Riwaya fupi: Ripoti

JOTO LA MOTO

JF-Expert Member
Apr 11, 2018
758
555
ripoti.jpeg


TITLE: RIPOTI YA MKAGUZI.

SEHEMU YA KWANZA.

NDANI-OFISI YA MZEE WOTA.
Mzee Wota, Bwana wa miaka 60 hivi, ameketi akiwa makini akisoma kilichopo kwenye Lap top, huku akibofya keyboard ya Lap top ile.
Mlango unagongwa, “ingia” anasema Mzee Wota huku bado akiwa amekazia macho kwenye Laptop yake.Mlango unafunguka anaingia Paul Siza, kijana mtanashati, miaka kama 35 hivi, akiwa amevalia nadhifu, anaingia na kusimama mbele ya meza ya Mzee Wota, Mzee Wota anainua kichwa kumuangalia Paul, “shikamoo Mzee” anasema Paul, “vipi mbona leo asubuhi asubuhi?” anauliza Mzee Wota, Paul anabaki kimya kwa sekunde kadhaa kisha anashusha pumzi, “Mzee kwa nini usirekebishe tu hiyo ripoti?”, anasema Paul, Mzee Wota anabaki anamuangalia Paul, “walau huu upepo upite” anaongeza Paul, Mzee wota anatoa miwani, “ndio kilichokuleta kwangu asubuhi hii Paul?” anauliza Mzee Wota kwa sauti ya chini, “Kijana huu ukaribu wetu usikufanye utake kunielekeza cha kufanya” anasema Mzee Wota huku amemkazia Paul macho,zinapita sekunde chache, Mzee Wota anavaa miwani na kurudi kuendelea kutumia lap top yake, Paul anabaki amesimama. Zinapita sekunde kadhaa, Mzee Wota anaacha anachofanya, anaifunga Lap top na kuiweka kwenye begi lililokuwa pembeni, anavua miwani na kuiweka kwenye mfuko wa koti, kisha anainuka anachukua lile begi na kuelekea mlangoni, kabla ya kuufungua mlango anageuka na kumuangalia Paul, “kijana ..mimi huwa sirudi nyuma” anasema Mzee Wota, “kawaambie waliokutuma kwangu kuwa hii ripoti itasomwa kama ilivyo..haitabadilishwa hata nukta” anaongeza Mzee Wota kisha anageuka na kufungua mlango na kutoka. Paul anabaki amesimama kwa muda kisha anatoa simu yake mfukoni na kuibofa mara kadhaa huku akielekea mlangoni na kutoka.

NJE-KWENYE PARKING-MCHANA.
Paul anaelekea ilipo Gari aina ya Rav 4 nyeupe, huku akiwa na simu sikioni, “naona Mzee bado ameshikilia msimamo wake” anasema Paul, “basi..wewe umeshamaliza kazi yako Siza..tuachie fanya mambo mengine” inasema sauti ya kwenye simu, “kupanga ni kuchagua..naona Mzee ameshachagua” inaongeza sauti ile ya kwenye simu, “lakini Enok...” anasema Paul na mara unasikika mlio wa kuashiria simu imekatika, Paul anaitoa simu sikioni, anafungua mlango wa gari, anaingia na kuondoa gari.

NJE-BARABARANI-MCHANA.
Gari aina ya Toyota Landcruiser V8 nyeupe ikiwa mwendo wa wastani inakatiza barabara ya uhuru kuelekea mtaa wa Jitegemee.Ndani ya Gari yupo Mzee Wota,na pembeni yupo Ben, kijana wa miaka 31 hivi akiwa kwenye usukani anaendesha. Wanaenda kwa muda huku wote wakiwa kimya kila mmoja akitafakari ya kwake, huku kwa mbali ikisikika sauti ya matangazo kutoka kwenye redio ya gari lile.“Mzee mimi naona kadri siku zinavyoenda na hii kazi inakuwa na mitihani” anasema Ben na kumfanya Mzee Wota ashtuke na kugeuka kumuangalia, “wamekufuata tena?” anauliza Mzee Wota, Ben anashusha pumzi “bado wananisumbua” anasema Ben, “wewe waambie kila wanachotaka kusikia..mimi sina shida Ben” anasema Mzee Wota, "usiingie matatizoni kwa ajili yangu" anaongeza Mzee Wota, “tatizo hawaniamini..wanaona kama kuna ninachowaficha” anasema Ben huku akinyonga usukani kuingia kwenye parking ya jengo moja la ghorofa mbili lililopo upande wa kushoto wa barabara, gari linafika parking na kusimama.

NJE-KWENYE PARKING YA JENGO-MCHANA.
Mita kadhaa pembeni kutoka liliposimama gari la Mzee Wota ipo Noah nyeupe yenye vioo vya giza (tinted). Mzee Wota anateremka na kisha anafungua mlango wa abiria na kubeba begi lake la Laptop, anageuka na kukutana uso kwa uso na Ziba, Bwana wa miraba minne, akiwa amevalia miwani nyeusi, “tuna shida na wewe Mzee” anatamka Ziba huku bastola ikiwa mkononi kwake, “hii ni nini tena?” anauliza Mzee Wota kwa mshtuko na mshangao huku anaangalia pembeni na kuwaona Enok na Kabwe, nao wakiwa wamevalia miwani nyeusi, “gari ile pale inakusubiri” anasema Ziba huku akielekeza kwa bastola ilipo ile Noah nyeupe.
Wakati huohuo Kabwe anafika upande ule alipo Ben “shuka chini” anaamrisha Kabwe,Ben anateremka, “twende” Kabwe anamuamrisha Ben kisha wote wanaongozana kuelekea ilipo Noah ile na kuingia.

NDANI-CHUMBA NAMBA 1-MCHANA.
Ben yupo kwenye kiti, Kabwe ameketi mita kadhaa mbele yake akiwa amekunja nne na sigara mdomoni, “nadhani tulikuelekeza wapi upeleke Gari?” anasema Kabwe, “siwezi kumsaliti Mzee Wota..yule ni kama Baba yangu” anasema Ben, “unajaribu kuwa shujaa sio?” anasema Kabwe kwa sauti ya kebehi, Ben anabaki kimya, Kabwe anapiga pafu ya sigara, “umefanya uchaguzi mmbaya sana dogo” anasema Kabwe na kupiga tena pafu moja ya sigara na kisha anakunjua miguu yake na kuketi kwa kuinamia mbele,“na vipi kuhusu hiyo nywila?” anauliza Kabwe kwa sauti ya chini na ya upole, “ukweli utakuweka huru” anaongeza Kabwe, Ben anashusha pumzi,
“hiyo ni siri yake mimi siifahamu” anasema Ben, Kabwe anashusha pumzi, anainuka na kutoa simu yake mfukoni na kuibofya, anaiweka sikioni, “itabidi twende kwenye plani B..mtafuteni Sele” anasema Kabwe na kisha anaitoa simu sikioni.

NDANI-CHUMBA NAMBA 2-MCHANA BAADAE.
Sele, Bwana wa makamo, yupo na Laptop ya Mzee Wota akibofyabofya, Mzee Wota ameketi kwenye kiti pembeni, nyuma yake amesimama Mbupu, bwana wa miraba minne akiwa ameshikilia SMG jirani na kichwa cha Mzee Wota, Enok amesimama mita chache kutoka pale, akiwa na simu sikioni, akionekana yupo makini kusikiliza simu ile, “ndio tupo hapa na mtaalamu wa mifumo tunaweka mambo sawa boss”, anasema Enok, zinapita sekunde kadhaa,“Sawa Boss nimekuelewa”, anasema Enok na kuitoa simu sikioni na kuja walipo wengine na kuketi juu ya meza anayoitumia Sele, “hivi haya yote ni kwa faida ya nani?” anauliza Mzee Wota na kumfanya Enok kugeuka na kumuangalia Mzee Wota kwa jicho korofi, “mnapoteza muda ..ipo siku ukweli wote utajulikana tu” anaongeza Mzee Wota huku bado Enok akimuangalia, kinapita kimya kifupi huku Sele akiendelea kubofya ile Laptop,“mimi naombeni nikajisaidie” anasema Mzee Wota na kukatisha ukimya ule, Enok anaangalia pembeni na kuchukua chupa kubwa tupu ya maji juu ya meza na kumrushia Mzee Wota, Mzee Wota bila kujigusa anaiacha chupa ile ikimgonga na kuanguka chini, kisha anashusha pumzi na kumuangalia Enok “walau uniheshimu kwa umri wangu basi” anasema Mzee Wota. Kimya kinaendelea huku Sele akiendelea kubofya ile Laptop.

NDANI-OFISI YA BOSS-SAA TATU USIKU.
Mzee Bosi, Mzee wa miaka 70 hivi, amesimama pembeni ya meza yake, mkononi ana glasi yenye pombe kali,Enok amesimama pembeni akiwa ameweka mikono nyuma mithili ya Mtu mtiifu sana kwa mkubwa wake, Mzee Bosi ameinamisha kichwa kama mtu anayefikiria jambo, “mmeachana nae saa ngapi?” anasema Mzee Bosi, “jioni hii..saa kumi na mbili” anasema Enok, wanabaki kimya kwa sekunde kadhaa.
“mmefanya maamuzi ya kipumbavu sana” anasema Mzee Bosi kwa sauti ya chini huku bado ameinamisha kichwa chake, “tulisubiri maelekezo yako boss” anasema Enok, “tumia akili Enok” anasema Mzee Bosi kwa ukali huku anainua kichwa kumuangalia Enok, “tutasahihisha Boss” anasema Enok,
“lini?” anauliza Mzee Bosi kwa ukali, “ndani ya saa 24” anasema Enok na kutulia, kunapita ukimya kwa sekunde kadhaa, “ondoka” anasema Mzee Bosi na kumshtua Enok, “sawa bosi” anasema Enok huku kwa haraka anageuka na kuondoka.

NDANI-NYUMBANI KWA PAUL-CHUMBANI-USIKU WA MANANE.
Miri, mwanamke wa miaka kama 30 hivi, amelala kitandani fofofo na mara anashtushwa na mguso wa kitu na kufungua macho, anainua kichwa kuangalia pembeni yake, “D” anaita Miri kwa sauti yenye mshtuko na uoga, anakuja Paul huku akiwa anavaa Sweta, “mambo yameshaharibika kule kwa Mzee Wota” anasema Paul huku akiwa anaketi na kuvaa viatu vyake vya michezo (raba), “Mungu wangu” anasema Miri kwa mshtuko, “kwa hiyo unaenda huko?” anauliza Miri, Paul bila kumjibu anainuka na kuelekea mlangoni, “nisubiri usiniache” anasema Miri huku kwa haraka akitoka pale kitandani.

....itaendelea...
 
TITLE:RIPOTI.

SEHEMU YA MWISHO.
NJE-NYUMBANI KWA MZEE WOTA-USIKU WA MANANE.
Gari la Paul linafika, ndani wapo Paul na Miri wanapokelewa na mwanga wa kumulimuli wa ambulance iliyosimama mlango mkuu wa nyumba ya Mzee Wota.Mita chache pembeni lipo gari dogo la silva, mara taa za gari lile dogo zinawaka na gari linakuja mpaka usawa wa gari la Paul, kioo kinashuka na anaonekana Enok, Paul anashusha kioo cha gari lake na kuangaliana macho kwa macho na Enok, “naomba kaa mbali na hizi ishu Siza” Enok anamwambia Paul, Paul anabaki kimya akimuangalia Enok, kioo cha gari ya Enok kinapanda huku akiondoa gari.Paul anageuka na kukutana na machela iliyobeba mwili wa Mzee wota ukiingizwa kwenye ile ambulance, huku pembeni kukionekana Watu kadhaa wake na waume wanaoonekana kugubikwa na huzuni kubwa.

NDANI-NYUMBANI KWA BEN-USIKU WA MANANE.
Paul na Ben wamesimama sebuleni huku Ben akiwa anavaa jaketi kwa haraka, “tunaondoka wote sasa hivi” anasema Paul, “Mke na Mtoto wabaki huko huko Morogoro kwa muda mpaka huku kutakapotulia” anaongeza Paul, “ni wapi tunaenda?” anauliza Ben, “utajua mbele ya safari” anasema Paul, “walau kwa sasa fanya ninavyokuambia” anaongeza Paul kisha anashusha pumzi, anamgonga Ben mgongoni kwa mkono, “you will be ok” anasema Paul huku Ben akimalizia kuvaa viatu, Ben na Paul wanatoka.

NJE-MTAA FULANI-USIKU WA MANANE.
Gari la Paul linafika nje ya nyumba moja kongwe ya udongo, Ben na Paul wanateremka, “ni nyumba ya mjomba wangu..amehamia mjini” anasema Paul huku akielekea mlangoni na kufungua kofuli iliyopo pale, anafungua nakuwasha tochi kwenye simu yake na kisha Paul na Ben wanaingia, “utakaa hapa kwa muda” anasema paul “kuna Mtu atakuja asubuhi” anaongeza Paul. “nashukuru kwa yote bro” anasema Ben, “usijali” anasema Paul na kisha anatoka na kuufunga mlango.

NDANI-KANISANI-MCHANA.
Watu kadhaa wapo kanisani, mbele kukiwa na jeneza, Mchungaji mmoja amesimama kwenye mimbari akitoa mahubiri, “kuna mengi yanasemwa juu ya huu msiba wa Mzee wetu Wota” Mchungaji anasema, “na ni kawaida kwa jamii inapompoteza Mtu mkubwa..kunakuwa na uvumi wa kila aina” anaendelea Mchungaji yule, “ripoti ya daktari inasema Mzee alipatwa na mshtuko wa moyo..kwa hivyo niwaombe ndugu jamaa na marafiki..tupuuze yote yanayoendelea kwenye mitandao” anaendelea kusema Mchungaji.Maneno haya yanaonekana kumchoma sana Paul aliyeketi siti ya mwishoni jirani na mlango mkuu, Paul anainamisha kichwa na kutoa leso yake na kujifuta machoni.Mara Paul anahisi kuguswa na mkono begani kwake kama ishara ya kupewa pole, Paul anabaki amejiinamia,zinapita sekunde chache mkono ule unatolewa na Mtu yule anaondoka kuelekea siti zilizopo mbele ya kanisani pale, Paul anainua macho kumuangalia na anagundua Mtu Yule ni Enok, paul anashtuka na kutulia kwa sekunde kadhaa kama Mtu aliyepigwa na shoti ya umeme, kisha anainuka na kuondoka kwa haraka na kutoka nje ya kanisa.

NJE-MTAA FULANI-MCHANA.
Gari ya Paul inafika kwa kasi na kufunga breki nje ya nyumba, paul anateremka kwa haraka na kuelekea mlangoni, “Ben” paul anaita huku akiufungua mlango na kuchungulia ndani, “Ben” anaendelea kuita Paul huku akiangalia huku na kule, anatoka pale na kuelekea nyuma ya nyumba, “Ben” anaendelea kuita Paul na mara anapatwa na mshtuko mkubwa baada ya kuona mwili wa mtu ukiwa mita kama thelathini kutoka pale, kwenye shamba lile lenye kahawa na Migomba, “shit” anatamka Paul kwa mshtuko mkubwa huku akisogelea ulipo mwili ule, “Ben..my God” anaita tena Paul kisha kwa uchungu na unyonge anaketi juu ya jiwe kubwa lililopo pale pembeni, anashusha pumzi na kuinamisha kichwa chake na kubaki ametulia.

NDANI-OFISI YA PAUL-MCHANA.
Paul yupo ofisini ameketi, mara mlango unafunguka anaingia Enok, Paul anashtuka, “vipi?” anasema Enok, Paul anashusha pumzi mithili ya Mtu aliyeshusha mzigo mzito, “utakaimu nafasi ya Mzee Wota” anasema Enok na kumfanya Paul kutoa macho, “Enok please..sipo tayari kwa hilo” anasema Paul, “sijakuuliza..nimekwambia” anasema Enok, “na kwa bahati mbaya huna choice kwenye hili Siza” anasemaa Enok, paul anabaki ameduwaa, “press ya uteuzi itafanyika baadae leo saa tano” anasema Enok na kubakia amesimama huku mikono yake ikiwa mifukoni, zinapita sekunde kadhaa za ukimya “hivi ni nini mwisho wa haya yote Enok?” anauliza Paul na kupokelewa na sauti kali ya Enok “acha us..ge Siza” anasema Enok huku anaitoa mikono yake mifukoni na kuiweka juu ya meza ya Paul na kuinamia kumuelekea Paul, “na hii tabia uliyoanzisha hapa karibuni tunakufuatilia kwa karibu” anasema Enok, “kuwa makini Siza” anaongeza Enok kwa sauti ya kitisho, wanabaki wanaangaliana kwa muda, Enok anainuka na kurudisha mikono yake mifukoni, anageuka kutaka kutoka, anasita na kugeuka kwa Paul, “by the way..salamu zako nyingi kutoka kwa Mzee” anasema Enok, “pamoja na huu ujinga unaoanza lakini bado ana imani kubwa na wewe” anaongeza Enok na kisha anaufungua mlango na kutoka, Paul anajiigemeza kwenye kiti mithili ya Mtu aliyechoshwa ka kazi ya siku nzima.

MIEZI KADHAA BAADAE

NDANI-OFISINI KWA MZEE BOSI-MCHANA.
Mzee Bosi ameketi kwenye kochi, akiwa amevaa fulana nyepesi na boxer, akionekana ni Mtu aliyejaa uoga huku akitetemeka kama Mgonjwa anayesikia baridi kali. Enok ameketi kwenye kiti pembeni akiwa ameinamisha kichwa, Mlango unafunguka anaingia Matola, Bwana wa makamo, wa miaka kama 60 hivi, “karibu mheshimiwa” anasema Enok, “Mzee anaendeleaje” anauliza Matola, Enok anashusha pumzi,“bado ni changamoto” anasema Enok, “huyo” Enok na Matola wanashtushwa na sauti kali ya Mzee Bosi, “huyo anakuja” anasema tena Mzee Bosi kwa sauti ya juu na kuwafanya Matola na Enok kubaki wameduwaa, “muondoeni hapa anataka kunikaba tena”, anasema Mzee Bosi huku akiinuka na kuingia chini ya meza, “anamaanisha nini?” Matola anauliza, “hapo anamaanisha anamuona Mzee Wota” anasema Enok, wanabaki kimya wakimuangalia Mzee Bosi akiwa pale chini ya meza, "ulimpata manyaunyau?" anauliza Matola,"ameshindwa" anasema Enok, "hata Mchungaji Devi ameamkia hapa wala hakuna nafuu yoyote" anaongeza Enok, zinapita sekunde kadhaa.Matola anashusha pumzi, “presha ni kubwa sana huko nje” anasema Matola, “muda ni mrefu sasa..lazima tuseme kitu” anaongeza kusema Matola, “sijui itakuwaje?” anasema Enok, “tumeandaa press saa nane..na wewe ndio utakuwa msemaji mkuu wa kinachoendelea” anasema Matola, “hapana mimi hilo sitoweza Mkuu” anasema Enok, “mimi nimemaliza Enok” anasema Matola, “muda wote umekuwa ni msemaji wa Mzee..na wewe ndio utasema kuhusu Mzee” anaongeza Matola, “sasa nitasema nini..niseme Mzee amerukwa akili?” anauliza Enok, “andaa cha kusema bado kuna muda wa kutosha mpaka saa nane” anasema Matola na kuondoka, Enok anabaki ameduwaa,anageuka na kumkuta Mzee bosi akiwa nyuma yake na chuma mkononi, “Wota ananiambia wewe ndio mbaya wangu” anasema Mzee Bosi na kisha kumpiga Enok na chuma kichwani, Enok anaanguka chini, Mzee Bosi anaendelea kumshambulia Enok kichwani kwa chuma kile,Enok anapiga mayowe ya kuomba msaada kisha anatulia tuli, Mlango unafunguka wanaingia Mlinzi 1 na 2, wanakimbia na kumshika Mzee Bosi, Enok anavuja damu nyingi kichwani, Mlinzi 1 anabaki amemshikilia Mzee Bosi, Mlinzi 2 anamuinua Enok na kumkokota kuelekea nje.Sekunde kadhaa baadae anarudi Mlinzi 2 akiwa na kamba ya kudu, “wanamkimbiza jamaa hospitali” anasema Mlinzi 2, kisha wanashirikiana kumfunga Mzee bosi kwa ile kamba.

NDANI-WODI YA SADARUKI-MCHANA.
Enok yupo kitandani akiwa hana fahamu na mipira kadhaa imefunika uso wake, mlango unafunguka, anaingia Paul na kufika pale kitandani, anasimama kwa muda akimuangalia Enok, “malipo ni hapahapa Enok” anasema Paul kwa sauti ya chini, mara mlango unafunguka anaingia Matola, “Dokta anasema jamaa amepata traumatic brain injury” anasema Matola, Paul anashtuka, “hiyo ni mbaya sana” anasema Paul, “hata akizinduka kwenye hii coma atakuwa Mtu wa kitandani maisha yake yote yaliyobaki”, anasema Matola, kinapita kimya kifupi, “ile ripoti halisi ya Mzee Wota si unayo?” anauliza Matola, “najua ilipo.. nitakukabidhi tukitoka hapa” anasema Paul, “ndio tutakayoiwasilisha kikao kijacho..sio hii aliyohaririwa” anasema Matola, "Mungu ni mkubwa" anasema Paul.

NDANI-CHUMBA CHA PRESS CONFERENCE-MCHANA.
Matola yupo mbele ya vipaza sauti kadhaa, mbele yake kuna umati wa Wana habari, “Mzee yupo nje ya nchi kwa matibabu..anasumbuliwa na presha” anasema Matola, “tunasubiri ripoti ya madaktari..na tutawajulisha kila hatua anavyoendelea” anaongeza Matola, “ila ni muda sasa umepita bila taarifa yoyote..kuna usalama kweli?” anauliza mmoja wa Waandishi kwa kushtukiza, “naomba nisijibu swali lolote kwa leo..itoshe tu kusema Mzee yupo kwenye matibabu..na kila kitu kipo kwenye utaratibu mzuri..tuchape kazi” anasema Matola kisha anainuka na kuondoka.

..MWISHO..
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom