Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,638
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA KWANZA
1
PALISHAKUCHA.
Pakuche mara ngapi?
Ni vile tu huyu Morena alilala chakari. Asubuhi hii ya saa nne, kwake ilikuwa ingali liamba. Alilala kifudifudi. Fofofo..
Ghafla, kuna mtu alimtoa katika ule ufofofo. Akamkera. Alimkera hasa!
Kivivu, aliinua shingo yake, akakigeuzia kichwa chake upande mwingine. Akasonya
Angali na mawenge ya usingizi. Si hayo tu, bali pia uvivu ulimjaa. Vikampa hali ya kutaka kuendelea kubadili uchago kila dakika, licha ya jua la asubuhi kuhanikiza nuru ya kutosha mle chumbani mwake.
Akilini, aliutaka utulivu kwa gharama yoyote ile. Japo apate kukimalizia hicho kipande cha usingizi. Wala hakujua kingekwisha saa ngapi. Alitaka kulala. Kulala tu mpaka pale mwili wake utakapomruhusu kutalikiana na kitanda.
Aliyemkera, akamkera tena.
“Eeh mchicha matembele majani ya kundeee… eeh mchicha tembeleee… eeh mchicha tembele majani ya mabogaaa”
Huyu muuza mboga ndiye aliyemgutua toka usingizini, kwani alikuwa akichuuza biashara yake ya mboga za majani karibu na dirisha la Morena. Dirisha lililokuwa upande wenye kichochoro kilichopakanisha chumba alichokuwemo na nyumba ya jirani.
Mchuuza mboga alisimama hapo kichochoroni pamoja na wateja wake waliokuwa wakichagua mboga toka kwenye tenga. Wakafanyiana mizaha ya hapa na pale iliyosindikizwa kwa vicheko vya juu na chini.
Kelele zao zikamfanya Morena ajihisi kama mtu anayepigiwa zumari sikioni. Akasonya tena. Msonyo mrefu uliobeba uzito wa makumi ya maneno. Maneno aliyotamani yawasilishe hisia zake kwa sauti ya kuhutubia umati. Alichefukwa.
Naam! Ikawa kama vile huo msonyo wake ulimuhimiza mchuuza mboga akolezee tena kibwagizo chake maradufu. Akamvumilia kidogo huku akiinua tena shingo yake na kuzisikiliza sauti za wateja wake. Akaitambua moja, ya mtoto wa mpangaji mwenzake.
“Somoe! We Somoe!” akaita kwa sauti ya kukaripia na Somoe mwenyewe akaginiza kwa sauti ya juu.
“Abeee!”
“Embu niondoshee huo mnada wenu hapo dirishani”
Morena akatoa amri yake kwa sauti ya chini kidogo huku akiyabana mate yaliyomjia ghafla kinywani. Hakuona pa kutemea. Akakunja ndita kadhaa usoni. Kwanza alikereka kwa kule kugutuliwa usingizini; pili, ile adha ya kujaa mate ilimkalfisha nafsi. Na mwisho, ombi lake kwa Somoe lilipita kimya kimya kama kivuli.
Muuza mboga naye kama mtu aliyefinywa alianza tena kuchuuza biashara yake kwa sauti. Safari hii Morena hakusubiri mbivu ziwe mbovu. Alitoka kitandani. Akasimama na kuikaza khanga yake kifuani. Ngoja nikamshikishe adabu! Akajiapiza.
Alipita katikati ya chumba chake, akivipamia vitu vilivyotupwa sakafuni shaghalabaghala; hapa nguo, pale viatu na makorokoro yake mengine chungu nzima.
Alihangaika na kitasa kwa takribani robo dakika wakati akiufungua mlango ambao ni dhahiri ulikuwa mbovu. Pale nje ya mlango wa chumba chake aliitafuta ndala yake moja na asiione, akaivaa hiyo moja iliyokuwepo na kuanza safari ya kuelekea nje.
Alimpungia mkono mpangaji mwenzake aliyepishana naye, akishindwa hata kuijibu sawasawa salamu aliyopewa, kwa kule kuyakonga mate kinywani. Aliukusanya mdomo wake akautanguliza mbele mithili ya mdomo wa bata.
Akatoka nje na kuyatema upenuni mwa nyumba. Akayafukia kwa mguu uliokuwa peku.
Haikuleta maana; kuivaa ile ndala moja na kisha kwenda kuyafukia mate kwa mguu uliopeku. Ila ndiyo falsafa ya maisha, kupata na kukosa; wanaokosa ndio wenye kutumika na kusulubika.
Twaibu! Morena aliiongoza miguu yake kuelekea ule upande wenye uchochoro. Alimfungia kibwebwe muuza mboga kana kwamba alitaka tena kwenda kulala akishamfukuzia mbali.
Alipoifikia ile kona inayoelekea uchochoroni, akausikia mlio wa bodaboda, mlio uliomgeuza shingo. Aliyemuona akamfanya ayasahau yote yaliyomtoa nje. Akakigeuza kiwiliwili kizima kumtazama mgeni aliyewasili.
Alikuwa rafikiye, Fatumata Mzinga. Somo yake wa kufa na kuzikana.
Alitulia akimtazama namna anavyoshuka toka kwenye bodaboda, mwili wake tipwatipwa uliogawanyika kike kisawasawa ukitibwirika. Na mshukaji nwenyewe akaongeza sifa za mkwezi kuudandia mnazi. Aliujaza madoido ule mtibwiriko!
Wanaume waliokuwa upande wa pili wa barabara palipo na karakana ya fenicha wakameza mate ya tamaa, wengine walijikohoza na wengine walikaribia kuviranda vidole. Umbile lake lilileta hali ya kubahashika pasi hiyari.
Wakaingia ndani, Morena akitangulia na Fatumata akimfuatia. Mle ndani Fatumata akayaanzisha maongezi mara tu baada ya kuufunga mlango na kwenda kuketi kitandani.
“Nilijua nikifika kwa Mzee Hizza n’takuta wanatembeza daftari la rambirambi” akazungumza akimtaja baba mwenye nyumba aliyopanga Morena.
“Aaah! kwa lipi?” Morena akauliza huku akiumba uso wa mshangao.
“Yale mapombe makali makali uliyogida jana. Mwanamke unakunywa kiama” Akampigia saluti. “Nikajua utaunguza hadi utumbo maana ile mijibaba jana ilikuvulia kofia ujue! Chupa ya tisa jicho kodo!... kope zimekusimama kama miiba ya nungunungu” Fatumata aliongea akitoa macho na kuchezesha mikono kuyasindikiza maneno yake.
Morena akacheka. Alicheka vile mwenzake alivyomsifu na kumsagua kwa pamoja.
“Tena mbona ungenikuta nimelala kama si muuza mboga mmoja mpuuzi alonikatishia usingizi wangu” Morena akalalamika akiutafuta mswaki wake kwenye stuli pana iliyokuwa na vitu vya kila aina; vipodozi, misumari, kalamu mbovu, dawa zilizokwisha muda wake mpaka karatasi za vocha zilizotumika. Stuli ilijaa hobelahobela!
Akaupata mswaki.
Pasipo dawa aliuchomeka mdomoni na kutoka nje. Alimuacha Fatumata anapitisha macho kwenye kipande cha gazeti kilichotumika kufungia dagaa mchele waliokwishaliwa tangu juzi.
Dakika moja Morena alirejea ndani, akautupia mswaki wake juu ya ile stuli.
“Kwanza nambie jana uliondoka na nani kwani… hukuokota garasa kweli?” Fatumata akamdodosa Morena aliyekuwa anaukagua uso wake kwenye kipande cha kioo.
Kioo kilichokuwa kimetundikwa kwenye msumari ukutani. Aliutazama uso wake, akazitazama nywele zake ndefu zilizopakwa rangi mbili tatu tofauti kiasi cha kufanana na mtu aliyejitwika jogoo kichwani.
Morena akacheka kwanza, kama ilivyo haiba yake. Alicheka akigeuka na kumtazama Fatumata kwa bashasha.
“Mimi huyu, niliyenyonyeshwa mataputapu. Nikalewe zile bia zenu za mafungu” akasonya. “Bia ya tisa nikikurembulia jua nimekuhurumia saaana”
“Kijukuu cha mwana harashi wewe!” Fatumata akashadidia akifinyanga kile kipande cha gazeti na kumtupia Morena, huku akitoka kitandani na kuketi sakafuni. Akatandaza miguu yake huu mashariki ule magharibi.
“Hizi kazi zetu ukijifanya unajua kulewa utakopesha kiuno hicho kila siku” akamjibu na kuendelea “Nimeingia kulala humu saa moja asubuhi” Morena akaachana na kioo na kukifuata kitanda.
“Eh! Nipe… nipe… michapo” Fatumata akasherehesha akipunga mikono hewani.
“Kitu Bokilo” Morena akatamka kwa mbwembwe akinyanyuka na kuketi sawa pale kitandani huku akilitaja jina la mwanaume aliyeondoka naye usiku uliopita.
“Yule Bokilo Mzaire?” Fatumata akauliza kishabiki, akitenga mikono kiunoni.
“Mzaire dada, mutu ya vitenge na bazee” Morena akafanya mbwembwe zake tena akipaza sauti.
“Pedeshee la Bukavu, Kinshasa na kati ya Lubumbashi, mutu ya suruali pande sita” Fatumata akaumalizia utambulisho.
“Kwani zile ni suruali? Kwa upana ule tuyaite mashuka tu dada”
Kikafuata kicheko kirefu cha kugongesha mikono, kisha wakarejea kwenye mjadala wao.
“Alikupeleka wapi? Maana wangu yule majinuni na akili zake za kuhesabu alijua kuninywesha tu. Tumefika kule Bondeni loji kwenye mbuyu akalala puh!”
“Ndani puh!” ikawa zamu ya Morena kushangaa.
“Puh! Nilitamani kumchumia mikwaju nimtandike fimbo za kitambi anijue mie nani” Fatumata hakusemea utani, alimaanisha kiasi cha kumchekesha mwenzake.
“Pole mwaya, mie kwanza alinipeleka gesti moja nzuri balaa maeneo ya Kigogo. Akanianzia na ahadi za mtaji wa biashara, nikaongeza bakora… chapa! chapa!” akakung’uta vidole. “Akaniahidi nyumba nzima. Dada upo?” Morena akalivuta neno la mwisho kwa mikogo mingi, Fatumata akiwa bado amemtumbulia macho.
“Nyumba nzima! Bokilo Mzaire huyo? Ulimvalia na njinjili?” Fatumata akauliza kwa midadi akijishikashika kiuno kumaanisha shanga zivaliwazo na wanawake kiunoni.
“Mie tena, nilimfungia hizi” akafunga dole gumba na kuviacha vinne hewani. “Sio watoto wa siku hizi wanaovamia fani na zigo la shanga ka’ fundo la msuli” Morena akamfanya Fatumata acheke mpaka machozi.
“Asubuhi kaacha elfu 50 kasema baadaye atan’tumia bajaji tukale kuku sekela mahali”
“Usinambie!” Fatumata akamaka. “Ngekewa hiyo dada. Mungu akitaka kukupa-” Fatumata akatamka akikomea njiani kwanza kisha kwa pamoja wakamalizia.
“Hakuandikii barua” wakamalizia kwa sauti za kuimbia irabu.
Wakacheka cheko lingine refu kisha wakatulia, wakiyaanza maongezi mengine.
Ilikuwa kawaida yao, kukutana namna hii na kuzungumzia maisha yao ya ukahaba almaarufu kama uchangudoa. Wangetambiana juu ya wanaume waliowaopoa, pesa walizopata na pengine hata ahadi hewa za hiki ama kile. Lakini pia, mara nyingine ingekuwa huzuni tupu, wangekutana kufutana machozi, kupeana pole na kusaidiana kwa suluba na madhila waliyokumbana nayo.
“Embu kaoge tutoke kwanza, twende mahali nikakupe akili za maisha leo” Fatumata sasa akaweka umakini kwenye mazungumzo yao.
“Kuna nini tena?”
“Kaoge tutoke mwe! hii mijumba yenu isiyo na silingibodi mtu akijamba hapa panya wa chumba cha tatu kule anasikia” Fatumata aliposema hivi Morena alicheka, na wapangaji waliokuwa nje nao wakasikika wakicheka. Dongo lile kuhusu nyumba walilisikia kama walivyoyasikia maongezi mengine yote.
“Kwako kuna nini?”Morena akasaili akinyanyuka toka kitandani.
“Hivi sijakwambia, baada ya ile harusi ya binamu, nyumba imejaa watu kama soko”
“Usinambie!” Morena akamtolea macho.
“Mwenzangu, ukipita nje utasema kuna meza ya muuza mitumba ndani… embu kaoge tutoke bwana” Fatumata akalijibu swali na kumuhimiza tena Morena ajihimu.
Alipotoka kuoga Morena alirejea chumbani kwake. Pasi kujali uwepo wa rafiki yake, akaitupilia mbali ile khanga moja iliyokuwa imesitiri maungo yake na kuanza kuranda mle chumbani akijipaka mafuta, akitafuta nguo ili mradi alikuwa na hekaheka za hapa na pale.
Morena alikuwa mrefu wa kadiri, ungemtazama kwa haraka haraka ungedhani ni mwanamke wa kisomali. Vile alivyojaaliwa nywele ndefu laini na wajihi mwembamba kiasi wenye pua iliyonyooka. Watu wengi walihisi Morena alikuwa na usomali ndani yake.
“Haya shanga ushatupa kule, kwanza huo mkufu kiunoni hauchuji?” Fatumata alimtupia swali mwenzake akimtazama vile alivyokuwa akimkatishia mtupu kama mwanga, huku akiuvaa huo mkufu wake.
“Dhahabu yenye gramu zake hii sio cheni zenu za vyuma chakavu ukinunua leo mtondogoo kutu imekutoa mapunye” Morena akajibu akianza kuvaa nguo zake.
“Hivi ulidunduliza miezi mingapi? halafu umenikumbusha Bintuni na cheni lake la kuhongwa”
“Yule nusura tumpeleke India kwa matibabu, sijui aliuokota wapi mcheni mzito kama mnyonyoro wa geti” Alidakia Morena na kuzua kicheko kingine mpaka kwa wapangaji waliokuwa koridoni wakidoea mazungumzo yao.
Morena alipomaliza kuvaa na kujipara, akajipulizia manukato yake. Manukato ghali kidogo kulinganisha na kipato chake cha kuungaunga.
Pamoja na uduni wa maisha yake na uzito wa majukumu aliyokuwa nayo, Morena hakuacha kujitafutia vitu alivyovipenda kwa dhati. Hata kwa kudunduliza senti moja kila siku, angeweka bila kusita wala kuchoka, aliamini haba na haba hujaza kibaba. Morena alipenda vidani vya dhahabu, na aliyapenda manukato.
Akamgeukia Fatumata.
“Haya twen’zetu sasa” akatamka huku akiufuata mkoba wake na kuweka sawa baadhi ya vitu vyake.
Wakatoka pamoja mpaka nje ambako walianza kutembea pole pole huku wakishauriana pa kwenda. Papo hapo, Fatumata akichombezea hizo akili za maisha alizotaka kumgawia mwenzake. Aliuremba mpango wake kiasi cha kumtia kiwewe mwenzake.
“Hili dili lililonifungisha safari likitiki… tutaununua huu mtaa mzima somo!” Fatumata akamfanya Morena adondoshe mguno.
“Ngoja tufike basi Kha!” akamtoa papara huku akijiandaa kuvuka barabara kuelekea mahali ziliposimama bodaboda.
Taratibu wakakaza mwendo kuwahi kupeana hizo akili za maisha. Wasijue tu namna ambavyo akili hizo zingekuja kuigharimu furaha yao maishani.
2
JUA la saba mchana liliwaka hasa!
Liliwakutia mgahawa maarufu wa Vitukoutata, maeneo ya Vingunguti. Kila mmoja alikwishaagiza chakula chake. Wakakishambulia chakula hicho haraka haraka, kana kwamba walikuwa wamekikamia.
Morena alikuwa wa kwanza kumaliza kula. Akamwita mhudumu amletee maji ya kunawa. Maana, mchuzi wa kongoro ulikwishamganda mikononi. Ikawa kero kwake. Wakati mhudumu anafika na beseni lake mkononi, Fatumata naye akawa amemaliza chakula chake. Akajiunga kwenye kunawa.
“Shing’ ngapi?” Fatumata aliuliza huku akikimbilia kutoa kijiti cha meno kwenye kichupa chake mara tu baada ya kumaliza kunawa.
Morena yeye alihangaika kuyachokonoa magego yake kwa ulimi.
“Vishalipiwa mbona!” Yule mhudumu alijibu akitabasamu, akiufurahia pia mshangao wa wanawake wawili mbele yake.
Wakatazamana kwa bashasha. Wakaendelea na mambo yao pasipo hata kusaili ni nani aliyewalipia. Nyakati zingine ofa kama hizi zilikuwa za kawaida kwao, hasa akiwepo Fatumata Mzinga. Wangelipiwa chakula, nauli na huenda wangepata ahadi za kupelekwa huku na kule kisha kuzungumza biashara.
Wateja wao walikuja kwa njia mbalimbali.
“Tawire! Haya leta habari habibti” Morena alijiweka sawa tayari kumsikiliza rafiki yake.
“Unamkumbuka yule bwana alonileteaga dili ya mawese?” Fatumata akaianzia mbali habari yake. Akakitupa kando kijiti cha meno.
“Bwana we hayo ya nani anafanya nini utanichanganya tu, hao mabwana zako wauza mawese nawajua kumi na…” Morena akajibu, akimfanya Fatumata amtukanie ukoo wake, akaliunga na tusi lingine la nguoni na Morena asijali.
“Kimboka” Fatumata alipolitaja jina Morena akadakia.
“Yule mpuuzi. Haya kafanyaje?” akauliza kwa sauti ya mkwara.
“Hujasamehe tu!”
“Muuza mawese yule aliyetaka kutulaza ndani kwa bia zake za mafungu.” Akasonya.
Uso wa Morena haukuwa na masihara hata kidogo. Alimpindishia mwenzake midomo.
“Tukio la mwaka juzi bado linakupandisha mavi ya kifua tu! Punguzaga vinyongo unenepe shaa!… embu sikia, Kimboka ana dili la mamilioni somo!”
Akayatumbua macho kimbeya.
Aliianza tena habari yake kwa madaha. Akimfanya Morena aukunje uso na kumeza mate mithili ya mtu aliyelambishwa kitu kichachu.
“La kuuza mawese yake?” Akauliza kwa dharau akibetua midomo.
“Sio mawese jamani!”
“Kumbe!?”
“Madini!” Alilitamka neno madini kwa sauti ya chini akikisogeza kichwa chake mbele zaidi ili Morena amsikie vizuri pamoja na kule kunong’ona.
Morena alitoa macho kana kwamba alichotamka Fatumata kilikuwa kitu cha kutisha mno. Akauliza kwa sauti ya mshangao. “Madini?”
“Mdomo huo mwanamke, shiii!” Fatumata akamuwahi, akimtaka apunguze sauti.
Morena akafunga mdomo wake wa kiganja chake cha kuume huku bado jicho likiwa limemtoka pima. Taratibu akamtazama mwenzake kama zumbukuku.
“Jela unaijua lakini Fatumata?”
“Jela ya nini?”
“Jela hizi za Segerea, Ukonga sijui Butimba?”
“Mie nilimsikia anaongelea biashara ya madini, sasa jela inahusikaje?”
“Mmh! Madini mwenzake utapeli Fatu, lakini haya! Kila la kheri kwenye huo mpango wako. Mie n’taendelea kuibia wanaume kwa mtaji huu chini mpaka siku yangu ikifika.” Alizungumza akiutazama huo mtaji wake.
“We huzitaki pesa?”
“Nazitaka ndio, ila hizo mishe mishe za lala apache alolo amka Bakhresa, Bongo hii, haya!”
“Mbona unan’tisha na sijamaliza, unajua nimekuita sababu kuna lingine na ndio hilo linaloniumiza kichwa?” Fatumata alimtazama mwenzake kwa uso mkavu usio hata na chembe ya utani.
Morena naye akamtazama kwa umakini kidogo, moyo ukimtokota. Alishaingia woga ghafla. Akauliza mboni za macho zikicheza kulia na kushoto kwa kasi ya ajabu. “Kitu gani?”
“Kuna kiroba cheusi hicho tukishikamana tunatoka huku uswazi”
“Eeeh!”
“Punguza mchecheto basi!”
“Haya niambie kuna nini kwenye hicho kiroba?” Morena akajiweka sawa, akitazama huku na kule kana kwamba alihofia watu wangewasikia wakiongelea mambo ya viroba.
“Ndio maana n’kakutoa kule kwenu.” Fatumata alimzodoa mwenzake, akiucheka ule mchecheto wa Morena. Huku akitaka kuziweka sawa akili za mwenzake, Fatumata aliendelea. “Sikia, wiki iliyopita, siku ile tuliyokesha Kiwalani sijui unaikumbua…”
“Tunakesha mara ngapi uko Kiwalani? We n’ambie moja mbili tatu basi!” Morena aliona anachelewa kuijua habari yenyewe.
“Haya twende, nililala kwa Kimboka pale, unajua tena kusikia mamilioni kidogo niingie wehu, sasa vile jasiri haachi asili….” Fatumata hakumalizia, Morena akamdaka.
“Ukaiba?”
“Hebu bwana we kha!” Fatumata alianza kukerwa na kule kukatishwa katishwa kila mara.
“Sikuiba, nilikuwa nafanya doria, nikatokezea stoo moja uchwara umo ndani. Na hapo ndio paliponifanya nikuite hapa n’kupe akili za maisha.” Alijieleza huku mwenzake akiitikia tu chapuchapu. Kichwa kikienda juu chini juu chini mara kadhaa.
“Nilikuta viroba hivi…” Alivikutanisha vidole vyake vya mikono yote kwa pamoja akimaanisha kumi.
“Enhee!” Morena akaendelea kuitikia.
“Nikafungua kimoja kidogo dogo. Nilichokiona sasa aaah!” Fatumata akanesa nesa akifuatisha maneno aliyoyatamka kwa kupanda na kushuka.
Morena hakumdaka, alimfuata kwa macho alivyonesa kulia na kushoto akingoja kuisikia habari kamili.
“Almasi!” Fatumata alimalizia mithili ya mtu aliyeubwaga mzigo mzito kupitiliza.
“Almasi!? Unazijua almasi wewe au unazisikia tu? Ukute uliona vipande vya chupa ukajua almasi.” Morena hakumwamini kabisa.
“Nimekuja mjini na lori za mpunga huku waitukei inatikisa dunia naanzaje kutoijua almasi? Mungu na Mtume vile ni almasi pyuwa!” Fatumata alisisitiza, akipitisha kidole cha shahada shingoni na kukinyooshea juu kuapia.
“Sasa?” Morena akaomba dira ya mwito.
“Nataka n’kitaifishe kimoja, tunakimbilia zetu Zambia au Msumbiji hapo, tunakula maisha huku tunasikilizia kwanza, kisha tunarejea kulijenga taifa. Naamini hata hela ya kumlipa tutakuwa tumepata.”
Morena alimtazama mwenzake kama vile alikuwa anaisoma hiyo ramani ya kufika Zambia usoni pa somoye. Kisha, akaguna akipiga kofi moja hafifu hewani.
“Shosti hebu tuagize bia ya baridi kwanza, hiki unachoongea ni kama vile koo limekukauka sana mwenzangu. Ukurupuke na kiroba cha watu uko, ukimbie nacho wapi sijui, ujifiche siku mbili tatu, urudi kuishi maisha ya kawaida? Narudia tena na tena hivi unaijua jela wewe? Unaijua almasi?” Morena hakuelekea kukubaliana na mwenzake.
“Umaskini matusi somo! Mie nimeuchoka. Na tatizo lako uoga umekuzidi pia. Hapo ulipo, umri unaenda bado umebanana mule kwenye chumba kimoja chenye dirisha moja. Mwili unaporomoka huo hata gari ya mtumba huna!” Fatumata aliuongea ukweli unaochoma nafsi.
“Kwa hiyo?” Morena akabweta.
Maneno ya Fatumata yalimkwangua roho. Hata hivyo, wazo la kukiiba kiroba halikumwingia.
“Maisha ukitaka kuyapatia lazima kuna mbilinge upitie.” Akamshawishi tena.
Mwenzake wala hakumsikiliza. Aliangaza huku na kule kama mtu anayetafuta kitu.
“Psiiiii! We kaka!” Morena alimwita mhudumu aliyepita karibu yao. Akamwagiza. “Niletee maji madogo ya baridi.”
Naye Fatumata akadandia. “Na mie niletee.”
Mhudumu alipoondoka wakatazamana tena.
“Kwa hiyo?” ikawa zamu ya Fatumata. Akiutafuta msimamo wa mwenzake.
“Wahenga walisema, mchuma janga….” Morena hakumalizia.
Fatumata naye alimkatisha. “Umeanza mambo yako, Kiswahili chenyewe ulipata mswaki huko shule. Ungewaelewa sana hao wahenga ungekuwa na mijidigriii leo. Si wanasemaga elimu ndio ufunguo wa maisha?”
Akamsuta mwenzake, akimpindishia midomo upande.
Morena akacheka.
Akili za rafiki yake zilikuwa za mafungu mafungu kama zake tu, ingawa kidogo yeye alimzidi mwenzake wepesi wa kuelewa. Aliwaza. Fatumata na umbole sheshe alilokuwa nalo, ungempa karatasi akuandikie hata hilo jina lake la Fatumata, si ajabu ungeitisha umati wa Mtume ukusaidie kusoma! Katu, asingekosea kama angeamua kumuita shogaye mbumbumbu mzungu wa reli.
“Kimboka anajua ulikiona hicho kiroba?” Morena aliuliza. Wakati huo, mhudumu alirejea na chano chenye chupa za maji na bilauri. Walipokaribishw
a, waliendelea na maongezi yao.
“Kimboka anajua?” Morena akalirudia swali lake.
“Angekuwa anajua nisingekuja hapa. Najua hajui na mle ndani mwake anaingiza dazeni kwa dazeni ya wanawake. Hivyo, anaweza asijue kabisa nani kamkwapulia. Huoni godeni chansi hiyo?” Fatumata akasisitiza.
“Naona na kizungu cha kuongelea uko Zambia ushajifunza tayari. Mambo ya golden chance, sijui good morning – how are you teacher – I am fine – thank you au siyo eeeh?” Morena alitamka akiigiza lafudhi ya Kizungu.
Wakaangua kicheko, wakigonga viganja vyao.
***
Haya, mwisho wa kicheko…?
Madada ndo wameshasuka mkakati wa kuuaga umasikini kwa kumzunguka Kimboka. Watafanikiwa? Njoo tena hapa tuwafuatilie…
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA KWANZA
1
PALISHAKUCHA.
Pakuche mara ngapi?
Ni vile tu huyu Morena alilala chakari. Asubuhi hii ya saa nne, kwake ilikuwa ingali liamba. Alilala kifudifudi. Fofofo..
Ghafla, kuna mtu alimtoa katika ule ufofofo. Akamkera. Alimkera hasa!
Kivivu, aliinua shingo yake, akakigeuzia kichwa chake upande mwingine. Akasonya
Angali na mawenge ya usingizi. Si hayo tu, bali pia uvivu ulimjaa. Vikampa hali ya kutaka kuendelea kubadili uchago kila dakika, licha ya jua la asubuhi kuhanikiza nuru ya kutosha mle chumbani mwake.
Akilini, aliutaka utulivu kwa gharama yoyote ile. Japo apate kukimalizia hicho kipande cha usingizi. Wala hakujua kingekwisha saa ngapi. Alitaka kulala. Kulala tu mpaka pale mwili wake utakapomruhusu kutalikiana na kitanda.
Aliyemkera, akamkera tena.
“Eeh mchicha matembele majani ya kundeee… eeh mchicha tembeleee… eeh mchicha tembele majani ya mabogaaa”
Huyu muuza mboga ndiye aliyemgutua toka usingizini, kwani alikuwa akichuuza biashara yake ya mboga za majani karibu na dirisha la Morena. Dirisha lililokuwa upande wenye kichochoro kilichopakanisha chumba alichokuwemo na nyumba ya jirani.
Mchuuza mboga alisimama hapo kichochoroni pamoja na wateja wake waliokuwa wakichagua mboga toka kwenye tenga. Wakafanyiana mizaha ya hapa na pale iliyosindikizwa kwa vicheko vya juu na chini.
Kelele zao zikamfanya Morena ajihisi kama mtu anayepigiwa zumari sikioni. Akasonya tena. Msonyo mrefu uliobeba uzito wa makumi ya maneno. Maneno aliyotamani yawasilishe hisia zake kwa sauti ya kuhutubia umati. Alichefukwa.
Naam! Ikawa kama vile huo msonyo wake ulimuhimiza mchuuza mboga akolezee tena kibwagizo chake maradufu. Akamvumilia kidogo huku akiinua tena shingo yake na kuzisikiliza sauti za wateja wake. Akaitambua moja, ya mtoto wa mpangaji mwenzake.
“Somoe! We Somoe!” akaita kwa sauti ya kukaripia na Somoe mwenyewe akaginiza kwa sauti ya juu.
“Abeee!”
“Embu niondoshee huo mnada wenu hapo dirishani”
Morena akatoa amri yake kwa sauti ya chini kidogo huku akiyabana mate yaliyomjia ghafla kinywani. Hakuona pa kutemea. Akakunja ndita kadhaa usoni. Kwanza alikereka kwa kule kugutuliwa usingizini; pili, ile adha ya kujaa mate ilimkalfisha nafsi. Na mwisho, ombi lake kwa Somoe lilipita kimya kimya kama kivuli.
Muuza mboga naye kama mtu aliyefinywa alianza tena kuchuuza biashara yake kwa sauti. Safari hii Morena hakusubiri mbivu ziwe mbovu. Alitoka kitandani. Akasimama na kuikaza khanga yake kifuani. Ngoja nikamshikishe adabu! Akajiapiza.
Alipita katikati ya chumba chake, akivipamia vitu vilivyotupwa sakafuni shaghalabaghala; hapa nguo, pale viatu na makorokoro yake mengine chungu nzima.
Alihangaika na kitasa kwa takribani robo dakika wakati akiufungua mlango ambao ni dhahiri ulikuwa mbovu. Pale nje ya mlango wa chumba chake aliitafuta ndala yake moja na asiione, akaivaa hiyo moja iliyokuwepo na kuanza safari ya kuelekea nje.
Alimpungia mkono mpangaji mwenzake aliyepishana naye, akishindwa hata kuijibu sawasawa salamu aliyopewa, kwa kule kuyakonga mate kinywani. Aliukusanya mdomo wake akautanguliza mbele mithili ya mdomo wa bata.
Akatoka nje na kuyatema upenuni mwa nyumba. Akayafukia kwa mguu uliokuwa peku.
Haikuleta maana; kuivaa ile ndala moja na kisha kwenda kuyafukia mate kwa mguu uliopeku. Ila ndiyo falsafa ya maisha, kupata na kukosa; wanaokosa ndio wenye kutumika na kusulubika.
Twaibu! Morena aliiongoza miguu yake kuelekea ule upande wenye uchochoro. Alimfungia kibwebwe muuza mboga kana kwamba alitaka tena kwenda kulala akishamfukuzia mbali.
Alipoifikia ile kona inayoelekea uchochoroni, akausikia mlio wa bodaboda, mlio uliomgeuza shingo. Aliyemuona akamfanya ayasahau yote yaliyomtoa nje. Akakigeuza kiwiliwili kizima kumtazama mgeni aliyewasili.
Alikuwa rafikiye, Fatumata Mzinga. Somo yake wa kufa na kuzikana.
Alitulia akimtazama namna anavyoshuka toka kwenye bodaboda, mwili wake tipwatipwa uliogawanyika kike kisawasawa ukitibwirika. Na mshukaji nwenyewe akaongeza sifa za mkwezi kuudandia mnazi. Aliujaza madoido ule mtibwiriko!
Wanaume waliokuwa upande wa pili wa barabara palipo na karakana ya fenicha wakameza mate ya tamaa, wengine walijikohoza na wengine walikaribia kuviranda vidole. Umbile lake lilileta hali ya kubahashika pasi hiyari.
Wakaingia ndani, Morena akitangulia na Fatumata akimfuatia. Mle ndani Fatumata akayaanzisha maongezi mara tu baada ya kuufunga mlango na kwenda kuketi kitandani.
“Nilijua nikifika kwa Mzee Hizza n’takuta wanatembeza daftari la rambirambi” akazungumza akimtaja baba mwenye nyumba aliyopanga Morena.
“Aaah! kwa lipi?” Morena akauliza huku akiumba uso wa mshangao.
“Yale mapombe makali makali uliyogida jana. Mwanamke unakunywa kiama” Akampigia saluti. “Nikajua utaunguza hadi utumbo maana ile mijibaba jana ilikuvulia kofia ujue! Chupa ya tisa jicho kodo!... kope zimekusimama kama miiba ya nungunungu” Fatumata aliongea akitoa macho na kuchezesha mikono kuyasindikiza maneno yake.
Morena akacheka. Alicheka vile mwenzake alivyomsifu na kumsagua kwa pamoja.
“Tena mbona ungenikuta nimelala kama si muuza mboga mmoja mpuuzi alonikatishia usingizi wangu” Morena akalalamika akiutafuta mswaki wake kwenye stuli pana iliyokuwa na vitu vya kila aina; vipodozi, misumari, kalamu mbovu, dawa zilizokwisha muda wake mpaka karatasi za vocha zilizotumika. Stuli ilijaa hobelahobela!
Akaupata mswaki.
Pasipo dawa aliuchomeka mdomoni na kutoka nje. Alimuacha Fatumata anapitisha macho kwenye kipande cha gazeti kilichotumika kufungia dagaa mchele waliokwishaliwa tangu juzi.
Dakika moja Morena alirejea ndani, akautupia mswaki wake juu ya ile stuli.
“Kwanza nambie jana uliondoka na nani kwani… hukuokota garasa kweli?” Fatumata akamdodosa Morena aliyekuwa anaukagua uso wake kwenye kipande cha kioo.
Kioo kilichokuwa kimetundikwa kwenye msumari ukutani. Aliutazama uso wake, akazitazama nywele zake ndefu zilizopakwa rangi mbili tatu tofauti kiasi cha kufanana na mtu aliyejitwika jogoo kichwani.
Morena akacheka kwanza, kama ilivyo haiba yake. Alicheka akigeuka na kumtazama Fatumata kwa bashasha.
“Mimi huyu, niliyenyonyeshwa mataputapu. Nikalewe zile bia zenu za mafungu” akasonya. “Bia ya tisa nikikurembulia jua nimekuhurumia saaana”
“Kijukuu cha mwana harashi wewe!” Fatumata akashadidia akifinyanga kile kipande cha gazeti na kumtupia Morena, huku akitoka kitandani na kuketi sakafuni. Akatandaza miguu yake huu mashariki ule magharibi.
“Hizi kazi zetu ukijifanya unajua kulewa utakopesha kiuno hicho kila siku” akamjibu na kuendelea “Nimeingia kulala humu saa moja asubuhi” Morena akaachana na kioo na kukifuata kitanda.
“Eh! Nipe… nipe… michapo” Fatumata akasherehesha akipunga mikono hewani.
“Kitu Bokilo” Morena akatamka kwa mbwembwe akinyanyuka na kuketi sawa pale kitandani huku akilitaja jina la mwanaume aliyeondoka naye usiku uliopita.
“Yule Bokilo Mzaire?” Fatumata akauliza kishabiki, akitenga mikono kiunoni.
“Mzaire dada, mutu ya vitenge na bazee” Morena akafanya mbwembwe zake tena akipaza sauti.
“Pedeshee la Bukavu, Kinshasa na kati ya Lubumbashi, mutu ya suruali pande sita” Fatumata akaumalizia utambulisho.
“Kwani zile ni suruali? Kwa upana ule tuyaite mashuka tu dada”
Kikafuata kicheko kirefu cha kugongesha mikono, kisha wakarejea kwenye mjadala wao.
“Alikupeleka wapi? Maana wangu yule majinuni na akili zake za kuhesabu alijua kuninywesha tu. Tumefika kule Bondeni loji kwenye mbuyu akalala puh!”
“Ndani puh!” ikawa zamu ya Morena kushangaa.
“Puh! Nilitamani kumchumia mikwaju nimtandike fimbo za kitambi anijue mie nani” Fatumata hakusemea utani, alimaanisha kiasi cha kumchekesha mwenzake.
“Pole mwaya, mie kwanza alinipeleka gesti moja nzuri balaa maeneo ya Kigogo. Akanianzia na ahadi za mtaji wa biashara, nikaongeza bakora… chapa! chapa!” akakung’uta vidole. “Akaniahidi nyumba nzima. Dada upo?” Morena akalivuta neno la mwisho kwa mikogo mingi, Fatumata akiwa bado amemtumbulia macho.
“Nyumba nzima! Bokilo Mzaire huyo? Ulimvalia na njinjili?” Fatumata akauliza kwa midadi akijishikashika kiuno kumaanisha shanga zivaliwazo na wanawake kiunoni.
“Mie tena, nilimfungia hizi” akafunga dole gumba na kuviacha vinne hewani. “Sio watoto wa siku hizi wanaovamia fani na zigo la shanga ka’ fundo la msuli” Morena akamfanya Fatumata acheke mpaka machozi.
“Asubuhi kaacha elfu 50 kasema baadaye atan’tumia bajaji tukale kuku sekela mahali”
“Usinambie!” Fatumata akamaka. “Ngekewa hiyo dada. Mungu akitaka kukupa-” Fatumata akatamka akikomea njiani kwanza kisha kwa pamoja wakamalizia.
“Hakuandikii barua” wakamalizia kwa sauti za kuimbia irabu.
Wakacheka cheko lingine refu kisha wakatulia, wakiyaanza maongezi mengine.
Ilikuwa kawaida yao, kukutana namna hii na kuzungumzia maisha yao ya ukahaba almaarufu kama uchangudoa. Wangetambiana juu ya wanaume waliowaopoa, pesa walizopata na pengine hata ahadi hewa za hiki ama kile. Lakini pia, mara nyingine ingekuwa huzuni tupu, wangekutana kufutana machozi, kupeana pole na kusaidiana kwa suluba na madhila waliyokumbana nayo.
“Embu kaoge tutoke kwanza, twende mahali nikakupe akili za maisha leo” Fatumata sasa akaweka umakini kwenye mazungumzo yao.
“Kuna nini tena?”
“Kaoge tutoke mwe! hii mijumba yenu isiyo na silingibodi mtu akijamba hapa panya wa chumba cha tatu kule anasikia” Fatumata aliposema hivi Morena alicheka, na wapangaji waliokuwa nje nao wakasikika wakicheka. Dongo lile kuhusu nyumba walilisikia kama walivyoyasikia maongezi mengine yote.
“Kwako kuna nini?”Morena akasaili akinyanyuka toka kitandani.
“Hivi sijakwambia, baada ya ile harusi ya binamu, nyumba imejaa watu kama soko”
“Usinambie!” Morena akamtolea macho.
“Mwenzangu, ukipita nje utasema kuna meza ya muuza mitumba ndani… embu kaoge tutoke bwana” Fatumata akalijibu swali na kumuhimiza tena Morena ajihimu.
Alipotoka kuoga Morena alirejea chumbani kwake. Pasi kujali uwepo wa rafiki yake, akaitupilia mbali ile khanga moja iliyokuwa imesitiri maungo yake na kuanza kuranda mle chumbani akijipaka mafuta, akitafuta nguo ili mradi alikuwa na hekaheka za hapa na pale.
Morena alikuwa mrefu wa kadiri, ungemtazama kwa haraka haraka ungedhani ni mwanamke wa kisomali. Vile alivyojaaliwa nywele ndefu laini na wajihi mwembamba kiasi wenye pua iliyonyooka. Watu wengi walihisi Morena alikuwa na usomali ndani yake.
“Haya shanga ushatupa kule, kwanza huo mkufu kiunoni hauchuji?” Fatumata alimtupia swali mwenzake akimtazama vile alivyokuwa akimkatishia mtupu kama mwanga, huku akiuvaa huo mkufu wake.
“Dhahabu yenye gramu zake hii sio cheni zenu za vyuma chakavu ukinunua leo mtondogoo kutu imekutoa mapunye” Morena akajibu akianza kuvaa nguo zake.
“Hivi ulidunduliza miezi mingapi? halafu umenikumbusha Bintuni na cheni lake la kuhongwa”
“Yule nusura tumpeleke India kwa matibabu, sijui aliuokota wapi mcheni mzito kama mnyonyoro wa geti” Alidakia Morena na kuzua kicheko kingine mpaka kwa wapangaji waliokuwa koridoni wakidoea mazungumzo yao.
Morena alipomaliza kuvaa na kujipara, akajipulizia manukato yake. Manukato ghali kidogo kulinganisha na kipato chake cha kuungaunga.
Pamoja na uduni wa maisha yake na uzito wa majukumu aliyokuwa nayo, Morena hakuacha kujitafutia vitu alivyovipenda kwa dhati. Hata kwa kudunduliza senti moja kila siku, angeweka bila kusita wala kuchoka, aliamini haba na haba hujaza kibaba. Morena alipenda vidani vya dhahabu, na aliyapenda manukato.
Akamgeukia Fatumata.
“Haya twen’zetu sasa” akatamka huku akiufuata mkoba wake na kuweka sawa baadhi ya vitu vyake.
Wakatoka pamoja mpaka nje ambako walianza kutembea pole pole huku wakishauriana pa kwenda. Papo hapo, Fatumata akichombezea hizo akili za maisha alizotaka kumgawia mwenzake. Aliuremba mpango wake kiasi cha kumtia kiwewe mwenzake.
“Hili dili lililonifungisha safari likitiki… tutaununua huu mtaa mzima somo!” Fatumata akamfanya Morena adondoshe mguno.
“Ngoja tufike basi Kha!” akamtoa papara huku akijiandaa kuvuka barabara kuelekea mahali ziliposimama bodaboda.
Taratibu wakakaza mwendo kuwahi kupeana hizo akili za maisha. Wasijue tu namna ambavyo akili hizo zingekuja kuigharimu furaha yao maishani.
2
JUA la saba mchana liliwaka hasa!
Liliwakutia mgahawa maarufu wa Vitukoutata, maeneo ya Vingunguti. Kila mmoja alikwishaagiza chakula chake. Wakakishambulia chakula hicho haraka haraka, kana kwamba walikuwa wamekikamia.
Morena alikuwa wa kwanza kumaliza kula. Akamwita mhudumu amletee maji ya kunawa. Maana, mchuzi wa kongoro ulikwishamganda mikononi. Ikawa kero kwake. Wakati mhudumu anafika na beseni lake mkononi, Fatumata naye akawa amemaliza chakula chake. Akajiunga kwenye kunawa.
“Shing’ ngapi?” Fatumata aliuliza huku akikimbilia kutoa kijiti cha meno kwenye kichupa chake mara tu baada ya kumaliza kunawa.
Morena yeye alihangaika kuyachokonoa magego yake kwa ulimi.
“Vishalipiwa mbona!” Yule mhudumu alijibu akitabasamu, akiufurahia pia mshangao wa wanawake wawili mbele yake.
Wakatazamana kwa bashasha. Wakaendelea na mambo yao pasipo hata kusaili ni nani aliyewalipia. Nyakati zingine ofa kama hizi zilikuwa za kawaida kwao, hasa akiwepo Fatumata Mzinga. Wangelipiwa chakula, nauli na huenda wangepata ahadi za kupelekwa huku na kule kisha kuzungumza biashara.
Wateja wao walikuja kwa njia mbalimbali.
“Tawire! Haya leta habari habibti” Morena alijiweka sawa tayari kumsikiliza rafiki yake.
“Unamkumbuka yule bwana alonileteaga dili ya mawese?” Fatumata akaianzia mbali habari yake. Akakitupa kando kijiti cha meno.
“Bwana we hayo ya nani anafanya nini utanichanganya tu, hao mabwana zako wauza mawese nawajua kumi na…” Morena akajibu, akimfanya Fatumata amtukanie ukoo wake, akaliunga na tusi lingine la nguoni na Morena asijali.
“Kimboka” Fatumata alipolitaja jina Morena akadakia.
“Yule mpuuzi. Haya kafanyaje?” akauliza kwa sauti ya mkwara.
“Hujasamehe tu!”
“Muuza mawese yule aliyetaka kutulaza ndani kwa bia zake za mafungu.” Akasonya.
Uso wa Morena haukuwa na masihara hata kidogo. Alimpindishia mwenzake midomo.
“Tukio la mwaka juzi bado linakupandisha mavi ya kifua tu! Punguzaga vinyongo unenepe shaa!… embu sikia, Kimboka ana dili la mamilioni somo!”
Akayatumbua macho kimbeya.
Aliianza tena habari yake kwa madaha. Akimfanya Morena aukunje uso na kumeza mate mithili ya mtu aliyelambishwa kitu kichachu.
“La kuuza mawese yake?” Akauliza kwa dharau akibetua midomo.
“Sio mawese jamani!”
“Kumbe!?”
“Madini!” Alilitamka neno madini kwa sauti ya chini akikisogeza kichwa chake mbele zaidi ili Morena amsikie vizuri pamoja na kule kunong’ona.
Morena alitoa macho kana kwamba alichotamka Fatumata kilikuwa kitu cha kutisha mno. Akauliza kwa sauti ya mshangao. “Madini?”
“Mdomo huo mwanamke, shiii!” Fatumata akamuwahi, akimtaka apunguze sauti.
Morena akafunga mdomo wake wa kiganja chake cha kuume huku bado jicho likiwa limemtoka pima. Taratibu akamtazama mwenzake kama zumbukuku.
“Jela unaijua lakini Fatumata?”
“Jela ya nini?”
“Jela hizi za Segerea, Ukonga sijui Butimba?”
“Mie nilimsikia anaongelea biashara ya madini, sasa jela inahusikaje?”
“Mmh! Madini mwenzake utapeli Fatu, lakini haya! Kila la kheri kwenye huo mpango wako. Mie n’taendelea kuibia wanaume kwa mtaji huu chini mpaka siku yangu ikifika.” Alizungumza akiutazama huo mtaji wake.
“We huzitaki pesa?”
“Nazitaka ndio, ila hizo mishe mishe za lala apache alolo amka Bakhresa, Bongo hii, haya!”
“Mbona unan’tisha na sijamaliza, unajua nimekuita sababu kuna lingine na ndio hilo linaloniumiza kichwa?” Fatumata alimtazama mwenzake kwa uso mkavu usio hata na chembe ya utani.
Morena naye akamtazama kwa umakini kidogo, moyo ukimtokota. Alishaingia woga ghafla. Akauliza mboni za macho zikicheza kulia na kushoto kwa kasi ya ajabu. “Kitu gani?”
“Kuna kiroba cheusi hicho tukishikamana tunatoka huku uswazi”
“Eeeh!”
“Punguza mchecheto basi!”
“Haya niambie kuna nini kwenye hicho kiroba?” Morena akajiweka sawa, akitazama huku na kule kana kwamba alihofia watu wangewasikia wakiongelea mambo ya viroba.
“Ndio maana n’kakutoa kule kwenu.” Fatumata alimzodoa mwenzake, akiucheka ule mchecheto wa Morena. Huku akitaka kuziweka sawa akili za mwenzake, Fatumata aliendelea. “Sikia, wiki iliyopita, siku ile tuliyokesha Kiwalani sijui unaikumbua…”
“Tunakesha mara ngapi uko Kiwalani? We n’ambie moja mbili tatu basi!” Morena aliona anachelewa kuijua habari yenyewe.
“Haya twende, nililala kwa Kimboka pale, unajua tena kusikia mamilioni kidogo niingie wehu, sasa vile jasiri haachi asili….” Fatumata hakumalizia, Morena akamdaka.
“Ukaiba?”
“Hebu bwana we kha!” Fatumata alianza kukerwa na kule kukatishwa katishwa kila mara.
“Sikuiba, nilikuwa nafanya doria, nikatokezea stoo moja uchwara umo ndani. Na hapo ndio paliponifanya nikuite hapa n’kupe akili za maisha.” Alijieleza huku mwenzake akiitikia tu chapuchapu. Kichwa kikienda juu chini juu chini mara kadhaa.
“Nilikuta viroba hivi…” Alivikutanisha vidole vyake vya mikono yote kwa pamoja akimaanisha kumi.
“Enhee!” Morena akaendelea kuitikia.
“Nikafungua kimoja kidogo dogo. Nilichokiona sasa aaah!” Fatumata akanesa nesa akifuatisha maneno aliyoyatamka kwa kupanda na kushuka.
Morena hakumdaka, alimfuata kwa macho alivyonesa kulia na kushoto akingoja kuisikia habari kamili.
“Almasi!” Fatumata alimalizia mithili ya mtu aliyeubwaga mzigo mzito kupitiliza.
“Almasi!? Unazijua almasi wewe au unazisikia tu? Ukute uliona vipande vya chupa ukajua almasi.” Morena hakumwamini kabisa.
“Nimekuja mjini na lori za mpunga huku waitukei inatikisa dunia naanzaje kutoijua almasi? Mungu na Mtume vile ni almasi pyuwa!” Fatumata alisisitiza, akipitisha kidole cha shahada shingoni na kukinyooshea juu kuapia.
“Sasa?” Morena akaomba dira ya mwito.
“Nataka n’kitaifishe kimoja, tunakimbilia zetu Zambia au Msumbiji hapo, tunakula maisha huku tunasikilizia kwanza, kisha tunarejea kulijenga taifa. Naamini hata hela ya kumlipa tutakuwa tumepata.”
Morena alimtazama mwenzake kama vile alikuwa anaisoma hiyo ramani ya kufika Zambia usoni pa somoye. Kisha, akaguna akipiga kofi moja hafifu hewani.
“Shosti hebu tuagize bia ya baridi kwanza, hiki unachoongea ni kama vile koo limekukauka sana mwenzangu. Ukurupuke na kiroba cha watu uko, ukimbie nacho wapi sijui, ujifiche siku mbili tatu, urudi kuishi maisha ya kawaida? Narudia tena na tena hivi unaijua jela wewe? Unaijua almasi?” Morena hakuelekea kukubaliana na mwenzake.
“Umaskini matusi somo! Mie nimeuchoka. Na tatizo lako uoga umekuzidi pia. Hapo ulipo, umri unaenda bado umebanana mule kwenye chumba kimoja chenye dirisha moja. Mwili unaporomoka huo hata gari ya mtumba huna!” Fatumata aliuongea ukweli unaochoma nafsi.
“Kwa hiyo?” Morena akabweta.
Maneno ya Fatumata yalimkwangua roho. Hata hivyo, wazo la kukiiba kiroba halikumwingia.
“Maisha ukitaka kuyapatia lazima kuna mbilinge upitie.” Akamshawishi tena.
Mwenzake wala hakumsikiliza. Aliangaza huku na kule kama mtu anayetafuta kitu.
“Psiiiii! We kaka!” Morena alimwita mhudumu aliyepita karibu yao. Akamwagiza. “Niletee maji madogo ya baridi.”
Naye Fatumata akadandia. “Na mie niletee.”
Mhudumu alipoondoka wakatazamana tena.
“Kwa hiyo?” ikawa zamu ya Fatumata. Akiutafuta msimamo wa mwenzake.
“Wahenga walisema, mchuma janga….” Morena hakumalizia.
Fatumata naye alimkatisha. “Umeanza mambo yako, Kiswahili chenyewe ulipata mswaki huko shule. Ungewaelewa sana hao wahenga ungekuwa na mijidigriii leo. Si wanasemaga elimu ndio ufunguo wa maisha?”
Akamsuta mwenzake, akimpindishia midomo upande.
Morena akacheka.
Akili za rafiki yake zilikuwa za mafungu mafungu kama zake tu, ingawa kidogo yeye alimzidi mwenzake wepesi wa kuelewa. Aliwaza. Fatumata na umbole sheshe alilokuwa nalo, ungempa karatasi akuandikie hata hilo jina lake la Fatumata, si ajabu ungeitisha umati wa Mtume ukusaidie kusoma! Katu, asingekosea kama angeamua kumuita shogaye mbumbumbu mzungu wa reli.
“Kimboka anajua ulikiona hicho kiroba?” Morena aliuliza. Wakati huo, mhudumu alirejea na chano chenye chupa za maji na bilauri. Walipokaribishw
a, waliendelea na maongezi yao.
“Kimboka anajua?” Morena akalirudia swali lake.
“Angekuwa anajua nisingekuja hapa. Najua hajui na mle ndani mwake anaingiza dazeni kwa dazeni ya wanawake. Hivyo, anaweza asijue kabisa nani kamkwapulia. Huoni godeni chansi hiyo?” Fatumata akasisitiza.
“Naona na kizungu cha kuongelea uko Zambia ushajifunza tayari. Mambo ya golden chance, sijui good morning – how are you teacher – I am fine – thank you au siyo eeeh?” Morena alitamka akiigiza lafudhi ya Kizungu.
Wakaangua kicheko, wakigonga viganja vyao.
***
Haya, mwisho wa kicheko…?
Madada ndo wameshasuka mkakati wa kuuaga umasikini kwa kumzunguka Kimboka. Watafanikiwa? Njoo tena hapa tuwafuatilie…