna kizizi kimoja kabla hujazungumza naye, nuia unavyotaka kisha litaje jina lake mara tatu kwa kumwita kabla hujazungumza naye iwe kwa simu au vyovyote.”

Maneno hayo aliambiwa na mchawi Dokta Zongo huku akikabidhiwa vizizi vya mti asioufahamu. Na hiko ndicho kilichochea kufanikiwa kuwaweka mafahari watatu kwenye zizi moja. Haikuwa nia yao ila nguvu za shinikizo la kichawi wakajikuta wote watatu wanatii na kuwa wapole mbele yake. Na mwaka huo ndio akajinadi kuwa ni mtume.

Mapenzi aliyokuwa anayaonesha kwa bintiye hayakuwahi kumfikirisha kama siku moja anaweza kumkatisha maisha binti yake. Lakini mwishoni mwa mwaka huo ndipo akapata taarifa za kijana Izani Nteze na kampeni yake ya kuhamasisha watu wa mitaani kutotumia madawa kwa kuwapa elimu huria ambayo hakujua amejifunzia wapi.

“Nataka mdomo wa huyo Izani uwe kinyume na kusudi la maneno yake.” Alitoa agizo siku moja alipokuwa anazungumza na Chikala.

“Tumuue?” Chikala akauliza.

“Hapana, nataka tumuweke jirani tukitumie kile alicho nacho. Akikaidi hapo ndio apotezwe. Kuanzia sasa tega rada zako afatiliwe kila hatua na panapowezekana arekodiwe na uniletee video zake.” Ndimbo akaitangaza nia yake ovu kwa Izani.

“Sawa bosi.” Chika akajibu kwa utii.

Izani akawa anafatiliwa nyendo zote bila kujijua. Hiyo ilikuwa kabla hata Anita hajamtambulisha baba yake taarifa za Izani ambazo zilianza kuwa gumzo mtandaoni. Mchungaji Ndimbo Masizi alikuwa anaelewa mengi kuhusu kijana huyo kuliko Anita alivyojua, na hakuwahi kufikiria kama siku moja tamaa yake itamfikisha kwenye hatua ya kumtoa kafara binti yake ili azidi kulinda heshima yake.

ITAENDELA......
 
MFUASI
10

Baada ya Chox kufanikisha kumpata Izani na kumfikisha kwenye kambi yake ya maficho akamfungia kwenye chumba maalum na kumuacha huko akisubiri amri ya bosi wake cha kumfanya.

Muda huo ikiwa ni usiku wa manane Chox alikuwa anaburudika na wanawake kwenye himaya yake akiwa hana wasiwasi wowote. Izani Nteze akiwa amefungiwa kule chumbani ndipo hali ambayo haikuwa ya kawaida ikamtokea.

Akaanza kutapika sana. Izani akatapika na kutapikiana mpaka akazimia bila Chox kumsikia wala kujua. Akabaki hivyo mpaka alfajiri ambapo Chox akawalipa wanawake aliokuwa anaburudika nao chumbhani kwake na kuwaruhusu waende huku yeye akijiandaa kupasha moto misuli. Lakini kabla ya kufanya hivyo akili ikamtuma akamchungulie Izani kule alipomfungia. Ndipo akaduwaa kumkuta Izani akiwa amelala chali katika ya matapishi huku mapovu yakianza kumtoka puani. Chox macho yakamtoka kwa mshtuko akamsogelea kuhakikisha kama bado anahema au tayari amefariki. Wasiwasi ukamvamia Chox huku picha ya bosi wake Chikala Gumbo ikimjia kichwani.
 
MFUASI
11

Ndimbo Masizi akawasili uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere, saa nne asubuhi. Tayari alishampigia Chikala ambaye muda huo alikuwa amefika kumpokea.

“Kila kitu kipo sawa?” Ndimbo akauliza.

“Kama ilivyopaswa kuwa bosi.” Chikala akajibu wakati huo walikuwa wanaingia kwenye gari aliyokuja nayo. Wakaingia na kuondoka taratibu eneo la uwanja wa ndege huku mazungumzo ya hapa na pale yakichukua hatua.

“Nafikiria sasa hatumuhitaji tena Izani….” Ndimbo akazungumza na kumeza mate huku akifikiri zaidi.

“...wala sidhani kama ni salama tena kuendelea kumwacha hai.” Akaweka tuo huku akimtazama Chikala aliyekuwa amemakinika na barabara wakati huo.

“Kesho napaswa kurudi tena Kenya nawe hakikisha kesho Izani anapotea kwenye macho ya ulimwengu huu na maiti yake ipotezwe kabisa usijulikane hata mfupa wake.” Ndimbo akaongea zaidi mpaka Chikala akashangaa.

“Sawa bosi.” Chikala akaitika bila kuongeza neno.

Safari ikagotea Mikocheni kwa mchungaji Ndimbo ambapo baada ya gari kuingia ndani ya geti na kushuka akalakiwa na watoto wake waliokuwa wameketi kwenye bustani wakisoma vitabu.

“Waoooo Dadiiii! we miss you..” Wakamkimbilia na kumkumbatia baba yao kwa upendo mkubwa.

Faraja ikanyanyuka moyoni mwa Ndimbo mbali ya ukweli kimawazo alikuwa mbali.

“Hamjambo watoto wangu wazuri.”

“Hatujambo baba… shikamoo”

“Marahabaa! .”

“Baba….” Doris akaita huku akimtingisha Ndimbo wakati wakiingia ndani.

“si tutaenda wote beach?” akauliza swali ambalo na Papii naye akaliunga mkono.

“Hatutamwacha baba tutaenda naye pia..”

“Kwani kuna safari ya beach?” Ndimbo akauliza.

“Wameng’ang’ana toka jana ulivyoondoka, sasa vyema umerudi mapema mwende baadae.” Sauti ya mkewe ndiyo ikamfanya Ndimbo akumbuke kutazama kwenye makochi ya sebuleni ambapo alimuona ameketi akiwa na ile picha ya mchoro wa Anita mapajani mwake.

Ndimbo akababaika machoni mwake na kushusha pumzi ndefu isiyoelewka kama ya uchovu wa safari ama shangazo la kuion tena ile picha ya Anita aliyomwamuru mkewe aifiche ndani.

Ndipo akashusha pumzi na kuwageukia watoto wake.

“Nendeni kamwambie Anko Chika atawapeleka.” Ndimbo akasema lakini watoto hawakukubali.

“No Dadi! Tunataka twende na wewe na mama pia.” Papii akazungumza, Doris akamwacha baba yake na kumfata mama yake pale sofani.

“Angekuwepo dada angetupeleka… si eti mama?” akamuuliza mama yake huku akiitazama ile picha ya Anita.

Kauli ya Doris ikamfanya Ndimbo aumie moyoni mwake na kumtazama mkewe kwa ghadhabu kiasi kabla hajaelekea chumbani akimwacha Papii amesimama bila kujua kama baba yake amekubali ama laa.

"Papii njoo mwanangu.” Mama mchungaji akamwita mwanaye baada ya kuona amesimama kinyonge. Wakati huo Doris akawa ameichukua yeye ile picha akimtazama dada yake huku kumbukumbu za upendo wake zikisheheni kichwani mwake. Papii naye akafika sofani na kukaa pembeni ya Doris naye akawa ameyaelekeza macho kwenye ile picha.

“Mama… kwani dada hatokuja tena?” Doris akauliza swali lililomfanya mama yake abaki kimya.

“Dada kaenda kwa Mungu na sisi tukienda tutaonana naye.” Papii akamjibu mdogo wake.

“Tukienda kwa Mungu si atatupeleka bichi etii eeh” Doris akauliza swali la kitoto lililomfanya mama yake atabasamu kwa uchungu.

“Haya basi watoto wazuri leo tutaenda wote bichi tutafurahi sawa eeeh.” mwishowe akasema kwa kuilazimisha furaha ili awafariji watoto.

“Na baba si tutaenda naye eti mama?” Doris akauliza.

“Ndio, haya naomba hiyo picha nikaiweke ndani.” akawaitika na kuichukua ile picha ya mchoro wa Anita.

Upande wa chumbani mchungaji Ndimbo alipoingia akajibweteka kitandani huku kichwa kikimgonga kwa mkanganyiko wa mambo. Siku hii ilikuwa ya tofauti zaidi kwa mkewe vile alivyomsoma.

Sikumbuki mara ya mwisho lini mama Anita amewahi kunitazama bila kunipokea nitokapo safari!

Moyo wake ukasema

Na kwanini anaing’ang’ania ile picha kuwaonesha watoto na nilishamwambia aifiche?

Akajiuliza zaidi, wakati huo ndipo mkewe akafungua mlango na kuingia. Akaelekea moja kwa moja kabatini na kufungua droo ya chini akaiweka ile picha kabla ya kumsogelea mumewe aliyebaki akimtazama kwa ghadhabu zilizoanza upya baada ya kuingia.

“Kwanini huzingatii nikwambiacho mama Papii?”

“Kipi tena mume wangu?”

“Picha!”

“Picha..? imefanyaje….aanha! Nilikuwa naifuta vumbi tu ndio nawe ukawa umeingia na kunikuta nayo pale, ila sijapanga kuirudisha ukutani.” mkewe akajibu huku akichukua mkoba aliotoka nao safari mumewe na kuutundika kwenye eneo maalum wanapoweka mikoba yao.

“Lakini si umesikia maneno yao? Kuanzia leo sitaki kabisa uzungumze na watoto chochote kuhusu dada yao. Mwacheni apumzike kwa amani binti yangu.” Ndimbo akazungumza kwa ukali akishindwa kuzuia hasira zilizoanza kumjaa kifuani. Mkewe akamshangaa!
“Eeh bwana Yesu simama katikati yetu shetani ashindwe. Mume wangu mbona sioni sababu ya kunifokea?” mama Anita akasema wakati huo Ndimbo akabaki kujikuna kichwa akijilamu kwa kumkaripia mkewe kiasi kile. Moyoni akajionya kuonesha makucha mbele ya familia yake.

“Mama Papii! Inabidi tujifunze sasa kuishi bila Anita. Kumbukumbu zake zinaniumiza sana natamani kila kilichomuhusu nisikione ili moyo wangu utuame kwa huzuni. Bwana msaidie mtumishi wako.” Ndimbo akazungumza kwa sauti ya chini na kujikuta machozi yakianza kumtoka. Mkewe akamhurumia na kumfariji kwa kumfuta.

“Bwana wa majeshi yuko nasi nina imani binti yetu yuko salama.” Mama Anita akazungumza huku naye machozi yakitabaruku usoni mwake.

Wote wakajikuta katikati ya huzuni. Ila huzuni mbili tofauti. Siri ya Ndimbo kutoa machozi na kumuomba Mungu amsaidie mtumishi wake, moyoni alimuwazia Dokta Zongo apate kufanikiwa kuifunga nafsi ya Anita ambayo ametabiriwa inaweza umsababishia aumbuke.

Baada ya utulivu kupita, ndipo mkewe akamuomba jambo ambalo Ndimbo lilimpasua moyo na wasiwasi kumchoma.



______***_______

| MOROGORO |

Hofu na mashaka yakawa kwa Chox kila alipomtazama Izani pale chini. Akabaki anajishauri iwapo kama kafariki ataelewekaje kwa Chikala ambaye amempa agizo la kumchunga.

Akamsogeza pale kwenye matapishi na kuhakiki mapigo ya moyo.

Kimya! Akashtuka na kutoka nje ya kile chumba huku harufu kali ya matapishi na mikojo yakikarahisha pua zake.

Akaamua kutoka na kufunga kile chumba akijitafakari nini afanye.

Akakumbuka alishaonywa asithubutu kumpeleka Izani hospitali hata amuone anaumwa vipi. Onyo hilo ndilo lilimfanya asiuone umuhimu wa Izani, lakini kauli ya Chikala mara zote alimsisitiza Choz kuwa Izani ni wa muhimu kuliko anavyochukulia. Na iwapo ikitokea amekufa basi ahakikishe anatoa sababu za msingi zitazomwingia akilini la sivyo naye takuwa nje ya uaminifu wake.

Sasa si kafa? Niwaambie nini kimemuua ikiwa sijui?

Akajiuliza

Aaah potelea pote, Kwani nimeua Kifaru au Twiga kusema nitaandamwa na Nchi! Kama nitalaumiwa nitamshangaa hata Chikala mwenyewe.

Akajisemea mwenyewe na kuhairisha kwenda hata huko mazoezini. Akatulia chumbani kwake na kunywa kiporo cha mzinga wa K Vant huku akishushia na bange.

Chox akatafakari namna ya kuzungumza na Chikala mpaka akajikuta usingizi wa asubuhi ukimpitia tena baada ya kumaliza ule mzinga. Alipokuja kustuka tayari ilikuwa saa tano kasoro asubuhi. Akarejea tena kule ndani kuhakikisha kile alichokiona awali. Akamkuta Izani amelala vilevile.

Huyu kweli kafa!

Akajihakikishia kwa kusema moyoni mwake kabla hajakifunga chumba na kurudi chumbani kwake ambao sasa akaamua kumpigia Chikala moja kwa moja.

Wakati huo Chikala alikuwa ndani ya uzio wa jumba la bosi wake akizungumza na mlinzi. Ndipo simu yake ikaita. Akaitazama na kupokea huku akisogea pembeni baada ya kujua ni Chox anampigia.

“Bosi Chika kuna jambo limetokea hapa, mtu wenu kabwaga ghafla asubuhi hii.” Chox akazungumza baada ya Chikala kupokea simu.

Alichojibiwa na Chikala kikamfanya abaki kinywa wazi.

“Oooh! Imekuwa vyema sana….! kama isingekuwa hivyo basi ilipaswa kuwa hivyo leo. Hakikisha unaenda kumtupa mbali maporini huko aliwe na wadudu.”

Chikala akazungumza kwa wepesi bila pingamizi. Chox akashangaa hajaulizwa maswali wala alivyofikiri haikuwa.

“Sawa bosi hamna shida.” akajibu na kulizwa kama kulikuwa na jipya lengine, akajibu hakuna.

“Zingatia basi hakikisha umakini wakati wa kufanikisha kumtupa usionwe.” Chikala akasisitiza kwa sauti ya chini huku naye akiwa makini asisikiwe na mtu hususani mlinzi aliyebaki ameketi nje ya kijumba chake kidogo kilichokuwa kartibu na geti.

Baada ya maongezi wakaagana na simu kukatwa.

Choxi akahema kwa nguvu kama aliyetuliwa mzigo mzito. Hakuamini kama mambo yamepokewa kwa wepesi kiasi kile. Hakufafanuliwa kiundani lakini yote ilichochewa na maneno ya mchungaji Ndimbo alipomwambia Chikala masaa machache nyuma kutaka Izani auawe.

Kilichofatia hapo, Choxi akaanza kujiandaa na akilini mwake akawa anatafakari pa kwenda kuutupa mwili wa Izani.

Msitu wa Dutumi….! Kisaki…mh! Yes, kwenye mapori ya Dutumi.

Akapata jibu alilooona sahihi. Akajiandaa haraka na kuchukua gari yake akaizungusha upande wa nyuma kweny chumba alichomfungia Izani na kuiegesha karibu.

Akilini aliwaza kufanya hayo haraka kabla mwili wa Izani haujavunda na kuzaa harufu kali. Ndimbo alipojiridhisha kwa namna alivyoiegesha gari ikambidi kuvaa ovaroli kama fundi gereji na mikononi akavaa gloves kubwa za mikono akarudi kwenye kile chumba na kujitutumua peke yake akafanikiwa kuubeba Izani mpaka kwenye gari na kumlaza chini ya siti za nyuma.

Akachukua mifuko ya viroba vitupu na kumfunika funika kabla hajafunga mlango na kuingia upande wa mbele, akawasha gari na kuondoka.

Lakini nyuma ya ukweli wa dhana yake hakujua siri!.

Chox hakujua kilichokuwa kinaendelea ulimwengu wa roho wala hakuviona viumbe wa huko muda wote kama yuko nao na kila afanyacho wanakiona. Hkujua kumbe Izani alifunikwa kwa nguvu za malaika wawili waliopokea habari toka kwa Malaika wa taarifa kuwa wamfunike Izani kwa mbawa zao ili adui zake waone amekufa nao watamtupa kwenye mikono salama. Ndivyo ilivyokuwa kwenye ulimwengu wa roho ambako Malaika wa taarifa aliishi akitumika kufikisha habari kwa malaika wenza au nafsi ya mtu iliyoacha mwili.

Malaika huyu alikuwa ndiye yule mwenye mbawa sita ambaye mara nyingi alikuwa anamtokea Anita.

ITAENDELEA......
 
MFUASI
12
| ARUSHA|

Wakati Zuberi akizungumza na mkewe baada ya kukubaliana kuwa pamoja katika hatua za kumfatilia Izani, ndipo yule malaika mwenye mbwa sita ambaye ndiye malaika wa taarifa akatokea kwa mara nyengine mbele yao.

Anita pekee ndiye alimuona na kutoka ndani ya Zuberi na kusimama mbele yake.

“Ongeza ushawishi, hongera umeukaribia mstari wa ushindi na umefungua taarifa za ulinzi kwa Izani ambaye sasa kafunikwa ndani ya saa hamsini na nne za kwenye dunia sawa na sekunde tisa za huku. Hawezi kufa ila hatopumua kwa muda huo nawe ongeza ushawishi ili jambo hili lifanyike mapema zaidi. Nje bado kuna vita inakutafuta hakikisha hutoki ovyo ndani ya Mwanahaki na usinyamaze kuzungumza naye hakika anakusikia kwa kuwa anajisikiliza ndani yake.” Malaika akazungumza.

“Asante sana malaika mwema.” Anita akasema na mara yule Malaika akatanua mbawa zake nne kati ya sita na kuondoka kwa kasi sana. Nafsi ya nita ikarejea tena ndni ya Zuberi Mwanahaki.

“Moyo wangu unanisukuma jambo hili nianze kulifatilia haraka sana. Kesho hatuna budi kudamka mapema tuanze safari ya Morogoro nikapaone pale nilipomwona Izani ndotoni huenda kuna hatua ya kunihakikishia hili imeachwa.” Zuberi akasema na Neema ambaye akamwitika kwa kukubaliana naye.

“Naamini mume wangu we ni wa kipekee, nami leo nataka nikuandalie chai ya kipekee nzito itayokukumbusha utamu wa ziwa lililokufanya ulie uliponyimwa utotoni!” Neema akasema huku akinyanyuka alipopakatwa na kumwacha Zuberi akicheka kwa masihara.

Akajifunga taulo na kuchukua mswaki ili aende kujisafi mwili ndipo alipokumbuka kuwa dawa ya meni imeisha. Ikabidi Neema avae kwanza na kuchukua shilingi elfu mbili.

“Beby naenda dukani mara moja dawa imetuishia.” akamuaga mumewe ambaye alimwitika kwa kichwa bila kumtazama kipindi akiwa anasoma moja ya habari makini kuhusu Izani.

Neema akatoka akiwa amejifunga kitenge na kujitanda kanga kichwani. Duka lilikuwa mtaa wa nyuma na nyumba waliyokuwa wanaishi.

Wakati huo upande wa nje katika hali ya mazingara jeshi la kichawi lililotumwa na Zongo lilikuwa tayari kumzonga. Neema alipotoka tu na kuvuka miale ya ulinzi ambayo hakuiona wala kuijua, Tutu akamtazama Ngondi ambaye alikuwa ameuvaa mwonekano wa Neema.

“Muda umefika. Nenda kamtokee mbele yake atapoduwaa nitakamata kivuli chake nawe uzame ndani yake ataporejea ndani uwe wewe umeingia uturahisishie kazi tufikie malengo ya mkuu.” Akatoa agizo hilo na palepale Ngondi akanuia hitaji lake la kichawi na kuondoka kam kishada na kutokea mbele ya Neema punde tu Neema alipokata kona baada ya kuvuka uzio wa ulinzi.

Neema akiwa hana hili wala lile akashangaa kukutana na mtu akiw utupu lakini anafanana na yeye kila kitu kwa mwonekano wa sura, umbo mpaka kimo.

“WHAT!” Neema akahamaki na kutumbua macho kwa mshtuko.

| DAR ES SALAAM |



Kilichomchoma Mchungaji Ndimbo moyoni mwake ni maneno ya mkewe kukazania kilekile ambacho watoto walimtaka punde tu alipofika. Safari ya kwenda ufukweni ilimtisha.

“Na wewe tena unataka niende! Kwani leo mmeamkaje familia yangu?”

“Hapana mume wangu, unajua watoto kuna muda hebu tufanye tu wanavyotaka nao wapate kujiona wanathaminika mbele ya wazazi. Nadhani kwa kuwa leo wametaka tafadhali nakuomba mume wangu chukua nafasi hii kuwasahaulisha upweke wa dada yao. Mimi niko tayari twende pamoja baadae kwenye fukwe nzuri yenye usalama wa kutosha. Tafadhali mume wangu twende tuwaunge mkono watoto wetu katika furaha zao hasa nyakati hizi.” Mama Anita akasisitiza kwa sauti ya bembelezi akijitahidi kuonesha hisia zake njema.

Mchungaji Ndimbo akazidi kupatwa mchecheto moyoni mwake akitafuta neno la kujiepusha kwenda ufukweni.

Jambo lililokuwa linamfanya ahofie kufika ufukweni ni sharti alilopewa na mchawi Zongo baada ya kupaka dawa ya kichawi kwenye nyayo na kuosha miguu yake kwenye beseni la nyota.

“Shika hii, paka miguuni nenda kaoshe nyayo zako kwenye beseni la nyota… Hakikisha ndani ya siku zote mbili hukanyagi mchanga wa bahari ukiwa peku. Tunamfatilia Anita kupitia wewe.”

Maneno ya Dokta Zongo yakajirudia tena kichwani mwake. Akajikuta akiishia kuhema na kuzidi mshangaza mkewe asijue ni uzito gani unaomfanya mume wake aweke pingamizi ya kwenda kutimiza furaha ya watoto ufukweni.

Lakini kipindi mkewe akiwaza na kujiuliza, naye alikuwa akiwaza na kujiuliza pia ingawa mawazo yao yalitofautiana lakini yalihusu jambo moja.

Kwanini waning’ang’anie kwenda nao kwenye michanga ya bahari leo?

Ndimbo akajiuliza mwenyewe bila kusema chochote. Akamgeukia mkewe na kumtazama

Au huyu naye kiguge kanimulika kwa siri anataka kuniangusha makusudi?

Akajiuliza zaidi kwa sauti moyoni mwake lakini mdomoni akatoa sauti yenye maneno tofauti na maswali yake.

“Sawa tutaenda mchana huu.” jibu lake na uso wake havikufanana kabisa. Ndimbo akawa kama si yeye aliyezungumza. Mkewe akabaki amenyamaza na kunyanyuka akatoka chumbani.
 
MFUASI
13

La mgambo likalia! Habari zikafika kwenye kijiji kile kidogo kilichokuwa karibu na msitu mkubwa. Kila aliyesikia mbiu ikipigwa wakajua kuna jambo kwa mjumbe. Kwa muda wa nusu saa Mugondogwa alimaliza kukizunguka kijiji na kila aliyesikia mbiu ya mgambo hakuchelea kuacha shughuli zake na kukimbilia kwa mjumbe kusikia kulikoni.

Tibwili Ze Don akiwa miongoni mwa wanakijiji waliokuwa kwenye kijiwe cha karata tatu wakivuta bangi akasikia mbiu hiyo ambayo ilipigwa na ndugu yake wa kuzaliwa.

“Oyaa we Muhondogwa nini tena?” Tibwili akamfata na kumuuliza ndugu yake wakati akiondoka.

“Kuna mtu katupwa hapo msituni lakini inaonesha si mtu wa kawaida.” muhondogwa akamjibu kaka yake huku wakitembea pamoja kurejea nyumbani ambapo wanakijiji wengine walishaanza kujikusanya baada ya kusikia mbiu ya mgambo.

Tibwili na Muhondogwa wote walikuwa watoto wa Mzee Siriaki.

Ingawa Tibwili maisha yake kwa miaka mingi yalikuwa jijini Dar es salaam, kabla hajakimbia kufuatia kukamwatwa kwa jambazi Bad Man Tania aliyekuwa rafiki yake wakishirikiana katika mambo ya kihalifu. Hata kipindi kunazuka michafuko ya vurugu za Mitaa na Polisi tayari Tibwili alikuwa kashatoroka jijini na kurudi kujificha kijijini kwao. Yeye alikuwa kiongozi mrithi wa Zombi Zomboko kwenye kikosi cha Simba wasiofugwa Tandale-Uwanja wa Fisi ambapo walikuwa wanasakwa vikali na polisi baada ya kukamatwa kiongozi wao mkuu Tania.

Mjumbe Mzee Siriaki akasimama na kuwatangazia wanakijiji kile kilichojitokeza kwenye msitu na kuwataka vijana waongozane na kijana wake Muhondogwqa kwenda kumkamata huyo mtu wamdhibiti kabla hajaleta madhara kijijini kwao.

Likatoka kundi la vijana wapatao tisa akiwemo Tibwili wakiwa na mikuki sambamba na Mbwa na safari ya kurudi alipotoka Muhondogwa ikaanza.

Wakati huo kule porini Izani alikuwa haelewi akihaha kutafuta mkoba wake wa dawa za kulevya mara baada ya kunyanyuka pale alipotupwa. Mwili wake ulidhoofu zaidi na hakuwa na nguvu hata ya kutembea vizuri. Akajikuta anazidi kupepesuka na kutetemeka mikono kila alivyokuwa anapambana na nyasi kupekua wapi mkoba wake ulipo.

Alosto ilimkamata, kichwa chake bado kilishindwa kumfunulia kumbukumbu wala kumjuza kama alipo ni porini. Yeye aliwazia sindano tu ajidunge, moyo wake utuame.
 
Simulizi: MFUASI |
14
(MWISHO)

***
|MOROGORO|



Safari ya Chox na Koplo Ponda ikawa ya kibubu bubu. Hakuna aliyemsemesha mwenzake. Mpaka wanafika katikati ya msitu wa kibungo, eneo ambalo lilikuwa kimya sana ndipo Chox akaiingiza gari pembeni na kusimama ghafla.

“Vipi?” Ponda akauliza

“Nahisi kuna tatizo naomba unisaidie kucheki tafadhali.” Chox akajibu huku akifungua dashbodi na kutoa bastola kinyemela wakati Ponda akifungua mlango wa gari kushuka.

“Afande kwani shida yako hasa nini mpaka unataka kumchunguza ndugu yangu na hayo madawa ikiwa unajua akili zake haziko sawa?” Chox akasema kwa wahka baada ya kushuka huku mikono akiwa ameificha bastola kwa nyuma. Ponda alishamstukia, akamtazama kwa makini akiwa amesimama mbele yake.

“Hilo ndilo tatizo ulilosema nikusaidie kucheki?” akamuuliza.

“Yaah tatizo ni wewe kiherehere kutaka kufatilia mambo yasiyokuhusu.” Chox akasema huku akimnyooshea Ponda mdomo wa bastola.

“Na leo ndio utakuwa mwisho na mwanzo wako kujitia mjuaji na mchunguzi kwenye mambo yasiyokuhusu! Sali sala zako za mwisho Koplo!” Akasema huku akitoa usalama wa bastola na kukiweka tayari kidole chake cha shahada kuachia risasi ambayo amekusudia kumtwanga kichwani askari aliyesimama mbele yake.

“Oooh! Kwahiyo unanithibitishia sasa kumbe wewe si mtu mwema na yule si nduguyo?” Ponda akauliza huku akinyoosha mikono hewani.

“Uko sahihi ila haina maana yoyote kwako. Kwaheri!” Chox akasema na ile anataka kufytua risasi tu akawa amechelewa!

Kwa kasi ya ajabu Koplo Ponda akarusha teke kali lililoupiga mkono wa Chox uliokuwa umeshika bastola kizembe. Chox akahamaki kutaka kuiwahi bastola ilipoangukia lakini akajikuta akiangukia mgongo kwa kupigwa ngwala ya teke mzunguko na Ponda ambaye alikuwa na uwezo mkubwa wa kupambana.

“Enhee! Je, haina maana yoyote kwangu?” Ponda akazungumza kwa kebehi akiwa amesimama huku mguu mmoja amemkanyaga Chox kifuani akiwa ametumbua macho pale chini.

Chox akajihami kwa kumputa mguu Ponda ili akabiliane naye ila ndivyo akazidi kufanya makosa. Akajikuta anabutuliwa mateke kama mpira kila alipotaka kusimama akarambishwa udongo.

Mwishowe akawa hoi akihema ulimi nje kama jibwa huku damu zikimvuja puani.

“Basi afandee… naomba tuzungumze nisamehe kaka!” Chox akatweta akiwa taabani. Ponda akamwinamia kwa hasira pale chini akamkemea zaidi.

“Nikusamehe ihali ulikuwa tayari kumuua afisa wa polisi kwa bastola?” huku akimshika kidevu akamtazama kwa ujirani. Akamgeuza na kumfunga pingu mikononi kabla hajamtupia ndani ya gari upande ule wa viti vya nyuma. Alipotazama mbele ya gari kulikuwa na gazeti, akalitumia kuikota ile bastola na kuiweka ndani ya dhashbod kisha akakamatia usukani mwenyewe akawasha gari Koplo Ponda na safari ikaendelea akiifata barabara ya mjini.



* *



Mzee Gulilo akaingia kazini kumtibu Izani kwa dawa za mitishamba. Ndani ya chumba kilichotengwa kwa ajili hiyo matibabu yakawa yanaendelea ambapo Izani baada ya kusafishwa na kupewa chakula, akalazwa kwenye ubao akiwa kama alivyozaliwa, Mzee Gulilo akaanza kumchanja na kumbandika majani aliyoyajua mwenyewe ambayo aliamini yana uwezo ya kunyonya sumu iliyosambaa kwenye damu ambayo inasababisha Izani atepete kwa Alosto. Tiba zilifanyika usiku kucha mzee Gulilo hakulala wala Tibwili hakusinzia kama Muhondogwa.

“Huyu kijana ana nyota ya bahati sana.” Mzee Gulilo akazungumza na Tibwili wakati huo Izani usingizi ulikuwa umemtuliza na mate kuacha kumtoka ovyo.

“Kwanini?” Tibwili akauliza.

“Alikuwa si wa kupona huyu mpaka sasa! Bila shaka hata aliyemtupa aliamini kashakufa.” Mzee Gulilo akasema, Tibwili akatulia kumsikiliza.

“Hii mifyonzamusu huwa inakunywa sumu taratibu kwa siku mbili mpaka tatu! lakini huyu jinsi inavyoelekea kesho tu ataanza kuwa sawa! Si unaona?” Mzee Gulilo akasisitiza huku akizidi kumkandika Izani majani aliyoyaita Mifyozamusu ambayo yalimnatia kama sumaku.

Kulipopambazuka Tibwili akajiandaa na kuchukua baiskeli akapiga pedeli kwenda eneo ambalo network ya simu ilipatikana.

Ilikuwa ni zaidi ya kilomita tano kutoka kijijini kwao. Alipofika huko mtu aliyefikiria kumpigia alikuwa mmoja tu! Zombi Zomboko ambaye aliwahi kuwa mkuu wake kipindi wakiwa kwenye kundi la Simba wasiofugwa kabla Zomboko hajaachana na mambo ya uhalifu.

Ingawa tokea hapo hawakuwa na urafiki wa karibu na Zomboko alibadili namba lakini hakuwahi kufuta namba yake wala Zomboko hakubadilisha namba yake.

Na kweli alipotulia eneo lenye mtandao baada ya kuwasha simu alipopiga namba ya Zomboko ikaita na haikuchelewa kupokewa. Tibwili mapigo ya moyo yakaongeza kasi lakini akajituliza na kuwa tayari kuzungumza punde sauti nzito ilipomwitika upande wa pili.

“Hallow..Nani?”

______***_______

| DAR ES SALAAM|



Kama ilivyokuwa destuli yake kila asubuhi Zomboko alienda uwanjani kupasha misuli kabla hajafungua saluni yake.

Na kipindi hiki akawa anatoka na mwanae Kine akimfunza ushupavu ili asiwe mwanaume mzembe kwenye maisha yake.

Baada ya tizi na kurejea nyumbani, akajiandaa na kuelekea ofisini kwake. Ilikuwa yapata saa tatu asubuhi akiwa anakaribia kufika ofisini kwake, simu iliyokuwa mfukoni ikatoa mtetemo na kuita. Akaitazama namba haikutoka na jina. Zomboko akaipokea na kuuliza anayepiga kabla ya mazungumzo zaidi.

“Ndugu yako Ze Don T naongea kaka Zomboko kwema?” Sauti ya Tibwili ikasikika upande wa pili, Zomboko akaitambua.

“Unajua lakini hatuna undugu sasa?”

“Ndio..!” Tibwili akakubali

“Haya sema shida…mida ya kazi hii!” Zomboko akaongea kibabe kwa sauti isiyotaka mazoea na mtu anayemsemesha.

“Huna habari yoyote kuhusu Izani umesikia?” Tibwili akauliza.

“Sema shida yako, sijakwambia uniulize maswali?”

“Daah! Mkubwa Zombi nina jambo muhimu lakini nataka nikwambie.”

‘Oyaa! Punguza maelezo zungumza kiume Tibwili acha kuzunguka kama shoga anayetafuta bwana.” Zomboko akasema kwa sauti kali wakati huo kashafika mbele ya saluni yake. Tibwili akasikika akishusha pumzi upande wa pili na kuzungumza.

“yule dogo wa kitaani Izani Nteze ametupwa kijijini kwetu huku ameokotwa jana akiwa hoi!”

“Eti nini, hebu rudia..” Zombko akahamaki na kushusha mzuka wake baada ya kusikia taarifa hizo. Tibwili akarudia na kuzungumza hatua zote walizochukua mpaka muda huo.

Akili ya Zomboko ikaunganisha matukio haraka akayakumbuka maswali aliyohojiwa na Markus Makata na zaidi akamtafakari dereva wa mchungaji Ndimbo Masizi kuja kunyoa saluni kwake na kwenda kunywa kwenye grocery yake, na kote huko aliwauliza watoto wake kuhusu Izani Nteze. Machale yakamcheza Zombi Zomboko akapata walakini juu ya taarifa zile za Izani Nteze.



***

|ARUSHA|



Lile Jitu la ajabu Tutu likazidi kushangaa kuona Anita haonekani kutoka ndani ya mwanahaki. Ukuta uliokuwa katikati ya nafsi ya Mwanahaki uliwazuia kuhakikisha. Mawasiliano kwa mkuu wao napo hayakuwa yamerejea. Akazidi kuhamaki kuona Mwanahaki akirejea akiwa mwingi wa simanzi wala asimuone Anita kama alivyotaraji.

Akaingia moja kwa moja na kujifungia ndani. Siku hiyo kwa mara ya kwanza Zuberi Mwanahaki akalia kama mtoto. Mpaka giza linaingia hakula chochote wala Neema hakurejea.

Kwa maumivu makubwa Zu beri akaoga na kuswaki kabla hajavaa kanzu yake na kutandika mswala na kuanza kusali huku akimlilia Mungu ampe nguvu na subira katika kipindi kile kigumu kilichomvamia moyoni mwake. Akaomba pia kama kuna nguvu ya kishetani imemwingia mkewe basi Mwenyezi Mungu amuokoe katika hilo.

“Yaa Allah nipe nguvu nishinde haya. Oooh Yaarabbi mlinde mke wangu na umuokoe na vitimbi vya kishetani ee Mungu wangu. Hakika wewe ndiye mjuzi na msikizi. Nakuomba yarabbi mimi ni mja dhaifu sijui kinachoendelea ndani ya mke wangu. Kwanini iwe hivi leo..! Kwanini anioneshe mabadiliko haya kwa kiwango hiki..! Eeeh Mwenyezi Mungu pokea dua hii umlinde huko aliko awe salama. Yaa Allah takabbar-Duaa!” Zuberi akasali na kuomba huku machozi yakimtoka. Akabaki pale kwenye mswala akiomba mpaka usingizi ukampitia.

Ndipo Malaika wa faraja alipomshukia akiwa usingizini na kumfunika kwa nuru ya mbawa yake iliyompelekea Mwanahaki kusafirishwa kwenye iliyomshangaza ambayo ilimjengea maswali ya majibu ya hatua anazopaswa kuchukua.

Zuberi Mwanahaki akajiona ndani ya ndoto akiikimbiza ile gari iliyompakia mkewe na mara akatokeza katikati ya msitu kijijini kwao Dutumi Morogoro.

“Neema…Neema…Mke wangu!” akawa anaita huku akifatilia alama za matairi ya gari ambayo mke wake alitoroshwa nayo. Alipotokeza mbele akashangaa ametokea kwenye nyumba ya Mjumbe wa kijiji chao ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa marehemu baba yake Mzee Mwanahaki.

“Vipi Zuberi… Mbona hivyo?” Mzee Siriaki akamuuliza huku akishangaa hali aliyokuwa nayo Zuberi.

“Kuna gari nilikuwa naifatilia imemteka mke wangu?”

“Hapana! Gari ile ilikuwa imemteka Izani Nteze na sasa tuko naye hapa anaendelea vizuri.” Mjumbe Siriaki akamjibu na mara akatokea Izani akiwa na kina Tibwili. Zuberi akabaki na mshangao mkubwa.

“Lakini mimi nilikuwa naifatilia gari iliyompakia mke wangu?” akauliza na ajabu Izani alipozungumza akaisikia sauti ya mkewe ndani yake.

“Mke wako atarudi ukishanichukua mimi naye utampata. Amefungwa kivuli na watu waliotumwa kumwangamiza Mfuasi wangu. Wala si yeye aliyekuwa anakujibu vile na wala yule aliyekimbia naye kwenye gari si Markus Makata wala hajawahi kuwa na mahusiano na mtu huyo. Pole sana..! Nifuate hakika ukinitoa hapa utampata mkeo.” Izani aliposema hayo mara Zuberi akashangaa kuona mazingira yanabadilika na mbele yake akamshuhudia mkewe amekamatwa na kiumbe wa ajabu.





35



“NEEEMAAA!” Akamwita huku akimkimbilia yule kiumbe na mara akastuka usingizini kabla hajamfikia. Akashangaa kuona tayari kulishakucha. Akanyanyuka na kuifata simu yake ilipokuwa akastaajabu zaidi kuona tayari majira yalisoma saa nne asubuhi.

Akiwa bado anatafakari Ndoto ile ya asubuhi mara simu ikaita mikononi mwake na alipotazama anayepiga likatokea jina ‘MY WIFE’

Mapigo ya moyo wake yakaongeza kasi akiwa bado anaiwazia ndoto iliyomkurupusha usingizi.

______***_______

| DAR ES SALAAM|

Usiku ulipoingia Zongo akamwacha Ndimbo Masizi na kuondoka kwenye anga ya jiji la Tanzania na kulifata jiji la Kenya alipotoka.

Lakini kabla hajaondoka akamwachia maneno yaliyounyong’onyesha moyo wa mchungaji Ndimbo Masizi na kuua tumaini lake la ushindi wa kile alichofikiri chepesi.

“Umekuwa mzembe kila wakati Ndimbo! Umeharibu mikakati yote dakika za mwisho. Sasa nakuacha upambane nayo mwenyewe hii vita ambayo itaanza baada ya masaa 54 kupita. Na imebaki siku moja tu ambayo ni kesho unatakiwa ufike kilingeni. Lakini kwa kukanyaga kwako mchanga wa bahari na kushindwa kumtoa mwanao wa kiume jiandae kulishuhudia anguko lako la fedheha.”

Sauti hiyo aliisikia Ndimbo pekee. Usiku huo kwake ukawa mzito kupita kawaida. Kwa mara ya kwanza mama Anita akamshuhudia mumewe akiweweseka na kusema maneno yaliyomstaajabisha usiku.

“Nitamtoa tuuu Mtumishi! Tafadhalii sitaki kufedheheka…! Ni mke wangu kaniponza… Sikukusudiaa aaah Hapanaaa! Nimekubali kazi iendelee.. Mtumishiii..Mtumishii..” Ndimbo akaweweseka kwa sauti usingizini wakati mama Anita yuko macho anamtazama kitandani.

Akajikuta anashindwa kumuamsha kwa taharuki asielewe nini maana ya maneno ya mumewe. Mwishowe akaamua kufanya maombi ambayo yakamkurupusha usingizini Ndimbo.

“Hebu acha mama Papii! Tulale mke wangu tafadhali nyamaza sijisikii vizuri usipige kelele.” Ndimbo akazungumza na kuzidi mshangaza mama Anita.

Leo hii mume wangu maombi yamekuwa kelele kwake?

Akajisemea moyoni pasipo kumwambia kwa mdomo mumewe. Ikabidi ajilazimishe kulala ingawa mashaka yaliyomzonga kichwani yakamfanya usingizi upae. Alitamani jumapili ifike haraka alifikishe tatizo la mumewe kwa wazee wa kanisa lake wapate kufanya ibada maalum ya kumrudisha mchungaji wao katika hali ya kawaida.

* *

Kwa upande wa Chikala baada ya kufatilia gari na kulipeleka gereji, akawa anatafakari vile Papii alivyokuwa anamkataa baba yake.

Watoto ni malaika kweli, yule mtoto itakuwa kuna mambo kayaona hayako sawa kwa baba yake… Daah!

Akasema moyoni mwake Chikala ambaye kutokana na mizunguko ya kutwa akashindwa kukutana tena na Kisa Kabeby.

Akiwa anarejea kutoka gereje alikopeleka gari baada ya kumaliza taratibu za kipolisi, simu yake ikaita. Alipotazama anayempigia alikuwa Chox ndipo akakumbuka kuwa hajamwambia kuhusu bosi wao mkubwa kupata ajali.

“Sema Chox umesikia chochote kuhusu bosi?” Chikala akazungumza baada ya kupokea simu.

“Hapana mkuu, bosi kafanyaje tena?”

“Amepata ajali ila yuko poa hajaumia sana.”

“Duh! Kweli ni ajabu maana na mimi nilikuwa nataka tuonane kesho kuna jambo nataka tuongee ila si kwa njia ya simu.” Chox akasema upande wa pili na kumshangaza Chikala.

“Jambo hilo lina uzito gani kama tumeweza kuzungumza kwa simu kummaliza Izani teja, je hilo ni kubwa kuliko hili?” Chikala akauliza kwa sauti ya kukereka kiasi. Chox akaomba msahama na kumhakikishia Chikala kuwa hawezi kusema kwa simu hilo jambo aliloliona ni kubwa na muhimu kuliko yale aliyozungumza naye kwa simu. Chikala akashangaa na kupata shauku ya kusikia.

“Okey sasa kesho itabidi nimsindikize mzee Nairobi. Kesho kutwa nitaika huko, na ole wako liwe jambo la kipuuzi.” Chikala akaweka onyo, na kukata simu baada ya mazungumzo.

Mpaka giza linaingia hakutoka baada ya kufika kwake akaamua kulala mapema siku hiyo huku akiwazia kujiengua kufanya kazi kwa Ndimbo Masizi.

Kunapoendea huyu mzee anaweza kuja kutuumiza hadi tuliokuwa nje ya familia. Hapana, kama pesa ninayo sasa ya kuishi mjini bila mawazo…heri niachane nae tu ayanywe mwenyewe aliyoanza kuyakoroga.

Akajisemea na kujiapiza moyoni Chikala. Usiku huo naye kwake ulikuwa wa kiutofauti mpaka kunakucha alikuwa na usingizi wa mang’amung’amu.

Kilichomwamsha asubuhi naye ni simu kutoka kwa Ndimbo Masizi akimtaka awahi mapema amsindikize Nairobi. Safari hii Chikala alikosa kisingizio akaamua kukubali kusafiri na bosi wake.



***

|MOROGORO|

Koplo Ponda aliendeesha gari mpaka makao makuu ya polisi mkoa. Njiani alikuwa akiwasiliana na aliyewahi kuwa mkuu wake wa kituo zamani ambaye naye alihamishiwa Makao makuu ya polisi Morogo akiwa kama mnadhimu wa kambi.RSM Jongo, na kumwelezea kila kitu.

“Vyema sana lilete hilo jambazi pia nazungumza na mkuu hapa aitwe mkuu wa kituo Mtamba tumuweke kizuizini leoleo. Vyema sana Sajenti…ooh No Koplo!” RSM Jongo akazungumza kwa simu na kumpongeza Ponda.

Na kweli baada ya Ponda kumfikisha mtuhumiwa akawekwa kwenye chumba maalum huku akiomba kesi ile asipewe yeyote kwakuwa ameianza mwenyewe basi aimalizie.

Kutokana na sifa zake kujulikana na makamanda wa makao makuu kuptia RSM Jongo, wakakubali wamwache Ponda amfanyie mahojiano mtuhumiwa wake aliyemleta kipindi taratibu za kumkamata mkuu wa kituo Mtamba zikiandaliwa.

Na hapo ndipo Chox akabanwa vikali na Ponda akilazimishwa kumpigia bosi wake baada ya kufunguka kuwa yeye anatumiwa tu na mtu anayeitwa Chikala Gumbo.

“Sikiliza wewe! Kwa usalama wako usiende kupotelea jela, mpigie na umwite huyo anayekutuma. Tukimkamata tutakuacha huru!” Ponda akasema kwa ushawishi ambao Chox alijua ni uongo wa polisi tu. Lakini pia hakuwa tayari kutektea mwenyewe. Akaamua kushirikiana na Polisi kumvuta Chikala Morogoro.

Na ndipo alipompigia Chikala akiwa makao makuu ya Polisi Morogoro, huku simu yake ikirekodiwa.

“Vyema sana koplo. Sasa kwakuwa huyu kashafika na tushatrack mawasiliano, tutawasiliana na wenzetu wa Dar waanze kumfatilia huyo mshenzi kesho si ndo wanasafiri na bosi wake? Lazima tuwatie kizuizini.” RSM Jongo akazungumza na Ponda baada ya kutoka kwenye chumba cha mahojiano alipofungiwa Chox.

Ponda akageuza kurejea Mtamba jioni hiyo wakati mkuu wake wa kituo akijiandaa kwenda makao makuu ya mkoa kuitika wito ambao hakujua kinachoendelea.



36

Asubuhi ya kizaa zaa ikawadia. Mkuu wa kituo cha polisi Mtamba akawekwa kitimoto na maafisa wa Taaasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) akihojiwa kwa tuhuma za kupokea rushwa iliyosababisha kumwachia mtuhumiwa aliyekutwa na dawa za kulevya.

Wakati huohuo pia Chox akabananishwa mpaka akasema alipoenda kumtupa Izani Nteze.

“Aisee! Kumbe ni yule kijana aliyekuwa anahimiza watu kupambana na dawa za kulevya nyinyi ndio mmemtenda ubaya sio? Mmeona anawaharibia biashara?” RSM Jongo akawaka vikali.

Koplo Ponda naye akawa amedamkia makao makuuya mkoa mapema kuendelea na hatua ya pili ya mahojiano na uchunguzi kwa mtuhumiwa wake. Alipofika baada ya kusalimiana na polisi wenzake akaingia ofisi ya RSM kuzungumza naye.

“Nimetoka naye mshenzi huyu kumbe kijana mwenyewe ni Izani Nteze! Hujasikia sekeseke lake mwaka jana?” Jongo akaongea na kumfanya Ponda afikiri bila kukumbuka.

“Wewe nawe hukumbuki ilivuma yule mchungaji Ndimbo Masizi aliibiwa na kijana wake aliyekuwa anarusha kipindi kwenye TV akiwasihi vijana wa mitaani kuachana na mihadarati?”

“Anhaaa! Sasa nimekumbuka mkuu. Si unajua tena toka tumepelekwa maporini habari za jiji zinatupita!”

“Sasa yule naye mshenzi, ila tushafanya mawasiliano na makao makuu inasemekana anasafiri kwenda Nairobi leo. Washatumwa askari wa kuwakamata washenzi hawa.” Jongo akaongea wakati huo msafara wa kamanda mkuu wa polisi mkoa RPC MAVUGO ulikuwa unawasili kituoni baada ya kutoka ziara ya kikazi Mvomero.

“Enhee nimesikia kuna jambazi lilitaka kumuua afisa wangu liko wapi kwanza nilione?” Ndilo lilikuwa swali la kwanza pindi RPS Mavugo alipowasili makao makuu. Moja kwa moja akaongozwa mpaka kule alipofungiwa Chox ambaye alikuwa hoi kwa mateso.

“Khaa! We kijana yaani unathubutu kuja kumnyooshea kija na wangu bastola?” Rpc akawaka na kumkata kofi Chox.

“Inspekta, nataka faili la huyu mpuuzi lije ofisini kwangu.” akatoa agizo na kutoka kwenye kile chumba.

“Sawa mkuu!” Inspekta aliyekuwa pembeni yake akaitika na kupiga saluti.

Siku hiyo ilikuwa ni ya kibano tu kwa Chox ambaye alitoa ushirikiano wa kutosha ili asiumie peke yake. Ndipo saa nne asubuhi akafungwa pingu na kupakiwa kwenye difenda iliyokuwa na zaidi ya askari nane kwenda Dutumi huko kwenye msitu alipoutupa mwili wa Izani Nteze.

______***_______

| DAR ES SALAAM|

Saa tatu asubuhi ndani ya jumba la mchungaji Ndimbo Masizi, Chikala akawasili akiwa tayari kuelekea na Ndimbo huko Nairobi.

Ndimbo siku hiyo aliamka akiwa mkimya hakuwa tayari kuzungumza na yeyote. Hata mkewe alipomsimesha hakumpa ushirikiano. Muda wote huo Anita alikuwa ndani ya Papii akiuongoza mwili wa ndugu yake usijikwae hatarini.

Alipofika Chikala na kuondoka na Ndimbo ndipo Anita naye akatoka kwenye mwili wa Papii baada ya kumwona Malaika wa taarifa akitua mbele yake.

“Salamu ewe Anita mwenye upendo. Kibali chako kimetunukiwa zawadi ya ushindi. Na habari njema katika yale masaa yaliyokuwa hatari sasa yamekuwa kinyume kwako. Adui yako anaenda kutiwa nguvuni sasa.” Malaika wa taarifa akasema maneno yaliyomfurahisha Anita.

“Na vipi kuhusu Izani?”

“Izani yuko kwenye mikono ya mkondo wa Mwanahaki ambaye naye atakuwa safarini leo pindi utapofanikisha kuiweka huru nafsi ya Neema naye utaweza kumwingia kuendeleza ushawishi wa safari hakika ataenda kumtwaa Izani.” Malaika akajibu, Anita akastaajabu zaidi.

“Je nitawezaje kuiweka huru nafsi ya mwanadamu mwenye mwili hali mwenyewe ni nafsi tupu! Niaiwezejae hiyo vita?”

“Vita yako umeirahisisha katika machaguo yako Anita. Laiti ungechagua kubaki kwa Mwanahaki ungechagua ubinafsi ambao ungekusababishia uishie kifungoni kwa mashetani yaliyokuwa yanakuandama. Lakini Mola wako amekupa tunu kwa chaguo lako la ukombozi kwa wengine naye amekufanyia ukombozi kwako. Na sasa nakujaza nguvu uende Arusha ukakikomboe kivuli cha Neema ili nafsi yake iwe huru, pia utumie nafasi hiyo kulipa kisasi kwa kumwangamiza Tutu, lile jitu la kishetani lililokunyonya damu na kuua mwili wako.”

Baada ya kusema hayo yule Malaika ikaanza kumtoka Nuru ya ajabu mithili ya moto na kumwingia Anita kisha akaondoka alipomaliza. Anita naye akajishangaa kujiona amekuwa wa kipekee ndani yake, haraka akaondoka kurudi Arusha kwenda kumwoko Neema ambaye hakuwa huru kinafsi.

* *

UWANJA WA NDEGE - DAR

ASP Mwita Mwitike akiwa na maafisa sita kutoka makao makuu wakiwa wamevaa kiraia, walikuwa tayari wameiweka shabaha yao ya kumkamata Mchungaji Ndimbo Masizi na kijana ake Chikala Gumbo ambaye waliitrack namba yake ya simu waliyotumiwa na wenzao wa Morgoro ambao kwa muda huo nao walikuwa safarini kwenda kuuchukua mwili wa kijana Izani Nteze.

“Habari zenu?” Mwita akawasabahi kina Chikala punde tu waliposhuka kwenye gari kabla hata hawajaingia uwanjani.

“Njema!” Mchungaji Ndimbo akaitika huku akiwa mwenye haraka zaidi.

“Hampaswi kwenda popote mzee kuanzia sasa mko chini ya ulinzi, mnatakiwa kuongozana nami makao makuu Posta.” ASP Mwita akasema huku akiifunua upande wa koti la suti aliyovaa na kuonesha kitambulisho chake.

Mchungaji Ndimbo almanusura aanguke kwa mshtuko, wakati Chikala alipotaka kuweka hoja tayari wakawa wametoka maafsi wengine wanne na kuwazunguka wakiwataka wajisalimishe kwa amani waongozane kabla hawajatumia nguvu kuwatoa.

“Lakini…..” Mchungaji Ndimbo akataka kutia neno.

“Hakuna cha lakini mzee, unahitajika kituoni huko ukatuambie lakini zako.” ASP Mwita akaweka mkazo wake na ndipo Mchungaji Ndimbo na Chikala Gumbo wakakamatwa kama utani.

***

|ARUSHA|

Anita akafika kwenye ile nyumba ya Mwanahaki ambapo Nafsi ya Neema ilikuwa bado kizuizini na lile jitu Tutu lililofura hasira.

Safari hii lilikuwa mwenyewe na likafanikiwa kumwona Anita na kujikuta linatabasamu. Akadharau bila kujua uwezo mpya aliokuwa nao Anita ambaye pia alikuwa na hasira kuu kuhusu lile jitu.

Akaja kwa kasi ya Kombora la Moto mpaka Tutu akashangaa na kujikuta akipasuliwa mkono aliokinga kumkamata Anita.

“AAAGHHHRRR” Likanguruma kwa hasira ya kuachwa na mkono mmoja ambao alitumia kudhibiti kivuli cha Neema. Ndipo likageuka na kwa hasira likauchomoa ulimi wake mrefu wenye ncha mbili zilizochongoka.

Sauti ya Malaika wa taarifa hakuwa mbali na Anita kumpa maelekezo namna ya kutumia nguvu zake wakati anakabiliana na lile jitu.ambalo ndilo lilikuwa shetani lililotegemewa na Dokta Zongo.



37

“Nyoosha kidole kimoja cha mwisho na cha mwanzo zungusha mara sabaaa” Anita akaisikia sauti ya Malaika wa taarifa. Naye alipofanya hivyo akashangaa mkono wa nafsi yake kugeuka panga la moto na kuukata ulimi wa jitu uliokuwa unamfata kwa kasi kila alivyokuwa anaukimbia hewani.

Safari hii Tutu akajikuta anashindwa kuhimili vishindo vya kuendelea kumzuia Neema kivuli. Akajikutaanamwacha huku likipiga kelele za maumivu na hasira.

Vile kivuli cha Neema kilivyoachiwa tu kikafunukia juu ya Anita na kutoa heshima ya shukurani kabla hakijapotea eneo lile kwa kasi kuyeyuka.

Sasa vita ikabaki kwa Neema na Tutu ambaye hakuwa na msaada wowote.

Anita akammaliza kwa kukita kichwa chake na kushuhudia damu za ajabu zikiambaa juu yake zikatokea nafsi nyingi zilizowahi kudhulumiwa miili yao na Tutu zikifurahi na kumshangilia Anita huku zikimwinamia kwa heshima.

“Hongera Anita.” Sauti ya Malaika wa taarifa ikasikika pia ikimpongeza Anita ambaye pia akafarijika kulipa kisasi kwa jitu la ajabu lililouzulumu mwili wake.

* *

Wakati Anita akilimaliza lile jitu, upande wa pili kivuli cha Neema kikarejea na kuiamsha nafsi yake iliyomtoa kwa nguvu Ngondi aliyekosa namna wala ujanja wa kuikabili.

Neema akastuka na kujikuta kwenye mtaro wa barabara. Akatazama pembeni yake na kuiona simu yake.

Mungu wangu! Mume wangu…!

Akahamaki na kunyanyuka akiwa anajishangaa kujiona pekupeku. Alipotoka kwenye mtaro ndipo akagundua alikuwa maeneo ya Daraja mbili. Akazidi kuhamaki hata asikumbuke alifikaje hapo. Ikabidi ampigie simu mume wake huku mashaka yakiwa yamemjaa kichwani.

Ndipo muda huo ambao Zuberi alishtuka usingizini baada ya kuota ndoto ya ajabu iliyomjuza cha kufanya. Akaisogelea simu yake kutazama muda tayari saa nne asubuhi, na mara simu yake ikaita.

Zuberi akastukaa kuona ni mkewe ndiye anampigia. Akaanza kwa kutamka “Bismillahi” ndipo akapokea simu ambay ikamshangaza kusikia Neema akilia upande wa pili.

“Haloow! Hallooow mke wangu.” Akaita lakini mara simu ikakatika. Alipopiga akashangaa Zuberi kusikia simu haipatikani.

Wakati huo huo Anita akamwingia Zuberi ndani yake na kumtuliza nafsi.

Oooh! Hapa sina budi kufata maelekezo ya ile ndoto. Naamini Allah atamlinda mke wangu nitamkuta salama.

Zuberi akatahayuri kwa msukumo wa Anita aliyekuwa ndani yake. Akajiandaa haraka akaoga na kuchukua vitu muhimu akaweka kwenye begi kabla hajafunga mlango na kuondoka kuwahi kituo cha mabasi Arusha.

Upande wa pili Neema akajikuta akigugumia baada ya kilio cha muda alipoisikia sauti ya mumewe. Lakini kwa bahati mbaya simu yake ikazima chaji. Hakuwa na namna tena ya kufanya zaidi ya kukodi bajaji baada ya kutembea hatua chache mbele. Alipofika akakuta tayari mumewe ameshaondoka. Uzuri kulikuwa na mahala maalum wanapoweka funguo za nyumba, ambapo alipafikia na kufungua mlango akaingia ndani na kutoka akiwa na pesa ya malipo ya nauli kwa bajaji aliyokodi. Alipomlipa dereva bajaji akarejea ndani na kuiweka kwenye chaji simu yake huku akiwa bado anatafakari mambo yalivyomwendea mpaka kujikuta amelala nje ya nyumbani kwake tena amemakia kwenye mtaro? Akaanza kulia tena mpaka moyo wake ulipotulia ndimbo akawasha simu na kuwasiliana na mumewe.

Safari hii akaweza kuzungumza vyema na akashangaa mumewe kumpokea katika hali ya kawaida bila kumsema vibaya.

“Usijali mke wangu kwakuwa umesharuddi kwako nisubiri mimi naelekea kumchukua Izani. Bila shaka mambo yote yatakuwa sawa mke wangu, najua haikuwa nia yako nami sina kinyongo kuwa na amani. Nakupenda” Zuberi akazungumza maneno yaliyompa faraja Neema na kujikuta tabasamu lake likirejea.

_____***_____

|NAIROBI|

Zongo akapiga yowe baada ya kukuta chumba chake cha sita kikinyesha mvua ya damu katikati ya mchoro wake wa kafara na juu yake ukatokea mwili wa Tutu! Ukiwa hauna kichwa wala mkono.

“Aaaaaaaaaaaaaahhhhhh Ndimbooooo! Lazima ulipeee” Akaapia na kumlilia Tutu kama mwehu. Hakika kwa mara ya kwanza hata Lululu akamuogopa Zongo vile alivyobadilika siku hiyo baada ya zoezi la jana yake kushindikana na muda huo lilikuwa limebaki lisaa limoja kwisha ule muda wa masaa hamsini na nne aliokuwa amempatia Ndimbo Masizi.

“Lululuuuu nataka Ndimbo Masizi akamatwe na ateseke kweywe kutumiaka kama Mtumwa wetu. Nataka ndani ya siku tatu aanze kutumikia haiwezekaniiii haaa! Haiwezekaniiiiii…! Tutuuuuuu!” Zongo akazidi kubwata akitoa agizo kwa mtumishi wake Lululu.

Lululu akamwinamia mkuu wake kwa heshima ya utayari wa kwenda kutimiza agizo hilo.

***

|MOROGORO|

Chox akawaongoza polisi mpaka kwenye msitu kule alipomtupa Izani siku moja iliyopita.

“Wewe liuaji? Ndio hapa?” Polisi wakamuuliza baada ya kufika eneo husika na kukuta hakuna mtu ingawa walihisi dalili za uwepo wa mtu za ya mmoja eneo lile kwa jinsi nyasi zilivyokuwa zimekanyagwa.

“Ndio hapa afandee! Ndio hapa kweli niliutupa hapa mwili na alikufa mwenyewe sijamuua mimi.” Chox akajitetea na kusema kwa kumaanisha akiwa chini ya ulinzi mkali.

Polisi wakapiga picha lile eneo na hawakuwa na budi zaidi ya kujigawa wengine wakarejea mjini na polisi wawili wenye silaha wakaachwa wafatilie njia ambayo ilionyesha kuna watu walipita kutokea pale alipohakikisha mtuhumiwa kuwa aliutupa mwili wa Izani Nteze.

Polisi walioachwa waendelee na utafutaji alikuwa ni Koplo Ponda na mwenzake kutoka makao makuu Morogoro.

Chox akapakiwa kwenye Difenda na kurudishwa mjini ambapo pia aliwafikisha polisi kule alipokuwa anaishi na kuwaonesha mzigo wa madawa uliobaki sambamba na mawasiliano yote aliyokuwa anafanya na Chikala Gumbo. Polisi wakachukua vidhibti muhimu na ile nyumba ikazungushiwa utepe na kuwa chini ya uangalizi wao.



* *

Saa kumi jioni Mwanahaki akawasili Morogoro mjini na kuamua kuchukua gari ya kukodi ili aweze kuwahi Dutumi siku hiyohiyo akiwa na lengo la kugeuza kesho yake mapema.

“Kaka kuna usalama kweli? Mbona polisi tena na bunduki porini huku?” Dereva wa gari alilokodi Mwanahaki akazungumza wakati wakiingia kwenye kijiji ambacho Zuberi alikuwa anamuelekeza. Hata yeye akashangaa kukuta askari kijijini kwao na watu wakiwa wengi kwa mjumbe.

“Usijali hapa kwetu ni salama siku zote, labda kuna mnyama pori kaua mwanakijiji.” Mwanahaki akasema kumuondoa hofu dereva.

Watu waliokuwa kwa mjumbe wote wakageuza macho kuitazama gari iliyokuwa inaingia kijijini muda huo ambao tayari ilikuwa yapata saa tatu usiku.

“Ooooh Mwanahaki mwenyewe kabisaaa.” Mzee Siriaki akamtambua Zuberi mara baada ya kushuka kwenye gari na kusogea walipokuwa. Akanyanyuka na kupeana mikono na wanakijiji waliokuwa kwa mjumbe ambao wengi walimjua mbali ya kukaa kwa muda mrefu bila kuwatembelea.

Zuberi alifanana sana na baba yake marehemu mzee Mwanahaki. Na hiyo ndio ikawa chachu ya Mzee Siriaki asimpotee machoni kijana yule.

“Kwema lakini baba yangu?” Zuberi akasema huku akikaa kwenye kigoda alichopishwa na Muhondogwa.

“Bwana kwema! Kisogo tuseme si kwema.” Mzee Siriaki akazungumza huku akiwageukia polisi wawili wenye bunduki waliokuwa wamekaa kwenye benchi.

“Jamani kina baba huyu ni kijana wangu naye ndiye msomi wa kijiji chetu anaitwa Zuberi Mwanahaki, imekuwa vyema pia amefika.” akasema na kumgeukia tena Zuberi. Akaanza kumsimulia tukio la Muhondogwa na Izani.

“...sasa huyo bwana Mungu alivyo mkubwa amekamatwa na alipofika kuonesha alipomtuma ndipo hawakukuta mtu. Na hawa polisi kwa werevu wao wameweza kufatilia mpaka wanafika kwangu na kwa maelezo yao nimwaambia mtu huyo tunajua taarifa zake na ninaye. Na ndio mara nawe unaingia…karibu sana kikao hiki kinakuhusu baba.” Mzee Siriaki alipokuwa anazungumza Mwanahaki akawa anaiona ile ndoto yake na kuzidi kuamini kweli Dunia inaendeeshwa na ulimwengu wa ndani ya ndoto zake.

“Huyo Mtu ni IZANI NTEZE?” akauliza na kumfanya Koplo Ponda na mwenzake washtuke kwa kumwangalia kwa makini na taharuki.





38





______***______

|DAR ES SALAAM|



Kwenye chumba cha mahojiano makao makuu ya jeshi la polisi, Posta mitaa ya Ohio na Ghana Avenue, mchungaji Ndimbo Masizi na dereva wake Chikala Gumbo wakawa wanahojiwa kwa zamu na ASP Mwita Mwitike ambaye alipewa agizo hilo moja kwa moja na IGP Mukan Mukazabe baada ya kujua kuwa mtuhumiwa anayefatiliwa ni mchungaji mkubwa na maarufu nchini.

“Mchungaji upo hapa kwa tuhuma za kuhusika na uuzaji wa dawa za kulevya. Kweli si kweli?” Mwitike akaanza kwa swali gumu lililomfanya Ndimbo astuke na kutumbua macho asiamini anachokisikia.

“Afande tuheshimiane tafadhali mbona unanitungia kashfa nisiyostahili? Nitakufungulia kesi kama itajuliakana unanisingizia kwa kashfa nzito ya kunichafua tafadhali…!” Mchungaji Ndimbo povu likamtoka huku akihema kwa tabu. Moyoni mwake hofu ilikuwa inamchemka lakini akawa anajaribu kuizuia machoni mwa afisa aliyekuwa anamuhoji.

ACP Mwitike akamtazama Ndimbo huku akicheka kwa kumsikitikia na kuandika maneno yake.

“Unamfahamu Izani Nteze?” Mwitike akauliza swali lililokata mazungumzo ya awali na vitisho vya Ndimbo akajikuta anajibu huku akishindwa kuizuia hofu machoni mwake.

“Izani? Nani yule mwizi..! Ndio vipi kwani?” akababaika.

Mwitike akaisoma hofu yake na kumkazia sura.

“Kwa hiyo ndo ukaagiza vijana wako wamuue na kumtupa porini?” akamchanganya kwa kugusa mulemule

“Nani? Wee afande mbo…”

“Wewe ni mchungaji muuaji au mponyaji?” Mwitike akamkamatia tena kwa juu Mhungaji Ndimbo ambaye presha ikazidi kumpanda kwa maswali yaliyomchanganya mpaka akahisi hana kichwa.

Baada ya kuchukuliwa maelezo ikawa zamu ya Chikala ambaye naye makosa yake yalifanana na Bosi wake ingawa naye alipinga kwa kukanusha.

* *

Habari ya kukamatwa mchungaji Ndimbo uwanja wa ndege ikafika kwa familia yake. Mama Anita akazidi kushangazwa na kustaajabu mauzauza yasiyokauka yanayowakuta tokea kifo cha binti yao Anita.

Akafika makao makuu kuzungumza kujua kesi inayomkabili mchungaji ndipo wote walistaajabu waliosikia. Taarifa zikasambaa kama upupu zikayawasha masikio ya kila aliyesikia kuwa Ndimbo Masizi anajihusisha na biashara za dawa za kulevya.

“Hapana jamani mbona hamumuogopi Mungu mnamsingizia mume wangu?” Mama Anita akajaribu kupinga pindi alipoambiwa na ACP Mwita kosa linalomkabili mumewe ambapo hatopewa dhamana mpaka afikishwe mahakamani kujibu mashtaka matatu yanayomkabili yakiwa na uuzaji wa madawa ya kulevya, utekaji nyara.

***

|MOROGORO|

“Unamfahamu vipi Izani Nteze?” Ponda akauliza

“Ni kijana aliyejitolea maisha yake kupambana na matumizi ya mihadarati na dawa za kulevya mitaani. Namfahamu kwakuwa nimekuwa Mfuasi wake siku zote nilimfatilia kwenye kipindi cha TV” Mwanahaki akafafanua na kuwafanya wale maafisa watazamane na kumtilia mashaka.

“Je, tunaweza kuongozana nawe kwa gari uliyokuja nayo tuwahi makao makuu muda huu, kwakuwa Izani tunaye na eneo hili mnara hausomi.” Ponda akabadili mwelekeo wa swali ambalo pia Mwanahaki akalielekea bila kusita akaliunga mkono.

“Bila shaka kwa maana lazima tumwanike shetani na matendo yake ili wanaojifunza kupitia sisi wasalimike. Duh! Mchungaji kumbe ni nyoka?” Mwanahaki akasema bila kubabaika, Koplo Ponda akaona wazi mtu yule si mtu mbaya. Anita akiwa ndani ya Mwanahaki akafurahi sana kumwona Izani ingawa Izani hadi muda huo alikuwa bado hajaanza kuzungumza ila ile alosto ilimpotea wala udenda haumtoki. .

Safari ya Zuberi Mwanahaki na kina Ponda ikafatia kwa ile gari ambayo alifika nayo baada ya kuikodi tokea Morogoro mjini. Mtu mwengine aliyejumuishwa kwenye safari hiyo ni Muhondogwa, Mzee Gulilo na mjumbe mzee Siriaki wote hao wakaenda kutoa maelezo yao ya kimaandishi kama mashahidi makao makuu ya Polisi mkoa.

Tibwili yeye alijificha tokea aliposikia kuna Polisi wamekuja kijijini kwao, hakutaka kuonekana mpaka walipoondoka usiku huo.



* *

- SIKU MBILI MBELE -

INASHANGAZA SANA! KUMBE MCHUNGAJI NDIMBO MASIZI NI ‘SHETANI MWENYE SURA YA MALAIKA’

Gumzo likateka vichwa vya habari za magazeti Tanzania. Kila mtu akastaajabu nchini kwa kesi ambayo hakuna aliyewahi kuifikiria hususani waumini wa kutupwa wa kanisa la mchungaji Ndimbo Masizi.

Siku hiyo ikawa siku ya kwanza kufikishwa Mahakamani watuhumiwa watatu wakiongozwa na mtuhumiwa Ndimbo Masizi.

Siri zake nyingi zikafichuka baada ya upekuzi wa kutosha uliofanywa na jeshi la Polisi kukuta vithibitisho vingi vya kumtia hatiani.

IGP Mukan Mukazabe akazungumza na vyombo vya habari baada ya upekuzi mkali wa vijana wake kukusanya vielelezo vya kutosha vilivyomtia hatiani Ndimbo Masizi na dereva wake Chikala Gumbo pamoja na Chox ambaye naye akahamishiwa Dar Es Salaam kuhukumiwa pamoja.

Mwanasheria Neema Hussein akaungana na mumewe kuhakikisha haki inatendeka kwa Izani Nteze, wakisimama kama wanasheria wake waliojitolea kuhakikisha naye anafaidika kupitia kesi ile baada ya kuharibiwa maisha yake na mipango yake mizuri.

Hali ya Izani ilianza kuleta matumaini baada ya kumbukumbu zake kuanza kurejea na kuweza kuzungumza kilichotokea mpaka anasingiziwa kesi ya wizi ambayo hakuitenda.

“Waliniteka…Wakanitesa…Wakanichoma sindano za madawa mara kwa mara mpaka nikawa sijikumbuki….” Izani akafunguka huku machozi yakimtoka. Mkasa wake ulimgusa mpaka muheshimiwa Rais na viongozi wengine wa serikali.

Watu walilaani baada ya kuujua ukweli ambao wengine uliwatoa machozi kumuona na kumsikia Izani akizungumza hadharani mbele ya vyombo vya habari kwa mara ya kwanza. Wengi wakakiri kweli Ndimbo Masizi ni Shetani Mwenye Sura ya Malaika. Na kila aliyekiri hilo akawa Mfuasi mpya wa Izani Nteze.

“Natoa agizo kwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama kuhakikisha pia wanachunguzwa wachungaji wote waliokuwa na urafiki wa karibu na Ndimbo Masizi pia nawaonya viongozi wa dini zote na kuwaomba wasitumie jina la Mungu kama kivuli cha kuficha maovu yao. Serikali yangu haitatazama hilo endapo utabainika muhalifu. Nawaomba sana na kuwakumbusha jamani tumuogope Mungu.”

Nukuu hiyo ikanukuliwa kwenye akaunti ya Twitter ya Rais wa Tannzania.

Kesi ya Ndimbo ilipotajwa kwa mara ya kwanza pale mahakamani ndipo Lululu akamtokea kichawi mchungaji Ndimbo Masizi akaanza kuweweseka mbele ya halaiki.

“Msiniue tafadhaliii…Nisamehe Lululu nimeangamia…Aaah” Ndimbo akapayuka na kumshangaza hata Hakimu. Kile alichokuwa anakiona hakuna mwengine aliona.

“Umeshindwa kuwa mtiifu Ndimbo. Umesababisha matatizo na sasa utaenda kuteseka na kutumikia katika ulimwengu wetu.” Lululu akasema huku akimchoma kisu cha kishetani Ndimbo Masizi kwenye moyo na kuanza kumvuta kimazingara bila waliokuwepo kung’amua zaidi ya kumshuhudia Ndimbo akianguka kizimbani.

Mahakama ikashangaa kuona mtuhumiwa Ndimbo Masizi akianguka huku amejishika moyo baada ya kuweweseka. Ikabidi zifanyike huduma za kumsaidia haraka na kesi kuhairishwa huku watuhumiwa wengine wakirudishwa rumande.



* *

Hatimaye Mchungaji Ndimbo Masizi akafariki akiwa anakimbizwa hospitali ambapo walipompima wakagundua amekufa kutokana na mshtuko wa moyo. Ingawa katika uhalisia muda huo Ndimbo alikuwa katekwa kichawi na kufikishwa kwenye himaya ya mateso makali na kutumikia ambayo ilikuwa chini ya Dokta Zongo na magwiji wenzake wa kishetani kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu.

Msiba mwengine ukamkuta mama Anita. Msiba ambao haukuwa na mvuto wa upendo. Waandishi wa habari na polisi wakawa wengi msibani kuliko waumini wa kanisa na raia wema. Ndimbo Masizi hakuzikwa kwa heshima ile aliyojitengenezea akiwa hai. Ingawa pia katika uhalisia kilichozikwa hakuwa Ndimbo Masizi ila ni kiini macho tu! Ndimbo akabaki kwenye kifungo cha mateso ya kishetani ambapo huko alipigwa muhuri wa mateso mpaka kifo cha kweli kitapomkuta.

Kesi ya Chikala na Chox haikucheleweshwa ilipotajwa mara pili na hukumu ikatolewa baada ya ushahidi kukamilika wote wakakutwa na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka thelathini kila mmoja.

Kisa Kabeby akakimbia na kuutelekeza Mgahawa baada ya kuhofia asije kujumuishwa kwenye kesi.

Yule Mkuu wa Kituo Mtamba akakutwa na hatia baada kuchunguzwa na Takukuru akashtakiwa kwa kosa la kupokea rushwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka miwili bila dhamana.

Koplo Ponda akapandishwa cheo kikubwa zaidi ya mwanzo alipokuwa jijini Dar. Akaapishwa na kuvishwa nyota moja iliyomtambulisha kuwa Isnpekta Msaidizi wa Polisi na kupewa kituo cha Mtamba kuwa mkuu wake mpya.

Izani Nteze akapelekwa nje ya Nchi na ofisi ya Rais kwa matibabu zaidi wakati nafsi ya Anita ikifunguliwa rasmi milango ya ulimwengu wa nafsi na kupokewa mahala pema alipoungana na nafsi nyengine njema.

Ndoa ya Zuberi Mwanahaki na Neema Hussein ikarejea kwenye amani na utulivu wake. Mawasiliano yao na Izani aliyefikishwa Marekani kwa matibabu yakawa yanaendelea kila siku kwa njia za video calls.

Kanisa la Ndimbo Masizi likachomwa moto na watu wasiojulikana na hata mama Anita akahofia kuendelea kuishi jijini na kuamua kurejea kijijini kwao akiwa na watoto wake Papii na Doris.

Huko akaamua kujikabidhi mbele ya Kristo kwa imani akisoma biblia na kuwahimiza watoto wake waishi kwa kumtegemea Mungu wala wasije kubabaishwa na tamaa za ulimwengu watapokuwa wakubwa.

(SIKU CHACHE BAADAE)

TANDALE - DAR ES SALAAM

“Samahani kaka Zomboko. Nataka kufanya kipindi na wewe. Jina lako limeombwa na wadau wengi wa Habari za Kitaa waliokusikiliza siku ile.” Markus Makata akazungumza baada ya kufika kwa mara nyengine uwanja wa Fisi kwenye saluni ya Zombi Zomboko, ambayo sasa aliibadili jina kutoka ZOMBOKO HAIR CUTTING SALOON na kuwa MFUASI HAIR CUTTING SALOON

“Unataka kunihoji au unaomba?” Zomboko akajibu kwa sauti kavu huku akimtazama Markus ambaye siku hiyo aliongozana na timu nzima ya kipindi chake waliofika na gari yao ndogo ya ofisini.

“Ok, samahani…Naomba!” Mark akajibu huku akishusha pumzi.

“Anhaa! Sawa, Je, nawe ni shabiki wa Izani Nteze?” Zomboko akauliza.

“Hapana…” Mark akajibu

“Ila,,,,” Zomboko akasema huku akimtazama Mark na timu aliyokuja nayo ambao walisimama nje wengine wakiwa wamebeba kamera kwaajili ya kuwaonesha watu wa mitandaoni.

“Mimi ni Mfuasi wake Izani Nteze.” Markus akajitambulisha.

“Weeh Hahahahahaaa Karibu sana Mfuasi mwenzangu.” Zomboko akacheka kwa mara ya kwanza Markus naye akacheka na hata alioongozana nao wakatabasamu na amani ikanyanyuka mioyoni mwao. Wakaandaa mazingira kwaajili ya kipindi ambacho sehemu kubwa ya nchi siku hiyo waliwasha redio kumsikiliza Zombi Zomboko ambaye kwa mara ya kwanza kwenye kipindi cha siku hiyo akajitambulisha hewani huku akirekodiwa na video kuwa naye ni MFUASI wa Izani Nteze na anamsubiri kwa hamu ataporejea kuendeleza mapambano ya vita vya uraibu na utumiaji wa dawa za kulevya
MWISHO
 
Simulizi: MFUASI |
14
(MWISHO)

***
|MOROGORO|



Safari ya Chox na Koplo Ponda ikawa ya kibubu bubu. Hakuna aliyemsemesha mwenzake. Mpaka wanafika katikati ya msitu wa kibungo, eneo ambalo lilikuwa kimya sana ndipo Chox akaiingiza gari pembeni na kusimama ghafla.

“Vipi?” Ponda akauliza

“Nahisi kuna tatizo naomba unisaidie kucheki tafadhali.” Chox akajibu huku akifungua dashbodi na kutoa bastola kinyemela wakati Ponda akifungua mlango wa gari kushuka.

“Afande kwani shida yako hasa nini mpaka unataka kumchunguza ndugu yangu na hayo madawa ikiwa unajua akili zake haziko sawa?” Chox akasema kwa wahka baada ya kushuka huku mikono akiwa ameificha bastola kwa nyuma. Ponda alishamstukia, akamtazama kwa makini akiwa amesimama mbele yake.

“Hilo ndilo tatizo ulilosema nikusaidie kucheki?” akamuuliza.

“Yaah tatizo ni wewe kiherehere kutaka kufatilia mambo yasiyokuhusu.” Chox akasema huku akimnyooshea Ponda mdomo wa bastola.

“Na leo ndio utakuwa mwisho na mwanzo wako kujitia mjuaji na mchunguzi kwenye mambo yasiyokuhusu! Sali sala zako za mwisho Koplo!” Akasema huku akitoa usalama wa bastola na kukiweka tayari kidole chake cha shahada kuachia risasi ambayo amekusudia kumtwanga kichwani askari aliyesimama mbele yake.

“Oooh! Kwahiyo unanithibitishia sasa kumbe wewe si mtu mwema na yule si nduguyo?” Ponda akauliza huku akinyoosha mikono hewani.

“Uko sahihi ila haina maana yoyote kwako. Kwaheri!” Chox akasema na ile anataka kufytua risasi tu akawa amechelewa!

Kwa kasi ya ajabu Koplo Ponda akarusha teke kali lililoupiga mkono wa Chox uliokuwa umeshika bastola kizembe. Chox akahamaki kutaka kuiwahi bastola ilipoangukia lakini akajikuta akiangukia mgongo kwa kupigwa ngwala ya teke mzunguko na Ponda ambaye alikuwa na uwezo mkubwa wa kupambana.

“Enhee! Je, haina maana yoyote kwangu?” Ponda akazungumza kwa kebehi akiwa amesimama huku mguu mmoja amemkanyaga Chox kifuani akiwa ametumbua macho pale chini.

Chox akajihami kwa kumputa mguu Ponda ili akabiliane naye ila ndivyo akazidi kufanya makosa. Akajikuta anabutuliwa mateke kama mpira kila alipotaka kusimama akarambishwa udongo.

Mwishowe akawa hoi akihema ulimi nje kama jibwa huku damu zikimvuja puani.

“Basi afandee… naomba tuzungumze nisamehe kaka!” Chox akatweta akiwa taabani. Ponda akamwinamia kwa hasira pale chini akamkemea zaidi.

“Nikusamehe ihali ulikuwa tayari kumuua afisa wa polisi kwa bastola?” huku akimshika kidevu akamtazama kwa ujirani. Akamgeuza na kumfunga pingu mikononi kabla hajamtupia ndani ya gari upande ule wa viti vya nyuma. Alipotazama mbele ya gari kulikuwa na gazeti, akalitumia kuikota ile bastola na kuiweka ndani ya dhashbod kisha akakamatia usukani mwenyewe akawasha gari Koplo Ponda na safari ikaendelea akiifata barabara ya mjini.



* *



Mzee Gulilo akaingia kazini kumtibu Izani kwa dawa za mitishamba. Ndani ya chumba kilichotengwa kwa ajili hiyo matibabu yakawa yanaendelea ambapo Izani baada ya kusafishwa na kupewa chakula, akalazwa kwenye ubao akiwa kama alivyozaliwa, Mzee Gulilo akaanza kumchanja na kumbandika majani aliyoyajua mwenyewe ambayo aliamini yana uwezo ya kunyonya sumu iliyosambaa kwenye damu ambayo inasababisha Izani atepete kwa Alosto. Tiba zilifanyika usiku kucha mzee Gulilo hakulala wala Tibwili hakusinzia kama Muhondogwa.

“Huyu kijana ana nyota ya bahati sana.” Mzee Gulilo akazungumza na Tibwili wakati huo Izani usingizi ulikuwa umemtuliza na mate kuacha kumtoka ovyo.

“Kwanini?” Tibwili akauliza.

“Alikuwa si wa kupona huyu mpaka sasa! Bila shaka hata aliyemtupa aliamini kashakufa.” Mzee Gulilo akasema, Tibwili akatulia kumsikiliza.

“Hii mifyonzamusu huwa inakunywa sumu taratibu kwa siku mbili mpaka tatu! lakini huyu jinsi inavyoelekea kesho tu ataanza kuwa sawa! Si unaona?” Mzee Gulilo akasisitiza huku akizidi kumkandika Izani majani aliyoyaita Mifyozamusu ambayo yalimnatia kama sumaku.

Kulipopambazuka Tibwili akajiandaa na kuchukua baiskeli akapiga pedeli kwenda eneo ambalo network ya simu ilipatikana.

Ilikuwa ni zaidi ya kilomita tano kutoka kijijini kwao. Alipofika huko mtu aliyefikiria kumpigia alikuwa mmoja tu! Zombi Zomboko ambaye aliwahi kuwa mkuu wake kipindi wakiwa kwenye kundi la Simba wasiofugwa kabla Zomboko hajaachana na mambo ya uhalifu.

Ingawa tokea hapo hawakuwa na urafiki wa karibu na Zomboko alibadili namba lakini hakuwahi kufuta namba yake wala Zomboko hakubadilisha namba yake.

Na kweli alipotulia eneo lenye mtandao baada ya kuwasha simu alipopiga namba ya Zomboko ikaita na haikuchelewa kupokewa. Tibwili mapigo ya moyo yakaongeza kasi lakini akajituliza na kuwa tayari kuzungumza punde sauti nzito ilipomwitika upande wa pili.

“Hallow..Nani?”

______***_______

| DAR ES SALAAM|



Kama ilivyokuwa destuli yake kila asubuhi Zomboko alienda uwanjani kupasha misuli kabla hajafungua saluni yake.

Na kipindi hiki akawa anatoka na mwanae Kine akimfunza ushupavu ili asiwe mwanaume mzembe kwenye maisha yake.

Baada ya tizi na kurejea nyumbani, akajiandaa na kuelekea ofisini kwake. Ilikuwa yapata saa tatu asubuhi akiwa anakaribia kufika ofisini kwake, simu iliyokuwa mfukoni ikatoa mtetemo na kuita. Akaitazama namba haikutoka na jina. Zomboko akaipokea na kuuliza anayepiga kabla ya mazungumzo zaidi.

“Ndugu yako Ze Don T naongea kaka Zomboko kwema?” Sauti ya Tibwili ikasikika upande wa pili, Zomboko akaitambua.

“Unajua lakini hatuna undugu sasa?”

“Ndio..!” Tibwili akakubali

“Haya sema shida…mida ya kazi hii!” Zomboko akaongea kibabe kwa sauti isiyotaka mazoea na mtu anayemsemesha.

“Huna habari yoyote kuhusu Izani umesikia?” Tibwili akauliza.

“Sema shida yako, sijakwambia uniulize maswali?”

“Daah! Mkubwa Zombi nina jambo muhimu lakini nataka nikwambie.”

‘Oyaa! Punguza maelezo zungumza kiume Tibwili acha kuzunguka kama shoga anayetafuta bwana.” Zomboko akasema kwa sauti kali wakati huo kashafika mbele ya saluni yake. Tibwili akasikika akishusha pumzi upande wa pili na kuzungumza.

“yule dogo wa kitaani Izani Nteze ametupwa kijijini kwetu huku ameokotwa jana akiwa hoi!”

“Eti nini, hebu rudia..” Zombko akahamaki na kushusha mzuka wake baada ya kusikia taarifa hizo. Tibwili akarudia na kuzungumza hatua zote walizochukua mpaka muda huo.

Akili ya Zomboko ikaunganisha matukio haraka akayakumbuka maswali aliyohojiwa na Markus Makata na zaidi akamtafakari dereva wa mchungaji Ndimbo Masizi kuja kunyoa saluni kwake na kwenda kunywa kwenye grocery yake, na kote huko aliwauliza watoto wake kuhusu Izani Nteze. Machale yakamcheza Zombi Zomboko akapata walakini juu ya taarifa zile za Izani Nteze.



***

|ARUSHA|



Lile Jitu la ajabu Tutu likazidi kushangaa kuona Anita haonekani kutoka ndani ya mwanahaki. Ukuta uliokuwa katikati ya nafsi ya Mwanahaki uliwazuia kuhakikisha. Mawasiliano kwa mkuu wao napo hayakuwa yamerejea. Akazidi kuhamaki kuona Mwanahaki akirejea akiwa mwingi wa simanzi wala asimuone Anita kama alivyotaraji.

Akaingia moja kwa moja na kujifungia ndani. Siku hiyo kwa mara ya kwanza Zuberi Mwanahaki akalia kama mtoto. Mpaka giza linaingia hakula chochote wala Neema hakurejea.

Kwa maumivu makubwa Zu beri akaoga na kuswaki kabla hajavaa kanzu yake na kutandika mswala na kuanza kusali huku akimlilia Mungu ampe nguvu na subira katika kipindi kile kigumu kilichomvamia moyoni mwake. Akaomba pia kama kuna nguvu ya kishetani imemwingia mkewe basi Mwenyezi Mungu amuokoe katika hilo.

“Yaa Allah nipe nguvu nishinde haya. Oooh Yaarabbi mlinde mke wangu na umuokoe na vitimbi vya kishetani ee Mungu wangu. Hakika wewe ndiye mjuzi na msikizi. Nakuomba yarabbi mimi ni mja dhaifu sijui kinachoendelea ndani ya mke wangu. Kwanini iwe hivi leo..! Kwanini anioneshe mabadiliko haya kwa kiwango hiki..! Eeeh Mwenyezi Mungu pokea dua hii umlinde huko aliko awe salama. Yaa Allah takabbar-Duaa!” Zuberi akasali na kuomba huku machozi yakimtoka. Akabaki pale kwenye mswala akiomba mpaka usingizi ukampitia.

Ndipo Malaika wa faraja alipomshukia akiwa usingizini na kumfunika kwa nuru ya mbawa yake iliyompelekea Mwanahaki kusafirishwa kwenye iliyomshangaza ambayo ilimjengea maswali ya majibu ya hatua anazopaswa kuchukua.

Zuberi Mwanahaki akajiona ndani ya ndoto akiikimbiza ile gari iliyompakia mkewe na mara akatokeza katikati ya msitu kijijini kwao Dutumi Morogoro.

“Neema…Neema…Mke wangu!” akawa anaita huku akifatilia alama za matairi ya gari ambayo mke wake alitoroshwa nayo. Alipotokeza mbele akashangaa ametokea kwenye nyumba ya Mjumbe wa kijiji chao ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa marehemu baba yake Mzee Mwanahaki.

“Vipi Zuberi… Mbona hivyo?” Mzee Siriaki akamuuliza huku akishangaa hali aliyokuwa nayo Zuberi.

“Kuna gari nilikuwa naifatilia imemteka mke wangu?”

“Hapana! Gari ile ilikuwa imemteka Izani Nteze na sasa tuko naye hapa anaendelea vizuri.” Mjumbe Siriaki akamjibu na mara akatokea Izani akiwa na kina Tibwili. Zuberi akabaki na mshangao mkubwa.

“Lakini mimi nilikuwa naifatilia gari iliyompakia mke wangu?” akauliza na ajabu Izani alipozungumza akaisikia sauti ya mkewe ndani yake.

“Mke wako atarudi ukishanichukua mimi naye utampata. Amefungwa kivuli na watu waliotumwa kumwangamiza Mfuasi wangu. Wala si yeye aliyekuwa anakujibu vile na wala yule aliyekimbia naye kwenye gari si Markus Makata wala hajawahi kuwa na mahusiano na mtu huyo. Pole sana..! Nifuate hakika ukinitoa hapa utampata mkeo.” Izani aliposema hayo mara Zuberi akashangaa kuona mazingira yanabadilika na mbele yake akamshuhudia mkewe amekamatwa na kiumbe wa ajabu.





35



“NEEEMAAA!” Akamwita huku akimkimbilia yule kiumbe na mara akastuka usingizini kabla hajamfikia. Akashangaa kuona tayari kulishakucha. Akanyanyuka na kuifata simu yake ilipokuwa akastaajabu zaidi kuona tayari majira yalisoma saa nne asubuhi.

Akiwa bado anatafakari Ndoto ile ya asubuhi mara simu ikaita mikononi mwake na alipotazama anayepiga likatokea jina ‘MY WIFE’

Mapigo ya moyo wake yakaongeza kasi akiwa bado anaiwazia ndoto iliyomkurupusha usingizi.

______***_______

| DAR ES SALAAM|

Usiku ulipoingia Zongo akamwacha Ndimbo Masizi na kuondoka kwenye anga ya jiji la Tanzania na kulifata jiji la Kenya alipotoka.

Lakini kabla hajaondoka akamwachia maneno yaliyounyong’onyesha moyo wa mchungaji Ndimbo Masizi na kuua tumaini lake la ushindi wa kile alichofikiri chepesi.

“Umekuwa mzembe kila wakati Ndimbo! Umeharibu mikakati yote dakika za mwisho. Sasa nakuacha upambane nayo mwenyewe hii vita ambayo itaanza baada ya masaa 54 kupita. Na imebaki siku moja tu ambayo ni kesho unatakiwa ufike kilingeni. Lakini kwa kukanyaga kwako mchanga wa bahari na kushindwa kumtoa mwanao wa kiume jiandae kulishuhudia anguko lako la fedheha.”

Sauti hiyo aliisikia Ndimbo pekee. Usiku huo kwake ukawa mzito kupita kawaida. Kwa mara ya kwanza mama Anita akamshuhudia mumewe akiweweseka na kusema maneno yaliyomstaajabisha usiku.

“Nitamtoa tuuu Mtumishi! Tafadhalii sitaki kufedheheka…! Ni mke wangu kaniponza… Sikukusudiaa aaah Hapanaaa! Nimekubali kazi iendelee.. Mtumishiii..Mtumishii..” Ndimbo akaweweseka kwa sauti usingizini wakati mama Anita yuko macho anamtazama kitandani.

Akajikuta anashindwa kumuamsha kwa taharuki asielewe nini maana ya maneno ya mumewe. Mwishowe akaamua kufanya maombi ambayo yakamkurupusha usingizini Ndimbo.

“Hebu acha mama Papii! Tulale mke wangu tafadhali nyamaza sijisikii vizuri usipige kelele.” Ndimbo akazungumza na kuzidi mshangaza mama Anita.

Leo hii mume wangu maombi yamekuwa kelele kwake?

Akajisemea moyoni pasipo kumwambia kwa mdomo mumewe. Ikabidi ajilazimishe kulala ingawa mashaka yaliyomzonga kichwani yakamfanya usingizi upae. Alitamani jumapili ifike haraka alifikishe tatizo la mumewe kwa wazee wa kanisa lake wapate kufanya ibada maalum ya kumrudisha mchungaji wao katika hali ya kawaida.

* *

Kwa upande wa Chikala baada ya kufatilia gari na kulipeleka gereji, akawa anatafakari vile Papii alivyokuwa anamkataa baba yake.

Watoto ni malaika kweli, yule mtoto itakuwa kuna mambo kayaona hayako sawa kwa baba yake… Daah!

Akasema moyoni mwake Chikala ambaye kutokana na mizunguko ya kutwa akashindwa kukutana tena na Kisa Kabeby.

Akiwa anarejea kutoka gereje alikopeleka gari baada ya kumaliza taratibu za kipolisi, simu yake ikaita. Alipotazama anayempigia alikuwa Chox ndipo akakumbuka kuwa hajamwambia kuhusu bosi wao mkubwa kupata ajali.

“Sema Chox umesikia chochote kuhusu bosi?” Chikala akazungumza baada ya kupokea simu.

“Hapana mkuu, bosi kafanyaje tena?”

“Amepata ajali ila yuko poa hajaumia sana.”

“Duh! Kweli ni ajabu maana na mimi nilikuwa nataka tuonane kesho kuna jambo nataka tuongee ila si kwa njia ya simu.” Chox akasema upande wa pili na kumshangaza Chikala.

“Jambo hilo lina uzito gani kama tumeweza kuzungumza kwa simu kummaliza Izani teja, je hilo ni kubwa kuliko hili?” Chikala akauliza kwa sauti ya kukereka kiasi. Chox akaomba msahama na kumhakikishia Chikala kuwa hawezi kusema kwa simu hilo jambo aliloliona ni kubwa na muhimu kuliko yale aliyozungumza naye kwa simu. Chikala akashangaa na kupata shauku ya kusikia.

“Okey sasa kesho itabidi nimsindikize mzee Nairobi. Kesho kutwa nitaika huko, na ole wako liwe jambo la kipuuzi.” Chikala akaweka onyo, na kukata simu baada ya mazungumzo.

Mpaka giza linaingia hakutoka baada ya kufika kwake akaamua kulala mapema siku hiyo huku akiwazia kujiengua kufanya kazi kwa Ndimbo Masizi.

Kunapoendea huyu mzee anaweza kuja kutuumiza hadi tuliokuwa nje ya familia. Hapana, kama pesa ninayo sasa ya kuishi mjini bila mawazo…heri niachane nae tu ayanywe mwenyewe aliyoanza kuyakoroga.

Akajisemea na kujiapiza moyoni Chikala. Usiku huo naye kwake ulikuwa wa kiutofauti mpaka kunakucha alikuwa na usingizi wa mang’amung’amu.

Kilichomwamsha asubuhi naye ni simu kutoka kwa Ndimbo Masizi akimtaka awahi mapema amsindikize Nairobi. Safari hii Chikala alikosa kisingizio akaamua kukubali kusafiri na bosi wake.



***

|MOROGORO|

Koplo Ponda aliendeesha gari mpaka makao makuu ya polisi mkoa. Njiani alikuwa akiwasiliana na aliyewahi kuwa mkuu wake wa kituo zamani ambaye naye alihamishiwa Makao makuu ya polisi Morogo akiwa kama mnadhimu wa kambi.RSM Jongo, na kumwelezea kila kitu.

“Vyema sana lilete hilo jambazi pia nazungumza na mkuu hapa aitwe mkuu wa kituo Mtamba tumuweke kizuizini leoleo. Vyema sana Sajenti…ooh No Koplo!” RSM Jongo akazungumza kwa simu na kumpongeza Ponda.

Na kweli baada ya Ponda kumfikisha mtuhumiwa akawekwa kwenye chumba maalum huku akiomba kesi ile asipewe yeyote kwakuwa ameianza mwenyewe basi aimalizie.

Kutokana na sifa zake kujulikana na makamanda wa makao makuu kuptia RSM Jongo, wakakubali wamwache Ponda amfanyie mahojiano mtuhumiwa wake aliyemleta kipindi taratibu za kumkamata mkuu wa kituo Mtamba zikiandaliwa.

Na hapo ndipo Chox akabanwa vikali na Ponda akilazimishwa kumpigia bosi wake baada ya kufunguka kuwa yeye anatumiwa tu na mtu anayeitwa Chikala Gumbo.

“Sikiliza wewe! Kwa usalama wako usiende kupotelea jela, mpigie na umwite huyo anayekutuma. Tukimkamata tutakuacha huru!” Ponda akasema kwa ushawishi ambao Chox alijua ni uongo wa polisi tu. Lakini pia hakuwa tayari kutektea mwenyewe. Akaamua kushirikiana na Polisi kumvuta Chikala Morogoro.

Na ndipo alipompigia Chikala akiwa makao makuu ya Polisi Morogoro, huku simu yake ikirekodiwa.

“Vyema sana koplo. Sasa kwakuwa huyu kashafika na tushatrack mawasiliano, tutawasiliana na wenzetu wa Dar waanze kumfatilia huyo mshenzi kesho si ndo wanasafiri na bosi wake? Lazima tuwatie kizuizini.” RSM Jongo akazungumza na Ponda baada ya kutoka kwenye chumba cha mahojiano alipofungiwa Chox.

Ponda akageuza kurejea Mtamba jioni hiyo wakati mkuu wake wa kituo akijiandaa kwenda makao makuu ya mkoa kuitika wito ambao hakujua kinachoendelea.



36

Asubuhi ya kizaa zaa ikawadia. Mkuu wa kituo cha polisi Mtamba akawekwa kitimoto na maafisa wa Taaasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) akihojiwa kwa tuhuma za kupokea rushwa iliyosababisha kumwachia mtuhumiwa aliyekutwa na dawa za kulevya.

Wakati huohuo pia Chox akabananishwa mpaka akasema alipoenda kumtupa Izani Nteze.

“Aisee! Kumbe ni yule kijana aliyekuwa anahimiza watu kupambana na dawa za kulevya nyinyi ndio mmemtenda ubaya sio? Mmeona anawaharibia biashara?” RSM Jongo akawaka vikali.

Koplo Ponda naye akawa amedamkia makao makuuya mkoa mapema kuendelea na hatua ya pili ya mahojiano na uchunguzi kwa mtuhumiwa wake. Alipofika baada ya kusalimiana na polisi wenzake akaingia ofisi ya RSM kuzungumza naye.

“Nimetoka naye mshenzi huyu kumbe kijana mwenyewe ni Izani Nteze! Hujasikia sekeseke lake mwaka jana?” Jongo akaongea na kumfanya Ponda afikiri bila kukumbuka.

“Wewe nawe hukumbuki ilivuma yule mchungaji Ndimbo Masizi aliibiwa na kijana wake aliyekuwa anarusha kipindi kwenye TV akiwasihi vijana wa mitaani kuachana na mihadarati?”

“Anhaaa! Sasa nimekumbuka mkuu. Si unajua tena toka tumepelekwa maporini habari za jiji zinatupita!”

“Sasa yule naye mshenzi, ila tushafanya mawasiliano na makao makuu inasemekana anasafiri kwenda Nairobi leo. Washatumwa askari wa kuwakamata washenzi hawa.” Jongo akaongea wakati huo msafara wa kamanda mkuu wa polisi mkoa RPC MAVUGO ulikuwa unawasili kituoni baada ya kutoka ziara ya kikazi Mvomero.

“Enhee nimesikia kuna jambazi lilitaka kumuua afisa wangu liko wapi kwanza nilione?” Ndilo lilikuwa swali la kwanza pindi RPS Mavugo alipowasili makao makuu. Moja kwa moja akaongozwa mpaka kule alipofungiwa Chox ambaye alikuwa hoi kwa mateso.

“Khaa! We kijana yaani unathubutu kuja kumnyooshea kija na wangu bastola?” Rpc akawaka na kumkata kofi Chox.

“Inspekta, nataka faili la huyu mpuuzi lije ofisini kwangu.” akatoa agizo na kutoka kwenye kile chumba.

“Sawa mkuu!” Inspekta aliyekuwa pembeni yake akaitika na kupiga saluti.

Siku hiyo ilikuwa ni ya kibano tu kwa Chox ambaye alitoa ushirikiano wa kutosha ili asiumie peke yake. Ndipo saa nne asubuhi akafungwa pingu na kupakiwa kwenye difenda iliyokuwa na zaidi ya askari nane kwenda Dutumi huko kwenye msitu alipoutupa mwili wa Izani Nteze.

______***_______

| DAR ES SALAAM|

Saa tatu asubuhi ndani ya jumba la mchungaji Ndimbo Masizi, Chikala akawasili akiwa tayari kuelekea na Ndimbo huko Nairobi.

Ndimbo siku hiyo aliamka akiwa mkimya hakuwa tayari kuzungumza na yeyote. Hata mkewe alipomsimesha hakumpa ushirikiano. Muda wote huo Anita alikuwa ndani ya Papii akiuongoza mwili wa ndugu yake usijikwae hatarini.

Alipofika Chikala na kuondoka na Ndimbo ndipo Anita naye akatoka kwenye mwili wa Papii baada ya kumwona Malaika wa taarifa akitua mbele yake.

“Salamu ewe Anita mwenye upendo. Kibali chako kimetunukiwa zawadi ya ushindi. Na habari njema katika yale masaa yaliyokuwa hatari sasa yamekuwa kinyume kwako. Adui yako anaenda kutiwa nguvuni sasa.” Malaika wa taarifa akasema maneno yaliyomfurahisha Anita.

“Na vipi kuhusu Izani?”

“Izani yuko kwenye mikono ya mkondo wa Mwanahaki ambaye naye atakuwa safarini leo pindi utapofanikisha kuiweka huru nafsi ya Neema naye utaweza kumwingia kuendeleza ushawishi wa safari hakika ataenda kumtwaa Izani.” Malaika akajibu, Anita akastaajabu zaidi.

“Je nitawezaje kuiweka huru nafsi ya mwanadamu mwenye mwili hali mwenyewe ni nafsi tupu! Niaiwezejae hiyo vita?”

“Vita yako umeirahisisha katika machaguo yako Anita. Laiti ungechagua kubaki kwa Mwanahaki ungechagua ubinafsi ambao ungekusababishia uishie kifungoni kwa mashetani yaliyokuwa yanakuandama. Lakini Mola wako amekupa tunu kwa chaguo lako la ukombozi kwa wengine naye amekufanyia ukombozi kwako. Na sasa nakujaza nguvu uende Arusha ukakikomboe kivuli cha Neema ili nafsi yake iwe huru, pia utumie nafasi hiyo kulipa kisasi kwa kumwangamiza Tutu, lile jitu la kishetani lililokunyonya damu na kuua mwili wako.”

Baada ya kusema hayo yule Malaika ikaanza kumtoka Nuru ya ajabu mithili ya moto na kumwingia Anita kisha akaondoka alipomaliza. Anita naye akajishangaa kujiona amekuwa wa kipekee ndani yake, haraka akaondoka kurudi Arusha kwenda kumwoko Neema ambaye hakuwa huru kinafsi.

* *

UWANJA WA NDEGE - DAR

ASP Mwita Mwitike akiwa na maafisa sita kutoka makao makuu wakiwa wamevaa kiraia, walikuwa tayari wameiweka shabaha yao ya kumkamata Mchungaji Ndimbo Masizi na kijana ake Chikala Gumbo ambaye waliitrack namba yake ya simu waliyotumiwa na wenzao wa Morgoro ambao kwa muda huo nao walikuwa safarini kwenda kuuchukua mwili wa kijana Izani Nteze.

“Habari zenu?” Mwita akawasabahi kina Chikala punde tu waliposhuka kwenye gari kabla hata hawajaingia uwanjani.

“Njema!” Mchungaji Ndimbo akaitika huku akiwa mwenye haraka zaidi.

“Hampaswi kwenda popote mzee kuanzia sasa mko chini ya ulinzi, mnatakiwa kuongozana nami makao makuu Posta.” ASP Mwita akasema huku akiifunua upande wa koti la suti aliyovaa na kuonesha kitambulisho chake.

Mchungaji Ndimbo almanusura aanguke kwa mshtuko, wakati Chikala alipotaka kuweka hoja tayari wakawa wametoka maafsi wengine wanne na kuwazunguka wakiwataka wajisalimishe kwa amani waongozane kabla hawajatumia nguvu kuwatoa.

“Lakini…..” Mchungaji Ndimbo akataka kutia neno.

“Hakuna cha lakini mzee, unahitajika kituoni huko ukatuambie lakini zako.” ASP Mwita akaweka mkazo wake na ndipo Mchungaji Ndimbo na Chikala Gumbo wakakamatwa kama utani.

***

|ARUSHA|

Anita akafika kwenye ile nyumba ya Mwanahaki ambapo Nafsi ya Neema ilikuwa bado kizuizini na lile jitu Tutu lililofura hasira.

Safari hii lilikuwa mwenyewe na likafanikiwa kumwona Anita na kujikuta linatabasamu. Akadharau bila kujua uwezo mpya aliokuwa nao Anita ambaye pia alikuwa na hasira kuu kuhusu lile jitu.

Akaja kwa kasi ya Kombora la Moto mpaka Tutu akashangaa na kujikuta akipasuliwa mkono aliokinga kumkamata Anita.

“AAAGHHHRRR” Likanguruma kwa hasira ya kuachwa na mkono mmoja ambao alitumia kudhibiti kivuli cha Neema. Ndipo likageuka na kwa hasira likauchomoa ulimi wake mrefu wenye ncha mbili zilizochongoka.

Sauti ya Malaika wa taarifa hakuwa mbali na Anita kumpa maelekezo namna ya kutumia nguvu zake wakati anakabiliana na lile jitu.ambalo ndilo lilikuwa shetani lililotegemewa na Dokta Zongo.



37

“Nyoosha kidole kimoja cha mwisho na cha mwanzo zungusha mara sabaaa” Anita akaisikia sauti ya Malaika wa taarifa. Naye alipofanya hivyo akashangaa mkono wa nafsi yake kugeuka panga la moto na kuukata ulimi wa jitu uliokuwa unamfata kwa kasi kila alivyokuwa anaukimbia hewani.

Safari hii Tutu akajikuta anashindwa kuhimili vishindo vya kuendelea kumzuia Neema kivuli. Akajikutaanamwacha huku likipiga kelele za maumivu na hasira.

Vile kivuli cha Neema kilivyoachiwa tu kikafunukia juu ya Anita na kutoa heshima ya shukurani kabla hakijapotea eneo lile kwa kasi kuyeyuka.

Sasa vita ikabaki kwa Neema na Tutu ambaye hakuwa na msaada wowote.

Anita akammaliza kwa kukita kichwa chake na kushuhudia damu za ajabu zikiambaa juu yake zikatokea nafsi nyingi zilizowahi kudhulumiwa miili yao na Tutu zikifurahi na kumshangilia Anita huku zikimwinamia kwa heshima.

“Hongera Anita.” Sauti ya Malaika wa taarifa ikasikika pia ikimpongeza Anita ambaye pia akafarijika kulipa kisasi kwa jitu la ajabu lililouzulumu mwili wake.

* *

Wakati Anita akilimaliza lile jitu, upande wa pili kivuli cha Neema kikarejea na kuiamsha nafsi yake iliyomtoa kwa nguvu Ngondi aliyekosa namna wala ujanja wa kuikabili.

Neema akastuka na kujikuta kwenye mtaro wa barabara. Akatazama pembeni yake na kuiona simu yake.

Mungu wangu! Mume wangu…!

Akahamaki na kunyanyuka akiwa anajishangaa kujiona pekupeku. Alipotoka kwenye mtaro ndipo akagundua alikuwa maeneo ya Daraja mbili. Akazidi kuhamaki hata asikumbuke alifikaje hapo. Ikabidi ampigie simu mume wake huku mashaka yakiwa yamemjaa kichwani.

Ndipo muda huo ambao Zuberi alishtuka usingizini baada ya kuota ndoto ya ajabu iliyomjuza cha kufanya. Akaisogelea simu yake kutazama muda tayari saa nne asubuhi, na mara simu yake ikaita.

Zuberi akastukaa kuona ni mkewe ndiye anampigia. Akaanza kwa kutamka “Bismillahi” ndipo akapokea simu ambay ikamshangaza kusikia Neema akilia upande wa pili.

“Haloow! Hallooow mke wangu.” Akaita lakini mara simu ikakatika. Alipopiga akashangaa Zuberi kusikia simu haipatikani.

Wakati huo huo Anita akamwingia Zuberi ndani yake na kumtuliza nafsi.

Oooh! Hapa sina budi kufata maelekezo ya ile ndoto. Naamini Allah atamlinda mke wangu nitamkuta salama.

Zuberi akatahayuri kwa msukumo wa Anita aliyekuwa ndani yake. Akajiandaa haraka akaoga na kuchukua vitu muhimu akaweka kwenye begi kabla hajafunga mlango na kuondoka kuwahi kituo cha mabasi Arusha.

Upande wa pili Neema akajikuta akigugumia baada ya kilio cha muda alipoisikia sauti ya mumewe. Lakini kwa bahati mbaya simu yake ikazima chaji. Hakuwa na namna tena ya kufanya zaidi ya kukodi bajaji baada ya kutembea hatua chache mbele. Alipofika akakuta tayari mumewe ameshaondoka. Uzuri kulikuwa na mahala maalum wanapoweka funguo za nyumba, ambapo alipafikia na kufungua mlango akaingia ndani na kutoka akiwa na pesa ya malipo ya nauli kwa bajaji aliyokodi. Alipomlipa dereva bajaji akarejea ndani na kuiweka kwenye chaji simu yake huku akiwa bado anatafakari mambo yalivyomwendea mpaka kujikuta amelala nje ya nyumbani kwake tena amemakia kwenye mtaro? Akaanza kulia tena mpaka moyo wake ulipotulia ndimbo akawasha simu na kuwasiliana na mumewe.

Safari hii akaweza kuzungumza vyema na akashangaa mumewe kumpokea katika hali ya kawaida bila kumsema vibaya.

“Usijali mke wangu kwakuwa umesharuddi kwako nisubiri mimi naelekea kumchukua Izani. Bila shaka mambo yote yatakuwa sawa mke wangu, najua haikuwa nia yako nami sina kinyongo kuwa na amani. Nakupenda” Zuberi akazungumza maneno yaliyompa faraja Neema na kujikuta tabasamu lake likirejea.

_____***_____

|NAIROBI|

Zongo akapiga yowe baada ya kukuta chumba chake cha sita kikinyesha mvua ya damu katikati ya mchoro wake wa kafara na juu yake ukatokea mwili wa Tutu! Ukiwa hauna kichwa wala mkono.

“Aaaaaaaaaaaaaahhhhhh Ndimbooooo! Lazima ulipeee” Akaapia na kumlilia Tutu kama mwehu. Hakika kwa mara ya kwanza hata Lululu akamuogopa Zongo vile alivyobadilika siku hiyo baada ya zoezi la jana yake kushindikana na muda huo lilikuwa limebaki lisaa limoja kwisha ule muda wa masaa hamsini na nne aliokuwa amempatia Ndimbo Masizi.

“Lululuuuu nataka Ndimbo Masizi akamatwe na ateseke kweywe kutumiaka kama Mtumwa wetu. Nataka ndani ya siku tatu aanze kutumikia haiwezekaniiii haaa! Haiwezekaniiiiii…! Tutuuuuuu!” Zongo akazidi kubwata akitoa agizo kwa mtumishi wake Lululu.

Lululu akamwinamia mkuu wake kwa heshima ya utayari wa kwenda kutimiza agizo hilo.

***

|MOROGORO|

Chox akawaongoza polisi mpaka kwenye msitu kule alipomtupa Izani siku moja iliyopita.

“Wewe liuaji? Ndio hapa?” Polisi wakamuuliza baada ya kufika eneo husika na kukuta hakuna mtu ingawa walihisi dalili za uwepo wa mtu za ya mmoja eneo lile kwa jinsi nyasi zilivyokuwa zimekanyagwa.

“Ndio hapa afandee! Ndio hapa kweli niliutupa hapa mwili na alikufa mwenyewe sijamuua mimi.” Chox akajitetea na kusema kwa kumaanisha akiwa chini ya ulinzi mkali.

Polisi wakapiga picha lile eneo na hawakuwa na budi zaidi ya kujigawa wengine wakarejea mjini na polisi wawili wenye silaha wakaachwa wafatilie njia ambayo ilionyesha kuna watu walipita kutokea pale alipohakikisha mtuhumiwa kuwa aliutupa mwili wa Izani Nteze.

Polisi walioachwa waendelee na utafutaji alikuwa ni Koplo Ponda na mwenzake kutoka makao makuu Morogoro.

Chox akapakiwa kwenye Difenda na kurudishwa mjini ambapo pia aliwafikisha polisi kule alipokuwa anaishi na kuwaonesha mzigo wa madawa uliobaki sambamba na mawasiliano yote aliyokuwa anafanya na Chikala Gumbo. Polisi wakachukua vidhibti muhimu na ile nyumba ikazungushiwa utepe na kuwa chini ya uangalizi wao.



* *

Saa kumi jioni Mwanahaki akawasili Morogoro mjini na kuamua kuchukua gari ya kukodi ili aweze kuwahi Dutumi siku hiyohiyo akiwa na lengo la kugeuza kesho yake mapema.

“Kaka kuna usalama kweli? Mbona polisi tena na bunduki porini huku?” Dereva wa gari alilokodi Mwanahaki akazungumza wakati wakiingia kwenye kijiji ambacho Zuberi alikuwa anamuelekeza. Hata yeye akashangaa kukuta askari kijijini kwao na watu wakiwa wengi kwa mjumbe.

“Usijali hapa kwetu ni salama siku zote, labda kuna mnyama pori kaua mwanakijiji.” Mwanahaki akasema kumuondoa hofu dereva.

Watu waliokuwa kwa mjumbe wote wakageuza macho kuitazama gari iliyokuwa inaingia kijijini muda huo ambao tayari ilikuwa yapata saa tatu usiku.

“Ooooh Mwanahaki mwenyewe kabisaaa.” Mzee Siriaki akamtambua Zuberi mara baada ya kushuka kwenye gari na kusogea walipokuwa. Akanyanyuka na kupeana mikono na wanakijiji waliokuwa kwa mjumbe ambao wengi walimjua mbali ya kukaa kwa muda mrefu bila kuwatembelea.

Zuberi alifanana sana na baba yake marehemu mzee Mwanahaki. Na hiyo ndio ikawa chachu ya Mzee Siriaki asimpotee machoni kijana yule.

“Kwema lakini baba yangu?” Zuberi akasema huku akikaa kwenye kigoda alichopishwa na Muhondogwa.

“Bwana kwema! Kisogo tuseme si kwema.” Mzee Siriaki akazungumza huku akiwageukia polisi wawili wenye bunduki waliokuwa wamekaa kwenye benchi.

“Jamani kina baba huyu ni kijana wangu naye ndiye msomi wa kijiji chetu anaitwa Zuberi Mwanahaki, imekuwa vyema pia amefika.” akasema na kumgeukia tena Zuberi. Akaanza kumsimulia tukio la Muhondogwa na Izani.

“...sasa huyo bwana Mungu alivyo mkubwa amekamatwa na alipofika kuonesha alipomtuma ndipo hawakukuta mtu. Na hawa polisi kwa werevu wao wameweza kufatilia mpaka wanafika kwangu na kwa maelezo yao nimwaambia mtu huyo tunajua taarifa zake na ninaye. Na ndio mara nawe unaingia…karibu sana kikao hiki kinakuhusu baba.” Mzee Siriaki alipokuwa anazungumza Mwanahaki akawa anaiona ile ndoto yake na kuzidi kuamini kweli Dunia inaendeeshwa na ulimwengu wa ndani ya ndoto zake.

“Huyo Mtu ni IZANI NTEZE?” akauliza na kumfanya Koplo Ponda na mwenzake washtuke kwa kumwangalia kwa makini na taharuki.





38





______***______

|DAR ES SALAAM|



Kwenye chumba cha mahojiano makao makuu ya jeshi la polisi, Posta mitaa ya Ohio na Ghana Avenue, mchungaji Ndimbo Masizi na dereva wake Chikala Gumbo wakawa wanahojiwa kwa zamu na ASP Mwita Mwitike ambaye alipewa agizo hilo moja kwa moja na IGP Mukan Mukazabe baada ya kujua kuwa mtuhumiwa anayefatiliwa ni mchungaji mkubwa na maarufu nchini.

“Mchungaji upo hapa kwa tuhuma za kuhusika na uuzaji wa dawa za kulevya. Kweli si kweli?” Mwitike akaanza kwa swali gumu lililomfanya Ndimbo astuke na kutumbua macho asiamini anachokisikia.

“Afande tuheshimiane tafadhali mbona unanitungia kashfa nisiyostahili? Nitakufungulia kesi kama itajuliakana unanisingizia kwa kashfa nzito ya kunichafua tafadhali…!” Mchungaji Ndimbo povu likamtoka huku akihema kwa tabu. Moyoni mwake hofu ilikuwa inamchemka lakini akawa anajaribu kuizuia machoni mwa afisa aliyekuwa anamuhoji.

ACP Mwitike akamtazama Ndimbo huku akicheka kwa kumsikitikia na kuandika maneno yake.

“Unamfahamu Izani Nteze?” Mwitike akauliza swali lililokata mazungumzo ya awali na vitisho vya Ndimbo akajikuta anajibu huku akishindwa kuizuia hofu machoni mwake.

“Izani? Nani yule mwizi..! Ndio vipi kwani?” akababaika.

Mwitike akaisoma hofu yake na kumkazia sura.

“Kwa hiyo ndo ukaagiza vijana wako wamuue na kumtupa porini?” akamchanganya kwa kugusa mulemule

“Nani? Wee afande mbo…”

“Wewe ni mchungaji muuaji au mponyaji?” Mwitike akamkamatia tena kwa juu Mhungaji Ndimbo ambaye presha ikazidi kumpanda kwa maswali yaliyomchanganya mpaka akahisi hana kichwa.

Baada ya kuchukuliwa maelezo ikawa zamu ya Chikala ambaye naye makosa yake yalifanana na Bosi wake ingawa naye alipinga kwa kukanusha.

* *

Habari ya kukamatwa mchungaji Ndimbo uwanja wa ndege ikafika kwa familia yake. Mama Anita akazidi kushangazwa na kustaajabu mauzauza yasiyokauka yanayowakuta tokea kifo cha binti yao Anita.

Akafika makao makuu kuzungumza kujua kesi inayomkabili mchungaji ndipo wote walistaajabu waliosikia. Taarifa zikasambaa kama upupu zikayawasha masikio ya kila aliyesikia kuwa Ndimbo Masizi anajihusisha na biashara za dawa za kulevya.

“Hapana jamani mbona hamumuogopi Mungu mnamsingizia mume wangu?” Mama Anita akajaribu kupinga pindi alipoambiwa na ACP Mwita kosa linalomkabili mumewe ambapo hatopewa dhamana mpaka afikishwe mahakamani kujibu mashtaka matatu yanayomkabili yakiwa na uuzaji wa madawa ya kulevya, utekaji nyara.

***

|MOROGORO|

“Unamfahamu vipi Izani Nteze?” Ponda akauliza

“Ni kijana aliyejitolea maisha yake kupambana na matumizi ya mihadarati na dawa za kulevya mitaani. Namfahamu kwakuwa nimekuwa Mfuasi wake siku zote nilimfatilia kwenye kipindi cha TV” Mwanahaki akafafanua na kuwafanya wale maafisa watazamane na kumtilia mashaka.

“Je, tunaweza kuongozana nawe kwa gari uliyokuja nayo tuwahi makao makuu muda huu, kwakuwa Izani tunaye na eneo hili mnara hausomi.” Ponda akabadili mwelekeo wa swali ambalo pia Mwanahaki akalielekea bila kusita akaliunga mkono.

“Bila shaka kwa maana lazima tumwanike shetani na matendo yake ili wanaojifunza kupitia sisi wasalimike. Duh! Mchungaji kumbe ni nyoka?” Mwanahaki akasema bila kubabaika, Koplo Ponda akaona wazi mtu yule si mtu mbaya. Anita akiwa ndani ya Mwanahaki akafurahi sana kumwona Izani ingawa Izani hadi muda huo alikuwa bado hajaanza kuzungumza ila ile alosto ilimpotea wala udenda haumtoki. .

Safari ya Zuberi Mwanahaki na kina Ponda ikafatia kwa ile gari ambayo alifika nayo baada ya kuikodi tokea Morogoro mjini. Mtu mwengine aliyejumuishwa kwenye safari hiyo ni Muhondogwa, Mzee Gulilo na mjumbe mzee Siriaki wote hao wakaenda kutoa maelezo yao ya kimaandishi kama mashahidi makao makuu ya Polisi mkoa.

Tibwili yeye alijificha tokea aliposikia kuna Polisi wamekuja kijijini kwao, hakutaka kuonekana mpaka walipoondoka usiku huo.



* *

- SIKU MBILI MBELE -

INASHANGAZA SANA! KUMBE MCHUNGAJI NDIMBO MASIZI NI ‘SHETANI MWENYE SURA YA MALAIKA’

Gumzo likateka vichwa vya habari za magazeti Tanzania. Kila mtu akastaajabu nchini kwa kesi ambayo hakuna aliyewahi kuifikiria hususani waumini wa kutupwa wa kanisa la mchungaji Ndimbo Masizi.

Siku hiyo ikawa siku ya kwanza kufikishwa Mahakamani watuhumiwa watatu wakiongozwa na mtuhumiwa Ndimbo Masizi.

Siri zake nyingi zikafichuka baada ya upekuzi wa kutosha uliofanywa na jeshi la Polisi kukuta vithibitisho vingi vya kumtia hatiani.

IGP Mukan Mukazabe akazungumza na vyombo vya habari baada ya upekuzi mkali wa vijana wake kukusanya vielelezo vya kutosha vilivyomtia hatiani Ndimbo Masizi na dereva wake Chikala Gumbo pamoja na Chox ambaye naye akahamishiwa Dar Es Salaam kuhukumiwa pamoja.

Mwanasheria Neema Hussein akaungana na mumewe kuhakikisha haki inatendeka kwa Izani Nteze, wakisimama kama wanasheria wake waliojitolea kuhakikisha naye anafaidika kupitia kesi ile baada ya kuharibiwa maisha yake na mipango yake mizuri.

Hali ya Izani ilianza kuleta matumaini baada ya kumbukumbu zake kuanza kurejea na kuweza kuzungumza kilichotokea mpaka anasingiziwa kesi ya wizi ambayo hakuitenda.

“Waliniteka…Wakanitesa…Wakanichoma sindano za madawa mara kwa mara mpaka nikawa sijikumbuki….” Izani akafunguka huku machozi yakimtoka. Mkasa wake ulimgusa mpaka muheshimiwa Rais na viongozi wengine wa serikali.

Watu walilaani baada ya kuujua ukweli ambao wengine uliwatoa machozi kumuona na kumsikia Izani akizungumza hadharani mbele ya vyombo vya habari kwa mara ya kwanza. Wengi wakakiri kweli Ndimbo Masizi ni Shetani Mwenye Sura ya Malaika. Na kila aliyekiri hilo akawa Mfuasi mpya wa Izani Nteze.

“Natoa agizo kwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama kuhakikisha pia wanachunguzwa wachungaji wote waliokuwa na urafiki wa karibu na Ndimbo Masizi pia nawaonya viongozi wa dini zote na kuwaomba wasitumie jina la Mungu kama kivuli cha kuficha maovu yao. Serikali yangu haitatazama hilo endapo utabainika muhalifu. Nawaomba sana na kuwakumbusha jamani tumuogope Mungu.”

Nukuu hiyo ikanukuliwa kwenye akaunti ya Twitter ya Rais wa Tannzania.

Kesi ya Ndimbo ilipotajwa kwa mara ya kwanza pale mahakamani ndipo Lululu akamtokea kichawi mchungaji Ndimbo Masizi akaanza kuweweseka mbele ya halaiki.

“Msiniue tafadhaliii…Nisamehe Lululu nimeangamia…Aaah” Ndimbo akapayuka na kumshangaza hata Hakimu. Kile alichokuwa anakiona hakuna mwengine aliona.

“Umeshindwa kuwa mtiifu Ndimbo. Umesababisha matatizo na sasa utaenda kuteseka na kutumikia katika ulimwengu wetu.” Lululu akasema huku akimchoma kisu cha kishetani Ndimbo Masizi kwenye moyo na kuanza kumvuta kimazingara bila waliokuwepo kung’amua zaidi ya kumshuhudia Ndimbo akianguka kizimbani.

Mahakama ikashangaa kuona mtuhumiwa Ndimbo Masizi akianguka huku amejishika moyo baada ya kuweweseka. Ikabidi zifanyike huduma za kumsaidia haraka na kesi kuhairishwa huku watuhumiwa wengine wakirudishwa rumande.



* *

Hatimaye Mchungaji Ndimbo Masizi akafariki akiwa anakimbizwa hospitali ambapo walipompima wakagundua amekufa kutokana na mshtuko wa moyo. Ingawa katika uhalisia muda huo Ndimbo alikuwa katekwa kichawi na kufikishwa kwenye himaya ya mateso makali na kutumikia ambayo ilikuwa chini ya Dokta Zongo na magwiji wenzake wa kishetani kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu.

Msiba mwengine ukamkuta mama Anita. Msiba ambao haukuwa na mvuto wa upendo. Waandishi wa habari na polisi wakawa wengi msibani kuliko waumini wa kanisa na raia wema. Ndimbo Masizi hakuzikwa kwa heshima ile aliyojitengenezea akiwa hai. Ingawa pia katika uhalisia kilichozikwa hakuwa Ndimbo Masizi ila ni kiini macho tu! Ndimbo akabaki kwenye kifungo cha mateso ya kishetani ambapo huko alipigwa muhuri wa mateso mpaka kifo cha kweli kitapomkuta.

Kesi ya Chikala na Chox haikucheleweshwa ilipotajwa mara pili na hukumu ikatolewa baada ya ushahidi kukamilika wote wakakutwa na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka thelathini kila mmoja.

Kisa Kabeby akakimbia na kuutelekeza Mgahawa baada ya kuhofia asije kujumuishwa kwenye kesi.

Yule Mkuu wa Kituo Mtamba akakutwa na hatia baada kuchunguzwa na Takukuru akashtakiwa kwa kosa la kupokea rushwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka miwili bila dhamana.

Koplo Ponda akapandishwa cheo kikubwa zaidi ya mwanzo alipokuwa jijini Dar. Akaapishwa na kuvishwa nyota moja iliyomtambulisha kuwa Isnpekta Msaidizi wa Polisi na kupewa kituo cha Mtamba kuwa mkuu wake mpya.

Izani Nteze akapelekwa nje ya Nchi na ofisi ya Rais kwa matibabu zaidi wakati nafsi ya Anita ikifunguliwa rasmi milango ya ulimwengu wa nafsi na kupokewa mahala pema alipoungana na nafsi nyengine njema.

Ndoa ya Zuberi Mwanahaki na Neema Hussein ikarejea kwenye amani na utulivu wake. Mawasiliano yao na Izani aliyefikishwa Marekani kwa matibabu yakawa yanaendelea kila siku kwa njia za video calls.

Kanisa la Ndimbo Masizi likachomwa moto na watu wasiojulikana na hata mama Anita akahofia kuendelea kuishi jijini na kuamua kurejea kijijini kwao akiwa na watoto wake Papii na Doris.

Huko akaamua kujikabidhi mbele ya Kristo kwa imani akisoma biblia na kuwahimiza watoto wake waishi kwa kumtegemea Mungu wala wasije kubabaishwa na tamaa za ulimwengu watapokuwa wakubwa.

(SIKU CHACHE BAADAE)

TANDALE - DAR ES SALAAM

“Samahani kaka Zomboko. Nataka kufanya kipindi na wewe. Jina lako limeombwa na wadau wengi wa Habari za Kitaa waliokusikiliza siku ile.” Markus Makata akazungumza baada ya kufika kwa mara nyengine uwanja wa Fisi kwenye saluni ya Zombi Zomboko, ambayo sasa aliibadili jina kutoka ZOMBOKO HAIR CUTTING SALOON na kuwa MFUASI HAIR CUTTING SALOON

“Unataka kunihoji au unaomba?” Zomboko akajibu kwa sauti kavu huku akimtazama Markus ambaye siku hiyo aliongozana na timu nzima ya kipindi chake waliofika na gari yao ndogo ya ofisini.

“Ok, samahani…Naomba!” Mark akajibu huku akishusha pumzi.

“Anhaa! Sawa, Je, nawe ni shabiki wa Izani Nteze?” Zomboko akauliza.

“Hapana…” Mark akajibu

“Ila,,,,” Zomboko akasema huku akimtazama Mark na timu aliyokuja nayo ambao walisimama nje wengine wakiwa wamebeba kamera kwaajili ya kuwaonesha watu wa mitandaoni.

“Mimi ni Mfuasi wake Izani Nteze.” Markus akajitambulisha.

“Weeh Hahahahahaaa Karibu sana Mfuasi mwenzangu.” Zomboko akacheka kwa mara ya kwanza Markus naye akacheka na hata alioongozana nao wakatabasamu na amani ikanyanyuka mioyoni mwao. Wakaandaa mazingira kwaajili ya kipindi ambacho sehemu kubwa ya nchi siku hiyo waliwasha redio kumsikiliza Zombi Zomboko ambaye kwa mara ya kwanza kwenye kipindi cha siku hiyo akajitambulisha hewani huku akirekodiwa na video kuwa naye ni MFUASI wa Izani Nteze na anamsubiri kwa hamu ataporejea kuendeleza mapambano ya vita vya uraibu na utumiaji wa dawa za kulevya
MWISHO
Shukrani mwandishi kitu konki mno kunya savanna ya barid
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom