Kashfa ya Richmond: Bunge laitupilia mbali taarifa ya serikali
* Serikali yapewa muda zaidi hadi Novemba la sivyo....
Waandishi Wetu, Dodoma, Dar
SUALA la utekelezaji wa maazimio 23 ya Bunge kuhusu mkataba wa kampuni tata ya Richmond Development LLC jana lilichukua sura mpya baada ya bunge kukataa ripoti ya serikali na kuitaka itekeleze maazimio yote yaliyofikiwa Februari mwaka jana na kutoa taarifa mpya katika mkutano wa Novemba mwaka huu.
Hatua hiyo ya Bunge imefikiwa baada ya Kamati ya Nishati na Madini chini ya Mbunge wa Bumbuli (CCM), William Shelukindo kuwasilisha maoni yake bungeni dhidi ya ripoti ya serikali ya utekelezaji wa maazimio hayo, iliyowasafisha watumishi wote wa umma waliotuhumiwa kwenye kashfa hiyo.
Shellukindo alisema serikali imeacha vipengele vingi vya maazimio hayo ya bunge, kikiwemo cha kuwashtaki wamiliki wa kampuni ya Richmond, ambako aliyeshtakiwa na kesi yake inaendelea mahakamani, Naeem Gire ni mdogo wa mhusika na si yule aliyekusudiwa.
Baadhi ya watendaji waliosafishwa na serikali ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) Dk Edward Hoseah na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Johnson Mwanyika, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Athur Mwakapugi na Kamishina wa Nishati, Bashir Mrindoko.
Hata hivyo, jana jioni Katibu Mkuu Kiongozi, Phillemon Luhanjo aliitisha mkutano wa waandishi wa habari na kueleza kuwa tuhuma ya uzembe dhidi ya watumishi hao zilithibitika, kwamba hawakufanya uchunguzi wa kutosha kujiridhisha, hivyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa kila mmoja kwa kiwango chake, kazi ambayo imeanza na inaendelea kufanyika.
Pamoja na serikali kupewa muda huo kukamilisha utekelezaji wa maazimio, wabunge wote waliochangia hoja, ukiondoa Mbunge wa Bukoba Vijijini, Nazir Karamagi aliyejiuzulu uwaziri kutokana na kashfa hiyo, walikuwa wakali kama nyuki kwa kile kilichoonekana kama mhimili wa dola (serikali) unadharau mhimili wa bunge.
Mbunge aliyekwenda mbali zaidi ni Dk Willibrod Slaa (Karatu-Chadema) aliyesema Rais Jakaya Kikwete hawezi kujivua lawama katika suala hilo la kushindwa kutekeleza maazimio ya bunge kwa kuwa linashughulikiwa na serikali yake, yeye akiwa mwenyekiti wa baraza la mawaziri.
Hivyo, mbunge huyo aliungana na wabunge wenzake waliopendekeza suala hilo lihitimishwe Novemba, vinginevyo serikali ijiuzulu na kuitisha uchaguzi mkuu.
Mheshimiwa spika mimi nashangaa tunaposema kuwa rais hakuhusika katika sakata zima la Richmond wakati yeye ndie mwenyekiti wa baraza la mawaziri, si kitendo cha kiungwana kabisa lazima tukubali kuwa hata yeye anatakiwa kuwajibika, alisema na kuongeza:
Hapa tunatakiwa kwenda mbele zaidi hivyo nasema kuwa ifikapo mwezi Novemba mwaka huu kama serikali haitatoa ufumbuzi wa kina juu ya jambo hili ni lazima ijiuzulu na tuingie kwa wananchi kuomba ridhaa tena katika uchaguzi, alisema.
Alisema Rais Jakaya Kikwete ndiye amelifikisha suala hilo hapa lilipo kutokana na serikali yake kushindwa kutekeleza maazimio ya bunge.
"Hawa ndio waliotufikisha hapa tulipo, na wawajibishwe kwa kupuuza maazimio ya bunge, ingekuwa nchi ya wenzetu hapa serikali ingejiuzulu na kurudi kwenye uchaguzi ili wananchi wachague upya
"Novemba serikali itoe tamko kuhusu hili (Richmond), kwa kuwa haiwezekani Hosea (Mkurugenzi wa Takukuru) anatuhumiwa halafu anapewa onyo, sielewi serikali inataka nini?" alihoji.
Hata hivyo, kauli ya mbunge huyo na nyingine za namna hiyo zilizowahi kutolewa nje ya bunge, zilipingwa baadaye na Luhanjo akisema kuwa maneno ya kuhusishwa kwa Rais Kikwete si ya kweli na hayana msingi wowote. Rais hajahusika na uamuzi wa tenda hiyo kupewa kampuni ya Richmond kama vile ambavyo hakuhusika na kupewa tenda kwa kampuni za Aggreko na Alstom.
Akichangia Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole- Sendeka, alishangaa kitendo cha serikali kusema kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Dk Edward Hoseah hana hatia, lakini hapo hapo akapewa onyo.
Mbunge huyo alisema haiwezekani kuwa Dk Hoseah hana hatia, wakati tayari alishaidangaya serikali kwa kusema kuwa mkataba huo ulikuwa safi, jambo ambalo limeonekana kuwa ni uongo mtupu.
Hapa serikali ituambie ukweli ni nani hasa anakwamisha suala hili na kwa nini Dk Hoseah aliyeitakasa Richmond bado yuko kazini hadi leo, anafanya nini hapo aondoke upesi na katika hili mimi nitasema hadi mwisho wa uhai wangu maana kero hii inatugusa sisi tuliosema kuwa wawajibishwe, alisema Ole-Sendeka.
Alisema kuwa anashangaa kwa nini serikali inashindwa kusema mkosaji ni nani wakati kama kosa limetokea lazima kuna mkosaji.
"Kama mamlaka imekataa ushauri na kama kuna waziri yuko kwenye kazi na imeshindikana kumchukulia hatua, tuambieni sisi tumchukulie hatua kwa kuwa ni lazima serikali iwe wazi," alisema.
Ole-Sendeka alisema asingependa kumhusisha Kikwete pamoja na mkewe Salma, lakini akashangaa kwa nini baadhi ya watumishi hao waliotuhumiwa walibaki maofisini wakati wanachunguzwa, huku wakiwa na jukumu la kuwachunguza walioko chini yao.
Kwa upande wake, Said Nkumba (Sikonge) alisema kuwa serikali ina mdhalilisha Rais Kikwete kutokana na kuwa kiongozi huyo wa nchi alikubali kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowasa, tayari alishatambua kuwa kulikuwa na kosa, hivyo ni lazima na wengine wawajibike.
Nkumba aliwataka wale wote wanaotuhumiwa katika sakata hilo wawajibike mara moja kuliko kuendelea kusubiri wawajibishwe na wengine.
Ukiona umechafuka kaa utulie,kuliko ukiendelea utachafuka zaidi na ikibidi usitake kuwachafua na wengine kwani kwa kufanya hivyo unaweza kuchafuka zaidi, na hiyo ni dhambi kwa Mungu, alisema Nkumba.
Akichangia katika mjadala huo mmoja wa watuhumiwa katika sakata la Richmond, Nazir Karamagi alisema kuwa Bunge la Tanzania halijawahi kumuonea mtu katika maamuzi yake kinachofanyika huwa ni kweli tupu na kuitaka serikali isipate kigugumizi katika kutoa maamuzi.
Kama mimi Karamagi nimefanya makosa basi niwajibishwe na ikibidi akaunti zangu zikamatwe kwa uchunguzi ili haki iweze kutendeka na sio kukaa muda mrefu ili kusubiri maamuzi ambayo hayajulikani yatatolewa lini.
Hata hivyo, baada ya wabunge kuzidi kuiwashia moto serikali Spika wa Bunge Samuel Sitta aliingilia kati kuiokoa, akakatisha wachangiaji na aliitaka serikali kuandaa majibu ya kina ya kumaliza suala hilo katika mkutano wa 17 na kuleta majibu sahihi.
Spika alimketisha chini Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja ambaye alianza kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za wabunge, akiwa tayari amekiri kuwa ni kweli kuna mapungufu katika utekelezaji.
Sitta alisema kwa muda huo waziri Ngeleja angeweza kutoa majibu ambayo hayatawaridhisha wabunge na hivyo kuzua mjadala mwingine.
Source: Mwananchi