Riwaya: Lidake tena chozi langu

Riwaya: Lidake tena chozi langu

mzaramo

JF-Expert Member
Joined
Sep 4, 2006
Posts
6,371
Reaction score
5,191
MTUNZI: George Iron Mosenya

TUNUKIO!

Simulizi hii ni maalumu kwa kila mtanzania na yeyote anayezungumza na kukisikia Kiswahili. Simulizi hii iondoke na mawazo finyu uliyonayo kuhusu walemavu
wa ngozi yaani Albino. Ufungue moyo wako iruhusu na
akili yako kubadilika sasa!! Badilika wewe mbadili na
mwenzako!!

George Iron Mosenya!!!

SEHEMU YA KWANZA
Mungu akulaze pahala unapostahili Judith!! Najua
wazi kuwa laiti kama ungekuwa hai leo hii basi huu
ungekuwa wakati wako wa kupoteza uhai kutoka na
uchungu ambao ungepitia. Uchungu uleule uliokuwa
ukipitia tangu tulipokuwa watoto wadogo, wanmafunzi
waliponiita kwa jina baya kabisa la Zeruzeru
ulichukizwa na licha ya kwamba ulikuwa msichana
ulijaribu uwezavyo kunipigania na mara nyingi
ulishinda. Walipokushinda kwa nguvu uliwashinda kwa
maneno!!
Laiti kama wangepatikana watetezi mia moja kama
wewe Judith huenda pasingekuwa na simulizi hii.
Naam! Ingetoka wapi sasa wakati pasingekuwa na
tofauti kati yetu sisi Albino na wenzetu wanaoamini
wamebarikiwa na Mungu anawapenda sana kwa
kuwapa ngozi hizo!!
Mungu hana upendeleo hata kidogo jama!!
Alivyokuumba hivyo usijihesabia kuwa wewe ulipendwa
zaidi, kamwe Mungu haumbi kiumbe asichokipenda!!
Looh! Judith ulikufa mapema sana Judy!! Ulikufa
wakati ule hata mauaji haya hayajawa kitu cha
kawaida!!
Ninapoyasimulia haya naamini roho yako ipo hapa
ikitiririkwa machozi na kutapatapa kwa hasira kali!
Nayasimulia haya kwa kuanza na jina lako Judy.
Naamini Judy ulikufa wakati ambao haukustahili
kufa!!
Eti ulikufa kwa homa kidogo tu mara ikawa homa kali
na hata hospitali hukufika!!
Nimeanza nawe Judy katika simulizi hii!!
Mungu aipumzishe nafsi yako pema lakini walau
aiamshe sasa na kuipa nafasi ya kuisikiliza simulizi hii
mwanzo hadi mwisho!!
Nakupenda Judy!!!
*****
Mnamo mwaka 1996 nikiwa darasa la kwanza ndio kwa
mara ya kwanza kabisa nilipiotambua kuwa palikuwa
na tofauti kati yangu mimi na watoto wengine pale
darasani.
Mama yangu hakuwahi kuniweka wazi kuwa nilikuwa
nina tatizo la ugonjwa wa ngozi lakini shule ilinuipa
majibu!!
Shule nzima ni mimi pekee nilikuwa albino.
Nilikuwa sina rafiki hadi pale alipohamia shuleni kwetu
msichana aliyeitwa Judith!!
Sijasahau kitu hata kimoja katika simulizi yangu,
miaka saba niliyokuwanayo inatosha kabisa kukumbuka
kila kitu.
Ninakumbuka hadi maonyo ya mama yangu, kuna
kipindi aliwahi kuniita na kuzungumza nami!!
Alinieleza kuwa kuna fununu zinatapakazwa na
imekuwa mazoea kabisa kuwa eti ni jambo la kawaida
kabisa kwa Albino kupotea hasahasa ukifika wakati
wao wa kuaga dunia!!
Naikumbuka sauti ya mama ambaye alinieleza kuwa
baba yangu alimkimbia baada tu ya kunizaa mimi
nikiwa albino!!!
“Mwanangu Majaliwa nilimuomba Mungu sana na
Mungu hadanganyi kamwe, Mungu akanijibu kuwa
alinipatia mtoto na huyo mtoto ni wewe. Wewe ni
mwanadamu kama wanadamu wengine, Majaliwa!!
Nilikuwa jasiri sana baba yako alivyonikimbia na wewe
jifunze kuwa jasiri pale ambapo watu watakukimbia.
Nitakusimamia mwanangu, utasoma hadi utamaliza
chuo kikuu sawa mwanangu”
Naam! Sijaisahau sauti ile ya mama, sauti
inayozungumza katika masikio yangu hadi leo hii!!!
Yale maneno ya mama yakaanza kutimia, wanafunzi
wakaanza kunitenga. Wakajiweka mbali nami kasoro
Judith tu!!
Naumia sana msikilizaji, naumia kwa sababu Judith
alikufa akiwa bado namuhitaji sana!!
Ila nisilalamike sana isijekuwa nafanya kufuru!!!
Nilifanikiwa kumaliza darasa la saba na kuchaguliwa
kujiunga kidato cha kwanza!!
Nilikutana na changamoto zilezile…. Lakini kwa
kutoka kwa wanafunzi hazikuwa na matatizo kwangu
kwa sababu mama alikuwa akinitia moyo kuwa
wananichukia kwa sababu nilikuwa na uwezo mkubwa
sana darasani kuwazidi.
Maneno ya mama yalikuwa yakiniimarisha sana!!
Lakini sikuweza kuwa imara pale mwalimu wangu wa
darasa siku ile nimechelewa kufika darasani wanafunzi
wakiwa kimya kabisa akanitamkia maneno ambayo kwa
mara ya kwanza yalianza kunipa mashaka katika
maisha yangu na hapo nikaitazama ngozi yangu mara
mbilimbili. Hadi ninaposimulia haya nakiri kuwa
sijawahi kumsamehe Yule mwalimu!!!
Yule mwalimu aliniambia kwa dharau kubwa kabisa.
“Jichunge sana kuchelechelewa huku watu
tunakutafuta sana wewe tuepukane na haka
kamshahara kadogo ka ualimu!!” maneno yake
yaliniingia na nikayashika kama yalivyo.
Yalikuwa maneno magumu kuyaelewa na mama alikuwa
ameniambia kuwa kila nikiambiwa maneno
nisiyoyaelewa nisiste kumweleza. Nikaenda kumweleza
mama kauli ile ya mwalimu wangu!!
Mama alihema juu juu, akajaribu kuongea hakuweza,
akabaki kutupa mikono huku na kule…. Neno pekee
aliloweza kutamka ni ‘yaani….. yaani…’ hakuweza
zaidi akaanza kulia. Ni hapo nikatambua kuwa kauli ya
Yule mwalimu ilikuwa kauli mbaya.
Mama hakulilazia damu, siku iliyofuata tukaenda wote
shuleni hadi kwa mkuu wa shule!!
Akamweleza mashtaka yale!!
Ajabu mkuu wa shule hakuonekana kushtuka!!
Akamtazama mama kasha akamuuliza.
“Mwanamke ni hili tu limekuleta?”
Mama akabaki kushangaa. Yule mwalimu akaendelea
tena.
“Mama tena bora umekuja mwenyewe, kwa sababu
nilikuwa nimepanga kukuita!! Na ninapenda kutoa
onyo mbele ya mtoto wako, mama hapa shuleni ni
mtoto wako pekee ambaye ana hali hii… sasa
nakwambia mama ni ama umtafutie uhamisho lakini
ikitokea shule yangu inapata matokeo mabovu basi
utanijua mimi ni nani??” alizungumza kwa ghadhabu
kasha akatoka nje na kutuachia ofisi.
Nilimtazama mama yangu akiwa na kanga yake
iliyochakaa akikosa la kufanya. Akageuka na
kunitazama nikayaona machozi yakimtoka mama yangu
ambaye alikuwa yu mweusi kabisa si kama mimi.
“Majaliwa mwanangu, Mungu ananiweka hai hadi sasa
ili nikulinde, kama baba yako mzazi alikukataa watu
baki kama hawa wanashindwa nini kukukataa, shule
zipo nyingi mwanangu na hawa wanakuchukui kwa
sababu tu una akili kuwazidi. Utasoma mwanangu
utasoma!!” alizungumza mama huku nikimsikia kuwa
alikuwa analia!!
Chozi la mama likanidondokea katika utosi wa kichwa
changu, likanisisimua nami kujikuta ninatokwa na kilio
huku nikimkumbatia mama yangu kwa nguvu zaidi!!!
Mwalimu mkuu akafika na kutuamrisha tutoke ofisini
kwake!!
Siku iliyofuata sikwenda shuleni bali niliongozana na
mama hadi kwa mkuu wa wilaya. Mama akajieleza
vyema kuhusu maneno makali ya mkuu wa shule na
Yule mwalimu wa darasa.
Mkuu wa wilaya hakuwa muongeaji sana. Akaandika
barua na kuifunga katika bahasha na kisha
akamwambia mama kuwa siku inayofuata aifikishe
barua shuleni.
Barua ile ikawa mwisho wa mwalimu mkuu ya Yule
mwalimu mwenzake kunitamkia maneno mabovu!!!
Hadi namaliza kidato cha nne hapakuwa na matatizo
sana na hiyo ilikuwa ni mnamo mwaka 2006!!
Ilikuwa heri nikachaguliwa kujiunga kidato cha tano.
Nikachagulia kwenda shule iliyopo kanda ya ziwa!!
Siichukii kanda ya ziwa hata kidogop na ninawapenda
sana watu wa kanda ya ziwa hadi ninapousimulia
mkasa huu lakini napenda kuwaeleza waziwazi bila
kificho kuwa ni hapohapo kanda ya ziwa mikono ya
albino wenzangu ilikatwa, sehemu zao za siri zilikatwa
tena bila ganzi, naumia sana naumia kwa sababu
niliona kwa jicho langu!!!
Niliona miguu ikikatwa, nilipata bahati mbaya zaidi
kushuhudia jicho la mwanadamu ambaye hajakata roho
likinyofolewa!!
Walionyofoa walikuwa wakitabasamu na bila shaka
walijiona watu waliobarikiwa sana kupata bahati ile ya
kuvipata viungo vya albino!!!
Zikipitishwa sura zao hapa hao wauaji hata wawe
wamezeeka vipi naapa kwa jina la Mungu
aliyeniumba….. naapa nitawakumbuka!! Akili yangu
haijawahi kuwasahau!!!
Kanda ya ziwa iliimeza damu ya wenzangu wengi tu!!!
Siichukii kanda ya ziwa lakini walaaniwe waliothubutu
kututenda vile!!!
Ni huku nilipochaguliwa kujiunga kidato cha tano na
cha sita!! Nilikuwa sina wasiwasi lakini mama yangu
alikuwa na mashaka tele. Aliniambia kuwa nilikuwa
nimekomaa akili basi nijifunze jinsi ya kujilinda!!
Nilikuwa muoga sana kuchinja kuku, mama
akanilazimisha niwe nachinja kuku. Nilipomuuliza ni
kwanini ananilazimisha alinifokea.
“Yaani wewe wanaweza wakatokea majambazi hapa
wakanipiga halafu wewe una kisu ukashindwa
kupambana nao”
Hayo yalikuwa ni maneno ya mama yangu mzazi!!!
Maneno ambayo ilifika siku nikaijua maana yake!!
Kumbe mama hakutaka tu kuniambia waziwazi kuwa
wapo watu wabaya sana duniani!!
Kule Kanda ya ziwa, nasikitika kuwa sitautaja huo
mkoa moja kwa moja. Sihitaji uuchukie mkoa ule bali
wachukie wale wauaji!!
Nilisoma pale kidato cha tano nikamaliza salama
kabisa, mama alijitahidi kuniandikia barua mara kwa
mara na ikafikia hatua akanunua simu yake ya kwanza
ya mkononi kwa ajili tu ya kuwasiliana na mimi.
Alinisihi sana niishi kwa tahadhari. Maneno ya mama
yalijikita katika kichwa changu vyema.
Kitu kibaya ni kwamba sikuona nini maana ya zile
tahadhari sasa ikiwa sijaona baya lolote likikaribia
kunitokea.
Amakweli mdharau mwiba mguu huota tende asilani!!
Na ni heri nusu shari kuliko shari kamili.
Nilipomaliza kidato cha sita nikajiona ya kuwa mimi
nimekuwa mtu mzima. Ile kujichanganya na watu
wasiokuwa na ulemavu kama mimi nikajiona nipo sawa
kabisa. Sikujua hata kidogo kuwa baya hujificha
likisubiri ukosee maelekezo ndipo liibuke.
Maisha magumu ya mama yangu yakanifanya nijione
mpuuzi sana kuendelea kukaa nyumbani nikiyasubiri
matokeo ya kidato cha sita. Mama hakuuchukulia
uwepo wangu nyumbani kama tatizo badala yake
alifurahia kuwa amekuza mtoto.
Maneno ya marafiki yakaanza kuibomoa akili yangu,
wakanisifia kuwa nilikuwa najua sana somo la hesabu
hivyo nitafute shule niwe nafundisha kwa muda ili
nimsaidie mama yangu.
Nilipomwambia mama akanipinga vikali sana
akaniambia nikae nyumbani.
“Majaliwa mwanangu wewe ndiye mwanangu wa pekee,
tangu baba yako anikimbie unajua wazi kuwa sijawahi
kuolewa tena. Kaa mwanangu tutakachopata tutakula
pamoja, bado unahitaji uangalizi wangu majaliwa we
kaa tu usijali!!” mama alinisihi lakini sikuelewa
nikalazimisha hatimaye akakubali.
Sikuwa na ujanja wa kutafuta shule mimi mwenyewe,
wale marafiki wakanieleza kuwa yupo mtu ana shule
yake anahitaji waalimu. Wakampatia mtu Yule namba
ya mama ili waweze kuwasiliana naye niweze kwenda
kufundisha shule yake!!
Sitazisahau nyakati hizo kamwe!!!
 
SEHEMU YA PILI

MAMA alipigiwa simu na watu hao asiowaelewa
wakajitambulisha kwa majina yao na vyeo vyao
walitaja vyeo vigumu vigumu ambavyo mama hakuweza
kuvishika ipasavyo!!
Wakadai kuwa sifa zangu wamezisikia kutoka mbali
wakaitaja shuleni niliyokuwa nasoma.
Na hatimaye wakamweleza mama kuwa wanahitaji
kufanya kazi na mimi!!
Wakati huo wote nilikuwa pembeni nimejilaza katika
bega la mama yangu nikizichezea nywele zake mbele
palikuwa na mafiga tukiwa tunaota moto.
Mama aliwauliza maswali mawili matatu kubwa
aliwauliza juu ya usalama wangu, wakamtoa hofu
kabisa kuwa kama itakuwa vyema basi mwakilishi wao
anaweza kufika nyumbani. Kisha wakaongezea kuwa
hata wao wanaelewa changamoto ambayo inalikabili
taifa letu kuhusiana na watu wenye ulemavu wa
ngozi!! Yaani albino!!!
MANENO yao yakamlainisha mama akawakaribisha
nyumbani!!
Wakaahidi kufika baada ya siku mbili.
Kweli ugeni wa wanaume wawili nadhifu kabisa ukafika
nyumbani kwetu baada ya hizo siku mbili.
Walikuwa wachangamfu sana na kwa kiasi kikubwa
walikuwa wanaonekana kujali sana, wakanishauri
mambo mengi sana huku wakimpongeza mama yangu
kwa kunizaa kunilea lakini kubwa zaidi kwa kunilinda
hadi umri ule niliokuwanao.
Lugha zao zilikuwa nadhifu kama wao, walipoondoka
wakamuachia mama kiasi cha shilingi elfu thelathini!!!
Mama akatabasamu huku akizipokea pesa zile.
Tabasamu lile likamaanisha kuwa alikuwa amekubali.
Ama kwa hakika usilolijua lina tofauti gani sasa na
usiku wa kiza kinene!!!
Naam! Tulikuwa gizani!!
Baada ya siku tatu wale watu wakafika na kunichukua,
nilipofungasha mzigo wangu mdogo ndipo nilipogundua
kuwa nilikuwa nampenda sana mama yangu
nilimkumbatia na nikayasikia maneno yake mengine.
“Fanya kazi mwanangu uheshimike, ukishakuwa na
pesa watajifanya hawaioni tofauti yako na hatimaye
sote tutakuwa sawa. Wewe si shetani, wewe si mchawi
wewe si jini Majaliwa, wewe ni mwanadamu.
Uliwakomesha shuleni wao waliongea wewe ukatenda,
sasa ni wakati wa wewe kufanya kazi kwa bidii
watakaa kimya tu!! Laiti ningekuwa na uwezo kifedha
nisingekuruhusu uondoke mwanangu, ningebaki kuwa
mlinzi wako daima. Ila sasa namuachia Mungu…
akulinde uendapo awe nawe daima!!!” alipomaliza
kuzungumza yale akaniachia kisha akanisogelea na
kunibusu shavuni kisha akanibusu paji langu la uso!!!
Sikujua kabisa kuwa mama alikuwa ananiaga,
ninapokusimulia haya natamani siku zingerejea nyuma
tena na kamwe nisikubali kuandamana na watu wale
huku nikiwa tayari kuwa mbali na mama yangu.
Mwanadamu mwanadamu mwanadamu!!!
_____
Tuliondoka na siku ile nililala hoteli nzuri sana,
nilijitazama na kuyaona matunda ya kusoma kwangu
yaani elimu ya kidato cha sita tu tayari nimeshaanza
kuheshimika!!
Lilikuwa jambo la kupendeza sana.
Nilifurahia hali ile ya kutukuzwa nikayakumbuka na
maneno ya mama na kujiapiza kuwa nitafanya kazi
kwa bidii sana hadi niheshimike.
Nililala huku nikiwa nina furaha kubwa!!
Asubuhi tuliianza safari kuelekea kanda ya ziwa.
Tulikuwa katika gari binafsi lakini safari hii nilikuwa
na watu wengine tofauti kabisa.
Wale wawili wa awali walidai kuwa wana mkutano na
waalimu wengine hivyo nitangulie na watu wale.
Safari ilianza vyema!!
Nilikuwa mkimya nikiwatazama tu wenyeji wangu
wakibadilishana mawazo, tulizidi kuchanja barabara
nikiwa natamani tufike upesi. Nilipata nafasi ya
kuwaza juu ya mshahara wangu wa kwanza kabisa.
Nilipanga mshahara wote nimpatie mama yangu, na pia
niliwaza kununua simu yangu ya kwanza ili niwe
nazungumza na mama yangu.
Yalikuwa ni masaa kadhaa tu tangu niachane naye na
tayari nilikuwa nimeukosa uwepo wake kwa hali ya juu
sana.
Baadaye mwendo wa gari ukawa unapungua na
hatimaye gari lilipaki pembeni. Wakaanza kujadiliana
juu ya ubovu wa gari lile!!
Niliwasikia wakizungumza na kwa mbali nikazisikia
dalili za kulala njiani.
Nilitamani isiwe kama nilivyowasikia lakini ilikuwa vile
ilikuwa hakuna safari iliyokuwa inaendelea pale
tulitakiwa kulala kwa sababu hapakuwa na namna
yoyote ya kufanikisha safari ile. Nilitamani kusema
neno ambalo lingeweza kubadilisha maamuzi yale lakini
sikuwa na neno lolote la kushauri, sikuwa najua
jambo lolote lile kuhusiana na magari.
Basi kwa shingo upande nikajipa moyo kuwa kila jambo
huja kwa sababu maalumu huenda tungesafiri usiku
ule tungeweza kupata ajali ama lolote baya.
Nikiwa nasubiri kupewa utaratibu nikaona si mbaya
ikiwa nitaanzisha maongezi walau niijue sehemu
ninayoenda niyajue mazingira ya kule ili niwe tayari
nikifika nisionekane mgeni sana.
“Aah! Samahani kaka hivi hiyo shule kuna wanafunzi
wengi eeh!” nilimuuliza. Hakunijibu upesi badala yake
alikuwa kama anayenishangaa.
Nikauliza tena nikidhani hajanisikia vizuri.
Badala ya kunijibu akanitupia swali.
“Unaitwa nani?”
“Naitwa Majaaliwa kwani hawakuwaambia jina langu,
hawakuwaambia kama mimi ni mwalimu naenda
kufundisha somo la hesabu?” niliwauliza katika namna
ya kuwashangaa.
Badala ya kunijibu niliona wawili wakivutana pembeni
na kuanza kuteta sikujua walilokuiwa wakizungumza.
Baada ya dakika kama moja hivi wawili wakarejea na
kunikabili.
“Aaah! Umesema unaitwa Mwalimu Majaaliwa, sasa
tuna tatizo la gari na inabidi tulale tu njiani hadi
kesho tena kuna kifaa tumeagiza kitafika asubuhi
hivyo tutaendelea na safari.” Alizungumza bwana yule
nami nikatikisa kichwa ishara ya masikitiko.
Baadaye kiza kilivyotanda kabisa tukapangiana namna
ya kulala.
Kiuwazi kabisa ilionekana kuwa tusingeweza kulala
katika gari lile. Basi ikaletwa hoja ambayo
ilinifadhaisha sana, hoja ambayo ndani yake ilionyesha
kutengwa!!
“Sasa Majaaliwa kama unavyojiona wewe una
matatizo, tumekutafutia hifadhi hapo kijiji cha jirani
utalala hapo na asubuhi tutakutana hapa. Haiwezi
kuwa salama kabisa kulala katika eneo hili sawa!!”
hakusubiri nitoe jibu lolote akamchagua bwana mmoja
akanishika mkono tukaondoka huku nafsi ikiwa
haijaridhia kabisa.
Hakika tuliifikia nyumba moja nikakaribishwa na kisha
kupewa maji nikaoga na baada ya hapo nikapatiwa
chumba ambacho nilitakiwa kulala.
Katika chumba kile alikuwa amelala mtoto mdogo kama
miaka sita ama nane kimakadirio.
Nilijilaza kitandani, nikajaribu kusinzia lakini usingizi
haukukubali kabisa. Nikajaribu kujigeuza bna hapo
nikajikuta nimemuamsha yule mtoto.
Pale ndani kulikuwa na mwanga kiasi fulani kwa sababu
ile ilikuwa ni nyumba isiyoezekwa vyema basi
mbalamwezi ilipenyeza mwanga wake.
Kile kitoto kikaamka na kupekecha macho yake kisha
kikaketi!!
“Shkamoo mzungu!!” kikanisalimia… hata kabla
sijajibu kikaendelea.
“Halafu wewe jana ulinidanganya ukasema utarudi
haujarudi, haya machungwa yangu nataka!!”
Nilimtazama nikahisi itakuwa ni ndotoni tu.
“Haya lala kesho ntakupa!!!” nilimweleza nikidhani
atalala. Haikuwa hivyo mtoto alikuwa anajitambua
kabisa.
“Halafu mzungu lile swali lako lile nimeliweza sasa..”
akazungumza huku akishuka kitandani akaenda na
kuchukua mfuko wake. Akatoa daftari, kweli nikakuta
kuna swali alikuwa ameandikiwa na alikuwa amejaza
jibu.
Hisia bado zilikuwa mbali kufikiria kuwa yule mtoto
kuna kitu cha msingi sana nilitakiwa kujua kutoka
kwake.
“Yaani nyie mkiondoka hamrudi, halafu waongo nyieee
we jana ulinidanganya wewe ni mwanamke huyoooo
nimejua!!” mtoto aliongea huku akiwa
ananichungulia.
Hapa akili ikasogeleana kuwa siku iliyopita ama hata
kama sio siku iliyopita basi siku kadhaa nyuma kuna
msichana ama mvulana mlemavu wa ngozi aliwahi
kupita na kulala pale.
“Mimi mwanaume bwana…..” nilimwambia.
“Sasa mbona uliniambia wewe mwanamke sijui wewe
mwalimu unaenda shuleni huko. Tena … tena ehee
ngoja…” kakaruka kale katoto na kufukua nguo zake
akatoka na picha.
Naam!! Ilikuwa picha ya msichana mwenye ulemavu wa
ngozi!! Kama mimi.
Moyo wangu ukapiga kwa nguvu sana.
Wale jamaa waliniambia kuwa pale shuleni hakuna
mwalimu mwenye ulemavu wa ngozi tena wakasema
mimi ndio wa kwanza kabisa sasa ile picha ilikuwa na
maana gani!!
Sikutaka kuionyesha ile hofu waziwazi kwa mtoto yule
nikajilazimisha kutabasamu lakini moyo wangu ulikosa
amani kabisa na hakika nisingeweza kulala pale.
Lakini hata kama nisingelala pale ningeenda kulala
wapi, walau basi yule angekuwa ni mtu mzima
nimuombe ushauri tatizo yule alikuwa ni mtoto mdogo.
“Kwa hiyo huyu dada yupo wapi?” nilimuuliza.
“Alinitoroka nikiwa nimelala huyo.” Kalinijibu huku
kakiwa kanalegeza macho yake ishara ya usingizi.
Na baada ya jibu hilo kikasinzia kitoto kile.
Nilisimama na kuanza kutapatapa pale ndani sikujua ni
wapi ambapo naweza kukikmbilia machale yalikuwa
yamenicheza kulikuwa na sintofahamu.
Nilitambua kuwa iwapo nitaamua kulala basi hii
inamaanisha kuwa nikiamka nitakuwa katika wakati
mbaya zaidi.
Nikaufungua mlango taratibu kabisa. Nikatazama
huku na kule eneo lilikuwa tulivu sana.
Nikapiga hatua mbele na kisha nikazitazama anga
nikamwomba muumba wangu.
Nilimwambia neno moja tu.
“Baba ulinipa uhai ukazijaza pumzi katika mwili huu
ukaupa na ulemavu, baba wewe hukosei katika kuumba
baba uliamua ile roho na pumzi kuziweka katika mwili
huu. Mwili wako upo matatani baba wanaitaka roho
yangu!!! Nipiganie sasa…”
Wakati namalizia kusema hayo mara nikasikia mbwa
wakibweka.
Nikafanya kosa nikajaribu kukimbia!!
Mbwa wawili wakawa wananibwekea huku
wakinikimbiza kwa kasi sana.
Nilianza kukimbia na kamwee nisijue ni wapi naelekea
na niliwasikia mbwa wakizidi kukikaribia.
Kwa mujibu wa saa yangu ya mkonomni ilikuwa yapata
saa nane za usiku. Katika kijiji nisichokijua kabisa!!!
 
SEHEMU YA 3

MBWA walizidi kunikimbiza na wala sikupiga hatua
nyingi zaidi NIKAJIKUTA napiga mweleka chini. Mbwa
walikuwa wamenifikia, mbwa mmoja aliyekuwa mkubwa
zaidi alinikwangua na makucha yake katika paja langui
nilipiga kelele kuomba msaada maana kukaa kimya
ningeweza kujisababishia balaa zaidi.
Ni heri ningekaa kimya!!
Lakini ningekaa vipi kimya wakati mbwa walikuwa na
lengo moja tu la kunidhuru!!
Nilivyopiga kelele wakazi wa ile nyumba niliyokuwa
nimepelekwa kulala wakatoka nje upesi.
Lahaula!! Walikuwa ni watu walewale ambao tulikuwa
katika safari moja kutokea mjini tulipoachana na wale
wageni wawili walionichukua kutoka katika mikono ya
mama. Walionilaghai kuwa wao watalala garini na mimi
wanaenda kunilaza sehemu salama!!
Hapo sasa nikakiri katika nafasi yangu kuwa hisia
zangu zilikuwa sahihi kabisa.
Nikabaki pale chini wakati wale watu wakijongea
kunikaribia.
“Mzunguu!!” nilisikia sauti ya kale katoto. Kalikuwa
kameamka pia kakiwa uchi.
Aliponiita vile akakoromewa na wale wenyeji wangu
ambao awali walisema kuwa watalala garini na mimi
nilale katika nyumba ile.
Kumbe sote kwa pamoja tulikuwa tumelala nyumba
moja!!
Hawakusema nami jambo lolote badala yake niliwasikia
wakihamasishana kuwa wafanye upesi.
Wakafika na kunibeba kisha wakaniingiza ndani, na
hapo jamaa mmoja akaanza kuwatukana wenzake
akiwaambia kuwa wameharibu dili.
Sikujua ni dili gani walilokuwa wakizungumzia lakini
amani sikuwanayo tena.
Mbaya zaidi wale watu hawakuniuliza lolote kuhusu ni
wapi nilikuwa naenda usiku ule.
Hali hiyo ilinifanya niumie sana nafsi na kujisikia kama
nusu mfu!!!
“Mpake dawa fasta!!” aliamrisha tena yule bwana.
Nikapakwa dawa iliyokuwa inauma sana. Nilijikazaa
lakini sikuweza nikapiga kelele. Hilo likawa kosa kubwa
sana.
Nikapigwa kibao kikali sana usoni ulikuwa ni usiku
hivyo niliziona nyotanyota vizuri.
“Mpumbavu mkubwa wewe…” alinifokea yule bwana
wakati huo niliyasikia macho yangu yakichonyota na
hatimaye chozi likanitoka!!
Nikayakumbuka maneno ya mama yangu!! Mama yule
alikuwa anaona mbali sana!!
Baada ya tiba ile wakazungumza pembeni kisha
wakanichukua na na kunivuta kuelekea mahali.
Sikujua ni wapi lakini sasa nilikuwa nawasihi
wanisamehe tu bila kujua kosa langu ni lipi!!!
Hawakujibu chochote.
Tulipofika eneo la nyuma ya nyumba bwana mmoja
alinichota miguu yangu. Halafu kwa jinsi
walivyojipanga na kwa namna walivyo na uzoefu
katika shughuli hiyo haramu walinidaka hata sikutua
chini.
Na hapo nikauona mfuko nikalazimishwa kuingia katika
kiroba kile.
Ndugu zangu, ninayokusimulieni haya endeleeni
kuyasikia tu na yabaki katika masikio na akili zenu
lakini kamwe msiyapitie kama nilivyoyapitia. Ni
magumu sana hasahasa kwa mwanadamu ambaye
uliumbwa kwa udongo!!
Sikuwahi kudhani kama ipo siku nitatabasamu na
kukubaliana na hali niliyonayo lakini natabasamu
sasa!!
Wale jamaa walinishika kwa nguvu na ndani ya dakika
moja tu nilikuwa ndani ya kiroba cha chumvichumvi.
Nilipojaribu kupiga kelele jamaa mmoja alinizamishia
soksi kubwa mdomoni. Ilikuwa inanuka sana jamani!!
Lakini iliingia katika mdomo wangu!!!
Na hapo sikuweza kuzungumza na nilikuwa napumua
kwa shida sana!!
Nilisema kimoyomoyo kuwa ile iwe ndoto ya ajabu sana
nizinduke nipige kelele na mama yangu aje kuniuliza
nini kimetokea lakini nilifumba na kufumbua hapakuwa
na ndoto pale!!!
Ilikuwa hali halisi Majaliwa mimi nilikuwa katika
matatizo makubwa sana, nilikuwa mdomoni mwa kifo!!
Licha ya kunijaza soksi ile mdomoni walikifunga kile
kiroba!!!
Wakanibeba nikiwa kama kiroba na safari ikaanza.
Niliumia sana kwa sababu kuna muda walinigusa macho
kuna muda walibinya tumbo. Hakika niliamini kuwa
wakinitoa ndani ya kile kiroba nitakuwa mfu tayari.
Lakini haikuwa hivyo walinifikisha hadi katika gari na
hapo walinifungua.
Waliponitoa na kunitupa nuje ile soksi nayo
ikachoropoka mdomoni.
Nilitapika vibaya mno, nilihema juu juu huku
nikitamani kuongea na sauti haikuweza kutoka!!
Kabla sijakaa sawa walinichukua tena na kunirusha
katika gari jingine. Hapo sasa nilitua kwa kutumia
mdomo, nikaacha kuchuruzika damu!!
Wale viumbe hawakuwa na huruma hata kidogo!!
Walipanda garini na hapo gari likaanza kuondoka,
sikujua hata ni wapi tulikuwa tunaelekea. Lakini njia
ilikuwa mbaya sana nilijigonga huku na kule gari
lilivyokuwa linarukaruka kwenye mabonde,.
Kadri tulivyozidi kwenda hatimaye mwezi ulitoweka na
mwanga ukaanza kutokea. Wale jamaa mwanga
ulivyoanza kutokea wakafunika turubai. Sasa hapo
tukaanza kuteseka na joto.
Ajabu wale wenzangu walikuwa wanaonekana
kutosumbuliwa kabisa na hali ile.
Mimi iliniendesha haswa.
“Jamani kwani ni nini nimewakosea?” hatimaye
nilifungua kinywa na kuzungumza.
Badala ya kunijibu yule bwana akainama na
kunionyesha soksi nyingine.
Nikajua anachomaanisha nikawa kimya.
Lakini katika ukimya ule nilikuwa nikitafakari sana juu
ya kujiokoa. Kwa sababu kuwaacha jamaa katika
utulivu waliokuwanao ilikuwa si sawa hata kidogo. Na
haikuwa njia ya kuniponya bali kunipeleka machinjioni
kirahisi.
Hapa tayari nilikuwa nimetambua ilikuwaje hadi watu
wakawa wanaishi na imani kuwa eti sisi walemavu wa
ngozi tukipoteza uhai huwa tunapotea tu kwa sababu
sio wanadamu wa kawaida!!
Kumbe kuna maharamia kama hawa wanatuteka na
kutuua.
Gari lilivyozidi kwenda nikafanya maamuzi magumu na
nikabaki kusubiri muda tu!!
Hatimaye gari lilipunguza mwendo.
Nikajirusha upesi nikalifunua lile turubai na kutua
nje.
Mungu wangu!! Sikujua kama nilikuwa sehemu mbaya
kiasi kile. Kushoto na kulia lilikuwa ni shimo kubwa.
Hivyo pale palijengwa daraja. Nilibaki nimeduwaa
baada ya kutua chini, ni kweli sikupenda kufa kifo
kibaya cha kukatwa na mapanga lakini hapohapo
sikuwa tayari kujirusha katika shimo lile.
Nikajaribu kukimbia lakini sikufika mbali wale vijana
wepesi wakanifikia na kunikamata hii ni baada ya
kupiga kelele na dereva kusimamisha gari.
Nilitambua fika kuwa nitapokea kipigo kikali sana
lakini haikuwa vile. Dereva aliwakataza kabisa
kunigusa wakanichukua na safari hii wakanifunga
kamba miguuni.
Walinikaza ipasavyo wauaji wale!!
Safari iliendelea kwa mwendo kasi mkali na wakati
mwingine mwendo wa taratibu ama wastani sikujua ni
wapi tunaelekea!
Baada ya safari ndefu tulisimama nikaachwa garini.
Ni wakati huo ambao nilitambua kuwa nilikuwa
nimelalia kitu ambacho kilikuwa kikinichoma sana
mgongoni, nikapapasa ili niweze kukitoa ndo hapo
nikachomoka na kitu kilichonipa mshtuko ambao ulitaka
kuondoka na uhai wangu, yaani muda wote huo wa
kuumia nilikuwa nimelalia kiungo cha mwili wa
mwanadamu.
Ulikuwa mkono na ulikuwa umegandiana na damu
kuonyesha kuwa haukuwa na muda mrefu sana tangu
ulipokuwa umekatwa.
Ndugu msikilizaji uliyebarikiwa kuwa na mikono yako
yote miwili, jitazame sasa itazame mikono yako,
itazame kwa sekunde chache tu kisha fumba macho
yako ujiulize.
Ni maumivu kiasi gani utayapata pale ambapo mkono
huo utakatwa tena kwa mapanga huku ukiwa
unajitazama.
Tumbo liliniuma na kibofu kikajaa mkojo nikajikuta
najikojolea palepale.
Hasira kali sana ilinikaba katika koo langu lakini
ningefanya nini na ile hasira yangu!!!
Nikachungulia nje na kuzitazama mbingu!!
Sikusema neno bali niliamini Mungu wetu halali kamwe
na kila muda yupo kazini nilijua ananiona na unyama
ule hakututuma duniani tuufanye!!!
Niliamini Mungu atajibu!! Lakini hapo hapo nikaingiwa
na uoga mkubwa sana, nikajiuliza mbona wezi wanaiba
hawakamatwi mbona watu wanaua na wanaachwa
hai!!
Inamaana Mungu ataniacha nami niteketekee katika
mikono ya watu wale wabaya!!!
 
Duuuhhh dunia hii mungu tunusuru.bora ukutane n simba klk binadam
 
Inakatisha tamaa kusoma riwaya za humu huwa zinaishia hewani.
 
Inakatisha tamaa kusoma riwaya za humu huwa zinaishia hewani.
 
mimi sio wa aina hiyo mkuu...pitia riwaya nyingine kama MPANGO WA KANDO,RIPOTI KAMILI,HILA NA PUMBAZO zote nilizibandika mimi na zilikuja mwanzo mwisho....tuwe pamoja muone tofauti yangu wakuu
Tutashkuru sana, we ndo Mosenya Mwenyewe? Napenda sana story zake/zako hakuna ambayo sijawahi soma
 
SEHEMU YA NNE
Kitendo cha kuuona mkono wa mwanadamu mwenye
ulemavu kama mimi katika gari kukanitia hofu na
kunifanya nitetemeke.
Nguvu zilizokuwa zimeanza kupotea zilirejea kwa kasi
nikatambua kuwa kuendelea kuwa pale zaidi nilikuwa
nahalalisha kifo changu kwa kukatwa na mapanga
huku nikiwa najioona.
Nilijiuliza juu ya yale maumivu yanayopatikana pale
mtu unapochomwa na mwiba kisha nikayakadiria
maumivu ambayo yanapatikana kwa kukatwa mkono
ama kiungo chochote kile. Hakika sikuhitaji mtu wa
kunijibu swali lile. Hisia zangu ziliniambia kuwa ni
maumivu makali sana!!!
Kufikia hapo nikajisemea kuwa hata katika vitabu vya
Mungu wanasema kuwa jisaidie naye atakusaidia.
Nikajivuta kwa taabu hadi nikaweza kupaona nje hapo
nikaishia kuona hali kama ya jangwa hapakuwa na
kiumbe yeyote yule. Nikarejea ndani kisha upesi
nikaanza kuzifungua zile kamba ngumu zilizokazwa
katika miguu yangu.
Zilikuwa ngumu sana na vile nilikuwa ninaoigopa basi
kila muda nilishindwa kujua ni namna gani ya
kuzifungua. Nilibinua huku ikashindikana nikajaribu
huku sikuweza. Mikono ilikuwa haina utulivu kabisa,
lakini hatimaye nikalipata fundo sahihi nikafanikiwa
kuupata mzunguko ule. Nilijifungua upesi sana huku
nikitambua wazi kuwa wale watu wakinikuta katika
jaribio lile basi nitakuwa katika wakati mgumu sana,
huenda wataniwekea tena zile soksi chafu mdomoni
ama wanaweza kuamua kuniua nitajuaje!!!
Nilipowaza juu ya kuuliwa nikajisikia kutetemeka sana
amakweli hakuna mtu mwenye urafiki na kifo!! Kila
nikigusa kamba mikono ilikuwa inateleza kutokana na
kutetemeka nikajaribu sana kuizuia akili yake isiishi
katika hofu, hatimaye hofu ikapungua kiasi na umakini
ukarejea.
Hatimaye nikafanikiwa kuzifungua na kubaki huru!!
Upesi nikaruka na kutua chini, na hapo nikatambua
kuwa kila pande palikuwa na hali za kufanana, hakuna
sehemu ambayo palikuwa na watu.
Nilifanya patapotea na kuamua kukimbilia upande
nilioamini kwangu mimi kuwa ni upande salama kabisa.
Nilikimbia sana hadi nilipoanza kukutana na mti mmoja
mmoja na vichaka kadhaa.
Baada ya kukimbia sana hatimaye kwa mbali nikaona
kundi la watu. Nikataka kukimbilia katika kichaka ili
niweze kujificha lakini macho yangu yakavutiwa
kutazama watu waliokuwa katika lile kundi.
Nilisimama kama nisiyekuwa na haja ya kujificha tena,
katika lile kundi kuna kitu nilikiona.
Awali sikuwa na uhakika sana lakini kadri walivyosogea
nilizidia kuamini kuwa sikuwa naidanganya nafsi
yangu.
Wazo langu la kujificha likaishia palepale.
Nilikuwa natazamana na baadhi ya watu ambao
tulikuwa tuna tatizo moja. Sote tukiwa ni walemavu
wa ngozi yaani Albino.
Walikuwa wakitembea kwa kujiburuza sana bila shaka
walikuwa wametoka umbali mrefu ama walikuwa na
njaa sana.
Ningeanza vipi kujificha sasa? Sawa ningeweza
kujificha na kisha kufanikiwa kutoroka na kuwa
huru!! Lakini ni usaliti wa hali ya juu ambao
ningekuwa nimeufanya, yaani kuwatoroka wenzangu
ambao walikuwa wanaenda kuuwawa!! Kuuwawa kwa
kukatwa na mapanga!!!
Lile kundi liliponikaribia nilimuona mtu mmoja mweusi
akinikimbilia kwa kasi kana kwamba hapo awali nilikuwa
nakimbia na yeye anajaribu kunikimbiza!! Wakati
nilikuwa nimesimama wima nikimsubiri anifikie!!
Kadri alivyonikaribia nilitambua wazi kuwa laiti kama
nikiamua kumkaba bwana yule kiubavu tulikuwa
tunawezana kabisa.
Lakini sikuhitaji kufanya vile kwa wakati huo kwani
ningehatarisha maisha ya wenzangu japokuwa tayari
yalikuwa katika hatari.
Yule mtu mweusi mfupi alinifikia nakujaribu kunikaba
kwa nguvu, sikujibu pigo lolote. Mwenzake akafika na
kunifunga kamba katika mikono yangu!!
Na wakati huo lile kundi lilikuwa limefika pale
nilipokuwa.
Kwa harakaharaka nikatambua kuwa jumla palikuwa
na walemavu wa ngozi sita na mimi nikiwa wa saba.
Jicho langu lilikutana na sura ambayo haikuwa ngeni
kabisa machoni kwangu. Nikajiuliza huyu msichana
nimewahi kumuona wapi.
Akili yangu haikuwa na hiyana ikanipatia jibu!!
Ilikuwa ni sura ya msichana niliyoiona katika picha ile
ndani ya kile chumba nilicholala na kale katoto
kachangamfu!!!
Tulitazama na hapo nikagundua kuwa alikuwa
amevimba sana uso na macho yake yalikuwa mekundu!!
Niliposhusha macho yangu chini nikaona damu ikiwa
imegandamana katika eneo lake la mguuni kutokea
pajani.
Maskini!! Sijui na yeye walimdanganya kuwa anakuja
kuwa mwalimu wa kwanza katika shule yao mwenye
ulemavu wa ngozi kama walivyonidanganya mimi!!!
Nilijiuliza huku safari ikiendelea!!!
Tukiwa tunaendelea na safari katika eneo lile
lililokuwa na mchanga tele mara nilisikia sauti ya
kitoto ikilia.
Awali sikuwa nimeona mtoto mdogo katika msafara
ule, nikageuka na kutazama ni wapi sauti ilikuwa
inatoka.
Nilipogeuka nikamuona yule binti ambaye nilifanikiwa
kumuona kwenye picha kabla ya kukutana naye pale
akibembeleza mtoto.
Kwa jinsi ya muonekano wake sikudhani kama
angeweza kuwa na mtoto kama yule. Hakufanania
kuwa mama kabisa.
“Mnyonyeshe mara moja!!!” yule jamaa mfupi mweusi
aliamrisha, nikamuona yule binti akitangaza sura ya
masikitiko.
Sikuona ambaye alijali kuhusu hilo.
Yule mtu mweusi alipoona amri yake haifanyiwi kazi
alifyatuka na kisha akamtishia kumnasa kofi, kisha
akamuamrisha tena amnyonyeshe.
“Sasa jamani mimi nitamnyonyeshaje? Maziwa
nitayatoa wapi ya kumpa!!” yule binti alilalamika sana
huku sauti yake ikionyesha wazi kukata tamaa. Na
kweli hakuwa na maziwa kwa mtazamo tu wa kifua
chake kidogo ambacho bado kichanga!!
“Ahaa unataka kujua maziwa yanapopatikana eeh!!”
yule jamaa mweusi alimweleza kisha akamfikia na
kuichana nguo yake na kukiacha kifua chake wazi.
Matiti yote yakawa nje, unyanyasaji wa namna gani
hu jama!! Mbele ya wanaume unamwacha msichana
akiwa kifua wazi!!
Ilisikitisha sana, ulikuwa udhalilishaji wa hali ya juu.
Nisingeweza kuvumilia zaidi msikilizaji..
Nikiwa nimefungwa kamba vilevile, nilitoka kwa kasi
kisha nikampiga teke kali yule mtu mfupi akatokwa na
yowe la hofu. Nikataka kumkimbilia tena lakini wale
wenzake wakaniwahi.
“Wauaji wakubwa nyie, mmetukamata bila sababu,
mnampango wa kutuua, sawa tumekuwa watulivu
mtufanye mnachotaka mnaanza kutudhalilisha.
Angekuwa dada yako ungekubali kuona anavuliwa nguo
hivi, ungekubali kuona analazimishwa kunyonyesha
wakati huenda hata hajawahi kuzaa na hana maziwa
katika kifua chake, nasema hivi sisi ni wakosefu
huenda kilio chetu hakitawaletea athari zozote lakini
nasema ole!! Ole wenu mnaokisikia kilio cha huyu
mtoto mdogo na kujifanya hamkisikii, Mungu aliye hai
atawapa adhabu kali sana, mtalia na kusaga meno
huku mtoto huyu akiwatazama kwa huruma kwa
sababu yeye si shetani kama nyie!! Sijui kama
nitakuwepo kushuhudia lakini ole wenu!!!” nilitokwa na
maneno yale makali kwenda kwa bwana aliyeonekana
kuwa mkuu wa msafara. Niliyasema yale kwa uchungu
sana!!!
Hakunijibu kitu chochote akatokwa na tabasamu!!
Nilitambua wazi kuwa lile halikuwa tabasamu kutoka
moyoni alidanganya tu kuwa ametabasamu hapakuwa
na tabasamu pale!!!
Yale maneno lazima yalimuingia!!
Yule bwana akachukua shuka la kimasai alilokuwa
amejifunika akamfunika nalo yule binti kumsitiri na
uchi ule!!
Msafara ukaendelea huku nikijisikia vibaya sana kuwa
mateka katika nchi huru!!
Nilipokuwa karibu kabisaa na yule binti nilimuuliza jina
lake akanijibu kuwa jina lake ni Grace!! Nikamuuliza
na yule mtoto ni wa nani akaniambia kuwa hajui lakini
anahisi kuwa mama yake ni aidha ameuwawa tayari
ama ni mama mweusi ambaye amezaa albino basi
wamemuibia mtoto wake.
Grace akanigusia pia kuwa hao watu wamembaka mara
mbili kila mmoja. Hakuwa amewahi kujihusisha na
mapenzi hivyo wamemuumiza sana!!
Niliumia ndugu unayenisikiliza ama utakayeyasoma
haya, yaani wanasema sisi sio wanadamu wa kawaida
na hapohapo wanathubutu kumbaka mtu asiyekuwa wa
kawaida. Hakika moyo wangu uliuma mno.
Hatimaye tukalifikia lile gari na hapo hapakuwa na
kuingia ndani ya gari badala yake tulikutana na sura
nyingine ngeni.
Baada ya kufika pale, wale watu wakatuzunguka na
kuanza kutukaguakagua, mara walalamike kikabila
mara wacheke.
Sisi tulikuwa kimya bila kujua jambo lolote.
Na hatimaye likafika gari jingine tena. Ilikuwa yapata
saa kumi na moja jioni. Lilikuwa gari ambalo lilikuwa
katika namna moja ya fuso tukaamuriwa kuingia mle
ndani.
Tukaingia na kuwakuta watu wengine watatu!! Kuna
sehemu kadha wa kadha zilikuwa zimefunikwa sikujua
hata ni kwa nini.
Tuliingia kisha gari likafungwa lile, na baada ya masaa
kadhaa taa zikawashwa mle ndani na zile sehemu
zilizokuwa zimefunikwa zikafunuliwa ni hapo ambapo
kamwe sitapasahau.
Niliwahi kukutana na mambo ya kutisha niliwahi kuota
ndoto kali za kutisha lakini kujikuta katika gari nikiwa
nimefungwa mikono na kisha macho yangu yanakutana
na mashoka, visu na mapanga huku akili ikitambua
wazi kuwa vinatakiwa kuukata mwili wangu!!! Ni
jambo ambalo akili yangu haitaweza kulisahau
kamwe!!
Najua unajiuliza inakuwaje hadi sasa nipo hai, hili
swali hata mimi najiuliza sana lakini nasema huenda
nilipona ili nije kuwa shuhuda.
Nikusimulie kilichotutokea mimi pamoja na albino
wenzangu.
Kisha nikusihi ulidake tena chozi langu!!!
 
SEHEMU YA TANO

WALE watu tuliowakuta mle ndani walikuwa
hawajatusemesha kitu chochote kile. Baada ya
mwanga ule wakajifunika vitambaa vyeusi usoni!!!
Kisha wakaenda mahali vilipokuwa vile visu na kuanza
kuchagua na kufanya kama wanavijaribisha makali
yake kama ni thabiti ama la!!
Niliwaona wenzake wakiwa wanalia.
Grace yule binti aliyebakwa alinisogelea na
kuninong’oneza huku sauti yake ikiwa imejaa uoga
mkubwa.
“Kaka tuokoe!!”
Kauli yake hii ilinifanya nijisikie fadhaa sana,
ningeweza vipi kuwaokoa kutoka katika janga lile
ambalo lilionekana wazi kuwa haliepukiki. Na hadi
kufikia kusema nami aliamini fika kuwa naweza
kuwasaidia.
“Unaweza kaka tuokoe!!!” alininong’oneza tena.
“Sina la kufanya dada Grace natamani sana iwe
hivyo!!” nilimjibu kwa sauti ya chini lakini
hakuridhishwa na jibu langu akabadili kauli.
“Tusikubali hili jambo litokee kirahisi… tupambane
tu!!” alinisihi kisha akaniambia iwapo naogopa basi
yeye ataanza. Nikamwambia kuwa siogopi tatizo ni
kwamba sijui nitaanzia wapi. Sikumbuki kama Grace
aliniaga lakini ghafla alijirusha na kukwapua kisu
kikubwa na sekunde iliyofuata alianguka chini na
mmoja kati ya wale wanaume na kilichofuata ulikuwa
mtafutano wa hali ya juu mle ndani.
Damu iliruka juu sana huku kelele kubwa ikitoka na
kuzima mara moja.
Wale wanaume wawili walibaki kuwa wamepigwa
butwaa!!!
Grace akasimama akiwa amelowana damu na vile taa
ilikuwa inawaka mle ndani alitisha kumtazama.
“Mwanaume yeyote na anisogelee sasa!!!” alitisha
huku akiwa anawatazama wale wanaume wawili ambao
hawakuwa eneo lenye vile visu.
Na sekunde nyingine alinitazama na ni kama ishara
alikuwa ananipa. Ishara ile ikanifungua akili,
nikaingilia kati lile pambano. Ni kweli ulikuwa ni muda
mrefu hatukuwa tumepata chakula zaidi ya maji lakini
nguvu ya ukombopzi hailetwi na chakula.
Nikamuwahi bwana mmoja akiwa amejifunika bado
kitambaa chake usoni.
Alipoanguka chini mara Grace akafika na kumchana na
kisu katika paja lake.
“Ladha ya kisu tamu eeh!!” akamuuliza yule bwana
hakujibu kitu alikuwa analia kama mtoto.
Wakati tumewakabili hawa wale wenzetu waliobaki
wakamkaba yule mmoja.
Baada ya kuwadhibiti ipasavyo kilichobaki ikawa ni
namna gani tunatoka mle ndani.
Yule aliyechomwa bisu na Grace hakuwa na dalili
zozote za uhai!!
Grace allipohangaika na kukosa kabisa namna ya
kutoka katika gari lile akatuita kwa ujumla na
kufanya kama ametukumbatia na sisi tukajikumbatia.
Kale katoto kadogo kakiwa kamelala Grace alianza
kuzungumza. Alizungumza kwa uchungu sana
akijielezea ni kwa namna gani amefika hapo alipo.
“Nimeonelea ni vyema tuzungumze sisi kwa sisi,
japokuwa hatujua kama tutatoka humu tukiwa hai
ama la basi ni vyema kuzungumza. Maana mazungumzo
pia ni tiba naamini kila mmoja analo la kusema kwa
upesi nitaanza mimi. Labda tukizungumza Mungu
aliyetuumba atakisikia kilio chetu na kututoa humu
ndani tukiwa wazima kabisa, ni jambo gani
analoshindwa Mungu kwani? Halipo” aliendelea
kuzungumza.
Alielezea juu ya familia yake yeye akiwa ni dada
mkubwa, wadogo zake wote hawana ulemavu wa ngozi
ni yeye tu na anapambana kumsaidia mama yake
ambaye ni mlemavu wa mguu na umri umemuacha!!
Alipambana hadi kufanikiwa kumaliza kidato cha nne
akaanzisha darasa lake kwa ajili ya kufundisha watoto
wadogo kusoma na kuandika, alifanya yale kutoka na
misukumo miwili kwanza kusaka kipato kwa ajili ya
kuilisha familia yake na pili kutokana na upendo
mkubwa alionao kwa watoto wadogo.
Hapakuwa na kipato kikubwa na baadhi ya wazazi
walikuwa wanagoma kuwapeleka watoto wao katika
darasa lake kutokana na ngozi aliyokuwanayo
walikuwa wakiamini kuwa yeye si mwanadamu wa
kawaida na ni hatari kwa watoto wao. Tatizo ni
kwamba watoto walikuwa wakimpenda sana.
Moyo wake huu wa kujitolea akajikuta akiwaruhusu
watoto wengine kuingia darasani bila kulipia ada
ndogo kabisa aliyokuwa ameipanga.
Kutokana na watoto kumpenda wakajikuta
wakimuelewa sana na hatimaye wazazi wakasahau
imani zao na kuwapeleka watoto wao katika darasa la
Grace.
Ni hapo ndipo wadhamini wakajitokeza na kutaka
kumsaidia Grace ili aweze kuwa na shule yake kabisa
kwa ajili ya watoto wadogo.
Mama yake alifurahi sana kutokana na nafasi hiyo
iliyomuangukia mwanaye.
“Niliisubiri sana hiyo siku ya siku ifike ili niweze
kubadili maisha ya familia yangu na kijiji changu kwa
ujumla. Na kweli hiyo siku ikafika…. Ndiyo siku
ambayo nilitekwa bila kujua iwapo nilikuwa
nimetekwa!!! Sijui iwapo nitarudi nyumbani salama,
na iwapo sitarudi najua tu lazima mama yangu
atakufa kwa sababu ya presha atakufa tu mama
yangu!!!” alinyamaza Grace na alikuwa akilia.
Tukajikuta tumesahau kabisa kuwa tupo katika wakati
mgumu na hatuwezi kutoka nje.
Alipomaliza kuzungumza akaingia kijana mwingine
ambaye kwa kumtazama angeweza kuwa na umri wa
miaka kumi na saba ama kumi na sita. Huyu alikuwa
hajazungumza hata kidogo alikuwa ni mvulana.
“Namchukia sana mama yangu mdogo…..” alianza
kusema kisha akajifuta machozi na kuendelea, “na
alaaniwe kwa yote mabaya aliyonifanyia hadi kufikia
hatua hii hapa nilipo. Nilimuona kwa macho yangu
akipokea pesa kisha kunikabidhi kwa watu wabaya.
Mama yangu mdogo, yaani anatoka marehemu mama
yangu kisha yeye ndiye anayeachiwa titi anyonye
lakini hakujali ukaribu ule. Aliniuza mama yangu
mdogo ili nife kifo cha kikatili. Na hata kabla
hajaniuza ni sawasawa tu alikuwa amenifanya kuishi
maisha mabaya sana nahisi hata marehemu mama
yangu angekuwepo angekataa katakata kumsamehe.
Mama yangu mzazi alimsomesha mama yangu mdogo
hadi kidato cha nne, na baada ya hapo akaugua.
Nakumbuka siku anayotuaga aliniita mimi akamuita na
mama yangu mdogo… sijayasahau kamwe maneno ya
mama alimwambia mama mdogo ‘Jovina mdogo wangu
sihitaji kuongea makuu mengi sana, hali yangu si
njema hata wewe unaniona hili sio la kusimuliwa.
Mama yetu alipofariki alinikabidhi nikupiganie
nimekupigania hadi hapo ulipofikia, sasa najiona hali
yangu ni mbaya naomba na mimi nikuachie huyu mtoto
wangu. Najua hata wewe utazaa siku moja tafadhali
umtunze kama mwanao wa kumzaa, umtunze kama
mimi nilivyokutunza wewe. Nitatabasamu nikiona
mwanangu anafurahi na kunisahau kabisa akiwa
katika mikono yako salama. Naamini hautaniangusha’
…… hayo yalikuwa maneno ya yule mama ambaye
kamwe sitayasahau. Lakini hata mwaka haukupita
mama mdogo akaanza kunifanyia visa, kila
ninalofanya kwake linaonekana baya. Mara ghafla
akanibadilikia na kuanza kunipenda huku akinisihi
kuwa eti mzimu wa mama yangu umemtokea na kumpa
onyo kali akaniomba msamaha. Maisha yakabadilika
sana, lakini baaya ya wiki tatu tu…. Akaniambia kuwa
anahitaji nimsindikize mahali. Haikuwa kawaida hata
kidogo lakini kwa sababu alikuwa ameniomba msamaha
tayari niliona kuwa si vibaya nikiongozana naye pasipo
na kinyongo. Ilikuwa yapata saa moja za usiku.
Tukaondoka na kufika katika nyumba ambazo
hayakuwa makazi ya watu wengi. Nikamuuliza mama
mdogo tunaenda huko kufanya nini, akaniambia kuna
marafiki zake huko anaenda kuwapelekea mzigo wao
wampatie pesa zake. Sikujua kabisa ule mzigo nilikuwa
mimi.
Nilipofika nikamuona anakabidhiwa pesa zake na kisha
kutoweka!!
Nilipiga kelele kumuita lakini hakuniitikia. Na wale
watu wakanikamata kwa nguvu sana.
Nikawa nimetekwa rasmi hadi hivi ninavyozungumza
nanyi!!! Ikitokea natoka hapa salama Mungu
atanisamehe kwa sababu nina hasira kali sana
nitamfanya mama mdogo jambo lolote baya na kama
kufa ni heri tufe wote!! Mtanisamehe siwezi
kuudanganya moyo wangu eti naweza kumsamehe yule
mwanamke katili.
Nitamuua!!!” alimaliza kuzungumza kijana yule.
Grace akadakia.
“Kabla ya huyo mama mdogo hivi ni kwanini tusianze na
hawa wanaojifanya wao ni Israel waliotumwa kutoa
roho zetu??”
Aligeuka na kuwatazama wanaume wale waliokuwa
wakivuja damu pale chini!!
Akiwa hajapata jibu lolote lile mara kutoka nje
ikasikika sauti ikiita.
“Prospa eeh!! Oya Prospaa bado tu!!”
Grace akatufanyia ishara za sote kuiziba midomo
yetu!!
Nilikuwa natetemeka na sikujua hata ni kitu gani
kitafuata!!!
Kutoroka lilikuwa jambo gumu sana!!!
 
HII NI SEHEMU YA SITA!!

Yule mtu aliendelea kuita kutokea nje lakini hakuna
jibu lolote lililotolewa kutoka mle ndani.
Yule mtu kule nje naye akakoma kuita baada ya muda
tukasikia sauti zikinong’ona kule nje. Kisha kimya
kikatanda, na mara ghafla milango ilifunguliwa na
wanaume watatu wakavamia mle ndani.
Grace akajitosa tena kukabiliana nao lakini safari hii
balaa likawa upande wetu, Grace akakutana na panga
kali, akatega mikono yake ili kujikinga na kujikuta
ameyashika yale makali.
Najisikia vibaya sana kwa sababu kumbukumbu ile
kamwe haitaki kutoka katika kichwa changu. Ushike
moyo wako ewe mtanzania na ulidake chozi la albino!!!
Nakumbuka jinsi mtu yule aliyekuwa ameshikilia lile
panga alivyolivuta kwa nguvu sana na kusababisha
mikono ya Grace ikachanika vibaya sana na kabla
hajaweza kujitetea kwa macho yangu nikamuona yule
mtu mtanzania mwenzetu akilinyanyua panga lake kali
na alipolishusha Grace alianguka chini na kamwe
hakuweza kusimama tena. Hawakumuacha alivyo,
waliendelea kumkata wakaitoa kabisa mikono yake.
Grace alitapatapa pale chini na kuna muda
niligonganisha naye macho ni kama alikuwa akihitaji
nifanye kitu lakini sikuwahi kukijua kamwe.
Nilitamani kufanya lolote ili kumuokoa lakini miguu
haikuwa na nguvu kabisa. Fahamu ni kama zilikuwa
zinaniruka na kurejea kila baada ya sekunde kadhaa.
Niliuona mwili wa Grace ambao ndani ya muda mchache
uliopita ulikuwa wima sasa ulikuwa umeanguka chini
sikuwai kuiskia sauti ya Grace tena. Binti yule mrembo
na jasiri. Ahadi zote alizokuwa amefanya kwa kijiji na
familia yake zikawa zimeishia pale pale.
“Yeyote atakayethubutu kuleta fujo zozote zile
hatutamuonya badala yake tutamfyeka mara moja.”
Alikaripia yule bwana huku panga likiwa bado linavuja
damu!!!
Damu ya mwanadamu!
Hakuna hata mmoja kati yetu ambaye alikuwa
anazungumza kila mmoja alikuwa amejikunyata
kivyake!!
Grace akafutika katika ramani ya duniani kwa hujuma
za watu wachache wapuuzi!!
Tukiwa bado eneo lile mara simu iliita kutoka mifukoni
mwa yule bwana. Akazungumza kwa dakika chache
kisha akamaliza na kuwaeleza wenzake kuwa
kinahitajika kitovu cha mtoto.
Nilisisimka sana nikageuka kumtazama yule mtoto
hakuwa akilia alikuwa ametulia tuli ni kama aliyekuwa
akifuatilia kila tukio lililokuwa linaendelea!!! Niliamini
alikuwa akitazama vyema ili siku ya kiama awashtaki
kwa Mungu aliyetuumba!!
Yule bwana akapiga hatua ili amchukue yule mtoto
nikaona hapana ngoja nijaribu kufanya lolote kwa ajili
ya yule mtoto, nikamshika yule mtoto na kumkumbatia
kwa nguvu, ndugu msikilizaji sikuwa tayari kuona
unyama ule mbele yangu sikutaka kushuhudia kitovu
cha mtoto yule asiyekuwa na hatia kikitolewa.
“Unakiita kifo kijana!!” alinieleza baada ya kufika
pale na kukuta nimemkumbatia mtoto kwa nguvu sana.
Hakurudia tena kuongea ananipiga kwa kutumia ubapa
wa panga lake.
Niliyapata maumivu makali lakini sikumuachia yule
mtoto nikaendelea kumngángánia walinipiga sana
hatimaye nikasalimu amri nikamuachia wakamchukua.
Naam kwa macho yangu yote mawili nikamshuhudia
yule mtoto mdogo asiyekuwa na hatia akipewa hukumu
kubwa sana.
Nilijiuliza sana ikiwa wale wanaume walikuwa
wameumbwa na Mungu huyu ambaye aliniumba mimi na
wewe unayesikiliza na kusoma simulizi hii. Kama kweli
ni Mungu aliwaumba basi alikuwa ananipa mtihani
mkubwa sana wa kuyashuhudia yale lakini kwa akili
yangu nilihisi wale ni mali ya shetani laiti kama
wangekuwa wa Mungu wala wasingeweza kumfanya
vile mtoto asiyekuwa na hatia.
Yaani wakamkata kata huku wakisaidizana!!
Mwili wangu uliingiwa na ubaridi sana nikashindwa
hata kulia nikajihisi kupararaizi. Moyo wangu nao
ulikufa ganzi, nilimwomba Mungu anichukue upesi ili
niweze kuyakwepa mambo mawili kwa pamoja. Kwanza
nikiepuke kifo kile cha mateso ama nikwepe kabisa
kushuhudia tena mwenzangu akikatwakatwa mapanga.
Ajabu macho yaliendelea kuwa na nguvu za kuona.
Sijui ilikuwaje labda ni Mungu alipanga iwe vile.
Baada ya kumalizana na yule mtoto wale watu sasa
kwa hasira walinifuata mimi na kitu cha mwisho
nilichokiona ni jinsi walivyokuwa wakinyanyua
mapanga yao juu na kisha kuyashusha kwa nguvu
sana.
Kiza kikatanda!!
Sikujua kilichoendelea tena.

****
Nilikuja kurejewa na fahamu tena nikajikuta nipo
katika kitanda cha kamba, nilitaka kujigeuza na hapo
nikatambua kuwa nilikuwa napatwa na maumivu makali
sana.
Nikajitazama ni kitu gani kilikuwa kinanitokea hadi
naumia vile!!
Ndugu msikilizaji moyo wangu ulipiga kwa nguvu sana
yaani ulipiga kwa nguvu mno!!
Nikajaribu kuyafumba macho yangu na kuyafumbua
tena huenda nitaona kitu tofauti lakini yaliendelea
kuona kitu kilekile.
Mkono wangu ulikuwa haupo!!
Mkono wangu ulikuwa umekatwa mpenzi msikilizaji!!
Nilianza kulia kwa sauti ya juu, nililia sana na hapo
wakatokea wazee wawili na mwanamke mmoja.
Wakaanza kusemezana kikabila.
Sikusubiri wazungumze nami neno lolote nikaanza
kuwaambia kwa uchungu.
“Kwanini mmeniacha hai, ni kwanini nasema
mmeniacha hai kwanini hamkuniua. Mmeuchukua
mkono wangu kwa nini hamjauchukua uhai wangu,
niueni niueni sasa hivi mashetani wangu…” walikuwa
kimya tu na mimi nikanyamaza na kuzitazama nyuso
zao zilizokuwa katika mshangao. Hawakufanania na
wauaji hawa, hawakufanana hata kidogo.
Sasa ni akina nani hawa!!!
Nilijiuliza bila kupata majibu. Na baada ya mimi
kunyamaza mzee mmoja alinisogelea kidogo huku
akionyesha ishara za kunituliza.
“Tulia mjukuu wane… tulia mjukuu…” alinisihi na mimi
nikatulia nimsikilize atakalosema.
“Hatuui sisi.. sisi wazuri tu… wazuri kabisa mjukuu
wangu. Wazuri sana tulia mjukuu wangu..” alinisihi
yule mzee.
Amakweli sauti ya mwema itabaki kuwa ya wema tu.
Inajulikana moja kwa moja!!
Nafsi yangu ikahisi kuwa nipo sehemu salama kabisa.
“Mletee amanche anywe…” alizungumza akichanganya
na kikabila ambacho sikukielewa!!
Baada ya muda nikaletewa maji ya kunywa kutoka
katika kibuyu.
Nikayagida kwa fujo na hapo nikatambua kuwa
nilikuwa nina njaa.
“Njaa inaniuma sana” nikamwambia yule mzee. Na
yeye akawaambia wenzake na baada ya muda
nikaletewa chakula. Nikala kwa fupo nikitumia mkono
wangu wa kulia maana ule wa kushoto haukuwepo
tena eneo lake.
Ulikuwa umekatwa na bila shaka kwenda kuuzwa!!!
Baada ya kula chakula niliwauliza wale wazee mkono
wangu ulikuwa umeenda wapi. Wakanieleza kwa shida
shida kwa sababu hawakuwa vizuri sana katika
Kiswahili.
Walinieleza kuwa waliniokota nikiwa nimepoteza
fahamu huko porini walipokuwa wameenda kuwinda,
mkono wangu mmoja ulikuwa umekatwa na nilikuwa
navuja damu sana. Wakanifunga kovu langu na ile
ilikuwa siku ya pili ndo nikarejewa na fahamu.
Waliniambia kuwa waliwahi kunihifadhi kwani
walitambua ni kitu gani kilikuwa kimenitokea,
walikuwa wakizisikia imani potofu za watu wanaokata
viungo vya albino.
Kwa maelezo yao na uzoefu wao walidai kuwa kuna
uwezekano mkubwa baada ya kukatwa mkono wangu
mmoja nilirukwa na akili na kutimua mbio kabla ya
kupoteza fahamu.
“Na wenzangu wapo wapi?” niliwauliza. Wakanijibu
kuwa hawajamuona mtu mwingine zaidi yangu.
Nikawasihi kuwa nilikuwa na wenzangu wengi tu.
Habari hizo wakazifikisha kwa mwenyekiti wa kijiji,
siku mbili baadaye nikaongozana nao kuelekea sehemu
ambayo niliwaeleza kuwa tulikuwa pale. Tulizunguka
huku na kule hatimaye tukafika lile eneo ambalo ndipo
kwa mara ya mwisho mkono wangu ulikuwa bado
haujakatwa sasa narejea pale nikiwa sina tena ule
mkono.
Wanakijiji kadhaa tulioandamana nao walianza
kupekua huku na huku wakidai kuwa watu wale huwa
hawasafiri na miili iliyopoteza uhai tayari. Kikubwa
huwa wanachukua viungo na kuondoka navyo.
Saa saba mchana jua likiwa limewaka haswa
tukamsikia mbwa akibweka kwa fujo. Awali
tulimpuuzia lakini baadaye tukafuata kilio cha mbwa
yule wananchi wakiwa na majembe na makoleo
walianza kufukua eneo lile.
Mungu wangu!! Nikashuhudia tena magumu mengine,
miili ya wale wenzangu ilikuwa imefukiwa kama mizoga
tu ya wanyama wengine, yote ilikuwa imeondolewa
viungo kadhaa macho na mikono na sehemu za siri.
Nikauona mwili wa kile kitoto kidogo.
Sikuweza kutazama tena nikaanguka na kiza
kikatanda!!!
 
SEHEMU YA SABA

MACHO yangu yalikuja kufunguka tena nikiwa gizani.
Sikujua ni wapi nilipokuwa lakini nilikuwa nipo juu ya
kitu fulani. Na nilikuwa nayumbayumba huku na kule.
Nikatulia bila kufanya papara zozote, akili ikanijia
vyema kuwa nilikuwa katika mgongo wa mtu.
Huyu ni nani tena!!! Nilijiuliza huku mapigo yangu ya
moyo yakipiga kwa kasi sana.
Nikiwa katika utulivu uleule nilimsikia mtu yule
akimuomba Mungu afanikiwe kufika salama aendapo.
Sasa anaenda wapi huyu huku akiwa amenibeba..
“Unanipeleka kuniua?” nikamuuliza nikiuvunja ukimya
katika namna ile.
Badala ya kushtuka yule mtu aligeuka akanitua chini
kisha akanisihi tupige magoti tumshukuru Mungu kwa
dua fupi.
“Nini kinatokea ndugu sielewi hata kidogo?”
nilimuuliza.
Akatabasamu kisha akaniambia kuwa ameniiba kutoka
mikono ya watu wabaya ambao waliambizana
kunichukua kisha kuniua kwa sababu nilikuwa ninaleta
mikosi katika ardhi ile. Kabla sijaulizia kuhusu wale
wazee akanieleza kuwa wasamaria walionisaidia kwa
mara ya kwanza walipewa onyo huku kijiji kikiahidi
kuwatenga ikiwa wataendelea kunitunza.
Nilijiinamia na kujiuliza hii mikosi na vizingiti
ninavyokumbana navyo ni matakwa yake Mungu ili
niendelee kuuona utukufu wake ama ni kitu gani
kinaendelea.
Yule bwana akadai kuwa yeye ameamua kunisaidia tu
kwa sababu nafsi ilimtuma kufanya hivyo.
“Sasa huku tunaelekea wapi?” nilimuuliza. Akaniambia
kuwa hana uhakika na tunapoelekea lakini ikiwa vyema
nipate mahali mbali na kijiji kile nikae huko siku
kadhaa kabla sijapata msaada wa kunirudisha
nyumbani kwetu.
Sasa tukaendelea kutembea ulikuwa ni usiku mnene
sana. Tulitembea tukiwa hatuna uelekeo rasmi. Kila
tuliposikia kundi la watu ama vishindo yule bwana
aliniambia nijifiche na yeye alikuwa akiendelea na
safari zake akikutana na watu anawasalimia na
wakiachana naye na mimi najitokeza tunaendelea na
safari.
Nilimuuliza ikiwa ahofii majambazi maana usiku ule ndo
nyakati zao. Alicheka kidogo kisha akasema kule kwao
hakuna majambazi kwa sababu haukuwa muda wa
mavuno baada ya kilimo.
Tulitembea sana hadi nikahisi kuwa siwezi kutembea
zaidi. Akaomba anibebe lakini nikamgomea kwa sababu
nilijua jinsi nilivyokuwa mzito na kwa mwendo ambao
alikuwa amenibeba kabla sijarejewa na fahamu
zangu. Nikamuomba tupumzike kidogo kisha
tutaendelea. Akaketi kisha tukajilaza.
Usingizi ukanipitia, sijui nilisinzia kwa muda gani lakini
nilikuja kushtuka mvua ikiwa imetanda angani muda
wowote ule ingeweza kunyesha.
Nikamtikisa yule bwana naye akaamka. Kitu cha
kwanza alishtushwa na lile anga.
Kabla hatujafikia muafaka wowote ule. Mvua ikaanza
kushuka.
Ilikuwa ni mvua kubwa sana, ilinyesha huku miale ya
radi ikiwaka huku na kule. Hali ikawa mbaya nikamsikia
yule mtu akiniuliza katika namna ya mashaka.
“Wale wenzangu walisema wewe ama watu kama wewe
ni ishara ya mikosi inaweza kuwa kweli? Mbona…
mbona… mbona siielewi hii mvua sasa…..”
Alizungumza kwa sauti ya juu ili niweze kumsikia lakini
sikuweza kusikia lolote.
Na hapo kipande cha mkono wangu uliosalia ukaanza
kuuma, maji yaliyokuwa yananimwagikia
yakalitonesha kovu!!
Wanasema maumivu ya jino sio mchezo lakini haya
maumivu niliyokuwa nayapata katika kile kipande cha
mkono wangu yalinifanya nilie kama mtoto.
“Mkono wangu unauma sana… nisaidie tafadhali
nisaidie…” nilimsihi yule bwana huku nikimuonyesha
mkono wangu ambao nisiuite mkono kwa sababu
haukuwepo tena. Kilikuwa kipande tu cha mkono
hakika nilikuwa naumia sana.
Yule bwana hakunijali tena kama ilivyokuwa awali,
mashaka yalikuwa katika macho yake na mashaka yale
yakamsababisha akimbie akiniacha katika mvua ile
kubwa!!!
Nisingeweza kumkimbiza kwa sababu haikuwa lazima
anisaidie, ama hata angeamua kunisaidia
angenisaidiaje basi!!
Sina sababu hata moja ya kumlaumu ilimradi
hakuonyesha dalili yoyote ya kunidhuru Mungu
ambariki popote alipo akiisikiliza simulizi hii.
Maji yakaunda mkondo mkubwa hatimaye yakanizoa na
mimi, zamani zile wala nisingeweza kushindwa kukata
maji yale. Wakati nipo kidato cha sita nilikuwa bingwa
wa kuogelea sana.,
Sasa sikuwa na mkono wangu mmoja nikagundua
umuhimu wa kuwa na mikono. Nikawalaani wale
walioukata mkono wangu kwa lugha zote nikavilaani
na vizazi vyao vyote.
Niliteseka ndugu msikilizaji maji yalinitupa huku na
kule, mara ile sehemu iliyokuwa inauma igongane na
vitu vikali na kuamsha maumivu mapya.
Kwa kifupi nilikubaliana na wale waliosema kilio cha
samaki machozi huenda na maji na asijulikane kama
analia ama la!!
Nilikuwa nalia na machozi yalienda na maji. Kuogelea
kwa mkono mmoja ilikuwa jambo gumu sana.
Na jaribio lile lilinishinda licha ya kupalangana sana.
Hatimaye mvua ilipungua na uhai bado ilikuwa ni mali
yangu!!!
Sikuwa na nguvu kabisa, nilikuwa hoi sana.
Uchovu ule ukanifanya nipitiwe na usingizi palepale.
****
MAISHA YA PEKE YANGU!!
KITENDO cha kunusurika katika kadhia zile ambazo
ziliniachia kumbukumbu mbaya kabisa kichwani mwangu
sasa sikuweza kumuamini mtu yeyote yule badala yake
nilijiamini mimi mwenyewe.
Maji yale yalinitupa huku na kule na pale nilipoibukia
palikuwa ni makazi ya watu. Sikuhitaji msaada wa mtu
yeyote yule niliamini kuwa ni Mungu tu
anayenisababisha niendelee kuwa hai. Hivyo ni yeye
ambaye atanionyesha njia.
Nikaamua kuishi maisha ya peke yangu!!
Wapi nitakula? Nini nitavaa? Wapi nitalala? Haya
yalikuwa ni maswali ambayo sikuyapa kipaumbele
kabisa.
Nilichotaka ni kuishi peke yangu hadi pale
nitakapopata namna ya kurejea nyumbani kwa mama
yangu kisha niuseme ukweli wote nilioushuhudia na
jamii itambue ni kiasi gani watu tulio na ulemavu wa
ngozi tunavyoishi kimashaka.
Nikiwa nawaza juu ya nitaishi vipi nikajiuliza pia juu
ya miili ya wale wenzangu. Sijui kama ilizikwa upya
ama iliendelea kufukiwa mithiri ya mizoga.
Palikucha nikiwa namuogopa kila mtu, bado sikuwa nja
uhakika wa moja kwa moja ni mahali gani pale nilikuwa
lakini baada ya muda nikatambua kuwa nilikuwa bado
nipo kanda ya ziwa!!
Na mji ule niliokuwepo nilikuwa naufahamu vizuri
kabisa.
Niliwahi kufika mji ule kwa sababu nilikuwa na
marafiki waliokuwa wakiishi kule.
Lakini muda ulikuwa umepita sasa halafu si ni
hawahawa marafiki walionipigia simu na kunieleza
kuwa kuna kazi ya ualimu.
Marafiki hawahawa waliniunganisha na wauaji ili
niuwawe kwa kukatwa viungo vyangu!!
Swali nililojiuliza na kubaki katika sintofahamu
lilikuwa je? Ni kweli hawa marafiki walitambua kuwa
wale ni watu wabaya?
Nani angenijibu!!! Hakuwepo.
Nikafikiria kucheza pata potea lakini nikajipa
tahadhari kuwa natakiwa kuwa makini sana na sitakiwi
kumuamini mtu yeyote yule.
Nikaamua kuzifanya harakati hizi kimyakimya!!
Nikafikiria wa kuanza naye wazo jema likawa ni kwa
mwanafunzi mwenzangu ambaye nilikuwa nalala naye
chumba kimoja enzi zile.
Lakini nilipanga kuwa hadi nihakikishe kuwa sijaweza
kupata njia nyingine kabisa mbadala hiyo ndo itakuwa
mbinu ya mwisho.
Maisha ya siku ile yakaanza, ama kweli ukiwa na
matatizo siku inakuwa fupi sana ama wakati mwingine
inakuwa ndefu sana.
Kwangu mimi usiku uliwahi sana kuingia, nilikuwa
nimejiweka mbali kabisa na macho ya watu. Nilikuwa
siruhusu mtu kunitambua mimi ni nani maana
hakuwepo wa kumuamini.
Yaani hadi viongozi wa dini walipita na sikujisumbua
kuwakimbilia maana hata wao ni wanadamu tu
wangeweza kunisaliti kisha nirejee katika mikono ileile
mibaya na huenda safari hii nisingeweza kuchomoka.
Majira ya saa moja hivi kimakadirio na lile giza njaa
ilikuwa imenishika na kile kiubaridi cha jioni kikaingia
na ukimya nao ukatawala.
Na hapo hofu ikaniingia tena.
Hofu haikuwa juu ya viumbe wakali lakini hofu yangu
ilikuwa juu ya wanadamu wenye roho mbaya kabisa.
Masaa yalizidi kwenda miguu ikaanza kuishiwa nguvu
na kisha likajirudia lile tatizo la kuumia mkono ule
uliokatika.
Mkono ulianza kuuma sana, nikajiona kuwa hii ya sasa
imekuwa mbaya zaidi natakiwa kupata msaada wa
haraka.
Nilikuwa nafahamu hospitali ilipokuwa hivyo
nilijikongoja kutoka katika giza lile nikiwa natokwa
machozi kutokana na uchungu. Nikaamua liwalo na
liwe.
Nikiwa napiga hatua zile mara nikaisikia sauti nyuma
yangu.
“SIMAMA HAPOHAPO!!” ilikuwa sauti ya kiume.
Moyo ukapiga paaa!!!!
 
HII NI SEHEMU YA NANE
Akili ikanituma kuwa kuendelea kwangu kusimama
ningeweza kujizulia balaa jingine kutoka kwa hao
watu ama mtu aliyekuwa akiniamuru kusimama.
Nikataka kukimbia lakini nikatambua kuwa kukimbia
kwangu pia ni kulikuza tatizo.
Upesi nikageuka na kutazama mahali sauti ilipokuwa
ikitokea!!
Pasi na shaka mtu yule hakutegemea mimi kugeuka
ghafla kiasi kile. Hapohapo akanimulika na tochi yake
usoni na mimi palepale nikafanya kitendo ambacho sijui
akili ipi iliamuru kifanyike.
Nikaachama mdomo wangu kisha nikaanza kumfuata
aisee yule bwana alipiga yowe huku anatimua mbio.
Sijui alikuwa ni mtu wa ulinzi shirikishi ama kijana tu
kama vijana wengine wanaopenda kupiga mkwara
wenzao na kujifanya wababe.
Sikupoteza muda maumivu ya mkono bado yalikuwa kwa
kiasi kikubwa.
Niliondoka pale safari hii nikitembea haraka haraka
zaidi hadi nikaingia barabarani.
Nikakata kulia huku maumivu makali yakiendelea
kunitafuna.
Hatimaye nikafika hospitali nikiwa sina hata shilingi
kumi mfukoni na mbaya zaidi nilikuwa nina njaa na
nilikuwa nimechafuka.
Nilifika hadi chumba cha daktari, hakuwepo!!
Nikawasihi sana manesi wanisaidie wakampigia simu
daktari.
Daktari akagoma kuwa hawezi kuja tayari yupo na
familia yake nyumbani akawaelekeza manesi
wanichome sindano fulani kisha siku inayofuata ndiyo
nije kwa ajili ya huduma.
Manesi wakafuata maelekezo ya daktari na kunichoma
sindano.
Hapo sasa kikazuka kizaazaa kumbe sindano ile
inatakiwa mgonjwa awe ameshiba kabisa kabla ya
kuchomwa sasa mimi nilikuwa nina njaa kali na sijatia
chochote mdomoni tangu asubuhi.
Mwili ukaishiwa nguvu nikakumbwa na kizunguzungu na
kuanguka chini. Manesi wakaanza kuhaha huku na kule
kutafuta namna ya kuniokoa na lolote baya ambalo
lilikuwa linaenda kutokea.
walimpigia simu daktari na baada ya kukata simu upesi
wakaniletea chakula na kunisihi nile kwa wingi.
Kwa njaa niliyokuwanayo hawakuwa na haja ya
kunisihi!!
Afadhali hata walifanya makosa!!
Nikapata kitanda cha kulala nikapata na chakula cha
kutosha pia nikashushia na maji mengi ya kunywa!!!
Asubuhi daktari alifika na kunitembelea!!
Nilipigwa na butwaa kubwa sana, daktari alikuwa ni
mwalimu wangu wa baiolojia wakati nikiwa kidato cha
nne!!
Yeye hakunitambua upesi lakini mara moja
nilimtambua.
“Sir. George!!” nilimuita. Akageuka upesi sana.
Na tulipogonganisha macho alinitambua… aliingiwa na
upweke mkubwa sana ghafla!!
“Majaliwa… wameukata mkono wako mwanangu….
Wameukata mkono wako watu wabaya!!!” hakuweza
kuendelea kuzungumza alianza kutokwa na machozi
akafika pale na kupiga goti.
“Ni kwanini wanathubutu kuwaua, ni kwanini na ni
nani aliyeileta imani hii mbaya kabisa ya kishirikina!!
Nilikutafuta sana Majaliwa, nilikutafuta hadi ikafikia
hatua nikahisi huenda na wewe wamekuua. Najua hii
sio ajali hebu niambie ni kitu gani kilikutokea?”
aliendelea kuzungumza. Sasa na mimi nilikuwa nimekaa
kitako.
Nilitamani kuzungumza lakini kuna kitu kama funda
lilikuwa limekaba koo langu.
Ili funda lile litokea sikuwa na budi kulia kwanza!!
Niliyaachia machozi yakatoka na mimi nikiwa nalia
sana. Daktari aliniacha nilie bila shaka alijua kuwa ile
ndiyo ilikuwa njia pekee ya kuyapooza machungu
yangu!!!
Baada ya kilio kile nilimueleza daktari kwa ufupi
kilichonitokea mimi na rafiki zangu na kisha
nikamuelezea safari yangu hadi kufika katika mji ule.
Daktari alinitia moyo sana akanieleza kuwa baada ya
juma moja ana safari ya kwenda Dar es salaam hivyo
tutaondoka wote na kisha ataniacha Dodoma ambapo
ndipo nilikuwa naishi na mama yangu. Mama ambaye
sikujua hata alikuwa na hali gani.
Lakini kwa juma hilo zima la kusubiri nitaishi nyumbani
kwake. Nyumba ambayo anaishi na mkewe pamoja na
watoto wao wawili na mfanyakazi wa ndani.
Ndugu msikilizaji niliusikia moyo wangu ukipata nafuu
kubwa hakika licha ya kujipa moyo kuwa nitayaweza
maisha ya kuishi bila kumwamini mtu lakini hapa
nilijikuta nikimuamini tena daktari.
Kwa mara ya kwanza kidonda changu baada ya
kukatwa mkono kilisafishwa kwa uangalizi mkubwa
sana na jioni ya siku hiyo niliondoka na daktari hadi
nyumbani kwake ambapo nilipokelewa vyema na familia
kwa ujumla akanitambulisha kwa ufupi kisha
akanikabidhi kwa kijana akanionyesha chumba cha
kulala.
Nikaanza maisha mapyya!!!
Kesho yake wakati anaenda kazini aliniitan na kunisihi
sana.
“Majaliwa hakuna sehemu salama hata moja, hili geti
lisikupe ujasiri wa kujiona kuwa upo salama hata
kidogo endelea kuishi kwa tahadhari kubwa hadi siku
ambayo tutaondoka sawa!!” alimaliza akaondoka.
Maneno yale huenda pia alizungumza na mkewe kwa
sababu mama yule hakuwa akinitafutia sababu za
kukaa nje hovyo, kila kitu kilikuwa ndani kwa ndani.
Siku nne zikakatika nikiwa ninayo amani ya nafsi
kabisa. Siku ya tano nikiwa pale nyumbani nilimuomba
mke wa daktari simu ili niweze kuzungumza na mama
yangu nyumbani namba yake bado ilikuwa katika
kichwa changu.
Ikawa bahati mbaya mama yule hakuwa na salio katika
simu yake, na wafanyakazi wote wawili hawakuwepo
alikuwa amewaagiza.
Nikamwomba niende mimi ye anielekeze tu duka lilipo.
Akapinga vikali akidai kuwa nisubiri tu atatafuta mtu
wa kumuagiza.
Sikuona hiyo kama ni sawa nikamsisitiza na hatimaye
akaniagiza nikaendsa kununua vocha.
Kitendo cha dakika tano tu nilikuwa nimeenda na
kurejea.
Sitaki kuamini hata kidogo eti kuna mtu ambaye
alikuwa amekaa kuwinda pale ili anione. Siamini hata
kidogo lakini moyo wa mwanadamu ni kichaka!!!
Kweli namba ya mama ilikuwa inapatikana, alifurahi
sana kunisikia na wala sikumgusia lolote baya
lililonitokea. Akaniuliza kazi inaendeleaje
nikamwambia inaendelea vizuri ndo kwanza tunaanza.
Siku ya tano ikapita.
Tukaingia siku ya sita na hatimayer siku ya saba
ambayo ndo ilikuwa siku yangu ya mwisho pale.
Nilikuwa nimejiandaa nikimsubiri daktari ambaye
alinieleza kuwa alikuwa anapita ofisini kumuhudumia
mteja mmoja kisha baada ya hapo atanipitia na gari
yake binafsi tuondoke.
Majira ya saa nne hivi nilisikia kelele na kisha pakawa
kimya nikajiuliza ni kweli nimesikia kelele ama ni
masikio yangu. Nikaendelea na shughuli zangu!!
Lakini ni kama nafsi ilinilazimisha kuamini kuwa kuna
kelele nilizisikia lakini zikakoma ghafla.
Nikaufungua mlango wa chumba changu na kutoka
nje.
Nikafika hadi sebuleni hapakuwa na bughudha yoyote
ile.
Mara nikasikia kelele za mwanaume akisisitiza kuwa
ameniona.
“Yule pale yulee…”nilisikia akisema.
Ama hakika nilipagawa yaani hadi katika nyumba ile
walikuwa wamenifuata.
Nilijaribu kukimbia lakini hapakuwa na sehemu zaidi ya
chumbani kwangu.
Nikajifungia huko.
Kimya kikatanda lakini baada ya dakika kadhaa
nikasikia watu mbele ya chumba changu.
“Majaliwa fungua mlango wananiua usipofungua!!”
ilikuwa sauti ya mama yule mpole kabisa mke wa
daktari.
Nikatambua kuwa hata nisipoufungua mlango bado
watauvunja na kuingia. Japokuwa nafsi ilijitabiria
mabaya lakini ningekuwa mkosefu wa shukrani ikiwa
nisingekisikia kilio cha yule mama.
Nikaamua kujitosa, nikaufungua mlango mara
wakanivamia na nilichokiona ni kisu kikubwa kikinijia
maeneo ya usoni na mara haikuwa usoni tena.
Sikio langu likafyekwa na mimi nikaanguka palepale na
kuziacha fahamu zangu!!!
 
Back
Top Bottom